GOGU NA MAGOGU, Katika biblia ni nani?

GOGU NA MAGOGU, Katika biblia ni nani?

Neno Gogu na Magogu limeonekana sehemu mbili katika biblia, Sehemu ya kwanza ni katika kitabu cha Ezekieli 38:2, na katika Ufunuo 20:8.

Sasa ni vizuri kujua kwanza Magogu ni nini, ndipo tuje kwa Gogu.

Magogu sio wingi wa Gogu.. hapana!.. bali ni jina la mtu mmoja, ambalo tunalipata katika kitabu cha Mwanzo 10:2.

Mwanzo 10: 1 “Hivi ndivyo vizazi vya wana wa Nuhu, Shemu, na Hamu, na Yafethi. Na kwao walizaliwa wana wa kiume baada ya gharika.

2 Wana wa Yafethi ni Gomeri, na MAGOGU, na Madai, na Yavani, na Tubali, na Mesheki, na Tirasi.

Hivyo “Magogu” alikuwa ni Mjukuu wa Nuhu, alikuwa ni Mtu. Sasa mtu huyu biblia haijaeleza alikuwa ni mtu mwenye sifa gani, lakini kutokana na uwepo wake katika sehemu nyingine za biblia, inaonekana wazao wake walikuja kuwa watu Hodari kipindi hicho, na mwenye uwezo mkubwa sana wa kijeshi, na kiuchumi, mfano wa Nimrodi aliyeujenga Babeli.

Na Magogu naye ni hivyo hivyo, uzao wake ulikuja kuwa Hodari..na kuwa Taifa lenye nguvu kijeshi, na watu hao wote kwa ujumla wakaitwa Magogu kufuatia jina la baba yao huyo.

Kama vile mji wa Moabu ulivyoitwa kufuatia jina la baba yao aliyeitwa Moabu. (Mwanzo 19:37 “Yule mkubwa akazaa mwana, akamwita jina lake Moabu; huyo ndiye baba wa Wamoabi, hata leo”)

Na Magogu ni hivyo hivyo, Uzao wake ulikuja kuitwa kwa jina hilo la Magogu, na nchi yao ikaitwa nchi ya Magogu, kufuatia jina la baba yao huyo aliyeitwa Magogu.

Tunalisoma hilo vizuri katika Ezekieli..

Ezekieli 38:1 “Neno la Bwana likanijia, kusema,

2 Mwanadamu, kaza uso wako, umwelekee GOGU, wa NCHI YA MAGOGU, mkuu wa Roshi, Mesheki, na Tubali, ukatabiri juu yake”,

Na nchi hiyo lilikuwa upande wa kaskazini mwa Asia na Ulaya, ambayo sasahivi ni Maeneo ya nchi ya Urusi.  Hatima ya hilo Taifa la Magogu, biblia haijaieleza, lakini ni wazi kuwa lilikuja kupotea kama yalivyopotea mataifa mengine yaliyokuwa hodari kama Babeli.

Sasa baada  ya kujua hilo, twende kipengele cha pili, cha GOGU. Kama tulivyotangulia kusema Magogu sio wingi wa Gogu. Bali Gogu ni kiongozi wa Taifa la Magogu. Yaani mfalme wa taifa la Magogu. Kwahiyo tunaposoma, neno Gogu na Magogu, Ni sawa na kusema Farao na Misri, au Sulemani na Israeli.

Ndio maana tunasoma hapo katika Ezekieli 38:3… “useme, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, mimi ni juu yako, Ewe GOGU, mkuu wa Roshi, na Mesheki, na Tubali;”

Umeona hapo mstari wa 2, unasema Gogu mkuu wa…. Neno “mkuu wa” linaashiria ni kiongozi, hivyo Gogu ni jina la kiuongozi kama vile Farao, au Sultani. Na Magogu ni Taifa hilo lenye nguvu ambalo linatawala mataifa mengine madogo madogo (Tubali, Mesheki na Roshi)

Sasa kama tulivyotangulia kusema huo mji wa Magogu haupo tena wala mkuu wake Gogu hayupo…Lilikuwepo enzi hizo, lakini sasa halipo tena, lakini huo unabii wa Ezekieli 38 bado haujatimia.. Ambapo ukisoma hiyo Ezekieli 38 yote, utaona inazungumzia Habari za vita vitakavyopiganwa Israeli, ambapo Mataifa mengi katika nchi ya mashariki ya kati (kwasasa ni mataifa ya kiarabu), yataungana pamoja na Gogu na Magogu, atakayekuwepo kipindi hicho kuja kuivamia Israeli, lakini biblia inasema Gogu atashindwa vibaya sana Pamoja na mataifa hayo aliyoshirikiana naye.

