SAA YA KUHARIBIWA IIJIAYO ULIMWENGU WOTE.

by Admin | 19 February 2020 08:46 pm02

Saa ya kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote Inakuja..

Ufunuo 3:10 “Kwa kuwa umelishika neno la subira yangu, mimi nami nitakulinda, utoke katika saa ya kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi”.

Kuna saa ya kuharibiwa inakuja huko mbeleni, ni wakati ambapo kila mtu kwa macho yake atakuwa anaona jinsi dunia inavyokwenda kuisha ndani ya kipindi kifupi sana, kutokana na dhiki, na mapigo, pamoja na mambo ya kutisha yatakayokuwa yanaendelea duniani wakati huo.. Kipindi hicho kitakuwa ni kifupi sana, kisichozidi miaka 7 tu. Na kitaanza muda mfupi tu baada ya unyakuo kupita.

Unyakuo ndio utakaokuwa kalenda ya kututambulisha kuwa dunia imebakisha umri wa miaka 7 tu. Na ndio maana itamgharimu Mungu awaondoe kwanza wale wateule wake watakatifu ambao walikuwa wanalishika Neno la Subira yake.. Watu ambao maisha yao yote, mawazo yao yote yalikuwa yanaelekea mbinguni tu, waliojikana nafsi, waliotengwa na ulimwengu, hao tu ndio Mungu atakaowanyakua ..Ili kupisha uharibifu huo kuchukua nafasi yake.

Kama tu vile alivyomwondoa Henoko, kwa kumnyakua asikutwe na gharika, …ndivyo itakavyokuwa kwa watu hao wachache sana, watanyakuliwa wasionekane duniani, kama vile alivyomtenga Ibrahamu akawa mbali na Sodoma na Gomora ndivyo itakavyokuwa kwa wale ambao wanaishi Maisha ya uaminifu sasa, wataondoshwa katika ulimwengu huu kabla ya siku ile ya uharibifu, na watakwenda kumlaki Bwana Yesu mawinguni na moja kwa moja safari ya kwenda kumwona Baba itaanzia hapo.

Lakini wale wengine ambao ni wakristo-vuguvugu, hawatakwenda popote, watakuwa mfano wa Nuhu wataishuhudia dhiki, wataingia katika misukosuko ya dhiki kuu na mateso makali ambayo biblia inasema haijawahi kuwepo tangu kuwekwa kwa misingi ya ulimwengu, kama vile Nuhu alivyokuwa katika dhiki ndani ya Safina..Kama vile Lutu alivyokuwa anapitia dhiki ile ya misukosuko sodoma ya Gomora ilivyokuwa inachomwa, siku zake zote alikuwa ni mbioni tu,..ndivyo itakavyokuwa kundi hilo kubwa la wakristo wanaosema wameokoka lakini Maisha yao hayana ushuhuda wowote hawaishi kama watu wanaomngojea Bwana wao. Dhiki hiyo itakuwa ni sehemu ya Maisha yao. Mpinga-kristo atawawinda huku na huko kama kuku..

Ndugu biblia inavyosema DHIKI basi ujue ni dhiki kweli kweli ,licha tu ile ya mpinga-kristo yatakuwepo pia mapigo mengine ya Mungu kwa wale watakaoipokea chapa, kasome Ufunuo 16, hadi mwisho kabisa , wanadamu wataadimika kama Dhahabu biblia inasema hivyo katika (Isaya 13),kama leo hii usivyoweza kuikota dhahabu kama mawe barabarani ndivyo itakavyokuwa kwa watu wakati huo, Kama alivyotoka tu Nuhu na wenzake 7 katika ya mabilioni ya watu ndivyo itakavyokuwa siku hiyo, kama walivyotoka watatu tu yaani Lutu na Watoto wake wawili ndivyo itakavyokuwa kwa mabilioni ya watu waliopo leo hii duniani.. kikundi kidogo sana, na tena watakuwa ni wale watakaowahifadhi wayahudi katika ule wakati wa dhiki za mpinga-kristo, Lakini wewe uliyepo leo hii unaipinga injili sasa , siku hiyo utakuwa ni jivu limelala hapo chini au mzoga, na ndege watakuwa wanakula nyama yako.

