2Nyakati 16: 9 “Kwa maana macho ya Bwana hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake”.
Tukisoma habari za wafalme katika biblia tunakuja kukutana na mfalme mmoja aliyeitwa ASA. Huyu biblia inasema aliiendea njia ya ukamilifu, alifanikiwa kuwaondoa watu wote waliokuwa mahanithi (Mashoga) katika nchi ya Yuda, akaondoa maashera yote pamoja na sanamu zote zilizokuwa zimewekwa na baba zake kabla yake. Kwa ujumbla ni mfalme aliyemtumainia sana Mungu kwa kila jambo na hivyo Mungu akamfanikisha sana(1Wafalme 15:9-15). Ilifikia hatua ambayo baada ya kugundua mama yake mzazi amesimamisha sanamu na kuziabudu, alimwondoa katika kiti chake cha umalkia bila kujali kuwa ni mama yake mzazi yupo hapo. Kwani kipindi kile cha wafalme, ilikuwa ni desturi mahali mfalme anapoketi ni lazima na mama yake awekewe kiti cha enzi kidogo pembeni yake.
Lakini Mfalme Asa mara baada ya kugundua kuwa mama yake Mzazi anaabudu miungu mingine, bila kujali hisia yoyote ya mtu alimwondoa asionekane tena katika jumba la kifalme daima. Jambo ambalo halikuwahi kufanywa na mfalme yeyote wa Israeli kabla yake… eti! Kumtoa mama yake aliyekuzaa katika cheo cha umalkia kisa tu kaisujudia miungu mingine?, Hakuna mfalme yeyote aliyedhubutu kufanya kitendo hicho cha kishujaa cha kumvunjia mamaye heshima na kumfanya kuwa kama mtu wa kawaida ili tu ailinde heshima ya Mungu wake japo wengi wao walikuwa wanawaona mama zao wakiwakosesha lakini walikaa kimya kulinda heshma za wazazi wao. Lakini kwa mfalme Asa ilikuwa tofauti, leo hii je! na sisi tunaweza kuyaweka mashauri ya wazazi wetu chini yale yanayopingana na Mungu na kuyaruhusu yale tu ya Mungu yasimame?. Mungu atusaidie katika hilo na sisi.
Mfalme Asa alisimamia kweli hakubakisha sanamu yoyote katika Yuda na Benjamini, aliingia maagano na Mungu kuwa yeye na watu wote wa Yuda watamtafuta Mungu kwa mioyo yao yote, kwa akili zao zote na kwa nguvu zao zote, akapiga mbiu katika nchi yote ya Yuda kwamba watu wote wamtufute Mungu muumba wa mbingu na nchi. Na wakakubaliana wote kuwa mtu yeyote ambaye hatamtafuta Mungu wa Mbinguni atauawa bila huruma, si mdogo, si mkubwa, si mwanamke, si mwanaume yeyote yule atauawa..
Hivyo Mungu akapendezwa sana na Mfalme Asa na hivyo akampa Amani na maadui zake wote waliokuwa wanamzunguka kwa muda mrefu tofauti na wafalme wengine waliosalia, na pindi maadui zake walipokuja kupigana naye Mungu aliwapa ushindi mnono, na nyara nyingi hivyo akaongezeka utajiri, na hofu kubwa ikawaangukia maadui zake wote waliokuwa wanamzunguka. Mungu akamjalia kuijenga Yuda kwa maboma, na minara na malango na makomeo makubwa, Na Hivyo mji ukathibitika na kuimarika kwa miaka mingi katika ufalme wake.
Lakini Bwana alimwambia Asa kwa kinywa cha Nabii Odedi ajitie nguvu wala mikono yake isilegee kwasababu kazi yake itakuwa ina malipo baadaye, haitakuwa bure aendelee hivyo hivyo kuulekeza moyo wake kwa Mungu, aondoe machukizo yote katika nyumba yake na katika Israeli aendelee hivyo hivyo kumtumaini Bwana wala asiwayategemee mataifa. Tunakuja kusoma ni kweli Mfalme ASA aliendelea kumsimamia Mungu kwa muda mrefu lakini ilifika wakati akapoa kidogo pindi maadui zake walipokuja kutaka kumzuia asitoke ndani ya mji wake, ndipo badala akimbilie kwa Mungu ambaye amekuwa akimtumainia na kumshindania kwa muda mrefu, Mungu ambaye amekuwa akimpigania vita vikubwa kwa muda mrefu, na kumfanikisha katika mambo yote siku zote za utawala wake, Mungu ambaye amekuwa akimpa amani pande zote, lakini badala yake akakimbilia kwa mfalme wa Shamu ili amsaidie kufanya vita na maadui zake, hivyo akampelekea na zawadi nyingi kutoka katika hazina ya nyumba ya Mungu, na kweli mfalme wa Shamu alimsaidia kupigana na maadui zake, na wale maadui zake wakaacha kuujengwa uzio wa kuwazuia, Hivyo nchi ikastarehe tena kwa muda mfupi.
Lakini jambo hilo halikumpendeza sana Mungu, kwasababu Mungu alimwona ASA kama ni mtu ambaye moyo wake ulimwelekea sana zaidi ya wengi waliotangulia, ni mtu ambaye Mungu angeweza kuonyesha uweza na nguvu zake zote kwa mataifa mengine kupitia yeye kama vile alivyoonyesha kwa Daudi na Sulemani, lakini sasa amefanya kitendo cha aibu, moyo wake kuwaelekea wanadamu na sio Mungu wake tena, kwenda kuwaomba wafalme wengine wa kipagani wamsaidie kupigana vita. Na ndio hapo tunakuja kusoma Mungu akimtumia nabii wake na kumwambia maneno haya.
2Nyakati 16: 7 “Wakati ule Hanani mwonaji akamwendea Asa mfalme wa Yuda, akamwambia, Kwa kuwa umemtegemea mfalme wa Shamu, wala hukumtegemea Bwana, Mungu wako, kwa hiyo limeokoka jeshi la mfalme wa Shamu mkononi mwako.
8 Je! Hao Wakushi na Walubi hawakuwa jeshi kubwa mno, wenye magari na wapanda farasi wengi sana? LAKINI, KWA KUWA ULIMTEGEMEA BWANA, ALIWATIA MKONONI MWAKO.
9 KWA MAANA MACHO YA BWANA HUKIMBIA-KIMBIA DUNIANI MWOTE, ILI AJIONYESHE MWENYE NGUVU KWA AJILI YA HAO, WALIOKAMILIKA MOYO KUELEKEA KWAKE. Kwa hayo umetenda upumbavu; kwani tangu sasa utakuwa na vita”.
Angalia hapo maneno hayo yalimjia mfalme Asa, hakujua kuwa macho ya Mungu yalishazunguka duniani kote kutafuta mtu aliyekamilika moyo ulioelekea kwake, ili Mungu ajionyeshe kuwa mwenye nguvu kwake, na akamwona ASA peke yake, lakini yeye hakulijua hilo, alidhani Mungu hakuwa anauthamini uthabiti wa moyo wake, alidhani Mungu hakumaanisha kumwambia yale maneno kuwa taabu yake kwake itakuwa na malipo (2Nyakati 15:7), yeye alichukulia juu juu tu, mpaka hapo alipoutoa moyo wake kwa Bwana na kuulekeza kwa wanadamu. Ndipo Mungu alipokasirika na kumwambia umefanya upumbavu…Mungu hapendi upumbavu kwa watu wanaomtumainia. Lakini pamoja na hayo yote Mfalme Asa alifanya mema machoni pa Mungu mpaka siku ya kufa kwake, na Bwana hakumwacha kabisa.
Leo hii ndugu yangu biblia inatufundisha na sisi tuwe ni mioyo iliyomwelekea Mungu. Kwasababu macho ya Mungu yanakimbia-kimbia duniani kote, ikiwa na maana Mungu anaangalia anarudi tena anaangalia, anarudi tena anaangalia aone mtu atakayekuwa na moyo mkamilifu utakaomwelekea yeye kwa kila kitu ili azionyeshe nguvu zake. Kama ilivyokuwa kwa mfalme Asa. Tuweke tegemeo letu lote kwa Mungu, tumtwike yeye fadhaa zetu zote, tusiwe wepesi kuwakimbilia wanadamu, bali mioyo yetu siku zote tuielekeze kwa Mungu muumba wa mbingu na nchi, kwasababu yeye anawaangalia watu kama hao waliokamilika mioyo aonyeshe nguvu zake zote. Tuvumilie na kumtegemea Mungu hatari inapojitokeza mbele yetu..Tusiwapendelee wanadamu hata kama ni ndugu zetu, bali sisi tuangalie tu kile Mungu anachosema basi, tusifanye ibada za sanamu, ambazo biblia inazitaja kama uasherati, na tama mbaya, bali tuvivunje vunje vikae mbali nasi, ndipo hapo Mungu atakapotuona na kazi yetu ikawa na faida kubwa. Na Mungu atatuimarisha.
Ikiwa haujampa Bwana maisha yako, mlango wa neema bado upo kwa ajili yako, damu ya thamani ya Yesu Kristo bado inafanya kazi hata sasa hivi, imebaki kipindi kifupi sana isimame kufanya kazi yake. Usisubiri kipindi Fulani kifike , hicho hakitafika ndugu yangu, hiyo ni injili ya shetani anayokuhubiria moyoni mwako.. muda wa wokovu ni sasa biblia inasema hivyo. Chukua uamuzi sasa wa kuyakabidhi maisha yako kwa Bwana Yesu kikamilifu, na utakapofanya hivyo kwa kudhamiria kabisa kutoka ndani ya moyo wako, kutubu kwa kuacha dhambi na maisha yako ya kale, basi yeye mwenye atakupa uwezo wa kuzishinda dhambi. Na haraka mara baada ya kuamini kwako unapaswa ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa kwa jina la YESU KRISTO, upate ondoleo la dhambi zako. Kisha Roho wa Mungu ataachiliwa juu yako kukulinda na kukuongoza katika kweli yote. Na baada ya hapo utakavyozidi kuuelekeza moyo wako kwa Mungu na kumtegemea yeye siku zote ndivyo utakavyouona mkono wake katika maisha yako, Na Mungu atakutumia wewe kuonyesha nguvu zake kwa wengine.
Ni matumaini yangu utafanya hivyo. Na Bwana akubariki sana.
Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Mada Nyinginezo:
MUNGU NDIYE ANAYEISHAWISHI MIOYO.
BWANA ALIMAANISHA NINI KUSEMA “HERI WALIOTASA, NA MATUMBO YASIYOZAA, NA MAZIWA YASIYONYONYESHA”?
Umeshawahi kujiuliza pale biblia inaposema ROHO MBAYA KUTOKA KWA BWANA ikamjia Sauli ni roho ya namna gani hiyo? Na ni kwanini Bwana atume roho mbaya kwa mtu, nasi tunajua siku zote Mungu huwa anaachilia roho nzuri, njema na ya amani kwa watu, anasema hapa roho mbaya kutoka kwa Bwana, inakuaje tena anaiachilia roho yake mbaya iende kwa mtiwa mafuta wake, tena inafanya kazi ya kumsumbua kiasi ambacho inataka kufanya uharibifu hata ya kuwadhuru watu wasio na hatia..Tukisoma kitabu cha Samweli inasema:
1Samweli 16:14-23
“14 Basi, roho ya Bwana ilikuwa imemwacha Sauli, na roho mbaya kutoka kwa Bwana ikamsumbua.
15 Nao watumishi wa Sauli wakamwambia, Angalia, sasa roho mbaya kutoka kwa Mungu inakusumbua.
16 Basi bwana wetu na atuamuru sisi watumishi wake waliopo hapa mbele yako watafute mtu aliye stadi
wa kupiga kinubi; basi itakuwa, roho ile mbaya kutoka kwa Mungu itakapokujilia, yeye atapiga kinubi kwa
mkono wake, nawe utapona.
17 Basi Sauli akawaambia, Vema, nitafutieni mtu aliye stadi wa kupiga kinubi, mkaniletee.
18 Ndipo akajibu mmoja wa watumishi wake akasema, Tazama, nimemwona mwana mmoja wa Yese,
Mbethlehemi, aliye stadi wa kupiga kinubi, tena ni mtu shujaa, hodari wa vita, anenaye kwa busara, mtu
mzuri, ambaye Bwana yu pamoja naye.
19 Basi Sauli akampelekea Yese wajumbe, akasema, Nipelekee Daudi mwanao, aliye pamoja na kondoo.
20 Yese akatwaa punda, wa kuchukua mikate, na kiriba cha divai, na mwana-mbuzi, akampelekea Sauli
kwa mkono wa Daudi mwanawe.
21 Basi Daudi akamwendea Sauli, akasimama mbele yake, naye akampenda sana; naye akapata kuwa
mtu wa kumchukulia silaha zake.
22 Kisha Sauli akapeleka watu kwa Yese, akasema, Tafadhali, mwache Daudi asimame mbele yangu;
maana ameona kibali machoni pangu.
23 Ikawa, ile roho mbaya kutoka kwa Mungu ilipomjilia Sauli, ndipo Daudi akakishika kinubi, akakipiga kwa
mkono wake, naye Sauli akaburudishwa, na ile roho mbaya ikamwacha”.
Ili kufahamu vizuri ni kwanini hayo yote yalimpata Sauli, turudi nyuma kidogo tuitazame historia ya Mfalme Sauli jinsi ilivyokuwa. Kama tunavyosoma katika maandiko tunaambiwa kuwa Sauli alikuwa ni kijana mzuri sana, mrefu, mwenye haya ya uso, mlaini, hakuwa hata mtu aliyezaliwa katika mbari za kikuhani au za waamuzi walioamua Israeli wakati ule, hakuwahi hata kupigana vita yeyote, wala hakuwa na dalili ya kuonyesha kama ni mtu aliyeweza kusimama vitani, na ndio maana tunakuja kuona pindi tu siku ile alipokuja kutiwa mafuta na Nabii Samweli na kutangazwa kwa Israeli wote kama mfalme wao, baadhi ya watu walimkebehi kwa kumtazama tu mwonekano wake wa nje na uzoefu wake hafifu, alionekana kama ni mtoto tu, mtu mwenye tabia kama za kitoto, pengine walipomwona sura yake laini na uzuri aliokua nao au mazungumzo yake yasiyo na uzoefu wowote wa uongozi, watu wakamdharau na kumwona kama si kitu hawezi kuongoza taifa kubwa la kishujaa kama Israeli. Na ni kweli ndivyo alivyokuwa, alikuwa hana uwezo wowote ule Sauli.
Lakini siku Mungu alipomtia mafuta biblia inasema Roho ya Mungu ikamjilia kwa nguvu juu yake naye akageuzwa na kuwa mtu mwingine. (1Samweli 10:6). Sasa kumbuku kwasababu mtu kama Sauli alitiwa mafuta ya kuwa mfalme kuongoza taifa kubwa na hodari kama Israeli, ni sharti roho ambayo itaachiliwa juu yake itakuwa ni roho ya uongozi, roho ya ujasiri, roho ya maamuzi magumu, na roho ya udhubutu na roho ya ushujaa. Hivyo jambo ambalo lingemtokea mfalme Sauli hapo ni lazima liwe la namna hiyo.
Lakini Mfalme Sauli hakulitambua hilo vizuri mpaka siku ambayo maadui wa ndugu zao walipotokea na kutaka kuwatawala, tena kwa mapatano ya kila myahudi kung’olewa jicho lake la kuume, vinginevyo watawauawa. Hivyo habari hizo zikafika katika miji mingine yote ya Israeli, watu wote wakalia sana, wakizingatia kuwa huyo adui wa ndugu zao huko Yabesh-gileadi ni mkuu sana, hakuna mtu anayeweza kusimama mbele yake kuwatetea na kushindana naye ili kuwaokoa ndugu zao..Hivyo wakalia sana lakini habari zilimfikia Sauli mwezi mmoja tu baada ya kutiwa mafuta ya kuwa mfalme, Sauli ambaye alidharauliwa na watu, Sauli ambaye hakuwa na uzoefu wowote wa vita ghafla akanyanyuka kwa ushujaa mwingi na HASIRA nyingi, na kusema maneno haya.
1Samweli 11:4 “Hivyo wajumbe wakafika Gibea ya Sauli, wakasema maneno hayo masikioni mwa watu; na watu wote wakainua sauti zao wakalia.
5 Na tazama, Sauli akaja akifuata ng’ombe kutoka kondeni; naye Sauli akauliza, Watu hawa wana nini,
hata wakalia? Wakamwambia maneno ya watu wale wa Yabeshi.
6 NA ROHO YA MUNGU IKAMJILIA SAULI KWA NGUVU, hapo alipoyasikia maneno yale, na hasira yake ikawaka
sana.
7 Naye akatwaa jozi ya ng’ombe, akawakata-kata vipande, kisha akavipeleka vile vipande mipakani mwote
mwa Israeli kwa mikono ya wajumbe, kusema, Ye yote asiyetoka nyuma ya Sauli na Samweli, ng’ombe
zake watatendwa vivi hivi. Basi utisho wa Bwana ukawaangukia wale watu, wakatoka kama mtu mmoja.
8 Naye akawahesabu huko Bezeki; Waisraeli walikuwa mia tatu elfu, na Wayuda thelathini elfu.
9 Nao wakawaambia hao wajumbe waliokuja, Waambieni watu wa Yabesh-gileadi, Kesho, wakati wa jua
kali, mtapata wokovu. Basi wale wajumbe wakaenda, wakawaarifu watu wa Yabeshi; nao walifurahiwa.
10 Kwa hiyo watu wa Yabeshi walisema, Kesho tutawatokea, nanyi mtatufanyia yote myaonayo kuwa ni
mema.
11 Ikawa, kesho yake, Sauli akawapanga watu katika vikosi vitatu; nao wakaingia katikati ya marago
kwenye zamu ya asubuhi, wakawapiga Waamoni hata wakati wa jua kali; kisha ikawa wale waliosalia
wakatawanyika, hata wasiachwe wawili wao pamoja.
12 Ndipo watu walipomwambia Samweli, Ni nani yule aliyesema, Je! Huyo Sauli atatutawala? Walete watu
hao, ili tuwaue.
13 Lakini Sauli akasema, Hakuna mtu atakayeuawa leo, maana leo Bwana amefanya wokovu katika Israeli”.
Sasa tunaweza kuona hapo Roho ya Bwana pindi tu ilipomshukia Sauli alipatwa na Hasira kali. Na Tunafahamu hasira siku zote ikimwaka hata mtu yeyote huwa hajali ni madhara gani atakutana nayo, atapambana nayo kwa hali yoyote ilimradi tu atimize lengo lake, Sasa hii hasira iliyokuwa inamjia Sauli. Inayomfanya ashindwe kujitawala mwenyewe pindi imjiapo ambayo si kila wakati ilikuwa inamjia bali pale tu inapopaswa itimize kusudi fulani, ilitoka kwa Mungu mwenyewe. Hiyo ndio iliyowaokoa wana wa Israeli katika mikono ya maadui zao sikuzote, katika vita vigumu na vizito vilivyokuwa vinawajia waisraeli. Mungu alikuwa anaituma Roho yake kwa hasira nyingi juu ya Sauli, na bila kuogopa wala kujali lolote Sauli alishuka vitani kama simba na kusambaratisha maadui zao wote. Hapo ndipo hata mashujaa hodari wa vita wa Israeli ndipo walipokuwa wanamwogopea Sauli kwa Roho hiyo iliyokuwa juu yake.
Waamuzi 14:19 “Roho ya Bwana ikamjilia juu yake kwa nguvu, naye akatelemkia Ashkeloni, akapiga watu waume
thelathini katika watu hao, na kuzitwaa nyara zao, na kuwapa hao waliokitambua kitendawili mavao hayo.
Hasira zake zikamwaka, naye akakwea kwenda nyumbani kwa baba yake”.
Na ndivyo ilivyokuwa kwa mfalme Sauli, kwasababu alikuwa ametiwa mafuta na Mungu mwenyewe, Mungu alizielekeza HASIRA zile kwa kusudi maalumu la kuilinda Israeli dhidi ya madui zao, lakini wakati mfalme Sauli alipoacha kufuata njia za Mungu na kufanya vitu ambavyo Mungu hakuwa anamwagiza, ndipo Bwana akaghahiri kumtumia tena, hivyo akauamishia utawala wake kwa jirani yake Daudi. Lakini kumbuka Mungu hakumtoa Roho wake juu ya Sauli, isipokuwa roho ya utawala iliondolewa juu yake.
Hapo tunajifunza nini?. Mungu akishakutia mafuta, amekutia mafuta, hawezi kuyaondoa tena juu yako milele. Isipokuwa yataachwa tu yajiongoze kwa hisia zako na akili zako na sio tena kwa uvuvio au uongozi wa Roho Mtakatifu na hiyo ndiyo mbaya zaidi kwasababu ndio hapo mtu atatumia vipawa Mungu alivyompa kutimiza matakwa yake mwenyewe binafsi. Hilo ndio jambo lililomkuta mfalme Sauli baada ya Mungu kumrarulia ufalme na kumpa Daudi, kuanzia huo wakati mfalme Sauli akapoteza dira kabisa na mwelekeo wa kuitawala Israeli, akaanza kuzitumia nguvu zile za Hasira kuulinda ufalme wake na enzi yake badala ya kuilinda Israeli na ndio hapo akawa anamwinda Daudi siku zote, na hata wakati mwingine akiwa amestarehe tu nyumbani kwake kukiwa na amani, ile Roho pindi imjiapo, anajikuta anarusha rusha tu pasipo kujizuia ili tu amuue Daudi mtu asiyekuwa na hatia. Wakati hasira hizo zingepaswa zielekezwe kwa maadui wa Israeli.
Ni jambo hilo hilo lilimpata na shetani, baada ya shetani kushindwa kuilinda enzi yake Mungu aliyompa. Ambaye alikuwa ni kerubi aliyetiwa mafuta kuliko makerubi wote, yeye hakutaka kuenenda katika utaratibu Mungu aliomuwekea, Hivyo Mungu akaamua kuurarua utawala wake na kuwapa wengine. Lakini kumbuka kama tulivyoona Mungu akishakutia mafuta, hawezi kuyaondoa juu yako. Utaendelea nayo hivyo hivyo lakini yatakuwa hayaongozwi na Roho Mtakatifu bali kwa hisia zako na akili zako kujiundia ufalme wako.
Na ndio maana shetani mpaka sasa hajaondolewa nguvu zake alizopewa na Mungu, lakini sasa anazitumia kujiundia ufalme wake wa giza, ili kutimiza matakwa yake mwenyewe. Na hiyo ndiyo inayoitwa Roho mbaya kutoka kwa Mungu.
Vivyo hivyo na manabii wa uongo,na walimu wa uongo, na wachungaji wa uongo, na waimbaji wa uongo… waliopo leo, jambo ni lile lile, utakuta mwanzoni walitiwa kweli mafuta ya kundi la Mungu, walifundishe, walilishe, waliongoze katika njia njema..Lakini kwa jinsi siku zilivyozidi kwenda wakaanza kuyahalifu maagizo ya Mungu kidogo kidogo kama ilivyokuwa kwa mfalme Sauli. Na mwisho wa siku Mungu akaghahiri kuwaita Watumishi wake, hivyo ile Roho njema ya uongozi kutoka kwa Mungu iliyoachiwa juu yao kulilinda kundi la Mungu inawaacha, wanabakiwa tu na mafuta Mungu aliyowapa ili wajiongoze kwa tamaa zao wenyewe na sio kwa tamaa za Roho Mtakatifu.
Na ndio hapo utamwona mtu anajiita nabii anaona maono sahihi kabisa anatabiria watu mambo yajayo,na kweli yanatokea, lakini bado ni mwasherati, bado anaishi kidunia hawi tena kielelezo cha kuwapeleka watu mbinguni, utakuta badala awaelekeze watu kwa Mungu wao, anawaelekeza kwake, muda wote anajisifia yeye tu, utukufu wote wa Mungu anauchukua yeye, anasahau kuwa mafuta yale aliyopewa hayakuja kwa juhudu zake bali yalitoka kwa Mungu kwa kutimiza kusudi la kundi la Bwana, lakini yeye hajali hilo kwasababu Roho wa Mungu kashamwacha siku nyngi bali ile roho mbaya itokayo kwa Mungu ndiyo inayomwendesha mwisho wa siku anaishia kuleta madhara makubwa kwenye kanisa na kuhusika kuwapeleka watu wengi kuzimu, na kuwapoteza yamkini hata na wale walio wateule wa Mungu. Na siku zinavyozidi kuendelea utakuta yeye ndiye anayekuwa adui wa kwanza wa watumishi wa kweli Mungu kama Sauli alivyokuwa anafanya kwa Daudi.
Ndugu unayesoma, vipawa vya Mungu si vya kuvichezea. Kabisa, Mungu hadhihakiwi, usidhani kunena kwako kwa lugha ni ishara kuwa unaye Roho Mtakatifu, usidhani kuona kwako maono ni dalili kuwa unampendeza Mungu, usidhani kutoa kwako unabii ni ishara madhubuti kuwa upo katika mstari sahihi. Hayo yote hayakusaidii kitu kama hutasimama katika mstari wa Neno la Mungu. Biblia inatuambia
Waebrania 12:14 “Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu ATAKAYEMWONA BWANA ASIPOKUWA NAO;”
Unaona, utafanya yote lakini kama utakatifu haupo ndani yako, ni mambo machafu tu yamejaa ndani yako, uzinzi,ulevi, anasa, pornography,miziki ya kidunia, mastubation,uchawi,ibada za sanamu, utukanaji n.k hayo yote, hata kama utakuwa unazungumza na malaika kila siku kiasi gani, mbingu hutaiona ndugu.
Embu tusiwe mojawapo ya hao walionza vizuri na kumaliza vibaya, embu tuiruhusu ile Roho njema tu ya Mungu ituongoze na sio fikra zetu ili mwisho wetu upate kuwa mzuri katika safari yetu hapa duniani.Kumbuka Bwana hampi mtu roho mbaya, isipokuwa sisi ndio tunayoitumia roho njema ya Mungu katika ubaya.
Bwana Yesu akubariki sana.
Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Mada Nyinginezo:
JE! MTU ANAYETUNGISHA MIMBA KWENYE CHUPA MAHABARA, ANAHATIA MBELE ZA MUNGU?
JE! MABALASI BWANA YESU ALIYOYATUMIA KUGEUZIA MAJI KUWA DIVAI, YALITUMIKA TU KWA KAZI HIYO?
VITA VYA KIFIKRA BAADA YA KUZALIWA MARA YA PILI
Wakati tunakaribia kumaliza Mwaka ni kipindi maalumu sana cha kukaa na kutafakari na kuchukua hatua ya kumshukuru Mungu kwa Mengi aliyotutendea…Jambo kubwa la kuweza kumshukuru Mungu, ni juu ya pumzi aliyotupatia mwaka mzima, Katika safari ya mwaka mzima, kuna vipindi vingi tumepita lakini bado tunaishi..jua linachomoza na kuzama kila siku, hatujapitia matetemeko ya ardhi mwaka mzima, hatujapigana vita mwaka mzima, Mungu katuepusha na majanga mengi, katuepusha na magonjwa mengi, na hata tulipopata ugonjwa Bwana alituponya n.k Unafikiri ni kwasababu ya nani? Mpaka Mungu atuepushe na hayo yote?
si kwasababu tuna unafuu mbele zake, au kwasababu tunazingatia mlo kamili, wala si kwasababu tunajitunza sana na kujipenda, wala si kwasababu tunaustaarabu mzuri wa maisha, wala si kwaajili ya haki yetu sisi, wala si kwasababu sisi ni watakatifu, wala sio kwasababu tunabidii ya kumtafuta yeye, wala si kwasababu tunatenda mema sana, wala si kwasababu tunafunga sana, wala si kwasababu tunaomba sana, wala si kwasababu ni washirika wazuri wa kanisani au watoaji sadaka wazuri au wenye upendo sana.. Hakuna hata jambo moja kati ya haya ambayo Baba yetu wa mbinguni anayaangalia ili kutunyeshea sisi mvua yake, au kutupa pumzi, au kutupatia mema, au kutupatia uzima au kutuangazia jua lake, Hakuna hata moja!!
Sasa swali linakuja kama sio kwa ajili ya hayo yote, tunaumaliza mwaka salama..basi ni kwasababu gani? Kama si kwaajili ya utakatifu wetu, au bidii zetu, au juhudi zetu, au matendo yetu, au utakatifu wetu ni kwasababu gani basi tunapokea neema hii?.
Jibu ni rahisi, ni kwasababu ya haki ya mtu mmoja, ni kwasababu ya utakatifu wa mtu mmoja, ni kwasababu ya bidii ya mtu mmoja, ni kwasababu ya juhudi ya mtu mmoja, ni kwasababu ya matendo ya mtu mmoja, ni kwasababu ya maombi ya mtu mmoja, na huyo mtu ni BWANA YESU KRISTO, kwa huyo Baba wa mbinguni ndiye aliyependezwa naye.
Baba wa mbinguni hakupendezwa na maelfu waliopo duniani, hakuona mwenye haki hata mmoja duniani, wote tulikuwa tumetenda dhambi, tunakasoro nyingi, zisizokuwa na hesabu.
Zaburi 14: 2 “Toka mbinguni Bwana aliwachungulia wanadamu, Aone kama yuko mtu mwenye akili, Amtafutaye Mungu Wote wamepotoka, wameoza wote pamoja, Hakuna atendaye mema, La! Hata mmoja”.
Unaona! Sasa kama hakuna hata mmoja aliyemwona duniani mwenye haki??..unadhani vipi kama kuna ambaye angestahili kupokea baraka yoyote kutoka kwake?..hakuna hata mmoja..angestahili kupata pumzi kwa haki yake,wote tumestahili hukumu ya milele, Ndio maana inapasa atoke mtu mwingine kutoka mbinguni mwenye haki ambaye angestahili kupokea baraka kutoka kwa Mungu, kwasababu duniani hakuna hata mmoja mwenye akili, wote tumepungukiwa na utukufu wa Mungu..Hakuna hata mmoja mwenye unafuu.
Kwasababu hiyo basi kwa kuwa Yesu Kristo pekee ndiye aliyekuwa mkamilifu, ambaye hakutenda dhambi tangu kuzaliwa kwake mpaka ameondoka, yeye peke yake ndiye aliyehesabiwa haki kwa matendo yake binafsi, yeye peke yake ndiye Baba wa mbinguni aliyemwona mwenye AKILI anayemtafuta Mungu, alimchungulia toka juu akamwona akamtangaza “Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” …hakusema hawa ndio wanangu wapendwa wangu..hapana bali “huyu ndiye”..maana yake yupo mmoja tu!! kwa haki yake amestahili kubarikiwa kwa kila namna. Ndugu mtu asikudanganye kwamba kuna wabarikiwa wengi..Mbarikiwa ni mmoja tu! Yesu Kristo.. Maandiko yanasema hivyo..
Mathayo 21:5 “Mwambieni binti Sayuni Tazama, mfalme wako anakuja kwako, Mpole, naye amepanda punda,
Na mwana-punda, mtoto wa punda.
6 Wale wanafunzi wakaenda zao, wakafanya kama Yesu alivyowaamuru,
7 wakamleta yule punda na mwana-punda, wakaweka nguo zao juu yao, naye akaketi juu yake.
8 Watu wengi katika ule mkutano wakatandaza nguo zao njiani; na wengine wakakata matawi ya
miti, wakayatandaza njiani.
9 Na makutano waliotangulia, na wale waliofuata, wakapaza sauti, wakisema, HOSANA , MWANA WA DAUDI; NDIYE MBARIKIWA , yeye ajaye kwa jina la Bwana; Hosana juu mbinguni”.
Sasa basi kwasababu ni mmoja tu! Ndiye aliyestahili baraka, Yesu Kristo pekee asiyestahili kufa wala kuangamizwa milele…Yeye Yesu Kristo Bwana wetu alitununua sisi tusiokuwa wakamilifu kwa Baba wa mbinguni, akatushirikisha baraka zake alizobarikiwa na Baba wa mbinguni, akatuhusisha katika fadhili zake alizofadhiliwa na Baba, japokuwa sisi hatukustahili kubarikiwa, wala kupewa uzima, wala kuangaziwa jua..lakini sasa tunayapata hayo yote kupitia Yesu Kristo.
Kwasababu hiyo basi hata kipindi hichi tunachomaliza mwaka, kama bado tunaishi…tusijisifu ni kwa matendo yetu, sio kwa matendo yetu hata kidogo, bali kwa ajili ya matendo ya Yesu Kristo aliyoyaishi hapa duniani yaliyompendeza Baba..si kwa ajili tuna bidii za kujitunza hapana…wapo waliokuwa na bidii ya kujitunza sana lakini wameondoka..ni kwaajili ya Huruma ya Yesu Kristo juu yetu.
Sio kwasababu ya juhudi zetu, ndio tumebarikiwa na kupata mema ya nchi hapana ni kwasababu ya Mbaraka Bwana Yesu aliobarikiwa na Baba yake kwa haki yake..na sisi ndio tunaoushiriki . Yesu Kristo pekee yake ndiye Mbarikiwa, sisi ni kama waalikwa tu! Tumealikwa kwenda kula baraka za Yesu Kristo..Ndio maana na sisi tunajumuishwa kama miongoni mwa waliobarikiwa, lakini Mbarikiwa ni mmoja tu!
Kwahiyo ndugu, tukimfahamu Yesu Kristo kwa namna hiyo, hatuna budi kumshukuru Mungu kwa ajili yake, hatuna budi kunyenyekea sana na kumwambia Bwana Ahsante…Ni wakati wa kumshukuru Mungu kwa jambo moja moja alilotutendea kuanzia mwanzo wa mwaka huu hata mwisho. Hata kama bado ni mgonjwa mshukuru sana! Hata kama bado hukupata mwaka huu ulichokitamani, mshukuru tu Maadamu bado unaishi…Kwa wakati wake ukifika, atakutimizia matakwa yako.
Mshukuru kwasababu bado upo kwenye Imani, hujaanguka, shetani alikutafuta mwaka mzima kama simba angurumaye..Mshukuru kwasababu amekuepusha na yule mwovu..mshukuru kwasababu kama sio yeye kukubaliwa na Baba wa mbinguni usingekuwa hapo ulipo..kama sio yeye kuishi maisha makamilifu tangu anazaliwa mpaka anakufa usingepata hata hiyo pumzi, kama sio yeye kuwa mwenye akili ya kumtafuta Mungu, kwa kufunga na kuomba, na dua na sala nyingi…leo hii dunia pengine isingekuwepo, wote tungekuwa ni wana wa Jehanum ya moto.
Mshukuru kwa kila nyanja ya maisha yako, na pia mwombe Neema zaidi kwa Mwaka unaokuja, ukazidi kumtafuta yeye na kumsogelea zaidi, na kumjua yeye zaidi na uwezo wake, Akakupe Neema zaidi ya kuushinda ulimwengu na mambo yake, maana mambo ya ulimwengu huu yanapita, na yeye yupo mlangoni kurudi, na maandiko yanasema atakuja kama mwivi usiku wa manane!..Siku moja inapopita ndivyo tunavyokaribia mwisho, mwaka mmoja unapopita ndivyo siku ile tunavyozidi kuikaribia. Tumwombe Bwana neema na yeye atatusaidia..
Bwana akubariki sana!
Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Mada Nyinginezo:
KWANINI USIICHAGUE TUZO ISIYOHARIBIKA?
Tukisoma biblia hatuoni mahali popote ikitoa msisitizo juu ya kusherehekea siku ya kuzaliwa au siku ya kufa kwa Bwana wetu YESU KRISTO. Kwamba ni jambo la lazima watu wote walifanye, au walizingatie kama sheria ya kidini, sasa swali linaweza kuulizwa kama ni hivyo basi hatupaswi kujiundia siku au kujiwekea utaratibu wa kuadhimisha siku ya kuzaliwa au siku ya kufa kwa mwokozi wetu duniani, kwasababu maandiko yahatuagizi kufanya hivyo?.
Hilo swali ni rahisi kulijibu kama tutakaa na kufikiria juu ya maisha yetu ya kila siku. Embu jaribu kufikiria katika maisha yako tangu ulipozaliwa hadi sasa unavyoishi umeshawahi kualikwa katika sherehe za kuzaliwa za watu [Birthday] mara ngapi? Au umeshawahi kufanya sherehe ya kuzaliwa kwako mara ngapi?, au umeshawahi kusikia sherehe za kuzaliwa za watu wengine zikisheherekewa mara ngapi?. Ni wazi utafahamu kuwa aidha kama wewe hujawahi kufanya, au hujawahi kuthamini siku ya kuzaliwa kwako na hivyo huna mpango wa kujisumbua na mambo hayo fahamu kuwa hiyo haimzuii mwingine kutokuithamini siku yake ya kuzaliwa na kufanya sherehe kubwa na kuwaalika rafiki zake na ndugu zake baada ya kuona umuhimu wa kumshukuru Mungu kumwongezea mwaka mwingine wa kuishi duniani.
Vivyo hivyo tukirudi katika ukristo, hakuna sharti lolote lililotolewa na Mungu juu ya kusheherekea sikukuu yoyote ile, iwe ni ya pasaka, iwe ni ya pentekoste, iwe ni ya kuzaliwa kwa Bwana YESU, iwe ni ya kubatizwa , iwe ni ya kitu chochote kile hakuna sharti lolote tulilopewa. Lakini wapo wanaothamini mambo kama hayo katika maisha yao. Wapo wanaoona umuhimu wa kuadhimisha sikukuu ya kuzaliwa mfalme duniani miaka 2000 iliyopita, hivyo wanaona si vema wauache mwaka upite hivi hivi bila kutafuta au kuchunguza ni siku ipi inayoweza kukaribiana na siku Bwana aliyozaliwa ili waisheherekee. Kadhalika wapo wanaodhimisha siku ya kufa kwa Bwana, wanaona umuhimu wa kifo cha Yesu msalaba kilichowaletea wokovu na hivyo hawawezi kujizuia kufurahia na kushangalia kwa sherehe siku hiyo, wapo pia wanaodhimisha siku za kubatizwa kwao, siku ambayo walizaliwa mara ya pili. Wapo pia wanaodhimisha siku za Bwana kuwajibu maombi yako .N.k.
Lakini jambo linalowakwamisha wengi ni pale wanaposhindwa kutambua ni siku ipi hasa ambayo Bwana YESU aliyozaliwa na hiyo inawapelekea wafikiri wanaabudu miungu mingine hususani wanapoona tarehe 25 Disemba, anahusishwa na sikukuu ya kuzaliwa kwa miungu ya kipagani ya kirumi, ndipo wanapoona kuwa ni dhambi mbele za Mungu hata siku hiyo kumfanyia Mungu ibada.
Ni kweli tukichunguka katika maandiko tunaona kuwa Bwana Yesu hakuzaliwa tarehe 25 Disemba, kulingana na baadhi vifungu vinavyodokeza majira ya kuzaliwa kwake, kwamfano kama tukisoma kitabu cha Luka tunaona kuwa malaika Gabrieli alimtokea Zakaria kuhani (babaye Yohana mbatizaji) siku za zamu za ukuhani wa ABIYA.
Luka 1: 5 “Zamani za Herode, mfalme wa Uyahudi, palikuwa na kuhani mmoja, jina lake Zakaria, wa zamu ya Abiya, na mkewe alikuwa mmojawapo wa uzao wa Haruni, jina lake Elisabeti.
6 Na wote wawili walikuwa wenye haki mbele za Mungu, wakiendelea katika amri zote za Bwana na maagizo yake bila lawama.
7 Nao walikuwa hawana mtoto, maana Elisabeti alikuwa tasa, na wote wawili ni wazee sana.
8 Basi ikawa, alipokuwa akifanya kazi ya ukuhani katika taratibu ya zamu yake mbele za Mungu,
9 kama ilivyokuwa desturi ya ukuhani, kura ilimwangukia kuingia katika hekalu la Bwana ili kufukiza uvumba”.
Kumbe katika siku za zamu za Abiya ambazo alikuwa anafanya kazi za kikuhani ndizo Zekaria alizotokewa na malaika Gabrieli. Na hivyo tukirudi katika agano la kale kuangalia zama ya Abiya ilikuwa ni ya ngapi na inadondokea mwezi gani ndipo tutakapopata majibu ya majira ya kipindi ambacho Zekaria alitokewa na Malaika Gabrieli. Na kama tunavyosoma katika 1Nyakati 24. Inasema:
1Nyakati 24: 7 “Kura ya kwanza ikamtokea Yehoiaribu, na ya pili Yedaya;
8 ya tatu Harimu, ya nne Seorimu;
9 ya tano Malkia, ya sita Miyamini;
10 YA SABA HAKOSI, YA NANE ABIA;
11 ya kenda Yeshua, ya kumi Shekania;
12 ya kumi na moja Eliashibu, ya kumi na mbili Yakimu;
13 ya kumi na tatu Hupa, ya kumi na nne Yeshebeabu;
14 ya kumi na tano Bilga, ya kumi na sita Imeri;
15 ya kumi na saba Heziri, ya kumi na nane Hapisesi;
16 ya kumi na kenda Pethahia, ya ishirini Ezekieli;
17 ya ishirini na moja Yakini, ya ishirini na mbili Gamuli;
18 ya ishirini na tatu Delaya, ya ishirini na nne Maazia”.
Kwahiyo hapo tunaona zamu ya Abiya ilikuwa ni ya NANE katika ufanyaji wa kazi za kikuhani. Na kazi hizo zilikuwa zinafanyia sabato mpaka sabato yaani wiki mpaka wiki, hivyo zama ya Abiya iliangukia wiki ya 8 katika utendaji kazi wa kikuhani. Na tunajua kuwa mwaka wa kiyahudi huwa unaanza mwanzoni mwa mwezi april, na hivyo ukihesabu hapo majuma mawili utaona zamu hiyo inadondokea katikati ya mwezi wa 6. Kwahiyo tunaona hapo Zekaria kumbe alitokewa majira ya mwezi wa 6 na muda mfupi baada ya hapo pengine mwezi wa 6 mwishoni au wa 7 mwanzoni mkewe Elizabethi alipata mimba, na biblia inatuambia pia miezi 6 baada ya kupata mimba kwake Elizabethi Malaika Gabrieli alimwendea Bikiria Mariamu na kumpasha habari za yeye kupata mimba ya Bwana Yesu (Luka 1:26).
Hivyo mpaka hapo tunaona ni mwezi wa 12 katikati au wa kwanza mwanzoni ndipo mimba ya Bwana YESU ilipotungishwa. Na tunajua kuwa baada ya miezi 9 mtoto huwa ndio anazaliwa, sasa ukipiga hesabu utaona kuwa uwezekano mkubwa wa kuzaliwa kwa Bwana wetu YESU KRISTO unaweza angukia katikati ya mwezi wa 9 au mwanzoni mwa mwezi wa 10, kwa kalenda yetu sisi. Na ndio maana utaona pia Bwana Yesu alianza kuhubiri akiwa na miaka 30 na akamaliza akiwa na miaka 33 na miezi 6, na siku aliposulibiwa ilikuwa ni Mwezi wa nne (April). Kwahiyo ukihesabu vizuri hapo utagundua alianza kuhubiri kati ya mwezi wa 9 hadi wa 10, ambao ndio mwezi aliozaliwa.
Zipo pia thibitisho nyingine zinaonyesha kuwa Kristo alizaliwa majira hayo lakini hatuwezi kuziandika zote hapa. Lakini je! wanaodhimisha siku hiyo tarehe 25 Disemba wanafanya makosa?. Jibu ni hapana kama tulivyotangulia kuona biblia haijatoa amri juu ya kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Yesu mahali popote, na hivyo yeyote anayefanya hivyo ikiwa ni kwa lengo lake binafsi kwamba anaona umuhimu wa kuunda siku yake inayoweza kukaribiana na siku ya kuzaliwa kwa Yesu ili amtukuze na kumfurahia Mungu, Iwe ni Aprili, iwe ni Agosti, iwe ni Septemba, Iwe ni Octoba, Iwe ni Disemba iwe ni siku yoyote ile hatendi dhambi maadamu kaiweka wakfu kwa Mungu wake, ili kumwabudu na kumshukuru.
