JE! NI CHEMCHEMI IPI INATOKA NDANI YAKO, YA MITO AU YA KISIMA?

JE! NI CHEMCHEMI IPI INATOKA NDANI YAKO, YA MITO AU YA KISIMA?

Mtu yeyote aliyeokoka, ndani ya moyo wake kunatokea chemchemi ya maji  yaliyo hai (Mithali 4:23). Na maji hayo huwa hayakauki, kwasababu yanatoka kwenye chanzo chenyewe  halisi ambacho ni Yesu Kristo,

Na Kama vile tunavyojua maji hufanya kazi zisizopungua nne.

  1. kukata kiu,
  2. kumeesha,
  3. kusafisha,
  4. na kugharikisha pale yanapozidi,

Ndivyo ilivyo kazi ya maji haya  katika moyo wa mtu, hukata kiu ya mambo maovu(Ufunuo 21:6, Yohana 4:14), humeesha mambo mema ya Mungu , husafisha moyo wa mtu, lakini pia  hugharikisha kazi za Yule  mwovu.

Ndio maana maandiko yanasema pepo limtokapo mtu hupitia mahali pasipo na maji, ni kwanini? Ni kwasababu eneo lenye maji  rohoni, pepo hawezi kukaa anaona gharika, na mafuriko makubwa hawezi kusogelea hapo. Na eneo lenye maji ni moyo wa mtu aliyeokoka.

Luka 11:24  Pepo mchafu amtokapo mtu, hupitia mahali pasipo maji, akitafuta mahali pa kupumzika; asipoona, husema,

25  Nitairudia nyumba yangu niliyotoka

26  Hata afikapo, akaiona imefagiwa na kupambwa, ndipo huenda akachukua pepo wengine saba, walio waovu kuliko yeye mwenyewe, wakaingia na kukaa humo; na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza

Sasa wengi wetu hatujui kuwa hayo maji, yanakuwa kama maji ya “KISIMA” tu, ambayo hutulia pale pale, ni neema ya bure ambayo kila mwamini amepewa. Lakini ili ayafanye maji hayo kuwa “MITO” yaani yatiririke mbali. Si jambo la kusema tu nimeokoka. Bali kitu cha ziada lazima kifanyike kwenye maisha ya mtu.

Kama tunavyojua mito, huenda mbali kuwasaidia, hata watu wasiojua chanzo chake kilianzia wapi, Kwamfano mamilioni ya  wakazi wa mji wa Kilimanjaro, kutegemea maji yanayotiririka kutoka katika mlima wa Kilimanjaro, Na ni wazi wengi wao hawajui chanzo ni mwamba gani. Lakini wananufaika. Hata Pale Edeni Mungu alitoa mto katikati ya bustani, lakini haukuishia pale bali ulitoka mpaka nje ya bustani, kuyanufaisha mataifa. (Mwanzo 2: 10-14)

Vivyo hivyo ili na wewe yale maji uliyoyapokea siku ulipookoka, kama chemchemi ya kisima, unataka yatoke nje, huna budi kufanya jambo lingine la ziada.

Ndio maana mitume walishindwa kulitoa lile pepo sugu, wakijiuliza kwanini, ndipo   Bwana Yesu alisema maneno haya

Mathayo 17:21  [Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]

Ni nini hiyo haitoki?

Ni maji yaliyo ndani yako. Kubadilika na kuwa mito, ni lazima uingie gharama za kuwa mwombaji. Si kuomba tu bali Kuomba bila kukoma. Mwombaji yoyote huuvutia uwepo wa Mungu maishani mwake. Maombi ni ‘pump ‘ya Mungu inayoyavuta yale maji nje! Yakawasaidie wengine. Huwezi kuwa mtu wa mafunuo kama huna desturi ya kuomba, huwezi kuwasaidia wengine rohoni, hata kuwaombea wasaidike, kama wewe si mtu wa kuomba. Unatazamia mumeo aache pombe, halafu sio mwombaji, utapona tu wewe peke yako, lakini hutaweza kumponya mwingine. Unatazamia familia yako iokoke, halafu wewe mwenyewe huingii gharama za mifungo na maombi, yasiyo koma, mara kwa mara, zitakuwa ni ndoto tu, labda Mungu awaguse kwa njia zake mwenyewe, lakini sio kwa matamanio yako.

Na si tu katika eneo la kuwasaidia wengine, bali hata katika maeneo ya maisha yako ambayo unataka uone maingilio Fulani ya Mungu makubwa. Huna budi kuyatoa hayo maji yaende kuponya hayo maeneo.

Maandiko yanasema imetupasa kumwomba Mungu sikuzote bila kukata tamaa (Luka 18). Hiyo ndio njia pekee itakayoleta majibu.

Yohana 7:38  Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.

Na Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

NI WAPI UTAKUTANA NA MALAIKA WA BWANA?

Mruba ni mdudu gani kwenye biblia?(Mithali 30:15)

Mto Frati upo nchi gani, Umuhimu wake katika biblia ni upi?

Rudi Nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments