Category Archive Mafundisho

TOFAUTI KATI MAASKOFU, MASHEMASI, WAZEE WA KANISA NI IPI?

Katika kanisa, Mungu aliweka huduma mbalimbali, karama mbalimbali, na utendaji kazi tofauti tofauti, ili kulikamilisha kanisa lake na kuupanda ufalme wake duniani kama alivyokusudia.

Sasa katika upande wa huduma, Mungu aliziweka huduma kuu tano, ambazo zenyewe zinasimama kama kuliongoza kanisa, kulikuza, kulichunga, ni kama nguzo za kanisa ambazo husimama wakati wote, Nao ni;

Mitume, manabii, wainjilisti, wachungaji na waalimu. (Waefeso 4:10-12)

Kwa urefu wa maelezo ya huduma hizo jinsi zinavyotenda kazi basi bofya hapa upitie >>> TOFAUTI YA MITUME, MANABII, WAINJILISTI, WACHUNGAJI NA WAALIMU NI IPI?

Lakini sambamba na hizo aliweka wengine katika kanisa, wanaoshirikiana na hawa watano (5).

Ambao ni  WAZEE WA KANISA, MAASKOFU na MASHEMASI

Tuangalie kazi ya kila mmoja;

1) WAZEE:

Tamaduni za kiyahudi tangu zamani walikuwa na desturi ya kuteuwa wazee (watu waliokomaa kiumri), wenye hekima na busara na uzoefu wa Kidini  kufanya maamuzi na Kutoa hukumu mbalimbali katikati ya jamii ya wayahudi Soma (Kutoka 3:16, Kumbukumbu 1:9-18)

Hata baadaye kanisa lilipokuja kuanza, nyakati za mitume, tunaona bado walirithi utaratibu huo katika nafasi za kiuongozi ndani ya kanisa. Isipokuwa haikuhitaji awe ni lazima mzee Kiumri, lakini ni lazima Awe amekomaa Kiroho.

Nafasi hii hasaa iliwahusu wanaume, Kwasababu katika nyaraka za mitume hatuoni mahali popote kama kuna mfano wa mwanamke aliyeteuliwa kuwa  mzee wa kanisa.

Ukisoma Tito 1:6, inaeleza sifa zao, anasema wazee wawe waume wa mke mmoja..

Tito 1:5-6

[5]Kwa sababu hii nalikuacha Krete, ili uyatengeneze yaliyopunguka, na kuweka wazee katika kila mji kama vile nilivyokuamuru;

[6]ikiwa mtu hakushitakiwa neno, naye ni mume wa mke mmoja, ana watoto waaminio, wasioshitakiwa kuwa ni wafisadi wala wasiotii.

(Matendo 14:23)

Zingatia: Hii haiwafanyi wanawake wasiwe na kazi yoyote katika kanisa hapana, wanaweza kusimama kama huduma-kivuli ambazo zaweza Kuonekana kama za wazee wa kanisa, waalimu, mashemasi, kama wasaidizi wenye huduma hizo, lakini sio rasmi kwao. Mfano wa hawa kwenye biblia walikuwa ni akina Fibi, prisila,

KAZI ZA WAZEE WA KANISA:

1). Kulichunga kundi,

Matendo 20:28

Jitunzeni nafsi zenu, na lile kundi lote nalo, ambalo Roho Mtakatifu amewaweka ninyi kuwa waangalizi ndani yake, mpate kulilisha kanisa lake Mungu, alilolinunua kwa damu yake mwenyewe.

(Soma pia 1Petro 5:1-4)

ii) Kufundisha vema watu. 

1 Timotheo 5:17

[17]Wazee watawalao vema na wahesabiwe kustahili heshima maradufu; hasa wao wajitaabishao kwa kuhutubu na kufundisha.

Tito 1:9

[9]akilishika lile neno la imani vile vile kama alivyofundishwa, apate kuweza kuwaonya watu kwa mafundisho yenye uzima, na kuwashinda wenye kupinga.

iii) Kutatua migogoro ya kiimani ndani ya kanisa.

Utakumbuka wakati ule makanisa ya mataifa yalikuwa yakitaabishwa, na wayahudi juu ya kushika torati, hivyo  kukatokea mkanganyiko mkubwa, na kuwalazimu wawafuate wazee kule Yerusalemu ili walitatue tatizo hilo, na kama tunavyosoma baada ya hoja nyingi, walifikia hitimisho sahihi la Roho Mtakatifu.

Matendo 15:6 Mitume na wazee wakakusanyika wapate kulifikiri neno hilo.

7 Na baada ya hoja nyingi Petro akasimama, akawaambia, Ndugu zangu, ninyi mnajua ya kuwa tangu siku za kwanza Mungu alichagua miongoni mwenu ya kwamba Mataifa walisikie neno la Injili kwa kinywa changu, na kuliamini

iv) Kuwaombea wagonjwa.

Yakobo 5:14-15

[14]Mtu wa kwenu amekuwa hawezi? Na awaite wazee wa kanisa; nao wamwombee, na kumpaka mafuta kwa jina la Bwana.

[15]Na kule kuomba kwa imani kutamwokoa mgonjwa yule, na Bwana atamwinua; hata ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.

2) MAASKOFU.

Maana ya Askofu ni mwangalizi.

Kazi yake kubwa ni kuliangalia kanisa,/ kulisimamia, mfano kusimamia malengo ya kikanisa, kulinda fundisho, na kusimamia uchungaji ulio bora.

Japokuwa mahali pengine maaskofu wanatajwa kama wazee wa kanisa. (Tito 1:5-9).

Lakini tofauti yao hasaa ni kwamba wazee wanayasimamia makanisa madogo madogo, lakini maaskofu ni waangalizi wa makanisa (yote/baadhi), Wazee wanaweza kuwa wengi, lakini maaskofu ni cheo, cha uangalizi hivyo aweza kuwa mmoja au wachache, wazee wanaweza kuwa na wajibu wa kufundisha, na kuchunga, lakini maaskofu hasaa katika kuongoza. Vilevile kwenye maandiko hatuoni mahali popote nafasi hii ikihusisha wanawake.

Sifa za maaskofu na wazee, wa kanisa zinafanana.

Sifa za mtu kuwa mzee wa kanisa. (Tito 1:5-9, 1Timotheo 3:1-7)

  1. Awe mtu asiyelaumika
  2. Awe Mume wa mke mmoja,
  3. Mwenye kiasi
  4. Mwenye busara
  5. Mtu wa utaratibu
  6. Mkaribishaji
  7. Ajuaye kufundisha
  8. Si mtu wa kuzoelea ulevi
  9. Si mpiga watu
  10. Awe mpole
  11. Si mtu wa kujadiliana
  12. Asiwe mwenye kupenda fedha
  13. Awezaye kuisimamia nyumba yake vema
  14. Asiwe mwongofu mpya.

3) MASHEMASI.

Mashemasi ni mtumishi wa kanisa.  Huduma hii ilitokea katika kanisa kwa mara ya kwanza, mitume walipokuwa wanahudumu na kuona kuwa baadhi ya mapungufu kwamba wajane wanasahaulika katika huduma ya kila siku, ndipo ikalazimika wateue watu saba, ndani ya kanisa watakaoweza kusimamia mambo yote ya kimahitaji ya kundi.  (Matendo 6:1-7), mmojawapo alikuwa ni Stefano.

Kazi za mashemasi:

i) Kulihudumia kundi katika masuala ya mahitaji ya mwilini ya kundi:

Hususani kwa maskini, wajane, wenye mahitaji,  mayatima.

ii) Kuongoza kwa mifano:

Lazima wawe kipaumbele kitabia, uaminifu, na nidhamu Na kuonyesha roho ya kiutumishi

iii) Kusimamia shughuli za kikanisa:

Ujenzi, taratibu za kiibada na mikutano, kusimamia hazina na mali za kanisa.

Sifa za mtu kuwa shemasi:

Zinatajwa kwenye 1Timotheo 3:8

1Timotheo 3:8 Vivyo hivyo mashemasi na wawe wastahivu; si wenye kauli mbili, si watu wa kutumia mvinyo sana,si watu wanaotamani fedha ya aibu.

9 wakiishika siri ya imani katika dhamiri safi. 10 Hawa pia na wajaribiwe kwanza; baadaye waitende kazi ya shemasi, wakiisha kuonekana kuwa hawana hatia.

11 Vivyo hivyo wake zao na wawe wastahivu; si wasingiziaji; watu wa kiasi, waaminifu katika mambo yote.

12 Mashemasi na wawe waume wa mke mmoja, wakiwasimamia watoto wao vizuri, na nyumba zao.

13 Kwa maana watendao vema kazi ya shemasi hujipatia daraja nzuri, na ujasiri mwingi katika imani iliyo katika Kristo Yesu

Hivyo wazee, maaskofu na mashemasi, ni nguzo muhimu za kulifanya kanisa kusimama, katika nidhamu ya kitabia na kimapokeo, pamoja na kihuduma.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

ZIFAHAMU KARAMA 9 ZA ROHO MTAKATIFU NA UTENDAJI KAZI WAKE.

Je huduma za mitume na manabii, zinaendelea kufanya kazi hadi sasa?

JINSI BWANA ALIVYOWACHAGUA MITUME WAKE.

Print this post

IFAHAMU NGUVU YA MAOMBI (Sehemu ya pili)

Maombi ya shabaha kwaajili ya Kazi/kibarua/shughuli/biashara/elimu.


UTANGULIZI: Ni muhimu kujua hili: lengo kuu au kiini cha Wokovu ulioletwa na BWANA YESU KRISTO sio sisi tuwe matajiri au tupate mafanikio ya huu ulimwengu!.

Mafanikio ya dunia hii ni moja ya faida za mwisho mwisho kabisa za kusudi la msalaba wa Bwana YESU kwasababuwalikuwepomatajiri kabla ya Bwana YESU kuja duniani, hivyo KRISTO asingeweza kuja kutegua mtego aukutatua tatizo ambalo lilishatatuliwa huko nyuma.

Ingekuwa lengo lake ni ili tufanikiwe tuwe matajiri, angetuambia tu tusikilize hekima za Sulemani na tungefanikiwa, hakukuwa na haja ya kuja kumwaga damu yake.

Lakini suala la ondoleo la dhambi hilo halikuwahi kufanyika huko nyuma, hakuna aliyewahi kuondolewa dhambi, kwani dhambi zilikuwa zinafunikwa tu! (Soma Waebrani 10:3-4)..

Sasa hiko ambacho kilishindikana kutendeka huko nyuma (katika Agano la kale) ndicho kilichokuwa cha kwanza na cha msingi kilichomleta BWANA YESU duniani, na kitu hiko si kingine zaidi ya ONDOLEO LA DHAMBI.…kiasi kwamba mtu akikosa ondoleo la dhambi hata awe na vitu vyote ulimwenguni bado anayo hasara kubwa soma (Mathayo 16:26).

Kwahiyo ni muhimu kujua msingi huu, ili tunapokwenda kujifunza juu ya MAOMBI JUU YA KAZI au BIASHARA, Usiweke moyo wako wote huko!.. Yatumie tu maarifa haya kama sehemu ya maisha, lakini jali zaidi hatima ya roho yako, kupitia damu ya YESU na UTAKATIFU.

Sasa tukirudi katika kiini cha somo!.. Ikiwa unafanya kazi za mikono, labda tuseme biashara, tumia kanuni hii ya Maombi kupata FAIDA YA KILE UNACHOKIFANYA!!.

Badala ya kuombea bidhaa zako, kama sabuni unazouza, au dawa unazouza, au kingine chochote kwamba kiwe na mvuto, kuanzia leo punguza kuomba maombi ya namna hiyo, badala yake omba maombi yafuatayo.

– Kila mteja anayekuja kwako mwombe neema ya Wokovu, ikiwa bado hajampokea YESU, maombi ya namna hiyo yanamtoa yule mtu kutoka katika vifungo vya ibilisi na hatimaye kumfungua kabisa, na anapofunguliwa aweza kuwa mteja wako wa ajabu sana, au akawaleta na wengine wengi mahali ulipo.

– Ikiwa tayari ameshampokea YESU mwombee azidi kusimama katika imani, na mwombee akawe Nuru kwa wengine wengi, ombea na familia yake kama unaijua, hiyo ndio njia bora ya kuombea kazi yako au biashara yako..

– Unafanya biashara ya chakula, na wateja wako ni watu wa kidunia, badala ya kuombea madishi na chakula unachokipika kwamba wakipende, hebu waombee wampende YESU, halafu uone kama hiko chakula chako hawatakipenda, zaidi ya vyakula vya wengine wote.

– Pale ofisini acha kuombea uso wako kwamba upate kibali, sawa waweza kuomba hivyo, lakini isizidi sana kiasi kwamba hujui kitu kingine cha kuomba zaidi ya hicho, badala yake anza kuomba watu wa ofisini kwako wamjue MUNGU, wakimjua MUNGU wewe utapata kibali tu!, wala hutatumia nguvu nyingi.

– Pale shuleni acha kuombea walimu wakupende, hebu waombee wamjue YESU na kumpenda, halafu uone kama hawatakupenda na wewe.

– Unauza bidhaa, waombee wateja wako wamjue YESU na kumpenda zaidi ya bidhaa zako, halafu uone matokeo.

Ukitaka kufunga kwaajili ya biashara yako!, Funga kwa maombi ya kuwaombea wateja wako wokovu na Neema zaidi, kama unayo list, anza mmoja baada ya mwingine, wapatanishe na KRISTO hivyo uone kama KRISTO pia hatakupatanisha nao, utaona kazi zako zinaenda, shule yako inaenda, biashara yako inaenda, kazi yako inaenda.

Lakini ukijikita tu kuziombea bidhaa kama vile waganga wanavyotoa dawa za kwaajili ya biashara, matokeo yake yatakuwa ni madogo sana.

Hivyo OMBA lakini omba kwa shabaha/target.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

IFAHAMU NGUVU YA MAOMBI:

MWONGOZO WA MAOMBI YA FAMILIA

KWANINI MUNGU HAJIBU MAOMBI?

Mistari ya biblia kuhusu maombi.

MWONGOZO WA MAOMBI YA WAHUDUMU/ WASIMAMAO MADHABAHUNI.

Print this post

VUNJA MADHABAHU, ANGUSHA NGUZO, KATA ASHERA NA CHOMA SANAMU.

Haya ni mambo manne yanayopalilia matatizo kuanzia ngazi ya kifamilia mpaka ya kitaifa!. (Madhabahu, Nguzo, Ashera na Sanamu).


Kumbukumbu 7:5-6 “Lakini watendeni hivi; zivunjeni madhabahu zao zibomosheni nguzo zao, yakateni maashera yao, ziteketezeni kwa moto sanamu zao za kuchonga.

6 Kwa maana wewe u taifa takatifu kwa BWANA, Mungu wako; BWANA Mungu wako, amekuchagua kuwa watu wake hasa, zaidi ya mataifa yote walioko juu ya uso wa nchi”

Labda utauliza mambo haya ni mambo gani kwa undani wake na yanaathiri vipi maisha.

   1. Madhabahu:

Madhabahu ni mahali popote panapotolewa dhabihu (sadaka).

Sadaka ina nguvu, ndio maana hakuna mganga anayetoa huduma bila sadaka,

Sasa si kwamba sadaka anahitaji tu  kwaajili ya mahitaji yake..La! bali anajua uchawi wake hautafanya kazi ipasavyo pasipo sadaka, kwahiyo madhabahu ni mahali mahususi kwa sadaka..

Katika biblia BWANA MUNGU aliwaagiza wana wa Israeli wazivunje madhabahu za wakaanani..

Na zilikuwa ni nyingi na za aina tofauti tofauti…na pasipo kuchagua waliambiwa wazivunje zotewasibakishe hata moja, kwani zitakuwa ni chanzo cha matatizo..

Ikimaanisha kuwa madhabu za mashetani ni za kuvunja si za kuziacha, kwani zinapeleka harufu mbaya mbele za MUNGU, na hivyo kuleta matatizo mengi…

Ikiwa kuna mahali ipo madhabahu wanapotolea sadaka karibu nawe, na hiyo madhabahu inakuhusu kwa namna moja au nyingine (kimila), ivunje bila kuogopa!..kama alivyofanya Gideoni, usiiache kwani yaweza kukuletea matatizo.

     2. NGUZO

Nguzo ni miimo ya Mahekalu ya ibada, yaweza kuwa Hekalu la MUNGU (soma 1Wafalme 7:21 na Mwanzo 28:22),  au yaweza kuwa hekalu la mashetani (Soma 2Wafalme 10:26-27).

Maana yake mahali popote penye msingi wa hekalu la miungu ni lazima pabomoshwe.

   3. ASHERA.

Ashera ni miti na maua yaliyokuwa yanazunguka mahekalu ya miungu, ambapo mimea hiyo iliaminika na kuabudiwa kama sehemu ya miungu.

Bwana aliwaambia wana wa Israeli wakate-kate maashera yote lisibaki hata moja (Kutoka 32:12-14).

Hali kadhalika yapo maashera hata sasa, utakuta upo mti fulani unaaminika kama ni wa kiungu na watu wanaenda kufanya matambiko hapo (hiyo ni ashera), ni ya kukata, wengine si miti bali maua tu…

Ondoa maashera katika nyumba yako, ondoa katika nyua yako na uzio wako kwani yaweza kuwa chanzo cha matatizo mengi.

   4. SANAMU.

Sanamu ni kitu chenye umbile la mtu kinachowekwa katika mahekalu na kuabudiwa.

Hizi nazo Bwana aliagiza zichomwe moto,

Sasa swali linakuja, vipi kama Madhabahu hizi, na ashera, na nguzo na sanamu zipo mbali?.

Kama zipo mbali na upeo wa kuzifikia, tunazo silaha zinazosafiri masafa marefu zaidi ya silaha zote zilizowahi kutengenezwa na mwanadamu au zitakazokuja kutengenezwa.

Silaha hiyo ni Maombi.

Maana yake katika maombi Unazivunja madhabahu kwa Imani, unaangusha Nguzo kwa imani, unakata maashera kwa imani, na unazichoma moto hizo sanamu kwa imani kupitia jina la YESU.

Na kwa jinsi utakavyotamka, zitateketea kule zilipo kwa namna hiyo hiyo, lakini usiingie kwenye maombi ya vita kama wewe si askari mwenye silaha hizi za Waefeso 6:10-15.(utajitafutia matatizo zaidi).

Pia usiache kuzibomoa kwa mikono yako kama zipo mbele ya upeo wa macho yako. (Upo unaziona sio tu kuombea, bali kuzimoa kwa mikono kabisa).

Ukifanya hivyo utakuwa umeusafisha uwanda, hakuna laana juu ya mahali ulipo.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

IFAHAMU NGUVU YA MAOMBI.

Sehemu ya kwanza.

Zaburi 66:20 “Na ahimidiwe Mungu asiyeyakataa maombi yangu, Wala kuniondolea fadhili zake”.

Maombi ni zaidi ya silaha yoyote ile yenye ubora inayofahamika, leo nataka tujifunze kupitia mfano mdogo sana wa simu ya mkononi.

Kawaida ili uweze kuongeza uwezo wa simu yako, huna budi kujiunganisha na internet..

Vichochezi

Internet ni mtandao usiookana kwa macho, unaoratibu mawasiliano ya haraka na taarifa za haraka.

Sasa simu yako inapoungwa na internet ndipo unapoweza kupakua (kudownload) vichocheo vya simu vinavyoitwa application.

Applications zile zinasaidia kuongeza uwezo wa simu yako..

Kama unataka simu yako iweze kusoma baadhi ya makala unahitaji kichocheo husika cha kusomea makala hizo.

Vile vile kama unahitaji simu yako iwe na uwezo wa kucheza nyimbo kwa mpangilio, itakugharimu kupakua (download) vichocheo hivyo n.k

Simu zenye vichocheo (applications) nyingi mbalimbali ndizo zenye uwezo mkubwa..na zile zisizo na vichocheo kabisa huwa zina uwezo mdogo na changamoto nyingi.

Sasa na mwili wa Mtu ni hivyo hivyo, kuna mambo hatuwezi kufanya wala kuwa nayo pasipo hivi vichocheo vinavyoongeza uwezo.

Kwamfano huwezi kusoma biblia na kuielewa kama hujaongezewa nguvu.. Utakuwa ukishika tu unalala!.

Huwezi kuhubiri kama hujaongezewa nguvu, utakuwa unaona aibu tu!.

Huwezi kuishi maisha masafi kama hujaongezewa nguvu utajaribu lakini utashindwa…n.k.

Sasa kazi ya Roho Mtakatifu ni kutuunganisha sisi na mtandao wa kimbinguni, kama vile simu inavyoungwa na internet.

Na tunapoungwa na mtandao wa kimbinguni basi tunaweza kupakua (download) vichocheo vya kimbinguni..

Na tunavipakua vichocheo hivyo kwa njia moja tu ya MAOMBI!.

Unapoomba maana yake unapakua (download) visaidizi vya kimbunguni, ambavyo vinakuongezea nguvu katika utu wa ndani.

KUMBUKA: Maombi hayakupi kitu! Balia YANAKUONGEZEA NGUVU YA KUFANYA NA KUPATA KITU.

Ndio maana baada ya maombi utaona ile nguvu ya kusoma Neno inaongezeka, ile nguvu ya kuhubiri inaongezeka, ile nguvu ya kushinda dhambi inaongezeka, ile nguvu ya kuendelea na wokovu inaongezeka..

Utaona ile nguvu ya kuendeleza maono yako inaongezeka,..ukiona hivyo jua ni vichochezi vya kimbinguni vimeingia ndani yako vinafanya kazi..HIYO NDIO NGUVU YA MAOMBI!!.

Na kawaida hata vichochezi vya simu (application) vinakuwa updated mara kwa mara, vivyo hivyo na mwombaji huwa haombi mara moja na kuacha, bali anakuwa na desturi ya kuomba mara kwa mara ili kuimarisha vichochezi vyake.

Lakini usipokuwa mwombaji, utabaki, hutaona mabadiliko yoyote katika eneo lolota la kiroho na kimwili…kila kitu kitakuwa kigumu hakiendi..

Na kama ulikuwa mwombaji na ukapunguza kuomba, na vile vichocheo pia vinapungua nguvu.

Anza kuwa mwombaji, kuna mambo hayawezekaniki pasipo maombi hususani yale ya mfungo.

Mathayo 17:21 “Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga”.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

NI KWA NAMNA GANI KRISTO ALIZIBEBA DHAMBI ZETU?

Ili kuelewa Msamaha wa dhambi jinsi unavyofanya kazi, kwamba ni kwa namna gani Bwana YESU alibeba dhambi zetu, twaweza kuelewa kwa kutafakari mfano huu mrahisi.

Katika sheria za Mahakama inapotokea mfungwa aliyehukumiwa  kifungo, akafariki katikati ya kifungo hiko, na ikathibitishwa na jeshi la magereza pamoja na ripoti za madaktari, na akazikwa basi kile kifungo chake kinakuwa kimefika mwisho, na kesi yake inakuwa haiendelei tena (inafutwa)..

Sasa ikitokea yule mtu akafufuka baada ya siku kadhaa anakuwa hana kesi tena (yupo huru) kwani  kesi yake ilishafutwa, kutokana na ripoti za mahakama na madaktari..

