NAO WAKADHANI YA KUWA YUMO KATIKA MSAFARA;

NAO WAKADHANI YA KUWA YUMO KATIKA MSAFARA;

Bwana wetu Yesu Kristo asifiwe ndugu yangu..

Nyakati hizi za mwisho tunazoishi sasa, ni nyakati ambazo zinakithiri kuwa na mseto wa watu wengi wanaojiita wakristo, leo hii ni rahisi kuona hata msanii wa kidunia anaimba nyimbo za Injili, ni rahisi kuona, mashoga wanatoa michango ya kujenga makanisa makubwa ulaya, wazinzi wanahudhuria kila jumapili ibadani, wengine mpaka wapo tayari kushiriki meza ya Bwana bila hofu nao wanaona ni kawaida tu. Ni kundi kubwa lenye mchanganyiko wa kila aina ya watu, wengine hawana hata mpango wa kufikiria maisha yao baada ya hapa, kinachowapeleka kwa Mungu tu, ni pengine waponywe waondoke, wengine wapate tu wachumba, wengine biashara zao ziende vizuri..basi hakuna cha zaidi baada ya hapo

Na wachache sana ndio wanaoutafuta wokovu wa kweli, ambao wapo tayari kumtii na kumfuata Yesu pale alipo yeye..

Embu leo kwa ufupi tuone habari moja ambayo, pengine unaijua sana, lakini tuiangalie kwa jicho lingine la ndani zaidi na naamini tutajifunza kitu kipya..

Na habari yenyewe ni ile ya Yesu akiwa bado kijana mdogo, alipokwenda na wazazi wake Yerusalemu kuila pasaka ya kila mwaka.. Lakini kama tunavyoijua habari baada ya sikukuu kuisha, ulipofika wakati wa kila mtu kurudi nyumbani kwake na katika taifa lake, wale waliotokea katika mikoa ya karibu kule Israeli walianza safari ya kurudi makwao, na wale waliotokea mataifa mengine ya mbali nao pia walianza kurejea makwao..

Lakini mambo yalikuwa tofauti kwa Bwana Yesu, yeye alibaki nyuma, wala hakuambata na makutano kurudi makwao, kama watu wengine walivyofanya, na kibaya zaidi hata wazazi wake hawakulijua hilo, wao wakakisia tu labda atakuwa katikati ya makutano wakirejea naye nyumbani…(Hilo ndio kosa linalofanywa na watoto wengi wa Mungu)

Luka 2:44 “Nao wakadhani ya kuwa yumo katika msafara; wakaenenda mwendo wa kutwa, wakawa wakimtafuta katika jamaa zao na wenzao;

45 na walipomkosa, wakarejea Yerusalemu, huku wakimtafuta.

46 Ikawa baada ya siku tatu wakamwona hekaluni, ameketi katikati ya waalimu, akiwasikiliza na kuwauliza maswali.

47 Nao wote waliomsikia walistaajabia fahamu zake na majibu yake.

48 Na walipomwona walishangaa, na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni.

49 Akawaambia, Kwani kunitafuta? Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu”?

Kama tunavyoona hapo, ni wazazi wake tu pake yao, ndio waliokuwa walau wanamfikiria  Yesu katikati ya ndugu zao wengi walioambatana nao, na walipoona Kristo hayupo katikati ya makutano, katikati ya wingi wa watu, katikati ya ndugu, katikati ya marafiki, katikati ya majirani, katikati ya wageni wa mataifa mengine, ndipo ikiwapasa wageuke wajaribu kwenda kuanza kumtafutia kule walipompotezea Yerusalemu.. ndipo wakamkuta yupo hekaluni katikati ya WAALIMU..

Na ni kama bahati tu walipita hekaluni, lakini kama wasingeingia kule, kamwe wasingemwona daima, wangehangaika Yerusalemu nzima wasingempata kwa muda mrefu sana..

NI KIPI MUNGU ANATAKA TUJIFUNZE?

Wakristo wachache wa leo hawajui kuwa, wapo katikati ya kundi kubwa la wakristo vuguvugu, linaloondoka mbali na mafundisho ya kweli ya Neno la Mungu.. na ndio maana wanapojaribu kumtafuta Kristo katikati yao ni kama vile hawamuoni, lakini wao bado wanataka kuendelea kutembea nao tu, hawajui kuwa kwa jinsi wanavyozidi kukaa nao ndivyo wanavyozidi kumpoteza YESU wasimpate kabisa..

Ndugu geuka kama ni wewe,..angalia ulipotoka, kule mlipotoka ndipo Kristo yupo,..Na! ulipotoka ni wapi?? Ni katikati ya waalimu, kule Kristo alipo, na waalimu makao yao huwa ni wapi?..Makao yao ni darasani sikuzote, wakiwafundisha wanafunzi, na hapo ndipo makao ya Kristo yalipo siku zote..

Hutampata sehemu nyingine yoyote, hutampata, kwenye michezo, maombezi, hutampata kwenye matamasha, hutampata kwenye taasisi za kidini, wala hutampata kwenye dhehebu lolote, wala katikati ya ndugu zako, au rafiki zao, au majirani zako, huko kote utapotea, Kristo hatembei katikati ya misafara ya watu wanaosafiri mbali na yeye bali Kristo utamwona PALE NENO LAKE LINAPOFUNDISHWA BASI..

Ukiona hupendi tena kujifunza Neno la Mungu basi ujue, upo mbali sana na Kristo kwa mujibu wa biblia, ukiona huna muda wa kusoma biblia, usijidanganye utakaa umwone Kristo akijifunua kwako, ukiendelea kudhani Kristo yupo katika msafara unaouona leo hii, wimbi la watu wengi wanaosema tumeokoka, lakini Neno la Mungu hawalifuati, ni wavivu katika kutamani kumjua Mungu, ukiwauliza habari ya unyakuo kwao ni kama habari mpya za kuchosha, ukiwauliza, habari za kwenda mbinguni kwao ni kama hadithi za kizee, muda wote ni kujionyesha tu, na kujisifia wameokoka, lakini biblia ni kama kitabu cha ziada tu kwao basi ujue wamempoteza Kristo katikati yao..

Bwana atusaidie nyakati hizi za hatari tusimpoteze yeye aliye mwamba wa wokovu wetu..

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

NI NANI ALIYEWALOGA?

NI NANI ALIYEWAONYA KUIKIMBIA HASIRA ITAKAYOKUJA?

https://wingulamashahidi.org/mafundisho-ya-ndoa/

JE YESU ATARUDI TENA?

Biblia inamaana gani kusema;aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi?

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
5 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Meckson William
Meckson William
8 months ago

Barikiweni na Bwana YESU Kwa mafundisho haya mazuri Neema ya MUNGU izidi kuwa pamoja na sote katika kutafakari neno lake Amina.

john mwanganda
john mwanganda
1 year ago

Kazi nzuri Jehova kupitia Roho wake mtakatifu azidikuwafunulia siri zaidi za neno lake amen

josphat muthuri
josphat muthuri
3 years ago

mungu asifiwa watu wa mungu,kwa kuwa ili neno liko tofauti na la dini yingi hapa nchini mwetu alafu namber yenu ya simu +255 kwetu ni +254 kama yangu +254712143154 au +254715473500