Neno Korbani linamaanisha nini? (Marko 7:11)

by Admin | 17 August 2020 08:46 pm08

SWALI: Neno “Korbani” linalozungumziwa katika Marko 7:11 lina maana gani?


JIBU: Ili tupate picha nzuri ya Neno hilo embu tusome sehemu zote mbili zinazozungumzia jambo hilo hilo moja.

Mathayo 15 :1-6

1 “Ndipo Mafarisayo na waandishi toka Yerusalemu walipomwendea Yesu wakisema, 

2 Mbona wanafunzi wako huyahalifu mapokeo ya wazee, kwa maana hawanawi mikono walapo chakula. 

3 Akajibu, akawaambia, Mbona ninyi nanyi huihalifu amri ya Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu? 

4 Kwa kuwa Mungu alisema, Mheshimu baba yako na mama yako, na Amtukanaye baba yake au mama yake kufa na afe. 

5 Bali ninyi husema, Atakayemwambia babaye au mamaye, Cho chote kikupasacho kusaidiwa na mimi ni wakfu, 

6 basi asimheshimu baba yake au mama yake. Mkalitangua neno la Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu”.

Marko 7:8-13 

“8 Ninyi mwaiacha amri ya Mungu, na kuyashika mapokeo ya wanadamu. 

9 Akawaambia, Vema! Mwaikataa amri ya Mungu mpate kuyashika mapokeo yenu. 

10 Maana Musa alisema, Waheshimu baba yako na mama yako, na, Amtukanaye babaye au mamaye kufa na afe. 

11 Bali ninyi husema, Mtu akimwambia babaye au mamaye, NI KORBANI, yaani, wakfu, kitu changu cho chote kikupasacho kufaidiwa nacho, huwa basi; 

12 wala hammruhusu baada ya hayo kumtendea neno babaye au mamaye; 

13 huku mkilitangua neno la Mungu kwa mapokeo yenu mliyopokeana; tena mwafanya mambo mengi yaliyo sawasawa na hayo.

Kama tunavyosoma hapo, biblia imeshatoa tafsiri ya hilo Neno Korbani mbele  kidogo kuwa linaamanisha WAKFU.

Kitu chochote kilichowekwa wakfu ina maana kuwa hakitumiwi kwa mtumizi mengine yoyote isipokuwa kwa Mungu tu. Sasa katika habari hiyo, utaona Bwana Yesu alikuwa anawelenga sana sana Mafarisayo na waandishi kwa unafki wao kwa kujifanya kuwa wanaishika torati yote, wakati yapo mambo mengine mengi ya torati walikuwa wanayakaidi.

Na ndio hapo Bwana Yesu akawatolea mfano mmojawapo, ambao ulihusu  kuwaheshimu wazazi, kama mojawapo ya amri ambazo Mungu alizitoa zishikwe na watu wote. Na biblia iliposema kuwaheshimu wazazi, ilikuwa sio tu kuwaonyeshea heshima na utiifu, hapana ilikuwa ni zaidi ya hapo ikiwemo kuwahudumia kifedha, hususani wakiwa wazee.

Sasa hawa waandishi walikuwa wanayapindisha hayo maagizo, kwa kuwashurutisha watu, kuepuka majukumu yao ya kuwahudumia wazazi wao, kinyume chake walikuwa wanawaambia hayo wanayoyapata kwa ajili ya wazazi  wanaweza tu kuyafanya kuwa wakfu(Korbani) mbele za Mungu,  na ikawa ni sawa tu na kama wamewahudumia wazazi wao, isiwe dhambi mbele za Mungu.

Hivyo kama mtu alikuwa ametenga fedha yake kiasi kwa ajili ya matumizi ya baba yake au mama yake kule kijijini, basi walihimiziwa walizete Hekaluni kwa ajili ya Mungu kama wakfu..

Na mzazi akimuuliza, mbona huniletei matumizi, basi Yule kijana atasema, fedha hii au nafaka hii  niliyoivuna ni wakfu kwa Mungu.

Hivyo watu wengi wakawa wanawaacha wazazi wao katika hali ya shida na umaskini wa hali ya juu. Jambo ambalo Mungu hakuliagiza.

Ndipo Yesu anawakemea hawa waandishi kwa kuyapindua maagizo ya Mungu, ya kutotimiza majukumu yao ya kuwahudumia wazazi  kwa kanuni zao walizojitungia.

Nini tunajifunza?

Kumbuka biblia haifundishi watu wakimbie majukumu yao ya kifamilia kwa wazazi wao hususani pale wanapokuwa wazee kwa kisingizio kuwa wanamtolea Mungu.. Biblia inasema usipowahudumia watu wa nyumbani kwako, wewe ni kuliko hata mtu asiyeamini(1Timotheo 5:8).. Lakini pia biblia haifundishi kuwa watu waache kumtolea Mungu kwa kisingizio kuwa wanayo majukumu mengi ya kifamilia.

Lazima ujue kila utoaji una sehemu yake, na Baraka zake. Watu wa nyumbani kwako wana sehemu yao, maskini wana sehemu yao, na Mungu pia anayosehemu yake..Usipojua hilo utakuwa nawe pia unatangua torati kwa kufuata mawazo yako mwenyewe uliyojitungia. Kwasababu wapo watu wengi leo hii, wameacha kupeleka fedha zao kanisani, au kwenye huduma za Mungu, wanasema sitoi sadaka yangu, na ukiwauliza ni kwanini?, wanasema mbona hatuoni zikienda kuwahudumia maskini na wajane kama ilivyokuwa katika kanisa la kwanza la mitume…Lakini mtu huyo huyo hajui kuwa watakatifu wa kanisa la kwanza sio kama hawa wa sasahivi, wale walikuwa wapo tayari kuuza mashamba yao na viwanja vyao na kuleta kwa Mungu, hivyo kwa namna ya kawaida nishati ya kutosha ni lazima iwepo nyumbani kwa Mungu hata kuwahudumia mpaka wajane.

Lakini kama wewe unampelekea Mungu shilingi, wakati hiyo fedha hata gharama za umeme kanisani hazijitoshelezi, unapata wapi ujasiri wa kutaka kujua mfuko wa kanisa unatumikaje?? Fikiria tu. Je wewe unaweza kuuza shamba lako kule kijijini, umletee Mungu?

Bwana atusaidie,. 

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

Je! Mwanamke anapaswa afunikwe kichwa anapokuwa ibadani?

WANA JUHUDI KWA AJILI YA MUNGU, LAKINI SI KATIKA MAARIFA.

MIJI YA MAKIMBILIO.

JE KUVAA PETE NI DHAMBI?

MAJONZI YA MTUME PAULO KWA NDUGU ZAKE.

YOTE NAMTOLEA YESU_Tenzi za Rohoni.

 Je kualikwa kwenye sherehe za watu ambao si wakristo ni dhambi?

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/08/17/neno-korbani-linamaanisha-nini-marko-711/