TOFAUTI YA MITUME, MANABII, WAINJILISTI, WACHUNGAJI NA WAALIMU NI IPI?

TOFAUTI YA MITUME, MANABII, WAINJILISTI, WACHUNGAJI NA WAALIMU NI IPI?

Huduma hizi 5 tunazisoma katika kitabu cha Waefeso..

Waefeso 4:11 “Naye alitoa wengine kuwa MITUME, na wengine kuwa MANABII; na wengine kuwa WAINJILISTI na wengine kuwa WACHUNGAJI na WAALIMU”.

Na madhumuni ya Bwana Yesu kuziweka huduma hizi tano (5), kama huduma za Uongozi katika kanisa ni kama mstari wa 12, unavyosema..

Tusome tena..

Wafeso 4:11 “naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu;

12 kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata mwili wa kristo ujengwe”.

Kumbe lengo la kwanza ni “KUWAKAMILISHA WATAKATIFU”, na pili ni “KAZI YA HUDUMA ITENDEKE”, na tatu “MWILI WA KRISTO UJENGWE”.  Na sio ili Kuwaharibu watakatifu, au kujitafutia utajiri, au Umaarufu.

Mtu yeyote anayejiita mtumishi wa Mungu, kama hayo Maono matatu hayapo ndani yake, basi ni mtumishi wa shetani!

Sasa tuangalie kwa ufupi kazi za Hizi huduma tano.. Zinashirikianaje kuujenga mwili wakristo, na kuwakamilisha watakatifu.

 1. MITUME

Mitume kama jina lake lilivyo “ni watu waliotumwa”.. na kama wametumwa maana yake kuna aliyewatuma, na aliyewatuma ni lazima kawapa ujumbe.

Kwahiyo wahasisi wa Imani ya kikristo wa kwanza kabisa ni Mitume, Na mitume hao ni wale 11 pamoja na Mathiya wa 12. Hao ndio waliotumwa wa kwanza, kuitangaza Imani ya kikristo, kwa watu wote.

Lakini bado hao pekee wasingetosha kuitangaza Imani duniani kote, Hivyo Bwana Yesu alinyanyua Mitume wengine tofuati na hao 12, ambao ndani yake ndio akina Paulo na wengineo.

Hawa waliipeleka Imani ya kikristo duniani kote.

Na sio tu kulipeleka Neno la Mungu bali pia, kupanda Makanisa. Ndio maana utaona Mtume Paulo alipanda makanisa mengi sana, maeneno ya Galatia na Makedonia.

Na hata sasa Bwana anao mitume wake ambao anawatuma kuitangaza Imani ya kikristo mahali ambapo  haijasikiwa kabisa, na vile vile kupanda makanisa ya Kristo, na si makanisa yao wenyewe.

 2. MANABII

Manabii ni kundi lingine la watu ambalo Bwana anawaweka ndani ya Kanisa. Hawa kazi yao ni kulijenga kanisa kwa kutoa jumbe za Faraja na maonyo kutoka kwa Mungu moja kwa moja, na jumbe hizo ni kwaajili ya kulifariji kanisa na kulionya kwa mambo yanayoendelea au yanayokuja.

Kwamfano katika biblia, agano jipya tunamwona Nabii mmoja aliyeitwa Agabo, ambaye Bwana alikuwa anazungumza naye na kumpa jumbe za kulionya kanisa juu ya mambo yanayokuja..

Matendo 11:27 “Siku zizo hizo manabii walitelemka kutoka Yerusalemu hata Antiokia.

28 Na tulipokusanyika akasimama mmoja wao, jina lake Agabo, akaonyesha kwa uweza wa Roho Mtakatifu kwamba njaa kubwa itakuja karibu katika dunia nzima, nayo ikatukia katika siku za Klaudio.

29 Na wale wanafunzi, kila mtu kwa kadiri ya alivyofanikiwa, wakaazimu kupeleka msaada kwa ndugu zao waliokaa Uyahudi.

30 Wakafanya hivyo, wakawapelekea wazee kwa mikono ya Barnaba na Sauli”.

Umeona hapo?.. Manabii kazi yao ilikuwa ni kutoa taarifa za mambo yajayo na kuyaambia makanisa, kwa faida ya kanisa.. na kwa kujitakia umaarufu wao, wala kutaka fedha kutoka kwa watu.

Hapo taarifa za unabii huo, zilipofika kwa makanisa yote, ndipo kila mtu akajiandaa kwa akiba ya kutosha.. Huoni hapo kanisa limejengeka?..lakini leo kuna manabii ambao hawaoni mambo yanayokuja lakini wanaona mifuko na pochi za watu. Na Zaidi ya yote hawawafundishi watu utakatifu bali mafanikio tu! (hawa ndio manabii wa uongo waliotabiriwa kuja katika siku za mwisho).

Lakini Pamoja na kuwepo na jopo kubwa la manabii wa uongo, wapo pia manabii wa kweli, kwasababu Roho Mtakatifu wa kweli bado yupo duniani na anatenda kazi.

 3. WAINJILISTI.

Wainjilisti ni kundi lingine Bwana aliloliweka katika kanisa kwa lengo la kuwavuta watu katika Imani ya Kikristo, likitumia maandiko kumthibitisha Yesu Kristo ni Njia, kweli na Uzima. Vyombo hivi Bwana kaviweka maalumu kuvunja mapando ambayo yamepandwa na adui shetani ndani ya vichwa vya watu kuhusu Ukristo. Hivyo kupitia wainjilisti, watu wengi ambao, hawakuuelewa vizuri ukristo, au wamefundishwa isivyopaswa kuhusu Yesu, wanafunguka.

Mfano wa Wainjilisti katika biblia ni mtu mmoja aliyeitwa Apolo. Huyu alivunja misingi ya elimu za giza zilizokuwa zimepandwa ndani ya vichwa vya watu..

Matendo 18:23 “Hata akiisha kukaa huko siku kadha wa kadha akaondoka, akapita kati ya nchi ya Galatia na Frigia, mji kwa mji, akiwathibitisha wanafunzi.

24 Basi Myahudi mmoja, JINA LAKE APOLO, mzalia wa Iskanderia, MTU WA ELIMU, akafika Efeso; NAYE ALIKUWA HODARI KATIKA MAANDIKO.

25 Mtu huyo alikuwa amefundishwa njia ya Bwana; NA KWA KUWA ROHO YAKE ILIKUWA IKIMWAKA, alianza kunena na kufundisha kwa usahihi habari za Yesu; naye alijua ubatizo wa Yohana tu.

26 Akaanza kunena kwa ujasiri katika sinagogi; hata Prisila na Akila walipomsikia wakamchukua kwao, wakamweleza njia ya Bwana kwa usahihi zaidi.

27 Na alipotaka kuvuka bahari aende mpaka Akaya, ndugu wakamhimiza, wakawaandikia wale wanafunzi wamkaribishe, naye alipofika akawasaidia sana wale waliokwisha kuamini kwa neema ya Mungu.

28 Kwa maana aliwashinda Wayahudi kabisa kabisa mbele ya watu wote, akionyesha kwa maneno ya maandiko ya kuwa Yesu ni Kristo”.

Na tabia ya Wainjilisti ni kutokukaa sehemu moja, kwasababu Bwana ameweka ndani yao, roho ya kuhubiri, kama Apolo.

Na Wainjilisti wa kweli si wapenda fedha, wala wanaopenda umaarufu wala fasheni za kidunia. Wainjilisti wa kweli, ni wale wanaougua wanapoona watu wanafundishwa vitu visivyo sahihi kimaandiko kama Apolo.

 4. WACHUNGAJI

Wachungaji ni kundi lingine ambalo Bwana ameliweka ndani ya kanisa, kwa lengo la kulichunga kundi (kanisa). Baada ya mtu kuamini kutokana na injili ya mitume au wainjilisti, hana budi kukaa katika ushirika wa kanisa. Na atakapokuwa katika kanisa hana budi kuchungwa kama vile kondoo.

