WENYE KUHADAA ROHO ZISIZO IMARA.

WENYE KUHADAA ROHO ZISIZO IMARA.

SWALI: Naomba kufahamu biblia inaposema wenye kuhadaa roho zisizo imara ina maana gani? (2Petro 14)

JIBU: Tusome;

2Petro 2:14 “wenye macho yajaayo uzinzi, watu wasiokoma kutenda dhambi, WENYE KUHADAA ROHO ZISIZO IMARA, wenye mioyo iliyozoezwa kutamani, wana wa laana;

15 wakiiacha njia iliyonyoka, wakapotea, wakiifuata njia ya Balaamu, mwana wa Beori, aliyependa ujira wa udhalimu;

16 lakini alikaripiwa kwa uhalifu wake mwenyewe; punda, asiyeweza kusema, akinena kwa sauti ya kibinadamu, aliuzuia wazimu wa nabii yule.

17 Hawa ni visima visivyo na maji, na mawingu yachukuliwayo na tufani, ambao weusi wa giza ni akiba waliyowekewa”.

Katika siku za mwisho biblia inatabiri kuwa litatokea kundi Fulani la watu mahususi, lenye kazi ya “kuhadaa roho za watu watu”.

Kuhadaa ni kudanganya, Lakini biblia bado haisemi kundi hili litahadaa kila mtu tu, hapana bali inasema, litahadaa watu “wenye roho zisizo imara”.

Hivyo lazima ujiulize roho zisizo imara ni zipi?

Kwa kawaida kitu kisicho imara ni kitu kisichoweza kudumu kwa muda mrefu, kisichoweza kustahimili mazingira ya mtikisiko, au mazingira magumu kwa muda mrefu kwasababu kimeundwa chini ya ubora. Kwamfano, ukinunua kiatu cha ngozi, na mwingine akanunua kile cha plastiki, mkavitembelea wote kwa pamoja, utaona baada ya muda mfupi kile cha plastiki, kinachakaa na kuisha kabisa, lakini kile cha ngozi kinaendelea kudumu, Kwasababu gani? Ni kwasababu kiatu kile cha plastiki sio imara.

Vivyo hivyo katika roho siku hizi za mwisho, Kuna wakristo walio imara, na wengine ambao sio imara, kuna wenye nguvu ya kudumu katika wokovu haijalishi ni mitikisiko mingapi inawakumba kwasababu hapo mwanzo walimaanisha kweli kweli kumfuata Kristo.. Hawa wana heri sana, ibilisi hawezi kuwahadaa.

Lakini kundi lililo hatarini ni hili  ambalo leo linaokoka kwa Bwana, kesho linarudi nyuma, leo ni moto kesho ni vuguvugu, leo linahudhuria mikesha, kesho linasahau, leo linaeleweka, kesho halieleweki, leo lipo ibadani wiki ijayo halifiki kabisa, likiwa na wapendwa linazungumza habari za Mungu, lakini likikaa na watu wa kidunia, linabadilika rangi, linafanana na wao. Lipo hapo katikati, Kudondoka kiwepesi katika dhambi ni jambo la kawaida kwao, ukiliuliza mbona umefanya hivi litakuambia nimepitiwa tu na shetani.

Sasa watu kama hawa ni lazima shetani atawahadaa tu,kwa hila zake, Na watakapodanganywa hawawezi kufahamu kwasababu wao ni roho zisizo imara. Kama Balaamu alipowahadaa wana wa Israeli, kwa kuwashawishi wazini, na mwisho wa siku Mungu akawapiga kule jangwani,  Pale Edeni Hawa alipodanganywa na nyoka hakujua  chochote, kwasababu moyo wake haukuwa imara kwa Mungu.

Ndugu kama na wewe ni mmojawapo tubu dhambi mgeukie Bwana, kisha maanisha kabisa kumfuata Yesu kwa gharama zozote, Kumbuka hizi ni nyakati za mwisho. Watu waliovuguvugu Bwana ameahidi kuwatapika, na wewe angalia usitapikwe. Au kudanganywa na ibilisi. Simama imara kwa Bwana. Kataa ukristo feki, au wa juu juu usioingia gharama.

1Wakorintho 16:13 “Kesheni, simameni imara katika Imani, fanyeni kiume, mkawe hodari”.

1Wathesalonike 3:12 “Bwana na awaongeze na kuwazidisha katika upendo, ninyi kwa ninyi, na kwa watu wote, kama vile sisi nasi tulivyo kwenu;

13 apate kuifanya imara mioyo yenu iwe bila lawama katika utakatifu mbele za Mungu, Baba yetu, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu pamoja na watakatifu wake wote”.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

KITABU CHA YUDA: SEHEMU YA 1

Nini maana ya mstari huu: (Mtu ambarikiye mwenzake kwa sauti kuu asubuhi na mapema; Itahesabiwa kuwa ni laana kwake.Mithali 27:14 )?

kwanini yule kijana aliitupa ile nguo ya kitani chini na kukimbia uchi?

Ni mlima gani Yule Mwanamke Msamaria aliokuwa anaumaanisha? (Yohana 4:19)

Ni wayahudi wa aina gani wanaotajwa kuwa sinagogi la shetani? (Ufunuo 2:9, Ufunuo 3:9)

Nini maana ya siku moja kwa Bwana ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja? (2Petro 3:8)

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments