JIBU: Tukumbuke kuwa “sala ya Toba” sio wokovu, Sala ya toba ni njia mojawapo, inayotumiwa kuukaribisha wokovu ndani ya mtu, lakini sala kama sala yenyewe sio wokovu, Ikiwa na maana zipo njia nyingine, Na ndio maana huwezi kuona mahali popote mitume waliwaambia watu wafuatisha sala fulani, kwamba kwa hiyo ndio wataokoka..Huwezi kuona.
Wokovu unatoka moyoni. Pale mtu anapojitambua kuwa ni mwenye dhambi, na hivyo anahitaji kukombolewa kutoka katika mauti na Yesu Kristo, kitendo kinachompelekea kuyasalimisha maisha yake yote kwa Bwana Yesu ayaongoze, na kuachana na mambo ya ulimwengu, Huo ndio wokovu.
Sasa jambo kama hili likishatokea ndani ya mtu, udhihirisho wa nje ndio unafuata, ambao mojawapo ndio kukiri kwa kinywa chako, na cha pili ni Matendo yako.
Kutimiza lile andiko la Warumi 10:9
“Kwa sababu, ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka”.
Sasa mabubu, hawajajaliwa kuongea, hawawezi kumkiri Kristo kwa vinywa vyao..Lakini wanaweza kuonyesha kuwa wamemwanini Kristo kwa matendo yao. Wakifanya hivyo tayari huo ni wokovu tosha, kutoka kwa Bwana.. Hivyo mtu kama huyu ikiwa tayari ameshamwani Bwana muhimize tu, aanze kuenenda sawasawa na kuamini kwake.
Tutakumbuka kisa kile cha Yule mwanamke ambaye Bwana Yesu alisema alikuwa na dhambi nyingi, jinsi alivyomwendea na kulia sana miguuni pake, kudhihirisha majuto ya makosa yake, kisha kumpangusa kwa nywele zake, Utaona pale Bwana Yesu hakuzungumza naye maneno yoyote, kwamba njoo nikuongoze sala ya toba, au sema maneno haya au yale, hapana isipokuwa alipoona tu moyo wake wa toba ulivyomaanisha kwelikweli alimwambia.. “Mwanamke umesamehewa dhambi zako”
Luka 7:36-48
“36 Mtu mmoja katika Mafarisayo alimwalika ale chakula kwake; akaingia katika nyumba yake yule Farisayo, akaketi chakulani.
37 Na tazama, mwanamke mmoja wa mji ule, aliyekuwa mwenye dhambi, alipopata habari ya kuwa ameketi chakulani katika nyumba ya yule Farisayo, alileta chupa ya marimari yenye marhamu.
38 Akasimama nyuma karibu na miguu yake, akilia, akaanza kumdondoshea miguu machozi yake, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake, akiibusu-busu miguu yake na kuipaka yale marhamu.
39 Basi, yule Farisayo aliyemwalika alipoona vile, alisema moyoni mwake, Mtu huyu kama angekuwa nabii, angemtambua mwanamke huyu amgusaye, ni nani, naye ni wa namna gani, ya kwamba ni mwenye dhambi…..
44 Akamgeukia yule mwanamke, akamwambia Simoni, Wamwona mwanamke huyu? Niliingia nyumbani kwako, hukunipa maji kwa miguu yangu; bali huyu amenidondoshea machozi miguu yangu, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake
45 Wewe hukunibusu; lakini huyu tangu nilipoingia hakuacha kunibusu sana miguu yangu.
46 Hukunipaka kichwa changu mafuta; bali huyu amenipaka miguu yangu marhamu.
47 Kwa ajili ya hayo nakuambia, Amesamehewa dhambi zake ambazo ni nyingi, kwa kuwa amependa sana; lakini asamehewaye kidogo, huyo hupenda kidogo.
48 Kisha alimwambia mwanamke, Umesamehewa dhambi zako.
Hii kuonyesha kwamba, pale unaoonyesha geuko la kweli moyoni mwako, kabla hata hujazungumza chochote tayari umeshasamehewa.
Ndivyo ilivyo kwa mabubu, haijalishi hawataweza kukiri sala yoyote kwa vinywa vyao, lakini ikiwa moyoni mwao wameonyesha mabadiliko, hicho ndicho Mungu anachokitaka. Imekuwa desturi leo hii kuona kundi kubwa la watu wanasema wameongozwa sala ya toba na kumkiri Yesu , lakini ukitazama matendo yao hayaendani na walichokikiri. Huo ni unafki ambao unamchukiza Bwana sana.
Mathayo 15:7 “Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema,
8 Watu hawa huniheshimu kwa midomo; Ila mioyo yao iko mbali nami”.
Bwana anataka tumfuata na tumwabudu katika Roho na kweli. Na sio katika maneno matupu. Ikiwa mtu asiweza kuongea, amesimama katika wokovu, huyo mtu ni wa thamani sana mbele za Mungu
Swali ni je wewe, uliyemkiri Bwana, unayemsifu, unayemuhubiri, unayemtangaza. Je! Ni kweli kitokacho mdomoni mwako, kimeambatana na badiliko la ndani?
Majibu tunayo.
Bwana atusaidie.
Shalom.
Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;
Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312
Mada Nyinginezo:
Utasi ni ugonjwa gani? (Marko 7:32).
Kiungo chako kimoja kikikukosesha kikate. Ina maana gani?
Dusumali ni nini katika biblia?
Matoazi na Matari ni nini? (Kutoka 15:20)
Je Malaika Mikaeli ndiye Yesu mwenyewe?
Tofauti kati ya mbinguni, peponi, Kuzimu, Jehanamu, na Paradiso ni ipi?
About the author