Tukiachilia mbali ile vita ya Harmagedoni, siku yenyewe ambayo Bwana atashuka na mawingu ambapo kila jicho litamwona, na watu watamwombolezea, misingi ya dunia hii unayoiona itatikisika, na kutakuwepo na tetemeko kubwa la ardhi ambalo halijawahi kuwepo, kumbuka wakati huo hayo yanaendelea tayari dunia imeshakuwa giza, hakuna jua wala mwezi, wala nyota yoyote angani, tetemeko hilo litaitikisa milima, mpaka hivi visiwa vyote unavyoviona leo hii vitahama, wewe wakati huo utakuwepo wapi Siku ya kuharibiwa? Wafalme, watakuwa wakilia wakiomba milima iwaungukie wafe, lakini wasikumbane na hiyo hasira ya mwana-kondoo.

Ufunuo 6:12 “Nami nikaona, alipoifungua muhuri ya sita, palikuwa na tetemeko kuu la nchi; jua likawa jeusi kama gunia la singa, mwezi wote ukawa kama damu,

13 na nyota zikaanguka juu ya nchi kama vile mtini upukutishavyo mapooza yake, utikiswapo na upepo mwingi.

14 Mbingu zikaondolewa kama ukurasa ulivyokunjwa, na kila mlima na kisiwa kikahamishwa kutoka mahali pake.

15 Na wafalme wa dunia, na wakuu, na majemadari, na matajiri, na wenye nguvu, na kila mtumwa, na mwungwana, wakajificha katika pango na chini ya miamba ya milima,

16 wakiiambia milima na miamba, Tuangukieni, tusitirini, mbele za uso wake yeye aketiye juu ya kiti cha enzi, na hasira ya Mwana-Kondoo.

17 Kwa maana siku iliyo kuu, ya hasira yao, imekuja; naye ni nani awezaye kusimama”?

Unaona?

Mambo haya utayashuhudia wewe ambaye bado upo nje ya Kristo, na wewe ambaye unaishi Maisha ya uvuguvugu sasahivi. Dalili zote zinathibitisha kuwa sisi watu wa kizazi hichi, haya mambo yatatupata, na dalili kubwa ni kuwa huu ni wakati ambao watu wanamejisahau, na pale watu walipojisahau na wanaona kuna Amani biblia inasema Hapo ndipo uharibifu unapokuja kwa ghafla (1Thesalonike 5:2)….Swali ni Je! Tumejiwekaje tayari..

Je! Bado unaishi Maisha ya kubahatisha? Utasema tena ni kwanini mnahubiri hivyo kana kwamba mnao uhakika kuwa Yesu atarudi wakati wetu..Ndio tunahubiri hivyo kwa nguvu zote kwasababu anayejua siku na saa ya kiama, ametuambia tuhubiri hivyo kwa nguvu sana…

Luka 14:33 “ Angalieni, kesheni, [ombeni], kwa kuwa hamjui wakati ule utakapokuwapo.

34 Mfano wake ni kama mtu mwenye kusafiri, ameiacha nyumba yake, amewapa watumwa wake amri, na kila mtu kazi yake, naye amemwamuru bawabu akeshe.

35 Kesheni basi, kwa maana hamjui ajapo bwana wa nyumba, kwamba ni jioni, au kwamba ni usiku wa manane, au awikapo jimbi, au asubuhi;

36 asije akawasili ghafula akawakuta mmelala.

37 Na hilo niwaambialo ninyi, nawaambia wote, Kesheni.

Sasa ikiwa wewe, unasikiliza injili ya mapepo inayokuhubiria kuwa dunia haitaangamizwa, ujue kuwa upo hatarini sana,. Kama hujamaanisha kumfuata Bwana Yesu, basi ni heri ukafanya hivyo sasa kabla mlango wa neema haujafungwa..Chaguo ni lako, uamuzi ni wako..Lakini fahamu tu wale wanaolishika Neno la Subira yake leo hii, hao ndio watakaoepushwa na saa ile ya kuharibiwa..

Bwana, Mkuu wa uzima wetu akubariki.

Maran Atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

SAKRAMENTI NI NINI, NA JE! IPO KATIKA MAANDIKO?

TOFAUTI KATI YA HEKALU, SINAGOGI NA KANISA NI IPI?

Kwanini Bwana Yesu, aliruhusu yale mapepo yawaingie nguruwe?

Ikiwa sisi tuliumbwa na Mungu,Je! Mungu aliumbwa na nani?

Nini maana ya huu mstari ” Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;”?(2Timotheo 4:7)

SALA YA ASUBUHI

NINI MAANA YA SISI KUWA WATOTO WA MUNGU?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/02/19/saa-ya-kuharibiwa-iijiayo-ulimwengu-wote/