TENGENEZA MAMBO YA NYUMBA YAKO.

TENGENEZA MAMBO YA NYUMBA YAKO.

Nakusalimu katika jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu katika mafundisho ya Neno la Mungu.

Ni vema tukafahamu tarajio la Mungu kwa kila mwanadamu ni lipi kabla ya kumaliza mwendo wake hapa duniani. Utaona kipindi kile kabla mfalme Hezekia hajafa, Neno la Mungu lilimjia kwa kinywa cha Nabii Isaya na kumwambia, atengeneze mambo yake, kwasababu kifo chake kimekaribia.

Isaya 38:1 Siku hizo Hezekia aliugua, akawa katika hatari ya kufa; na Isaya nabii, mwana wa Amozi, akaenda kwa mfalme, akamwambia, Bwana asema hivi, Tengeneza mambo ya nyumba yako; maana utakufa, wala hutapona

Kwanini Mungu hakumwambia, “pumzika sasa usihangaike-hangaike” kwasababu kipindi si kirefu utaenda kufa? Lakini anamwambia “TENGENEZA”, mambo yako.

Mungu alijua kabisa  nyenzo pekee ya kuwa salama kule ng’ambo ya pili ni kutengeneza sasa mambo yako angali unaishi.

Inasikitisha kuona, watu wengi, wanaishi tu hohe-hahe, wakihubiriwa habari za wokovu, wanakuwa wepesi kusema, ‘siku moja nitaokoka!’ . Wakidhani kuwa mbinguni ni kuingia kama vile mtu aingiavyo kwenye basi/daladala, ambapo siku hiyo hiyo atakata tiketi, na siku hiyo hiyo utasafiri.

Mbingu ina maandalizi. Na maandalizi yake ni hapa duniani, ukiyakamilisha hayo utaonekana umestahili kuingia mule. Bwana anatazamia si tu Uokoke, halafu basi.  anatazamia pia Uache Urithi wa rohoni kwa vizazi vingine, huko ndiko kutengeneza mambo ya nyumbani mwako.  Kama vile tu mtu mwenye busara ambaye anajua anapokaribia kufa ni sharti aache urithi kwa watoto wake. Lakini kama hana urithi atawaachia nini?.

Lazima ujue umewekwa na Mungu pia umzalie matunda. Kwahiyo usiwe na amani kuondoka duniani, kienyeji-enyeji tu, anza kutengeneza wokovu wako leo, uwe na faida kwenye ufalme wa mbinguni. Hata utakapofika kule Bwana aone, ile talanta aliyokupa walau imeongeza jambo Fulani katika ufalme wa Mungu duniani.

Mathayo 25:20  Akaja yule aliyepokea talanta tano, akaleta talanta nyingine tano, akisema, Bwana, uliweka kwangu talanta tano; tazama, talanta nyingine tano nilizopata faida. 21  Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako. 22  Akaja na yule aliyepokea talanta mbili, akasema, Bwana, uliweka kwangu talanta mbili; tazama, talanta nyingine mbili nilizopata faida. 23  Bwana wake akamwambia, Vema, mtumwa mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako. 24  Akaja na yule aliyepokea talanta moja, akasema, Bwana, nalitambua ya kuwa wewe u mtu mgumu, wavuna usipopanda, wakusanya usipotawanya; 25  basi nikaogopa, nikaenda nikaificha talanta yako katika ardhi; tazama, unayo iliyo yako. 26  Bwana wake akajibu, akamwambia, Wewe mtumwa mbaya na mlegevu, ulijua ya kuwa navuna nisipopanda, nakusanya nisipotawanya; 27  basi, ilikupasa kuiweka fedha yangu kwa watoao riba; nami nikija ningalipata iliyo yangu na faida yake. 28  Basi, mnyang’anyeni talanta hiyo, mpeni yule aliye nazo talanta kumi. 29  Kwa maana kila mwenye kitu atapewa, na kuongezewa tele; lakini asiye na kitu, hata kile alicho nacho atanyang’anywa. 30  Na mtumwa yule asiyefaa, mtupeni mbali katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno

Je! Mali zako, vitu ulivyo navyo, elimu yako, ujuzi wako, karama yako, vina sehemu gani katika kuundeleza ufalme wa Mungu?.  Kama mtu uliyeokoka Je! Moyo wako kimaombi upo wapi?, Usomaji wako wa Neno umeufichia wapi?. Ukuaji wako wa kiroho umekwama wapi. Tusijione salama katika hayo mazingira na angali muda unakwenda. Ipo hatari, tusipoyatengeneza maisha yetu ya kiroho. Upo wa kusimama mbele ya kiti cha enzi cha hukumu, ambapo kila mmoja atatoa hesabu ya mambo yake mwenyewe.

Hivyo huu ni wakati wetu kila mmoja kujitathimini ndani, kwasababu hapa duniani ni wapitaji tu, hatuna maisha marefu, hujui ni lini utaondoka, au Bwana atarudi lini. Tufahamu tu huko tuendako kama hatujajitengeneza vema sasa, kuingia haiwezekani.

Bwana atupigishe hatua.

Shalom.

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

Mithali 24:17 inamaana gani kusema Tengeneza kazi yako huko nje?

ANGALIA JINSI USIKIAVYO:

TENGENEZA  NYAVU ZAKO, OSHA NYAVU ZAKO.

BASI NIKAOGOPA, NIKAENDA NIKAIFICHA TALANTA YAKO.

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 14 (Yoeli, na Obadia).

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments