VIGEZO VYA NEEMA YA MUNGU.

VIGEZO VYA NEEMA YA MUNGU.

Tangu mwanzo mwanadamu alikuwa akijaribu kujiokoa kwa njia yake mwenyewe ikiwemo kuonyesha matendo yake mazuri, na mwenendo wake mkamilifu lakini hakuweza. Pengine aliweza kushinda wizi kikamilifu lakini uongo ukamshinda, aliweza kushinda uzinzi wote, lakini tamaa zikamtawala, aliweza kushinda ibada za sanamu na vinyago, lakini kusamehe kukamshinda. Alipoweza kushinda kimoja, nyuma yake kulikuwa na elfu vinavyo mhukumu.

 

Na hiyo ilimfanya asikidhi vigezo vya kuingia mbinguni, kwasababu watakaoiona mbingu na Mungu ni watakatifu asilimia mia wasio na doa lolote. Ndio maana maandiko yanasema wote wameoza,wamepotoka hakuna amtafutaye Mungu. Bali tunahesabiwa haki bure kwa neema ya Bwana Yesu Kristo.

 

Warumi 3:11  Hakuna afahamuye; Hakuna amtafutaye Mungu. 12  Wote wamepotoka, wameoza wote pia; Hakuna mtenda mema, la! Hata mmoja.

 

Ndio sababu ya Yesu kuja duniani, ili kwa kupitia kumwamini yeye tuipokee hiyo neema ya kuitwa watakatifu, bila kuonyesha kwanza kipimo chochote kwa Mungu. 

Maana yake ni kuwa mimi na wewe tunapomwamini Yesu Kristo, ni moja kwa moja tunaitwa watakatifu, tuliosamehewa dhambi zetu, na kuondolewa pia. 

 

Ikiwa umemwamini leo Yesu Kristo, moja kwa moja Mungu hakuhesabii tena dhambi yoyote kama mkosaji. Ijapokuwa utakuwa hujakamilika bado.  Hii ndio maana ya neema, yaani kukubaliwa kusikostahili. Ilikupasa kwanza uwe na matendo makamilifu asilimia 100 kama Bwana Yesu, ndio uitwe mtakatifu uliyestahili kumwona Mungu. Lakini sasa kwa kuupokea ukombozi wa Yesu Kristo, dhambi zako, zimefuta unaitwa mtakatifu, kabla hata ya ukamilifu wa utakatifu wenyewe kukufikia. Ndio maana sisi tulio ndani ya Kristo hatuna budi kuwa na amani, na furaha wakati wote. Kwasababu ule mzigo mzito wa kujitahidi sisi wenyewe kuingia mbinguni umeondolewa na Yesu Kristo Bwana wetu, kwa kifo chake pale msalabani.

 

 

Lakini sasa, katika nyakati hizi za mwisho suala hili la neema limetafsirika vibaya, kama tu nyakati zile za zamani, na hapo yatupasa  tuwe makini sana. Ni sawa na taifa litangaze neema kwa nchi yake na kusema, sasa huduma zote za maji ni bure, hakuna kulipia bili,matumizi ni kama unavyotaka. halafu uone watu wanatumia fursa hiyo kwenda kufungulia  mabomba yatiririshe maji kwenye mitaro na mabarabarani, kila mahali kuwe ni maji tu,  Bila shaka utasema hawa watu wamerukwa na akili, hawana sifa ya kupewa huduma hiyo tena.

 

Ndivyo ilivyo kwa jambo linaloitwa neema, tusijipojua kanuni zake, tutajikuta badala ya kupokea wokovu, tunapokea maangamizi. Badala ya kukazana kumpendeza Mungu, tunastarehe katika dhambi,  Na ndicho kinachoendelea sasa kwa sehemu kubwa miongoni watu na madhehebu.

 

Yafuatayo ni mambo ambayo ujiepushe nayo kwa nguvu zote, wewe uliyeipokea neema ya Mungu.

 

  1. Kuipokea neema bure,

2 Wakorintho 6:1

[1]Nasi tukitenda kazi pamoja naye twawasihi msiipokee neema ya Mungu bure.

Ukisoma vifungu vichache vya nyuma anasema mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya, ya kale yamepita tazama yamekuwa mapya.

 

Mtu ambaye hataki geuko, baada ya kusamehewa dhambi zake, huyo ni mtu ambaye ameipokea neema bure, haithamini, ameitwa mtakatifu, halafu hataki kuishi maisha matakatifu, anaendelea na maisha yake yale yale ya kale.. Mtu kama huyo asijidanganye neema hiyo ni batili. Mtu yeyote aliyeokoka  wakati huo huo una wajibu wa kuanza kupiga hatua za mabadiliko, na unapaswa uithamini sana hiyo zaidi ya vyote, kwasababu ni Mungu ndiye akutakasaye baada ya hapo.

 

Lakini pia mtu ambaye amekaa muda mrefu hamzalii Mungu matunda, anahesabika kama aliyeipokea neema ya Mungu bure, na hivyo mwisho wake unakuwa ni kukatwa.

 

Tito 2:11  Maana neema ya Mungu iwaokoayo wanadamu wote imefunuliwa;12  nayo yatufundisha kukataa ubaya na tamaa za kidunia; tupate kuishi kwa kiasi, na haki, na utauwa, katika ulimwengu huu wa sasa; 

 

Je! Umeitii neema hii inayokufundisha kukataa machafu ya duniani?. Leo yapo madhehebu yanayosema, ukiokoka umekoka milele, kazi yako imeisha, hata usipoonyesha  bidii nyingine yoyote kwa Mungu,huwezi potea. Ndugu yangu kuwa makini sana na imani hizi. Neema haipokelewi bure.

 

  1. Kuipungukia Neema

Epuke pia  kuipungukia neema.

 

Waebrania 12:15-17

[15]mkiangalia sana mtu asiipungukie neema ya Mungu; shina la uchungu lisije likachipuka na kuwasumbua, na watu wengi wakatiwa unajisi kwa hilo. 

[16]Asiwepo mwasherati wala asiyemcha Mungu, kama Esau, aliyeuuza urithi wake wa mzaliwa wa kwanza kwa ajili ya chakula kimoja. 

[17]Maana mwajua ya kuwa hata alipotaka baadaye kuirithi baraka, alikataliwa (maana hakuona nafasi ya kutubu), ijapokuwa aliitafuta sana kwa machozi.

Kuipungukie neema Ni tabia ya kuishusha thamani neema, na kuilazimisha  itende kazi hata katika kiwango ambacho si chake.

 

Hii hasa huja kwa watu ambao wanazoelea kufanya dhambi mara kwa mara wakiamini kuwa kwasababu Mungu hawahesabii makosa basi hata wakifanya kosa lolote hawawezi kupotea.

Ndugu, neema si kuhalalisha maisha ya dhambi. 

Biblia inasema..

Warumi 6:1  Tuseme nini basi? Tudumu katika dhambi ili neema izidi kuwa nyingi? 2  Hasha! Sisi tulioifia dhambi tutaishije tena katika dhambi?

3  Hamfahamu ya kuwa sisi sote tuliobatizwa katika Kristo Yesu tulibatizwa katika mauti yake?

4  Basi tulizikwa pamoja naye kwa njia ya ubatizo katika mauti yake, kusudi kama Kristo alivyofufuka katika wafu kwa njia ya utukufu wa Baba, vivyo hivyo na sisi tuenende katika upya wa uzima.

Usitende dhambi za mazoelea, ukadhani neema itakuwa sikuzote kukufunika. Ukiifanyia jeuri neema, itaondoka kwako.

 

Waebrania 6:4  Kwa maana hao waliokwisha kupewa nuru, na kukionja kipawa cha mbinguni, na kufanywa washirika wa Roho Mtakatifu,

5  na kulionja neno zuri la Mungu, na nguvu za zamani zijazo, 6  wakaanguka baada ya hayo, haiwezekani kuwafanya upya tena hata wakatubu; kwa kuwa wamsulibisha Mwana wa Mungu mara ya pili kwa nafsi zao, na kumfedhehi kwa dhahiri.

 

  1. Kuibadili neema ya Mungu.

 

Yuda 1:4  Kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri, watu walioandikiwa tangu zamani hukumu hii, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi, nao humkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana wetu Yesu Kristo.

 

Neema ya Mungu inaweza badilishwa ikamaanishwa kivingine kabisa. Kwamfano utaona leo hata mashoga, wanavyama vyao wakisema sisi tupo chini ya neema. Walevi nao, wenye dhambi nao wanasema neema ya Yesu ipo duniani sasa, kumwokoa kila mtu.

 

Hivyo watakuambia maneno kama usihukumu usije ukahukumiwa. Na wana amani na ujasiri katika hayo wanayoyafanya na wengine wanajiita maaskofu na wachungaji, wakihalalisha kila kitu kiovu kufanyika kwa kivuli cha neema.

 

Hao ndio waibadilishao neema ya Bwana Yesu kuwa ufisadi, hilo Neno ufisadi ni zaidi ya uasherati, Ni pamoja na matendo yote maovu kupita kiasi. Lakini neema ya Yesu,.haikuja kufunuki dhambi, bali ilikuja kuondoa dhambi ndani ya mtu. Usiwe mmojawapo aibadilishaye neema ya Mungu.

 

Hivyo kwa vifungu hivyo itoshe kusema kuwa NEEMA tunaipokea bure, lakini ili iweze kufanya kazi lazima tujue sifa zake,  kisha tuzikubali, vinginevyo tutajidanganya na kuangamia.  Ni sawa na mtu akupe gari bure, lakini usipoliweka mafuta, na kujua kuliendesha linakuwa halina tofauti na mdoli wa gari.

Lakini ukiithamini neema, itakutunza, itakuhifadhi na kuyaficha makosa yako yote, Hivyo utaendelea kuonekana mkamilifu asilimia mia mbele za Mungu, na hata ukifa, ni moja kwa moja mbinguni.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

JINSI YA KUITUMIA VYEMA NEEMA YA MUNGU ILIYO JUU YANGU.

MANENO YA MUNGU YANAPINDULIWAJE?

JINSI MWISHO ULIVYOKARIBIA.

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments