KWA KUWA TUMEKABIDHIWA MAUSIA NA MUNGU.

KWA KUWA TUMEKABIDHIWA MAUSIA NA MUNGU.

Kuna mambo ambayo Mungu anaweza kukuagiza ufanye, ukayaona kama hayana maana yoyote rohoni,ukayapuuzia tu na ukaendelea na shughuli zako kama kawaida, hata ukawa unaendelea kumtumikia Mungu, lakini hujui kuwa machoni pa Mungu ukaoekana kuwa si kitu.

Kwa mfano tukirudi kwenye maandiko, utaona kuna wakati mtume Paulo, alipokea kweli ufunuo wa Roho Mtakatifu kuwa tohara ya mwilini hamfikishi myahudi popote, awe ametahiriwa awe hajatahiriwa kama mtu huyo haishiki torati basi ni sawa na kazi bure tu.(Warumi 2:25-29)

Lakini utaona anasema tena, tohara ni muhimu kwao kwa kila njia, ikimaanisha kuwa sio jambo la wao kulipuuzia hata kidogo, Soma..

Warumi 3:1 “Basi Myahudi ana ziada gani? Na kutahiriwa kwafaa nini?

2 Kwafaa sana kwa kila njia. Kwanza kwa kuwa wamekabidhiwa mausia ya Mungu”.

Unaona, japokuwa aliwahubiria wayahudi kuwa tohara ya mwilini haiwezi kuondoa dhambi zao, lakini aliwahimiza watahiriwe wote, kwasababu lilikuwa tayari ni agizo la Mungu.

Sasa hilo lilikuwa ni agizo kwa wayahudi..

Vipi kuhusu sisi wakristo, ambao sheria yetu ililetwa na Bwana wetu YESU KRISTO?.

Yeye alisema..

Marko 16:16 “Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa”.

Kama tunavyosoma hapo sio kuamini tu, bali na kubatizwa pia..Lakini cha kushangaza wapo wakristo wanaosema, ubatizo haumpeleki mtu mbinguni, unaweza ukawa umebatizwa na maji hata ya mto Yordani na mbinguni bado usiende, kwasababu maji hayaondoi dhambi za mtu isipokuwa damu ya Yesu …mtu huyo anaendelea kusema kinachojalisha ni kumwamini Yesu tu basi,ukishatubu ndio tayari umeupata wokovu wenyewe..hayo masuala ya kubatizwa, tena kwa kuzamishwa, sio lazima kwa mkristo.. Wewe amini tu inatosha, imani yako ndio itakayokupeleka mbinguni..

Lakini Kristo anataka ufahamu jambo hili, kwamba ubatizo wafaa sana kwa kila njia, na kwanza ni kwasababu yeye ametupa maagizo hayo..hata kama kwetu hayana maana lakini kwake yanayo maana kubwa..

Tukijiona sisi ni wa rohoni sana kuliko yeye mwenyewe aliyetupa maagizo hayo, na kwamba tunajua kumtumikia kuliko kuyafuata maagizo yake.. Basi siku zote tuyakumbuke maneno yake haya aliyoyasema:

Luka 6:46 “Na kwa nini mnaniita, Bwana, Bwana, walakini hamyatendi nisemayo?

47 Kila mtu ajaye kwangu, na kuyasikia maneno yangu na kuyatenda, nitawaonyesha mfano wake.

48 Mfano wake ni mtu ajengaye nyumba, na kuchimba chini sana, na kuweka msingi juu ya mwamba; na kulipokuja gharika, mto uliishukia nyumba ile kwa nguvu, usiweze kuitikisa; kwa kuwa imejengwa vizuri.

49 Lakini yule aliyesikia ila hakutenda, mfano wake ni mtu aliyejenga nyumba juu ya ardhi pasipokuwa na msingi, mto ukaishukia kwa nguvu, ikaanguka mara; na maangamizi yake nyumba ile yakawa makubwa”.

Sisi tulio na masikio na tusikie maneno ya Bwana na tuyatii.Kumbuka Neno ubatizo tafsiri yake ni kuzamwishwa/kuzikwa, hivyo unapofikiria kwenda kubatizwa maana yake ni kuwa unakwenda kuzamishwa katika maji, mwili wote unapotelea majini, na sio kunyunyiziwa,.Na ndio hapo suala la maji mengi/ maji tele linakuja sawasawa na (Yohana 3:23). Na hiyo inaweza ikafanyika popote pale aidha mtoni, au bwawani, au baharini, au kwenye kisima kilichochimbwa, au popote pale maadamu tendo hilo liwe ni la kuzamwishwa mwili wote majini.

Vilevile ubatizwe uwe ni kwa jina lake yeye aliyekuagiza yaani YESU KRISTO anayeweza kuzifuta dhambi zetu sawasawa na (Matendo 3:38,8:16,10:48, 19:5)..Ukikamilisha hayo maagizo ipasavyo basi ujue kuwa wokovu wako ni thabiti, Na kama ingekuwa ni kupewa cheti cha kimwili basi mbingu ingekupa. Hivyo kama hujawahi kubatizwa kabisa au ulibatizwa isivyopaswa, basi wakati ndio huu kwako kwenda kufanya hivyo.

Na Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

MITHALI AU METHALI ZA BIBLIA

UTASIMAMA PEKE YAKO SIKU ILE.

RAFIKI MWEMA.

Je! Ni halali kuoa/kuolewa na mtu ambaye tayari anao watoto?

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments