Je Bwana Yesu alikuwa na nywele ndefu?

Je Bwana Yesu alikuwa na nywele ndefu?

JIBU: Picha nyingi zinazochorwa kumweleza Yesu, takribani nyingi ya hizo  zinamwonyesha ni mtu mwenye nywele ndefu. Lakini Je uhalisia wake ni upi, ni kweli alikuwa na nywele ndefu au fupi?

Maandiko yanaeleza utamaduni wa wayahudi, kwa wanaume ilikuwa kuacha nywele zirefuke kama zile za mwanamke ni aibu kwa mtu huyo. Anajivunjia heshima kubwa.

1Wakorintho 11:14  “Je! Hayo maumbile yenyewe hayawafundishi ya kwamba mwanamume akiwa na nywele ndefu ni aibu kwake? 15  Lakini mwanamke akiwa na nywele ndefu ni fahari kwake. Kwa sababu amepewa zile nywele ndefu ili ziwe badala ya mavazi”

Hivyo hakukuwa na mtu aliyekuwa na nywele ndefu isipokuwa tu mtu aliyeitwa mnadhiri wa Mungu.

Lakini Je! Yesu alikuwa ni Mnadhiri ?

Kabla ya kufahamu kama Yesu alikuwa mnadhiri au la! Tufahamu kwanza mnadhiri alikuwa ni nani, na sheria ya mnadhiri ilikuwaje

Mnadhiri ni mtu aliyetengwa au aliyejitenga mwenyewe/ aliyejitoa wakfu kwa Mungu, kufuata na sababu binafsi, aidha kwa sababu ya shukrani yake ya kutendewa jambo Fulani kama vile kuponywa ugonjwa, au  kupatiwa mtoto, au kupata kitu Fulani kwa Mungu alichokuwa anamwomba. Hivyo katika agano la kale, kulikuwa na sheria ya mnadhiri. Na mnadhiri alikuwa yoyote Yule aidha mwanamke au mwanaume.

Sheria za mnadhiri ni zipi?

Kulingana na Hesabu 6:1-8

  1. Hakuruhusiwa kunywa divai, wala zabibu, wala juisi ya zabibu,  wala mbegu zake. Yaani kwa ufupi kitu chochote kilichomzao wa zabibu hakuruhusiwa kunywa
  2. Hakuruhusiwa kukata nywele zake, tangu siku hiyo aliyomwekea Mungu nadhiri mpaka atakapoitoa
  3. Hakuruhusiwa kugusa maiti. Hata kama ni ndugu yake wa karibu amekufa, baba yake au dada yake. Hakuruhisiwa  kufanya hivyo
  4. Ni lazima awe mtakatifu kwa Bwana; Maana yake ajitenge na mambo yote yaliyo najisi kipindi chote awapo katika kiapo chake.

Katika biblia, kulikuwa na makundi mawili ya wanadhiri

  1. Wanadhiri wa daima: Hawa ni waliotengwa tangu tumboni mwa mama zao: Mfano wao alikuwa  ni Samsoni, Samweli, Yohana Mbatizaji.. Hawakukatwa nywele zao, lakini pia hawakunywa divai maisha yao yote.
  2. Wanadhiri wa muda: Hawa ni aidha waliamua wenyewe katika kipindi Fulani katika maisha yao waingie kwenye viapo hivyo kwa Mungu, yaani wamtumikie yeye daima mpaka kufa kwao, au waliokuwa na nadhiri za muda, ambapo pengine baada ya miezi miwili, au mwaka mmoja wanaiondoa na kwenda kunyoa nywele zao, na kuendelea kutumia mizabibu nk. Mfano wa Hawa alikuwa ni mtume Paulo, ambaye kipindi Fulani anashuhudia naye alikuwa na nadhiri hiyo.

Matendo 18:18  “Baada ya hayo Paulo akazidi kukaa huko siku nyingi, kisha akaagana na ndugu akaabiri kwenda Shamu; na Prisila na Akila wakaenda pamoja naye, alipokwisha kunyoa kichwa chake huko Kenkrea; maana alikuwa ana nadhiri”

Sasa tukirudi kwa Bwana Yesu.

Je! Na Yeye alikuwa ni mnadhiri?

Jibu ni hapana, kwasababu Bwana alikunywa mzao wa mzabibu.

Mathayo 26:29  Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.

Kuonyesha kuwa hapo kabla alikuwa anakunywa.

Soma pia  Mathayo 11:19, Na Yohana 2:1-12, inatupa picha alitumia mzao wa mzabibu. Halikadhalika aligusa maiti, (Marko 5:41), na zaidi ya yote Bwana hakufungwa na sheria za torati.

Hivyo kwa kifupisho ni kwamba Bwana Yesu hakuwa na nywele ndefu, yawezekana alikuwa na nywele nyingi lakini hazikuwa ndefu kama za mwanamke, mfano wa aonekanavyo kwenye baadhi picha zinazochorwa.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

JE! NYWELE ZAKO ZINAOTA AU ZIMESIMAMA?

WINGU KUBWA LA MASHAHIDI.

Je! sheria ilikuwaje dhaifu kwasababu ya mwili? (Warumi 8:3)

NGUVU YA MNADHIRI WA BWANA.

MAUTI NA KUZIMU ZIKAWATOA WAFU WALIOKUWAMO NDANI YAKE.

Nini maana ya Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza (Yakobo 4:9)

Fahamu maana ya Mithali 29:4 “Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments