MUNGU HANA MBARAKA MMOJA TU!..MWAMINI.

MUNGU HANA MBARAKA MMOJA TU!..MWAMINI.

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe daima, karibu tujifunze biblia.

Imani ni kuwa na uhakika wa mambo yatarajiwayo.. Je! Una uhakika wa mambo yatakayokuja ambayo bado hujayaona wala kuyafikia?..Na kama ndio, je kwa kiwango gani?.

Ili Imani yako ionekane kuwa kubwa ni lazima uwe na uwezo wa  kuamini vitu visivyoweza kuaminika. Yaani uwe na kila sababu itakayokufanya kuwa na uhakika kwamba jambo Fulani lazima litokee.

Kwamfano ukizungumza na mtu kwenye simu, aliye umbali Fulani akakwambia panda gari (daladala) unifuate mahali nilipo baada ya lisaa limoja…bila shaka kama utakuwa na fedha ya kutosha mfukoni mwako, hutakuwa na wasiwasi wa kufika pale alipo…kwasababu unajua hata Ukikosa daladala utatafuta tax, na hata ukikosa hiyo  bado unaweza kupanda pikipiki ukafika pale alipo katika muda ule ule. Hivyo huo uwezo wa kuwa na kila sababu ya kufika pale kwa muda unaotakiwa ndio unaoitwa IMANI (una uhakika wa mambo yatarajiwayo yatafanikiwa asilimia 100). 

Lakini kama huna fedha kabisa au unafedha kidogo tu ya daladala, utakuwa na wasiwasi, utasema itakuwaje endapo nikikosa gari? itakuwaje endapo gari nitakalopanda likiharibikia njiani?..si nitachelewa n.k Hivyo unakuwa huna uhakika sana wa mambo yatarajiwayo..Hapo inahesabika kuwa Imani yako ya kufika unakotaka kwenda kwa muda unaotakiwa ni ndogo au huna kabisa.

Sasa tukirudi katika Biblia ni hivyo hivyo..Ili uweze kuhesabika kuwa na Imani kubwa ya kutosha ya kuweza kupata kile unachokihitaji kwa Asilimia zote, ni lazima uwe na Hazina ya kutosha ya UELEWA WA MAANDIKO, ili uweze kukipata kile kitu. Kumbuka hapo ninasema ni UELEWA WA MAANDIKO, na si IDADI YA MAANDIKO. Mtu mwenye idadi kubwa ya maandiko pasipo kuyaelewa huyo ni sawa redio yenye idadi kubwa ya sauti na nyimbo zinazotoka ndani yake, lakini yenyewe haielewi chochote.

Hivyo kinachojalisha kwetu ili tuhesabike kuwa na Imani ya kuweza kupokea jambo lolote lile ni HAZINA YA KUYAELEWA MAANDIKO NA KUYACHAMBUA. 

Hebu tujifunze mfano mmoja kwenye biblia ya Mtu aliyekuwa na hazina na uwezo wa kuyaelewa maandiko vyema na kuyagawanya..

Mathayo 15:22  “Na tazama, mwanamke Mkananayo wa mipaka ile akatokea, akampazia sauti akisema, Unirehemu, Bwana, Mwana wa Daudi; binti yangu amepagawa sana na pepo. 

23  Wala yeye hakumjibu neno. Nao wanafunzi wake wakamwendea, wakamwomba, wakisema, Mwache aende zake; kwa maana anapiga kelele nyuma yetu. 

24  Akajibu, akasema, Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli

25  Naye akaja akamsujudia, akisema Bwana, unisaidie. 

26  Akajibu, akasema, Si vema kukitwaa chakula cha watoto na kuwatupia mbwa. 

27  Akasema, Ndiyo, Bwana, lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao. 

28  Ndipo Yesu akajibu, akamwambia, Mama, imani yako ni kubwa; na iwe kwako kama utakavyo. Akapona binti yake tangu saa ile”.

Unaweza kuona hapo, anakatishwa tamaa kwa maneno ya YESU, na kama tunavyojua maneno ya Yesu ni Neno la Mungu. Lakini kwa maneno hayo hayo, mwanammke anayafafanua vizuri kwa Bwana, na hatimaye anapata haki yake.. “ni kweli si vyema kutwaa chakula cha watoto kuwatupia mbwa, lakini hata mbwa wanakula makombo yaangukayo chini ya meza za Bwana zao”…Maana yake ni kwamba sistahili kweli kupewa hichi ninachokitafuta, (ni kweli mimi ni kama mbwa).. Lakini kuna vile vidogo vichache vinavyobakigi..ipo neema kidogo inakuwepo kwa Mungu kwa wale wasiomcha yeye…Hiyo ndio ninayoihitaji mimi!..Ni kweli Mungu hasikii maombi ya waovu, lakini bado Mungu huyo huyo anawanyeshea mvua waovu na wema…anawaangazia jua lake wenye haki na wasio haki..

Ni kweli mimi sio mkamilifu mbele zake, lakini bado wale waovu kuliko mimi anahakikisha wanafikiwa na miale ya jua, anahakikisha upepo mwanana unawaburudisha, anahakikisha wanapata hewa safi ya oksijeni kila dakika..hivyo kwa rehema hizo, ni lazima na mimi na mimi lazima nipone, lazima nibarikiwe na kufanikiwa katika yote..Mungu hana mbaraka mmoja tu!.

Hebu tujifunze Zaidi kisa cha Esau na Yakobo.

Tusome..

Mwanzo 27: 33 “Isaka akatetemeka tetemeko kuu sana, akasema, Ni nani basi yule aliyetwaa mawindo akaniletea? Nami nimekwisha kula kabla hujaja wewe, nikambariki; naam, naye atabarikiwa.  

34 Esau aliposikia maneno ya babaye, akalia kilio kikubwa cha uchungu sana, akamwambia babaye, Nibariki na mimi, mimi nami, Ee babangu. 

 35 Akasema, Nduguyo amekuja kwa hila, akauchukua mbaraka wako.  

36 Akasema, Je! Hakuitwa Yakobo kwa haki, maana amejitia mahali pangu mara mbili hizi? Alichukua haki yangu ya mzaliwa wa kwanza, na sasa amechukua mbaraka wangu. Akasema, Je! Hukuniwekea na mimi mbaraka? 

 37 Isaka akajibu, akamwambia Esau, Tazama, nimemfanya awe bwana wako, na ndugu zake wote nimempa kuwa watumishi wake; kwa nafaka na mvinyo nimemtegemeza, nami nikufanyie nini sasa, mwanangu? 

 38 ESAU AKAMWAMBIA BABAYE, UNA MBARAKA MMOJA TU, BABANGU? Unibariki mimi, mimi nami, Ee babangu. Esau akapaza sauti yake, akalia.  

39 Isaka, baba yake, akajibu, akamwambia,Angalia,penye manono ya nchi patakuwa makao yako,Na penye umande wa mbingu unaotoka juu”.

Hebu tafakari Esau, angenyamaza asingelia kuomba na yeye abarikiwe, hebu tafakari angeishia kuondoka kwa majonzi leo hi angeishia kuwa kama Kaini, asingekuwa na baraka yoyote….Lakini japokuwa aliikosa ile Baraka kuu, lakini alilia kwa baba yake..akamwambia baba yake nibariki na mimi, kwani una mbaraka mmoja tu??? Na mwishowe akabarikiwa akaambiwa palipo na manono ya nchi patakuwa mahali pake, ingawa Mungu alimchukia Esau(Warumi 9:13)… lakini bado alimbariki alikuwa na mali nyingi hata Zaidi ya Yakobo kasome (kasome Mwanzo 33:9)

Na sisi ni hivyo hivyo, (simaanishi kuwa tuwe waovu, Mungu atusaidie), nachomaanisha ni kuwa ikiwa wewe ni mkristo hupaswi kukata tamaa hata kama inaonekana mambo yameshashindikana…Tujue tu! Mungu hana mbaraka mmoja tu!, usijiangalie ukamilifu wako!..Esau Mungu alimchukia lakini kwa kupambana akambariki hivyo hivyo…

Ukiona jambo Fulani katika Maisha kama haliwezekani, basi jua huo ndio uthibitisho kwamba linawezekana….kibiblia kutokuwezekana ndio uthibitisho wa kuwezekana kwa jambo. Amini tu! Amini tu.. usiache kumwamini Mungu kamwe.

Mwisho kabisa kama tulivyosema… “kubarikiwa wakati mwingine sio uthibitisho wa kumpendeza Mungu”..Esau hakumpendeza Mungu lakini alibarikiwa, na wengine wengi katika biblia…na hata leo Mungu ni yule yule…anawanyeshea mvua waovu na wema…Kwahiyo kuzimu watakuwepo matajiri sana, na mbingu pia watakuwepo maskini, hivyo lililo la Muhimu sana ni kutafuta kuyatenda mapenzi ya Mungu, ambayo hiyo inakuja kwa kutubu na kumpokea Yesu kama Bwana na mwokozi wa Maisha yako na kutafuta ubatizo sahihi wa kimaandiko (Matendo 2:38), na kupokea Roho Mtakatifu, hilo ndio jambo la muhimu na la kwanza, mengine yatafuata. Lakini kama unahitaji jambo lolote…Mwombe Mungu kwa bidii na kumwamini, utaona majibu…

Bwana anakupenda, Bwana anatupenda, na Bwana atubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

LAKINI USIKU WA MANANE, PAKAWA NA KELELE.

HIZI NI NYAKATI ZA KUJIINGIZA KWA NGUVU.

JIFUNZE KULIGAWANYA VYEMA NENO LA MUNGU.

Atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani? Maana yake nini?

BWANA SI MWEPESI WA HASIRA, LAKINI BWANA NI MWINGI WA HASIRA.

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia..!!

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
3 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Subira Kaserero
Subira Kaserero
2 years ago

Amen.

Mohamed kassim
Mohamed kassim
3 years ago

🙌🙌🙌🙌 aseee thanks alot