NAMI NINAZO FUNGUO ZA MAUTI, NA ZA KUZIMU.

NAMI NINAZO FUNGUO ZA MAUTI, NA ZA KUZIMU.

Ufunuo 1: 17 “…Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho,

18 na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu”.

Hayo ni Maneno ya Bwana wetu Yesu Kristo, akiliambia kanisa.. Sasa ukiona mpaka Bwana Yesu anasema anazo funguo za mauti, na kuzimu, ni dhahiri kuwa hapo mwanzo hakuwa nazo, zilikuwa kwa mwingine..Na huyo si mwingine zaidi ya Ibilisi.

Kumbuka Tahadhari ya kwanza Mungu aliyowapa Adamu na Hawa pale Edeni, kuhusu kula Tunda, haikuwa kwamba matokeo yake watakuwa uchi, au watajua mema na mabaya au watakula kwa jasho, au watazaa kuwa uchungu . Hapana, bali tahadhari aliyowapa ya kwanza na ya mwisho ilikuwa ni kuwa WATAKUFA(‘KIFO’)..Siku watakapokula matunda ya mti ule watakufa..akimaanisha watakufa kweli kweli..sio kwamba watakufa halafu siku moja watafufuka hapana, bali watakufa moja kwa moja..

Kwasababu Mungu alimwona muhasisi wa kifo hicho pale Edeni, Lakini wazazi wetu hawakuzingatia hilo badala yake wakala, Na matokeo yake ndio yale tuliyoyaona yalifuata baada ya pale..watu wakawa na makao mengine, baada ya pale yaliyoitwa KUZIMU. Chini ya mungu wao mpya aliyeitwa Ibilisi.

Na ndio maana katika agano la kale, hakukuwa na mtu aliyekuwa na uhakika wa maisha baada ya kifo, ni waisraeli tu ndio walifahamu hilo, nao si wote, isipokuwa wale tu waliokuwa wanafuatailia masuala ya Mesiya, ambaye alitabiriwa kuwa huko mbele atakuja kuwafufua wafu, lakini wengine waliosalia hawakujua hilo…

Na ndio maana tena utaona kulikuwa na mapambano makali kati ya mafarisayo na masadukayo, wengine waliamini kuna ufufuo wa wafu, na wengine hawakuamini hicho kitu (Soma, Matendo 4;1-2,23:7-8, Marko 12:18)..Ni kwasababu gani? Ni kwasababu suala la wafu kufufuliwa lilikuwa si jambo lililoandikwa kwa uwazi sana katika maandiko kama wengi wanavyodhani.. isipokuwa tu waliotambua jambo hilo ni wale waliokuwa wanafuatilia habari za Mesiya kuwa atakuja kufanya jambo hilo.

Kwahiyo wakati wote huo watu walikuwa wametawaliwa na roho ya mauti ya ibilisi.

Warumi 5:14 “walakini mauti ilitawala tangu Adamu mpaka Musa, nayo iliwatawala hata wao wasiofanya dhambi ifananayo na kosa la Adamu, aliye mfano wake yeye atakayekuja”.

Unaona wakati huo wote shetani alikuwa na funguo hizo, alikuwa wakati mwingine anao uwezo hata wa kuwaendea wafu walio watakatifu na kuzungumza nao, soma habari za samweli(1Samweli 28)..

Lakini sasa Kristo alipokuja alipindua kila kitu,(majira yakageuka), kwanza aliiondoa hofu ya mauti ambayo ilikuwa imewatawala wanadamu kwa muda mrefu tangu zamani..

Waebrania 2:14 “Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi,

15 awaache huru wale ambao kwamba maisha yao yote kwa hofu ya mauti walikuwa katika hali ya utumwa”.

Na pili akaiteka ile Kuzimu iliyokuwa chini ya shetani, ambayo ndio ilikuwa makao ya wafu wote…

Na ndio maana siku ile alipokufa tu, utasoma makaburi yalipasuka na watakatifu wengi wakatoka makaburini

Mathayo 27:51 “Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka;

52 makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala;

53 nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi”.

Tangu huo wakati hadi leo ibilisi hajui wafu wapo wapi na wanafanya nini saa hii, anachojua tu, ni kuwa wale watakatifu wapo upande wa PEPO(Paradiso) na wale waovu wapo sehemu ya mateso (Jehanum)..Hana uwezo wa kuleta mzimu wa mtu yeyote aliyekufa kwasababu sasahivi Kristo ndiye anayewamiliki walio hai na waliokufa soma Warumi 14:9. Kwahiyo hivyo vinavyoonekana na watu vyenye sura kama za wapendwa waliokufa..kiuhalisia sio wale watu wenyewe, bali ni roho tu za mapepo zilizovaa sura za watu waliokufa…

Kristo sasa ameshashikilia mamlaka yote, ya mbinguni, ya duniani na ya kuzimu..Haleluya.

Hivyo ikiwa wewe ni mtakatifu, kama utakufa leo basi ujue roho yako na nafsi yako itakwenda sehemu salama, yenye raha na pumziko la kweli, mahali pasipoelezeka panapoitwa Pepo, lakini wewe ambaye ni mwenye dhambi, ukifa leo, shetani hakuchukui bali utakayekuchuwa na Mungu mwenyewe na kwenda kukutupa katika jehanamu ya moto ukingoja hukumu ya siku ile ya mwisho..

Unatanga tanga nini kwa waganga wa kienyeji? Hao hawatakusaidia chochote, unawatafuta wanadamu, hao nao hawawezi kukuondolea hofu ya mauti na mashaka uliyonayo sasa, kwamba ukifa utakwenda wapi..Anayeweza kufanya hivyo ni Kristo tu peke yake, mwenye funguo za mauti na kuzimu.Yeye ndiye atakayeweza kukufanya uwe huru na hofu ya kifo, kiasi kwamba hata ikitokea unakufa leo, utakuwa na uhakika kuwa roho yako imekwenda sehemu salama. Ukingojea siku ile kuu ya kwenda mbinguni kwa Baba.

Hivyo leo mpe Kristo maisha yako kama bado hujampa, vivyo hivyo kama ni vuguvugu huu ni wakati wa kuwa moto!.. Tubu dhambi zao kwa kumaanisha kuziacha, hizi ni nyakati za mwisho, parapanda italia wakati wowote, na Yesu atawafufua kwanza wale waliokufa katika haki nao kwa pamoja na sisi tulio hai tutakwenda kumlaki mawinguni,..lakini jiulize wewe mwenye dhambi utakuwa wapi siku hiyo?..Au ukifa leo hii ni nani atayekusaidia huko uendako? Shetani anaivizia roho yako kwasababu anajua ukifa katika dhambi ni umepotea kwelikweli hata yeye mwenyewe hata kuona milele…Hivyo acha leo ulevi, wizi, rushwa, anasa, uasherati, vipodozi unavyopaka, vimini unavyovaa, matusi unayotukana na mambo yote yanayofanana na hayo..Na upokee Roho Mtakatifu ambaye ni ahadi kwetu tutakaomwamini Yesu.

Uamuzi ni wako, tafakari tena kisha chagua uzima. Wokovu ni bure kwa wote wanaouhitaji..Kristo anaokoa kweli.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

TOFAUTI KATI YA HEKALU, SINAGOGI NA KANISA NI IPI?

Nifanye nini ili niondokane na Hofu maishani mwangu?

SI KWA FAIDA YA MWENYEZI, BALI KWA FAIDA YETU.

MWAKA WA BWANA ULIOKUBALIWA.

NAO WAKADHANI YA KUWA YUMO KATIKA MSAFARA;

Nini maana ya maneno haya ya Bwana? “Nami nikiinuliwa juu ya nchi,NITAWAVUTA WOTE KWANGU”(Yohana12:32).

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Anonymous
Anonymous
2 years ago

Amen