JE! UNAIONA ILE NCHI NZURI YA KUMETA-META MBELE YAKO?

by Admin | 24 June 2021 08:46 am06

Tofauti na makabila mengine 11 ambayo Yakobo aliyabariki kama tunavyosoma katika kitabu cha Mwanzo ile sura ya 49. Kabila la Isakari ndio kabila, lililokubali utumishi, tena sio utumishi tu ilimradi utumishi bali utumishi kama wa Punda kwa watu wa Mungu. Unaweza kusema wana wa Isakari walikuwa wajinga, kuongozwa na roho ya punda kama wasemavyo watu sasa hivi. Lakini maandiko yanatuambia, walifanya hivyo kwasababu waliona ni nini kipo mbele yao. Waliona nchi nzuri ya utukufu ikiwangojea, waliona mahali pa mapumziko ya milele pako mbele yao panawasubiri, na hivyo ili kufikia nchi hiyo ni sharti leo hii watumike sana. Soma..

Mwanzo 49:14 “Isakari ni punda hodari, Ajilazaye kati ya mazizi ya kondoo;

15 Akaona mahali pa raha, kuwa pema, Na nchi, ya kuwa ni nzuri, Akainama bega lake lichukue mizigo, Akawa mtumishi kwa kazi ngumu”.

Unaona, alikubali kujishusha, ili awe mtumishi wa kazi ngumu. Kama vile Punda moja anayebeba chakula cha kondoo wengi zizini. Ndivyo alivyojiona kwa wengine.  Na matokeo yake biblia inatuambia, wana wa Isakari walikuja kuwa wenye akili nyingi za kujua majira ya nyakati Zaidi ya wote. Ndio waliokuwa wanategemewa na Israeli nzima, kutoa taarifa juu ya nyakati za neema na hukumu zilizoamriwa na Mungu. Akili hizo na hekima hizo walipewa na Mungu mwenyewe.

1Nyakati 12:32 “Na wa wana wa Isakari, watu wenye akili za kujua nyakati, kuyajua yawapasayo Israeli wayatende; vichwa vyao walikuwa watu mia mbili na ndugu zao wote walikuwa chini ya amri yao”.

Je! Na sisi tunaweza kufananishwa na wana wa Isakari? Unajua ni kwanini leo watu hatutaki kumtumikia Mungu, ni kwasababu hatuoni yaliyo mbele yetu, tunaona ya hapa hapa tu, hatuona majira ya neema yanayokuja huko mbeleni, hatuioni Yerusalemu mpya na nchi mpya tuliyoahidiwa na Mungu. Hatuoni Karamu ya mwanakondoo ambayo Yesu alikwenda kutuandalia kwa miaka 2000 sasa ipo karibuni kuanza. Na ndio maana hatutaki leo hii kujitia katika utumishi wa Mungu. Tunachojua ni kujitia katika utumishi wa kusumbukia maisha, tupate magari, tupate majumba, mashamba, tuwe mabilionea., hayo tu, Mambo ambayo fahari yake inaishia hapa hapa duniani.

Hata kuhudhuria ibada tunaona ni mzigo mzito, lakini tupo radhi kufanya kazi siku 365 bila kuchoka, usiku na mchana, tupo radhi kutazama Tv kila siku, lakini kusoma aya moja ya biblia na kuitafakari ni mtihani kwetu..Kama hayo yakitushinda tutawezaje, kuwa watumishi wa Mungu?

Wana wa Isakari waliitambua ile kauli ya Bwana Yesu kabla hata ya yeye mwenyewe kuja..kwamba ukubwa katika ufalme wa mbinguni, sio kuwa na sifa, na ujuzi, na vyeo, na kutumikiwa, hapa duniani, bali ni katika utumishi kwa wengine.. ndio maana wao wakaamua kuwa vile.

Mathayo 20:25 “Lakini Yesu akawaita, akasema, Mwajua ya kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha.

26 Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu;

27 na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu;”

Je! Na sisi tunaiona sawasawa hiyo nchi nzuri na ya kumeta meta kule ng’ambo? Kama ndivyo basi tuwe radhi kuwa Punda kwa kondoo wa Mungu, kama ilivyokuwa kwa wana wa Isakari. Tukubali kumtumikia Mungu,bila kutafuta faida zetu wenyewe. Tukubali kuwatanguliza wengine, na sio sisi tu wenyewe na matumbo yetu, kila siku. Ili siku ile Kristo akaketi  pamoja na sisi katika kiti chake cha enzi mbinguni.

Kumbuka hizi ni siku za kumalizia, wakati tuliobakiwa nao ni mfupi sana,Injili tuliyonayo sio ya kuliliwa liliwa tena uokoke. Kwasababu muda wake umeshaisha, tumebakiwa na injili ya Ushuhuda tu. Ili siku ile watu wasije wakasema hawakuhubiriwa injili. Embu jiulize wewe ambaye upo kwenye mawazo mawili mawili, ni ujasiri gani unapata kuishi maisha ya namna hiyo?

Unyakuo ukipita leo hii usiku na ukaachwa utamweleza nini Kristo? Au kifo kikikuta ghafla, huko unapokwenda utakuwa mgeni wa nani? Kuzimu ipo na haishi watu kama maandiko yanavyosema. Na ibilisi anataka uendelee katika hali hiyo hiyo, ili mabaya yakukute kwa ghafla, kama yalivyowakuta wenye dhambi wote waliotangulia kuzimu.

Tubu dhambi zako, na Zaidi sana ukawe mtumishi wa Mungu, ufanye kusudi lake hapa duniani. Kwasababu hilo ndilo uliloitiwa.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

WAENDEE WANA WA ISAKARI, UWE SALAMA.

UFUNUO: Mlango wa 17

NI VIZURI SISI KUWAPO HAPA.

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 1

ZIFAHAMU KAZI TATU ZA ROHO MTAKATIFU KATIKA ULIMWENGU.

Wibari ni nani?(Mithali 30:26)

Rudi nyumbani

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2021/06/24/je-unaiona-ile-nchi-nzuri-ya-kumeta-meta-mbele-yako/