Title October 2024

NYWELE ZAKO ZIKUFUNDISHE, SAUTI YA MUNGU.

Kwanini Mungu akuumbe hivyo ulivyo? Kwanini asingeweka pembe kichwani kwako, au kwanini asingekuwekea  vilemba vya nyama kama vile vya kuku kichwani, au antena mbili kama zile za konokono au mdudu, bali amekuwekea nywele kichwani pako.

Sauti ya Mungu ipo katika maumbile yetu. Sisi kujikuta hivi tulivyo sio kwamba, ndio umbile bora zaidi ya yote Mungu aliloona linamfaa mtu, hapana,  tungeweza kuumbwa vizuri zaidi hata ya mwonekano huo tulionao, lakini tumebuniwa hivi, kwa kusudi la kipekee ambalo tunapaswa tulijue, na sio kwa kusudi la urembo.

Kwamfano usipoweza kuelewa utendaji kazi wa mwili wako jinsi viungo vinavyoshirikiana huwezi kuelewa jinsi kanisa la Kristo linavyopaswa kufanya kazi likutanikapo, kwasababu sisi tunaitwa viungo mbalimbali ndani ya mwili wa Kristo.Umeona? Bwana akasema kiungo kimoja kikiumia, vyote vimeumia.

Hivyo tumeumbwa, kimalengo sio kimwonekano bora au kiuzuri,. Ni sawa na mtu aulizwe kati ya jiko, na maua kipi kina umuhimu zaidi kuwepo ndani mwako. Ni wazi kuwa atasema jiko,kwasababu litamsaidia kupika. Hakulichagua kwasababu lina mwonekano bora, lakini kwasababu lina matumizi muhimu zaidi ya vingine.

Vivyo hivyo na wewe ujitazamapo mwili wako, usijitazame kiuzuri kuliko  viumbe vingine, au wanadamu wenzako, bali fikiria tu katika picha ya matumizi ya kila kiungo ulichopewa, kinakufundisha nini kuhusu muumba wako au kinatimiza kusudi gani kwa Mungu wako. Hilo ndio lengo hasaa la wewe kubuniwa hivyo ulivyo.

Leo tutaanza na NYWELE, kisha wakati mwingine tutatazama na viungo vingine;

Utazamapo nywele zako Bwana anataka ujue yafuatayo;

  1. Mambo yako yote, yapo katika hesabu za Mungu.

Mathayo 10:30  lakini ninyi, hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. 31  Msiogope basi; bora ninyi kuliko mashomoro wengi

Ni kawaida  kudhani kuwa Mungu hathamini, au hajui kila kitu, au anasahau sahau. Lakini sivyo, ukimfuata Mungu, vitu vyako vyote vinavyotoka na kuingia vipo kimahesabu, hakuna kitu kinachotokea kwa ghafla tu, bila yeye kujua au kuruhusu, Hivyo mashaka yakija, kumbuka nywele zako zilivyo nyingi lakini zimehesabiwa, vivyo hivyo mambo yako yote yamehesabiwa.

  1. Huwezi epukana na maadui.

Zaburi 69:4 Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua

Jinsi nywele zako zilivyo nyingi, maadui nao vivyo hivyo. Na maadui zetu sio wanadamu bali ni mapepo ambayo mara nyingine huweza pia yavaa wanadamu, kutudhuru. Hivyo usiwe mtu wa kunung’unika au kulamimika, ujue kila mwanadamu yupo vitani. Kama Bwana wetu Yesu Kristo hakuwa na dhambi hata mmoja lakini alikuwa na jopo la maadui kwanini wewe usiwe nao. Hivyo kuwashinda ni kuwa mwombaji daima, na kutembea katika njia za Bwana sikuzote. Ukikumbuka kuwa maadui ni jambo la kawaida, kama tu nywele zako zilipo hapo kichwani.

  1. Si kila kitu unaweza kufanya. hivyo kuwa na kiasi.

Mathayo 5:36  Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kufanya unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi.

Wakati mwingine, tunajiaminisha na kujihakikishia mambo na kuweka na viapo juu yake kana kwamba mambo yote yapo ndani ya uwezo wetu. Kauli kama, “leo nife,kama sitakupa hiyo fedha” au “Mungu anipige hapa hapa kama ninalokuambia ni uongo” Kauli  kama hizi, za kuongezea hakikisho lingine juu, hazitokani na Mungu, maneno yetu tumeambiwa yawe ndio ndio, au sio sio, zaidi ya hapo yanatokana na Yule mwovu. Kwahiyo popote unapojiona unakaribia kuzidi mipaka kumbuka hizo nywele zilizo juu yako hujawahi kuzifanya ziwe hivyo ulivyo, Bwana ndiye azibadilishaye, hivyo jiwekee mipaka.

