Title August 2019

WALIOITWA NI WENGI, ILA WATEULE NI WACHACHE.

Kama Ukijifunza Biblia kwa undani utagundua kuwa Bwana Yesu hakuwa na wanafunzi 12 tu! Bali alikuwa na wanafunzi wengine wengi sana Zaidi ya 70 biblia inasema hivyo katika (Luka 10:1-2)…Lakini baadaye alikuja kuteua wanafunzi 12 tu miongoni mwao wakutembea naye kila mahali alikokwenda ambao aliwaita Mitume. 

Sasa kama ukizidi kufuatilia kwa makini, utagundua kuwa Bwana Yesu alianza kwanza kuchagua wanafunzi wake wengi katika hatua ya Kwanza, ikiwemo wale 12, kwahiyo tuseme lilikuwepo jopo la watu kama 80 hivi waliochaguliwa na Bwana, na ni wazi kuwa wote Bwana aliowaita aliwaambia kuwa watakuwa na shughuli ya uvuvi wa watu…alipita huko na huko kuwaita kutoka katika ulimwengu, katika njia ile alikutana na mvuvi Petro akamwita, katika njia nyingine akakutana pengine na fundi wa nyumba akamwita, sehemu nyingine akakutana na Mathayo mtoza ushuru akamwita…wengine pengine walikuwa hawana shughuli yoyote wapo mtaani akawaita, likawa kundi moja la watu kama 80 hivi walioitwa….Na wote walioitwa walikuwa sawa machoni pa Bwana Yesu, hakuna aliyekuwa mkubwa zaidi ya mwingine, na wote aliwaambia waache vyote wamfuate, na walimtii..Sasa hiyo ilikuwa ni hatua ya kwanza ya wito..kundi kubwa la wanafunzi liliitwa…. (Kwa somo refu jinsi gani Bwana aliwachagua wanafunzi wake na jinsi anavyowachagua sasa unaweza kututumia ujumbe inbox tutakutumia hilo somo).

Hatua ya pili ilifuata kipindi kifupi baadaye, pengine baada ya miezi kadhaa, ambapo Bwana akaanza tena kuwatenga wanafunzi 12, miongoni mwa lile kundi kubwa la wanafunzi wake…kumbuka hawa 12, hawakuteuliwa moja kwa moja kutoka kwenye ulimwengu, hapana! bali kutoka katika lile kundi la wanafunzi wengine aliokuwa nao…Huo ndio ulikuwa mchujo wa pili, Ndio siku ile Bwana Yesu alipokwenda kukesha kwenye maombi na Mungu akamfunulia mitume 12 miongoni mwa lile kundi…

Luka 6:12 “ Ikawa siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu. 13 Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; AKACHAGUA KUMI NA WAWILI MIONGONI MWAO, ambao aliwaita Mitume; 14 Simoni, aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na Filipo na Bartolomayo, 

15 na Mathayo na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote, 

16 na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa msaliti. 

17 Akashuka pamoja nao, akasimama mahali tambarare, pamoja na wanafunzi wake wengi, na makutano makubwa ya watu waliotoka Uyahudi wote na Yerusalemu, na pwani ya Tiro na Sidoni; waliokuja kumsikiliza na kuponywa magonjwa yao; 18 na wale waliosumbuliwa na pepo wachafu; waliponywa”

Unaona?..Mitume 12 walichaguliwa miongoni mwa kundi la wanafunzi wengi…sasa hawa 12 hawakuchaguliwa kwasababu ya jitihada yao yoyote waliyokuwa nayo, au kwasababu ya utakatifu wao, au kwasababu walikuwa wanajuhudi kuliko wengine, au kwasababu mbele za Mungu wenyewe ndio walikuwa wanaonekana wanaunafuu…Hapana, walichaguliwa kwa Neema tu… Neno ‘neema’ linakaribiana sana kufanana na neno ‘bahati’….lakini sio bahati…Neema ni Zaidi ya bahati, bahati mara nyingine inamwangukia mtu ambaye amestahili, lakini Neema siku zote ni kwa mtu ambaye hajastahili…Hivyo hawa 12 waliochaguliwa katika mchujo wa Pili walipata NEEMA na sio BAHATI. Walikuwa hawastahili kuchaguliwa lakini walichaguliwa…Na hata hao wengine pia sio kwamba hawakuchaguliwa kwasababu walikuwa waovu au kwasababu walikuwa watakatifu sana, hapana! ni uchaguzi tu wa Mungu! Ndivyo ilivyompendeza awachague wale na hao wengine awaache, hatuwezi kuelezea kibinadamu, na wala hatuwezi kumwuliza Mungu kwanini kafanya hivyo! (soma Warumi 9:13-25).

Sasa katika hatua hii ya Pili ndipo linapotimia Neno hili “walioitwa ni wengi ila wateule ni wachache”…Hapo liliitwa kundi kubwa pengine la watu Zaidi ya 80, lakini walioteuliwa kwa Neema kuwa mitume ni 12 tu!.

Lakini bado mchujo unaendelea kwasababu hata miongoni mwa hao walioteuliwa 12, bado kuna uwezekano wa kupotea…Sio kwasababu tu! Umeitwa Mteule basi ndio tiketi ya kusema nimeokolewa…

Biblia inatuambia kuwa hata “wateule wanaweza kudanganyika”.

Mathayo 24:23 “Wakati huo mtu akiwaambia, Tazama, Kristo yupo hapa, au yuko kule msisadiki. 

24 Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; WAPATE KUWAPOTEZA, KAMA YAMKINI, HATA WALIO WATEULE.

25 Tazama, nimekwisha kuwaonya mbele.

 26 Basi wakiwaambia, Yuko jangwani, msitoke; yumo nyumbani, msisadiki.

 27 Kwa maana kama vile umeme utokavyo mashariki ukaonekana hata magharibi, hivyo ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu”.

Yuda alikuwa miongoni mwa wateule 12, lakini alidanganyika na kupotea!…na hapo biblia inatuonya kuwa katika siku za mwisho watatokea makristo wa Uongo, watatoa ishara na maajabu wapate kuwapoteza kama yamkini hata walio wateule…

Wakati huo tunaoishi ni sasa, wateule wanaozungumziwa hapo ni wale wote ambao Bwana ameshawaita watoke katika ulimwengu, na kuwateua miongoni mwa watu wake, na kuwapa neema ya kuzijua siri za ufalme wa mbinguni kama wewe unayesoma hapa…Kumbuka sio mambo yote Bwana Yesu alikuwa anawaambia makutano, ni machache sana ndio alikuwa anawaambia makutano, siri zake nyingi alikuwa anawafunulia wale mitume 12 tu aliowachagua…wengine wote alikuwa anawafundisha kwa mifano…

Mathayo 13:10 “Wakaja wanafunzi, wakamwambia, Kwa nini wasema nao kwa mifano? 

11 Akajibu, akawaambia, Ninyi mmejaliwa kuzijua siri za ufalme wa mbinguni, bali wao hawakujaliwa”.

Unapopata Neema ya kusikia injili popote pale, tena unapata kuzijua siri za ufalme wa mbinguni ambazo wengine hawazioni wala kuzipata, na kuna kitu ndani kinakushuhudia kuwa ni kweli… fahamu kuwa wewe ni mteule, lakini katika hizi siku za mwisho wateule wengi watadanganyika kama tu vile Yuda alivyodanganyika na kuishia kumsaliti Bwana Yesu… Yuda alishawishika kabisa ndani ya moyo wake kumwamini Bwana Yesu katika hatua za kwanza za wito wake, alipata ufunuo kabisa kuwa Yesu ndiye masihi aliyetabiriwa, na hivyo akaingia gharama ya kuacha kila kitu na kumfuata Yesu, kwasababu hakuna mtu yeyote ambaye angemfuata Yesu bila kuacha kila kitu na kujikana nafsi yake, Yuda alifanya vyote hivyo, aliitikia wito inavyopaswa….lakini ilifika wakati akaanza kulizoelea Neno, akaanza kuingiwa na tamaa ya vitu vya ulimwengu, akaanza wizi kidogo kidogo, akaanza kuipenda dunia kidogo kidogo, Bwana hakumfukuza asiambatane naye, alimwacha mpaka mwisho, wala upako wake haukukatika aliendelea nao alitoa pepo na kuombea watu kama kawaida na kupokea uponyaji, lakini mwisho wake ulikuwa mbaya, alipasuka matumbo (Matendo 1:16-20).

Na hata leo, ulianza vyema kusikia injili na kuamua kumfuata Yesu kwa moyo, hapo ni Bwana alikuita kweli na akakuteua kuwa karibu naye Zaidi ya wengine, uliacha vyote na kumfuata…lakini imefika kipindi sasa umelizoelea Neno, umeoza ndani, unamwibia Bwana, umekuwa ni mwana wa ulimwengu huku, huku bado unatembea na Yesu, kumbuka Bwana hatakufukuza wala hatakutenga, ataendelea kutembea nawe kama alivyotembea na Yuda, wala hataonesha dalili ya kukudharau wala kukuvunjia heshima, na wala nguvu ya kufanya miujiza hatakupokonya, lakini mwisho wako utakuwa kama wa Yuda!…ili maandiko yatimie , Yuda alikuwa ni mteule lakini Bwana alisema ni kheri asingezaliwa mtu kama huyo kuliko mambo mabaya ambayo yatakwenda kumpata!…Hebu fikiria Mtu aliyeteuliwa na Mungu mwenyewe anaambiwa maneno hayo?.

Ndugu hizi ni siku za mwisho sana, Hayo ya akina Yuda yalitokea ili kutufundisha sisi watu wa siku hizi za mwisho, kuwa tufanye IMARA WITO wetu na UTEULE WETU. Kama maandiko yanavyotuambia..

2 Petro 1:10 “Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi KUFANYA IMARA KUITWA KWENU NA UTEULE WENU; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe”.


Imarisha wito wako ewe Mteule. Ni wakati wa kumrudia Bwana pasipo mguu mmoja nje wala mguu mmoja ndani, kabla wakati wa kupasuka matumbo haujafika, kabla wakati wa kujutia kama Yuda haujafika, kabla wakati wa kula tonge la mwisho la Bwana, na shetani kukuingia haujafika, siku hiyo mlango utakuwa umefungwa, Yuda baada ya kulila lile tonge shetani alimwingia, ikawa ndio mwisho wake pale. Tengeneza wakati wako, linda wito wako na utendee kazi uteule wako.jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

UMEITIKIA WITO INAVYOPASWA?

JE! UMECHAGULIWA KABLA YA KUWEKWA MISINGI YA ULIMWENGU?

JE! KARAMA NI UTHIBITISHO WA KUWA NA MUNGU?


Rudi Nyumbani


Maran atha!

Print this post

TUKAZE MWENDO ILI TUUFIKILIE UTIMILIFU.

Mambo ya dunia hii yanatupa picha halisi ya mambo yanayoendelea rohoni, Kwamfano tukiangalia mataifa yaliyoendelea kama ya Ulaya, tukiyalinganisha na mataifa ambayo hayajaendelea kama vile ya Afrika, utagundua kitu kimoja cha tofauti, utaona watu wa huku wanapambana maisha yao yote ili kupata yale mahitaji ya msingi (Basic needs) kama vile Chakula, malazi na mavazi,.Na mtu aliyefanikiwa kuwa na hivyo vitu basi anaonekana tayari ametoka kimaisha ndio maana tunajulikana kama mataifa machanga..Lakini ukitazama yale mataifa yaliyoendelea utagundua kuwa vitu kama hivyo sio kipaumbele chao kwani karibu kila raia anao uhakika wa kupata mahitaji hayo ya msingi wengine tangu wanazaliwa tayari wanayo, kwani serikali tayari ilishaandaa mazingira mazuri kwa raia wao..

Wao kipaumbele chao kikubwa kipo katika mambo ya utafiti, utakuta jopo kubwa la watu limejikita katika mambo ya utafiti maisha yao yote, na matokeo yake ndio tunayoyaona sasa kwa teknolojia wanazozianzisha duniani, uwezo wa kusafiri katika anga za mbali na mambo ya mawasiliano n.k…Na hiyo ndio inayowafanya waonekane kuwa ni mataifa makubwa na watu wake waonekane kama ni watu bora kuliko wengine tukizungumza kibinadamu.

Vivyo hivyo katika mambo ya rohoni, Mtume Paulo aliona baadhi ya makanisa yapo katika hali ya Uchanga, kipindi kirefu kinapita hata wakati mwingine maisha yao yote lakini bado wanahangaika na mambo yale yale ya msingi ya awali, hawaonyeshi dalili ya kuendelea mbele, Watu wanataka kila siku wapigiwe kelele juu ya mafundisho yale yale ya awali,.wanyweshwe maziwa tu na sio vyakula vigumu vya rohoni, Sio kana kwamba Mtume Paulo alikuwa hawezi kuwafundisha mengine, hapana lakini alikuwa anaona kama tu yale ya msingi wanapata shida kuyatii haya mengi watawezaje?..

Na mafundisho yenyewe aliyoyoataja pale ni kama haya: Mafundisho ya TOBA, mafundisho ya kumwamini Mungu, Mafundisho ya Ubatizo, mafundisho ya ufufuo unaokuja, mafundisho ya Hukumu za Mungu zinazokuja, na mafundisho ya ukombozi(kuwekea watu mikono).

Ambayo kimsingi haya yote ni mafundisho ambayo kila siku tunajifunza na tunafundishwa, makanisani, mitandaoni, mikutanoni n.k..

Hapo Je! sisi si, watoto wachanga?, sisi si maskini wa kiroho?.

Waebrania 5:10 “kisha ametajwa na Mungu kuwa kuhani mkuu kwa mfano wa Melkizedeki.

11 Ambaye tuna maneno mengi ya kunena katika habari zake; na ni shida kuyaeleza kwa kuwa mmekuwa wavivu wa kusikia.

12 Kwa maana, iwapasapo kuwa waalimu, (maana wakati mwingi umepita), mnahitaji kufundishwa na mtu mafundisho ya kwanza ya maneno ya Mungu; nanyi mmekuwa mnahitaji maziwa wala si chakula kigumu.

13 Kwa maana kila mtu atumiaye maziwa hajui sana neno la haki, kwa kuwa ni mtoto mchanga.

14 Lakini chakula kigumu ni cha watu wazima, ambao akili zao, kwa kutumiwa, zimezoezwa kupambanua mema na mabaya”.

Waebrania 6 :1 “Kwa sababu hiyo, tukiacha kuyanena mafundisho ya kwanza ya Kristo, tukaze mwendo ili tuufikilie utimilifu; tusiweke msingi tena wa kuzitubia kazi zisizo na uhai, na wa kuwa na imani kwa Mungu,

2 na wa mafundisho ya mabatizo, na kuwekea mikono, na kufufuliwa wafu, na hukumu ya milele.

3 Na hayo tutafanya Mungu akitujalia”.

Hivyo kabla ya kumwomba Mungu atupeleke katika hatua nyingine ya kujifunza siri za ndani za Yesu Kristo, kama hizo ambazo mtume Paulo alizidokeza alipomfananisha na Melkizedeki, kwa jinsi Melkizedeki alivyokuwa hana baba, wala mama, wala mwanzo wa siku wala mwisho, na ndivyo Bwana wetu Yesu alivyokuwa, mfano wa Melkizedeki kuhani wa milele, kuna siri nyingine nyingi sana zimuhusuzo Bwana wetu Yesu Kristo hatuzijui bado , ambazo tukizijua hizo, hatutaishi kama tulivyo..

Kwasababu ni wazi kuwa bado Kristo anajifunua kwetu kila siku, mpaka Yule malaika wa 7 atakapokuwa tayari kupiga baragumu lake, hapo ndipo Siri yote ya Mungu itakapotimizwa.. Na itakapotilimilika SIRI hiyo (Ambayo inamuhusu Yesu Kristo mwenyewe), Mwisho wa kila kitu utakuwa umefika..

Ufunuo 10:5 “Na yule malaika niliyemwona, akisimama juu ya bahari na juu ya nchi, akainua mkono wake wa kuume kuelekea mbinguni,

6 akaapa kwa yeye aliye hai hata milele na milele, yeye aliyeziumba mbingu na vitu vilivyomo, na nchi na vitu vilivyomo, na bahari na vitu vilivyomo, ya kwamba hapatakuwa na wakati baada ya haya;

7 isipokuwa katika siku za sauti ya malaika wa saba atakapokuwa tayari kupiga baragumu; hapo ndipo siri ya Mungu itakapotimizwa, kama alivyowahubiri watumishi wake hao manabii”.

Hivyo tumwombe Mungu atusaidie tuvute katika hii hatua ya uchanga tuliyopo sasa, Tusifurahie tu wakati wote kuhubiriwa habari za kutubu dhambi, na kubatizwa,..hayo ni maziwa ndugu, bado hatujaanza kula chakula, Tukiweza kuvuka hayo ndipo Mungu atakapotupeleka katika hatua nyingine..Toba na Ubatizo ni mafundisho ya awali ya msingi, lakini jengo lenyewe bado halijasimama…Lengo ni kupandisha jengo sio msingi, ndio maana tunahitaji kukua kila siku…

TUKAZE MWENDO ILI TUUFIKILIE UTIMILIFU.

Shalom. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

VIGEZO VYA KUWA KARIBU NA YESU KRISTO KATIKA ULIMWENGU UJAO.

UMEIZALIA MATUNDA MIAKA 4 YA NEEMA ULIYOPEWA?

SAUTI AU NGURUMO?


Rudi Nyumbani

 

Print this post

YAKUMBUKE YA NYUMA.

Nguvu ya kuendelea mbele tunaipata kwa kutazama tulipotokea…Usipokuwa na jicho la kutazama ulipotokea, usipokuwa na jicho la kukumbuka ni wapi ulipitia, utaishia kuwa mtu wa kunung’unika na kulalamika …

Ili tuweze kuishi Maisha ya ushindi siku zote katika haya Maisha ya hapa duniani, ni lazima tuishi Maisha ya kutafakari ni mambo gani ya nyuma Mungu aliyotutendea….unatazama kama Mungu wakati fulani alikupigania kwa kile, wakati huu atanipigania pia kwa hichi, Imani ndio inapokuja hapo..Ukishindwa kukumbuka ya nyuma kamwe hutaweza kuyashinda yanayokuja.

Ndio maana kuna umuhimu mkubwa sana, wakati mwingine kuandika chini, mambo yote makubwa na madogo Mungu anayokutendea ili usisahau, hiyo itakusaidia pindi utakapokutana na tatizo kama hilo basi utakumbuka kirahisi uweza wa Mungu aliokupigania huko nyuma na utapata nguvu mpya.

Uweza wa Mungu unadhihirika mahali palipo na Imani, na Imani haiwezi kuja kama utayasahau matendo makuu ya Mungu aliyokutendea nyuma…Ndicho kilichowatokea wana wa Israeli wakati wanatoka Misri, ilikuwa kila mara wanasahau mambo makuu Mungu aliyowatendea nyuma na hivyo kuishia kumdharau Mungu kwa mambo madogo yanayotokea mbele yao, Walipotuma wapelelezi kuipeleleza nchi ya Kaanani na kukuta wenyeji wa kule ni majitu makubwa, badala wakumbuke kuwa Mungu alishawapigania huko nyuma kumwangusha Farao ambaye alikuwa na nguvu kuliko hayo majitu, wao wakasahau na kuanza kujiona nafsi zao kama mapanzi, hivyo ikawa dhambi kubwa mbele za Mungu,

Hayo yamewapata ili kutuonya sisi watu wa zamani hizi, tunapaswa tukumbuke uweza wa Mungu..aliotutendea huko nyuma pindi tunapokutana na jaribu fulani mbele yetu..Hata mwanafunzi ili aweze kulipata swali kisahihi, ni lazima awe na uwezo wa kukumbuka ni wapi alishafanya swali kama hilo, na wapi mtego wa swali hilo upo..asipokuwa na uwezo huo kila kitu kwake kitakuwa ni kipya.

Na ndio maana katika agano la kale Wanyama ambao walikuwa hawacheui walijulikana kama najisi, Mnyama anayecheua ni ambaye anao uwezo wa kula chakula na kukihifadhi tumboni baadaye anakirudisha na kikitafuna tena na kukimeza kama vile ng’ombe,..Inafunua kuwa sisi kama wanyama wa Kristo tusio najisi, tunapaswa tuwe na uwezo wa kukumbuka mambo yote makuu Mungu aliyotutendea nyuma, huko ndio kutafuna tena kile tulichokula, lakini tukiwa wasahauji, ndio yatatukuta kama yale ya wana wa Israeli.

1 Wakorintho 10:9 “Wala tusimjaribu Bwana, kama wengine wao walivyomjaribu, wakaharibiwa na nyoka.

10 Wala msinung’unike, kama wengine wao walivyonung’unika, wakaharibiwa na mharabu.

11 Basi mambo hayo yaliwapata wao kwa jinsi ya mifano, yakaandikwa ili kutuonya sisi, tuliofikiliwa na miisho ya zamani.

12 Kwa hiyo anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke

Unapopitia kupungukiwa kidogo, kumbuka kuna kipindi ulipitia hali ngumu kuliko hiyo na Mungu alikufungulia mlango, hivyo tumia huo ushuhuda kukabili tatizo lililopo sasa, useme kama Mungu alinipigania kipindi kile cha taabu atanipigania na sasahivi, kwasababu Mungu ni yule yule habadiliki!…Kama unapitia ugonjwa fulani sasa, kumbuka kipindi fulani nyuma ulipitia ugonjwa wa hatari na Bwana akafungua mlango wa wewe kupona…tumia huo ushuhuda kukataa mawazo ya kukata tamaa sasa..

Kama umezungukwa na hatari, au unakabiliana na hatari, au tatizo mbele yako, sio wakati wa kupaniki, ni wakati wa kurudisha kumbukumbu zako nyuma na kukumbuka Bwana alivyokuokoa kwenye mikono ya waovu, na alivyokuepusha na hatari kimiujiza miujiza.n.k n.k, na kusema kama alifanyia vile, atanifanyia na hata sasa vile vile kama aliwafanyia wale, atakufanyia na wewe,…Mungu aliwaambia wana wa Israeli maneno haya wakati wanakwenda kukabiliana na maadui zao katika nchi ya Kaanani..

Kumbukumbu 7:17 “Nawe kama ukisema moyoni mwako, Mataifa haya ni mengi kunipita mimi; nitawatoaje katika milki yao?

18 Usiwaogope; KUMBUKA SANA Bwana, Mungu wako, alivyomfanya Farao na Misri yote;

19 uyakumbuke hayo majaribu makuu yaliyoyaona macho yako, na hizo ishara, na maajabu, na mkono wa nguvu, na mkono ulionyoka, aliokutolea nje Bwana, Mungu wako; ndivyo atakavyowafanya Bwana, Mungu wako, mataifa yote unaowaogopa.

20 Tena Bwana, Mungu wako, atampeleka mavu kati yao, hata hao watakaosalia, hao wajifichao, waangamie mbele zako.

21 Usiingiwe na kicho kwa sababu yao; kwa kuwa Bwana, Mungu wako, yu katikati yako, Mungu mkuu, mwenye utisho.”

Bwana akubariki!, kama utapenda kujifunza Zaidi na kwa urefu juu ya “kukumbuka wema wa Mungu, aliokufanyia nyuma” unaweza kufungua ujumbe huu >>> MAISHA ULIYOPITIA NYUMA NI USHUHUDA TOSHA WA WEWE KUMTUMIKIA MUNGU

Maran atha! . jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Print this post

JINSI ROHO MTAKATIFU ANAVYOKUJA JUU YA MTU.

Katika agano la kale, wayahudi walivyochanganyikiwa sana juu ujio wa masihi mpaka kupelekea kugawanyika makundi mengi, ndivyo ilivyo hata katika agano jipya watu wengi wanavyochanganyikiwa katika habari ya Roho Mtakatifu jinsi anavyokuja juu ya mtu, hadi sasa imepelekea kutokea makundi mengi tofauti tofauti ambalo kila moja linaamini katika uthibitisho wake.

Kama tunavyofahamu katika agano la kale biblia ilishatabiri kuwa Masihi (YESU KRISTO) atakuja, lakini kwa bahati nzuri au mbaya haikueleza katika mtitiriko unaoeleweka sana, bali sisi wa agano jipya kwa Kutazama maisha ya Kristo ndio tunaoelewa jinsi maandiko yalivyotimia ,..Lakini katika agano la kale ilikuwa ni ngumu sana kuelewa, na saa nyingine maandiko yaliyonekana kama yanajichanganya..Kwamfano unabii alioutoa Isaya kuhusu Kristo katika (Isaya 53), inaonyesha kuwa Masihi atakuja kuteswa na kuuliwa kwa ajili ya dhambi za watu wengi..Lakini sehemu nyingine katika kitabu hicho hicho cha Isaya inasema Masihi atakuwa mfalme, naye ataketi katika kiti cha enzi cha Daudi, naye atadumu milele.

Unaona sehemu moja inasema atakufa lakini sehemu nyingine inasema atadumu milele,..Lakini je! Wale walioshikilia tu unabii mmoja labda tuseme wale walioamini kuwa Masihi atasulibiwa, au wale walioamini tu Masihi ataishi milele, je! wote Hawapo sawa? Jibu ni La!..Sisi tunaoishi katika agano jipya ndio tunaojua kuwa Wote wapo sawa kabisa, lakini wote walioweza kuamini nabii zote mbili ndio wapo sawa zaidi kuliko wale wengine, kwani ni Kweli kuna wakati Kristo atasulibiwa atakufa lakini atafufuka na atarudi tena, na atakaporudi atakuja kama Mfalme wa Wafalme na Bwana wa Mabwana, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho kama nabii zote mbili zilivyotabiri.

Yohana 2:33 “Aliyanena hayo akionyesha ni mauti gani atakayokufa.

34 Basi mkutano wakamjibu, Sisi tumesikia katika torati ya kwamba Kristo adumu hata milele; nawe wasemaje ya kwamba imempasa Mwana wa Adamu kuinuliwa? Huyu Mwana wa Adamu ni nani?

35 Basi Yesu akawaambia, Nuru ingaliko pamoja nanyi muda kidogo. Enendeni maadamu mnayo nuru hiyo, giza lisije likawaweza; maana aendaye gizani hajui aendako”.

Sasa tukirudi katika habari za Roho Mtakatifu, kama tusipoweza kuyavunja maandiko na kufahamu utendaji kazi wake, tutaishia kuchanganyikiwa sana, na mwisho wa siku kila mmoja ataamini anachokiamini…

Leo hii kuna watu wanaomini kuwa uthibitisho pekee wa mtu kuwa na Roho Mtakatifu ni kudhihirisha karama Fulani ndani yake, kama vile kunena kwa lugha, kutoa unabii, kufundisha, kuhubiri n.k…na mtu yeyote asipodhihirisha mojawapo ya karama yoyote basi huyo bado hajapokea Roho Mtakatifu na maandiko wanayoyasimamia ni haya …

Matendo 2:17 “Itakuwa siku za mwisho, asema Mungu, nitawamwagia watu wote Roho yangu, na wana wenu na binti zenu watatabiri; na vijana wenu wataona maono; na wazee wenu wataota ndoto.

18 Naam, na siku zile nitawamwagia watumishi wangu wanaume na wanawake Roho yangu, nao watatabiri”

Na ….

1Wakoritho 12:4 “Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule”:

Vile vile wapo wengine wanaoamini kuwa uthibitisho wa Roho Mtakatifu, ni kuwa atakuongoza na kukutia katika kweli yote sawasawa na Yohana 16:13 “Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa kweli, atawaongoza awatie kwenye kweli yote; kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo atawapasha habari yake.” ….

na hivyo uthibitisho mwingine wowote mbali na huo ni uongo..

Halikadhalika wapo wanaoamini kuwa uthibitisho pekee wa Roho Mtakatifu ni pale anapokushuhudia ndani yako kuwa wewe ni mwana wa Mungu, …sawasawa na Warumi 8:16 “Roho mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu;”

Wapo wengine wanaoamini uthitisho wa Roho Mtakatifu peke yake ni kukufanya uwe mtakatifu kama vile jina lake lilivyo.…

Na makundi mengine mengi…

Lakini swali ni kama lile lile tu la watu wa agano la kale, je! Wote hawa ni waongo?…Jibu ni hapana wote wapo sawa kabisa!!, isipokuwa tu wanashindwa kutofuatisha utendaji kazi wa Roho Mtakatifu juu ya mtu kulingana na wakati na majira. Kama tu vile wale wa agano la kale walivyoshindwa kufahamu kuwa kuna kuja kwa kwanza kwa Kristo na kuja kwa pili.

Ifahamike kuwa Bwana Yesu aliposema hakuna mtu anaweza kuja kwake kama hakuvutwa na Baba yake aliyempeleka, alimaanisha kusema vile, Leo hii “huwezi hata kuchomwa moyo na maneno ya Mungu kama siyo matunda ya Roho Mtakatifu yanayofanya kazi ndani yako”, ukiona tu unaamini kuna Mungu, ukiona unatamani kumfahamu Mungu hata kama hujaokoka, ukiona unahukumiwa ndani yako kwa ajili ya dhambi zako, ukiona una hofu ya Mungu, basi ufahamu kuwa huyo ni Roho Mtakatifu anatenda kazi ya kukuvuta kwake,..Jambo ambalo si watu wote wanalo, usidhani kuwa injili unayoisikia na kukuchoma moyo inamchoma kila mtu duniani, dhambi uzifanyazo na kusikia kuhukumiwa zinamuhukumu kila mtu duniani, kama ingekuwa hivyo kusingekuwa na vitendo vya kinyama unavyoviona kila mahali..Si wote wapo hivyo, na ndio maana hupaswi kuichezea hiyo neema kwasababu kuna wakati utafika Roho Mtakatifu hatakuvuta tena kwa Mungu, ukishafika huo wakati ndugu, hata Bwana Yesu mwenyewe akutokee hapo, na malaika wote mbinguni, hutakaa ugeuke, kwasababu Roho wa kukuvuta hayupo.

Sasa, ikitokea mfano Yule mtu akautii ule wito na kuamua kutubu dhambi zake, na kufuata vigezo vyote alivyoambiwa na Bwana Yesu vya kwenda kubatizwa, katika maji mengi na kwa Jina la BWANA YESU, hapo ndipo Yule Roho aliyekuwa anamvuta anapata kibali cha kuingia ndani yake, na kufanya maskani humo, na akishaingia anakuwepo huko milele, mtu huyo ndio anakuwa amezaliwa mara ya pili..Sasa kwa kuwa Yule mtu bado ni mchanga kiroho, Roho Mtakatifu anaanza kazi kadha wa kadha ndani yake..mojawapo ni kumsafisha na kuua baadhi ya vitu ambavyo alikuwa hawezi kuviacha, Roho Mtakatifu anamfanya upya tena..

Tito 3:5 “si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu;’’

Anaanza kumfanya aupende utakatifu kuliko kitu kingine chochote, hapo ndipo hamu ya baadhi ya mambo ya kidunia inakufa kabisa…hizo ni dalili za awali kuwa Roho Mtakatifu yupo ndani yako..Kwa nje unaweza usione chochote, wala usisikie msisimko wowote lakini ndani kunawaka moto wa kutaka kuwa kama Mungu..

Pili anatenda kazi ya kumwongoza na kumtia katika kweli yote: Hapa Anaanza kumwongoza katika vyanzo sahihi vya Neno lake, anaanza kumpa kiu ya kujifunza Neno la Mungu, faraja yake mtu huyo inakuwa kwenye Neno la Mungu tu, na si mahali pengine, anaanza kuona Mungu kwake ndio kila kitu..Uthibitisho ni kuwa hapo kabla hayo mambo alikuwa hayaoni…Ile kiu inaongezeka siku baada ya siku.

Jambo lingine analolifanya Roho Mtakatifu ni kumshuhudia huyo mtu kuwa yeye ni mwana wa Mungu, kushuhudiwa huku sio kusikia sauti inakuambia wewe ni mwana wa Mungu, hapana, bali ni kuona maisha yako unayopitia yanafanana na wana wote wa Mungu waliopita huko nyuma,…..yaliyowapata watakatifu wa nyuma na wewe yanakupata yawe ni mema yawe ni mabaya..Biblia ndio itakuwa uthibitisho wako..Mungu kwako anajidhihirisha kama Baba.

1Petro 5:9 “….mkijua ya kuwa mateso yale yale yanatimizwa kwa ndugu zenu walioko duniani.”

Jambo lingine ni anakuwa kwako kama mfariji, na mshauri(1Thesalonike 1:16, 2Wakoritho 13:14)): Utaona tu, jinsi atakavyokuwa anakutia nguvu wakati baada ya wakati, unapoishiwa nguvu, utashangaa anaachilia jambo Fulani kubwa ambalo linakupa nguvu ya kuendelea mbele kwa muda mrefu sana…Na ndio maana tunasema mtu yeyote aliye na Roho Mtakatifu kweli hawezi kuishia njiani katika safari yake ya wokovu..(Isaya 40:27-31)

Na ndio maana katika hicho kipindi chote Roho wa Mungu anachokutengeneza, hupaswi kumzimisha,..Wengi wanamzimisha kwa kuanza kuyarudia yale machafu waliyoyaacha huko nyuma, tayari Mungu alishawafanya kuwa huru, lakini bado wanaurudia utumwa..Hapo ndipo mtu hakui wala hasongi mbele kiroho, anabakia kuwa katika hali ile ile, miaka nenda miaka rudi..yeye ni mchanga tu.

Lakini ikiwa mtu huyu atatembea na Roho Mtakatifu kwa uaminifu wote, Roho anakuwa anajaa ndani yake kidogo kidogo, mpaka anafikia ujazo kamili wa Roho Mtakatifu, na ujazo huo ni uhitimu. Hapo ndipo Roho Mtakatifu anakuvika nguvu za kuweza kuwa shahidi wake, kama vile Bwana Yesu alivyoaambia mitume wake..

Matendo 1:8 “Lakini mtapokea nguvu, akiisha kuwajilia juu yenu Roho Mtakatifu; nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi”.

Hichi ndio kile kilichomkuta Bwana Yesu wakati ule anakwenda kubatizwa, sio kana kwamba ile ndio ilikuwa mara yake ya kwanza kumpokea Roho hapana bali Roho alikuwa naye tangu kuzaliwa kwake, lakini kwasababu ya kazi ilimpasa Mungu amwongezee nguvu kwa Roho Yule aliyekuwa ndani yake ili kushuhudia habari za ufalme wa mbinguni. Na ndicho kilichokuwa juu ya Mitume sio kwamba kipindi walichokuwa wanatembea na Bwana walikuwa hawana Roho Mtakatifu, walikuwa naye, ndio yule aliyemfunulia Petro kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu n.k isipokuwa walikuwa naye si katika kile kiwango kile Mungu alichokikusudia kwa kazi yake waliyokuwa wanakwenda kuifanya hapo mbele.

Ndivyo ilivyo hata sasa, wengi tunatamani tupokee Roho Mtakatifu katika hatua ya mwisho, lakini sio kuanzia katika hatua ya kwanza.. siku hiyo hiyo tumempa Kristo maisha yake, bado siku hiyo hiyo wanataka Roho Mtakatifu atupe nguvu ya kuwa mashahidi wake kwa mfano wa mitume,..Ni kweli Roho anaweza kufanya yote kwa pamoja, lakini fahamu kuwa ndani yake, bado utakaa chini tu akufundishe,atembee na wewe, akuandae na akuthibitishe.

Hivyo kaka/dada, fahamu kuwa Roho Mtakatifu ni zaidi ya kunena kwa lugha, au kuona maono..Usifurahie kusema tu nilipokea Roho Mtakatifu siku ile nilipoamini,,jiulize je! Hadi sasa Roho Mtakatifu anatembea na wewe, au ulishamzimisha siku nyingi..Je! anakurudisha katika utakatifu?, Je! Anakushuhudia kuwa wewe ni mwana wa Mungu. Je! Anakuongoza katika kweli yote..Je! anakupasha bahari ya mambo yanayokuja?..Ikiwa hivi vitu vimekufa ndani yako, tubu upesi umgeukie Mungu, mwambie Bwana nataka nianze na wewe upya.

