Category Archive Wazazi na Watoto

Fahamu Mithali 20:11 Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake;

SWALI: Nini maana ya Mithali 20:11 inaposema;

Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; Kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili.


JIBU:  Mwandishi anatuonyesha kuwa tabia ya mwanadamu yoyote, huwa haijifichi kufuatana na umri wake, kwamba yaweza kukaa ndani  tu kipindi cha utotoni isionekane ikaja kudhihirika ghafla ukubwani. Hapana, anasema “Hata mtoto hujijulisha kwa matendo yake; Kwamba kazi yake ni safi, kwamba ni adili”.

Ikiwa na maana katika utoto ule ule unaweza kuuchunguza mwenendo wa mtoto, ukautambua. Na hiyo itakupa fursa ya kuurekebisha ukiwa ni mbaya, au kuuimarisha ukiwa ni mzuri, akiwa katika vipindi kile kile. Usione mwanao anayotabia ya udokozi, ukasema huyu ni mtoto tu, haelewi anachokifanya. Hapana unapaswa umrekebishe mapema, kwasababu hicho kitu kipo ndani yake, Ukiona mtoto anapenda kutazama biblia, anapenda kukaa kanisani, anapenda kusikiliza nyimbo za injili. Usiseme, huyu ni mtoto, ukampuuzia tu, kwa kuishia  kusema ‘ubarikiwe mwanangu’ kinyume chake, mwendelezee mazingira hayo, kwasababu mwelekeo wa maisha yake, ni huko.

Ndivyo ilivyokuwa kwa Bwana wetu Yesu Kristo, tabia zake zilianza kuonekana tangu utotoni, wazazi wake walimstaajabia, kumwona  katika umri ule mdogo, yupo hekaluni, amekaa na waalimu na wakuu wa dini akiwauliza maswali, Kinyume chake wazazi wake hawakumkemea, bali waliyaweka yote mioyoni mwao, na kukubali kuutambua mwelekeo wa mtoto wao.

Hii ni kufundisha nini? 

Lipo funzo la rohoni, lakini pia la mwilini.

La mwilini ni kuwa yatupaswa tuwatazame watoto, bila kupuuzia kitendo chochote wanachokidhihirisha katika umri ule wa chini. Ikiwa ni chema tukipalilie, ikiwa ni kibaya, tukikemee, na kushughulika nacho kwelikweli kabla hakijaweka mizizi. Hivyo hakuna mzazi au mlezi anaweza kusema, huyu mwanangu kabadilika tu ghafla. Ukweli ni kwamba mabadiliko yalianza kuwepo tangu zamani, isipokuwa kwa namna moja au nyingine tulipuuzia, tulipoyaona ndani yao tukadhani ni tabia za utoto tu. Wazazi wanaowajenga wanao katika maadili na vipawa tangu utotoni, ukiwatazama watoto wao wanapokuwa watu wazima, huwa wanakuwa na ufanisi na ujuzi wa hali ya juu sana, zaidi ya wale ambao watajijengea wenyewe wanapokuwa watu wazima. Hivyo mzazi jali maisha ya kiroho ya mwanao.

Vilevile rohoni, wapo ambao ni wachanga kiroho. Ikiwa na maana katika kanisa ni wale ambao wameokoka hivi karibuni. Halikadhalika hawa nao utaweza kutambua karama zao, sio mpaka wawe wakomavu kiroho. Aliye Mwinjilisti, utaona anapenda kushuhudia, lakini pia anauwezo wa kuwavuta wengine kwa Bwana.  Aliye mwalimu, utaona anapenda sana kujifunza, aliye nabii, utaona karama za maono, ndoto, huwa zinamjia mara kwa mara, hata kwa namna ambazo hazielewi elewi, mwimbaji atapenda wakati mwingi kujifunza kuimba hata kama hawezi. Hivyo, kila mmoja wetu, kitu ambacho Mungu amekiweka ndani yake, hujidhihirisha mapema sana pindi ameokoka. Sio mpaka awe amekomaa sana kiroho kama wengi wanavyodhani.

Pindi unapookoka, kipindi hicho hicho karama yako inaanza kufanya kazi, unapachopaswa tu, ni kujishughulisha na utumishi wa Bwana, ndivyo utakavyoruhusu mambo hayo kutokea kwa wepesi na urahisi zaidi?

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine

MZAZI, JALI MAISHA YA KIROHO YA MTOTO WAKO.

(TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

Uasherati wa Kiroho maana yake nini?(Opens in a new browser tab)(Opens in a new browser tab)

MAANA WEWE, BWANA HUKUWAACHA WAKUTAFUTAO”.(Opens in a new browser tab)

Rudi nyumbani

Print this post

BARAKA ZA WAZAZI KWA WATOTO.

Masomo maalumu kwa wazazi/walezi.

Je unazijua kanuni za kuwabariki watoto wako?.. Wengi tunaijua kanuni moja tu ya kuwatamkia Baraka!..Hiyo ni sahihi kabisa na ipo kibiblia..(kwasababu maneno ya kinywa yana nguvu).

Lakini ni vizuri kufahamu jambo moja, kama Maneno yako hayataambatana na matendo yako, uwezekano wa hayo uliyoyasema kutokea bado utakuwa ni mdogo sana.

Kama unataka mtoto wako apate Baraka zote ulizozitamka juu yake, (na kwa njia ya maombi) ikiwemo Baraka katika kumjua Mungu, kuwa na afya na mafanikio, basi ongezea yafuatayo..

   1.MFUNDISHE SHERIA ZA MUNGU.

Wafundishe watoto wako sheria za Mungu, huku wewe mwenyewe ukiwa kielelezo cha kuzifanya, ili wasione kama ni sheria tu za MUNGU bali hata zako wewe mzazi!.. Mtoto wako anapaswa azione sheria za Mungu kama ni za kwako wewe. Lakini asipoona wewe mwenyewe ukizifanya hata yeye hataweza kukusikiliza wala kuzitenda, hata kama kwa mdomo atakuitikia.

Mithali 1:8 “Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, Wala usiiache sheria ya mama yako,

9 Kwa maana hayo yatakuwa kilemba cha neema kichwani pako, Na mikufu shingoni mwako”.

   2. USIMNYIME MAPIGO.

Yapo makosa yanayoweza kurekebishwa kwa maneno peke yake na mtoto akajengeka na kubadilika, lakini yapo yanayohitaji kurekebishwa kwa maneno pamoja na kiboko, hususani yale ya kujirudia rudia tena ya makusudi.

Biblia inasema ukimpiga hatakufa bali utakuwa umemwokoa roho yake na kuzimu.. (Hapo utakuwa umembariki pakubwa Zaidi ya kumtamkia tu baraka za maneno halafu hufanyi chochote).

Mithali 23:13 “Usimnyime mtoto wako mapigo; Maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa.

14 Utampiga kwa fimbo, Na kumwokoa nafsi yake na Kuzimu”.

   3. MFUNDISHE KUSHIKA ELIMU

Badala ya kumtakia tu Baraka kwa kinywa (au kumwombea tu katika chumba chako cha ndani), tenga muda wa kumfundisha Umuhimu wa Elimu (kwanza ya Mungu) na pili ya dunia… Hapo utakuwa umembariki kwa vitendo na si mdomo tu.

Mithali 4:13 “Mkamate sana elimu, usimwache aende zake; Mshike, maana yeye ni uzima wako”

    4. MFUNDISHE KUSHIKA SHERIA ZA NCHI na KUWAHESHIMU WENYE MAMLAKA (Wafalme).

Badala ya kumtamkia tu mafanikio, na kumwombea.. tenga muda kumfundisha umuhimu wa kuwatii wenye mamlaka na kuzingatia sheria ya nchi, hiyo itakuwa Baraka kwake katika siku zijazo za maisha yake.

Mithali 24:21 “Mwanangu, mche Bwana, NA MFALME; Wala usishirikiane na wenye kigeugeu;

    5. MFUNDISHE KATIKA NJIA INAYOMPASA

Ni njia gani inampasa katika umri wake na jinsia yake?.. Je! Katika umri wake huo anapaswa amiliki simu??..je katika umri wake anapaswa asemeshwe maneno hayo unayomsemesha?..je katika umri wake anapaswa atazame hayo anayoyatazama katika TV?.. je katika umri wake huo anapaswa awepo hapo alipo?..anapaswa afanye hicho anachokifanya?.Je! Kwa jinsia yake anapaswa kuvaa hayo mavazi unayomvika??..

Ni muhimu sana kujua mambo yampasayo mwanao/wanao kwa rika walilopo na jinsia zao…

Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee”

Ukiyafanya hayo na mengine kama hayo pamoja na MAOMBI umwombeayo kila siku, basi utakuwa umembariki mwanao/wanao  kweli kweli.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

JE! UMEYABATILISHA MAMBO YA KITOTO?

FIMBO YA HARUNI!

MANENO YA MUNGU YANAPINDULIWAJE?

NINI TOFAUTI KATI YA MATENDO YA SHERIA NA MATENDO YA IMANI?

MAOMBI YA KUOMBEA WATOTO.

Rudi nyumbani

Print this post

MAOMBI YA KUOMBEA WATOTO.

(Masomo maalumu kwa wazazi na walezi)

Marko 9:21 “Akamwuliza babaye, Amepatwa na haya tangu lini? Akasema, TANGU UTOTO

Na mara nyingi amemtupa katika moto, na katika maji, amwangamize; lakini ukiweza neno lo lote, utuhurumie, na kutusaidia

23  Yesu akamwambia, Ukiweza! Yote yawezekana kwake aaminiye”.

Kuna umuhimu Mkubwa sana wa kuwaombea watoto, KILA SIKU (ZINGATIA HILI: KILA SIKU!!!!). Kwanini kila siku?..kwasababu adui naye anawatafuta kila siku, kwamaana anajua imeandikwa (Uzao wako utamponda kichwa (Mwanzo 3:15))

Vifuatavyo ni vipengele vya Maombi kwaajili ya mtoto/watoto.

        1.WOKOVU/NEEMA.

Mwombee mtoto wako Neema ya kumjua Mungu, na kuzungumza naye tangu akiwa tumboni, na ikiwa ulichelewa kuanza kufanya hivyo, basi bado unayo nafasi ya kumwombea hata sasa.

Andiko la kusimamia: 1 Timotheo 3:15  “na ya kuwa TANGU UTOTO umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu”

     2. UTII NA HESHIMA

Mwombee mtoto wako/watoto wako roho ya Utii..Ili wapate miaka mingi ya kuishi na ya kheri.

Andiko la kusimamia: Waefeso 6:1 “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki.

2  Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, 6.3  Upate heri, ukae siku nyingi katika dunia”.

       3. ULINZI

Waombee watoto wako ulinzi wa kiroho na kimwili,  Wakiroho- wasivamiwe wala kutumiwa na nguvu za giza angali wakiwa wadogo na hivyo kuaathirika tabia zao, vile vile wasiharibiwe na dunia wala wasijengeke katika misingi isiyofaa.

Andiko la kusimamia: 1Yohana 5:21  “Watoto wadogo, jilindeni nafsi zenu na sanamu”

      4. UKUAJI (KIROHO NA KIMWILI)

Waombee watoto wako wakue katika kumjua Mungu, vile vile wasipate shida yoyote ya kiafya itakayowaletea ulemavu au udumavu. Akili zao zikue vizuri na wawe na afya bora, vile vile magonjwa yasiwapate iwe ya kuambukiza au kuirithi.

Andiko la kusimamia: Luka 2:39 “Basi, walipokwisha kuyatimiza yote kama yalivyoagizwa katika sheria ya Bwana, walirejea Galilaya mpaka mjini kwao, Nazareti.

40  Yule mtoto akakua, akaongezeka nguvu, amejaa hekima, na neema ya Mungu ilikuwa juu yake”.

       5. ELIMU

Waombee watoto wako wawe watu wa kupenda kusoma, na pia kufanya vizuri katika Elimu ya dunia.

Andiko la kusimamia: Mithali  4:13 “Mkamate sana elimu, usimwache aende zake; Mshike, maana yeye ni uzima wako”

      6. ROHO MTAKATIFU.

Waombee watoto wako wajazwe na Nguvu za Roho Mtakatifu katika nyakati zote, wakiwa tumboni kama Yohana Mbatizaji (Luka 1:15) na hata baada ya kuzaliwa na katika vipindi vyote vya ukuaji wao.

Andiko la kusimamia: Matendo 2:38 “ Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu.

39  Kwa kuwa ahadi hii ni kwa ajili yenu, na kwa watoto wenu, na kwa watu wote walio mbali, na kwa wote watakaoitwa na Bwana Mungu wetu wamjie”.

Kama ukiweza kutumia muda wa kutosha kumwombea Mtoto wako/watoto wako katika vipengele hivyo (KILA SIKU, Asubuhi na jioni)  basi utamweka utawaweka katika nafasi nzuri sana kiroho na mafanikio katika wakati ujao.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

NINI MAANA YA SISI KUWA WATOTO WA MUNGU?

FAIDA ZA MAOMBI YA USIKU

Nini maana ya “Andiko huua, bali Roho huhuisha (2Wakorintho 3:6)

MWONGOZO WA MAOMBI YA WAHUDUMU/ WASIMAMAO MADHABAHUNI.

NI YESU YUPI UNATEMBEA NAYE?

Rudi nyumbani

Print this post

NINYI AKINA BABA MSIWACHOKOZE WATOTO WENU

Majukumu ya Mzazi ni kumlea mtoto katika njia inayompasa, kwasababu hekima ya Mungu inasema, hataiacha njia hiyo hata atakapokuwa mzee.

Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee”

Lakini pamoja na kumlea mtoto katika njia impasayo ya kiMungu, mzazi pia hapaswi kumchokoza mwanae sawasawa na maandiko yafuatayo…

Waefeso 6:4  “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana”.

Wakolosai 3:21 “Ninyi akina baba, msiwachokoze watoto wenu, wasije wakakata tamaa”

Sasa utauliza nini maana ya kuchokoza?

Kuchokoza kama ilivyotumika hapo, ni “kitendo cha kumfanya mtoto awake hasira, pasipo kuwa na sababu ya msingi”

Na baadhi ya sababu hizo ambazo zinaweza kumfanya mtoto awake hasira, hata kufikia hatua ya kukata tamaa au kufanya dhambi  kama za kutoa maneno mabaya mdomoni au moyoni..ni kama zifuatazo.

1.Ukali wa mzazi uliopitiliza.

Mzazi anapokuwa mtu wa kufoka mara kwa mara, na kushutumu kwa ukali mambo yasiyo na mashiko ni rahisi kumfanya mtoto akate tamaa au awake hasira, na kitendo hicho kibiblia kinatafsirika kama “Mzazi kamchokoza mwanae”.

2. Kumwadhibu mtoto mara kwa mara bila kuwa na sababu ya msingi.

Wapo wazazi ambao mtoto akifanya kosa dogo tu, tayari wamekamata kiboko na kutoa adhabu kali. Ni lazima mzazi apime kosa, kama linastahili adhabu au linastahili kuonya tu!.. Lakini sio kila kosa hukumu yake iwe viboko!. Hilo linaweza kumfanya mtoto achukizwe sana badala ya kujengeka, na kibiblia ikahesabika kama umemchokoza mwanao na si kumjenga.

3. Kumdhalilisha mtoto

Wapo wazazi wasiowatia moyo watoto wao, badala yake wanawadhalilisha mbele ya watoto wenzao, au mbele ya jamii.. Jambo kama hili pia kibiblia linatafsirika kama mzazi kamchokoza mwanae.

Tunapaswa siku zote kuwathaminisha watoto wetu mbele ya watoto wengine, vile vile kuwatia moyo katika mambo mazuri wanayoyafanya.

Na wazazi wengi hawajui kama wanawachokoza watoto wao, na kuwaharibu utu wao wa ndani kwa ukali wao.

Hivyo kama mzazi, zingatia mambo hayo (Usiwachokoze watoto wako) na Bwana atakubariki na vile vile kuwabariki watoto wako.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Mada Nyinginezo:

NINI MAANA YA SISI KUWA WATOTO WA MUNGU?

MZAZI, JALI MAISHA YA KIROHO YA MTOTO WAKO.

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

Je! Wana wenu huwatoa kwa nani? maana yake ni nini?

KILEMBA CHA NEEMA, JE! UMEMVIKA MWANAO?

Rudi nyumbani

Print this post

NAFASI YAKO WEWE MAMA KWA MTOTO NA WAJUKUU WAKO NI IPI?.

Jina la Bwana na Mwokozi wetu Yesu, lihimidiwe.. karibu tujifunze biblia..

Neno la Mungu linasema..

Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee”

Faida ya kumlea mtoto wako katika njia inayompasa ni kwamba atakapokuwa mzee hataiacha, na maana yake zaidi ni kwamba hawezi kufikia uzee kabla na yeye kuwa na watoto wake.. hivyo na wajukuu wako pia watanufaika kwa malezi yako wewe kwa mwanao, kwasababu kile mwanao alichokipokea kutoka kwako, na yeye atawafundisha watoto wake, hivyo kizazi chako chote hata cha tatu na cha nne au zaidi ya hapo kitakuwa kitakatifu na cha baraka.

Ukiona kuna shida kwa mjukuu, basi ujue kuwa shida ilianzia kwa bibi au babu, ikaingia kwa mtoto na kisha ikamalizikia kwa mjukuu.. Lakini kama babu au bibi alimlea mwanae katika njia inayompasa, ya kumcha Mungu na kumpenda Mungu, huyo mtoto naye pia ni lazima atawafundisha watoto wake njia hiyo hiyo, na hivyo wajukuu watakaozaliwa basi watakuwa wenye mwenendo mwema wa kumpendeza Mungu.

Tuangalie mfano mmoja wa kwenye biblia wa mtu aliyemlea vyema mtoto wake, na hata mjukuu aliyezaliwa akawa na mwenendo mzuri.

Mtu huyo si mwingine zaidi ya BIBI LOISI, ambaye alikuwa na binti yake aliyeitwa EUNIKE, ambaye ndiye aliyemzaa Askofu Timotheo, mtumwa wa Bwana..

2Timotheo 1:4  “Nami natamani sana kukuona, nikiyakumbuka machozi yako, ili nijae furaha;

5  nikiikumbuka imani uliyo nayo isiyo na unafiki, ambayo ilikaa kwanza katika bibi yako Loisi, na katika mama yako Eunike, nami nasadiki wewe nawe unayo”.

Hapa tunaona Paulo anamwandikia waraka Timotheo, na kukiri chanzo cha imani yake Timotheo, kwamba ilianzia kwa bibi yake Loisi, na hatimaye kwa mama yake aliyeitwa Eunike, na ndipo ikaja kwake, ikimaanisha kuwa msingi wa Timotheo kumpenda Mungu haukuanzia kwake, bali ulianzia kwa bibi yake huko.. Ndio maana ikawa hata vyepesi Timotheo kuiamini injili ya Bwana Yesu na hata kuja kuwa Askofu wa makanisa mengi,  na ndiye aliyekuwa pamoja na Paulo mpaka hatua ya mwisho.

Timotheo hakuwa Mwisraeli moja kwa moja, bali mama yake ndiye aliyekuwa mwisraeli, lakini baba yake alikuwa myunani… pamoja na mchanganyiko huo lakini malezi ya bibi yake na mama yake yalimfanya awe mwenye mwenendo bora kuliko vijana wengi.

Matendo 16:1  “Basi akafika Derbe na Listra, na hapo palikuwa na mwanafunzi mmoja jina lake Timotheo, mwana wa mwanamke Myahudi aliyeamini; lakini babaye alikuwa Myunani.

2  Mtu huyo alishuhudiwa vema na ndugu waliokaa Listra na Ikonio.

3  Paulo akamtaka huyo afuatane naye, akamtwaa akamtahiri kwa ajili ya Wayahudi waliokuwako pande zile; kwa maana wote walijua ya kuwa babaye ni Myunani”.

Je na wewe kama mzazi un akitu gani cha kuwarithisha watoto wako na wajukuu wako?… je ni elimu tu ndio unayoona ni ya muhimu kwao???….

Nataka nikuambie kama watakuwa na elimu ya kidunia halafu hawana Mungu, basi jua kuwa umewapoteza wanao, haijalishi watakuwa mamilionea huko mbeleni!!.. Bibi Loisi, aliona utukufu wa mjukuu wake mbeleni, na kwamba atakuja kuwa mtumishi wa MUNGU hodari katika kuwavuta watu kwa Mungu, hivyo akaanza kuweka msingi bora kwa binti yake Eunike, na Eunike akamfundisha mwanae Timotheo malezi bora.

Walikuwepo vijana wengi wenye elimu nyakati za akina Timotheo, lakini wapo wapi leo??..walikuwepo vijana mamilionea kipindi cha akina Timotheo, lakini hakuna hata mmoja habari yake tunaisoma leo, lakini Timotheo habari zake tunazisoma na zinawaponya mamilioni ya watu duniani hata leo. Bwana amempa Timotheo kumbukumbu lisilofutika..

Walikuwepo wamama wengi na wabibi wengi nyakati za akina Timotheo, lakini hakuna hata mmoja tunayezisoma habari zake, ila hawa wawili Loisi pamoja na mwanae Eunike, habari zao tunazosoma hadi leo..

Na Mungu ni yeye Yule, hajabadilika..ikiwa na sisi tutatembea katika kanuni zake atatupa kumbukumbu ambalo halitafutika. Ikiwa na sisi tutawalea watoto wetu katika njia zitupasazo basi kumbukumbu letu pamoja na watoto wetu, na wajukuu wetu, na vitukuu vyetu, na vilembewe na vilembwekeze litadumu milele na milele.

Anza kuwafunza watoto wako biblia, wafundishe wamjue Yesu zaidi ya Hisabati, wafundishe wazijue amri za Mungu, na kuwa waombaji na watu wa ibada zaidi hata ya shule za ulimwengu. Ukimfanya Mungu wa kwanza katika maisha yao, na Mungu atawafanya wa kwanza katika mambo yao.

Bwana atubariki sote.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

“Si watu wa kutumia mvinyo sana”, je tunaruhusiwa kutumia mvingo kidogo?(1Timotheo 3:8).

KWANINI UNAPASWA UWE BIBI ARUSI NYAKATI HIZI ZA MAJERUHI?

MWANAMKE, BINTI, MAMA.( Sehemu ya 1)

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

Je! Mfalme Abiya na Mfalme Asa walikuwa ni ndugu?

Rudi nyumbani

Print this post

USIOGOPE KUMWADHIBU MWANAO.

Tunaishi katika ulimwengu ambao, maadili yameporomoka sana, na bado yanaendelea kuporomoka kwa vijana na watoto..Na hiyo inatufanya tuelekeze lawama kwa watoto; tukisema watoto wa siku hizi wamebadilika sana, lakini ukweli ni kwamba wazazi ndio wamebadilika, watoto ni walewale.

Malezo ya mzazi kwa mtoto ni muhimu sana, mtoto si kama nyau, ambaye kitu pekee anachohitaji ni chakula tu na sehemu ya kulala, hata ukimwacha mwaka mzima bila kumjali kwa vingine, hakuna hasara yoyote, bado ataendelea kuwa paka..

Lakini kwa mwanadamu sivyo..yeye hafugwi, bali analelewa..na malezi ni zaidi ya chakula na nguo na mahali pa kulala.. Hapo ndipo wazazi wengi wanashindwa kuelewa.

Kwasababu mtoto atahitaji kuwa na maarifa, nidhamu, uadilifu, hekima, busara, upendo, utiifu, upambanuzi n.k. Ili aweze kuishi vema katika huu ulimwengu.

Hivi vyote hazaliwi navyo, bali anajifunza anapokuwa duniani..hivyo akikosa msaada sahihi, basi ibilisi atatumia fursa hiyo kumfundisha elimu yake na nidhamu yake hapa ulimwenguni.

Hivyo wewe kama mzazi au mlezi una jukumu kubwa sana zaidi ya lile la kumlisha na kumvisha na kumsomesha..hizo ni hatua 3 katika ya 1000, anazopaswa azijue.

Ikiwa hukupata masomo yaliyotangulia ya malezi ya watoto, basi waweza kututumia ujumbe kwa namba hii, ili tuweze kukutumia chambuzi za nyuma. Au tembelea website yetu hii www.wingulamashahidi.org. au tutumie ujumbe kwa namba hizi +255693036618

Leo tutaona njia nyingine ya kumlea mtoto vema.

Na njia yenyewe si nyingine zaidi ya kutumia KIBOKO.

Lugha hii inaweza isiwe nzuri masikioni mwa wazazi lakini ni tiba nzuri kwa malezo yao. Hata ‘panadol’ haina ladha nzuri mdomoni, lakini pale inapotutibu tunaishukuru, ndio maana tunayo siku zote majumbani kwetu.

Lakini ni kwanini utumie kiboko kwa mtoto?

Sababu zipo mbili.

1) Ni kwasababu ujinga umefungwa moyoni mwake

2) Mungu naye huwa anatuadhibu sisi.

  1. Tukianzana na sababu ya kwanza biblia inatuambia..

Mithali 22:15

[15]Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali.

Ni vizuri ukafahamu kuwa mtoto kama mtoto huwa ana ujinga mwingi ndani yake..yule si kama wewe, unapoona anang’ang’ania kitu fulani kisichopendeza halafu wewe kama mzazi unaamua tu kumwachia kisa anakililia, usidhani kuwa anaelewa matokeo ya kile anachokitaka..

Kumbuka yule hatafakari, wewe unatafakari, hivyo basi ukimsikia anatukana, usisubiri apumzike bali hapo hapo shika kiboko chapa. Ukiona unamwagiza kitu hatii, chapa..ukiona hawaheshimu watu wazima hata baada ya kuonywa mara nyingi..chapa..usiogope labda atakufa…biblia inasema kiboko cha adili hakiui..

Mithali 23:13

[13]Usimnyime mtoto wako mapigo; [14] Maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa.

Hiyo itamsaidia sana kuundoa ujinga mwingi wa kipepo ambao mwingine kwa maneno tu, peke yake au kwa kufundishwa hauwezi kutoka..

  • 2) Mungu naye anatuadhibu.

Na sababu ya pili kwanini tuwaadhibu watoto wetu kwa kiboko pale wanapokosea..ni kwasababu Mungu naye anatuadhibu sisi watoto wake.

Biblia inasema hivyo..

Waebrania 12:6-7

[6]Maana yeye ambaye Bwana ampenda, humrudi, Naye humpiga kila mwana amkubaliye.

[7]Ni kwa ajili ya kurudiwa mwastahimili; Mungu awatendea kama wana; maana ni mwana yupi asiyerudiwa na babaye?

Umeona..Sisi hatuna hekima ya kumzidi Mungu, tengeneza picha Bwana angekuwa anatuona tunatukana wengine halafu hachukui hatua yoyote anacheka tu..si tungaangamia..Mungu alipomuona Daudi anamchukua mke wa Huria halafu anaendelea kusema wewe ni mtumishi wangu unayeupendeza moyo wangu..Daudi leo angekuwa wapi kama sio kuzimu? Lakini Mungu alimuadhibu vikali…na baadaye akatubu akapona..

Nasi pia biblia inatuambia tutakuwa wakamilifu kama Baba yetu wa mbinguni alivyomkamilifu..(Mathayo 5:48)

Mzazi unayemtazama mwanao, anafanya ujinga, unaogopa kumchapa atalia..bado hujawa mkamilifu kama Mungu.

Hivyo anza sasa kutimiza huduma hii, ili kesho mtoto huyo afanyike baraka na neema kwa ulimwengu.

Lakini zingatia: Haimaanishi kuwa umpige pige mtoto ovyo kila saa anapokosea..hapana zipo sehemu zinastahili kiboko, zipo zinazostahili maonyo, zipo zinazostahili kuelimishwa..Zote zina umuhimu wake mkubwa bila kupuuzia hata moja.

Bwana akubariki

Shalom

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

MZAZI, JALI MAISHA YA KIROHO YA MTOTO WAKO.

KILEMBA CHA NEEMA, JE! UMEMVIKA MWANAO?

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

NINI MAANA YA SISI KUWA WATOTO WA MUNGU?

NI NINI KINATOKA KINYWANI MWA MTOTO WAKO?

MALEZI YA MTOTO MCHANGA.

Rudi nyumbani

Print this post

KAMA “MAMA” UMEBEBA HATIMA YA MTOTO WAKO WA KIUME.

Jina la Bwana Yesu libarikiwe, karibu tujifunze tena maneno ya Uzima ya Bwana wetu, Yesu Kristo. Neno la Mungu ni taa inayoongoza miguu yetu, na Mwanga wa njia zetu! (Zab. 119:105).

Ipo hali Fulani ambayo, Watoto wa kiume wengi wanakuwa na mapenzi mengi kwa mama zao, na kinyume chake asilimia kubwa ya Watoto wa kike wanakuwa na mapenzi Zaidi kwa baba zao kuliko mama zao.  Ingawa si wakati wote au kwa Watoto wote inakuwa hivi, lakini asilimia kubwa inatokea kuwa hivyo.

Na biblia pia utaona imetaja au kuonyesha kuwepo kwa aina hii ya mahusiano kati ya wazazi na Watoto wa jinsia tofauti.

Hebu tusome visa kadhaa vya baadhi ya  wafalme wa kwenye biblia, kisha kisha tuendelee mbele.

  1. MFALME SEDEKIA.

Yeremia 52:1 “SEDEKIA alikuwa na umri wa miaka ishirini na mmoja hapo alipoanza kumiliki; naye akamiliki miaka kumi na mmoja huko Yerusalemu; NA JINA LA MAMA YAKE ALIITWA HAMUTALI, BINTI YEREMIA WA LIBNA.

2 NAYE ALITENDA YALIYO MABAYA MACHONI PA BWANA, sawasawa na yote aliyoyatenda Yehoyakimu.

3 Maana, kwa sababu ya hasira ya Bwana, mambo haya yalitokea katika Yerusalemu na katika Yuda, hata akawaondosha wasiwe mbele za uso wake, naye Sedekia akamwasi mfalme wa Babeli.

Hapa tunaona Mama wa Sedekia anatajwa kama sababu ya Ubaya wa Mfalme Sedekia… Sasa sio huyo tu!

  1. MFALME REHOBOAMU, Mwana wa Sulemani.

1Wafalme 14:21 “Rehoboamu akaanza kutawala alipokuwa mwenye miaka arobaini na mmoja, akatawala miaka kumi na saba huko Yerusalemu, mji aliouchagua Bwana miongoni mwa kabila zote za Israeli, ili aliweke jina lake huko. NA JINA LA MAMAYE ALIITWA NAAMA, MWAMONI.

22 BASI YUDA WAKAFANYA MAOVU MACHONI PA BWANA; WAKAMTIA WIVU, KWA MAKOSA YAO WALIYOYAKOSA, KULIKO YOTE WALIYOYAFANYA BABA ZAO.

Ijapokuwa Rehoboamu alikuwa ni mwana wa Sulemani, na mjukuu wa Daudi, lakini mama yake anatajwa kumfanya awe mbaya…(sasa sio huyo peke yake..)

  1. MFALME YEROBOAMU

1Wafalme 15:1 “Mwaka wa kumi na nane wa mfalme Yeroboamu mwana wa Nebati, Abiya alianza kutawala juu ya Yuda.

2 Miaka mitatu akatawala huko Yerusalemu; NA JINA LA MAMAYE ALIITWA MAAKA, BINTI ABSALOMU.

3 AKAZIENDEA DHAMBI ZOTE ZA BABAYE, ALIZOZIFANYA KABLA YAKE; wala moyo wake haukuwa mkamilifu na Bwana, Mungu wake, kama moyo wa Daudi babaye”.

Si huyu peke yake…

  1. MFALME AHAZIA.

1Wafalme 8:26 “Ahazia alikuwa na umri wa miaka ishirini na miwili alipoanza kutawala; akatawala mwaka mmoja huko Yerusalemu. NA JINA LA MAMAYE ALIITWA ATHALIA BINTI OMRI MFALME WA ISRAELI.

27 Akaiendea njia ya nyumba ya Ahabu, AKAFANYA YALIYO MABAYA MACHONI PA BWANA, kama walivyofanya nyumba ya Ahabu, kwa kuwa alikuwa mkwe wa jamaa ya Ahabu”.

Sio hawa tu…Unaweza kusoma pia habari za Mfalme Yothamu (2Wafalme 15:33), na Mfalme Manase (2Wafalme 21:1-2) na wengine wengi katika biblia, ambao utaona Uovu wao umesababishwa na mama zao.

Vile vile walikuwepo watu wa kawaida ambao hawakuwa wafalme, ambao pia tabia zao ziliathiriwa na mama zao, mfano wa hao ni yule kijana wa mwanamke wa kiisraeli, ambaye Habari zake tunazisoma katika Walawi 24:10-14, kijana huyu alimtukana Mungu, na akapigwa mawe mpaka kufa,  na wengine wengi.

Lakini pia walikuwepo wafalme ambao walifanya mazuri, na Uzuri wao huo, Pamoja na sifa zao mbele za Bwana zilisababishwa na Mama zao..

  1. MFALME YEHOSHAFATI.

1Wafalme 22:42 “Yehoshafati alikuwa mwenye miaka thelathini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka ishirini na mitano huko Yerusalemu. NA JINA LA MAMAYE ALIITWA AZUBA BINTI SHILHI.

43 AKAIENDEA NJIA YOTE YA ASA BABAYE; WALA HAKUGEUKA, AKIFANYA YALIYO MEMA MACHONI PA BWANA…..”.

  1. MFALME YEHOASHI.

1Wafalme 14:2 “Naye alikuwa na umri wa miaka ishirini na mitano alipoanza kutawala; akatawala miaka ishirini na kenda katika Yerusalemu; NA JINA LA MAMAYE ALIITWA YEHOADANI WA YERUSALEMU.

3 AKAFANYA YALIYO MEMA MACHONI PA BWANA, ila si kama babaye Daudi; akafanya kama yote aliyoyafanya baba yake Yoashi”.

  1. MFALME UZIA.

1Wafalme 15:2 “Alikuwa na umri wa miaka kumi na sita alipoanza kutawala; akatawala miaka hamsini na miwili huko Yerusalemu. NA JINA LA MAMAYE ALIITWA YEKOLIA WA YERUSALEMU.

3 AKAFANYA YALIYO MEMA MACHONI PA BWANA, kama yote aliyoyafanya babaye Amazia”.

Sasa katika maandiko hayo yote, unaweza kujiuliza ni kwanini ni waMama, wanahusishwa na si waBaba?.. Ni kwasababu kuna muunganiko wa kipekee kati ya Mama na mtoto wake wa kiume, ambapo Mama asipoutumia vizuri huo muunganiko, anaweza kujikuta anaharibu hatima ya  mtoto wake wa kiume moja kwa moja. (Ni vizuri kulijua hili mapema, ili mambo yatakapoharibika huko mbeleni, usije ukasema ulikuwa hujui!!)

Mama unapokuwa mtu wa kidunia, unakuwa mtu wa kumkataa Mungu, fahamu kuwa na mtoto wako wa kiume ni rahisi sana, kuamini hiyo njia yako kuwa ni njia sahihi, kuliko hata mtoto wako wa kike.

Lakini mtoto wako wa kiume anapokuona wewe ni mtu unayemcha Mungu, ni mtu unayeutafuta sana uso wa Mungu, na kuukataa ubaya, ni rahisi sana, mwanao  wa kiume, na yeye kuwa kama wewe, hiyo ni (Siku zote weka hilo akilini).

Wafalme wote waliofanya machukizo kwa Bwana, waliharibiwa na Mama zao. Vile vile wafalme wote waliofanya Mema mbele za Bwana, na hata kusifiwa ni kutokana na Mama zao. Hakuna mahali popote wababa wametajwa, katika kutenengeneza hatima za Watoto wao wa kiume.

Hivyo kama Mama, Jifunze kuwapeleka Watoto wako Kanisani, ukiwapeleka wewe Zaidi ya baba hawawezi kuiacha hiyo njia, hata kama watakuja kuyumba kidogo, lakini watairudia tu njia hiyo siku moja!..

Vile vile wafundishe kusoma Neno, na kushika vifungu vya biblia, na kuomba.. Ukifanya hayo kwa Watoto wako wewe kama Mama, ni rahisi mambo hayo kuwaingia Zaidi kuliko kama angefanya Baba.

Halikadhalika msifie mwanao katika mambo ya ki-Mungu na mema, zaidi ya mambo ya ulimwengu huu tu…sauti yako ina thamani kubwa zaidi kwake kuliko baba yake, angefanya hivyo.

Na vile vile wewe Mtoto wa kiume, jifunze kumsikiliza Mama yako, anayekufundisha njia za Mungu, na kukuelekeza njia sahihi.. Kwasababu usipomsikiliza huyo, hakuna mwingine utakayekuja kumsikiliza tena katika Maisha yako.

Ipo methali ya watu wa ulimwengu isemayo “ASIYEFUNZWA NA MAMAYE, HUFUNZWA NA ULIMWENGU”. Ni watu wa kidunia wameitunga methali hii kufuatia uhalisia waliouona, kuwa kwa Mama kunayo mafunzo makuu, Zaidi ya kwa baba.

Hivyo Wewe kama Mama mtengeneze mwanao katika njia ya haki Mithali 22:6 “Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee”., ..na wewe kama mtoto wa kiume, msikilize Mama yako.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312


Mada Nyinginezo:

MWANAMKE, BINTI, MAMA.( Sehemu ya 1)

MWANAMKE, BINTI, MAMA. (Sehemu ya 2)

Je suruali ni vazi la kiume tu?

Ni kweli Paulo alipuuzia maonyo aliyopewa ya kwenda Yerusalemu?

VIJANA NA MAHUSIANO.

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

Rudi nyumbani

Print this post

MISTARI YA BIBLIA KUHUSU WATOTO.

  1. MISTARI YA WAZAZI/WALEZI KUHUSU WATOTO.

Haya Mafungu ya biblia ambayo wazazi/walezi wanapaswa wayajue kuhusu watoto wao.

Zaburi 8:2a “Vinywani mwa watoto wachanga na wanyonyao Umeiweka misingi ya nguvu;..”

Mungu anaonyesha kuwa kupitia watoto wachanga, ambao unaweza kuwadharau hawajui kitu, hapo ndipo Mungu ameweka nguvu zake. Hivyo anza kumlea mtoto katika misingi ya kumcha Mungu tangu akiwa mdogo, kwasababu hapo ndipo Mungu anapoketi.

 Na ndio maana biblia inasema..

Mithali 22:6 Mlee mtoto katika njia impasayo, Naye hataiacha, hata atakapokuwa mzee.

Tabia ya kudharau watoto, au kuona kama umri wao wa kumjua Mungu bado, Yesu aliukemea sana, tunalithibitisha hilo katika..

Marko 10:13 “Basi wakamletea watoto wadogo ili awaguse; wanafunzi wake wakawakemea.

14 Ila Yesu alipoona alichukizwa sana, akawaambia, Waacheni watoto wadogo waje kwangu, msiwazuie; kwa maana watoto kama hawa ufalme wa Mungu ni wao.

15 Amin, nawaambieni, Ye yote asiyeukubali ufalme wa Mungu kama mtoto mdogo hatauingia kabisa.

16 Akawakumbatia, akaweka mikono yake juu yao, akawabarikia”.

Biblia inasema pia..

Zaburi 127:3 “Tazama, wana ndio urithi wa Bwana, Uzao wa tumbo ni thawabu”.

Biblia bado inasisitiza wazazi, wasiwaudhi watoto wao, kwasababu zisizo na msingi, kisa tu wao ni watoto,

Waefeso 6:4 “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni katika adabu na maonyo ya Bwana.

Kwasababu malaika wao mbinguni wanawatazama uwatendeapo mabaya..

Mathayo 18:10 “Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika wao mbinguni siku zote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni”.

Zaidi pia Bwana Yesu anataka wazazi/walezi wajifunze kupitia watoto walionao, hivyo kwa kupitia wao tutapata kujua siri kubwa za ufalme wa mbinguni.

Mathayo 18 : 1-5

“1 Saa ile wanafunzi wakamwendea Yesu wakisema,

2 Ni nani basi aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni? Akaita mtoto mmoja, akamweka katikati yao,

3 akasema, Amin, nawaambia, Msipoongoka na kuwa kama vitoto, hamtaingia kamwe katika ufalme wa mbinguni.