Sasa huyo Gogu na Magogu, atakuwa ni nani, kama mji huo ulishapotea kitambo?..

Gogu atakayeasisi vita hivyo vya Ezekieli 38, Uthibitisho wote unaonyesha kuwa atakuwa si mwingine Zaidi ya Mkuu wa Taifa la URUSI .

Kwanini ni Taifa la Urusi, ndio linalofananishwa na Magogu na si Taifa lingine?.

Kwasababu ndio taifa lililopo kaskazini mwa Asia na ulaya, eneo lile lile Magogu walipokuwepo, pili ndio taifa lenye nguvu kijeshi kaskazini mwa Ulaya, mfano wa magogu wa mwanzo.

Hivyo Urusi ndiyo itakayotimiza unabii huo wa Gogu na Magogu, wakati wa vita hivyo.

Mbali na hilo tunakuja kuona tena Gogu na Magogu, wakitokea mwishoni mwa Utawala wa miaka elfu moja. Sasa ni muhimu kufahamu kuwa sio wale wale, wamezaliwa tena upya..hapana…bali ni roho ile ile iliyokuwa inaiendesha Gogu na Magogi kipindi cha zamani, sasa imerudi tena kutenda kazi katika zama hizo, ni kama tu vile Babeli ilivyokuwepo wakati wa zamani na kupata nguvu na kujulikana duniani kote, na kutiisha mataifa yote chini,  lakini ikaja kuanguka, ikapotea kabisa…Lakini bado tena tunakuja kuiona ipo, imerudi tena katika kitabu cha Ufunuo. Sasa haimaanishi kwamba ni Babeli ile ile imerudi,  bali ni ile roho iliyokuwa inaiendesha Taifa hilo nyakati za zamani, imerudi na kuivaa na kuliendesha Taifa Fulani lingine siku za mwisho..

Hivyo Gogu na Magogu, wa kwenye Mwanzo wa kwenye Ezekieli 38 (yaani Taifa la Urusi), sio wa kwenye Ufunuo 20:8 (mwishoni mwa utawala wa miaka elfu), ingawa roho ni ile ile moja, inayofanya kazi ya kukusanya mataifa na kupambana na Taifa la Mungu.

Je umempokea Kristo? Kama bado, kumbuka tunaishi ukingoni mwa nyakati kabisa na Kristo yupo karibuni kurudi, na mpinga kristo kuanza kufanya kazi yake, ya kuwatia watu chapa. Kama unafikiri ni utani kwamba Kristo hatarudi, siku moja utayahikiki haya maneno unayoyasikia. Wakati huo waliokudanganya na wao watagundua kuwa walidanganywa, itakuwa ni huzuni sana.. Je utakuwa wapi siku hiyo?. Kama hujampokea Kristo na leo hii unasema upo tayari kumpokea Kristo na kudhamiria kutubu basi fungua hapa kwa msaada >> SALA YA TOBA

Mungu akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 8 (Kitabu cha Ezekieli)

JE WEWE NI LAZARO YUPI, WA KWANZA AU WA PILI?

WAFALME WATOKAO MAWIO YA JUA.

Watakaodanganywa baada ya miaka 1000,watatoka wapi?

ULIMWENGU WA ROHO UPO NA UNA MADHARA KATIKA MAISHA YETU! 

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
4 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Cleven Nassary
Cleven Nassary
2 years ago

Amen Mungu azidi kuwainua watumishi wa Bwana

Denis
Denis
2 years ago

Hongereni sana Mungu anawatumia kufungua wengi