Sifa za wachungaji wa kweli ni zile zile za Uaskofu zinazotajwa katika kitabu cha 1Timotheo  3:1-7, kwamba asiwe mtu wa kupenda fedha, asiyekuwa mlevi,mwenye kuitunza nyumba yake vyema, na mwenye ushuhuda mzuri katikati ya watu.

Katika enzi za kanisa la kwanza wachungaji wa ukweli walikuwa ni wengi kuliko wa uongo, lakini katika siku hizi za mwisho, wachungaji wa uongo ni wengi kuliko wa ukweli, na hiyo yote ni kwasababu tunaishi katika siku za mwisho sawasawa na unabii, na siku yoyote Parapanda inalia.

 5. WAALIMU

Hili pia ni kundi lingine Bwana Yesu aliloliweka ndani ya kanisa. Lengo kuwepo  Waalimu ni kulifundisha Neno la Mungu, kwa watu walio makanisani. Waalimu wanakuwa na uwezo wa kufundisha, na kumfanya mtu aelewe, kama tu walimu wa elimu za kidunia walivyo. Lengo ni ili wakristo wajae ambayo Bwana anayahitaji..

Na siku hizi za mwisho waalimu wa uongo ni wengi, kuliko wa kweli. Kwasababu ile ile ya kuwa tunaishi katika siku za mwisho. Sifa kuu ya Waalimu wa Uongo ni kuhubiri mambo ya ulimwengu huu na kupenda fedha na mambo ya kiulimwengu.

Kwa hitimisho ni kuwa Roho Mtakatifu yupo mpaka sasa, na Mitume wa ukweli, Manabii wa ukweli, Wainjilisti wa ukweli, Wachungaji wa ukweli na Waalimu wa Ukweli, mpaka leo Bwana amewaweka katika makanisa yake.

Na pia karama huduma hizi zinaingiliana, kuna Mtu anaweza kuwa Mtume na pia akawa Mwinjilisti, hali kadhalika mwingine anaweza kuwa Mchungaji na akawa Mwalimu pia, na mwingine anaweza kuwa Mtume na kuwa mwalimu kama Mtume Paulo (1Timotheo 2:7), ndio maana utaona Mtupe Paulo, katoa mafundisho mengi sana katika nyaraka zake..na kwasababu alikuwa Mtume na hapo hapo Mwalimu.

Lakini kamwe hatupaswi kujisifia karama wala huduma tulizonazo, kwasababu Roho Mtakatifu hajavitoa vipawa hivyo kwa lengo la kutufanya sisi tuwe maarufu, au tuonekane wa tofauti..bali kwa lengo la kulijenga kanisa, na kuwakamilisha watakatifu.

Hekima ya Mungu ni kuu, sana. Na Bwana ni mzuri sana. Je! Umempokea Bwana Yesu, na kubatizwa? Na kupokea Roho Mtakatifu? Kama bado unasubiri nini?..kumbuka hizi ni siku za mwisho, na Yesu yupo mlangoni kurudi.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312


Mada Nyinginezo:

Nini maana ya “Torati na manabii”?

Nini maana ya msiwe waalimu wengi (Yakobo 1:3)?

Nini maana ya “Roho za manabii huwatii manabii?

AKAZIDI KUENDELEA KATIKA HEKIMA NA KIMO.

Nini maana ya “Torati na manabii”?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
10 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Anonymous
Anonymous
1 year ago

Nyie mnamfahamu William Branham? Au mna uhusiano wowote Naye?

Daniel Bilima
Daniel Bilima
1 year ago

Kindly I need class for learning

Anonymous
Anonymous
2 years ago

AMEN mtumishi

Friedrich%the son of JESUS
Friedrich%the son of JESUS
2 years ago

Amina,mtumishi Nuru ya Bwana izidi kukuangazia!

Anonymous
Anonymous
2 years ago

Amina

M
M
2 years ago

Shukran kwa mafundisho..ubarikiwe

MUNGU AKUTUNZE Kwa somo zuri
MUNGU AKUTUNZE Kwa somo zuri
2 months ago
Reply to  Admin

MUNGU