Na ikiwa bado Roho Mtakatifu yupo mbali na wewe nikimaanisha kuwa hujamkabidhi bado Bwana maisha yako, fahamu kuwa biblia ipo wazi inasema, Warumi 8:9… “Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake”.

Pasipo huyo, usidhani kuwa utaiona mbingu, au utamfahamu Mungu..Tubu leo kwa kumaanisha kumfuata Kristo itii injili, kisha nenda kabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi, na kwa jina la Bwana Yesu Kristo, Roho Mtakatifu aingie ndani yako na aanze kufanya kazi kwako.

Bwana akubariki sana. Tafadhali “Share” Ujumbe huu kwa wengine. Na Bwana atakubariki. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazondana:

Je! Umepokea kweli Roho Mtakatifu?

Hatua za Roho Mtakatifu katika kutuongoza.

Je! karama ni uthibitisho pekee wa kuwa na Mungu?

HOME

Print this post

UDHAIFU WA SADAKA!

Moja ya nguzo muhimu sana katika Imani ya Kikristo ni SADAKA, Sadaka ni nguzo muhimu sana, kwasababu hata Kristo mwenyewe alifanyika sadaka kwa ajili yetu ili sisi tuokolewe…Kama Kristo asingejitoa nafsi yake kwa ajili yetu sisi tusingekuwa popote, tungekuwa ni wana wa Jehanamu wote, hakuna hata mmoja ambaye angepona.

Kwahiyo kama Kristo alivyojitoa kwetu na sisi pia lazima tujitoe kwa wengine…Ndio maana sadaka ni Muhimu, Roho iliyokuwa ndani ya Kristo ilimpeleka kujitoa nafsi yake kuwa fidia kwa roho nyingi, halikadhalika na sisi kama tumeipokea Roho ile ile ambayo ilikuwa ndani yake, ni lazima itatusukuma na sisi kujitoa kwa ajili ya wengine, kulingana na karama tulizopewa…

Sadaka sio lazima kutoa mali, bali hata kujitoa Maisha ili kwamba wengine wapate uzima, kama Bwana Yesu hakutoa fedha ili sisi tuokolewe bali aliitoa damu yake na Maisha yake kwa kuishi na kufundisha watu njia ya wokovu ili waokolewe. Hiyo ni sadaka kubwa sana na kuu kuliko zote, kutoa Maisha kwaajili ya mwingine ili aokoke. Kama Biblia inavyotuambia katika..

1 Yohana 3:16 “Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu”.

Na sadaka sio mchango. Mchango ni kitu unachotoa kuchangia jambo Fulani liendelee mbele lakini sadaka, ni kitu kinachohusisha wewe kupungukiwa ili mwingine aongezewe, au wewe kupoteza ili mwingine apate, hiyo ndiyo maana ya sadaka…haina tofauti sana na neno MUHANGA..Kwahiyo sadaka ni KITU kikubwa Zaidi ya Mchango…Hivyo unapomtolea Mungu sadaka kwaajili ya kazi yake, zingatia kutoa kitu kikubwa Zaidi ya mchango, toa kitu ambacho kimekugharimu sana….ukitoa mchango utapata thawabu lakini sadaka ina thawabu kubwa Zaidi.

Sasa leo hatutaingia sana kuzungumzia Umuhimu wa Sadaka au nguvu ya sadaka, lakini tutazungumzia UDHAIFU WA SADAKA.

Utauliza, sadaka ina madhaifu?..Jibu ni ndio, sadaka ina madhaifu na mipaka..Inayo nguvu ya kubadilisha mambo lakini pia inayo mipaka ambayo haiwezi kupita..kuna mambo ambayo haiwezi kubadilisha…Hebu tusome mistari michache ifuatayo kisha tuendelee…

1 Samweli 15:20 “Sauli akamwambia Samweli, Hakika mimi nimeitii sauti ya Bwana, nami nimemleta Agagi, mfalme wa Waamaleki, tena nimewaangamiza Waamaleki kabisa.

21 Ila watu waliteka nyara, kondoo na ng’ombe walio wazuri, katika vitu vilivyowekwa wakfu, kusudi wavitoe dhabihu kwa Bwana, Mungu wako, huko Gilgali.

22 Naye Samweli akasema, je! Bwana huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu Sawasawa na kuitii sauti ya Bwana? Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, Na kusikia kuliko mafuta ya beberu.

23 Kwani kuasi ni kama dhambi ya uchawi, Na ukaidi ni kama ukafiri na vinyago; Kwa kuwa umelikataa neno la Bwana, Yeye naye amekukataa wewe usiwe mfalme”.

Habari hiyo inamzungumzia Mfalme wa kwanza wa Israeli aliyeitwa Sauli, ambaye alilikaidi Neno la Mungu, aliambiwa akaangamize vitu vyote na watu wote (Waamaleki) asiache chochote, hata ng’ombe na mbuzi na kondoo wote auwe, lakini yeye akaangamiza vyote lakini akawaacha wafalme wa ile nchi hai pamoja na ng’ombe walionona na kondoo na kuvileta Israeli kwaajili ya kumtolea Mungu dhahibu, (dhabihu ni sadaka ya kuteketezwa). Kwa moyo wake alijua Mungu anapendezwa Zaidi na Sadaka kuliko kuyashika maagizo yake.. Hakujua kuwa nguvu ya sadaka sio kubwa kuliko nguvu ya kushika maagizo yake. Hivyo akajitumainisha kwa sadaka zile na Mungu akamkataa..

Huo ndio udhaifu wa Sadaka!..Ni kweli Mungu aliagiza watu wamtolee sadaka zilizonona, tena wasimtolee vilema, kwasababu ukimtolea sadaka kilema ilikuwa ni kujitafutia kulaaniwa badala ya kubarikiwa.(soma Malaki 1:13-14). Lakini sadaka hiyo hiyo, ina mipaka. Haiwezi kubadilisha mambo yote, haiwezi ikalivuka Neno la Mungu. Hatuwezi kumuonga Mungu kwa sadaka zetu, ili abadilishe Neno lake..Hapana! tutaongeza baraka tu kwa sadaka lakini si kulibadilisha Neno lake, akisema kuwa roho ya mwenye dhambi itakufa, hata tutoe fedha kiasi gani kama hatutalitii hilo neno na kuacha dhambi! Hizo sadaka hazina msaada wowote, kufa tutakufa tu!…Akisema waasherati na walawiti na waabudu sanamu sehemu yao ni katika lile ziwa la moto! Hata tutoe hazina zote za ulimwengu na kujitoa hata miili yetu, kama hatutatii na kuacha hivyo vitu…Jehanamu haiepukiki.

Sasa habu tuangalie mfano wa Mwisho ambao ni Bwana Yesu mwenyewe aliuota kuonesha udhaifu wa Sadaka!..Tusome.

Mathayo 5:23 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako,

24 iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.

25 Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani.

26 Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho”

Mfano huo Bwana Yesu alioutoa kutufundisha kuwa tusiitegemee sadaka, kubadilisha Neno la Mungu..Katika habari hiyo anasema “kabla ya kuitoa sadaka yako, patana kwanza na mshtaki wako”…Ikiwa na maana kwamba kama kuna mtu anakudai, au kuna mtu umemdhulumu, au kuna mtu umegombana naye, na wewe ndiye mwenye makosa na hivyo bado kidogo atakwenda kukushitaki… usikimbilie kwenda kutoa sadaka! Kana kwamba hiyo sadaka uliyoitoa itakukuokoa….Kitu cha kwanza Kimbilia kwanza kwenda kupatana naye, kwasababu usipopatana naye ukachelewa kidogo tu! na yeye akaenda kuripoti polisi, na polisi wakaja kukuchukua na kukuweka ndani! Biblia inasema hutatoka huko…Na hiyo sadaka uliyoitoa ambayo ulitegemea kukusaidia, wakati huo haitakusaidia chochote kukutoa huko gerezani…Mungu hatakuwa upande wako hata kidogo…Hivyo Bwana anasema…Nenda kwanza kapatane naye kabla hajakwenda kukuripoti…sadaka utatoa tu! Nenda kwanza kapatane naye! kwasababu Neno lake linasema…

Warumi 12:18 “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote”.

Sasa ukikaa kwa vurugu na watu wote, hata utoe fedha kiasi gani kwa Mungu! Haitaruka Neno lake hilo kwamba “mkae na amani na watu wote”…Huo ndio udhaifu wa sadaka, haipiti Neno la Mungu….. “kutii ni bora kuliko dhabihu na kusikia kuliko Mafuta ya Beberu”.

Hivyo ndugu, inawezekana unatoa sadaka nyingi nzuri sana, hilo ni Jema Mungu atakulipa kwa ukarimu wako, lakini sadaka hiyo haiwezi kulipita Neno la Mungu linalosema…

Ufunuo 21:8 “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili”.

Wala kulipita Neno hili..

Wagalatia 5:19 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,

20 ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,

21 husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu”.

Sadaka nzuri ni ile inayoambata na kulitii Neno la Mungu.

Uchaguzi unao wewe ambaye hujampa Kristo Maisha yako!..Kumwamini Yesu, na kutubu na kuamua kumgeukia huku ukidhamiria kuacha dhambi kabisa, utakapoamua kugeuka na kusema Kuanzia leo hii mimi na ulimwengu basii!! Kristo akiiona nia yako ndani yako kwamba kweli umedhamiria kuacha kwa vitendo, basi atakupa nguvu ya Roho wake Mtakatifu ambaye atakusadia kuweza kuzishinda dhambi kama ulivyosema kutoka katika kinywa chako mwenyewe. Mlango wa Neema bado upo wazi, lakini tunaishi kipindi cha kumalizia, ambapo parapanda siku yoyote inalia na watakatifu wataondolewa ulimwenguni, na ulimwengu kuharibiwa. Hivyo usikiapo maneno haya usifanye moyo wako mgumu, kama ulishampa Kristo Maisha yako, lakini umekuwa vuguvugu ni wakati wakuwa moto, kwasababu walio vuguvugu wote, Kristo alisema atawatapika. 

Bwana akubariki.

Maran atha! .jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

NATAKA REHEMA, WALA SI SADAKA!

ALIFANYIKA SADAKA KWA AJILI YETU!

TOFAUTI KATIKA YA ZAKA NA SADAKA NI IPI?

SADAKA ILIYOKUBALIKA NI IPI?


Rudi Nyumbani

Print this post

USITAFUTE FAIDA YAKO MWENYEWE BALI YA WENGINE.

1 Wakorintho 10:23 “Vitu vyote ni halali; bali si vitu vyote vifaavyo. Vitu vyote ni halali; bali si vitu vyote vijengavyo

24 Mtu asitafute faida yake mwenyewe, bali ya mwenzake.

25 Kila kitu kiuzwacho sokoni kuleni, bila kuuliza-uliza, kwa ajili ya dhamiri;

26 maana, Dunia ni mali ya Bwana na vyote viijazavyo.”

Hapo biblia inasema “vitu vyote ni halali” na inasema pia kila kitu kiuzwacho sokoni kuleni, bila kuuliza uliza…

Sasa tunajua sokoni kuna vitu vingi vinauzwa, sio tu chakula, bali hata nguo, viatu, vyombo, vifaa mbali mbali, simu,tv n.k..Hivyo aliposema kila kitu kinachouzwa sokoni tule pasipo kuuliza uliza, tunapaswa tutumie hekima na sio kutafsiri tu mstari kama tunavyousoma…hivyo pale hakumaanisha kuwa kila kitu kinachouzwa sokoni kama kiatu, pombe,mabegi, nguo, sumu za panya, majembe, na mashoka tuyale! Tuyale kwasababu tu yanauzwa masokoni na maandiko yamesema kila kitu kinachouzwa tule bila kuuliza uliza.. Tukitafsiri maandiko kwa namna hiyo, hatutapata chochote!..Ndio maana pia inachanganya wengi sana, pale Mtume Paulo aliposema “nataka ninyi nyote mnene kwa lugha 1 Wakoritho 14:5” na kuutafsiri mstari kama unavyosomeka pale..bila kuelewa kwanini Mtume Paulo alisema vile…

Tunapaswa tuingie ndani ya mstari huo na kujua Maandiko yalikuwa yanamaanisha nini kuwa ‘kila kitu kinachouzwa sokoni tule bila kuuliza uliza’..

Aliposema kila kitu kuizwacho tule, alikuwa anazungumzia katika engo ya vyakula! Sio bidhaa nyingine tofauti na chakula ambazo zinauzwa masokoni, alikuwa anazungumzia tofauti ya aina ya vyakula, kwamfano umeenda China leo kuhubiri wenyeji wakakukaribisha na kukupeleka kwenye masokoni yao ya umma wanaponunuaga vyakula…na huko ukakuta kuna aina ya vyakula tofauti na vile ulivyovizoea kuviona vinauzwa katika jamii yako ya kiafrika..ukakuta pengine samaki wamechanganywa na majani ya mimea Fulani ambayo hujaijua bado, au nyama ya kuku imepikwa na kuchanganywa na vitu usivyovijua bado.. na wakaenda kukuandalia,Hapo ndio unaambiwa usiulize ulize wewe kula! Bila kuuliza uliza kwamba ni nyama ya kiumbe gani imetengenezewa. Wala usiwe na hofu moyoni mwako kwamba unamkosea Mungu wewe kula hivyo vyakula.. kwaajili ya dhamira zao.

Kwasababu wakikuona wewe unakataa kula aina Fulani ya chakula ambacho hata sio kilevi, bali pengine ni mchanganyiko tu wa vitu usivyovifahamu, wataanza moyoni kushtuka na kujiuliza kwanini huyu mtu hali chakula chetu! Ambacho sisi tunaona ni cha heshima, Kwahiyo watakuwa na maswali mengi ambayo hayana msingi wowote wa kuwavuta wao kwa Kristo, kwasababu hata hicho unachokataa wewe kukila Mungu hajasema usikile! Lakini endapo wamekwambia kwamba hichi ni chakula cha miungu yetu! Hapo utakataa ili wao wasije wakaona kwamba na wewe unakubaliana na wanachokifanya, lakini si kwasababu chakula kile ni najisi.

Au fikiria Mchina anakuja huku kwetu unamkaribisha kwako na unampikia mtori asubuhi, unamtengea ghafla! Anakwambia subiri kwanza! Huu mtori umetengenezwa na nini? Anataka umwelezee kila kitu kabla yeye hajaanza kula!!..kwa mtu mwenye roho nyepesi anaweza akakwazika kwa kitendo hicho tu!..Na kuanza kusema moyoni kwani huyu mtu ananifikiriaje?, anadhani mimi ninaweza kumwekea sumu? Au naweza kumwekea kilevi,? Au anakidharau chakula chetu! Au anatuonaje labda! Na mambo kama hayo!..Lakini utakapoona umemwandalia na yeye akakipokea vizuri hata kama hakula kingi, ni wazi kuwa moyoni mwako utafurahi na ni rahisi Zaidi kukipokea kile alichokileta kuliko endapo angekataa au kuanza kukitolea kasoro chakula chako…

Sasa mambo kama hayo ndio Biblia inasema tuyaepuke! Unapofika ugenini ni Dhahiri kuwa wanajua wewe ni mhubiri au mkristo, hivyo hawawezi kukuwekea sumu mezani, wala kilevi kwasababu ulishawahubiria, hivyo ukitengewa kula bila kuuliza uliza. Ili ndani ya dhamiri zao wasije wakajikwaa, na kukikosa hata kile kizuri ulichowapelekea. Hivyo wakati mwingine hata kama umefika mahali wamekutengea vyakula ambavyo huvipendi, kula tu hata kidogo ili mioyoni mwao wasije wakakwazika na kukikataa hata kile kizuri cha rohoni ulichowapelekea. Na sio tu unapokwenda kuhubiri hata unapoalikwa na rafiki yako au mtu yeyote usiwe mtu wa kuuliza uliza.

Sasa endapo ukiwa sokoni peke yako una uhuru wa kuchagua upendacho, , lakini kwa watu wenye Imani changa, epuka uchaguzi uchaguzi mbele yao, ni rahisi kuwapoteza…

Fanya vitu kwa faida ya wengine na sio faida yako wewe.

Kadhalika, unapokwenda kumhubiria kahaba, usifike tu na kumhukumu kwa mwonekano wake kwa mara ya kwanza, wala usikatae kumkaribisha kwako akiwa na mavazi yake ya kikahaba, ukimshutumu kwa mara ya kwanza tu kwa mwonekano wake pasipo hata kumhubiria chochote ni rahisi kumpoteza moja kwa moja, ataishia kukuchukia tu! Ndani ya dhamiri yake na kujiepusha na wewe.

Lakini ukaanza kumweleza kwanza mambo ya msingi, habari za Yesu Kristo na tumaini analotoa na hatima ya mambo yote ya ulimwengu huu, ataguswa moyo hata kama sio siku hiyo hiyo lakini baada ya muda Fulani atakwambia nifanyaje au yeye mwenyewe utaona anaanza kubadilika…Bwana Yesu alipokutana na yule mwanamke Msamaria kisimani habari ya kwanza hakuanza na kumwambia wewe ni kahaba, unawaume watano…

hakumwambia hayo mambo, alianza kuzungumza naye habari za ufalme wa mbinguni kwanza, baadaye sana ndipo alipoanza kumwambia habari za Maisha yake kuwa ana waume watano, na huyu aliyenaye sio wake..lakini angeanza tu kwa kumwambia wewe ni kahaba utakwenda motoni! Unadhani ni nini kingetokea? Hapo hakufanya jambo kwa faida yake binafsi, bali kwa faida ya ufalme wa Mbinguni.

Kadhalika unapomhubiria mtu asiye wa Imani yako labda muislamu, asiyejua chochote kuhusu Imani ya kikristo usianze kwa kumwambia unajua kula nguruwe ni ruksa!..sio najisi?..Hivyo kula nguruwe! Huku unamwonyeshea mistari….Ukifanya hivyo ataishia kukuchukia tu na pengine kuanzisha malumbano…Anza kwa kumweleza Habari za Yesu Kristo, na nguvu ya msalaba…hayo mambo mengine yatakuja baadaye sana…kwani asipokula nguruwe Maisha yake yote, siku ile ya hukuma Bwana atamwuliza kwanini ulikuwa huli nguruwe duniani?..unaona! hataulizwa hayo mambo…kwahiyo mambo mengine hayana maana sana kuyakazania kwa watu wachanga!. Hatupaswi kuhubiri ili kutimiza wajibu Fulani au kujionesha tunajua maandiko, bali tunapaswa tuhubiri kwa NIA thabiti kabisa ya kutafuta roho zilizopotea.

1 Wakoritho 8:1“…. Twajua ya kuwa sisi sote tuna ujuzi. Ujuzi huleta majivuno, bali upendo hujenga”

Kadhalika ukikutana na Muislamu na kuanza kumwambia YESU NI MUNGU! Hatakuelewa hata kidogo, mambo hayo yanahitaji ufunuo wa Roho, ambao huo ni Mungu mwenyewe anamfunulia mtu taratibu taratibu, sasa kwa mara ya kwanza mtu asiyemjua Mungu jambo hilo haliwezi kumwingia akilini, anahitaji kukaa chini ya madarasa ya Roho kwanza, taratibu taratibu Roho Mtakatifu baadaye sana ataanza kumfunulia SIRI YA YESU KRISTO kuwa ni Mungu sawasawa (1Timotheo 3:16)..

Wanafunzi wa Bwana Yesu wenyewe iliwachukua muda kuelewa jambo hilo, sembuse mtu anayemsikia Kristo leo kwa mara ya kwanza??..Hivyo unapaswa umhubirie kwanza nguvu za msalaba..Nini kilitokea Edeni na ni kwanini kwa kupitia mtu mmoja dhambi iliingia…na ni kwanini kwa kupita mtu mmoja dhambi isifutike!…hapo kidogo kidogo unaanza kumleta kwa YESU, acha amwelewe kuwa Yesu ni nabii tu, kwa kipindi cha mwanzo mwanzo, akishamwelewa kuwa ni nabii, na kumwamini baadaye Roho atampandisha hatua moja Zaidi na kumfunulia kuwa ni mwana wa Mungu, baadaye yeye mwenyewe ndiye atakayekuja kukuthibitishia kwa maandiko kuwa YESU NI MUNGU! Kwahiyo kila kitu ni hatua!

Hata sisi tulipokuwa wadogo hatukuambiwa Watoto wanapatikana wapi, badala yake tulidanganywa tu wanakwenda kununuliwa, lakini tulipokuwa kiufahamu ndipo tulielewa mambo yote kuwa wanazaliwa, na Watoto wa Kiroho ndio hivyo hivyo, hawawezi kujua au kuelewa mambo yote kwa mara ya kwanza.

Ndio maana kwenye huo mstari wa 24 Mtume Paulo anasema “mtu asitafuta faida yake mwenyewe bali ya wengine”

Bwana akubariki sana.

Kama hujaokoka! Kumbuka wokovu unaanzia hapa hapa duniani!…kama vile hukumu inavyoanza hapa hapa duniani, hivyo kama hujampa Bwana maisha yako kwa kutubu na kudhamiria kabisa kuacha dhambi bado unayo nafasi hiyo sasa kabla mlango wa Neema haujafungwa, tubu sasa na ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa Jina la YESU kwa ajili ya ondoleo la dhambi na Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu, kumbuka biblia inasema wote wasio na Roho wa Yesu hao sio wake (Warumi 8:9) Hivyo tafuta Roho Mtakatifu..Huo ndio muhuri wa Mungu.

Maran atha!

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

JE! MKRISTO ANARUHUSIWA KULA NGURUWE?

UPENDO NI NINI NA JE! KUNA AINA NGAPI ZA UPENDO?

KARAMA ILIYO KUU NI IPI?.

KALAMU YA CHUMA.


Rudi Nyumbani

Print this post

UDHAIFU WA SADAKA!


Moja ya nguzo muhimu sana katika Imani ya Kikristo ni SADAKA, Sadaka ni nguzo muhimu sana, kwasababu hata Kristo mwenyewe alifanyika sadaka kwa ajili yetu ili sisi tuokolewe…Kama Kristo asingejitoa nafsi yake kwa ajili yetu sisi tusingekuwa popote, tungekuwa ni wana wa Jehanamu wote, hakuna hata mmoja ambaye angepona.

Kwahiyo kama Kristo alivyojitoa kwetu na sisi pia lazima tujitoe kwa wengine…Ndio maana sadaka ni Muhimu, Roho iliyokuwa ndani ya Kristo ilimpeleka kujitoa nafsi yake kuwa fidia kwa roho nyingi, halikadhalika na sisi kama tumeipokea Roho ile ile ambayo ilikuwa ndani yake, ni lazima itatusukuma na sisi kujitoa kwa ajili ya wengine, kulingana na karama tulizopewa…

Sadaka sio lazima kutoa mali, bali hata kujitoa Maisha ili kwamba wengine wapate uzima, kama Bwana Yesu hakutoa fedha ili sisi tuokolewe bali aliitoa damu yake na Maisha yake kwa kuishi na kufundisha watu njia ya wokovu ili waokolewe. Hiyo ni sadaka kubwa sana na kuu kuliko zote, kutoa Maisha kwaajili ya mwingine ili aokoke. Kama Biblia inavyotuambia katika..

1 Yohana 3:16 “Katika hili tumelifahamu pendo, kwa kuwa yeye aliutoa uhai wake kwa ajili yetu; imetupasa na sisi kuutoa uhai wetu kwa ajili ya hao ndugu”.

Na sadaka sio mchango. Mchango ni kitu unachotoa kuchangia jambo Fulani liendelee mbele lakini sadaka, ni kitu kinachohusisha wewe kupungukiwa ili mwingine aongezewe, au wewe kupoteza ili mwingine apate, hiyo ndiyo maana ya sadaka…haina tofauti sana na neno MUHANGA..Kwahiyo sadaka ni KITU kikubwa Zaidi ya Mchango…Hivyo unapomtolea Mungu sadaka kwaajili ya kazi yake, zingatia kutoa kitu kikubwa Zaidi ya mchango, toa kitu ambacho kimekugharimu sana….ukitoa mchango utapata thawabu lakini sadaka ina thawabu kubwa Zaidi.

Sasa leo hatutaingia sana kuzungumzia Umuhimu wa Sadaka au nguvu ya sadaka, lakini tutazungumzia UDHAIFU WA SADAKA.

Utauliza, sadaka ina madhaifu?..Jibu ni ndio, sadaka ina madhaifu na mipaka..Inayo nguvu ya kubadilisha mambo lakini pia inayo mipaka ambayo haiwezi kupita..kuna mambo ambayo haiwezi kubadilisha…Hebu tusome mistari michache ifuatayo kisha tuendelee…

1 Samweli 15:20 “Sauli akamwambia Samweli, Hakika mimi nimeitii sauti ya Bwana, nami nimemleta Agagi, mfalme wa Waamaleki, tena nimewaangamiza Waamaleki kabisa.

21 Ila watu waliteka nyara, kondoo na ng’ombe walio wazuri, katika vitu vilivyowekwa wakfu, kusudi wavitoe dhabihu kwa Bwana, Mungu wako, huko Gilgali.

22 Naye Samweli akasema, je! Bwana huzipenda sadaka za kuteketezwa na dhabihu Sawasawa na kuitii sauti ya Bwana? Angalia, kutii ni bora kuliko dhabihu, Na kusikia kuliko mafuta ya beberu.

23 Kwani kuasi ni kama dhambi ya uchawi, Na ukaidi ni kama ukafiri na vinyago; Kwa kuwa umelikataa neno la Bwana, Yeye naye amekukataa wewe usiwe mfalme”

Habari hiyo inamzungumzia Mfalme wa kwanza wa Israeli aliyeitwa Sauli, ambaye alilikaidi Neno la Mungu, aliambiwa akaangamize vitu vyote na watu wote (Waamaleki) asiache chochote, hata ng’ombe na mbuzi na kondoo wote auwe, lakini yeye akaangamiza vyote lakini akawaacha wafalme wa ile nchi hai pamoja na ng’ombe walionona na kondoo na kuvileta Israeli kwaajili ya kumtolea Mungu dhahibu, (dhabihu ni sadaka ya kuteketezwa). Kwa moyo wake alijua Mungu anapendezwa Zaidi na Sadaka kuliko kuyashika maagizo yake.. Hakujua kuwa nguvu ya sadaka sio kubwa kuliko nguvu ya kushika maagizo yake. Hivyo akajitumainisha kwa sadaka zile na Mungu akamkataa..

Huo ndio udhaifu wa Sadaka!..Ni kweli Mungu aliagiza watu wamtolee sadaka zilizonona, tena wasimtolee vilema, kwasababu ukimtolea sadaka kilema ilikuwa ni kujitafutia kulaaniwa badala ya kubarikiwa.(soma Malaki 1:13-14). Lakini sadaka hiyo hiyo, ina mipaka. Haiwezi kubadilisha mambo yote, haiwezi ikalivuka Neno la Mungu. Hatuwezi kumuonga Mungu kwa sadaka zetu, ili abadilishe Neno lake..Hapana! tutaongeza baraka tu kwa sadaka lakini si kulibadilisha Neno lake, akisema kuwa roho ya mwenye dhambi itakufa, hata tutoe fedha kiasi gani kama hatutalitii hilo neno na kuacha dhambi! Hizo sadaka hazina msaada wowote, kufa tutakufa tu!…Akisema waasherati na walawiti na waabudu sanamu sehemu yao ni katika lile ziwa la moto! Hata tutoe hazina zote za ulimwengu na kujitoa hata miili yetu, kama hatutatii na kuacha hivyo vitu…Jehanamu haiepukiki.

Sasa habu tuangalie mfano wa Mwisho ambao ni Bwana Yesu mwenyewe aliuota kuonesha udhaifu wa Sadaka!..Tusome.

Mathayo 5:23 “Basi ukileta sadaka yako madhabahuni, na huku ukikumbuka ya kuwa ndugu yako ana neno juu yako,

24 iache sadaka yako mbele ya madhabahu, uende zako, upatane kwanza na ndugu yako, kisha urudi uitoe sadaka yako.

25 Patana na mshitaki wako upesi, wakati uwapo pamoja naye njiani; yule mshitaki asije akakupeleka kwa kadhi, na kadhi akakupeleka kwa askari, ukatupwa gerezani.

26 Amin, nakuambia, Hutoki humo kamwe hata uishe kulipa senti ya mwisho”

Mfano huo Bwana Yesu alioutoa kutufundisha kuwa tusiitegemee sadaka, kubadilisha Neno la Mungu..Katika habari hiyo anasema “kabla ya kuitoa sadaka yako, patana kwanza na mshtaki wako”…Ikiwa na maana kwamba kama kuna mtu anakudai, au kuna mtu umemdhulumu, au kuna mtu umegombana naye, na wewe ndiye mwenye makosa na hivyo bado kidogo atakwenda kukushitaki… usikimbilie kwenda kutoa sadaka! Kana kwamba hiyo sadaka uliyoitoa itakukuokoa….Kitu cha kwanza Kimbilia kwanza kwenda kupatana naye, kwasababu usipopatana naye ukachelewa kidogo tu! na yeye akaenda kuripoti polisi, na polisi wakaja kukuchukua na kukuweka ndani! Biblia inasema hutatoka huko…Na hiyo sadaka uliyoitoa ambayo ulitegemea kukusaidia, wakati huo haitakusaidia chochote kukutoa huko gerezani…Mungu hatakuwa upande wako hata kidogo…Hivyo Bwana anasema…Nenda kwanza kapatane naye kabla hajakwenda kukuripoti…sadaka utatoa tu! Nenda kwanza kapatane naye! kwasababu Neno lake linasema…

Warumi 12:18 “Kama yamkini, kwa upande wenu, mkae katika amani na watu wote”.

Sasa ukikaa kwa vurugu na watu wote, hata utoe fedha kiasi gani kwa Mungu! Haitaruka Neno lake hilo kwamba “mkae na amani na watu wote”…Huo ndio udhaifu wa sadaka, haipiti Neno la Mungu….. “kutii ni bora kuliko dhabihu na kusikia kuliko Mafuta ya Beberu”.

Hivyo ndugu, inawezekana unatoa sadaka nyingi nzuri sana, hilo ni Jema Mungu atakulipa kwa ukarimu wako, lakini sadaka hiyo haiwezi kulipita Neno la Mungu linalosema…

Ufunuo 21:8 “Bali waoga, na wasioamini, na wachukizao, na wauaji, na wazinzi, na wachawi, na hao waabuduo sanamu, na waongo wote, sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti. Hii ndiyo mauti ya pili”.

Wala kulipita Neno hili..

Wagalatia 5:19 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,

20 ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,

21 husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu”.

Sadaka nzuri ni ile inayoambata na kulitii Neno la Mungu.

Uchaguzi unao wewe ambaye hujampa Kristo Maisha yako!..Kumwamini Yesu, na kutubu na kuamua kumgeukia huku ukidhamiria kuacha dhambi kabisa, utakapoamua kugeuka na kusema Kuanzia leo hii mimi na ulimwengu basii!! Kristo akiiona nia yako ndani yako kwamba kweli umedhamiria kuacha kwa vitendo, basi atakupa nguvu ya Roho wake Mtakatifu ambaye atakusadia kuweza kuzishinda dhambi kama ulivyosema kutoka katika kinywa chako mwenyewe. Mlango wa Neema bado upo wazi, lakini tunaishi kipindi cha kumalizia, ambapo parapanda siku yoyote inalia na watakatifu wataondolewa ulimwenguni, na ulimwengu kuharibiwa. Hivyo usikiapo maneno haya usifanye moyo wako mgumu, kama ulishampa Kristo Maisha yako, lakini umekuwa vuguvugu ni wakati wakuwa moto, kwasababu walio vuguvugu wote, Kristo alisema atawatapika. 

Bwana akubariki sana.jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Print this post

MZEITUNI HALISI UTAKAPOPACHIKWA.

Kuna watu wanasema sasa tunaishi katika agano jipya hivyo Mungu hatazami tena Taifa, wala mtu wala jinsia bali wote ni sawa kulingana na Wagalatia 3:28. Na hivyo wanadai kuwa hakuna kitu kama hicho taifa la Israeli kurudiwa na Mungu tena na Mungu kutembea nao kama ilivyokuwa katika agano la kale, sisi wote ni sawa na Kristo hivyo hakuna haja ya kutazama kinachoendelea Israeli, lile ni kwasasa ni taifa tu kama mataifa mengine. Ni kweli kabisa mbele za Kristo hakuna hivyo viambazi, wote ni sawa hakuna myahudi wala myunani, wala mke au mume, lakini katika kanuni ya utendaji kazi wake, ameweka mipango, mipaka, na kanuni na taratibu, na muda..

Kwamfano ilimpasa Mungu awapige upofu kwanza wayahudi(yaani Waisraeli) ili sisi, yaani mimi na wewe tuipokee neema, Mungu aliwafanya wawe vile kwa makusudi kabisa kwa ajili yetu na laiti asingefanya vile, leo hii sisi tusingemjua Kristo. Wokovu huu ungebakia kuwa ni wa wayahudi tu biblia inasema hivyo…Vile vile kama pia ukitazama kwa ukaribu utaona Neema ilipokuja kwa mataifa, haikuja na kukaa kila mahali kwa wakati mmoja japo kweli ilisikika ulimwenguni kote,lakini neema haikukaa kila mahali, ilikuwa inazunguka ukisoma maandiko na historia utoana ilianza bara la Asia, baadaye ikaja kuenea bara la Ulaya, baadaye ikafika Marekani, na mwisho wa siku sasa ipo kwetu huku Afrika..Na ndio maana utaona kuna mwitikio mkubwa wa watu kumtafuta Kristo huku kuliko mabara mengine yote duniani, lakini mfano kama ungekuja kipindi cha karne ya 19 huku Afrika, ungekutana na uchawi na ushirikina tu, wakati ulaya ndio ulikuwepo uamsho mkuu wa Roho.

Hivyo neema hii inatabia ya kutembea, na sasa inakaribia kuondoka na kurejea Israeli ilipoanzia, Na Bwana aliahidi kabla haijarudi atarudisha watu wake Israeli katika Taifa lao nao watakaa salama, kisha baadaye atawaletea uamsho. Jambo hilo tumeliona likitimia mwaka 1948, baada ya kukaa zaidi ya miaka 2500, ugenini kwenye mataifa mengine.Tofauti na wale wanaosema kuwa Israeli hawatarudiwa tena..Biblia ilitabiri kuwa watarudi nchini kwao.

Yeremia 34:23 “Kisha neno la Bwana likamjia Yeremia, kusema,

24 Je! Hufikiri neno hili walilolisema watu hawa, wakinena, Jamaa zile mbili alizozichagua Bwana amezitupilia mbali? Hivyo ndivyo wanavyowadharau watu wangu, ili wasiwe taifa tena mbele yao.

25 Bwana asema hivi, Ikiwa agano langu la mchana na usiku halikai imara, ikiwa mimi sikuziamuru kawaida za mbingu na dunia;

26 ndipo nitawatupilia mbali wazao wa Yakobo, na Daudi, mtumishi wangu, hata nisitwae wazao wake watawale juu ya wazao wa Ibrahimu, na Isaka, na Yakobo; kwa maana nitawarudisha wafungwa wao, nami nitawarehemu.”

Unaona hapo Bwana anasema kama vile agano lake la mchana na usiku likivunjika, yaani siku moja ipite kusiwe mchana, au kusiwe usiku basi na atawatupilia mbali watu wake wayahudi, lakini kama halijawahi kutanguka, basi kwame hatakaa awasahau wayahudi.

Nataka nikuambie ndugu Uamsho wao utakuwa wa kipekee sana, ni ule Mtume Paulo alisemea juu ya mzeituni halisi uliokatwa na kurudishwa kwenye shina lake halisi, unategemea vipi matunda yasitoke halisi zaidi, ikiwa sisi tuliokuwa mizeituni mwitu tukapachikwa kwenye mzeituni halisi na tukatoa matunda halisi, je si zaidi hao waliokuwa halisi wenyewe, watatoa kilicho bora zaidi..

Warumi 11:15 “Maana ikiwa kutupwa kwao kumeleta upatanisho kwa ulimwengu, je! Kukubaliwa kwao kutakuwa nini kama si uhai baada ya kufa?

16 Tena malimbuko yakiwa matakatifu, kadhalika na donge lote; na shina likiwa takatifu, matawi nayo kadhalika.

17 Lakini iwapo matawi mengine yamekatwa, na wewe mzeituni mwitu ulipandikizwa kati yao, ukawa mshirika wa shina la mzeituni na unono wake,

18 usijisifu juu ya matawi yale; au ikiwa wajisifu, si wewe ulichukuaye shina, bali ni shina likuchukualo wewe.

19 Basi utasema, Matawi yale yalikatwa kusudi ili nipandikizwe mimi.

20 Vema. Yalikatwa kwa kutokuamini kwao, na wewe wasimama kwa imani yako. Usijivune, bali uogope.

21 Kwa maana ikiwa Mungu hakuyaachia matawi ya asili, wala hatakuachia wewe.

22 Tazama, basi, wema na ukali wa Mungu; kwa wale walioanguka, ukali, bali kwako wewe wema wa Mungu, ukikaa katika wema huo; kama sivyo, wewe nawe utakatiliwa mbali.

23 Na hao pia, wasipokaa katika kutokuamini kwao, watapandikizwa; kwa kuwa Mungu aweza kuwapandikiza tena.

24 Kwa maana ikiwa wewe ulikatwa ukatolewa katika mzeituni, ulio mzeituni mwitu kwa asili yake, kisha ukapandikizwa, kinyume cha asili, katika mzeituni ulio mwema, si zaidi sana wale walio wa asili kuweza kupandikizwa katika mzeituni wao wenyewe?

25 Kwa maana, ndugu zangu, sipendi msiijue siri hii, ili msijione kuwa wenye akili; ya kwamba kwa sehemu ugumu umewapata Israeli, mpaka utimilifu wa Mataifa uwasili.

26 Hivyo Israeli wote wataokoka; kama ilivyoandikwa, Mwokozi atakuja kutoka Sayuni; Atamtenga Yakobo na maasia yake.

27 Na hili ndilo agano langu nao, Nitakapowaondolea dhambi zao.”

Ndugu yangu kuna wakati unafika hii neema inayochezewa na watu itarudi makao yake makuu (Israeli), na hawa wayahudi ambao unawaona sasa hawana habari na Yesu, wapo vuguvugu, hawaeleweki, biblia inasema ndani ya siku moja Mungu atawamwagia Roho ya neema, nao watatubu kwa kumaanisha kabisa, yaani mji mzima wa Yerusalemu utakuwa unaomboleza siku hiyo , wakimwombolezea Bwana Yesu ambaye walikuwa wakimpinga tangu zamani.

Zekaria 12:10 “Nami nitawamwagia watu wa nyumba ya Daudi, na wenyeji wa Yerusalemu, roho ya neema na kuomba; nao watamtazama yeye ambaye walimchoma; nao watamwombolezea, kama vile mtu amwombolezeavyo mwanawe wa pekee; nao wataona uchungu kwa ajili yake, kama vile mtu aonavyo uchungu kwa ajili ya mzaliwa wake wa kwanza.

11 Siku hiyo kutakuwa na maombolezo makuu huko Yerusalemu, kama maombolezo ya Hadadrimoni katika bonde la Megido.

12 Nayo nchi itaomboleza, kila jamaa peke yake; jamaa ya nyumba ya Daudi peke yao, na wake zao peke yao; jamaa ya nyumba ya Nathani peke yao, na wake zao peke yao;

13 jamaa ya nyumba ya Lawi peke yao, na wake zao peke yao; jamaa ya nyumba ya Shimei peke yao, na wake zao peke yao.

14 Jamaa zote zilizosalia, kila jamaa peke yake, na wake zao peke yao”.

Wakati huo, neema itakuwa imeshaondoka kwenye mataifa yote dunia, hapo ndipo Mungu ataitumia Israeli kuwa fimbo kwa mataifa yote, usitamani wakati huo ukukute..Leo hii tumeshaanza kuona dalili ndogo ndogo, jiulize kwanini taifa la Israeli ni dogo kuliko hata mkoa wa Songwe, halina kitu chochote cha kuvutia wala haina teknolojia ya kutisha sana kama mataifa ya mashariki na Magharibi lakini kila mtu anaizungumzia, isitoshe bado wanaigopa, na hapo hata Mungu hajatia mguu wake kutembea nao, jiulize wakati huo ukifika itakuwaje?.

Ndugu ni mambo mengi ya kutisha yapo mbele yetu ambayo hata sisi wenyewe hatuyajui vizuri, ni heri tukabakia katika upande salama, Vita ya Harmagedoni ambayo itakuja kupigwana kipindi kifupi baada ya unyakuo itapiganiwa pale pale Israeli…( ukihitaji maelezo marefu juu ya vita hii, nitumie ujumbe inbox nitakutumia somo lake..)

Huu ni wakati wa kuweka mambo yetu sawa, ikiwa bado hujatubu, mgeukie muumba wako sasa, na ikiwa bado upo nusu nusu, vuguvugu, uimarishe wito wako sasa, kabla nyakati za hatari hazijafika.

Bwana akubariki sana. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Mada Zinazoendana:

MAMBO YATAKAYOTOKEA ISRAELI SIKU ZA HIVI KARIBUNI

UFUNUO: Mlango wa 7 & 11

AMIN! NAWAAMBIA KIZAZI HIKI HAKITAPITA!


Rudi Nyumbani

Print this post

MUNGU MWENYE HAKI.


Shalom mtu wa Mungu karibu tujifunze juu ya Haki ya Mungu.

Ni wazi na inajulikana na wote kuwa Mwenyezi Mungu aliyetuumba sisi viumbe vyake vyote ni Mungu mwenye haki, hilo halina kipingamizi, lakini ni vizuri kuijua kwa mapana haki hiyo ya Mungu inatendaje kazi katikati ya viumbe vyake. 

Kazi anazofanya shetani na malaika wake walioasi ndio hizo hizo wanazozifanya Malaika wa Mbinguni ambao hawajaasi, shetani na Malaika zake wanajishungulisha sana na mambo ya wanadamu namna ya kuwavuta wanadamu wengi upande wao, kadhalika na Malaika watakatifu wanajishughulisha sana na mambo ya wanadamu namna ya kuwavuta wanadamu upande wa Mungu.

Sasa anayepambana na shetani si Mungu, Mungu hashindani na kiumbe chochote kile, yeye ni Mkuu kupita upeo wa fahamu zetu wote, hivyo hawezi kushindana na kiumbe chochote alichokitengeneza yeye…Kwahiyo anayeshindana na shetani ni Mikaeli pamoja na malaika wenzake watakatifu na si Mungu. Mikaeli ni Malaika mkuu wa vita aliyeko mbinguni aliye kiongozi wa vita kama vile shetani alivyo kiongozi wa malaika wengine walioasi….wapo malaika wa aina tofauti tofauti.

Ufunuo 12:7 “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake;

8 nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni

9 Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye”.

Sasa kama Mungu hashindani na shetani, swali linakuja yeye atakuwa anafanya kazi gani?

Jibu: Mungu anasimama kama wakili au hakimu, kuwapatia haki wale wanaostahili haki…

Hivyo kazi ya malaika watakatifu ni kusisimama kututetea sisi wanadamu kila siku mbele za uso wa Mungu, na kazi ya shetani na malaika zake ni kutushitaki…maana tafsiri yenyewe ya jina ‘shetani’ ni ‘mshitaki’…kazi yake ni kutafuta kasoro ndogo ndogo na kubwa katika Maisha yetu na kuzipeleka kwa Hakimu Mkuu (Mungu) kutafuta haki ya kututesa au kutuangamiza.

Sasa anapokuja kwako na kukuta kuwa wewe ni mwasherati, au mchawi, na unafanya hayo huku ukijua kabisa ni dhambi…..moja kwa moja anakimbiza hizo hoja mbele za Mungu, na kutaka ruksa ya kukutawala Maisha yako, atamwambia Mungu huyu kwa mapenzi yake mwenyewe anafanya hayo, na wala hajalazimishwa, ananitumikia mimi, amesikia injili yako na anajua kabisa kwa matendo yake atakwenda kuzimu, lakini bado anayafanya hayo..hivyo huyu ni wangu.. nipe ni wangu huyo.

Na wale malaika wa Mungu wanapokosa kitu cha kukutetea mbele za Mungu, kutokana na mambo unayoyafanya ya umakusudi na ukiwa na akili timamu, shetani anashinda hoja mbele za Mungu na kupewa haki yake..Mungu hana upendeleo hata kidogo ndio asili yake hiyo, anamlipa kila mtu kulingana na anachostahili, shetani anampa haki yake na Malaika vile vile anawapa haki zao… Ndio hapo mtu anajikuta ghafla ulinzi wa kiMungu umeondoka juu yake, anaanza kupitia hili na lile..na wakati mwingine hata kufa.

Lakini anapokuja na kukuta umemwamini Bwana Yesu Kristo, na umeoshwa kwa damu yake, na unaishi Maisha matakatifu, hata kama kuna viudhaifu vidogo vidogo, hivyo havitoshi kumpa shetani ushindi juu ya Maisha yako, kwasababu wale malaika ambao kazi yao ni kutembea na sisi wanautazama uso wa Baba yetu mbinguni kila siku kupeleka taarifa njema juu yetu,(Mathayo 18:10) hivyo hoja zao za kutumilikisha sisi kwa Mungu zinashinda kila siku na kujikuta tunaishi Maisha ya ulinzi na amani. Hiyo yote ni kwasababu umefunga milango yote shetani kupata vijisababu vya kukushtaki…(Kwa maelezo marefu juu ya huduma za hawa malaika watakatifu unaweza ukatutumia ujumbe inbox, tutakutumia maelezo yake kwa urefu)…

Lakini unaposikia injili na huku moyoni mwako unajua kabisa ni maneno ya Mungu ya uzima, na unaidharau kwa namna moja au nyingine, basi hiyo tayari ni point kubwa sana kwa shetani kuipeleka mbele za Mungu kupata kibali cha kuyatawala Maisha yako. Wale malaika wanaokulinda wanashindwa kukutetea na kuondoka..

Hivyo ni jambo la muhimu sana na kuzingatia kuyahakiki maisha yetu kila siku, kwasababu biblia inasema shetani adui yetu ni kama simba angurumaye anazunguka huko na huko kumtafuta mtu wa ammeze..

1 Petro 5:8 “Mwe na kiasi na kukesha; kwa kuwa mshitaki wenu Ibilisi, kama simba angurumaye, huzungukazunguka, akitafuta mtu ammeze”.

Shetani hawezi kuyatawala Maisha yako ukiwa ni mtu wa unayeishi Maisha ya kumpendeza Mungu, ukiwa chini ya Damu ya mwanakondoo..Usalama wetu ni kuwa chini ya Damu ya Yesu tu , na huko sio kusema tu ‘najiweka chini ya Damu ya Yesu’..unaposema hivyo ni sawa na kusema ‘najiweka chini ya sheria za nchi’..je ukisema hivyo itakuwa na madhara yoyote?..unaona ukitaka kujiweka chini ya sheria za nchi ni kuziishi zile sheria,kuzileta kwenye Maisha yako, sio kuzitamka tu!…kadhalika kujiweka njini ya damu ya Yesu ni kuileta ile damu kwenye Maisha yako sio kuitamka tu!..kutamka kunakuja baada ya kuileta kwenye matendo hiyo damu.

Kadhalika shetani hatumnyanganyi mamlaka juu ya Maisha yetu kwa kutamka tu! (na kusema Shetani huna mamlaka juu ya Maisha yangu), hapo bado hatujamwondoa…Ili kumwondoa ni lazima tuvidhibiti vifursa vyake vyote anavyovitumia kutushitaki sisi mbele za Mungu…Na baada ya kuvifunga hivyo ndipo tunamalazia na kutamka kuwa shetani huna mamlaka yoyote juu ya Maisha yetu.

Hakuna pepo lolote linaloweza kumwingia mtu kabla halijapata kibali mbele za Mungu…Ukiona kuna roho ipo ndani yako basi jua kuna mahali mlango umeufungua maishani mwako, na hivyo shetani kapata kijisababu cha kukushitaki mbele za Mungu na kushinda.

Baadhi ya milango inayosababisha roho za mapepo kuingia ndani ya watu ni uasherati, ibada za sanamu, ushirikina, matumizi ya vipodozi na uvaaji mbaya ikiwemo mawigi, uvaaji suruali kwa wanawake, vimini, na nguo zinazobana, na upakaji wa lipstick,wanja, uvaaji hereni na uchoraji wa tattoo, utazamaji pornography, usikilizaji miziki ya kidunia ..na mambo mengine yanayofanana na hayo…

Mambo hayo ndiyo yanayoongoza kumpa shetani nafasi ya juu ya kutawala Maisha ya watu, ikiwemo kuleta magonjwa, ugomvi, shida, taabu, kukosa amani, kukosa furaha na raha pamoja na kifo.

Hivyo ukitaka kukaa mbali na shetani, suluhisho ni kutofungua mlango wowote wa kumpa shetani upenyo wa kukushtaki kwa kukaa mbali na hivyo vitu tulivyovitaja hapo juu na vingine vyote vinavyofanana na hivyo..

Kumbuka pia kukamilisha hatua zako za wokovu kama hujakamilisha, hatua hizo zipo tatu, 1)KUAMINI, 2)KUBATIZWA, na 3)KUPOKEA ROHO MTAKATIFU. Hatua hizo ni za muhimu, na pia kumbuka ubatizo sahihi ni wa kuzama mwili wote kwenye maji mengi kama neno lenyewe ubatizo linavyomaanisha, na pia ni kwa JINA LA BWANA YESU kulingana na Matendo 2:38, Na Roho Mtakatifu ni Mungu mwenyewe anakupa kwasababu ni ahadi yake aliyowaahidi wale wote wamwombao. Na hapo sasa shetani atakapojaribu kwenda kukushitaki mbele za Mungu atashindwa, kwasababu umekamilishwa ipasavyo katika wokovu.

hivyo ukiwa hujakamilisha hatua hizo bado unayo nafasi sasa, zikamilishe kabla mwisho haujafika, kwasababu tunaishi katika siku za Mwisho, muda wowote parapanda inalia na wafu watafufuliwa na sisi tulio hai tutanyakuliwa na Bwana kwenda mawinguni, Je utakuwa mmoja wao wa watakaoenda na Bwana?

Bwana akubariki sana. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Zinazoendana:

KUNDI LA MALAIKA WALETAO MABAYA.

HUDUMA YA MALAIKA WATAKATIFU.

BIBLIA INASEMA “HAMJUI YA KUWA MTAWAHUKUMU MALAIKA? (1WAKORINTHO 6:2-3)”JE! SISI TUTAWAHUKUMUJE MALAIKA?.


Rudi Nyumbani

Print this post

MWISHO WA HAO WAMSAHAUO MUNGU.

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe daima, karibu tujifunze maneno ya uzima, Kama tunavyofahamu tunaishi ukingoni kabisa mwa wakati, siku zile ambazo Bwana Yesu alisema upendo wa wengi utapoa duniani kwasababu ya kuongezeka kwa maasi (Mathayo 24:12) Ndizo tunazoishi sasa.

Sasa Upendo unaozungumziwa hapo sio tu upendo wa ndugu, bali pia upendo wa kumpenda Bwana utapoa ndani ya watu wengi.

Unakuta mtu alianza vizuri na Bwana, mwanzoni, alikuwa amesimama vizuri, anamtafuta Mungu kwa bidii, anasali, anajilinda na ulimwengu, anavaa mavazi ya heshima, na Zaidi ya yote anawahubiria wengine habari njema.. lakini kwasababu ulimwengu wasasa umebadilika, na yeye anabadilika nao, hapo mwanzo alikuwa haendi disco lakini sasa ameanza kuwa muhudhuriaji mzuri, hapo mwanzo alikuwa havai suruali na vimini lakini sasa ni mvaaji hodari, hapo mwanzo alikuwa ni mwombaji mzuri lakini sasa kasongwa na kampani za watu wa kidunia, mizunguko ya huku na kule kila kukicha haiishi, na kwasababu smartphone zimekuja sasa, utamkuta ule muda ambao angepaswa awe analiafakari Neno la Mungu nyumbani kwake na familia yake, utamkuta ana chat kwenye mitandao na katika magroup ya whatsapp hata 50 yasiyokuwa na maana, na kutazama mambo yasiyostahili mitandaoni, na pornograph.

Na hali hiyo inaendelea hivyo hivyo mpaka baadaye anajikuta kamsahau Mungu kabisa ambaye alishamwokoa zamani, anaona sasa wokovu hauna maana tena, hauna faida yoyote, ni kujinyima tu bure kusikokuwa na sababu za msingi, na hivyo anaamua kuishi maisha ya kidunia huku akidhani kuwa ndio kayapenda maisha yake kumbe ndio ameyaangamiza…Biblia inasema:

Ayubu 8:8 “Basi, uwaulize, tafadhali, vizazi vya zamani, Ujitie kuyaangalia yale baba zao waliyoyatafuta;

9 (Kwani sisi tu wa jana tu, wala hatujui neno, Kwa kuwa siku zetu duniani ni kivuli tu;)

10 Je! Hawatakufunza wao, na kukueleza, Na kutamka maneno yatokayo mioyoni mwao?

11 Je! Hayo MAFUNJO yamea pasipo matope Na MAKANGAGA kumea pasipo maji?

12 Yakiwa yakali mabichi bado, wala hayakukatwa, Hunyauka mbele ya majani mengine.

13 NDIVYO ULIVYO MWISHO WA HAO WAMSAHAUO MUNGU; Na matumaini yake huyo mbaya huangamia;

14 Uthabiti wake utavunjika, Na matumaini yake huwa ni nyuzi za buibui.

15 Ataitegemea nyumba yake, isisimame; Atashikamana nayo, isidumu.

16 Yeye huwa mti mbichi mbele ya jua, Nayo machipukizi yake huenea katika bustani yake.

17 Mizizi yake huzonga-zonga chuguu, Huangalia mahali penye mawe.

18 Lakini, aking’olewa mahali pake, Ndipo patamkana, na kusema, Mimi sikukuona.

19 Tazama, furaha ya njia yake ni hii, Na wengine watachipuka kutoka katika nchi.”

Unaona hapo mwandishi anasema, Sisi ni wa juzi tu, tuwaulize watu walitutangulia zamani, tuwaulize wakina Sulemani, n.k. je! MAFUNJO yamea pasipo matope Na MAKANGAGA kumea pasipo maji?. Mafunjo na makangaga ni aina ya mime mirefu ambayo hiyo huwa inaota sehemu za mabwawa au maziwa, sehemu zenye maji mengi, mahali pengine popote palipo na upungufu wa maji haziwezi kuota, ni sawa tu na yale magugu maji,…Na ndio hapo anauliza je! Mimea hiyo inaweza kuota katika nchi kame kama vile katani iotavyo jangwani,?…Jibu ni La!, anasema ndivyo ilivyo kwa watu wale wamsahauo Muumba wao.

Mpaka mtu amsahau Mungu, ni wazi kuwa hapo nyuma alikuwa ameshafahamiana naye, huwezi kumsahau mtu ambaye humfahamu, vivyo hivyo wanaozungumziwa hapo ni wakristo wale ambao hapo nyuma walikuwa sawa na Mungu lakini sasa wamepoa, hapo kabla walikuwa moto kwa Mungu lakini sasa wamevutwa na ulimwengu. Wala hawazungumziwi watu wasiomjua Mungu kabisa..

Mwandishi anaendelea kusema.. “Yeye huwa mti mbichi mbele ya jua,”. Ikiwa na maana kuwa mpaka huo mti umekuwa mbichi ni wazi kuwa ulishawahi kuwepo pembezoni mwa mito ya maji, lakini ghafla haupo tena katika mito bali upo mbele ya jua.. Unatazamia vipi mti huo utakuwa na maisha marefu?. Vivyo hivyo na sisi tunapomsahau Mungu katika dunia hii mbovu inayopita, siku za mwanzoni tunaweza tusione matokeo yoyote, hiyo ni kwasababu ule ubichi bado upo ndani yetu, lakini siku chache mbeleni, tutakapo kauka ghafla ndipo tutakapojua kuwa kumbe tulikosea na tutakapotaka kugeuka tumrudie yeye hatutaweza tena kwasababu tayari tulishakatwa siku nyingi.. Hata leo hii ukikuta mti mkubwa, huwezi kuona matokeo ya kukauka majani yake siku hiyo hiyo, lakini nenda rudi baada ya siku mbili, tatu ndipo uakapoona tofauti.

Zaburi 50:22 “Yafahamuni hayo, Ninyi mnaomsahau Mungu, Nisije nikawararueni, Asipatikane mwenye kuwaponya.”

Katika nyakati hizi za hatari njia pekee ya kuishi maisha ya kutokumsahau Mungu ni kuhakikisha, kwanza kila siku unalitafakari Neno la Mungu, sio kusoma tu, hapana bali kutenga muda wa kutosha kulitafakari Neno, wengi wanaishia katika kusoma tu kama vile kitabu halafu basi, hiyo haikuongezei chochote, ni sawa na umetengewa sahani ya ugali, lakini ule ugali wote hauwezi kwenda tumboni moja kwa moja kama usipopitia kinywani, utafunwe, uvunjwe vunjwe na meno kisha uingie kidogo kidogo mpaka wote uishe, vivyo hivyo, ukiwa na pupa ya kulisoma Neno la Mungu kama kitabu tu ama gazeti, kama kutimiza wajibu Fulani ulioambiwa na mhubiri Fulani…

kisha kwenda kulala, litakuboa tu, na hutapata jambo jipya ndani yake, utaona kuna mambo magumu, hayaeleweki, lakini kwanza ukichukua muda kusali na kumwomba Roho Mtakatifu akusaidie, kisha ukatafakari lile unalolisoma hata kama ni mstari mmoja kwa muda mrefu ukililinganisha na maisha yako kisha, ukaweka mipango ya kulitendea kazi, basi lile Neno la Mungu litakuwa na manufaa makubwa sana kwako. Hatuhesabiwi haki kwa kumaliza kuisoma biblia yote, bali kwa kuielewa..

Kumbukumbu 8:11 “Jihadhari, usije ukamsahau Bwana, Mungu wako, kwa kutozishika amri zake, na hukumu zake, na sheria zake, ninazokuamuru leo”.

Pili, jenga desturi ya kuhudhuria ibadani, ukutane na waaminio wenzako, kaa na ndugu ambao ni wakristo wenzako wenyewe nia ya kwenda mbinguni pamoja na wewe, tafuta marafiki wenye faida za kimbinguni..Chuma hunoa chuma, lakini kama muda wako wote utakaa na marafiki wa kidunia ambao hao wakati wote hata habari na Mungu hawana, na wewe uliyempokea Kristo unaendelea kukaa nao, ipo dalili kubwa sana ya kumsahau Mungu.

Na mwisho kuwa mtu wa maombi. Ukizingatia vigezo hivyo ni ngumu kujikuta umerudi nyuma kwa sababu yoyote ile. Kumbuka nyakati hizi ndio zile nyakati za hatari sana ambazo zilitabiriwa kuwa watu watakuwa wa kupenda sana anasa kuliko kumpenda Mungu..Hivyo tunaaswa kuwa makini sana katika safari yetu ya wokovu.

Waefeso 5:15 “Basi angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima;

16 mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu.

17 Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya Bwana.

18 Tena msilewe kwa mvinyo, ambamo mna ufisadi; bali mjazwe Roho;

19 mkisemezana kwa zaburi na tenzi na nyimbo za rohoni, huku mkiimba na kumshangilia Bwana mioyoni mwenu;

20 na kumshukuru Mungu Baba sikuzote kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo;

21 hali mnanyenyekeana katika kicho cha Kristo.”

Bwana akubariki sana. Tafadhali “Share” Ujumbe huu kwa wengine. Na Bwana atakubariki. Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group


Mada Zinazoendana:

NINI MAANA YA KUISHI KWA KUUKOMBOA WAKATI?

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

ZIKUMBUKE FADHILI ZA MUNGU


Rudi Nyumbani

Print this post