UUMBAJI BORA WA MUNGU, UPO NDANI YA MWANADAMU.

by Admin | 25 May 2020 08:46 pm05

Habari ya uumbaji ina mafunzo mengi sana. Biblia inatuambia Mungu alimuumba mwanamume na mwanamke kwa mfano wake(Mwanzo 1:27). Lakini katika siku sita za uumbaji, Tunaona kulikuwa na uumbaji mmoja muhimu ulikosekana., Embu tengeneza picha mpaka Mungu anastarehe siku ya saba, mwanamke hakuwepo,..Ni kama vile Mungu alijifanya amemsahau hivi..Lakini kulikuwa na sababu kubwa mno ya yeye kufanya hivyo.

Alimwacha Adamu awepo peke yake duniani kwa kipindi fulani kirefu, aone uumbaji wake wote, aushangae huo, aseme ama kweli Mungu ameumba..kila kitu kweli ni kizuri, tazama jua, tazama, nyota, tazama twiga, tazama nyangumi, tazama hiki tazama kile, vyote ni vikamilifu, vimejitosheleza kweli kweli, sihitaji kingine…

Lakini hakujua kuwa Mungu alikuwa hajaukamilisha uumbaji wake bado (hiyo siri alikuwa nayo mwenyewe), ameihifadhi mpaka wakati mtimilifu utakapofika.

Sasa baada ya Mungu kumuacha Adamu kwa kipindi chote hicho kirefu, pengine miezi, miaka inapita aendelee kufikiria hivyo hivyo kuwa kila kitu ndio tayari, mpango wote umekamilika, Mungu kamaliza uumbaji wake, , shughuli zinaendelea kama kawaida bustanini.. Lakini wakati ulipofika wa Mungu kuikamilisha kazi yake alishuka bustanini tena kama muumbaji yule yule wa zamani..

Tungeweza kudhani labda angeshuka ardhini amtoe mwanadamu mwingine kwenye udongo mwekundu, lakini mambo yalikuwa ni tofuati, alimkabili Adamu moja kwa moja..Na mara moja Akamletea usingizi mzito sana. Wakati Adamu akiwa ndotoni, mkono wa Mungu ulianza kupita sehemu ya ubavu wake, pengine mfano wa kisu kikali(hatujui), tunachojua ni kuwa aliundoa ubavu wake mmoja, jaribu kutengeneza picha operasheni iliyokuwa inafanyika pale ni ya namna gani..Si ajabu hata Mungu alimletea usingizi mzito..

Hatushangai hata madaktari wa leo wameiga mbinu hiyo ya Mungu ya kufanya operasheni, yaani kumpiga kwanza mtu nusu-kaputi ili apotelee usingizini kabla ya kumfanyia matibabu makubwa..Wanafanya hivyo Si kwamba hawapendi mtu aone operasheni ile hapana, kwanza ni ili kuepuka usumbufu, chukulia mfano ikiwa mtu yule ataona tumbo linakatwa na utumbo unatolewa nje au anaona kichwa chake kinapasuliwa, anaweza asikubali, au akaogopa kupitiliza na mwisho wa siku akasababisha operesheni isiende vizuri au hata kifo kabisa..Na ndivyo ilivyokuwa kwa Mungu..Alikuwa anamfanyia Adamu operasheni yenye umakini sana, ya kuumba kitu bora kuliko vyote alivyovifanya ndani ya siku zile 6.. Hivyo ikamgharimu atafute njia itakayomfanya awe na utulivu, na ndio akatumia njia ya usingizi mzito, kwasababu kinachokwenda kuumbwa ni bora sana.

Sasa Mungu alipomaliza kuutoa ubavu wake mmoja, akarudishia nyama eneo lile, ndipo akauchukua ule ubavu akamuumbia Hawa. Na kazi ilipomalizika, bwana Adamu akazinduka usingizini, kujitazama anajiona kama vile mwili umepungua, na kuangalia pembeni anamwona mgeni, ambaye si wa pale bustanini. Na kumtazama vizuri anaona hafanani na swala, hafanani ni mbuzi bali anafanana na yeye, anazungumza kama yeye, anaumbile linalokaribia kufanana na la kwake.. Hapo ndipo alipogundua kuwa ni ile sehemu ya mwili wake ameumbwa yule mtu.

Na Adamu alipomwangalia tena hakuona wa kulinganishwa naye katikati ya uumbaji wote ambao Mungu alishawahi kufanya.

Sasa Ni jambo gani Mungu alikuwa anamwonyesha Adamu?

Alikuwa anamwonyesha kuwa uumbaji wake bora unatoka ndani ya mtu, na si penginepo.. Hakuna mwanaume asiyejua katika uumbaji wote wa Mungu hakuna hata kimoja kinachoweza kufananishwa na mwanamke.

Vivyo hivyo somo hilo Mungu hakumfundisha Adamu tu peke yake,..Bali na Hawa pia, pale alipomwekea uwezo wa kubeba mimba, ambapo aliruhusu kiumbe kikae ndani ya tumbo lake kwa miezi 9, lakini baada ya ya hapo, ghafla anatokea tena mwanamume..

Na vivyo hivyo hakuna mwanamke asiyejua kuwa katika uumbaji wote wa Mungu, hakuna kilichoumbwa bora kama mwanamume…Lakini mwanamume huyo anatoka katika tumbo lake na sio mbinguni au ardhini tena. Na kwa kupitia mzunguko huo huo duni leo imejaa watu.

Mambo hayo hayo yanaendelea rohoni hata sasa, Uumbaji mkamilifu wa Mungu unatimia ndani ya Maisha ya wanadamu..ikiwa tu tutamruhusu aifanye kazi yake mwenyewe ndani yetu bila kusumbuliwa..Mungu anataka kufanya makubwa kupitia sisi, kuliko angefanya yeye mwenyewe. Lakini ni sisi hatuwi watulivu kufanyiwa operasheni.

Tunashindana na Mungu, kwa mambo mengi maovu,anapotuambia tuache Maisha ya dhambi, hatuwi tayari kufanya hivyo, tunapoambiwa tusivae nguo zisizompa Mungu utukufu hatuwi tayari, tunapoambiwa tuombe, hatutaki, tunapoambiwa tuikimbie zinaa sisi tunairidhia, biblia inapotuonya tuache hiki au kile hatutaki kutii, tunachosema ni Mungu haangalii mwili anaangalia mavazi, tunapoambiwa tujitenge na mambo ya ulimwengu, tunamwona kama anatunyima uhuru wetu, kila siku tunashindana na mkono wake.. na wakati huo huo tunataka Mungu aumbe mambo makubwa maishani mwetu..Ataumbaje katika hali hiyo ya masumbufu?

Mungu anahitaji utulivu wa roho, tukiukosa huo tusitazamie uumbaji wowote. Tusitazamie Mungu kufanya miujiza maishani mwetu. Ikiwa wewe ni mwenye dhambi, huu ni wakati wako sasa wa kumrudia Mungu, Anza kujenga uhusiano wako vizuri na Mungu, ndipo Mungu naye achukue nafasi ya kuumba mambo mazuri ndani yako.

Tubu dhambi kwa kumaanisha kuziacha, na pia nenda kabatizwe kulingana na matendo 2:38, na Bwana atakupa kipawa cha Roho wake mtakatifu atakayekuongoza na kukutia katika kweli yote na kukupa utulivu wa roho.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

JE! MTUMISHI KUTOKUWA NA FEDHA NI ISHARA KUWA KUNA TATIZO KATIKA IMANI YAKE?

JE KUPONYWA NI UTHIBITISHO WA MUNGU KUWA NA WEWE?

KWANINI DAUDI ALIKUWA NI MTU ALIYEUPENDEZA MOYO WA MUNGU?

MJUMBE WA AGANO.

Je! Ule mwiba uliokuwa katika mwili wa Paulo ulikuwa ni nini?

MAHALI UNAPOPASWA USIMVUMILIE SHETANI HATA KIDOGO.

KUWA WEWE.

Rudi Nyumbani:

DOWNLOAD PDF
WhatsApp

Source URL: https://wingulamashahidi.org/2020/05/25/uumbaji-bora-wa-mungu-upo-ndani-ya-mwanadamu/