MTUMWA SI MKUU KULIKO BWANA WAKE.

by Admin | 6 January 2020 08:46 am01

Jina la Mwokozi wetu Yesu Kristo libarikiwe.


Yohana 13:13 ‘Ninyi mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo.

14 Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi.

15 Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo.

16 Amin, amin, nawaambia ninyi, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka.

17 Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda’.

Bwana Yesu alisema..Mtu akitaka kuwa mkubwa kuliko wote ni sharti awe mtumishi wa wote..

Mathayo 20: 26 “Lakini haitakuwa hivyo kwenu; bali mtu ye yote anayetaka kuwa mkubwa kwenu, na awe mtumishi wenu;

27 na mtu ye yote anayetaka kuwa wa kwanza kwenu na awe mtumwa wenu;

28 kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi”.

Maana yake ni kwamba mbele za Mungu..yule anayewatumikia wengine huyo ndio mkubwa kuliko wote anaowatumikia mbele za Mungu…Na thawabu yake mbinguni ni kubwa kuliko wote…

Wengi wetu huwa hatupendi kusikika hivyo…lakini huo ndio utaratibu Mungu aliouweka…sisi wanadamu, aliye mtumishi wetu ndiye mdogo kuliko wote.

Na Yesu Kristo Bwana wetu kuonyesha kielelezo yeye alikuwa mdogo kuliko wote…hata kufikia hatua ya kutoka kwenye kiti na kuwakalisha wanafunzi wake, na yeye ambaye asili yake ni mbinguni alishuka chini, akashika miguu ya wanafunzi 12 kwa usiku mmoja…Jumla ya miguu 24, yenye mavumbi na isiyovutia ya wavuvi..aliishika na kuiosha, na kuifuta kwa kitambaa…Huyo ni Mkuu wa Uzima ambaye sisi leo tunamwita Bwana. Kashika miguu ya watu waliomkana na kumsaliti. Inatupasaje mimi na wewe?.

Ndugu siku zote Mungu anajifunua katika udogo sana mambo yaliyodharaulika katika ulimwengu huu Mungu ndiyo anayoyaangalia…Wengi wetu leo hii ni ngumu hata kuwapa mikono wakristo wenzetu, tutawezaje kuwaosha miguu?. Nimewahi kumsikia Mtu anasema… “kuoshana miguu kwa sasa hakupo”..Pale Bwana alikuwa anaonyesha mfano tu!!.

Tutaficha wapi nyuso zetu, siku ile tutakapokutana na Bwana uso kwa uso?…Yeye mkuu wa Uzima aliosha miguu watumwa wake sisi hatujawahi hata siku moja?..Si atatuambia tutoke mbele zake?. Maana anasema ….

“14 Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi.

15 Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo.

16 Amin, amin, nawaambia ninyi, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka. ”

Mtumwa si mkuu kuliko Bwana wake, sasa wewe ni mkuu kuliko Yesu?..Tukikataa kuoshana miguu maana yake wewe ni mkuu kuliko Yesu, agizo hili ni la msingi na la lazima kwa kila mwamini, haijalishi ni mchungaji, nabii, mwalimu, askofu, mtume au mtu yoyote yule… Hakuna urembo wala utanashati katika kunyenyekeana…Na siku ile wengi watatupwa nje kwa kukosa tu hichi kitu…Kwasababu mbinguni hataingia yoyote ambaye anajiona ni mkuu kuliko Yesu. Na anasema “yeyote ajikwezaye atashushwa, naye ajishushaye atakwezwa.”

Hivyo ndugu kama ulikuwa huna desturi hiyo tunazidi kukumbushana..anza leo, kama mahali unapoabudu hawafanyi hivyo…mwulize mchungaji wako kwanini hafanyi hivyo?…Mwulize pia kama na yeye anafanya hivyo?. Kama hafanyi hivyo basi fahamu kuwa “mchungaji wako kajiweka kuwa mkuu kuliko Bwana wako Yesu”…Sasa utapenda kukaa mahali ambapo Bwana wako Yesu Kristo anashika nafasi ya pili?.

Tendo la kuoshana miguu ,licha ya kumtii tu Kristo lakini pia linafaida kubwa sana kiroho..kama ulikuwa hupatani na watu kitendo cha kujishusha na kuosha miguu ya mwamini mwenzako, roho Fulani ya maelewano na ya mapatano inakuvaa…na roho zote za magomvi na kutokuelewana zinakuondoka..kwa kufanya tu hicho kitendo cha kuoshana miguu..(Maroho ya Adui yanakukimbia kwa hicho kitendo tu..watu wengi hawajui hilo).

Kuna siri kubwa sana katika kuoshana miguu, hivyo hakikisha mahali unapokusanyika jambo hilo linafanyika…Miguu yako inapooshwa na mwamini mwenzako, na yeye anapoosha ya kwako..Kuna Neema Fulani kubwa sana ya kiroho inaachiliwa …

Neema ya umoja na ushirikiano..Sio tu kanisani, lakini hata mnapokusanyika wawili au watatu, mnaweza kufanya tendo hilo.

Sasa shetani analijua hilo, na hataki watu wafanye hivyo…au anataka watu wafanye isivyopaswa ili aharibu mambo juu ya maisha ya huyo mtu…Na moja ya njia shetani anayoitumia isiyofaa ni…kuoshana miguu kwa jinsia mbili tofauti…(Miguu inapaswa waoshane wanaume kwa wanaume katika kanisa na wanawake kwa wanawake..na sio kuchanganya)

Vivyo hivyo njia nyingine shetani anayoitumia kuharibu tendo la kuoshana miguu ni “wanawake kuoshwa miguu kwenye saluni za kike”..Wanawake wengi wanaoshwa miguu na wanaume katika masaluni na katika vibaraza…Kuna hatari kubwa sana ya kiroho kufanya hivyo (Tutakuja kuona madhara ya kufanya kitu hicho siku ya kesho kutwa Bwana akitupa Neema).

Lakini zidi kukumbuka Neno hili “Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka”..Jishushe na Bwana atakukweza kwa wakati wake.

Maran atha.

Mada Nyinginezo:

MEZA YA BWANA, NA KUTAWADHANA MIGUU.

JISHUSHE ILI MUNGU AKUHUDUMIE.

HERI YULE ATAKAYEKULA MKATE KATIKA UFALME WA MUNGU.

TUMTOLEE MUNGU VILE VINAVYOTUGHARIMU ZAIDI.

URIMU NA THUMIMU NI NINI KATIKA BIBLIA?

ALIKUWAKO NAYE HAYUKO, NAYE YU TAYARI KUPANDA KUTOKA KUZIMU.

MZEITUNI HALISI UTAKAPOPACHIKWA.

WATAMTAZAMA YEYE AMBAYE WALIMCHOMA; NAO WATAMWOMBOLEZEA.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/01/06/mtumwa-si-mkuu-kuliko-bwana-wake/