YESU NI MFALME WA AINA GANI KWAKO? 

by Admin | 28 April 2021 08:46 am04

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tuyatafakari maandiko pamoja.

Je Bwana Yesu ni Mfalme katika maisha yako?..Kama una tabia zifuatazo, hajawa bado Mfalme kwako, haijalishi utamkiri kiasi gani.

Kama unamtafuta kwaajili ya faida zako za kimwili, ikiwemo kupata mali, kupata mke, kupata mume, kupata kupata watoto, kupata umaarufu, na mambo mengine yote ya kimwilini , Tambua kuwa yeye si mfalme kwako, haijalishi utamtangaza kwa watu kuwa ni mfalme kwako, lakini yeye hakujui!!.

Utauliza tunasoma wapi katika maandiko?.. Hebu tukitafakari kisa kifuatacho kwa ufupi kisha tutapata majibu…

Yohana 6:10  “Yesu akasema, Waketisheni watu. Na mahali pale palikuwa na majani tele. Basi watu waume wakaketi, wapata elfu tano jumla yao.

.11  Basi Yesu akaitwaa ile mikate, akashukuru, akawagawia walioketi; na kadhalika katika wale samaki kwa kadiri walivyotaka.

12  Nao waliposhiba, aliwaambia wanafunzi wake, Kusanyeni vipande vilivyobaki, kisipotee cho chote.

13  Basi wakavikusanya, wakajaza vikapu kumi na viwili, vipande vya mikate mitano ya shayiri vilivyowabakia wale waliokula.

14  Basi watu wale, walipoiona ishara aliyoifanya, walisema, Hakika huyu ni nabii yule ajaye ulimwenguni.

15  Kisha YESU, HALI AKITAMBUA YA KUWA WALITAKA KUJA KUMSHIKA ILI WAMFANYE MFALME, AKAJITENGA, AKAENDA TENA MLIMANI YEYE PEKE YAKE”.

Hebu jiulize, kwani! Bwana Yesu, hataki au hapendi kuitwa Mfalme??.. Hata hivyo ndicho anachokitengeneza sasa, anatengeneza ufalme wake, na yeye ndiye atakuwa Mfalme wa wafalme. Lakini hapa tunaona anaukataa na kuukimbia ufalme??..Ni kwanini?..Jibu ni rahisi, ni kwasababu yeye hatengenezi wala hatafuti ufalme wa kidunia.

Yohana 18:33  “Basi Pilato akaingia tena ndani ya Praitorio, akamwita Yesu, akamwambia, Je! Wewe ni Mfalme wa Wayahudi?

34  Yesu akamjibu, Wewe wasema hivi kwa nafsi yako, au watu wengine walikuambia habari zangu?

35  Pilato akajibu, Ama! Ni Myahudi mimi! Taifa lako na wakuu wa makuhani ndio waliokuleta kwangu. Umefanya nini?

36  Yesu akajibu, UFALME WANGU SIO WA ULIMWENGU HUU. Kama ufalme wangu ungekuwa wa ulimwengu huu, watumishi wangu wangenipigania, nisije nikatiwa mikononi mwa Wayahudi. Lakini ufalme wangu sio wa hapa”

Hiyo ndio sababu aliwakimbia wale makutano waliotaka kumfanya awe mfalme wao… Waliona wakimpata atawasaidia kujenga miji yao, atawasaidia kunyanyua uchumi wa nchi yao, atawasaidia kupata fedha nyingi, atawasaidia kutokomeza umasikini.  Lakini Yesu aliwakimbia… na walimtafuta kwa bidii na walipompata sehemu nyingine aliwaambia maneno yafuatayo..

Yohana 6:24  “Basi mkutano, walipoona ya kuwa Yesu hayuko huko wala wanafunzi wake, waliingia mashuani wenyewe, wakaenda Kapernaumu wakimtafuta Yesu.

25  Hata walipomwona ng’ambo ya bahari, walimwambia, Rabi, wewe umekuja lini hapa?

26  Yesu akawajibu, akasema, AMIN, AMIN, NAWAAMBIENI, NINYI MNANITAFUTA, SI KWA SABABU MLIONA ISHARA, BALI KWA SABABU MLIKULA ILE MIKATE MKASHIBA.

