Nini maana ya vifungeni viuno vya Nia zenu? (1Petro 1:13).

by Admin | 7 February 2022 08:46 am02

Tusome,

1Petro 1:13 “Kwa hiyo vifungeni viuno vya nia zenu, na kuwa na kiasi; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo.

14 Kama watoto wa kutii msijifananishe na tamaa zenu za kwanza za ujinga wenu”.

Popote panapozungumziwa “kujifunga viuno” katika biblia panamaanisha “kuwa na utayari”. Kama ni msomaji mzuri wa biblia utakumbuka kipindi wana wa Israeli wanatolewa Misri na Mungu, ile siku ya  kwanza, wakiwa wanamla Yule pasaka, Bwana Mungu aliwaambia wamle huku wamevaa viatu vyao miguuni, na kujifunga mikanda viunoni (maana yake wawe katika mazingira ya kuondoka)..sio wawe katika mazingira ya kulala baada ya kula, bali mazingira ya kuondoka baada ya kula.

Kutoka 12:10 ‘Wala msisaze kitu chake cho chote hata asubuhi, bali kitu kitakachosalia hata asubuhi mtakichoma kwa moto.

11 Tena mtamla hivi; MTAKUWA MMEFUNGWA VIUNO VYENU, mmevaa viatu vyenu miguuni, na fimbo zenu mikononi mwenu; nanyi mtamla kwa haraka; ni pasaka ya Bwana”.

Kwahiyo “kujifunga viuno” kunamaanisha “kujiweka tayari”. Hivyo tunaposema “tujifunge viuno vya akili zetu” tutakuwa tunamaanisha “tuwe tayari kiakili”.. Vile vile tunaposema “tujifunge viuno vya roho zetu, wakati wa kumngojea Bwana”..tutakuwa tumemaanisha “tujiweke tayari katika roho zetu katika kumngoja Bwana” kama Bwana alivyosema katika Luka 12:35..

Luka 12:35 “Viuno vyenu na viwe vimefungwa, na taa zenu ziwe zinawaka;

36 nanyi iweni kama watu wanaomngojea bwana wao, atakaporudi kutoka arusini, ili atakapokuja na kubisha, wamfungulie mara.

37 Heri watumwa wale, ambao bwana wao ajapo atawakuta wanakesha. Amin, nawaambieni, atajifunga na kuwakaribisha chakulani, atakuja na kuwahudumia”.

Vile vile tunaposema “tujifunge viuno vya Nia zetu” maana yake ni “tuwe/tujiweke tayari Nia zetu” Kwa jambo fulani linalofuata.

Kwahiyo huo mstari wa 1Petro 1:13 badala ya kusema “vifungeni viuno vya Nia zenu”…tunaweza kuuweka hivi “Kwa hiyo kuwenu tayari katika Nia zenu; mkiitumainia kwa utimilifu ile neema mtakayoletewa katika ufunuo wake Yesu Kristo”.

Je! Na sisi  viuno vyetu vimefungwa?…tupo tayari katika Nia zetu?, Tupo tayari kwenda mbinguni?..Tupo tayari kuihubiri injili?, tupo tayari kumtumikia Mungu kwa mioyo yetu yote na nguvu zetu zote?

2Timotheo 4:1 “Nakuagiza mbele za Mungu, na mbele za Kristo Yesu, atakayewahukumu walio hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake na kwa ufalme wake;

2 lihubiri neno, UWE TAYARI, WAKATI UKUFAAO NA WAKATI USIOKUFAA, karipia, kemea, na kuonya kwa uvumilivu wote na mafundisho”.

Hizi ni siku za Mwisho na Kristo anarudi siku yoyote, na atakaporudi alisema atarudi na ujira wake..

Ufunuo 22:12 “Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.

13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho”.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Kuhubiri injili kwa husuda na fitina ndio kupi?

KIKWAZO CHA EUODIA NA SINTIKE.

Je ni sahihi kuweka walinzi kulinda mali zetu?

Ni kwa namna gani, upendo husitiri wingi wa dhambi? (1Petro 4:8).

CHAMBO ILIYO BORA.

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2022/02/07/nini-maana-ya-vifungeni-viuno-vya-nia-zenu-1petro-113/