Nzige, Parare, madumadu na tunutu ni wadudu gani? (Yoeli 2:25)?

Nzige, Parare, madumadu na tunutu ni wadudu gani? (Yoeli 2:25)?

Swali: Hawa wadudu, tunaowasoma katika Yoeli 2:25  (Nzige,Parare, madumadu na tunutu) ni wadudu gani na wanabeba ujumbe gani kiroho?

Tusome,

Yoeli 2:25 “Nami nitawarudishia hiyo miaka iliyoliwa na NZIGE, NA PARARE, NA MADUMADU, NA TUNUTU, jeshi langu kubwa nililotuma kati yenu”.

Hizi ni jamii za wadudu waharibifu wanaokula mazao hususani ya nafaka!.(Tazama picha juu)

1. NZIGE.

Hii ni jamii ya Panzi, ambayo ndio jamii kubwa kimaumbile kuliko jamii zote za panzi, Nzige wanasifa ya kutembea kimakundi na wanahama kutoka ukanda mmoja kwenda mwingine, na wanapotua mahali wanaharibu mazao ndani ya muda mfupi sana. Sifa ya nzige ni kwamba hawana kiongozi kama walivyo wadudu wengine kama Nyuki au Mchwa. (Soma Mithali 30:27).

Mfano wa hao Nzige ni wale Wamisri walioletewa na Mungu, ambapo walitua na kula kila mmea uliopo juu ya uso wa nchi yote ya Misri kasome (Kutoka 10:12-15), Na pia jamii ya mfano wa Nzige ni wale waliotua katika sehemu ya ukanda wa Afrika mashariki, wajulikanao kama Nzige wa Jangwani.

Lakini Nzige wanatabia ya kula Matawi ya Nafaka na kubakisha mapengo mapengo na kisha kuondoka.

2. PARARE.

Parare ni jamii nyingine ya Panzi, ambayo yenyewe inakula sehemu zile Nzige (walizobakisha/walizosaza). Parare kimaumbile ni wadogo kuliko Nzige, na kimwonekano wanayo miiba katika Miguu.. Parare si waharibifu kama Nzige, ingawa kwa nafaka ambazo tayari zimeshaharibika basi wenyewe wanaongezea uharibifu kwa kula vile vilivyosalia.

3. MADUMADU.

Madumadu ni jamii ya Panzi wadogo, wale (wanaokaa katika Nyasi)..Hii ndio jamii ya panzi wadogo kuliko wote, na sifa yao kubwa ni kula sehemu za majani zilizo ndogo sana, ambazo Nzige wala Parare hawawezi kula.

4. TUNUTU.

Tunutu ni vimelea vidogo kabisa vya wadudu, ambavyo vipo kama minyoo. Wadudu wengi warukao kabla ya kufikia hatua ya kukomaa huwa wanapitia hii hatua, ambapo wanakuwa kama viminyoo vidogo ambayo huwa vinakula mabua au sehemu ya majani ambayo Nzige, Parare, au Madumadu hawawezi kula. (Tazama picha chini)

Sasa tukirudi katika hiyo Yoeli 2 kwanini Bwana awataje wadudu hao?

Ili tuelewe vizuri hebu tusome tena kuanzia mstari wa 1.

Yoeli 1:1 “Neno la Bwana lililomjia Yoeli, mwana wa Pethueli.

 2 Sikieni haya, enyi wazee; Sikilizeni, enyi wenyeji wote wa nchi. Je! Mambo haya yamekuwako katika siku zenu, Au katika siku za baba zenu? 

3 Waarifuni watoto wenu habari yake, Watoto wenu wakawaambie watoto wao, Na watoto wao wakakiambie kizazi kingine.

 4 YALIYOSAZWA NA TUNUTU YAMELIWA NA NZIGE; NA YALIYOSAZWA NA NZIGE YAMELIWA NA PARARE; NA YALIYOSAZWA NA PARARE YAMELIWA NA MADUMADU

5 Levukeni, enyi walevi, mkalie; Pigeni yowe, ninyi nyote mnywao divai; Kwa sababu ya divai mpya; Maana umekatiliwa mbali na vinywa vyenu”

Umeona hapo?.. Bwana anamwonesha Yoeli hali ya kimwili ya wana wa Israeli jinsi alivyowapiga kwa Hawa wadudu Nzige, Parare, Madumadu, na Tunutu kutokana na Makosa yao. (Ambapo janga hili lilitokea dhahiri kabisa katika Israeli kwa miaka kadhaa, wakaishiwa chakula mpaka sadaka za unga zikakoma kutolewa katika nyumba ya Mungu kutokana na upungufu wa chakula).

Sasa wadudu hawakuishia kuwa wa kimwili tu, bali waliendelea kuwa hadi wa kiroho.. Maana yake ni kwamba Bwana kawaletea Nzige katika roho, Parare katika roho, Madumadu katika roho, na Tunutu katika roho, na kuyaharibu maisha yao. Na hiyo ikasababisha maisha yao kupukutika hata vile vichache walivyobakiwa navyo pia vikapukutika kama vile madumadu wanavyokula hata vile vidogo kabisa visivyoonekana.

Maana yake ni kwamba Mungu aliyaharibu maisha yao hata hawakubakiwa na kitu.. aliwaletea mikosi, na maafa na hasara, na wakaishiwa kabisa..kwasababu walimwacha!.

Hiyo ikifunua kuwa Na sisi tukimwacha Mungu, basi atalituma jeshi hili kuyaharibu maisha yetu, Utajikuta unafanya kazi kweli unapata pesa nyingi au faida nyingi, lakini itakapoishia hutajua, utajikuta tu hujasalia na chochote, utajikuta mara hili limezuka mara lile.. Ukiona hali kama hiyo basi jua kuwa ni Mungu kalituma jeshi hilo la Nzige, parare, madumadu na tunutu katika roho kula kila kitu ulicho nacho, na hata kukufanya usibakiwe na chochote.

Hagai 1:5 “Basi sasa, Bwana wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu.

 6 Mmepanda mbegu nyingi mkavuna kidogo; mnakula lakini hamshibi; mnakunywa lakini hamkujazwa na vinywaji; mnajivika nguo lakini hapana aonaye moto; na yeye apataye mshahara apata mshahara ili kuutia katika mfuko uliotoboka-toboka.

 7 Bwana wa majeshi asema hivi, Zitafakarini njia zenu”.

Hivyo kama hujaokoka!..Fahamu kuwa maisha yako ya kimwili na kiroho kila siku yatazidi kuharibika, lakini kama leo hii ukiamua kumgeukia Mwokozi Yesu, kwa kutubu na kumaanisha kugeuka na kuacha dhambi kwa matendo, basi Bwana Yesu mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake mtakatifu na zaidi ya yote, atairejesha ile miaka yote ambayo imeliwa na Parare na Nzige, na Madumadu sawasawa na Neno lake katika Yoeli 2:25

Yoeli 2:22 “Msiogope, enyi wanyama wa kondeni; maana malisho ya jangwani yanatoa miche, na huo mti unazaa matunda yake, mtini na mzabibu inatoa nguvu zake.

 23 Furahini, basi, enyi wana wa Sayuni, mkamfurahie Bwana, Mungu wenu; kwa kuwa yeye huwapa ninyi mvua ya masika, kwa kipimo cha haki, naye huwanyeshea mvua, mvua ya masika, na mvua ya vuli, kama kwanza. 

24 Na sakafu za kupepetea zitajaa ngano, na mashinikizo yatafurika kwa divai na mafuta.

25 Nami nitawarudishia hiyo miaka iliyoliwa na NZIGE, NA PARARE, NA MADUMADU, NA TUNUTU, jeshi langu kubwa nililotuma kati yenu.

 26 Nanyi mtakula chakula tele na kushiba, na kulihimidi jina la Bwana, Mungu wenu, aliyewatendea mambo ya ajabu; na watu wangu hawatatahayari kamwe”.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

kwanini Yakobo amefananishwa na mdudu?(Isa 42:14)

Nondo ni nini kama tunavyosoma katika biblia?

Kula uzao wa tumbo lako maana yake nini? (Kumbukumbu 28:53)

Nini maana ya “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi”?

Ulafi ni nini kibiblia?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
2 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Anonymous
Anonymous
1 year ago

Nimejifunza ubarikiwe sana mtumishi

Anonymous
Anonymous
1 year ago

Somo zuri nimejifunza kitu