AINA YA MAADUI UTAKAOKUTANA NAO KATIKA SAFARI YAKO YA WOKOVU.

by Admin | 16 January 2020 08:46 pm01

Pale unapookoka au unapoamua kumtumikia Mungu ni vizuri kufahamu, aina za maadui ambao utakutana nao kuiharibu imani yako kwa namna moja au nyingine. Hiyo itakusaidia ili siku utakapokutana nao usiyumbishwe kiasi cha kukata tamaa ya kuendelea mbele.

#1 Adui wa kwanza ni Shetani na mapepo yake:

Luka 22:31 “Akasema, Simoni, Simoni, tazama, Shetani amewataka ninyi apate kuwapepeta kama vile ngano;

32 lakini nimekuombea wewe ili imani yako isitindike; nawe utakapoongoka waimarishe ndugu zako”.

Shetani akishaona umeokoka kweli kweli, hawezi kutulia tu kukuangalia unafanikiwa rohoni kiwepesi wepesi tu ni lazima atanyanyuka ili kukuandalia baadhi ya visa, hapo ndipo wengine atawaletea misiba, wengine atawasababishia kufukuzwa kazi, wengine magonjwa Fulani ya ajabu ajabu tu, wengine atawaletea majanga n.k. hiyo yote ni kwa lengo tu la kumfanya utetereke na ukate tamaa uiche imani yako, umkufuru Mungu..Kama alivyojaribu kufanya kwa Ayubu, kumletea majanga yote yale.

#2 Watu ya nyumbani kwako mwenyewe:

Mathayo 10:36 “na adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake.

37 Apendaye baba au mama kuliko mimi, hanistahili; wala apendaye mwana au binti kuliko mimi, hanistahili.

38 Wala mtu asiyechukua msalaba wake akanifuata, hanistahili”.

Hapa ndipo shetani anapopenda kupatumia hasaa kwa mtu ambaye ndio kwanza mchanga kiroho, aliyekusudia kujitwika misalaba wake na kumfuata Yesu. Dada/Kaka unapoamua kumfuata Yesu kwa kujikana..jiweke tayari kupishana na baba yako au mama yako, au ndugu zako, au watoto wako, au jamii yako na marafiki zako, jiandae kuonekana umerukwa na akili, au umelogwa. Na Wakati mwingine kutengwa, kudharauliwa, na wengine wanafikia hatua hata ya kufukuzwa nyumbani, au kuzuiwa kula chakula au kunyimwa ada ya shule n.k. Ikiwa Yesu ni Bwana wetu ambaye hakuwa na dhambi hata moja hakuaminiwa na ndugu zake, (soma Yohana 7:5), Zaidi walipomwona anaanza kuhubiri walitaka kwenda kumkamata na kusema amerukwa na akili (Soma Marko 3:21). Si zaidi mimi na wewe ambao tunakasoro nyingi?.

Hata wewe ukimfuata yeye, utakutana na hayo hayo. Huwezi ukaelewana na ndugu zako wote moja kwa moja kwa uamuzi uliouchukua. Ipo sehemu utapishana nao tu. Lakini hilo lisikuvunje moyo. Songa mbele katika Imani…Ni shetani anawatumia tu lakini hao ni ndugu zako …Na hatawatumia hivyo milele kwa hivyo wapende tu.

#3 Ndugu yako wa karibu sana katika Imani:

Tofauti na ndugu wa mwilini. Adui mwingine ambaye unapaswa uweke akili kuwa unaweza kukutana naye mahali Fulani katika safari yako ya wokovu au huduma, ni ndugu mwenzako wa karibu sana katika imani.

Huyu ni Mtu ambaye huwezi kumtegemea, ni miongoni mwa wale ambao pengine unasali nao kila siku, unashirikishana nao kila siku habari njema za wokovu, unaokwenda kushuhudia nao, mnafanya kazi ya Mungu pamoja. Ghfla tu akakugeuka bila sababu yoyote yenye mashiko…anaweza kuingiliwa na kitu tu Fulani kidogo sana pengine tamaa Fulani, Na hiyo ikamfanya awe tayari kukusaliti au kuwa adui yako bila kujali mmekuwa katika safari pamoja kwa muda gani , bila kujali kwa kukusaliti huko kunakuachia madhara makubwa nyuma kiasi gani…

Hichi Ni chanzo ambacho huwezi kukitegemea, Hivyo jiweke tayari kiakili ili kusudi kwamba ikikutokea usivunje moyo kiasi cha kushindwa kuendelea mbele..

Mfano wa mtu wa namna hii ni Yuda. Alikuwa tayari kumuuza Bwana wake kwa tamaa ndogo tu ya fedha.

Zaburi 41: 9 “Msiri wangu tena niliyemtumaini, Aliyekula chakula changu, Ameniinulia kisigino chake”.

#4 Manabii wa uongo:

Mathayo 7:15 “Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani ni mbwa-mwitu wakali.

16 Mtawatambua kwa matunda yao. Je! Watu huchuma zabibu katika miiba, au tini katika mibaruti”?

Hawa licha tu ya kuwa na lengo la kukupotosha kwa mafundisho yao ya uongo., lakini pia kama wewe ni mtu wa Mungu uliyesimama wapo tayari hata kutoa ushuhuda wa uongo kinyume na wewe kwa lengo la aidha kujisafisha wao au kukuangusha wewe kwa makusudi ili wapate faida Fulani kutoka kwako.(3Yohana 1:10).

Hawa nao jiandae kukutana nao katika utumishi wako, au ukristo wako.

#5 Watumishi wenzako:

Hawa sio lazima wawe wa uongo, wanaweza wakawa wa ukweli, lakini kama hawajasimama vizuri, na kukosa ufahamu wa kuyapambanua maandiko vizuri, wanaweza kwa sehemu Fulani shetani akawatumia kuwafanya kuwa maadui wa Imani yako kwa muda.. Lakini bado wataendelea kubakia kuwa watumishi wa Mungu.

Mfano wa hawa ni Elfazi, Sofari, na Bildadi, Marafiki wa Ayubu. Ni wazee waliokuwa na hekima, washauri wa karibu sana wa Ayubu. Lakini walipoona Ayubu amekumbwa na matatizo kama yale, wao pasipo kukaa chini na kumwuliza Mungu ni nini maana yake..Wao wakakimbilia moja kwa moja kumlaumu Ayubu kuwa ametenda dhambi ndio maana yale yote yakampata..Na wakatumia vipengele kabisa vya maandiko ili kuthibitisha wanachokisema.. Na hiyo ndiyo iliyomfanya Ayubu akafadhaike zaidi hata ya kufiwa na watoto wake.

Kwasababu wale aliowategemea kuwa watakuwa na hekima ya kupambanua kilicho sahihi na kisicho sahihi, ndio wamekuwa wa kwanza kuwa mwiba kwake.

Vivyo hivyo, wapo watumishi ambao ni kweli wameitwa na Mungu, lakini watakapokuona unapitia katika hali Fulani kwenye imani tofauti na matazamio yao pengine ulitegemea na wao wawe wa kwanza kukuelewa..Ndio wanakuwa wa kwanza kukupinga tena wanatumia maandiko ..pengine ili tu kumridhisha mtu Fulani.

Hivyo hawa nao utakutana nao sehemu Fulani katika safari yako ya wokovu. Usiwachukie bali waombee kama Ayubua alivyowaombea marafiki zake, na baada ya muda mambo yote yatakuwa sawa.

#6 Viongozi wa dini za Uongo:

Nikisema viongozi wa dini za uongo simaanishi tu wale wa dini za mbali hapana, namaanisha wale ambao wanaonekana wapo katika Imani yako. Hawa ndio maadui wa ngazi ya juu sana, akitoka shetani na mapepo yake, hawa ndio wanaofuata .. wanaitumia serikali na wakati mwingine hata dola kupingana na kushindana na watu wa Mungu wa kweli.

Na hii itakupata ikiwa unaihubiri kweli kinyume na mafundisho yao. Wapo tayari kukupeleka mabarazani kukuhoji, na kukupiga na wakati mwingine hata kukuua..Vifo vingi vya mashahidi wa Yesu na mitume vilisababishwa na hawa.

Hawa ndio mfano wa Mafarisayo na Masadukayo. Walimpinga Bwana Yesu wakati wote, na kumpeleka kwa Herode na Pilato ili auawe.

Hata sasa, wapo wameshikamana na dola sana, na katikati ya hawa ndipo Yule mpinga-Kristo atakapotokea. Ibada za sanamu na mafundisho ya kipagani yasiyoambatana na maandiko ndiyo wanayoyahubiri.

Mathayo 10:17 “Jihadharini na wanadamu; kwa maana watawapeleka mabarazani, na katika masinagogi yao watawapiga;

18 nanyi mtachukuliwa mbele ya maliwali na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushuhuda kwao na kwa mataifa”.

Bwana anasema tazama nimekwisha kuwaonya mbele..(Mathayo 24:25).

Lakini pamoja na majaribu yote hayo, Mungu aliahidi kuwa hatamwacha mtu yeyote atakayemwendea,.Anamwachilia nguvu ya ziada ya kuweza kukabiliana na hivyo vizuizi,..Hapo ndipo mtu aliyeokoka anapojua kweli Mungu yupo pamoja na yeye. Lakini pia kwa kupitia hayo yote mwisho wake hauwi bure..

Ukiyastahimili hayo yote basi ufahamu kuwa thawabu yako ni kubwa sana mbinguni. Na Mungu atakufanya chombo chake kiteule kwa kazi yake.

Hivyo zidi kusonga mbele katika Imani ikiwa wewe upo tayari safarini katika wokovu. Ukifahamu kuwa taji lako limeshawekwa tayari mbinguni…

Luka 6:22 “Heri ninyi watu watakapowachukia, na kuwatenga, na kuwashutumu, na kulitupa nje jina lenu kama neno ovu, kwa ajili ya Mwana wa Adamu.

23 Furahiwani siku ile na kuruka-ruka, kwa kuwa, tazama, thawabu yenu ni kubwa mbinguni, maana, baba zao waliwatenda manabii vivyo hivyo”.

Hivyo furahi, kwasababu mbinguni unaheshimika. Kadhalika kumbuka pia kuwaombea wote wanaokuudhi, wote wanaotumika na shetani pasipo wao kujijua..waombee heri wala usiwaombee shari kama Bwana wetu Yesu Kristo alivyotufundisha..(katika Mathayo 5:43-46 na warumi 14:12).

Bwana akubariki sana.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe au piga namba hii 0789001312

Mada Nyinginezo:

ZIFAHAMU HUDUMA KUU (10) ZA SHETANI DUNIANI.

ZIFAHAMU HOJA SABA ZENYE NGUVU MBELE ZA MUNGU.

NILIMWONA SHETANI, AKIANGUKA KUTOKA MBINGUNI.

NENO LA MUNGU NI DAWA ILIYO TOFAUTI NA DAWA NYINGINE.

NENO LA MUNGU NI DAWA ILIYO TOFAUTI NA DAWA NYINGINE.

JE! WATOTO WACHANGA WANAWEZA KUHUKUMIWA NA KUTUPWA MOTONI.

JE WAJUA?

NI NINI KINAKUPATA UNAPOIPUUZIA INJILI?

URIMU NA THUMIMU NI NINI KATIKA BIBLIA?

BONDE LA KUKATA MANENO.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/01/16/aina-ya-maadui-utakaokutana-nao-katika-safari-yako-ya-wokovu/