27  Msikitendee kazi chakula chenye kuharibika, bali chakula kidumucho hata uzima wa milele; ambacho Mwana wa Adamu atawapa, kwa sababu huyo ndiye aliyetiwa muhuri na Baba, yaani, Mungu”.

Na jitihada zao zote za kumtafuta awe mfalme, hata hakuwa mfalme wao, Yesu aliwaepuka. Kilichowatokea wale ndicho kinachotutokea kanisa la sasa. Biblia inasema…

Waebrania 13:8  “YESU KRISTO NI YEYE YULE, JANA NA LEO NA HATA MILELE.

9  Msichukuliwe na mafundisho ya namna nyingine nyingine, na ya kigeni; maana ni vizuri moyo ufanywe imara kwa neema, wala si kwa vyakula, ambavyo wao waliokwenda navyo hawakupata faida”.

 Ndugu Bwana Yesu hajabadilika kama watu wanavyombadilisha sasa, Ni yeye Yule, jana, na leo na hata milele!!!…maana yake tabia zako ni zile zile hazijabadilika, kama aliwakimbia wale makutano, waliotaka kumfanya mfalme wao, atatukimbia na sisi pia vile vile, kama tukimwendea kwa mtindo ule.

Kama Bwana Yesu atawakana siku ile watu waliotoa pepo kwa jina lake, na huku mioyo yao ipo mbali naye??..si zaidi wewe aliyekupa mali leo na bado ni mlevi?. Hao amewapa uwezo wa kutoa pepo lakini kawakana mwisho wa siku?..jiulize wewe uliyepewa nyumba na gari na tumbo lako kufunguliwa na bado unavaa kidunia, jiulize utasilimika vipi siku ile?, wewe uliyeponywa kimiujiza na bado hutaki kujikana nafsi yako na kumfuata Yesu, utasalimika vipi?, wewe uliyeponywa ugonjwa kimiujiza na bado hutaki kuuacha ulimwengu, jiulize utasalimikaje siku ile?..

Unadhani Bwana kukupa wewe mali, au mtoto, au kukuponya ugonjwa wako uliokuwa sugu, ndio kitu cha kwanza anachokitafuta kwako??..lengo la kukufanyia hayo ni ili tu ugeuke! Utubu na uwe mkamilifu kama yeye na si kwa lengo lingine. Ukitafsiri kwamba Bwana kakuponya ugonjwa wako kwasababu anapendezwa na wewe..fahamu kuwa umepotea!..Ukitafsiri kuwa Bwana kaifanikisha biashara yako kwasababu eti anataka uwe bilionea, fahamu kuwa umepotea!!.. Ameifanikisha hiyo biashara yako kusudi kwamba utubu na umrudie yeye, uwe mkamilifu. Lakini ukidhani kuwa ni kwasababu amependezwa na wewe, na moyoni ukijitumainisha kwamba ni mfalme wako, na Bwana wako, siku ile atakukana, pamoja na kwamba ni yeye ndiye aliyekufanikisha!!

Kama hujampokea Yesu maishani,  mlango wa neema bado upo wazi, ingawa hautakuwa hivyo siku zote. Huu ni wakati wako wa kumpokea Yesu, kwa kumwamini moyoni mwako, na kukiri kwa kinywa chako, na kuamua kwa dhati kuacha dhambi zote ulizokuwa unazifanya.. Unaziacha kwa vitendo, kama ulikuwa ni mlevi unavunja vikao na makundi yote ya ulevi, kama ulikuwa ni kahaba, unachoma nguo zote za kikahaba ulizokuwa unavaa ikiwemo suruali zote, na lipstick, wanja na mengineyo, kama ulikuwa unasikiliza miziki ya kidunia unaifuta yote katika simu yako, au popote pale ulipoihifadhi, kama ulikuwa ni shabiki wa mambo ya kidunia kama mipira, filamu, na mambo yanayofanana na hayo, unayaacha yote.

Na baada ya kufanya hivyo unatafuta ubatizo sahihi, kama bado hujabatizwa, kumbuka ubatizo sahihi ni ule wa maji tele, na kwa jina la Yesu Kristo, na baada ya hapo Bwana atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu, ambaye atakuongoza katika kuijua kweli yote ya maandiko, na kukusaidia kuushinda ulimwengu.

Bwana akubariki.

afadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp


Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/04/28/yesu-ni-mfalme-wa-aina-gani-kwako/