4 Basi, ye yote ajinyenyekeshaye mwenyewe kama mtoto huyu, huyo ndiye aliye mkuu katika ufalme wa mbinguni.

5 Na ye yote atakayempokea mtoto mmoja mfano wa huyu kwa jina langu, anipokea mimi;”

Lakini bado Mungu anasisitiza juu ya kuwarekebisha watoto, kwamba ni jukumu la kila mzazi/mlezi kumwadhibu mtoto wake, pale anapokosea . Hilo ni agizo la Mungu. Usipomwajibisha mtoto wako, Mungu atakuwajibisha wewe siku ile, kwa kutomtengeneza mwanao.

Mithali 22:15 “Ujinga umefungwa ndani ya moyo wa mtoto; Lakini fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali”.

Mithali 23: 13 “Usimnyime mtoto wako mapigo; Maana ukimpiga kwa fimbo hatakufa.

14 Utampiga kwa fimbo, Na kumwokoa nafsi yake na Kuzimu”.

2) WAJIBU WA MTOTO.

Vilevile mzazi, unapaswa umfundishe mwanao wajibu wake kama mtoto, Sawasawa na Neno la Mungu linavyosema,

Na mojawapo ni kuwafundisha kukutii wewe.

Waefeso 6:1 “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki.

2 Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi,

3 Upate heri, ukae siku nyingi katika dunia”.

Mithali 1:8 “Mwanangu, yasikilize mafundisho ya baba yako, Wala usiiache sheria ya mama yako,

9 Kwa maana hayo yatakuwa kilemba cha neema kichwani pako, Na mikufu shingoni mwako”.

Pia umfundishe kujua wajibu wake wa kumtafuta Mungu tangu akiwa mdogo..kwasababu kwa Mungu hakuna utoto.

Yeremia 1:6 “Ndipo niliposema, Aa, Bwana MUNGU! Tazama, siwezi kusema; maana mimi ni mtoto.

7 Lakini Bwana akaniambia, Usiseme, Mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila mtu nitakayekutuma kwake, nawe utasema kila neno nitakalokuamuru”.

Na mwisho Mkumbushe pia hata watoto watahukumiwa, na  kuzimu wapo watoto ambao hawakuwajibika katika kuwatii wazazi wao, na kumcha Mungu.

Ufunuo 20:12 “Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao”.

Bwana akubariki.

Maran atha.

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post

JE NI LAANA KULELEWA NA BABA AU MAMA WA KAMBO?

Shalom, Jina la Bwana wetu, Yesu Kristo libarikiwe. Karibu tujifunze biblia, Neno la Mungu wetu.

Katika ulimwengu wa sasa, ukitaja mama wa kambo, au baba wa kambo, tayari picha ya kwanza inayotengenezeka kwenye vichwa vya wengi ni MATESO.

Lakini leo napenda tujifunze kitu kingine tofauti na hicho, ili tusije tukajikuta tunazuia baraka zetu pasipo sisi kujua.

Jambo la kwanza la kufahamu kabla hatujaingia kwenye kiini cha somo ni kwamba, popote pale unapojikuta upo, au umezaliwa, na kulelewa..jua Mungu kakuweka hapo kwa kusudi maalumu, ambalo ni la baraka.

Sasa turudi kwenye swali letu!. Je! Ni laana au mkosi, kuzaliwa au kulelewa na mama wa kambo au baba wa kambo?.

Tutalijibu swali hili, kwa kujifunza juu ya maisha mmoja katika biblia, na huyo si mwingine zaidi ya Bwana Yesu, Mkuu wa uzima..

Maandiko yanasema “tujifunze kwake”..Maana yake tumtazame yeye, tuyaangalie maisha yake, na tupate masomo (Mathayo 11:29).

Na leo tutapata somo lingine kutoka katika maisha yake.

Sasa wengi wetu hatujui kuwa Bwana wetu Yesu, alilelewa na Baba wa kambo katika mwili (Ni lugha ngumu kidogo hii, lakini ndivyo ilivyo).

Yusufu hakuwa Baba kamili wa Bwana Yesu. Mimba aliyoipata Mariamu haikumhusisha baba, ilikuwa ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu (soma Mathayo 1:18).

Baba wa Bwana Yesu, alikuwa ni Roho Mtakatifu.

Hivyo ni sahihi kabisa kusema, Yusufu alikuwa ni baba wa kambo wa Bwana Yesu.

Lakini ulishawahi kujiuliza ni kwanini Mungu aruhusu aishi na baba wa kambo?, kwani alishindwa kumfungulia Mariamu mlango, aishi mwenyewe tu na mtoto Yesu?.. Mungu angeweza kufanya hivyo, kwani yeye ni mweza wa kila kitu.

Angeweza kufungua mlango wa mali nyingi, kipindi Bwana Yesu anazaliwa na kumfanya Mariamu aishi maisha ya kifahari peke yake na mtoto Yesu, na pia angeweza kuzuia Yusufu asipose Mariamu kabisa..

Lakini hakufanya hivyo bali kinyume chake, baada tu ya Mariamu kuposwa ndipo mimba inaonekana..Na baada ya Yesu kuzaliwa, akaanza kubebwa na baba huyo huyo wa kambo, na hata wakati wa kazi ya ufundi, alifanya kazi ya baba huyo huyo wa kambo!.

Bwana aliruhusu maisha yake yawe hayo, ili kutufundisha na sisi kuwa si laana kuishi hayo maisha.

Sasa kulikuwa kuna nini kwa Yusufu, mpaka mkuu wa Uzima, Yesu Kristo apitie pale?

Yusufu alikuwa ni maskini kweli, hakuwa tajiri, lakini alikuwa amebeba ahadi ya kifalme, kumbuka Mungu alimwahidi Daudi, kwamba kupitia uzao wake atatokea Mfalme. Na Yusufu alikuwa ni wa Uzao wa Daudi.

Hivyo ili Bwana Yesu awe mfalme kupitia ahadi hiyo ya Daudi, ilikuwa hana budi azaliwe katika Hema ya Yusufu..angezaliwa pengine popote, ahadi hiyo ya Mungu isingetimia.

Mpaka hapo utakuwa umeanza kuona hata wewe ni kwasababu gani… umelelewa na huyo baba wa kambo Au mama wa kambo.

Haijalishi anakutesa kiasi gani, au ni maskini kiasi gani, lipo kusudi kwanini upo hapo, au umelelewa hapo, kuna baraka ambazo huwezi kuziona kwa macho!..

Kuzaliwa kwa Bwana kwenye lile zizi, chini ya Bwana Yusufu asiyekuwa na kitu, kulikuwa na maana kubwa.

Na wewe vile vile..tengeneza mambo yako vizuri sasahivi kwasaababu kuna baraka tele, mbele yako.

Ishi na Baba yako huyo vizuri, mheshimu, mbariki kwasababu ni Mungu ndiye aliyekuweka hapo, hujajiweka mwenyewe..na Mungu ndiye anayeijua mbele yetu..

Usianze kuharibu mambo kwa kunung’unika, unapopitia vikasoro vidogo vidogo, wewe tazama mbele, ongeza utii na heshima.

Kadhalika na kama wewe ni baba au ni mama na una watoto wa kambo, ishi nao vizuri, kwasababu nao pia wamebeba ahadi, ahadi hiyo isingeweza kukamilika pasipo wewe. Na mwisho utaona faida kubwa mbeleni.

Utasema vipi na mama wa kambo?

Musa alilelewa na Mama wa kambo, Binti Farao, hakujua atakuja kuwa nani..lakini maandiko yanasema, baadaye Mungu alikuja kumfanya Musa kuwa kama “mungu kwa Farao”.

Kutoka 7:1 “BWANA akamwambia Musa, Angalia, nimekufanya wewe kuwa kama Mungu kwa Farao; na huyo ndugu yako Haruni atakuwa nabii wako”.

Alienda kwa binti Farao, ili kupata jina hilo MUSA, Jina hilo alipewa na “mama wa Kambo”…hakupewa na mama yake mzazi, wala halikuwa jina la kiyahudi..

Na cha ajabu ni kwamba, Mungu hakumbadilisha jina Musa…aliendelea nalo hilo hilo, Sauli alibadilishwa na kuwa Paulo, Yakobo alibadilishwa na kuwa Israeli, lakini Musa amebakia kuwa Musa mpaka leo…kumbe wito wake ulikamilishwa pia na mama wa kambo.

Hivyo tunachoweza kujifunza ni kuwa macho ya kiroho kuona mbele na si hapa tu..katika nafasi uliyopo kama unaishi na baba au mama wa kambo, mheshimu kama Baba yako na kama mama yako, unapoona shetani ananyayuka na kujaribu kuharibu uhusiano wenu.. basi ni wakati wa wewe nyanyuka na kuongeza maombi…usiende kusikiliza simulizi za kishetani zinazosimuliwa huko na huko katika mitandao na katika vijiwe kuhusu ubaya wamama au wababa wa kambo, utajizolea elimu zitakazoharibu maisha yako..Biblia ndio kitabu chetu na mwongozo wetu.

Kama Bwana Yesu aliishi na Baba wa kambo, na kufanya naye kazi moja na bado akawa mfalme, ni kitu gani kitakachokuzuia wewe kufikia baraka zako, kupitia huyo mzazi au mlezi ambaye si wako?.

Kadhalika na kama wewe ni mzazi, au mlezi wa mtoto ambaye si wako, usimkatae mtoto wa kambo, kwasababu hujui ana ahadi gani kupitia wewe.. Na Mungu amekuchagua wewe, kwasababu na wewe pia unabaraka juu yake.

Hivyo kwa hitimisho ni kwamba hakuna laana yoyote kuishi au kulelewa na Baba au mama wa kambo. Vile vile hakuna laana yoyote au mkosi, kulea mtoto wa kambo.

Bwana akubariki.

Ikiwa bado hujamwamini Bwana Yesu, ni vyema ukakata shauri sasa kwasababu siku tunazoishi hizi ni siku za mwisho.

Na Bwana Yesu alisema.. “Itatufaidia nini tupate ulimwengu mzima halafu tupate hasara ya nafsi zetu”

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

MWANAMKE, BINTI, MAMA. (Sehemu ya 3)

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

YANAYOENDELEA SASA KATIKA MADHABAHU YA MUNGU ROHONI.

Rudi nyumbani

Print this post

Je! Siku ya unyakuo watoto wachanga watanyakuliwa?

SWALI: Je! Siku ya unyakuo watoto wachanga watanyakuliwa? Na vipi kuhusu walio bado tumboni, na wenyewe watanyakuliwa au wataachwa?


JIBU: Hili ni moja ya swali gumu  kwasababu biblia haijaeleza moja kwa moja ni nini kitawatokea watoto siku ile ya Unyakuo, Hivyo tutajaribu kueleza kwa kadiri ya tunavyoona katika baadhi ya vifungu kwenye maandiko.

Ukitazama katika biblia, utaona, wapo watoto walipata neema kutokana na haki za wazazi wao, mfano wa hawa ni watoto wa Nuhu, na Lutu,  vilevile wapo watoto walioadhibiwa kutokana na makosa ya wazazi wao. Utaliona hilo pia katika vile vizazi vyote vya Sodoma na Gomora, pamoja na gharika  vyote viliteketezwa, hadi watoto walipata adhabu kwa dhambi za wengine. Lakini hiyo haimaanishi kuwa wataadhibiwa tena baada ya kifo.

Pia tukumbuke kuwa hata katikati ya kipindi cha dhiki kuu, bado watu wataendelea kutungishwa mimba na kuzaliwa, hivyo litakuwepo kundi la vichanga ambavyo vitazaliwa katikati ya dhiki kuu na vitakufa katika maangamizi yao..Hilo tunalithibitisha katika andiko hili;

Mathayo 24:19 “Ole wao wenye mimba na wanyonyeshao siku hizo!

20 Ombeni, ili kukimbia kwenu kusiwe wakati wa baridi, wala siku ya sabato.

21 Kwa kuwa wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe.

22 Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo”.

Unaona? Kwahiyo siku ile ikifika, kuna uwezekano wa watoto wengine kunyakuliwa (hata wale walio tumboni), na vilevile wengine kubaki, japo hatuwezi kusema hivyo ndivyo ilivyo, Yote tunamwachia Mungu. Ikiwa ni wote watanyakuliwa, au ni baadhi, Tunachopaswa kufahamu ni kuwa Mungu ni wa haki, atayaleta yote katika mizani, na yote yatakuwa sawa tu mwisho wa siku, na tutaona kabisa hukumu zake ni za haki. Kama vile Malaika mbinguni wanavyokiri hivyo..

Ufunuo 16:7 “Nikaisikia hiyo madhabahu ikisema, Naam, Bwana Mungu Mwenyezi, ni za kweli, na za haki, hukumu zako”.

Cha muhimu tunachopaswa kujua ni kuwa sisi ambao tayari tumeshafikia kimo cha kuyajua mema na mabaya, Kama hatutayatengeneza mambo yetu sasa, kwa kumpokea Bwana Yesu Kristo kwa kumaanisha kabisa, na kujitwika misalaba yetu na kumfuata, tujue kuwa unyakuo ukipita tutaachwa. Na matokeo yake, yatakuwa ni kuingia katika mateso makali ya dhiki kuu pamoja na Jehanamu ya moto.

Je! Umeokoka? Je! Umebatizwa katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la Yesu Kristo kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako? Kumbuka Unyakuo ni wakati wowote, tubu umruidie muumba wako. Parapanda ni siku yoyote inalia, hakuna dalili iliyosalia..

Bwana Yesu akubariki.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post