  1. Zithamini nguvu zako za rohoni.

Nywele zako hufunua nguvu zako za rohoni. Wanadhiri wote wa Mungu hawakuruhusiwa kukatwa nywele, Samsoni alipewa nguvu, kwa agano la kutokatwa nywele, kufunua kuwa watakatifu wote nywele zao za rohoni ndio nguvu zao. Lakini unapoacha mpango wa Mungu adui anazikata, kama ilivyokuwa kwa Samsoni. Lakini baadaye alipojua amefanya makosa ziliota tena lakini katika gharama za ‘kutoona’ tena.

Waamuzi 16:22 Lakini zile nywele za kichwa chake zikaanza kukua tena baada ya kunyolewa kwake.

Tunza nguvu zako, usiruhusu kiwembe chochote cha mwovu kikupitie. Kwasababu hata zikirejea tena, hutakuwa kama hapo mwanzo.

  1. Uwe na nyakati za maombolezo.

Yeremia 7: 29 Zikate nywele zako, Ee Yerusalemu, uzitupe, Ukafanye maombolezo juu ya vilele vya milima; Kwa maana Bwana amekikataa na kukitupa Kizazi cha ghadhabu yake.

Zamani, kukatwa nywele zote kuisha kabisa ilikuwa ni ishara ya kuingia kwenye maombolezo, kwasababu utukufu wako umeuvua.

Maombolezo, kwa agano jipya sio kulia kama msiba, hapana bali kuingia kwenye maombi ya ndani kabisa, ya kuutafuta uso wa Mungu, ambayo huambatana na mifungo. Na leo, ni kila mara tunakwenda saluni kukata nywele zetu. Tujue Bwana anatutaka kama vile tukatavyo nywele zetu mara kwa mara ndivyo tukumbuke maombi ya kujimimina sana mbele zake.

Je! Somo hilo unajifunza mwilini mwako?

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Je Bwana Yesu alikuwa na nywele ndefu?

ILI TUONEKANE WAKAMILIFU MBELE ZA MUNGU.

MWOMBENI BWANA WA MAVUNO APELEKE WATENDA KAZI.

Rudi Nyumbani

Print this post

Kusujudu ni nini, na je tuna sharti la kusujudu kwa Mungu?

Swali: Je kusujudu ni nini, na sisi wakristo tunayo amri ya kusujudu mbele za Mungu?


Kusujudu ni kitendo cha kuinama kwa kuelekeza kichwa chini kama ishara ya kuabudu au kutoa heshima kwa Mungu, mtu au shetani.. Zaidi ya kuinama tu, kusujudu pia kunaweza kuhusisha kupiga magoti na kuinamisha kichwa chini mpaka kufikia kugusa ardhi (soma 2Nyakati 7:3).

Maandiko yanatuonyesha mara kadha wa kadhaa watu wakimsujudia Mungu, na watu wakiwasujudia wanadamu na vile vile wakimsujudia shetani.

     1.Watu kumsujudia Mungu

Mfano wa watu waliosujudu mbele za Mungu ni yule Mtumwa, Ibrahimu aliyemtuma kwenda kumtafutia mwanae Isaka, mke.. Maandiko yanasema alipokutana tu na Rebeka na kupata uhakika kuwa ndiye binti aliyechaguliwa na Bwana, basi yule mtumwa alisujudu mbele za Bwana mpaka chini..

Mwanzo 4:24 “Akasema, Mimi ni binti wa Bethueli mwana wa Milka, aliyemzalia Nahori.

25 Tena akamwambia, Kwetu kuna majani na malisho ya kutosha, na mahali pa kukaa wageni.

26 YULE MTU AKAINAMA AKAMSUJUDU BWANA. 

27 Akasema, Na atukuzwe Bwana, Mungu wa bwana wangu Ibrahimu, ambaye hakuacha rehema zake na kweli yake kwa bwana wangu. Bwana akaniongoza mimi nami njiani hata nyumba ya nduguze bwana wangu”.

Wengine waliosujudu mbele za Bwana katika biblia ni Musa (soma Kutoka 34:8-9) na Wana wa Israeli kipindi utukufu umeshuka juu ya Nyumba ya Mungu (2Nyakati 7:3)…pamoja na mwandishi Ezra na wenzake katika Nehemia 8:6.

    2. Watu kusujudia Malaika.

Mfano wa watu waliowasujudia Malaika ni Yohana, Mtume wa Bwana YESU.

Ufunuo 22:8  “Nami Yohana ndimi niliyeyasikia na kuyaona mambo hayo. Na hapo nilipoyasikia na kuyaona nalianguka, ili NISUJUDU mbele ya miguu ya malaika yule mwenye kunionyesha hayo.

9  Naye akaniambia, Angalia, usifanye hivi; mimi ni mjoli wako, na wa ndugu zako manabii, na wa wale wayashikao maneno ya kitabu hiki. MSUJUDIE MUNGU”.

Mwingine aliyejaribu kumsujudia Malaika ni Yoshua (soma Yoshua 5:14)

    3. Watu kuwasujudia wanadamu.

Mfano wa watu waliomsujudia mwanadamu katika biblia ni wale wana 11 wa Yakobo, ambao walisujudu mbele ya ndugu ya Yusufu, walipofika nchi ya Misri.

Mwanzo 43:27 “Akawaulizia hali yao, akasema, Je! Baba yenu, yule mzee mliyemnena, hajambo? Angali hai?

28 Wakasema, Mtumwa wako baba yetu hajambo, angali hai; WAKAINAMA, WAKASUJUDU”.

Mwingine aliyemsujudia mwanadamu ni Jemedari Yoabu (2Samweli 14:22), mwengine tena ni Arauna (2Samweli 24:20) na yule mwanamke wa Tekoa (2Samweli 14:4).., Hamani aliyesujudiwa na watu (Esta 3:2)

     4. Watu kumsujudia shetani na jeshi lake.

Mfano wa watu waliomsujudia shetani na majeshi yake ni Wana wa Israeli, kipindi wanakatiza Moabu, ambapo waliisujudia miungu ya Moabu, na kufanya dhambi kubwa mbele za Mungu..

Hesabu 25: 1 “Basi Israeli akakaa Shitimu, kisha watu wakaanza kuzini pamoja na wanawake wa Moabu;

2 kwa kuwa waliwaalika hao watu waende sadakani, sadaka walizowachinjia miungu yao; watu wakala chakula, WAKAISUJUDU HIYO MIUNGU YAO. 

3 Ikawa Israeli kujiungamanisha na Baal-peori; hasira za Bwana zikawaka juu ya Israeli”.

Mwingine aliyesujudia mashetani ni Mfalme Yeroboamu (1Wafalme 16:31)

Swali ni je! Watu waliozaliwa mara ya pili (wa agano jipya) ni sahihi KUSUJUDU??

Jibu ni NDIO!.. Lakini anayepaswa na kustahili kusujudiwa ni MUNGU PEKE YAKE!… Wengine waliosalia ambao ni wanadamu au malaika hatupaswi kuwasujudia hata kidogo.. Maandiko kwa kupitia kinywa cha Bwana wetu YESU KRISTO yanatufundisha hilo moja kwa moja..

Mathayo 4:8 “Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake,

9  akamwambia, Haya yote nitakupa, UKIANGUKA KUNISUJUDIA.

10  Ndipo Yesu alipomwambia, Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, MSUJUDIE BWANA MUNGU WAKO, UMWABUDU YEYE PEKE YAKE.

11  Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia”

Hivyo anayestahili KUSUJUDIWA ni Mungu peke yake sawasawa na maandiko hayo..

Lakini pia kusujudu na kuabudu ni lazima kufanyike katika roho na kweli ndivyo biblia inavyotufundisha, Kusujudu (kwa kuanguka chini) kunafaa sana kwa maombi ya Rehema na Toba, vile vile kwafaa sana kwa maombi ya maombi ya kupeleka mahitaji, kwani ni ishara ya unyenyekevu na kujishusha mbele za Mungu.

Na kusujudu si kanuni ya maombi, kwamba kila maombi ni lazima yaambatane na kusujudu, na kwamba usiposujudu basi maombi yako hayatasikiwa wala kukubalika,… bali ni tendo linaloambatana na msukumo wa kiungu na mzigo wa Roho Mtakatifu ndani.

Bwana atusaidie.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

FAIDA ZA MAOMBI.

UNAMFAHAMU MUNGU WA KWELI?

KWANINI MUNGU HAJIBU MAOMBI?

HUDUMA YA MALAIKA WATAKATIFU.

KUNA AINA NGAPI  ZA MAOMBI?

Rudi Nyumbani

Print this post