Bwana Yesu mara nyingi alipokuwa akiwafundisha makutano, hakuzungumza nao moja kwa moja, kwa kufafanua mambo, bali kama kwa njia ya mafumbo, hivyo wengi walikuwa wakitoka na maswali mengi kichwani, au wengine hawakumuelewa kabisa, na wengine walimwona kama vile mtunga hadhithi tu zisizo na maana, lakini alifanya hivyo kwa makusudi ili ajue ni wangapi walio tayari kujifunza , na ndio maana tunaona baada ya kumaliza ile mifano ni kikundi cha watu wachache tu(wanafunzi wake) kati ya maelfu kilichoenda kumuuliza tafsiri ya ile mifano yote aliyokuwa anazungumza,
Na ndipo hapo anapowafunua macho yao na kuwaelewesha tafsiri ya mifano ile na kuponyeka roho zao, bali wale wengine waliosalia ambao hawakutaka kujifunza zaidi kwao ilikuwa ni kama hadhithi tu. Na mahali popote Bwana alipokuwa akifundisha kwenye makutano mengi hiyo ndiyo ilikuwa desturi yake. Na ndivyo anavyofanya hata sasa.