Title March 2025

Je wazo la Herode kutafuta kumuua mtoto YESU lilitoka wapi?

Wakati Herode anaua watoto kule Bethlehemu baada ya kuzaliwa YESU je roho iliyokuwa ndani yake ilikuwa inatoka wapi?.. Kama ni shetani, je shetani hakujua kama Yusufu na Mariamu wametoka na wameelekea Misri?.


Jibu: Awali ya yote ni muhimu kujua kuwa roho iliyokuwa ndani ya Herode ni ya “shetani” na wala hazikuwa akili zake Herode..Kwasababu kitabu cha Ufunuo kinaonyesha wazi kuwa ni Joka (yaani shetani mwenyewe) ndiye alikuwa anatafuta kumwangamiza Bwana YESU wakati anazaliwa na si Herode (Herode alitumika tu kama chombo)

Ufunuo 12:3 “Ikaonekana ishara nyingine mbinguni; na tazama, joka kubwa jekundu, alikuwa na vichwa saba na pembe kumi, na juu ya vichwa vyake vilemba saba.

4  Na mkia wake wakokota theluthi ya nyota za mbinguni, na kuziangusha katika nchi. Na yule joka AKASIMAMA MBELE YA YULE MWANAMKE ALIYE TAYARI KUZAA, ILI AZAAPO, AMLE MTOTO WAKE.

5  Naye akazaa mtoto mwanamume, yeye atakayewachunga mataifa yote kwa fimbo ya chuma. Na mtoto wake akanyakuliwa hata kwa Mungu, na kwa kiti chake cha enzi”.

Sasa swali kwanini shetani asiahirishe ajenda yake ya kuua watoto Bethlehemu baada ya kujua kuwa mtoto hayupo tena Bethlehemu?..

Kikawaida uwezo wa shetani si kama wa MUNGU.. MUNGU anaweza kufanya pasipo ushirika na yoyote, na anaweza kufanya jambo likabadilika kwa muda mfupi, lakini si shetani..

shetani anaposhindwa kufanikisha jambo lake lolote baya kupitia mapepo wake, huwa anatumia wanadamu.. kwamfano akishindwa kumuua amtu kimazingara, basi anaweza  kutumia mtu/watu kufanikisha adhimio lake hilo,  hivyo anaweza kuweka wazo ndani ya mtu la kuua, na huyo mtu akaanza maandalizi ya mauaji (jambo ambalo linaweza kuchukua muda mrefu) tofauti na hiyo njia ya kwanza ya kimiujiza-ujiza ambayo ni ya haraka tu ikiwa mtu huyo hana ulinzi wowote wa kiMungu.

Lakini njia ya kumtumia mtu kuua inachangamoto kubwa kwa shetani, Kwasababu ni lazima kwanza amwandae huyo mtu (atakayemtumia kuua), pengine amwekee wivu ndani yake au hasira, na pia amshawishi vya kutosha na kumfundisha njia, sasa mpaka yule mtu aelewe na kutenda kama shetani anavyotaka inaweza kuchukua muda,

Na vile vile si rahisi kulitoa wazo ndani ya mtu (alilokwisha kumwekea), na kubadilisha mpango kwa haraka, kwamfano kama alikuwa amemfundisha mtu aue kwa sumu, na akataka ambadilishie wazo hilo amwekee lingine la kumuua kwa kumchoma kisu, haiwezi kuwa ni jambo la haraka, itamgharimu shetani muda mwingine wa kutosha kufuta wazo la kwanza na kupandikiza wazo la pili ndani ya mtu.

Ndio maana utaona baada ya mtoto kukimbizwa Misri, bado wazo lile la ibilisi ndani ya Herode la kumuua mtoto halikutoka, matokeo yake Herode aliendelea na mauaji….hivyo kubadilisha mpango kwa haraka ilikuwa ni ngumu, zilihitajika taarifa zimfikie Herode kwamba mtoto hayupo kakimbilia Misri, na Herode aamini, na kuahirisha wazo lile.

Kwahiyo shetani alishajua mtoto kakimbilia Misri, lakini kulibadilisha wazo kwenye kichwa cha Herode halikuwa jambo jepesi la dakika moja.

Hiyo pia ikifunua kuwa dhambi ndani ya mtu inayo maandalizi, huwa haiji ghafla, ni lazima kwanza shetani apandikize magugu ndani ya mtu ndipo mwisho aitekeleze, Hivyo ni lazima tuikatae dhambi katika msingi wake, Laiti Herode angeikataa dhambi katika msingi wake pale wivu ulipoingia ndani yake, bila shaka asingeendelea na hatua zinazofuta za mauaji, lakini aliporuhusu wazo la ibilisi lichipue ndani yake ndipo akawa kifaa tosha cha ibilisi.

Vile vile Kaini alionywa na MUNGU, juu ya dhambi ya wivu inayochipuka ndani yake, laiti kama angemsikiliza MUNGU asingefikia hatua ya mauaji, lakini alidharau maonyo ya MUNGU na mwisho akawa kifaa cha ibilisi cha mauaji.

Mwanzo  4:6 “Bwana akamwambia Kaini, Kwa nini una ghadhabu? Na kwa nini uso wako umekunjamana? 

7 Kama ukitenda vyema, hutapata kibali? Usipotenda vyema dhambi iko, inakuotea mlangoni, nayo inakutamani wewe, walakini yapasa uishinde.

8 Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani]Ikawa walipokuwapo uwandani,Kaini akamwinukia Habili nduguye, akamwua”.

Vile vile na sisi ni lazima tuikatae dhambi katika uchanga wake, mawazo mabaya yajapo ni wakati wa kuyakataa kabla hayajatupeleka katika matendo, fikra mbaya zijapo ni wakati wa kuzikataa katika uchanga wake, hasira ijapo, chuki zijapo, uchungu ujapo na mambo mengine yote mabaya ni wakati wa kukataa, kama hayajafikia kukomaa..

Vile vile dhambi ikiisha kukomaa ni ngumu kuiacha, ndio maana ilikuwa ni ngumu shetani kumbadilishia Herode mpango kwa haraka, kwasababu tayari ile dhambi imeshikamana naye.

Shalom.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

YULE JOKA WA ZAMANI.

Kwanini Herode aliwakasirikia watu wa Tiro na Sidoni? (Matendo 12:20)

CHACHU YA MAFARISAYO NA CHACHU YA HERODE.

FAHAMU MAISHA YA YESU KABLA YA HUDUMA.

NGUVU ZA ZAMANI ZIJAZO:

Print this post

NITAACHAJE DHAMBI?.

Jina la Mwokozi wetu YESU KRISTO libarikiwe, karibu tujifunze Biblia, Neno la MUNGU wetu lililo Taa na Mwanga wa njia zetu (Zab.119:105).

1 Petro 4:1 “Basi kwa kuwa Kristo aliteswa katika mwili wake, ninyi nanyi jivikeni silaha ya nia ile ile; KWA MAANA YEYE ALIYETESWA KATIKA MWILI AMEACHANA NA DHAMBI”.

Kumbe KUTESWA KATIKA MWILI ndio kanuni ya KUACHANA NA DHAMBI!

Sasa ni nani aliyewahi kuteswa katika mwili na akaachana na dhambi,ili tuuige mfano wake?..

Huyo si mwingine zaidi ya Bwana wetu YESU KRISTO, yeye aliteswa katika mwili na kuachana na dhambi…

Sasa hakuteswa kwaajili ya dhambi zake kwasababu yeye hakuwahi kufanya dhambi, bali Baba alimtwika dhambi zetu na hivyo akahesabika mwenye dhambi kuliko watu wote…..na akateswa kwaajili ya dhambi hizo (za ulimwengu),

Na baada ya kuteswa alikufa,na baadaye akafufuka bila zile dhambi (huo ni muujiza mkubwa sana), kwani aliziacha zile dhambi zote kaburini.

Warumi 6:10 “Maana kwa kule kufa kwake, aliifia dhambi mara moja tu; lakini kwa kule kuishi kwake, amwishia Mungu”.

Na sisi ili tuachane na dhambi ni lazima tufuate kanuni hiyo hiyo, ya KUTESWA, KUFA na KUFUFUKA.

Lakini kwa kuwa hakuna mwanadamu yoyote anayeweza kutembea katika ile njia ya BWANA YESU asilimia mia moja, yeye Bwana katurahisishia zoezi zima hilo la KUTESWA, KUFA na KUFUFUKA.

Kwamba tunapomwamini na kubeba misalaba yetu, na kuukataa ulimwengu (Hapo ni sawa na KUTESWA)..

Vile vile tunapozama katika yale maji mengi wakati wa ubatizo (Hapo ni sawa tumekufa pamoja naye)

Na tunapoibuka kutoka katika yale maji wakati wa ubatizo (Hapo ni sawa tumefufuka pamoja naye).

Wakolosai 2:12 “Mkazikwa pamoja naye katika ubatizo; na katika huo mkafufuliwa pamoja naye, kwa kuziamini nguvu za Mungu aliyemfufua katika wafu”.

Na kama hatua hizo tatu (kujikana nafsi na ubatizo) zinalinganishwa kisahihi kabisa na Kuteswa, kufa na kufufuka..basi lile andiko la kwamba “YEYE ALIYETESWA KATIKA MWILI AMEACHANA NA DHAMBI (1Petro 4:1)”.  Linafanya kazi hapa hapa..

Wagalatia 5:24 “Na hao walio wa Kristo Yesu wameusulibisha mwili pamoja na mawazo yake mabaya na tamaa zake”.

Sasa ukiona bado dhambi inakutawala kiasi kwamba uasherati una nguvu juu yako, ulevi una nguvu juu yako, uuaji una nguvu juu yako, uchawi, udui, wivu, husuda na mambo mengine yote yaliyotajwa katika Matendo 5:19-20, ni ishara kuwa bado haujausulibisha mwili wako kwa KRISTO, na hiyo ndio sababu dhambi inakutawala.

Suluhisho ni Kujikana nafsi na kubeba msalaba, kisha kutafuta ubatizo sahihi wa maji mengi na kwa jina la BWANA YESU (Matendo 2:38) na ubatizo wa Roho Mtakatifu.

Ukiyapata mambo hayo matatu dhambi haina nguvu tena juu yako!, kwasababu unakuwa umeifia dhambi..

Warumi 6:2 “Hasha! Sisi tulioifia dhambi tutaishije tena katika dhambi?”

Ni sawa na mgonjwa aliyekuwa anasumbuliwa na homa, baada ya kupata dawa, ile homa yote inaondoka…Naam ni hivyo hivyo mtu anayejikana nafsi kweli kweli na kumfuata YESU, anakuwa amemeza kidonge cha kwanza cha matibabu ya dhambi inayomtesa, kidonge cha pili na cha tatu ni ubatizo wa maji mengi na ubatizo wa Roho Mtakatifu.

Warumi 6:10 “Maana kwa kule kufa kwake, aliifia dhambi mara moja tu; lakini kwa kule kuishi kwake, amwishia Mungu

11 Vivyo hivyo ninyi nanyi jihesabuni kuwa wafu kwa dhambi na walio hai kwa Mungu katika Kristo Yesu

12 Basi, dhambi isitawale ndani ya miili yenu ipatikanayo na mauti, hata mkazitii tamaa zake”.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

Maana ya Mithali 29:9 Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu; Akikasirika au akicheka, pia hapana raha. 

 Mithali 29:9 Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu; Akikasirika au akicheka, pia hapana raha.


Mstari huo kwa lugha rahisi tunaweza kuuweka kwa namna hii. “Mwenye hekima akijadiliana na mpumbavu, akijibu kwa kicheko au kwa hasira, matokeo ni yaleyale tu hakuna amani au suluhisho”

Unafunua sifa za mpumbavu, kwamba sikuzote mwitikio wake wowote hauwezi kuleta mabadiliko. Kwamfano labda hoja imetolewa na ikamuumiza kiasi cha kumfanya ajibu kwa hasira. Sasa wewe waweza tarajia pengine jambo hilo limemgusa kweli moyo, litambadilisha lakini matokeo yake ni kwamba anakuwa vilevile, Halikadhalika waweza kutoa hoja ikamfanya acheke ukitarajia kitaambatana na  badiliko lolote ndani yake lakini hakuna.

Maana yake mpumbavu, haguswi kwa ukali au kwa wepesi wa maneno ya aina yoyote…Na hivyo ni kuachana naye Tu.

Tukiachia wapumbavu wa kawaida tunaowafahamu..Mpumbavu hasaa ni yule mtu anayeikataa kweli ya Mungu mfano wa wale waandishi na mafarisayo wakati wa Bwana Yesu (Mathayo 23:17), mtu wa namna hii unapomuhubiri injili, hata imchomeje au imchekesheje hawezi kufikiri hata chembe kubadilika, kinyume Chake ni mapambano tu.

Bwana Yesu alitufundisha na kutuambia kuwa si kila mtu ni wa kumtupia lulu zetu, maana yake wanaweza kutugeukia na Kuturarua. Ukiona mtu anaishia kwenye ubishi tu na mashindano, ni kuachana naye na kugeukia waliotayari kupokea.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Mpumbavu ni nani katika biblia? (Zaburi 14:1, Mithali 10:14)

Elewa tafsiri ya Mithali 27:22 Hata ukimtwanga mpumbavu kwa mchi kinuni.

KILINDI CHAPIGIA KELELE KILINDI.

Print this post

Theolojia ni nini?. Na je ni sahihi kuisoma?

Theolojia ni elimu ya kujifunza sifa za Mungu na mapenzi yake na jinsi anavyohusiana na wanadamu na ulimwengu  kwa ujumla.

Neno Theolojia limezaliwa kutoka katika maneno mawili ya kigiriki ‘theos’, na ‘logos’

Theos likiwa na maana ya Mungu, na logos ni neno/wazo/elimu/maarifa.

Hivyo tukiunganisha maneno hayo, ni sawa kusema theolojia ni mafundisho au maarifa au elimu kuhusu Mungu.

Ni utafiti kuhusu  Mungu katika mpangilio na mtiririko maalumu. Ukweli ni kwamba theolojia haiwezi kumfafanua Mungu katika ufasaha wote, ikiwa mtu ataitegemea  theolojia tu kumjua Mungu, ukweli ni kwamba amepotea, lakini ikiwa itasomwa vema (si kwa lengo la kitaaluma), bali kwa lengo la kupanua upana wa fikra kuhusu Mungu na maandiko, inafaa sana katika uelewa wa nyanja mbalimbali, hususani kwa wale viongozi na waangalizi kama vile wachungaji, na wahubiri. Si lazima isomwe kwenye vyuo maalumu, mtu yeyote akitia nia kujifunza theolojia anaweza jifunza, kwa kupitia mafundisho mengi, majadiliano na waalimu walio na upeo mpana wa biblia, semina, na kujisomea mwenyewe n.k.

Na Haya ni matawi makuu ya theolojia katika kuichambua biblia.

1) Theolojia ya ki-biblia.

Imejikita katika kutafiti Maudhui au fundisho kuu la biblia, inaangazia jinsi gani vitabu mbalimbali kwenye biblia, vinavyoelezea mpango wa Mungu katika nyakati tofauti tofauti tangu mwanzo hadi mwisho. Mfano kujifunza MAAGANO, katika agano la kale na jipya yalivyotenda kazi na jinsi Yesu alivyoanza kutambulishwa tangu Edeni kama mzao wa mwanamke, hadi nyakati za manabii Isaya 53, hadi wakati wa kutokea kwake duniani Luka 24:27.

Upo umuhimu wa kuijua hii theolojia kwasababu itakupa kujua kiini cha biblia ni nini? Zipo habari nyingi, hadithi nyingi, nyimbo nyingi, mifano mingi, lakini ni vema ujue maudhui zao ni zipi ili usijikute unatoka nje ya shabaha ya imani.

2) Theolojia ya ki-mpangilio/Mada

Inaegemea kujifunza biblia katika migawanyo maalumu ya mada, kwa mfano,

Fundisho la Mungu (theolojia),

Fundisho La Yesu Kristo (Kristolojia),

Fundisho La Roho Mtakatifu (niumatolojia),

Fundisho La wokovu (Soteriolojia),

Fundisho La kanisa,(Ekleziolojia)

La Siku za mwisho.(Esokatolojia)

La mwanadamu (Anthropolojia)

La malaika (Angeolojia)

3) Theolojia ya ki-vitendo

Inajikita kujifunza jinsi maagizo ya kibiblia yanavyoweza kutendewa kazi katika,, huduma kwa mfano kuhubiri na kufundisha , katika uangalizi wa kichungaji, katika umisheni, na katika taratibu za kiibada, na katika kutoa mashauri ya kikristo kama vile kuwaonya wenye matatizo ya kiroho,  kifikra, vifungo n.k.

4) Theolojia ya ki-historia.

Inaangazia jinsi gani imani ya kikristo imekuwa ikipiga hatua katika vipindi mbalimbali vya kihistoria, inaangazia mabaraza mbalimbali ya makanisa yaliyokaa katika kujadili fundisho na misingi ya imani. Kwamfano lile baraza la Nikea (325WK). Mpaka nyakati za matengenezo mfano akina Martin Luther, calvin, na wengine.

Hii inakusaidia kujua historia na chimbuko la imani yetu, na sababu ya ukristo kuonekana katika muundo huu leo.

5) Theolojia ya kimaadili.

Hii inaegemea katika ukristo na jamii, kwamfano mtazamo wa ukristo katika maeneo ya kijamii mfano ndoa, biashara, taratibu za kijamii, haki za kibinadamu, vita,

Zipo theolojia nyingine kama vile theolojia za tafsiri, za kulinganisha, za utetezi, za kifalsafa. n.k. Kwasababu ya upana wa theolojia, haya ni  matawi baadhi tu, kati ya mengi. Hivyo, kama watu wa Mungu, pamoja na kutegemea Bwana kutufunulia mwenyewe maandiko, upo pia wakati ambao hatuna budi kuyamulika maandiko kiundani (Kitheolojia), tukiwa na lengo la kumjua Mungu kwa upana na sio kuwa wasomi, au wanataaluma.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Mwanazuoni ni mtu gani kibiblia?

Kwanini kuna tafsiri nyingi za Biblia, na tafsiri ipi ni sahihi?

Yesu anapoitwa mwana wa Azali, maana yake nini?

Print this post

Je tumepewa kujua nyakati na majira ya kurudi kwa Bwana au la?.

Swali: Katika Matendo 1:7, tunaona Bwana anasema si kazi yetu kujua nyakati na majira ya kuja kwake,

Lakini katika 1Wathesalonike 5:1-2 tunasoma Mtume Paulo akisema kuhusu nyakati na majira kuwa hana haja ya kutuandikia kwasababu sisi wenyewe tunajua…je hii imekaaje?..je kuna mkanganyiko hapo?


Jibu: Awali, tuirejee mistari hiyo…

Matendo 1:6 “Basi walipokutanika, wakamwuliza, wakisema, Je! Bwana, wakati huu ndipo unapowarudishia Israeli ufalme?

7 Akawaambia, Si kazi yenu kujua NYAKATI WALA MAJIRA, Baba aliyoyaweka katika mamlaka yake mwenyewe”.

Tusome tena habari ya Paulo…

1 Wathesalonike 5:1 “Lakini, ndugu, kwa habari ya NYAKATI NA MAJIRA, hamna haja niwaandikie.

2 Maana ninyi wenyewe MNAJUA yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku”.

Ni muhimu kufahamu kuwa hakuna mkanganyiko wowote kwenye biblia, na wala haijichanganyi,

Sasa Paulo aliposema kuwa “hana haja ya kuandika kuhusu nyakati na majira kwasababu tayari wameshajua”.. hakumaanisha kuwa tayari wameshajua/tumeshajua siku na tarehe za kurudi Bwana YESU, LA! Hakumaanisha hivyo, vinginevyo angekuwa ameenda kinyume na maneno hayo ya Bwana YESU aliyosema kuwa “Si kazi yetu kujua majira na nyakati” na tena aliposema “hakuna ajuaye siku wala saa”.

Sasa ni kitu gani Paulo alichomaanisha kuwa tayari wameshakijua, au tumeshakijua kuhusu nyakati na majira?.

Kitu ambacho tayari Wathesalonike pamoja na sisi tumeshakijua kuhusu Nyakati na Majira ya kurudi kwa YESU sio ile tarehe atakayokuja, hapana!.. bali tulichokijua kuhusu Nyakati na Majira ya kurudi kwa YESU ni kwamba “ATAKUJA KAMA MWIVI”… Hicho ndicho Paulo alichokimaanisha.

