USIJARIBU KUMGEUZA MUNGU MGANGA WA KIENYEJI,UTAKUFA.

USIJARIBU KUMGEUZA MUNGU MGANGA WA KIENYEJI,UTAKUFA.

Ipo mifano mingi katika biblia ya watu ambao, walijaribu kumgeuza Mungu kama mganga wa kienyeji na mwisho wao ukawa mbaya sana. Siku zote watu wanaokwenda kwa waganga utagundua wengi wao hawafahamiani hata na hao waganga wanaowaendea, wala hawana uhusiano nao wowote.

Wakifika pale wanaeleza tu matatizo yao, kisha mganga anawatamizia haja zao, kisha wanakwenda zao..Sasa jambo kama hilo usijaribu kulifanya kwa Mungu ni hatari mno.

Wana wa Israeli kuna wakati Fulani walikuwa wanajaribu kufanya hivyo hivyo, unakuta mtu kamwacha Mungu zamani, ndani yake kuna vinyago, hashiki torati ya Mugu, lakini pale anapokumbwa tu na matatizo fulani labda anaumwa, au anataka kufanya jambo Fulani ndipo anataka kwenda kumuuliza Mungu kwa kupitia nabii wake..Sasa karibu wote waliokuwa wanafanya hivyo Mungu alikuwa anawaua bila huruma.

Utajiuliza anawauaje?

Kama huyo nabii ni nabii wa kweli wa Mungu aliyesimama. Mungu atamwambia moja kwa moja kuwa atakufa. Ndicho pia kilichomkuta Yeroboamu na mkewe walipokwenda kuuliza habari za uzima wa mtoto wao kwa nabii Ahiya, walitabiriwa mabaya na vifo soma (1Wafalme14).

Lakini kama nabii huyo ni nabii wa uongo au vuguvugu..Mungu anachofanya ni anamdanganya Yule nabii aliyemwendea, Na Mungu anajua kabisa kwasababu unamwamini nabii Yule kwamba chochote atakachokuambia utafanya, kumbe huo ndio unakuwa mtego wa kwenda kukuangamiza wewe, Mfano huo tunaouna kwa mfalme Ahabu, pale alipotaka kwenda kupigana vita na mfalme wa Shamu, na biblia inasema Mungu akawadanganya wale manabii 400 wote wakamtabiria ushindi kumbe ndio ulikuwa unakwenda kuwa mwisho wake.. Mungu atakuahikishia hata kwa nabii zaidi ya mmoja unachokifanya ni sahihi, kumbe ni uongo ujue kabisa amekusudia kukuua soma (1Wafalme 22:1-39)..Ndicho kilichomkuta Balaamu, ilikuwa ni nusu afe, punda ndiye aliyemuokoa japokuwa ni Mungu ndiye aliyemwambia aende (Hesabu 22:1-34)..Wote hawa ni mfano wa watu waliojaribu kumgeuza Mungu mganga wa kienyeji kwamba wao wapewe tu haja za mioyo yao, mengine zaidi ya hayo hawataki..

Angalia jambo aliloambiwa Ezekieli na Mungu..

Ezekieli 14:1 Ndipo baadhi ya wazee wa Israeli wakanijia, wakaketi mbele yangu.

2 Ndipo neno la Bwana likanijia, kusema,

3 Mwanadamu, watu hawa wametwaa vinyago vyao na kuvitia mioyoni mwao, nao wameweka kwazo la uovu wao mbele ya nyuso zao. Je! Ni laiki yangu niulizwe na wao katika neno lo lote?

4 Basi sema nao, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Kila mtu wa nyumba ya Israeli atwaaye vinyago vyake na kuvitia moyoni mwake, na kuliweka kwazo la uovu wake mbele ya uso wake, na kumwendea nabii; mimi, Bwana, nitamjibu neno lake sawasawa na wingi wa sanamu zake;

5 ili niwakamate nyumba ya Israeli kwa mioyo yao wenyewe, kwa sababu wamefarakana nami kwa vinyago vyao……

7 Kwa maana kila mtu wa nyumba ya Israeli, au wa wageni wakaao katika Israeli, ajitengaye nami, na kuvitwaa vinyago vyake na kuvitia moyoni mwake, na kuliweka kwazo la uovu wake mbele ya uso wake, kisha kumwendea nabii, na kuniuliza neno kwa ajili ya nafsi yake; mimi, Bwana, nitamjibu, mimi mwenyewe;

8 nami nitaukaza uso wangu juu ya mtu yule, na kumfanya kuwa ajabu, awe ishara na mithali, nami nitamkatilia mbali, asiwe kati ya watu wangu; nanyi mtajua ya kuwa mimi ndimi Bwana.

9 Na nabii akidanganyika, na kusema neno, mimi, Bwana, nimemdanganya nabii yule, nami nitaunyosha mkono wangu juu yake, na kumwangamiza, asiwe kati ya watu wangu Israeli.

10 Nao watauchukua uovu wao; uovu wa nabii utakuwa sawasawa na uovu wake yule amwendeaye aulize neno;

Unaona hapo mstari wa 9? Anasema mimi Bwana nimemdanganya nabii Yule.. Kama ulikuwa unahitaji kupona, pengine nabii Yule atakupa maagizo Fulani ambayo ni kweli ameyapokea kutoka kwa Mungu, labda tuseme atakuambia Mungu kaniambia, funga siku tatu, kisha kula chakula kisichokuwa na chumvi tu, baada ya hapo utakuwa mzima..Kumbe jambo hilo ndio linakwenda kukuangamiza kabisa.. Na Mungu anafanya hivyo kwasababu umemdharau yeye kwa kumgeuza kuwa kama mganga wa kienyeji, angali ulikuwa unajua kabisa ndani ya moyo wako kuna dhambi umekataa toba, na utakatifu halafu unamwendea yeye akupe haja ya moyo wako wa dhambi..

Hata leo hii, Mungu anawaangamiza watu wengi kwa namna hiyo pasipo wao kujijua.. Wakati Mungu anawapigia kelele kila siku watubu, waache dhambi, watoe vinyago ndani ya mioyo yao, hawataki kusikia wala kuzingatia maagizo hayo, wanadhani Mungu anafurahishwa nao, wanadhani Mungu ni wa neema siku zote badala yake wakiwa bado ni walevi, wala rushwa, wazinzi, waabudu sanamu, washirikina, watazamaji pornography, wasagaji wanamwendea Mungu, kwa kupitia mtu anayejiita nabii, au mtume, au mchungaji, amwombee au amtatulie matatizo yake pengine ya kiafya, au ya kiuchumi, au ya kifamilia…Wahudumiwe tu kisha waondoke wakaendelee na maisha yao ya kawaida ya kila siku..

Ndugu kama ni wewe mmojawapo usijaribu kufanya hivyo tena,..Kwasababu UTAKUFA.. nenda kawatafuta waganga wa kienyeji itakuwa ni salama kwako, lakini sio Mungu kama unamwendea Mungu halafu hutaki kuacha dhambi.. Nakuambia ukweli UTAKUFA NDUGU…

Utaishia kudanganywa tu,..tena na Mungu mwenyewe, unakimbilia mafuta ya upako, unausahau mafuta ya roho yako (Roho Mtakatifu) ambayo yanaokoa roho yako, unakimbilia maji, unasahau maji ya uzima ambayo yanaokoa roho yako.. Timiza kwanza agizo la msingi ambalo ni wokovu na utakatifu..Ndipo Mungu akupe neema ya kutatuliwa na hayo mengine.

Vinginevyo utakufa, hata kama sio kwa njia hiyo, itakuwa kwa nyingine.

Au wewe ni mlevi, mzinzi, mwendaji disko, mlaji rushwa, halafu unakwenda kanisa kila siku, kunakufaidia nini sasa? na kibaya zaidi unashiriki na meza ya Bwana kabisa..Huko ni kujitafutia kifo ndugu. Break! ya kwanza kwa Mungu ni utakatifu (Waebrania 14:12),Mungu hapambwi kwa sadaka, au kwenda kwako kanisani, anachohitaji kwako ni Utakatifu kama yeye alivyo mtakatifu. Nje ya hapo wewe ni adui wa Mungu.

Hiyo ni tahadhari kwako, wewe..Umekwisha sikia, Mungu hadhihakiwa, apandacho Mtu ndicho atakachokuna maandiko yanasema hivyo.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

UNAWAFAHAMU MANABII WA UONGO?

CHUKIZO LA UHARIBIFU

MPINGA-KRISTO

JE! UMEBATIZWA UBATIZO SAHIHI?

TAZAMA KRISTO YUPO HAPA,AU YUKO KULE MSISADIKI.

NGURUMO SABA

JUMA LA 70 LA DANIELI

DANIELI: Mlango wa 1

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
1 Comment
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
BARAKA MBUNGA
BARAKA MBUNGA
3 years ago

Leave your message arifu mfalme yesu kristo