MWANAMKE, BINTI, MAMA.( Sehemu ya 1)

MWANAMKE, BINTI, MAMA.( Sehemu ya 1)

Nakusalimu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo, karibu katika sehemu ya kwanza ya  mfululizo wa masomo ya wanawake.

Yapo masomo mengine kwa wanawake yameshapita nyuma , ikiwa yalikupita na utapenda kuyapata, basi utanitumia msg inbox nikutume.

Lakini leo tutatazama, namna ambavyo Bwana Yesu alivyowatambua wanawake aliokutana nao, katika kipindi chote cha huduma yake alipokuwa hapa duniani.

  • Kuna wakati alipokutana na mwanamke Fulani, alimtambua kama BINTI
  • Kuna wakati tena alipokutana na mwanamke Fulani, alimtambua kama MAMA
  • Na kuna wakati pia alipokutana na mwanamke Fulani alimtambua kama MWANAMKE.

Haya ni mambo ambayo unapaswa uyaelewe, na kuyazingatia sana unaposoma biblia. Kwasababu kila utambulisho ulibeba ujumbe maalumu kwa kundi husika.

1) Leo tutaangazia Utambulisho wa kwanza wa Bwana ambao ni  MWANAMKE.

Unajua mpaka mtu akuite “mwanamke” ni wazi kuwa halengi kitu kingine Zaidi ya “jinsia” yako, halengi umri wako, au ukubwa wako, au umbo lako, hapana bali jinsia. Ndicho alichokifanya Bwana Yesu alikupokutana na baadhi ya wanawake, hakuwa na nia ya kuwaita kwa vyeo vyao au kwa  mionekano yao labda ni wadogo au wakubwa, au wazee au vijana hapana bali aliwaita “mwanamke” kulenga jinsia yao Zaidi..

Kufunua kuwa, ujumbe ulio nyuma yake, ni mahususi kwa watu wa jinsi hiyo. Hivyo, embu tusome kwa pamoja habari ya yule mwanamke aliyekuwa na dhambi nyingi, tuone ni nini alikifanya mpaka ikampelekea Bwana Yesu kumtambua kama mwanamke na sio, kitu kingine..

Tusome..

Luka 7:37 “Na tazama, mwanamke mmoja wa mji ule, aliyekuwa mwenye dhambi, alipopata habari ya kuwa ameketi chakulani katika nyumba ya yule Farisayo, alileta chupa ya marimari yenye marhamu.

38 Akasimama nyuma karibu na miguu yake, akilia, akaanza kumdondoshea miguu machozi yake, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake, akiibusu-busu miguu yake na kuipaka yale marhamu.

39 Basi, yule Farisayo aliyemwalika alipoona vile, alisema moyoni mwake, Mtu huyu kama angekuwa nabii, angemtambua mwanamke huyu amgusaye, ni nani, naye ni wa namna gani, ya kwamba ni mwenye dhambi.

40 Yesu akajibu akamwambia, Simoni, nina neno nitakalo kukuambia. Akasema, Mwalimu, nena.

41 Akasema, Mtu mmoja mkopeshaji alikuwa na wadeni wawili; mmoja amwia dinari mia tano, na wa pili hamsini.

42 Nao walipokuwa hawana cha kumlipa, aliwasamehe wote wawili. Katika hao wawili ni yupi atakayempenda zaidi?

43 Simoni akajibu akasema, Nadhani ni yule ambaye alimsamehe nyingi. Akamwambia, Umeamua haki.

44 Akamgeukia yule mwanamke, akamwambia Simoni, Wamwona mwanamke huyu? Niliingia nyumbani kwako, hukunipa maji kwa miguu yangu; bali huyu amenidondoshea machozi miguu yangu, na kuipangusa kwa nywele za kichwa chake.

45 Wewe hukunibusu; lakini huyu tangu nilipoingia hakuacha kunibusu sana miguu yangu.

46 Hukunipaka kichwa changu mafuta; bali huyu amenipaka miguu yangu marhamu.

47 Kwa ajili ya hayo nakuambia, Amesamehewa dhambi zake ambazo ni nyingi, kwa kuwa amependa sana; lakini asamehewaye kidogo, huyo hupenda kidogo.

48 KISHA ALIMWAMBIA MWANAMKE, UMESAMEHEWA DHAMBI ZAKO”.

Unapoitafakari habari hiyo unaona nini kwa huyu mwanamke aliyekuwa gwiji wa dhambi, aliyefahamika mji mzima..? Utagundua kuwa Toba au kibali chake hakikuja katika maneno yoyote? Bali katika vitendo ambavyo Bwana Yesu aliona hata wakuu wa dini waliomwalika karamuni, hawakuvitenda.

Mwanamke huyu alitoa mafuta yake yenye thamani nyingi sana, akaanza kuusafisha mwili wa Kristo, ambao aliouna umechafuka sana, alianza kujitoa bila kujali ni nini anapoteza, na kikubwa Zaidi akatumia na nywele zake za thamani, jambo ambalo si la kawaida kwa wanawake wa kidunia wapendao urembo kufanya, kama tu mvua ikimdondokea atatafuta kibanda ajifiche ili tu nywele zake zisiharibike, sembuse kupangusa miguu michafu kwa nywele zake?

Lakini huyu mwanamke alikuwa radhi kufanya hivyo..Na kwa kitendo kile, moyo wa Bwana uliguswa sana, hadi kumsamehe dhambi zake, japokuwa hakutoa Neno lolote kinywani mwake…akasema “mwanamke” umesamehewa dhambi zako.

Na wewe kama mwanamke kabla hujafikiria kujifunza kwa akini Petro, embu chukua muda kwanza, ujifunze kwa wanawake kama hawa, ambao mpaka sasa tunasoma habari zao, ambao Bwana Yesu aliwaona wanathamani kubwa kuliko hata yule Farisayo tajiri (Simoni), aliyemwalika nyumbani kwake, kula chakula..

Mwanamke Ikiwa utatamani, Kristo akusamehe, au akupe kibali, au akufungue, au akuponye,  Maisha yako. Basi Jibidiishe, kuusafisha mwili wa Kristo, kwa kumaanisha kweli, kweli. Tukisema mwili wa Kristo, tunamaanisha, Kanisa lake, na kazi yake. Jitoe kwa hali na mali zako. Hata kama huna chochote, kapige deki, kasafishe hiki au kile.. Lakini usiwe mwombaji tu wa maneno.

Hichi ndicho Bwana alichokiona wa wanadamu wa jinsia hii, (wanawake). Kumjali Kristo ni sehemu ya wito wao hapa duniani, na unathamani kubwa kama tu karama nyingine za kitume zilivyo mbele ya Kristo.

Muhudumie Bwana mwanamke..

Luka 8:2 “na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba,

3 na Yoana mkewe Kuza, wakili wake Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao”.

Bwana akubariki.

Maran atha

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Mwendelezo wa sehemu ya pili unakuja…ambapo tutaona kwanini Bwana aliwatambua baadhi ya wanawake na kuwaita binti zake, na sio, kwa vyeo vyao au ukubwa wao..

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
3 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Isack Mboma
Isack Mboma
11 months ago

Mbarikiwe sanaa tunawapenda