Na ni lini tulijua hilo?…tulijua kupitia maneno ya Bwana YESU mwenyewe..
Mathayo 24:40 “Wakati ule watu wawili watakuwako kondeni; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa;
41 wanawake wawili watakuwa wakisaga; mmoja atwaliwa, mmoja aachwa.
42 Kesheni basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu.
43 Lakini fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angaliijua ile zamu mwivi atakayokuja, angalikesha, wala asingaliiacha nyumba yake kuvunjwa.
44 Kwa sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani Mwana wa Adamu yuaja”

Ndio maana tukiendelea mistari ya mbele kidogo mpaka ule mstari wa tatu tutaona Paulo analielezea zaidi…

1 Wathesalonike 5:1 “Lakini, ndugu, kwa habari ya NYAKATI NA MAJIRA, hamna haja niwaandikie.

2 Maana ninyi wenyewe MNAJUA yakini ya kuwa siku ya Bwana yaja kama vile mwivi ajavyo usiku.

3 Wakati wasemapo, Kuna amani na salama, ndipo uharibifu uwajiapo kwa ghafula, kama vile utungu umjiavyo mwenye mimba, wala hakika hawataokolewa”.

Kwahiyo biblia haijichanganyi popote, wala Paulo hakusema kitu chochote tofauti na BWANA YESU.

Je umempokea Mwokozi YESU?..Je wajua kuwa dakika yoyote parapanda italia, na watakaonyakuliwa ni wale tu waliojitaka, je utakuwa wapi siku ile ikiwa leo hii hutaki kubadili njia zako?.

Jibu unalo!

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post

Je Paulo, alihimiza kusikiliza nyimbo za kidunia kulingana na Matendo 17:28

Matendo 17:28 Kwa maana ndani yake yeye tunaishi, tunakwenda, na kuwa na uhai wetu. Kama vile mmoja wenu, mtunga mashairi alivyosema, Maana sisi sote tu wazao wake.

29 Basi, kwa kuwa sisi tu wazao wa Mungu, haitupasi kudhani ya kuwa Uungu ni mfano wa dhahabu au fedha au jiwe, vitu vilivyochongwa kwa ustadi na akili za wanadamu.

JIBU: Paulo alipofika Athene, na kuona jinsi mji ule ulivyojaa sanamu nyingi, maandiko yanatuambia moyo wake ulichukizwa sana, hivyo kama ilivyo desturi yake kuhubiri injili, alijua njia mojawapo ya kuwavuta watu ni “kujiungamanisha nao”, kwa kuwagusia kwanza yale mambo mema waliyoyafikiri au kuyatenda.

Ndio maana utaona kabla ya kuwagusia kuhusu huyo mtunga mashairi, aliwaambia kuhusu madhabahu waliyoijenga, ambayo waliipa jina la “MUNGU ASIYEJULIKANA”

Matendo 17:23 Kwa sababu nilipokuwa nikipita huko na huko na kuyaona mambo ya ibada yenu, naliona madhabahu iliyoandikwa maneno haya, KWA MUNGU ASIYEJULIKANA. Basi mimi nawahubirini habari zake yeye ambaye ninyi mnamwabudu bila kumjua.

Paulo akaanza kuwahubiria Kristo kwa kupitia huyo wanayemwabudu kimakosa, Lakini tunajua Paulo, hakuwa na ushirika wowote na mifumo yao ya kipagani, wala hakuwahimiza waendelee kumwabudu Kristo kwa njia yao hiyo hiyo.

Tunaona katika kuendelea kujiungamanisha zaidi ya wenyeji wale wa Athene, Paulo akagusia tena habari nyingine za mtunga mashairi, ambaye alikuwa maarifu katikati yao, nyimbo zake zilivuma na kila mmoja alikuwa anazijua, na ndani ya mashairi yake, aliweka vina vinavyoeleza kuwa sisi sote ni wazao wake, au kusema sisi sote ni watoto wa Mungu.

Hivyo akatumia tena fursa hiyo, kuwaeleza uhai wa Mungu, ikiwa sisi tumezaliwa na yeye, basi haiwezekani Baba yetu akawa mfano wa sanamu, ni lazima tu atakuwa mwenye akili, ufahamu, na uelewa kama sisi na zaidi, na sio kama kipande cha mti.

Kwa njia hiyo Paulo akawapata watu wengi, kwa Kristo.

Lakini hatuoni mahali popote akiwaambia wawe wafuatiliaji au  mashabiki, wa nyimbo za kidunia.Hiyo ilikuwa njia ya kuwapata wapagani, wamjue Kristo.

Kinyume chake Paulo katika nyaraka zake, anahimiza, waamini kutofuatisha namna ya dunia hii (Warumi 12:1). Na kuhimiza uimbaji unaomtukuza Mungu na kutujenga sisi nafsi zetu kwake ndio unaopaswa kwa wakristo.

Waefeso 5:19 mkisemezana kwa zaburi na tenzi na nyimbo za rohoni, huku mkiimba na kumshangilia Bwana mioyoni mwenu;

20 na kumshukuru Mungu Baba sikuzote kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo;

Wakolosai 3:16 Neno la Kristo na likae kwa wingi ndani yenu katika hekima yote, mkifundishana na kuonyana kwa zaburi, na nyimbo, na tenzi za rohoni; huku mkimwimbia Mungu kwa neema mioyoni mwenu.

17 Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye.

Hivyo hatuoni mahali popote Paulo akikubaliana na usikilizaji wa nyimbo za kidunia, wala sisi kama wakristo, hatupaswi kujikita huko, kwasababu tumeshajua ni nani hasaa wa kumwimbia na kumsifu, na wa kumburudikia.

Mungu akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Kuharimishwa ni nini, na kwanini Paulo aombe hivyo?(Warumi 9:2).

Uchambuzi na mwandishi wa kitabu cha Waefeso.

Ni kwa namna gani Bwana YESU alikula Siagi na Maziwa? (Isaya 7:15)

Print this post

Yaya ni nani? (Mwanzo 24:59).

Swali: Huyu yaya aliyeenda na Rebeka ni nani kama tunavyomsoma katika Mwanzo 24:59?

Jibu: Turejee…

Mwanzo 24:59 “Ndipo wakampeleka Rebeka ndugu yao, na YAYA wake, na mtumishi wa Ibrahimu, na watu wake”.

Yaya maana yake ni muuguzi (yaani mwangalizi wa mtu aliye katika udhaifu fulani au ugonjwa)...kwa kiswahili kingine chepesi ni NESI.

Kwahiyo Rebeka wakati anachukuliwa ili apelekwa kwa Isaka…aliambatana na Nesi wake huyo(Yaya).

Sasa biblia haijaelezea kwa undani sababu za kwenda naye, kwamba ni kwasababu za ugonjwa Rebeka aliokuwa nao (ambao pia haujatajwa) au labda kwa dharura endapo angepata shida fulani katika njia anayoiendea basi apate msaidizi kwani safari ile ilikuwa ni ndefu sana….

Au labda alimuhitaji yaya mbeleni katika maisha yake ya ndoa, baada ya kujifungua n.k hakuna anayejua, biblia imesema tu alienda na Yaya wake.

Neno hili pia limeonekana sehemu nyingine katika biblia..

2 Samweli 4:4 “Naye Yonathani, mwana wa Sauli alikuwa na mwana aliyekuwa na kilema cha miguu. Alikuwa amepata miaka mitano, habari za Sauli na Yonathani zilipofika Yezreeli, na yaya wake akamchukua akakimbia ikawa, alipokimbia kwa haraka, huyo mtoto akaanguka, akawa kilema. Na jina lake aliitwa Mefiboshethi”

Soma pia 2Nyakati 22:11 utaona pia  neno hilo.

Naam kiroho YAYA wetu ni YESU KRISTO, tuwapo wadhaifu au katika dhiki au hali za kuishiwa nguvu na kuhitaji msaada, ni YESU KRISTO tu pekee awezaye kututunza na kututoa katika hizo hali.

Lakini Bwana hawezi kuwa mlezi wetu ikiwa hatutamruhusu awe hivyo, lakini tukiruhusu aingie maishani mwetu, na pia tukimheshimu na kuzishika amri zake hakika hatatuacha katika mateso sawasawa na ahadi zake.

Zaburi 41:3 “BWANA atamtegemeza alipo mgonjwa kitandani. Katika ugonjwa wake umemtandikia”

Je unaye YESU moyoni, na je maisha yako yanaakisi wokovu wa kweli?.

Kama bado upo nje ya YESU tafuta msaada mapema kwa YESU kabla mambo hayajaharibika zaidi.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255693036618 au +255789001312

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Print this post