Na zaidi sana mahakama haziamini ufufuo, hivyo itaendelea kuamini kuwa yule mtu alishakufa na taarifa zilithibtishwa na jeshi la magereza pamoja na madaktari.

Sasa ni hivyo hivyo kwa Bwana YESU, yeye alikubali kubeba hatia zetu na makosa yetu yaliyo mengi na akakubali kuhukumiwa kama yeye ndiye aliyeyatenda yale makosa..

Lakini alipokuwa anaanza kukitumikia kile kifungo kwa mateso makali (ambayo kiuhalisia yamgekuwa ya daima)..alikufa katikati..

Na sheria ya hukumu ni kwamba kifo kinahitimisha kifungo cha Mtu, hivyo Kristo alipokufa kifungo chake cha adhabu na mateso kikafikia mwisho, akawa hana hatia tena wala ule mzigo wa dhambi (yupo huru na dhambi sawasawa na maandiko).

Warumi 6:7 “kwa kuwa yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi”

Lakini muujiza ni kwamba baada ya siku tatu akaonekana yu hai, na kwasababu hukumu yake ilishafutwa kwa kifo chake, akawa huru na kifungo hiko baada ya kufufuka, ndio maana hatuoni akilia kwa uchungu wa maumivu baadaa kufufuka, bali tunaona ana utukufu mwingi.

Kwahiyo laiti Kristo asingekufa angeendelea kuhesabika laana na mwenye hatia kwaajili ya dhambi zetu nyingi alizozobeba, ingempasa aendelee kukaa katika hali ya adhabu daima, na aendelee kutengwa na MUNGU daima.

Wagalatia 3:13 “Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti”

Lakini kifo chake kimehitimisha hukumu yake, ambayo sisi ndio tungepaswa tuitumikie.

Sasa tunapomwamini ndipo tunaingia katika huo mkondo wa kuondolewa dhambi..

Lakini tunapomkataa basi dhambi zetu zinabaki palepale..ni rahisi tu hivyo!.

Je umemwamini Bwana YESU?..Je umebatizwa kwa ubatizo sahihi wa Maji mengi na wa Roho Mtakatifu?.

Kama bado unasubiri nini?…je bado huoni tu gharama kubwa Bwana YESU aliyoingia kwaajili yetu ili tupate ondoleo la dhambi?.

Mpokee YESU leo wala usingoje kesho.

Maran atha!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

ELOI ELOI LAMA SABAKTHANI?

Zaburi 22:1 Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu, Na maneno ya kuugua kwangu? 2 Ee Mungu wangu, nalia mchana lakini hujibu Na wakati wa usiku lakini sipati.

Maneno haya ukiyatafakari, utagundua ni ya mtu aliyefikia hatua mbaya sana ya kukaribia kukata tamaa kwasababu ya aidha magumu, au huzuni, au mateso yasiyoelekeza anayoyapitia, akiangalia kulia, haoni  tumaini lolote, akiangalia kushoto haoni mkono wowote wa Mungu ukimsaidia licha ya kuomba na kulia sana, kwa muda mrefu.

Sehemu nyingine anasema, amekataliwa kila kona, amekuwa kama msikwao kwa ndugu zake.

Zaburi 69:10 Nilipolia na kuiadhibu roho yangu kwa kufunga, Ikawa laumu juu yangu.

11 Nilipofanya gunia kuwa nguo zangu, Nikawa mithali kwao. 12 Waketio langoni hunisema, Na nyimbo za walevi hunidhihaki. 13 Nami maombi yangu nakuomba Wewe, Bwana, Wakati ukupendezao; Ee Mungu, Kwa wingi wa fadhili zako unijibu, Katika kweli ya wokovu wako.

14 Uniponye kwa kunitoa matopeni, Wala usiniache nikazama. Na niponywe nao wanaonichukia, Na katika vilindi vya maji. 15 Mkondo usinigharikishe, wala vilindi visinimeze, Wala shimo lisifumbe kinywa chake juu yangu.

16 Ee Bwana, unijibu, maana fadhili zako ni njema, Kwa kadiri ya rehema zako unielekee. 17 Wala usinifiche uso wako, mimi mtumishi wako, Maana mimi nimo taabuni, unijibu upesi.

Mwandishi huyu alikuwa ni  Daudi, alipitia kipindi kirefu sana cha kujiona kama vile Mungu kamtupa, hadi kuna wakati akaona heri aende kuomba hifadhi kwa maadui zake wafilisti ambao hapo mwanzo aliwafukuza na kuwaita makafiri (wasio tahiriwa), lakini safari hii kwa unyenyekevu wote, anaenda kuwa mmoja wa askari wao, ili tu apate hifadhi, asiangamie kabisa. Huyo ni mtu ambaye maji ya shingo yalimfikia kwelikweli.

Sio kwamba alikuwa haombi, au hamlili Mungu?. Au kwamba ana dhambi kuliko wengine, mpaka awe mtu wa bahati mbaya hivyo Hapana, nyakati zote alikuwa mwombaji, lakini akafika mahali katika uhalisia wa kibinadamu aliona kama Mungu amemwacha kabisa.

Lakini kwasababu huruma za Mungu zilikuwa nyingi juu yake alimpa moyo mkuu, wa kuendelea kumngoja Bwana. Ndio maana  sehemu nyingi katika Zaburi anasisitiza sana Neno hili ‘mngojeeni Bwana’ (Zaburi 37:7, 25:3, 31:24,38:15, 40:1).

Sasa moja ya  maneno machache ya Daudi yaliyonikuliwa na Bwana Yesu lilikuwa ni hili.

Mungu wangu, Mungu wangu, Mbona umeniacha?

Mathayo 27: 45 Basi tangu saa sita palikuwa na giza juu ya nchi yote hata saa tisa.

46 Na kama saa tisa, Yesu akapaza sauti yake kwa nguvu akisema, Eloi, Eloi, lama sabakthani? Yaani, Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha?

Je! Unadhani kauli hiyo Yesu aliyoitoa alimaanisha kweli ameachwa?

Hapana, tangu mwanzo alikuwa anajua Mungu yupo pamoja naye, na kwamba saa yake imekaribia, muda si mrefu anakwenda kuinuliwa na kutukuzwa, tena sehemu nyingine anasema alishangalia pale msalabani (Wakolosai 2:15). Lakini kuinukuu kauli ile ni kuonyesha ubinadamu wetu, unavyoweza kutuhubiria tuwapo katikati ya shida, kwamba Mungu ametuacha hususani pale tunapopitia shida, na mateso.

Yesu alinukuu ubinadamu wetu kukumbuka mfano wa yale aliyoyapitia Daudi..

Lakini tunaona dakika chache baada ya pale, pindi tu alipokata roho, makaburi yakapasuka, wafu wakatoka makaburini, pazia la hekalu likapasuka, na baada ya siku tatu akafufuka, ukombozi wetu mkuu ukapatikana, ‘Lakini ni kwa maneno ya kudhaniwa kuwa Mungu amemwacha’.

Mathayo 27:50 Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake.

51 Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka;

miamba ikapasuka; 52 makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala; 53 nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi.

Ndugu, upitiapo hatua hizo ambazo mawazo yako yanakufundisha kuwa Mungu hayupo na wewe tena, amekuacha, kwasababu ya shida unazozipitia muda mrefu, magonjwa yasiyokoma, umeomba mpaka umechoka, umelia hadi ukomo,wewe ona ni kawaida,…. Piga moyo konde Mngojee Bwana. Daudi alistahimili hatimaye akathibitishwa kwenye ufalme ambao ulidumu pamoja na vizazi vyake vingi tofauti na wafalme wengine wa Israeli. Mngojee Bwana, kimaombi, kwasababu baada ya joto huja mvua.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KWANINI YESU ALIMUITA BABA YAKE “ABA”?

kiaramu ni lugha gani? je ilizungumzwa na Yesu?

Nzi wa Misri, na Nyuki wa Ashuru vilimaanisha nini? (Isaya 7:18-20).

Print this post

Theolojia ni nini?. Na je ni sahihi kuisoma?

Theolojia ni elimu ya kujifunza sifa za Mungu na mapenzi yake na jinsi anavyohusiana na wanadamu na ulimwengu  kwa ujumla.

Neno Theolojia limezaliwa kutoka katika maneno mawili ya kigiriki ‘theos’, na ‘logos’

Theos likiwa na maana ya Mungu, na logos ni neno/wazo/elimu/maarifa.

Hivyo tukiunganisha maneno hayo, ni sawa kusema theolojia ni mafundisho au maarifa au elimu kuhusu Mungu.

Ni utafiti kuhusu  Mungu katika mpangilio na mtiririko maalumu. Ukweli ni kwamba theolojia haiwezi kumfafanua Mungu katika ufasaha wote, ikiwa mtu ataitegemea  theolojia tu kumjua Mungu, ukweli ni kwamba amepotea, lakini ikiwa itasomwa vema (si kwa lengo la kitaaluma), bali kwa lengo la kupanua upana wa fikra kuhusu Mungu na maandiko, inafaa sana katika uelewa wa nyanja mbalimbali, hususani kwa wale viongozi na waangalizi kama vile wachungaji, na wahubiri. Si lazima isomwe kwenye vyuo maalumu, mtu yeyote akitia nia kujifunza theolojia anaweza jifunza, kwa kupitia mafundisho mengi, majadiliano na waalimu walio na upeo mpana wa biblia, semina, na kujisomea mwenyewe n.k.

Na Haya ni matawi makuu ya theolojia katika kuichambua biblia.

1) Theolojia ya ki-biblia.

Imejikita katika kutafiti Maudhui au fundisho kuu la biblia, inaangazia jinsi gani vitabu mbalimbali kwenye biblia, vinavyoelezea mpango wa Mungu katika nyakati tofauti tofauti tangu mwanzo hadi mwisho. Mfano kujifunza MAAGANO, katika agano la kale na jipya yalivyotenda kazi na jinsi Yesu alivyoanza kutambulishwa tangu Edeni kama mzao wa mwanamke, hadi nyakati za manabii Isaya 53, hadi wakati wa kutokea kwake duniani Luka 24:27.

Upo umuhimu wa kuijua hii theolojia kwasababu itakupa kujua kiini cha biblia ni nini? Zipo habari nyingi, hadithi nyingi, nyimbo nyingi, mifano mingi, lakini ni vema ujue maudhui zao ni zipi ili usijikute unatoka nje ya shabaha ya imani.

2) Theolojia ya ki-mpangilio/Mada

Inaegemea kujifunza biblia katika migawanyo maalumu ya mada, kwa mfano,

Fundisho la Mungu (theolojia),

Fundisho La Yesu Kristo (Kristolojia),

Fundisho La Roho Mtakatifu (niumatolojia),

Fundisho La wokovu (Soteriolojia),

Fundisho La kanisa,(Ekleziolojia)

La Siku za mwisho.(Esokatolojia)

La mwanadamu (Anthropolojia)

La malaika (Angeolojia)

3) Theolojia ya ki-vitendo

Inajikita kujifunza jinsi maagizo ya kibiblia yanavyoweza kutendewa kazi katika,, huduma kwa mfano kuhubiri na kufundisha , katika uangalizi wa kichungaji, katika umisheni, na katika taratibu za kiibada, na katika kutoa mashauri ya kikristo kama vile kuwaonya wenye matatizo ya kiroho,  kifikra, vifungo n.k.

4) Theolojia ya ki-historia.

Inaangazia jinsi gani imani ya kikristo imekuwa ikipiga hatua katika vipindi mbalimbali vya kihistoria, inaangazia mabaraza mbalimbali ya makanisa yaliyokaa katika kujadili fundisho na misingi ya imani. Kwamfano lile baraza la Nikea (325WK). Mpaka nyakati za matengenezo mfano akina Martin Luther, calvin, na wengine.

Hii inakusaidia kujua historia na chimbuko la imani yetu, na sababu ya ukristo kuonekana katika muundo huu leo.

5) Theolojia ya kimaadili.

Hii inaegemea katika ukristo na jamii, kwamfano mtazamo wa ukristo katika maeneo ya kijamii mfano ndoa, biashara, taratibu za kijamii, haki za kibinadamu, vita,

Zipo theolojia nyingine kama vile theolojia za tafsiri, za kulinganisha, za utetezi, za kifalsafa. n.k. Kwasababu ya upana wa theolojia, haya ni  matawi baadhi tu, kati ya mengi. Hivyo, kama watu wa Mungu, pamoja na kutegemea Bwana kutufunulia mwenyewe maandiko, upo pia wakati ambao hatuna budi kuyamulika maandiko kiundani (Kitheolojia), tukiwa na lengo la kumjua Mungu kwa upana na sio kuwa wasomi, au wanataaluma.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Mwanazuoni ni mtu gani kibiblia?

Kwanini kuna tafsiri nyingi za Biblia, na tafsiri ipi ni sahihi?

Yesu anapoitwa mwana wa Azali, maana yake nini?

Print this post

Kwanini Mungu alimchagua Musa, na si mtu mwingine?

Mungu hakumchagua Musa kwasababu ya wema, au kipawa, au ujuzi fulani aliokuwa nao tofauti na wengine. Hapana almchagua ili ‘kutumiza kusudi lake la kuchagua’ ambalo tunalisoma kwa urefu katika (Warumi 9:11-17). Linalomaanisha Mungu humchagua mtu na kumfanya awe kama anavyotaka mwenyewe, na sio kwa jinsi Yule mtu atakavyo.  Kwamfano alimchagua Farao, kisha akamwekea moyo mgumu,ili atimize kusudi lake mwenyewe, kujichotea utukufu kwa mapigo yale kumi,aliyoyaachia kwa wamisri, vivyo hivyo na kwa Musa alimchagua na kumpa neema ile kubwa ya hofu ya Ki-Mungu na upole ili atimize kusudi lake la kuwakomboa wana wa Israeli.

Lakini hakuwa na tendo lolote jema alilowahi kutenda lililomshawishi Mungu amchague yeye tofauti na wengine.

Na ndivyo anavyofanya hata sasa kwa wanadamu wote. Tunaokolewa na kutumiwa na Mungu kwa neema tu, na si kwasababu ya matendo Fulani mema tuliyowahi kumtendea Mungu.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Nini tofauti ya Majira na Wakati?

Tofauti ya kazi ya Damu ya Yesu na Jina la Yesu ni ipi?

NAAM, HATA WABAYA KWA SIKU YA UBAYA. 

Print this post

KILA MTU NA AMCHE BABA YAKE NA MAMA YAKE.

(Mafunzo maalumu kwa watoto na walezi).

Kama wewe ni mtoto basi jifunze haya, na kama ni mzazi basi pia jifunze haya na pia mfunze mwanao…

Mambo ya Walawi 19:3 “Kila mtu na amche mama yake, na baba yake, nanyi mtazitunza Sabato zangu; mimi ndimi BWANA, Mungu wenu”

Biblia imetumia neno “kumcha” kuonyesha msisitizo wa jambo hilo, jinsi lilivyo la msingi.

“Kumcha mzazi” sio “kumwabudu” bali ni kumpa heshima ya hali ya juu sana, ikiwemo kumsikiliza, kumtii na kufanya yale anayosema bila kumsumbua sumbua ikiwa jambo hilo si nje na mapenzi ya MUNGU.

Maana yake kama tunavyomcha MUNGU, kila atuambiacho tunakizingatia, kwasababu tunajua kwake kuna baraka na laana, kadhalika na wazazi hivyp hivyo wanaweza kutubariki na kutulaani.

Sasa wengi wetu inapofika eneo hili la kutafakari mzazi na mtoto akili zetu huwa zinalenga kufikiri wale watoto walio chini ya malezi ya wazazi, pasipo kujua kuwa hata uwe na miaka 70 na kama mzazi wako yupo hai bado hiyo amri inakuhusu hata wewe ya kumcha mzazi wako, kwani wewe bado ni mtoto kwake.

Amri ya watoto kuwatii na kuwaheshimu wazazi inawahusu hata wenye ndevu na hata wazee wenye mvi, haijalishi wewe sasa ni bibi au babu na unao wajukuu…kama mzazi wako yupo hai unayo amri ya kumcha..

Lakini ukimvunjia heshima mzazi kwasababu ni mzee, basi fahamu kuwa bado hujayajua maandiko.

Mithali 23:22 “Msikilize baba yako aliyekuzaa, Wala usimdharau mama yako akiwa mzee”

Jifunze kumcha Mzazi, wapo watu wanapambana na wazazi wakati wote, wanagombana na wazazi, na hata kuwaita wachawi, usiwe jamii ya hao watu waliotabiriwa..

Mithali 30:11,”Kuna kizazi cha watu wamlaanio baba yao; Wala hawambariki mama yao”. 

Yafuatayo ni madhara machache ya kutomcha Mzazi.

    1. Jicho kung’olewa.

Mithali 30:17 “Jicho la mtu amdhihakiye babaye, Na kudharau kumtii mamaye; Kunguru wa bondeni wataling’oa Na vifaranga vya tai watalila”

Mtu aliyetolewa macho ni kipofu, hawezi kuona ya mbele wala ya nyuma katika maisha yake, atabaki anapapasa tu.

  2. Kifo.

Mithali 20:20 “Amlaaniye babaye au mamaye, Taa yake itazimika katika giza kuu”.

Maana ya Taa kuzimika ni “kifo”. (Soma Ayubu 21:17).

Yapo na madhara mengine mengi ikiwemo kukosa Heri mashani..

Je unamcha mzazi wako?..je unameombea?..je umepatana naye?. Kama bado hujafanya hayo yote basi anza leo.

Bwana akubariki na atusaidie.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

Uchambuzi wa kitabu cha pili cha Paulo kwa Timotheo (2Timotheo).

Huu ni waraka wa Pili ambao mtume Paulo aliuandika kwa mwanae Timotheo akiwa kama mfungwa kule Rumi (2Timotheo 1:17)

Ni waraka wa Kitume zaidi, akimweleza Timotheo mambo mengi anayopaswa ayafanya, na ayaelewe kuhusiana na kazi ya Mungu.

Maudhui makuu ya Paulo yalikuwa ni haya;.

  1. Kumtaka Timotheo ajithibitishe vema katika huduma, 
  2. Lakini pia kumjuza juu ya tabia za wahudumu mbalimbali atakaokutana nao katika kazi ya Mungu, 
  3. Tabia zitakazoonekana siku za mwisho, jinsi asili ya watu itakavyokuwa na namna ya kukabiliana nazo.

Haya ni maelezo mafupi katika maeneo hayo makuu:

1) Wito kwa Timotheo kuwa kamili Na thabiti Katika huduma.

> Paulo Anaanza kwa kumtaka Timotheo aichochee karama iliyo ndani yake, aliyoipokea kwa kuwekewa mikono na yeye. Akionyesha kuwa huduma ni kama moto ambao ili kuufanya uendelee kuwaka inahitaji wakati wote uchochewe.(2Timotheo 1:6-8)

> Anamsihi kama askari mwema, ajikite katika kazi moja ya injili, Asipeleke fikra zake katika shughuli za kidunia, akimtaka afahamu hilo ili aweze kuvipiga vita vizuri vya imani, bila kuvutwa na mambo mengi.

2 Timotheo 2:3-7

[3]Ushiriki taabu pamoja nami, kama askari mwema wa Kristo Yesu.

[4]Hakuna apigaye vita ajitiaye katika shughuli za dunia, ili ampendeze yeye aliyemwandika awe askari.

[5]Hata mtu akishindana katika machezo hapewi taji, asiposhindana kwa halali.

[6]Yampasa mkulima mwenye taabu ya kazi kuwa wa kwanza wa kupata fungu la matunda.

[7]Yafahamu sana hayo nisemayo, kwa maana Bwana atakupa akili katika mambo yote.

> Anamtaka pia ajionyeshe Kuwa amekubaliwa na Mungu, Mtu awezaye kuligawanya Neno la Mungu vema, (2:15)

> Azikimbie tamaa za ujanani (2:22)

> Awe tayari kuhubiri injili Wakati wote  ufaao na usiofaa.(4:1-2)

> Awe na kiasi katika mambo yote, avumilie mabaya, atimize huduma yake. (4:5)

> Akumbuke pia akikubali kuishi maisha ya utauwa ataudhiwa.(3:12)

2) Tabia mbalimbali za wahudumu wenza.

Paulo anatoa habari za tabia alizokutana nazo kwa baadhi wa wahudumu wenza,

makundi hayo ni kama yafuatayo;

> Walioshirika na yeye nyakati zote kwa uaminifu,  mfano wa hawa ni Onesiforo na watu wa nyumbani mwake, pamoja na Luka(1:16).

> Waliotengana naye  kwasababu njema za mtawanyiko wa kihuduma mfano wa hawa ni Kreste na Tito,(4:9b)

> Lakini wapo ambao walimwacha kwa kupenda dunia mfano wa hawa ni Dema.(4:9)

> Na wengine kwa kujiingiza kwenye mafundisho ya uongo mfano wa hawa ni Himenayo na Fileto.(2:17-18)

> Na wengine walifanyika kabisa wapinzani wake. Mfano wa hawa ni Iskanda mfua shaba.(4:14)

Lengo la Paulo kumjuza juu ya watu hawa ni kumtaka ajifunze kuvumilia, na pia kujiepusha nao hususani wale wapingamizi, na kuweka misingi ya kimafundisho kwa kuwatahadharisha watu wasiyafuatishe mafundisho mengine, kwani makundi hayo atakutana nayo, na yatakuwepo.

3) Nyakati za hatari, katika siku za mwisho.

Paulo anampasha habari Timotheo uhalisia juu ya nyakati za mwisho, ambazo tangu wakati ule zilikuwa tayari zimeshaanza..

2 Timotheo 3:1-5

[1]Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari.

[2]Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi,

[3]wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema,

[4]wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu;

[5]wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.

makusudi yake ni kumtaka avumilie, na kusimama  imara katika huduma, kwasababu nyakati ngumu atakutana nazo za watu wengi kujiepusha na mafundisho ya uzima.

Anasema pia kutazuka wimbi la waalimu wa uongo,  wapinzani wa injili mfano wa Yane na Yambre, ambao watashindana na kweli, (3:8-9).

Hatua za kuchua:

> Adumu katika mafundisho na mwenendo wote alioupokea kwake (3:10, 14)

> Awakabidhi wengine mapokeo hayo. .(2:1)

> Ajiepushe na mashindano ya kidini, na maneno yasiyokuwa na maana (2:16, 23-26)

Mwisho.

Paulo anaeleza mwisho wake, na sababu ya kuvipiga vita vema na kusimama imara katika Imani,  ni kwasababu aliiona ile  taji ya haki aliyowekewa Na Mungu mbinguni. Akitumai na Timotheo atasukumwa kuvipiga vita vema kwa kuiona thawabu hiyo hiyo aliyowekewa mbinguni.

2 Timotheo 4:6-8

[6]Kwa maana, mimi sasa namiminwa, na wakati wa kufariki kwangu umefika.

[7]Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;

[8]baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Uchambuzi wa kitabu cha kwanza cha Paulo kwa Timotheo (1Timotheo)

MAMBO NANE (8), AMBAYO WEWE KAMA KIONGOZI UTAIGWA.

UNALITUMIA KWA HALALI NENO LA KWELI?.

Print this post