Monthly Archive 3 July 2026

Kauli ya Bwana ya “Heri kutoa kuliko kupokea” tunaisoma wapi?

Swali: Katika Matendo 20:15, tunasoma Mtume Paulo akirejea kauli ya Bwana kwamba akisema “Heri kutoa kuliko kupokea”.. Je ni wapi katika Injili nne, Bwana YESU alisema maneno hayo?

Jibu: Tuanzie kusoma ule mstari wa 33..

Matendo 20:33 “Sikutamani fedha wala dhahabu, wala mavazi ya mtu.

34 Ninyi wenyewe mnajua ya kuwa mikono yangu hii imetumika kwa mahitaji yangu na ya wale waliokuwa pamoja nami.

35 Katika mambo yote nimewaonyesha ya kuwa kwa kushika kazi hivi imewapasa kuwasaidia wanyonge, NA KUYAKUMBUKA MANENO YA BWANA YESU, JINSI ALIVYOSEMA MWENYEWE, NI HERI KUTOA KULIKO KUPOKEA”.

Katika vitabu vyote vinne vya injili (yaani kitabu cha Mathayo, Marko, Luka na Yohana) hakuna mahali popote pameandikwa  maneno hayo ya Bwana kama yalivyo kwamba “heri kutoa kuliko kupokea”. Lakini ni wazi kuwa aliyasema mahali fulani ila hayakuandikwa katika vitabu vinne vya injili.

Tunalithibitisha vipi hilo?.. Turejee kitabu cha Yohana 21:24..

Yohana 21:24 “Kuna na mambo mengi aliyoyafanya Yesu; ambayo yakiandikwa moja moja, nadhani hata ulimwengu usingetosha kwa vile vitabu vitakavyoandikwa”.

Hapa Mtume Yohana anasema, yapo mambo mengi aliyoyafanya Bwana YESU ambayo hayakuandikwa katika vitabu hivyo..maana yake yapo maneno mengi aliyoyafundisha na mifano mingi na ishara nyingi alizozifanya ambazo laiti kama zingeandikwa moja baada ya nyingine, dunia isingetoshea kwa vitabu..

Kwa mantiki hiyo basi tunaanza kuelewa kuwa maneno hayo ya “heri kutoa kuliko kupokea” ni kweli Bwana YESU aliwahi kuyasema mahali fulani, isipokuwa tu hayakunukuliwa na waandishi wa vitabu vinne vya injili.

Lakini pamoja na hayo, yapo maneno aliyoyasema yenye mlengo huo huo wa “uheri wa kutoa kuliko kupokea”

Luka 6:38 “Wapeni watu vitu, nanyi mtapewa; kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na kusukwa-sukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa”.

Hii ni kauli ya Bwana YESU akitufundisha faida za kuwapa watu vitu, kwani tunapotoa ndivyo tutakavyopokea, na si tupokee kwanza na ndipo tutoe.. hiyo ikithibitisha kuwa ni kweli Bwana alifundisha uheri wa kutoa kuliko kupokea, na pia alituonya tujilinde na “uchoyo”.

Luka 12:15  “Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo”.

Je umempokea YESU?.. Je una uhakika akirudi leo utakwenda naye?

Kama bado tengeneza maisha yako kwani majira tunayoishi ni ya hatari na parapanda ya mwisho imekaribia sana kulia.

Bwana atusaidie.

 

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

MAISHA YA IMANI NI KAMA SIFA YA MTI.

Mti una sifa moja, hautembei kutoka sehemu moja Kwenda nyingine, Utaupanda eneo fulani, utaridhika kubakia hapo hapo, haijalishi ni pabaya kiasi gani, utaenda utarudi miaka na miaka utaukuta pale pale, tofauti na viumbe hai vingine, ambavyo vyenyewe, vikiona hali si nzuri ya mahali, huama na Kwenda kutafuta makazi pengine. Lakini Mti hauna sifa hiyo, na bado utaendelea kustawi na kuwepo kwa miaka mingi zaidi ya viumbe hai vingine,  haijalishi ni kipindi gani kitapita.

Siri ya mti ipo wapi?

Jibu ni kwenye mizizi yake. Ijapokuwa hautembei kwa juu, lakini chini unatembea. Kwa juu utauna upo pale pale, lakini kwa chini mizizi yake ina mwendo, kila siku inaendelea katika safari ya huku na huko kutafutia virutubisho na maji.

Ni nini Bwana anatufundisha katika maisha ya mti.

Yeye hutupanda apendako.

Leo hii ni rahisi kulalamika, kwanini nimezaliwa hili taifa, kwanini hili kabila, kwanini hii familia, kwanini hii jinsia, kama ningezaliwa kwenye nchi ile, kabila lile, familia ile yenye Uchumi mkubwa ningekuwa mbali sana, ningestawi vizuri sana, ningeimarika kiroho kwa kasi kubwa mno… Kama umekuwa na Mawazo hayo, basi kuna tatizo la kiufahamu.

Mafanikio ya mwanadamu hayapo katika mazingira yake sasa. Mafanikio yake yapo katika mizizi yake rohoni. Mti ukikosa mizizi, hata uwe kwenye udongo mzuri kiasi gani hauwezi kukua popote.

Kama mwamini fahamu mzizi uliyopewa inauwezo wa kukustawisha popote, isipokuwa sifa yake ni ile ile yaani huwa haionekani kwa juu, hukaa matopeni, na huzidi Kwenda chini kila siku sio kurudi juu. Vivyo hivyo na sisi tujue nguvu yetu ipo rohoni, (pasipoonekana), Na katika unyenyekevu kwa Mungu wetu kila siku, ndivyo tutakavyoleta ustawi mema wa maisha yetu.

Kunyenyekea kiroho ni mjumuiko wa mambo : kumkubali Kristo, kutii maagizo yake (ikiwemo maombi, ushirika), kuliishi Neno, na kumtumikia yeye.

Huko ndiko kurefusha mizizi.

2 Wafalme 19:30

[30]Na mabaki yaliyookoka ya nyumba ya Yuda yatatia mizizi chini, na kuzaa matunda juu. 

Kristo alipaswa aishi Yerusalemu, mji  wenye sifa za kiroho na kisomi, lakini alipelekwa Nazareti , mji mnyonge, lakini huko huko alimzalia Mungu matunda, kwasababu mizizi yake ilienea sana.

Yusufu aliuuzwa utumwani, akawa msikwao, asiye na makazi kule Misri, lakini aliendea kuiimarisha mizizi yake, ijapokuwa kwa nje, hakukuonekana dalili ya badiliko lolote, lakini hatimaye, Mungu akamwinua akawa, mkuu kule kule Misri, Ndivyo ilivyokuwa kwa Danieli, Ayubu na watumishi wa Mungu.

Kabla ya kulalamikia mazingira, jiuliza kwanza je! Mizizi yangu, ipo sawa? Kwasababu haiwezekani mizizi ikawa sawa, mti ukafa. Haiwezekani ukawa mtakatifu halafu ukamezwa na mazingira.

Imarisha kiroho chako.

Shalom.

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Print this post