Dhambi inakuja ni pale siku kama hiyo ambayo tayari umeshawakwa wakfu kuwa ibada kwa Mungu, halafu siku hiyo inageuzwa na kuwa siku ya kufanya sherehe za ulafi, ibada za sanamu,ulevi, pombe, anasa, uasherati n.k. hiyo ni sawa na kumkufuru Mungu moja kwa moja, na dhambi ya kumkufuru Mungu ni dhambi ya juu sana kuliko dhambi zote. Ni heri kama usingeichukulia kama ni sikukuu ya imani yako, kuliko kuiona hivyo halafu bado unainajisi. Hiyo ni sawa imeiweka nadhiri kwa Bwana halafu umeshindwa kuitoa.
Utakuta mtu ametoka kanisani siku hiyo, pengine hata kashiriki meza ya Bwana, na anajua kabisa siku kama hiyo inapaswa iwe takatifu, kama ni kusheherekea isheherekewa kwa upendo wa Kristo, isheherekewe kwa kuzingatia vigezo vya utakatifu na biblia, lakini badala yake mtu akitoka hapo na kwenda kunywa pombe, na kwenda kuzini, na kwenda kuzurura kwenye vikundi vya ngoma na disco, na kwenda kuabudu sanamu na kuzunguka kwa waganga, kuna hatari kubwa sana. Na Hivyo siku hiyo kwake inageuka kuwa ni laana badala ya Baraka.
Ndugu yangu upo sasa katika majira haya yanayoitwa ya sikukuu, embu kama umependa kuzifanya kuwa ni za Kristo, zifanye ziwe hivyo kweli kweli, uzilinde, na kuzifanya takatifu, vinginevyo itakuwa ni ibada ya kipagani kwako zaidi hata ya hao wapagani wenyewe. Ni maombi yangu wewe kama mkristo utapata akili katika hayo, kumbuka ni majira unayokwenda kuvuka mwaka, mambo mengi Mungu amekuepushia mabaya, tafakari miezi yote hiyo umevukishwa salama, hivyo usimalize mwaka wako vibaya kwa Bwana. Huu ni wakati wa kujinyenyezeka ili Mungu akupe rehema za Mwaka unaoanza.
Mungu akubariki sana.
Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Nikutakie sikukuu njema, na Heri ya Mwaka mpya katika jina la YESU KRISTO BWANA WETU.
Mathayo 24: 24 “Kwa maana watatokea makristo wa uongo, na manabii wa uongo, nao watatoa ishara kubwa na maajabu; wapate kuwapoteza, kama yamkini, hata walio wateule”.
Manabii wa uongo wa agano la kale ni kivuli cha manabii wa uongo katika agano jipya. Mfano wa yale yaliyokuwa wanayafanya agano lake ndio hayo hayo wanayoyafanya sasa katika agano jipya.
Waliwapoteza wale waliokuwa wachanga kiimani kadhalika walifanikiwa pia kuwapoteza hata baadhi ya wale waliokuwa wamesimama kiimani. Mfano wa manabii hao tunamwona mtu kama Hanania aliyetokea kipindi cha wafalme, wakati ambapo Mungu alisema Yerusalemu utateketezwa na watu wake kupelekwa utumwani Babeli, yeye alisimama kwa ujasiri mkubwa mbele ya mfalme na mbele ya makuhani wa Bwana na mbele ya watu wote na kusema Bwana anasema hivi haitatimia miaka miwili mpaka vile vyombo na vitu vyote Nebukadreza alivyovichukua kwenye ile awamu ya kwanza na kuvipeleka Babeli kurudishwa tena Israeli,.. Lakini kama tunavyosoma kumbe Mungu hakumtuma na unajua kwa namna ya kawaida mtu akitoa maneno ya faraja hata kama yawe ni ya uongo kiasi gani atapendwa tu!. Na ndio maana tunakuja kuona nabii kama Yeremia alipokuja kusema kuwa Yerusalemu utateketezwa na watu wake kuchukuliwa mateka alionekana kama ni mpinga-kristo, asiyeutakia mema Yerusalemu mji wa Mungu, hivyo mfalme na wale watu wakaamuru kwamba afungwe, katika vifungo vya mateso. Habari hizo tunazisoma katika kitabu cha Yeremia 28.
Kadhalika Walikuwepo na manabii wengine 400 enzi hizo hizo za wafalme wa Israeli waliokuwa wakimtabiria mfalme Ahabu siku zote, lakini ilipofika wakati ambapo Mungu amekusudia kuleta jambo baya juu ya mfalme Ahabu kutokana na maovu yake, ndipo likazuka jopo kubwa la manabii wa uongo wakaanza kumtabiria mfalme habari za kufanikiwa kwake atakapokwenda vitani. Lakini kulikuwa na nabii mmoja aliyeitwa Mikaya yeye hakupenda kusimamia upande wowote, lakini yeye kwa uaminifu kabisa alimwomba Mungu na kuuliza habari za mfalme Ahabu na ndipo Mungu akamwambia ni lazima Ahabu afe atakapokwenda vitani, lakini kwa kuwa mfalme aliona ni manabii wengi wanaomtabiria mafanikio yake zaidi ya uharibifu wake, na kwasababu yeye mwenyewe siku zote anapenda mambo ya faraja tu! hivyo akaamua kuwasikiliza wale wengi na kwenda vitani na kama tunavyosoma alipokwenda tu alikufa.(2Nyakati 18).
Sasa hawa wote ni mifano wa manabii wachache ambao hata sasa wapo kwenye agano jipya. Kadhalika lipo kundi lingine la manabii wa uongo lilikuwa kwenye agano la kale, Na hilo ndilo libaya zaidi kwasababu linatumika mahususi kuwaangusha wale wanaoonekana kusimama katika imani, hilo linaweza kuwaangusha hata walio manabii wa ukweli, na mfano wa kundi hilo tunaweza kulisoma habari yake katika kitabu cha 1Wafalme 13
Embu tusome pamoja na Bwana atatusaidia kupata kitu hapo:
1Wafalme 13:1-32
1 Na tazama, akatoka mtu wa Mungu katika Yuda kwa neno la Bwana, akafika Betheli. Naye Yeroboamu alikuwa akisimama penye madhabahu, afukize uvumba.
2 Basi mtu huyo akapiga kelele juu ya madhabahu, kwa neno la Bwana akasema, Ee madhabahu, madhabahu, Bwana asema hivi, Angalia, mtoto atazaliwa katika nyumba ya Daudi, jina lake Yosia; na juu yako atawachinja makuhani wa mahali pa juu, wanaofukiza uvumba juu yako, na mifupa ya watu itateketezwa juu yako.
3 Akatoa ishara siku ile ile, akasema, Hii ndiyo ishara aliyoinena Bwana, Tazama, madhabahu itapasuka, na majivu yaliyo juu yake yatamwagika.
4 Ikawa, mfalme Yeroboamu alipoyasikia maneno ya yule mtu wa Mungu, alipopiga kelele juu ya madhabahu huko Betheli, alinyosha mkono wake pale madhabahuni, akasema, Mkamateni. Basi ule mkono wake aliounyosha ukakatika, wala hakuweza kuurudisha kwake tena.
5 Madhabahu ikapasuka, majivu ya madhabahuni yakamwagika, sawasawa na ishara aliyoitoa mtu wa Mungu kwa neno la Bwana.
6 Mfalme akajibu, akamwambia yule mtu wa Mungu, Umsihi sasa Bwana, Mungu wako, ukaniombee, ili nirudishiwe mkono wangu tena. Yule mtu wa Mungu akamwomba Bwana mkono wa mfalme ukarudishwa tena, ukawa kama ulivyokuwa kwanza.
7 Mfalme akamwambia mtu wa Mungu, Karibu nyumbani kwangu ujiburudishe, nami nitakupa thawabu.
8 Mtu wa Mungu akamwambia mfalme, Ujaponipa nusu ya nyumba yako, sitaingia pamoja nawe, wala sitakula chakula, wala sitakunywa maji mahali hapa;
9 maana ndivyo nilivyoagizwa kwa neno la Bwana, kusema, Usile chakula cho chote wala usinywe maji, wala usirudi kwa njia ile uliyoijia.
10 Basi akaenda zake kwa njia nyingine, wala hakurudi kwa njia ile aliyoijia Betheli.
11 Basi nabii mmoja mzee alikuwa akikaa katika Betheli; na wanawe wakamwendea wakamwambia kila neno alilolitenda yule mtu wa Mungu siku ile katika Betheli; na maneno aliyomwambia mfalme, hayo nayo walimwambia baba yao.
12 Baba yao akawaambia, Amekwenda zake kwa njia ipi? Kwa maana wanawe walikuwa wameiona njia ile aliyoiendea yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda.
13 Akawaambia wanawe, Nitandikieni punda. Wakamtandikia punda, naye akampanda.
14 Akamfuata mtu wa Mungu, akamkuta ameketi chini ya mwaloni, akamwambia, Je! Wewe ndiwe yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda? Akamwambia, Mimi ndiye.
15 Akamwambia, Karibu kwangu nyumbani, ule chakula.
16 Naye akamwambia, Siwezi kurudi pamoja nawe, wala kuingia pamoja nawe; wala sili chakula wala sinywi maji pamoja nawe hapa;
17 kwani nimeambiwa kwa neno la Bwana, Usile chakula wala usinywe maji huko, wala usirudi kwa njia ile uliyoijia.
18 Akamwambia, Mimi nami ni nabii kama wewe, na malaika akaniambia kwa neno la Bwana, kusema, Mrudishe pamoja nawe nyumbani kwako, ale chakula, akanywe maji. Lakini alisema uongo.
19 Basi mtu yule akarudi pamoja naye, akala chakula, akanywa maji nyumbani mwake.
20 Hata ikawa, walipokuwa wameketi mezani, neno la Bwana likamjia nabii yule aliyemrudisha;
21 akamlilia yule mtu wa Mungu aliyetoka katika Yuda, akinena, Bwana asema hivi, Kwa sababu umeiasi kauli ya Bwana, wala hukuishika amri ile aliyokuamuru Bwana, Mungu wako,
22 bali umerudi, ukala chakula ukanywa maji, hapo alipokuambia, Usile chakula, wala usinywe maji; maiti yako haitaliingia kaburi la baba zako.
23 Basi ikawa, alipokwisha kula chakula na kunywa maji, yule nabii aliyemrudisha akamtandikia punda.
24 Na alipokuwa amekwenda zake, simba alimkuta njiani, akamwua. Maiti yake ikatupwa njiani, na yule punda akasimama karibu naye; na yule simba naye akasimama karibu na maiti.
25 Na tazama, watu wakapita, wakauona mzoga umetupwa njiani, na yule simba akisimama karibu na mzoga, wakaenda, wakatoa habari katika mji ule alimokaa yule nabii mzee.
26 Na yule nabii aliyemrudisha njiani alipopata habari, akasema; Ndiye yule mtu wa Mungu, aliyeiasi kauli ya Bwana; kwa hiyo Bwana amempambanisha na simba, simba akamrarua, akamwua, sawasawa na neno la Bwana alilomwambia.
27 Akawaambia wanawe, akasema, Nitandikieni punda. Wakamtandikia.
28 Akaenda, akamwona yule maiti ametupwa njiani, na punda na simba wamesimama karibu na maiti; yule simba alikuwa hakumla maiti, wala hakumrarua punda.
29 Nabii yule akamtwaa maiti wa yule mtu wa Mungu, akamweka juu ya punda wake, akamrudisha; yule nabii mzee akaenda mjini mwake, kukaa matanga, na kumzika.
30 Akamweka maiti katika kaburi lake mwenyewe; wakamlilia, wakisema, Aa! Ndugu yangu!
31 Hata ikawa, alipokwisha kumzika, akawaambia wanawe, akasema, Nikifa mimi, nizikeni katika kaburi hili alimozikwa yule mtu wa Mungu; iwekeni mifupa yangu kando ya mifupa yake.
32 Kwa maana neno hilo alilolia juu ya madhabahu katika Betheli, kwa neno la Bwana, na juu ya nyumba zote za mahali pa juu zilizo katika miji ya Samaria, hakika litatimizwa.
Amen.
Ukifuatilia utaona huyu mtu wa Mungu, alikuwa amethibitika kabisa katika Imani kiasi kwamba hata mfalme Yerobohamu mwenyewe licha ya utajiri wake na fahari yake kuwa nyingi hakuweza kumshawishi kukaa na kuyaasi maagizo ya Mungu. Wala hakukuwa na mtu yeyote njiani aliyeweza kumshawishi ayatupilie mbali maagizo ya Mungu aliyompa. Lakini alipofika mbali kidogo na kukaribia kuimaliza safari yake, ndipo akazuka mmoja wa wale manabii wa uongo wale ambao kazi yao siku zote ni KUTAMKA MANENO YA FARAJA kinyume na maagizo ya Mungu.
Embu fikiria huyu mtu wa Mungu katika safari yake yote ya kuukatiza mji, bila kula wala kunywa, jua kali, uchovu mwingi, ni kweli angetamani hata apate mahali pa kustarehe kwa muda mfupi ili ale na kunywa apate nguvu kisha baada hata ya siku moja au mbili aende zake nyumbani, lakini Mungu hakuwambia afanye hivyo, Mungu hakutaka mtumishi wake aliyemtia mafuta mwaminifu akae au ashirikiane na watu waovu wanaoishi kwenye mji uliojaa sanamu uliojaa sanamu na machukizo. Mji uliojaa manabii vuguvugu, wanaopenda kutabiri mambo ya amani tu, siku zote, wanaopenda kutabiri mambo ya kuwafurahisha watu, yale mengine ya hukumu hawataki kuyazungumza. Lakini huyu mtu wa Mungu hakuisikia sauti ya Bwana ndipo nabii huyu mzee wa uongo ambaye kazi yake ni kutabiri mambo ya faraja akaja kumletea habari kwamba Bwana amemwambia arudi kwake ale, anywe..Kumbe hajui kuwa anakwenda kuiponza roho yake mwenyewe. Na mwisho wa siku kama tunavyosoma hakufika mbali simba akamuua.
Ndugu Hizi ni nyakati mbaya zile zilizobiriwa kuwa watatokea manabii wa uongo wapate kuwapoteza hata yamkini walio wateule. Inawezakana ikawa wewe ni mteule wa Mungu, inaweza ikawa hata wewe ni mtumishi mwaminifu wa Mungu na unatembea katika njia zilizonyooka za Yesu Kristo, mfano wa huyu mtu wa Mungu tuliyesoma habari zake. Lakini kumbuka dunia ya sasa inapumbaza sana, na wanaoipumbaza ni manabii wa uongo, hao ambao kazi yao kubwa ni kutabiri mambo ya Baraka tu, mambo malaini tu, mambo ya matumaini tu, kana kwamba Mungu wakati wote anapendezwa na dunia hii ya sasa iliyojaa dhuluma na uchafu kuliko hata ile ya sodoma na Gomora.
Hivyo kwa kuwa husikii tena ukikemewa dhambi au husikii tena habari za dhiki kuu ambayo inakaribia kuikumba hii dunia siku sio nyingi, kama ulivyokuwa unasikia hapo zamani, wewe unastarehe na kulegeza kamba zako za wokovu, na kuwa vuguvugu. Kwa kuwa husikii tena manabii hao wakizungumzia juu ya siku za mwisho wewe unaona kumbe mwisho bado sana, na wala uharibifu hautaikumba dunia leo wala kesho. Kwa kuwa hawagusii tena uvaaji wako, angali wewe hapo mwanzo ulikuwa ni mwanamke mtakatifu vimini huvai wala suruali, lakini sasa unaona watiwa mafuta wa Bwana hawakemei tena hivyo vitu wanakwambia vyote ni sawa na wewe unasikiliza uongo wao unaanza kuvaa vuguvugu tu kama wanawake wa kidunia. Hujui kuwa unachukuliwa na wimbi hilo la manabii wa uongo kukupoteza wewe. Uende kuzimu.
Ndugu usitazame ni jinsi gani wanaona maono ambayo ni sahihi kabisa, ni kweli hata wale wa agano la kale walikuwa vivyo hivyo, walikuwa wanaona maono ya ukweli na ndio maaana waliaminiwa na watu pamoja na wafalme kirahisi, lakini linapokuja suala la kutabiri juu ya uharibifu na hukumu za Mungu, na kiama hapo ndipo utakapoweza kuyatenga magugu na ngano. Kwasababu hilo kundi lingine halipendi kutabiri juu ya hayo, lenyewe ni maneno ya faraja tu siku zote, Unamwona huyu Nabii, aliyempotosha Nabii mwenzake aliwe na Simba alichofanya?? Baada ya kumfariji na kumdanganya kwamba Bwana kamwambia arudi ale pamoja na yeye, alijua kabisa Bwana hakumwambia lakini kamdanganya makusudi…
Yeremia 14: 14 “Ndipo Bwana akaniambia, Hao manabii wanatabiri uongo kwa jina langu mimi; mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru, wala sikusema nao; wanawapeni unabii wa maono ya uongo, na uaguzi, na neno la ubatili,” na hadaa ya mioyo yao. 15 Basi, kwa hiyo Bwana asema hivi, Kwa habari za manabii wanaotabiri kwa jina langu, wala mimi sikuwatuma, LAKINI HUSEMA, UPANGA NA NJAA HAVITAINGIA KATIKA NCHI HII; Kwa upanga na njaa manabii hao wataangamizwa. 16 Na watu hao, waliopewa unabii na wao, watatupwa nje katika njia kuu za Yerusalemu kwa sababu ya upanga na njaa; wala hawatakuwa na mtu wa kuwazika, wao na wake zao, na wana wao, na binti zao; maana nitamwaga uovu wao wenyewe juu yao”.
Unaona?. Huu si wakati wa kuziamini kila roho zinazokutakia mafanikio tu, na wala hazijali hatma ya maisha yako baada ya kifo, zichunguze sana, leo zitakutabiria utajifungua mapacha, kesho zitakutabiria utajenga jumba, mwezi ujao zitakutabiria faraja za ajabu, lakini hazitakutabiria madhara ya dhambi baada ya kifo, hazitakutabiria madhara ya sanamu ndani ya moyo wako, hazitakutabiria Neno la Yesu linalosema “ukiwa vuguvugu nitakutapika” Biblia inasema mbingu na nchi zitapita lakini maneno ya Mungu hayatapita kamwe, Bwana alisema dunia itaangamizwa, ni kweli itaangamizwa, alisema ufalme wa mbinguni umekaribia ni kweli umekaribia, alisema kutakuwa na dhiki kuu, ni kweli dhiki kuu lazima ije, alisema yupo mlangoni kurudi, ni kweli yupo mlangoni, alisema tujiepushe na hichi kizazi cha ukaidi kilichopotoka, na alisea pia “hakuna mtu atakayemwona yeye asipokuwa mtakatifu Waebrabia 12:14” Je! wewe leo umejiwekaje?. Ni matumaini yangu utaanza kuufanya wito wako na uteule wako imara kuanzia sasa, na kuacha kujitumainisha na mafundisho ya faraja ya hao wanabii wa uongo ambao wapo wengi duniani. Na kuanza pia kutazama siku za vilio ambazo nazo zinakuja mbeleni.
Bwana akubariki sana.
Tafadhali “Share” ujumbe huu kwa wengine na Bwana atakubariki.
Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Je Damu ya yesu inanenaje mema kuliko ya habili?..Nini madhara ya kuidharau sauti ya Damu ya thamani ya Yesu Kristo?
Shalom! karibu tujifunze Neno la Mungu kwa pamoja, Leo tutajifunza juu ya damu ya YESU kwa ufupi. Naamini utaongeza kitu juu ya vile ulivyojaliwa kuvijua na Bwana..
Tukisoma katika kile kitabu cha Mwanzo, tunamsoma Kaini aliyemwua ndugu yake Habili, kwasababu sadaka yake haikukubaliwa na Mungu, na ya ndugu yake kukubaliwa..Habari hiyo tunaisoma katika kitabu cha…
Mwanzo 4: 8 “Kaini akamwambia Habili nduguye, [Twende uwandani]Ikawa walipokuwapo uwandani,Kaini akamwinukia Habili nduguye,akamwua.
9 Bwana akamwambia Kaini, Yuko wapi Habili ndugu yako? Akasema, Sijui, mimi ni mlinzi wa ndugu yangu?
10 Akasema, Umefanya nini? SAUTI YA DAMU YA NDUGU YAKO INANILILIA KUTOKA KATIKA ARDHI.
11 Basi sasa, umelaaniwa wewe katika ardhi, iliyofumbua kinywa chake ipokee damu ya ndugu yako kwa mkono wako;
12 utakapoilima ardhi haitakupa mazao yake; utakuwa mtoro na mtu asiye na kikao”.
Tunaona hapo Bwana alimwambia Kaini “sauti ya damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika ardhi.”..kumbuka haikusema “sauti ya roho ya ndugu yako”, hapana bali ilisema “sauti ya damu”..ikiwa na maana kuwa damu ina sauti na inanena.
Pia haikusema “sauti ya damu inanililia kutoka mbinguni”..bali ilisema “sauti inanililia kutoka katika ardhi”..kwahiyo kuna uhusiano pia wa damu na ardhi..tutakuja kuiona huko mbeleni..
Lakini pia tukisoma kitabu cha Waebrani Mlango 12: 24 inasema “Na Yesu mjumbe wa agano jipya, na damu ya kunyunyizwa, INENAYO MEMA kuliko ile ya Habili”.
Hapa tunaona kuna damu mbili ya Kwanza ni ya Habili na ya pili ni ya Bwana Yesu…Lakini tunasoma damu ya YESU KRISTO inanena mema kuliko ile ya Habili.
SASA DAMU YA YESU INANENAJE MEMA KULIKO YA HABILI?
Habili tunamsoma alikuwa ni mtu wa Haki, na alienda katika ukamilifu, hata akapata ufunuo bora wa kumtolea Mungu sadaka, na zaidi ya yote alimtolea katika sehemu zilizonona na katika wazaliwa wa kwanza wa wanyama wake…Ikionyesha kabisa kuwa alikuwa ni mtu wa Haki aliyemjali Mungu, na kumfanya Mungu kuwa wa kwanza katika maisha yake..Na pia alikuwa anakwenda katika maagizo yake na sheria zake…Na hivyo mpaka kufikia wakati anauawa na ndugu yake, hakuwa na hatia yoyote na hivyo damu yake ikawa ni kama damu ya mtu asiyekuwa na hatia..Na ilipofika ardhini ikaanza kutoa sauti ikimlilia Mungu..
Na kadhalika Bwana Yesu Kristo, aliuawa pasipo hatia yoyote, yeye hakuwa na kosa lolote hata kuuawa pale Kalvari,
Matendo 4: 25 “Nawe ulinena kwa Roho Mtakatifu kwa kinywa cha babaetu Daudi, mtumishi wako, Mbona mataifa wamefanya ghasia, Na makabila wametafakari ubatili?
26 Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake.
27 Maana ni kweli, Herode na Pontio Pilato pamoja na Mataifa na watu wa Israeli, walikusanyika katika mji huu juu ya Mtumishi wako mtakatifu YESU, ULIYEMTIA MAFUTA,”
Lakini Tunaona matokeo ya damu ya Habili kumlilia Mungu kutoka katika ardhi ni ndugu yake Kaini kulaaniwa juu ya ardhi na kuwa mtu mtoro asiyekuwa na kikao….Kwahiyo kwa ufupi damu ya Habili ilinena hukumu juu ya Kaini juu ya nchi.
Lakini tukirudi kwa upande wa Yesu Kristo, tunaona matokeo ya Damu ya Yesu Kristo hayakuwa hukumu kwa wale waliomwua..Bali yalikuwa ni rehema na msamaha, na kuhesabiwa haki bure kwa Neema..Na ndio maana Bwana kabla hajakata roho alimaliza na Kusema “Baba wasamehe” kwakuwa hawajui watendalo…lakini Habili hakusema hivyo, na zaidi ya yote Bwana Yesu alisema “Imekwisha” lakini Habili hakusema hivyo…Kwahiyo damu ya Yesu ni Bora kuliko ya Habili, Damu ya Yesu imetuletea msamaha wa dhambi badala ya hukumu, Damu ya Yesu imetuletea Baraka badala ya Laana..Kwahiyo Inanena mema sana..
Kwa ufupi wale wote waliomsulibisha Bwana Yesu Kristo pale msalabani, pamoja na sisi sote tunaomsulibisha sasa Yesu Kristo kwa matendo yetu, tulistahili kulaaniwa juu ya ardhi kama alivyolaaniwa Kaini na hata zaidi ya pale, kwasababu tulimwua Mwana wa Mungu asiyekuwa na hatia…Lakini kwasababu Damu yake inanena mema kuliko ya Habili..tumepata rehema badala ya Hukumu, ardhi imebarikiwa kwa ajili yetu badala ya kulaaniwa..zaidi sana tumepewa tumaini la uzima wa milele Haleluya!.
Huo ni msamaha wa kipekee sana, Hakuna mwanadamu yoyote duniani leo ambaye mwanawe mpendwa auawe kikatili tena pasipo hatia, halafu badala ya kuwalipizia kisasi wale wauaji,na kuwalaani anawabariki kupitia mauti ya mwanae..Huo ni upendo usio kuwa na kipimo.
Damu ya Yesu ilimwagwa juu ya ardhi hapa duniani, miaka 2,000 iliyopita na si mbinguni..ili inene mema kwa wanadamu wa vizazi vyote vya duniani. Kwa kupitia damu ya Bwana isiyoharibika, mambo yote yanafanyika kuwa mapya, na kwa kupitia damu ya Bwana tunakikaribia kiti cha Neema kwa ujasiri.
Tukiyajua hayo, ni wakati wa kujichunguza na kuogopa, na kutetemeka kwasababu kama tulistahili kulaaniwa kama Kaini lakini Bwana hajatulaani, sio wakati tena wa kuidharau hii DAMU YA THAMANI YA YESU KRISTO, sio wakati wa kujisifu kuwa tunajua..Jambo ambalo watu wengi hawalifahamu ni kwamba Neema yote tunayoiona leo hii duniani ni kwasababu damu ya YESU bado inafanya kazi juu ya NCHI. Mvua tunazozipata kwa wakati ni kwasababu ya Damu ya thamani ya Yesu bado inafanya kazi, majanga tunayoepushwa nayo duniani ni kwasababu Damu ya Yesu bado inafanya kazi licha ya kwamba maasi ya sasa yamezidi yale ya Sodoma na Gomora lakini bado tunafaidika na neema hii kwa kitambo.,
tunavipindi vizuri vya usiku na mchana, na hewa safi ni kwasababu damu ya thamani ya Yesu ipo inayonena Mema.Unafuu wowote tunaouona duniani ni kwasababu ya Damu ya Yesu. Utafika wakati Hii damu itafikia mwisho wa kufanya kazi yake ya kunena na mambo mengine yatafunguliwa, kwasababu kumbuka sio wakati wote Mungu atakuwa anafanya kazi ya kuokoa, upo wakati wa mambo mengine kufunguliwa..hapo ndipo ile dhiki kuu itakapoanza…wakati huo hakuna mtu atakayeweza kununua wala kuuza pasipokuwa na chapa ya mnyama…wakati huo maji ya dunia nzima, na chemichemi zote zitakapogeuzwa kuwa damu, wakati huo ambao Jua litatiwa giza na nyota za mbinguni zitakapoanguka, wakati huo ambao gonjwa zito ya ajabu yataikumba dunia nzima,
Kipindi hicho sio cha kutamani kufika, ni kheri ujisalimishe Kwa Yesu Kristo leo kama hujafanya hivyo, kabla ya nyakati hizo, ukatubu na kubatizwa katika ubatizo sahihi wa maji mengi na Kwa jina la Yesu Kristo, upate ondoleo la dhambi zako, usiidharau hii Neema iliyopo leo na kufanya dhambi kwa makusudi, na kama ulikuwa hujasimama imara katika wokovu wako huu ni wakati wa kuweka mambo yako sawa..Biblia inasema katika..
Waebrania 10: 26 “Maana, kama tukifanya dhambi kusudi baada ya kuupokea ujuzi wa ile kweli, HAIBAKI TENA DHABIHU KWA AJILI YA DHAMBI;
27 bali kuna kuitazamia hukumu yenye kutisha, na ukali wa moto ulio tayari kuwala wao wapingao.
28 Mtu aliyeidharau sheria ya Musa hufa pasipo huruma, kwa neno la mashahidi wawili au watatu.
29 MWAONAJE? HAIKUMPASA ADHABU ILIYO KUBWA ZAIDI MTU YULE ALIYEMKANYAGA MWANA WA MUNGU, NA KUIHESABU DAMU YA AGANO ALIYOTAKASWA KWAYO KUWA NI KITU OVYO, NA KUMFANYIA JEURI ROHO WA NEEMA?
30 Maana twamjua yeye aliyesema, Kupatiliza kisasi ni juu yangu, mimi nitalipa. Na tena, Bwana atawahukumu watu wake.
31 NI JAMBO LA KUTISHA KUANGUKA KATIKA MIKONO YA MUNGU ALIYE HAI.”
Ndugu yangu/kaka yangu unayesoma haya ambaye ni mlevi, ni mwasherati, unafanya anasa, unakula rushwa, unatazama pornography, n.k mambo hayo yote ni njia panda ya kuelekea kuzimu,Dada unayesoma haya..unayevaa vimini na suruali, unayepaka lipstick na wanja, unayevaa hereni na wigi na unayesokota dread, unayesikiliza na kushabikia miziki na fashion za kidunia..mambo yote hayo kama hautaamua kuyaacha yatakupeleka kuzimu.
Mkabidhi Bwana leo maisha yako kikamilifu, pasipo kuwa vuguvugu..ili damu ile izidi kunena Mema juu yako.
Bwana akubariki sana.
Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine na Bwana atakubariki,
Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
JE!, INAKUBALIKA KUMTOLEA MTU MWENGINE DAMU?(BLOOD TRANSFUSION).
JE! ADAMU ALIWASALIANA NA MUNGU KWA LUGHA IPI PALE BUSTANINI?
Je! Umefunuliwa akili?..Baada ya Bwana Yesu kufufuka, tunasoma habari ya vijana wawili waliokuwa wanaenda kijiji kimoja kilichopo mbali kidogo na mji wa Yerusalemu, na walipokuwa njiani wakizungumza habari za kufufuka kwa Bwana biblia inatuambia Bwana wenyewe aliungana nao pasipo hata wao kujua, kwani macho yao yalifumbwa wasimtambue lakini baadaye mwisho wa safari yao walikuja kumtambua..tunasoma habari hiyo katika..
Luka 24.13 “Na tazama, siku ile ile watu wawili miongoni mwao walikuwa wakienda kijiji kimoja, jina lake Emau, kilichokuwa mbali na Yerusalemu kama mwendo wa saa mbili.
14 Nao walikuwa wakizungumza wao kwa wao habari za mambo hayo yote yaliyotukia.
15 IKAWA KATIKA KUZUNGUMZA NA KUULIZANA KWAO, YESU MWENYEWE ALIKARIBIA, AKAANDAMANA NAO.
16 Macho yao yakafumbwa wasimtambue.
17 Akawaambia, Ni maneno gani haya mnayosemezana hivi mnapotembea? Wakasimama wamekunja nyuso zao.
18 Akajibu mmoja wao, jina lake Kleopa, akamwambia, Je! Wewe peke yako u mgeni katika Yerusalemu, hata huyajui yaliyotukia humo siku hizi?
19 Akawauliza, Mambo gani? Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote;
20 tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha.
21 Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli. Zaidi ya hayo yote, leo ni siku ya tatu tangu yalipotendeka mambo hayo;
22 tena, wanawake kadha wa kadha wa kwetu walitushitusha, waliokwenda kaburini asubuhi na mapema,
23 wasiuone mwili wake; wakaja wakasema ya kwamba wametokewa na malaika waliosema kwamba yu hai.
24 Na wengine waliokuwa pamoja nasi walikwenda kaburini wakaona vivyo hivyo kama wale wanawake walivyosema, ila yeye hawakumwona.
25 Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii!
26 Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake?
27 Akaanza kutoka Musa na manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe.
28 Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, NAYE ALIFANYA KAMA ANATAKA KUENDELEA MBELE.
29 Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao.
30 Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa.
31 Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao.
32 Wakaambiana, Je! Mioyo yetu haikuwaka ndani yetu hapo alipokuwa akisema nasi njiani, na kutufunulia maandiko?”.
Wengi tunatamani Kristo atutokee siku moja, na kuanza kutembea nasi, ndipo tuamini Yupo na sisi, lakini hatujui kwamba Kristo yupo pamoja na sisi kila siku, akitufundisha na kutufunulia maandiko…kama Neno lake linavyosema “walipo wawili watatu wamekusanyika kwa jina langu, nami nipo papo hapo katikati yao.”…Unaona hapo kwa wakati huo Macho yetu ya mwilini yanakuwa yamefumbwa yasimwone lakini macho yetu ya rohoni yanamwona.
Ndicho kilichowatokea hawa watu wawili waliokuwa wanaenda Emau..Bwana alipojiunga katikati yao Macho yao ya mwilini yalifumbwa wasimtambue lakini macho yao ya rohoni yalikuwa yanamwona Bwana, alipokuwa anawafunulia maandiko kumhusu yeye.
Ni kwanini Bwana alijiunga nao? Ni kwasababu “tayari walikuwa wameshakusanyika wawili kwa jina lake, wakizungumza habari zake” ..hivyo Kristo lazima atimize Neno lake “la kuwepo katikati yao”.
Sasa maana ya kuwepo katikati yao sio kumwona sura yake hapana! Bali kumwona yeye katika Neno lake. Ndio maana wale watu wawili Bwana hakuwafumbua macho yao wamwone sura yake, bali alianza kwanza kuwafunulia maandiko wamwone yeye katika Neno lake.
Kwahiyo unaweza kuona Bwana havutiwi sana, na sisi kumwona yeye uso wake, bali anavutiwa sana na sisi kumwona yeye katika Neno lake. Ndio maana leo hatokei wengi, kwasababu anataka tumjue katika Neno lake, zaidi ya uso wake.
Ukiendelea kusoma habari za hawa vijana wawili, utagundua hata baada ya Bwana kumaliza kuwafunulia maandiko, hakutaka kuwafumbua macho ya mwili wamwone, badala yake utaona alitaka kuondoka kuwaacha katika hali ile ile ya kutomtambua, alitaka kuendelea mbele na safari yake, Ni kwanini alifanya vile? Ni kwasababu lengo lake halikuwa kuwaonyesha uso wake, bali lengo lake lilikuwa wamwelewe katika maandiko..Na baada ya kutimiza kusudi lake la kuwafunulia maandiko kazi ilikuwa imeshakwisha, alitaka kutengana nao… Lakini walipomshawishi sana ndipo akaamu kwenda kula nao, na huko ndio akawafumbua macho yao ya mwilini wamwone.
“28 Wakakikaribia kile kijiji walichokuwa wakienda, NAYE ALIFANYA KAMA ANATAKA KUENDELEA MBELE.
29 Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha. Akaingia ndani kukaa nao”.
Na ndio maana tunakuja kusoma pia Bwana alimkemea Tomaso kwa kutokumwamini…yeye alitaka auone uso wa Bwana na majeraha yake ndipo aamini, lakini Bwana hakutaka amwamini kwa njia hiyo..alitaka Tomaso amwamini kwa njia ya maandiko?..alitaka Tomaso amwamini kwa ufunuo wa maandiko, sio kwa kumwona uso..alitaka Tomaso amtambue yeye kwa kuyajua yaliyotabiriwa kumhusu yeye kuanzia kwa Musa, zaburi na kwa manabii wote, na hayo mengine yawe baadaye sana kama yana umuhimu.
Ndugu sura ya Yesu haiwezi kutufanya tumwamini yeye hata kidogo, kitakachotufanya tumwamini Bwana Yesu ni ufunuo katika Neno lake, ni kumtambua kupitia Neno lake, kumwona ametabiriwa wapi katika maandiko, na nafasi yake ni ipi katika Roho sasa.
Wanafunzi hata baada ya kumwona Bwana YESU uso wake,akiwa amefufuka hawakumwamini, walimtilia mashaka, walidhani wanaona mizimu..Na hata kama Bwana angewatokea mara 100 kama asingewafunulia akili zao wayaelewe maandiko wasingemwamini…wangeendelea kumtilia mashaka tu!..Tunaona mtu kama Yuda yeye sio kutokewa tu dakika chache halafu basi, hapana bali yeye aliishi, alikula, alilala na Yesu lakini mwisho wa siku akaja kumsaliti.
Luka 24.36 “Na walipokuwa katika kusema habari hiyo, yeye mwenyewe alisimama katikati yao, akawaambia, Amani iwe kwenu.
37 Wakashituka, wakaogopa sana, wakidhani ya kwamba wanaona roho.
38 Akawaambia, Mbona mnafadhaika? Na kwa nini mnaona shaka mioyoni mwenu?
39 Tazameni mikono yangu na miguu yangu, ya kuwa ni mimi mwenyewe. Nishikenishikeni, mwone; kwa kuwa roho haina mwili na mifupa kama mnavyoniona mimi kuwa nayo.
40 Na baada ya kusema hayo aliwaonyesha mikono yake na miguu yake.
41 Basi walipokuwa hawajaamini kwa furaha, huku wakistaajabu, aliwaambia, Mna chakula cho chote hapa?
42 Wakampa kipande cha samaki wa kuokwa.
43 Akakitwaa, akala mbele yao.
44 Kisha akawaambia, Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa nikali pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika Torati ya Musa, na katika Manabii na Zaburi.
45 NDIPO AKAWAFUNULIA AKILI ZAO WAPATE KUELEWA NA MAANDIKO.
46 Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu;
47 na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu”.
Je! na wewe leo amefunua akili zako, ili upate kuyaelewa maandiko??..ukiona huna hamu ndani yako ya kuyasoma maandiko, na hakuna msukumo wowote ndani yako wa kupenda kusoma Neno, mwombe Bwana leo hii akupe Neema…akupe hiyo nguvu, maana hawezi kukufunulia macho yako ya rohoni uyaelewe maandiko kama maandiko huyasomi… kuna hatari kubwa sana ya kukosa kulijua Neno la Mungu.. Kumbuka Kristo hakufungui macho uuone uso wake yeye, wala halitamani hilo…ingekuwa anataka tuuone uso wake, angeruhusu wakati ule picha yake ichorwe na iifadhiwe kwa vizazi vyetu hivi, kama neno lake limeweza kuhifadhiwa kwa vizazi vyote hivyo si zaidi picha? Ni kitu kidogo sana kuifanya picha yake ihifadhiwe kwa vizazi vyote lakini hakutaka… au angekuja kipindi hichi cha teknolojia ambapo kila mtu angeweza kumpiga picha na kuweka katika chumba chake cha ndani…Lakini hiyo sio njia anayoitumia ili sisi tumwamini yeye…yeye anataka tumwamini yeye, na tumjue, na tumfahamu sana kwa ufunuo wa Neno lake, biblia takatifu. Tukimtafuta katika nyuso tutamkosa hayupo huko…alimwambia Tomaso wana heri wale wasioona wakasadiki.
Je! na wewe ndugu unamtafuta Bwana leo kwa njia ipi? Kwa njia ya uso au maandiko?…Je Bwana amefunua akili zako uweze kumwona? Unasema unampenda Yesu wa kwenye picha au Yesu wa kwenye maandiko?..Na kama ni wa kwenye maandiko je! unayapenda maagizo yake yote aliyoyatoa?. Je! unajumuika na wengine wenye imani moja na wewe kwa maana alisema “wakusanyikapo wawili watatu kwa jina lake atakuwepo katikati yao”. Ni lazima tukusanyike kuanzia wawili na kuendelea ili Kristo, ajumuike pamoja nasi kutufunulia maandiko. Ni muhimu sana kuhudhuria bible study, au kukusanyika na mwenzetu kujifunza biblia kila iitwapo leo maadamu siku ile inakaribia, ndipo tutakapomwona Yesu.
Bwana akubariki sana.
Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine, Bwana akubariki.
Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP
Mada Nyinginezo:
JE! NI KWELI KUNA VIUMBE VINAVYOISHI SAYARI NYINGINE (ALIENS)?
Luka 8: 30 “Yesu akamwuliza, Jina lako nani? Akasema, Jina langu ni Jeshi; kwa sababu pepo wengi wamemwingia.
31 Wakamsihi asiwaamuru WATOKE KWENDA SHIMONI.
32 Basi, hapo palikuwa na kundi la nguruwe wengi wakilisha mlimani; wakamsihi awape ruhusa kuwaingia wale. Akawapa ruhusa.
33 Pepo wakamtoka mtu yule wakawaingia nguruwe, nalo kundi lilitelemka gengeni kwa kasi, wakaingia ziwani, wakafa maji”.
Shalom! Mtu wa Mungu, ni siku nyingine Bwana ametupa neema ya kuliona jua lake, sifa na utukufu ni vyake milele, karibu tujifunze pamoja maneno ya uzima ya Yesu Kristo Bwana wetu, leo tukilitazama kwa undani tukio hilo walilokutana nalo Yesu na wanafunzi wake, mara baada ya kuvuka bahari ya Galilaya pale walipokutana na Yule mtu mwenye jeshi la mapepo waliomsumbua sana kwa muda mrefu, lakini tunaona jambo la kwanza kabisa kama tunavyosoma wale mapepo walichofanya, ni kumsihi Bwana kwa nguvu asiwapeleke SHIMONI..Swali la kujiuliza hapo ni kwanini shimoni na sio sehemu nyingine, na huko shimoni ni wapi?.
Ni wazi kabisa kama tukichunguza mawazo ya hayo mapepo tunaona kuwa yalikuwa yanafahamu kabisa hilo eneo, lakini hayakuwepo kwa wakati huo , na ndio maana jambo la kwanza walipokutana tu na mtu anayewatambua vizuri na makao yao wastahiliyo kuwepo kwa wakati huo moja kwa moja waliona ni heri wajisalimishe na kuomba sharti ya amani mapema, kabla ya mambo mabaya kutokea ya kuamriwa kurudi Shimoni, waliona ni heri wapitie nusu shari kuliko shari kamili.
Mfano leo hii ukiona mtu mwenye akili timamu anachagua kwenda kuishi porini sehemu isiyo na huduma zozote za kijamii kuliko kuishi Mogadishu Somalia, utajua kuwa anazosababu zake za msingi kuchagua hivyo. Jambo la kwanza utajua aidha alishawahi kuishi katika mazingira yote mawili na kuona kule porini ni bora zaidi ya Mogadishu, au alishawahi kusikia habari za kule Mogadishu kwamba sio sehemu salama ya kuweka makazi ya kudumu kwa mtu yeyote kutokana na vita au vitendo vya kigaidi vinavyoendelea kutokea huko mara kwa mara, hivyo akaona bora achague mahali penye unafuu zaidi..
Hali Kadhalika na haya mapepo vivyo hivyo, yalifahamu kabisa hali halisi ya huko shimoni jinsi kulivyo, na ubaya wake, na shida zake na mateso yake, kutokana na kwamba aidha walishawahi kuwepo huko kwa kipindi Fulani au waliwaona wenzao wakiteseka katika makao hayo ya shida, na hivyo wao nao hawataki kwenda huko.
Biblia inasema.
2Petro 2: 4 “Kwa maana ikiwa Mungu hakuwaachilia malaika waliokosa, BALI ALIWATUPA SHIMONI, akawatia katika vifungo vya giza, walindwe hata ije hukumu”;
Unaona? Kama tunavyosoma hapo, makao ya malaika wote ambao hawakuilinda enzi yao, malaika wote ambao hawakuisimamia kweli, malaika wote ambao hawakudumu katika mipaka ya msingi waliyowekewa na Mungu, malaika wote waliokaidi kanuni za Mungu walizopewa waziendee walikuja kutupwa wote shimoni baadaye, katika vifungo vya giza wakae huko mpaka siku ile ya mwisho ya hukumu.
Kama tunavyofahamu mtu akitumbukia katika Shimo refu basi mtu huyo anakuwa katika hali ya mashaka na ya kukosa matumaini, kwasababu makao yake yatakuwa ni pale pale daima isipokuwa labda mtu amekuja kumtoa. Hivyo malaika wote walioasi makao yao yanapaswa yawe ni shimoni kwa sasa, kwenye vifungo vya milele wakingojea hukumu ya mwisho. Lakini pia si wote walio humo kwasasa biblia inasema hivyo, wapo baadhi wanaozunguka zunguka duniani pamoja na mfalme wao ibilisi, Sababu za Mungu kuwaruhusu wao wawe hivyo hatujui Bwana anazijua, lakini wakati utafika Shetani naye atatupwa katika shimo hilo kwa muda wa miaka 1000 akiungana na wale waliokuwa wamefungwa tangu zamani, kisha baadaye ataachiliwa kwa muda mfupi kwa kutimiza kusudi Fulani duniani. Na baada ya hapo ndipo kwa pamoja watatupwa wote kwenye lile ziwa la moto.
Ufunuo 20:1” Kisha nikaona malaika akishuka kutoka mbinguni, mwenye ufunguo wa kuzimu, na mnyororo mkubwa mkononi mwake.
2 Akamshika yule joka, yule nyoka wa zamani, ambaye ni Ibilisi na Shetani, akamfunga miaka elfu;
3 akamtupa katika kuzimu, akamfunga, akatia muhuri juu yake, asipate kuwadanganya mataifa tena, hata ile miaka elfu itimie; na baada ya hayo yapasa afunguliwe muda mchache”.
KAMA KUNA BAADHI YA MAPEPO AMBAYO HAYAPO SHIMONI KWA SASA, BASI MAKAO YAO YAKO NI WAPI ?
Hakuna pepo lolote lenye makao ya kustarehe duniani, hakuna mahali popote pepo anapata unafuu isipokuwa ndani ya mtu tu! basi. Nje ya hapo, ni dhiki kubwa na mateso. Na ndio maana wanafanya bidii sana kila mmoja walau apate mahali pa kujiegesha ndani ya mtu duniani. Sasa mara baada ya pepo kumtoka mtu baada ya kuombewa au baada ya mtu kumpa Kristo maisha yake haliendi kustarehe mahali Fulani tu, hapana linakwenda mahali pa jangwa, mahali penye ukame. Bwana Yesu alisema hivi.
Mathayo 12:.43 “Pepo mchafu, amtokapo mtu, HUPITIA MAHALI PASIPO MAJI, akitafuta mahali pa kupumzika, asipate.
44 Halafu husema, Nitarudi nyumbani kwangu nilikotoka; hata akija, aiona tupu, imefagiwa, na kupambwa.
45 Mara huenda, akachukua pamoja naye pepo wengine saba walio waovu kuliko yeye mwenyewe, nao huingia na kukaa humo; na mtu yule hali yake ya mwisho huwa mbaya kuliko ya kwanza. Ndivyo itakavyokuwa kwa kizazi hiki kilicho kibaya”.
Unaona hapo linakwenda mahali pasipo maji ni sawa na kusema linakwenda mahali pa jangwa pasipo na uhai, mahali pa shida na dhiki pasipo kuwa na kiburudisho chochote. Sasa pepo linapomtoka mtu ndipo katika roho linakuwa katika hali kama hiyo ya mtu aliyeachwa jangwani mwenyewe pasipo na msaada wowote. Kumbuka Hapo ni tofauti na shimoni, na kwa jinsi atakavyoendelea kukosa mahali pa kutulia ndivyo hali yake itakavyozidi kuwa mbaya zaidi, sawasawa tu na wale walioko shimoni. Ataendelea hivyo hivyo mpaka siku ile ya mwisho ya Hukumu ambayo wote kwa pamoja na wale walio vifungoni kwenye mashimo sasahivi watakapotupwa kwenye lile ziwa la moto.
Hivyo unaweza ukuona ni shida nyingi kiasi gani hivi viumbe vilivyolaaniwa vinapitia vinapokosa mahali pa kustarehe, lakini sasa pale mtu anapovipa makao katika mwili wake, mtu huyo naye anafanyika kuwa mwana wa laana, Mungu anamwona mtu kama huyo naye anastahili kutupwa shimoni. Naye pia anashiriki laana zile zile walizowekewa hayo mapepo tangu zamani.
Na ndio hapo sasa mtu mwovu akifa, pindi tu anapokata roho moja kwa moja anajikuta anashuka kwenye shimo refu la giza, kwenye vifungo vya milele sasa huko chini kuna taabu na mateso yasiyoneneka Mahali ambapo baadhi ya hayo mapepo yalipo sasahivi, mateso ya huko ni makubwa jaribu kifikiria hata mapepo yaliyopo duniani hayataki kupelekwa huko, ni mahali pabaya kiasi gani.
Sasa wote kwa pamoja wataendelea kukaa huko wakisubiria hukumu ya siku ile ya mwisho kisha watupwe kwenye lile ziwa la moto. Hayo ndio mambo yaliyowakuta hata watu wa kipindi cha Nuhu na watu wa kipindi cha Sodoma na Gomora biblia inasema sasahivi wapo katika vifungo hivyo vya milele, wapo shimoni wakingojea hukumu ya mwisho na ndipo wahukumiwe na kutupwa kwenye lile ziwa la moto.
Yuda 1:6 “Na malaika wasioilinda enzi yao wenyewe, lakini wakayaacha makao yao yaliyowahusu, amewaweka katika vifungo vya milele chini ya giza kwa hukumu ya siku ile kuu.
7 Kama vile Sodoma na Gomora na miji iliyokuwa kando-kando, waliofuata uasherati kwa jinsi moja na hawa, wakaenda kufuata mambo ya mwili yasiyo ya asili, imewekwa kuwa dalili, wakiadhibiwa katika moto wa milele”.
2Petro 2: 4 “Kwa maana ikiwa Mungu hakuwaachilia malaika waliokosa, bali aliwatupa shimoni, akawatia katika vifungo vya giza, walindwe hata ije hukumu;
5 wala hakuuachilia ulimwengu wa kale, bali alimhifadhi Nuhu, mjumbe wa haki, na watu wengine saba, hapo alipoleta Gharika juu ya ulimwengu wa wasiomcha Mungu;
6 tena akaihukumu miji ya Sodoma na Gomora, akiipindua na kuifanya majivu, akaifanya iwe ishara kwa watu watakaokuwa hawamchi Mungu baada ya haya;”
Unaona hapo? Kuna hatari nyingi sana leo hii tukiifanya miili yetu kuwa makao ya mashetani, mtu yeyote ambaye bado hajasafishwa kwa damu ya YESU KRISTO na kupata ondoleo la dhambi zake na kubatizwa ipasavyo na kupokea Roho Mtakatifu, basi mtu huyo yeye ni makao na kimbilio la roho chafu za mashetani zilizoasi.. Mtu yeyote ambaye ni mwasherati na mzinzi basi yeye ni hifadhi wa makao ya mapepo, mtu yeyote ambaye ni mwabudu sanamu, kadhalika yeye naye ni makao ya mapepo, mtu yoyote aliye mshirikiana na mchawi, na anayejihusisha na masuala ya waganga wa kienyeji, mwili wake ni makao ya mapepo wachafu..mwanamke yeyote ambaye anavaa nguo za uchi, na vimini na suruali basi huyo ni makao ya mapepo. Na akiendelea hivyo hivyo mpaka siku atakapokufa naye moja kwa moja atajikuta kwenye vifungo vya shimo hilo la kuzimu pamoja na watu wa sodoma na gomora na watu wa kipindi cha Nuhu pamoja na yale mapepo wakisubiria hukumu ya siku ya mwisho. Kisha wakatupwe kwenye lile ziwa la moto.
Zamani katika agano la kale mtu mwenye pepo hukumu yake ilikuwa ni kifo.
Walawi 20: 26 “Nanyi mtakuwa watakatifu kwangu mimi; kwa kuwa mimi Bwana ni mtakatifu nami nimewatenga ninyi na mataifa, ili kwamba mwe wangu.
27 TENA MTU MUME AU MTU MKE ALIYE NA PEPO, au aliye mchawi, hakika atauawa; watawapiga kwa mawe; damu yao itakuwa juu yao”.
Tukiyajua hayo, na tukifahamu kuwa shetani na mapepo yake yanazunguka kila siku duniani yakitafuta hifadhi ndani ya wanadamu. Basi tutaishi maisha ya kujichunga kila siku. Tutazijaribu hizi roho zote zinazokuja mbele yetu na mafundisho yake ya uongo. Tutaishi maisha ya uangalifu huku tukimruhusu Roho Mtakatifu achukue sehemu yote ya maisha yetu.
Bwana akubariki.
Tafadhali “share” kwa wengine ujumbe huu. Na Mungu atakubariki.
Mada Nyinginezo:
NABII ELISHA ALIKUWA ANA MAANA GANI KULIA NA KUSEMA”GARI LA ISRAELI NA WAPANDA FARASI WAKE”?
2 Wakorintho 6:14 “Msifungiwe nira pamoja na wasioamini, KWA JINSI ISIVYO SAWASAWA; kwa maana pana urafiki gani kati ya haki na uasi? Tena pana shirika gani kati ya nuru na giza?”
Biblia inasema tusifungiwe Nira pamoja na wasioamini..NIRA ni KIFAA kinachowekwa katikati ya wanyama wawili wa jamii moja, kinachowafunga pamoja…ili kutimiza kusudi la kazi Fulani, kama vile kulima, kusafirisha mizigo n.k mfano ng’ombe wawili wanaweza kufungwa nira pamoja kwa kazi ya kilimo, na kulivuta lile jembe nyuma yao…kadhalika farasi wawili wanaweza kufungwa nira moja ili kulivuta gari la kubebea watu au vitu nyuma yao..Punda nao wanaweza kufungwa nira pamoja ili kusaidia kuvuta mzigo Fulani nyuma yao…
Tukirudi katika maandiko biblia inatuonya tusifungwe nira pamoja na wasioamini, Kumbuka haikumaanisha tukae mbali kabisa na wasioamini, au tusizungumze nao, au tusifanye nao kazi, au tusiishi nao, au tusisome nao au tusile nao, au tusisalimiane nao…hapana haikumaanisha hivyo… ukisoma kwa makini huo mstari unasema “msifungiwe nira pamoja na wasioamini kwa jinsi isivyo sawasawa”..Sasa zingatia hilo neno “kwa jinsi isivyo sawasawa”… Ikiwa na maana kuwa kumbe kuna jinsi iliyo sawasawa ambayo tunaweza tukafungwa nao nira, unaweza ukafanya kazi ofisi moja na mtu asiyeamini, unaweza ukasoma darasa moja na mtu asiyeamini, unaweza ukala sahani moja ya chakula na mtu asiyeamini kama Bwana alivyofanya n.k…Lakini kuna mipaka ambayo hatupaswi kufungiwa nao Nira.
Kwa mfano, mtu asiyeamini anaweza akawa ni mwizi, au mwasherati, au mtukanaji sasa kama ni shuleni tunaweza tukawa naye darasa moja, tukazungumza naye kwa upendo na kujaribu kumvuta kwa KRISTO lakini, kukaa naye katika mazingira yake ya utukanaji, au ya uasherati, au ya wizi au ya usengenyaji hayo tumeonywa tujiepushe nao…kushirikiana naye katika anasa, au ulevi hivyo vyote tumeonywa tukae mbali navyo..tukiwa shuleni tutashirikiana nao katika masuala ya shuleni tu basi, lakini masuala ya kwenda disko, au kwenye starehe za kidunia, au kutazama picha chafu, au kufanya nao mustarbation hayo tumeonywa..vivyo hivyo kazini tutashikamana nao kwa masuala ya kazini tu basi..lakini katika eneo la maisha ya rohoni hilo tumeonya tujiepushe nao.
Sasa kwanini Bwana alituonya tusijifunge Nira nao kwa jinsi isivyopaswa?.
Kwani tukiishi nao hivyo hivyo kuna shida gani??..si tutajiepusha nao tu!!
Hekima ya Mungu ni kuu kuliko hekima ya mwanadamu… Umewahi kujiuliza kwanini watu wa ukanda Fulani wana lafudhi zinazofanana? Au wana tabia zinazofanana?..Unadhani wote walipenda wawe wanalafudhi zinazofanana? Au walishauriana wawe vile?..Utakuja kugundua kwamba ni “kule kukaa pamoja kwa muda mrefu” ndiko kuliko wafanya wote wafanane tabia na lafudhi bila hata wenyewe kujijua kuwa wapo hivyo.
Kwahiyo unaweza ukaona kuwa kuna nguvu Fulani ya kumbadilisha mtu ipo katika ya jamii anayojiunganisha nayo..hata kama yeye hataki lakini kwa jinsi anavyokaa na ile jamii atajikuta tu kwa muda Fulani ameshafanana na jamii ya wale watu kiusemi, na kifikra.
Ndio maana katika agano la kale Bwana alitoa maagizo punda na ng’ombe wasifungwe nira pamoja…punda afungwe na punda mwenzake na ng’ombe afungwe na ng’ombe mwenzake… Kumbukumbu 22: 10 “Usilime kwa ng’ombe na punda wakikokota jembe pamoja”.
Sababu ni kwamba watakapofungwa nira pamoja punda na ng’ombe..kuna tabia ng’ombe alizo nazo punda atakazoanza kuziiga na kadhalika kuna baadhi ya tabia za punda ng’ombe ataziiiga hivyo itazaliwa tabia moja ambayo haifai katika shughuli zozote za kazi..
Fuatilia utaona kuwa mahali palipo na mchanganyiko wa kuku na bata, utaona bata kuna wakati wanaonyesha tabia Fulani kama za kuku na kuku vivyo hivyo kuna wakati wanaonyesha tabia kama za Bata..Mimi nimewahi kushuhudia hilo na pia kitafiti limethibitishwa…Pia kwa wanyama wengine wote ndio hivyo hivyo, wakichanganyikana pamoja wanakuwa wanaingiliana tabia…
Hivyo ndivyo Bwana alivyoviumba viumbe vyake vyote ikiwemo wanadamu kwamba…tabia ya mmoja inaweza kumuathiri na kumgeuza mwingine endapo wakikaa pamoja kwa muda mrefu.
Ndio maana maandiko yanazidi kusema katika ..
Mithali 22: 24 “Usifanye urafiki na mtu mwenye hasira nyingi; Wala usiende na mtu wa ghadhabu nyingi; .. USIJE UKAJIFUNZA NJIA ZAKE; NA KUJIPATIA NAFSI YAKO MTEGO”.
Unaona hapo?..inasema usije ukajifunza njia zake? HIYO KUJIFUNZA sio kujifunza kwa kutaka hapana! Hakuna mtu yoyote anapenda kujifunza njia mbaya…hiyo kujifunza ni tabia ambayo inaingia ndani ya mtu pasipo hata yeye kujijua, kama alikuwa sio msengenyaji na akakaa na mtu ambaye ana tabia ya kuzungumzia habari za watu wengine kila wakati..na yeye baada ya muda Fulani atajikuta tu anaanza anazungumzia habari za wengine kila mahali…
Kama alikuwa hana hasira nyingi lakini akajiunganisha na mtu wa hasira nyingi na anaye kufoka foka..mara ya kwanza ataishangaa ile tabia lakini baada ya muda Fulani, ataona ile hali ni ya kawaida tu! Kutukana na kukasirika ni kawaida…hivyo na yeye atakapoudhiwa kidogo tu hasira zitamjia na kuanza kufoka na kutukana kama mwenzake anavyofanya, kwasababu moyo wake ulishakufa ganzi siku nyingi..Hata mara ya kwanza ukipita mahali penye kelele nyingi na harufu nyingi tofauti tofauti siku ya kwanza utaona kuna usumbufu mkubwa na harufu nyingi lakini kwa jinsi utakavyoendelea kupita hapo kila siku, unakuja kuona ile sehemu ni ya kawaida tu! Unapazoea!! Harufu zinapotea na kelee huzioni tena kuwa ni nyingi..Watu wanaoishi machinjioni ukiwauliza hivi huwa hamwisikii hiyo harufu mbaya ya damu, watakujibu hawasikii kitu wanaona kawaida tu! Ni kwasababu gani ni kwasababu wameshakufa ganzi katika yale mazingira.
Kwahiyo ni kujihadhari kama Bwana anavyotuonya..Yeye ndiye aliyetuumba sisi, ana hekima kuliko sisi, unajua madhaifu yetu yapo wapi, na ndio anatuambia “tusifungwe nira pamoja nao kwa jinsi isivyopaswa” Kinyume chake tujifunge nira na wanaoamini, maana hao nao watatuambukiza tabia zao njema zinazompendeza Mungu..ndio maana Bwana alipowatuma wanafunzi wake aliwatuma wawili wawili..kuonyesha kwamba Bwana anatufunga nira yake kuanzia wawili na kuendelea? Kwasababu na yeye Bwana anayo Nira yake, anayotufunga sisi watoto wake pamoja, lakini anasema Nira yake ni laini na mzigo wake ni mwepesi..Maagizo yake sio mazito tunapokuwa wawili au watatu kwa jina lake, tunakuwa tuna uwezo wa kushinda kwasababu tumefungwa nira yake pamoja.
Ni matumaini yangu, kuanzia leo utaangalia mazingira yanayokuzunguka, na watu unaojishughulisha nao, je! ni kwa mambo ya maana tu, au wanaingilia mpaka utaratibu wako wako Imani. TUJILINDE!
Bwana akubariki.
Tafadhali tangaza habari njema za ufalme popote ulipo, kama umeshampa Bwana maisha yako, na pia kama hujamkabidhi Bwana maisha yako, ni vyema ukafanya hivyo leo kabla nyakati za hatari hazijaanza, maana tunaishi katika kipindi cha siku za mwisho, ambacho Bwana yupo karibu sana kurudi.
Mada Nyinginezo:
JE! TUNARUHUSIWA KUMUOMBEA MTU AMBAYE HAWEKI BAYANA KILE ANACHOHITAJI KUOMBEWA?
KUWAHUDUMIA MALAIKA PASIPO KUJUA.
VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 6
Mathayo 10:16 “Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua.”
Sentensi hiyo imekuwa ikiwatatiza wengi, wakijiuliza ni kwanini Bwana YESU alisema maneno kama hayo: IWENI NA BUSARA KAMA NYOKA. Kwani nyoka anayobusara gani, kwanini hapo asingesema iweni na busara kama simba au mnyama mwingine wa mwituni na sio nyoka?. Tunafahamu katika biblia nyoka ni mnyama aliyepoteza sifa kuliko wanyama wote aliowaumba Mungu, kadhalika ni mnyama aliyelaaniwa kuliko wanyama wote, katika biblia mnyama anayefananishwa na shetani ni nyoka peke yake, tofauti na wanyama wengine kama njiwa ambaye anaonekana akimwakilisha Roho Mtakatifu na wanyama wengine kama kondoo, ng’ombe, na simba lakini nyoka hastahili hata kutamkwa kwenye vinywa vya wakristo kwa sifa njema lakini hapa Bwana kamtaja.
Na zaidi ya yote Bwana wetu YESU anatuonya na kutumbia; basi iweni na busara kama nyoka, Leo hii tutafunza ni busara gani nyoka aliyokuwa nayo.
Awali ya yote ukisoma kuanzia ule mstari wa 1 utaona kuwa maneno hayo Bwana Yesu alikuwa anawaambia wale wanafunzi wake 12. Muda huo alikuwa anawapa maagizo ya msingi ya kuzingatia katika kwenda kufanya kazi ya utumishi. Ni mahusia ya msingi kabisa ambayo walipaswa wazingatie na sio tu katika kile kipindi walichokuwa na Bwana Yesu pindi walipotumwa bali pia hata baada ya kuondoka kwake. Na ndio hapo tunakuja kusoma huo mstari wa 16, akiwaambia maneno hayo akisema: “Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu;”.. Umeona hapo? Mpaka hapo tumeshafahamu kuwa maneno hayo yanawahusu wale tu WANAOTUMWA!, na si watu wengine.
Sasa hao ndio walioambiwa katika kutumwa kwao wanapaswa wawe na tabia kama kondoo katikati ya mbwa-mwitu, na sio kama simba katikati ya mbwa-mwitu, hii ikiwa na maana kuwa watakapotendewa mabaya au watakapopigwa au watakapoudhiwa wasirudishe baya kwa baya, bali wajifanye kama kondoo wasioweza kufanya lolote. Bwana alikuwa anayomaana ya msingi kabisa kuwaambia hivyo, kwasababu alijua umuhimu wake katika kuziokoa roho za watu. na ndio tabia tuliokuja kuiona kwanza kwa Bwana wetu YESU Kristo kisha kwa mitume wake baadaye..Sasa baada ya hapo, ndipo akawapa maagizo haya kwamba huko mtakapokwenda IWENI NA BUSARA KAMA NYOKA. NA KUWA WATU WAPOLE KAMA HUA.
Ni busara gani aliyonayo NYOKA?
Nyoka anavyozungumziwa hapa ni nyoka jinsi alivyokuwa katika asili yake pale Edeni.Embu jaribu kifikira Adamu na Hawa watu ambao Mungu alikuwa anazungumza nao uso kwa uso wakiisikia sauti yake kila siku kwa kipindi cha muda kirefu sana, wakiyatimiza maagizo yake yote aliyowapa kwa muda mrefu kwamba wasile matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya, halafu kirahisi rahisi tu ndani ya siku moja wakate shauri waache kuyatii maagizo ya Mungu na kuasi..Usidhani ni jambo jepesi jepesi kufikia hatua ya kula lile tunda, ushawishi wa namna hiyo unahitaji maarifa na busara ya hali ya juu sana..
Nyoka alijua kabisa ili kuwapata wale watu sipaswi kutumia nguvu ya aina yoyote, kama angejaribu kufanya hivyo basi yeye mwenyewe angejikuta kwenye hali mbaya sana kwasababu Adamu asingemvumilia. Alijua kabisa hapaswi kutumia maneno ya kufuru kwa Mungu wao, kama angefanya hivyo basi Adamu asingemvumilia pia kwa hilo, alijua kabisa kuzungumza na Adamu ni ngumu hivyo akatafuta njia mbadala mahali palipo dhaifu ili afanikishe mpango wake wa kuwadondosha. Alitumia busara nyingi kuupindua mpango wa Mungu uliokuwa ndani ya wanadamu. Hivyo japo aliruhusu busara yake itumiwe vibaya na shetani lakini bado mbele za Mungu alionekana kuwa ni mnyama mwenye busara nyingi..
Hata baada ya kulaaniwa, unamwona katika mawindo yake, hatumii papara, huwa unatulia sana, na kukamata mawindo yake kwa ghafla, hana mikono, hana miguu, lakini anamkamata panya mwenye uwezo mkubwa wa kusikia, na kuponyoka.
Unaukumbuka ule mfano Bwana alioutoa katika Luka 16:1-9, wa Yule wakili aliyekuwa mwizi, lakini katika wizi wake alikuwa na busara?…Kama hukuwahi kuupitia basi kaupitie tena, naamini utajifunza kitu.
Vivyo hivyo na wale wanaotumwa na Bwana kupeleka injili, Bwana YESU anawaambia IWENI NA BUSARA KAMA NYOKA. Alimaanisha kuwa huko waendako watakutana na watu waliojikita katika misingi ya imani zao potofu, hata ufanyeje huwezi kuwang’oa mahali walipo..Shetani ameshawahubiria kwa miaka mingi, kwamba akitokea mtu mwingine anawaletea habari za Imani nyingine zaidi ya hiyo waliyofundishwa hawawezi kuwaamini wala kuwapokea. Hivyo kama huyo anayetumwa kupeleka Injili hataweza kutumia busara kuwahubiria habari mpya ya wokovu katika Kristo Yesu basi anaweza kujikuta anampoteza kondoo Yule au anajitafutia matatizo yeye mwenyewe yasiyo ya lazima.
Leo inasikitisha kuona mtu anasema ni mtumishi wa Kristo na ni mhubiri lakini mambo anayoyafundisha kwa watu ambao wapo katika misingi ya imani nyingine mbali na Kristo, haina busara kabisa..Utamkuta anakutana na mtu labda pengine haamini katika kula nyama ya nguruwe. Lakini yeye kwasababu anajua kuwa nguruwe si kitu mbele za Mungu, badala ya kumfundisha mambo ya msingi, halafu kwa jinsi atakavyoendelea kukua kiiamini baadaye ndipo amwambie na habari hizo pia, jambo la kwanza ataanza kwa kumwambia nguruwe si dhambi!, ataanza kuwaambia dini yenu ni ya kigaidi, ataanza kuwaambia mnaabudu majini n.k. Unadhani itakuwa ni rahisi kumvuta huyo mtu kwa Kristo? Jibu ni hapana Kinyume chake utazua migongano na malumbano na kusababisha jina la Mungu kutukanwa.
Mtume Paulo katika safari yake ya kutangaza injili alikutana na watu wengi tofauti tofauti, lakini alifanikiwa kuwageuza wengi wao kwa busara ya Roho iliyokuwa ndani yake. Tunasoma hayo katika
1Wakorintho 9: 20 “Nalikuwa kama Myahudi kwa Wayahudi, ili niwapate Wayahudi; kwa wale walio chini ya sheria, nalikuwa kama chini ya sheria, (ingawa mimi mwenyewe si chini ya sheria), ili niwapate walio chini ya sheria.
21 Kwa wale wasio na sheria nalikuwa kama sina sheria, (si kwamba sina sheria mbele za Mungu, bali mwenye sheria mbele za Kristo), ili niwapate hao wasio na sheria.
22 Kwa wanyonge nalikuwa mnyonge, ili niwapate wanyonge. Nimekuwa hali zote kwa watu wote, ili kwa njia zote nipate kuwaokoa watu.
23 Nami nafanya mambo yote kwa ajili ya Injili ili kuishiriki pamoja na wengine”.
Wakolosai 4:5 “Enendeni kwa hekima mbele yao walio nje, mkiukomboa wakati.
6 Maneno yenu yawe na neema siku zote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.
Unaona hapo?. Tukikosa busara, tutazua mashindano ya dini badala ya wokovu kwa watu. wengine wanapotukanwa tu kidogo wao nao wanarudisha matusi, hawajui kuwa wale ni mbwa-mwitu ni kawaida yao kutukana, sasa na wao kwa kukosa busara wanarudisha na wao dhihaka, sasa hapo ni mtu gani unatazamia aupokee wokovu?. Matokeo yake badala ulete faida katika ufalme wa mbinguni unaleta hasara kwa jambo dogo tu la kukosa busara.
Upo mitandaoni, badala ya kuwavutia watu Kristo wampokee ndani yao, unakwenda kutafuta sehemu za madhaifu yao na kuanza kuwakasirisha kwa maneno ya hasira, hujui kuwa ipo siku utaulizwa na Bwana kwa hiyo huduma unayoifanya: Sisemi kuwa hupaswi kukosoa mabaya, lakini katika ukosoaji wako tumia busara. Angalia mwisho wa siku unamshawishi nani?. Au malengo yako ni nini? kukoa au kuonyesha kuwa wale hawako sahihi na wewe upo sahihi?. Jichunguze lengo lako ni nini? kujenga au kutaka kuonyesha kuwa una ujuzi mwingi?..Biblia inasema upendo hujenga, bali ujuzi huleta majivuno (1 Wakoritho 8:1)
Luka 12:42 “Bwana akasema, Ni nani, basi, aliye wakili mwaminifu, MWENYE BUSARA, ambaye bwana wake atamweka juu ya utumishi wake wote, awape watu posho kwa wakati wake?
43 Heri mtumwa yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta anafanya hivyo.
44 Kweli nawaambia, atamweka juu ya vitu vyake vyote.
45 Lakini, mtumwa yule akisema moyoni mwake, Bwana wangu anakawia kuja, akaanza kuwapiga wajoli wake, wanaume kwa wanawake, akila na kunywa na kulewa;
46 bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wasioamini.”
Unaona?. Ni maombi yangu kwa kusoma haya sisi sote hatutaanza kuwa mawakili wenye busara wa Kristo, ambao tutawapa posho wale walio nje kwa wakati, na sio kuwapiga, na kuwaudhi, na kuwadharau ili Bwana atakapokuja atupe thawabu iliyostahili, na tufanikiwe kuleta matunda mengi kwa Bwana.
Ubarikiwe sana.
Tafadhali “share” ujumbe huu kwa wengine na Bwana atakubariki.
Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp
Mada Nyinginezo:
BWANA ALIMAANISHA NINI ALIPOSEMA″ HAKUNA MTU ASHONAYE KIRAKA CHA NGUO MPYA KATIKA VAZI KUKUU?
NITASHINDAJE HALI YA KUUMIZWA NA MANENO YA WATU!