Category Archive Home

Yakobo 1:5 inasema tuombapo hekima, Mungu hakemei, maana yake ni nini.

SWALI: Katika Yakobo 1:5 inasema tuombapo Mungu hakemei, maana yake ni nini.


JIBU:

Yakobo 1:5

[5]Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa. 

Kabla ya kuona maana hilo neno “wala hakemei naye atapewa”. Tuone kwanza tafsiri ya kifungu chote.

Hapa mtume Yakobo kwa uongozo wa Roho, anandika juu ya suluhisho la kupungukiwa kwa jambo muhimu sana ndani ya mwanadamu. Nalo ni Hekima.

Haandiki ikiwa mtu amepungukiwa na mali, au na umaarifu au na fursa, au watoto…hapana bali na hekima, na aombe dua.

Lakini hekima aisemayo sio hekima ya duniani, bali hekima ya ki- Mungu. Ambayo ni ufahamu wa Ki-Mungu unaoingia moyoni mwa mtu kumsaidia aweze kupambanua vema mambo yote, katika ufasaha wote ili kuleta matokeo aliyoyatarajia.

Hivyo sisi wote tunaihitaji hekima katika yote tuyatendayo. Vinginevyo hatutaweza kuzalisha chochote. 

Lakini bado anatoa kanuni ya kuipata, hasemi tukae chini tuwaze, au tukahubiri, au tukatoe sadaka, au tuende kwenye shule za biblia. Hapana anasema na tuombe dua kwa Mungu.

Tunaipata kwa kuomba. Kwa kuchukua muda kupiga magoti na kuomba. Sio kuomba dakika mbili, na kusema Amen au yale maombi ya kumalizia siku unapokwenda kulala. Hapana bali ni maombi yaliyochanganyikana na kiu ya dhati kupata hekima ya Ki-Mungu katika eneo fulani, unalotaka Bwana akusaidie.

Vilevile hatupaswi kuomba bila dira. Kwamfano kusema.. “Mungu naomba unipe hekima”.. Hapana tunaomba tukielekeza eneo ambalo tunataka Bwana atusaidie kupata hiyo hekima ya kupambanua.

Kwamfano hekima katika kuyaelewa maandiko, hekima katika kuhubiri, hekima katika kufundisha, katika kuombea wagonjwa, katika kufanya biashara, katika kuimba. n.k.

Na hapo ndipo Mungu mwenyewe anaongeza ufahamu wake juu ya hicho unachokiomba na hatimaye utaona tu, mabadiliko, au njia ya kitu hicho unachotaka akusaidie.

Sasa tukirudi kwenye swali, pale anaposema

“awapaye wote, kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa”

Maana yake, kwasababu Mungu ana ukarimu, basi hachagui wa kumpa, anawapa wote. Hii ahadi yake kuwa kila aombaye humpa. Haleluya.

Na tena anasema “hakemei”. Tofauti na sisi wanadamu

Kwamfano sisi tuwafuatapo wazazi wetu na kuwaomba kitu, wakati mwingine, hutugombeza, au huwa wakali, au kutaka utoe kwanza hesabu ya kile cha nyuma ulikitumiaje, kabla ya kukupa hichi kingine. Na ndio maana ulikuwa na hofu, kujifikiria mara mbili mbili hicho unachotaka kwenda kuomba, ukiulizwa hivi, ujibu vipi. Sio tu kwa wazazi, lakini kwa wanadamu wote, sifa hiyo wanayo tuwafuatapo kuwaomba kitu, si kivyepesi vyepesi kama tunavyodhani.

Lakini kwa Mungu wetu sio, hakemei, haangaali ya nyuma kukushutumu, hakuuliza makosa yako. Anakupa tu, bila sharti lolote.

Ni furaha iliyoje. Mimi na wewe tuliomwamini tunapokwenda kumwomba Mungu hekima, hatushutumiwi kwa lolote, au kwa madhaifu yetu. Bali kinachohitajika tu ni kumwamini  yeye asilimia mia, bila kutia shaka katika hilo unaloomba, kwasababu ukitia shaka, maombi hayo hayaendi kwake bali kwa mungu mwingine asiyeweza yote. 

ndio maana anataka tumfuatapo tusiwe na shaka ya kutojibiwa, ili maombi yetu yafike kwake kwelikweli, yeye aliyemweza wa yote.

Anasema hivyo katika vifungu vya mbeleni.

Yakobo 1:6-8

[6]Ila na aombe kwa imani, pasipo shaka yo yote; maana mwenye shaka ni kama wimbi la bahari lililochukuliwa na upepo, na kupeperushwa huku na huku.

[7]Maana mtu kama yule asidhani ya kuwa atapokea kitu kwa Bwana.

[8]Mtu wa nia mbili husita-sita katika njia zake zote. 

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Je Elisha alimdanganya Ben-hadadi kuwa hatakufa kwa ugonjwa wake?

NGUVU YA HEKIMA NA AKILI

IVUMBUE INJILI YA KRISTO KUTOKA KATIKA KILA JAMBO.

Rudi Nyumbani

Print this post

Watu wa nyumbani mwa Kaisari ni watu gani? (Wafilipi 4:22).

Swali: Watu wa nyumbani mwa Kaisari wanaotajwa na Mtume Paulo katika Wafilipi 4:22 walikuwa ni watu wa aina gani?


Jibu: Turejee…

Wafilipi 4:21 “Mnisalimie kila mtakatifu katika Kristo Yesu. Ndugu walio pamoja nami wawasalimu. 

22 Watakatifu wote wawasalimu, hasa wao walio wa NYUMBANI MWA KAISARI”

Kaisari anayezungumziwa hapo ni yule mfalme mkuu wa Rumi (ambaye ndiye aliyekuwa mfalme wa dunia wakati ule).

Sasa watu wa nyumbani mwake wanaozungumziwa hapo si watoto wake, bali ni watu waliokuwa wanatumika katika nyumba yake.

Katika enzi yake walikuwepo wengi (maskini na matajiri, wanaume kwa wanawake) waliokuwa wanatumika katika nyumba yake, sasa miongoni mwa hao ambao Paulo hajawataja majina yao, walimwamini Bwana YESU na kuokoka.

Na ndio hao Paulo anafikisha salamu zao kwa kanisa la Filipi.

Hii ikifunua kwamba injili ya Bwana YESU ilipenya hata katika majumba ya wafalme wa dunia.

Na si Kaisari tu! Utaona pia hata aliyekuwa mke wa wakili wa Herode aliyeitwa Yoana alikuwa mfuasi wa Bwana YESU, na ndiye aliyekuwa anamhudumia Bwana kwa mali zake pamoja na baadhi ya wanawake, huyu naye alikuwa miongoni mwa watu wa nyumba ya Herode.

Luka 8:2 “na wanawake kadha wa kadha ambao walikuwa na pepo wabaya na magonjwa wakaponywa; nao ni Mariamu aitwaye Magdalene aliyetokwa na pepo saba, 

3 na Yoana mkewe Kuza, wakili wake Herode, na Susana, na wengine wengi, waliokuwa wakimhudumia kwa mali zao”.

Na sisi hatupaswi kuionea haya injili, wala kubagua watu wa kuwahubiria, bali injili inawastahili watu wote (maskini na matajiri, wenye cheo na wasio na cheo), kwa maana ni uweza wa Mungu uletao wokovu kama maandiko yasemavyo..

Warumi 1:16 “Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia”

Maran atha.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618.

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

VYA MUNGU MPENI MUNGU.

Heri walio maskini wa roho; Maana ufalme wa mbinguni ni wao.

FUNDISHA NENO KANISANI NA NYUMBANI.

TUJIFUNZE JAMBO KWA WANAWAKE HAWA WAWILI.

MAASI KUONGEZEKA NI ISHARA YA NINI?.

Rudi Nyumbani

Print this post

Ayubu alimaanisha nini kusema ‘nami nitarudi tena huko uchi vilevile;?

SWALI: Ayubu alimaanisha nini kusema..Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; Aliwezaje kurudi tena tumboni mwa mama yake tena uchi je hilo jambo linawezekana?


JIBU: Kauli hiyo aliisema Ayubu baada ya kupotelewa na familia yake na mali zake. Lakini Kwa ujasiri akamtukuza Mungu katika hali hiyo pia, kwa kusema maneno hayo; 

Ayubu 1:21

[21]akasema, Mimi nilitoka tumboni mwa mama yangu nili uchi, nami nitarudi tena huko uchi vilevile; BWANA alitoa, na BWANA ametwaa; jina la BWANA na libarikiwe. 

Lakini swali lipo hapo, katika kurudi tumboni mwa mama yake uchi. maana yake ni nini?

Ikumbukwe kuwa sisi hatukutoka tu  katika tumbo la wanamke bali pia katika tumbo la ardhi, hiyo ndio mama wa ulimwengu. yaani mama wetu wa kwanza.

soma; 

Zaburi 139:15

[15]Mifupa yangu haikusitirika kwako, 

Nilipoumbwa kwa siri, Nilipoungwa kwa ustadi pande za chini za nchi; 

Mhubiri 12:7

[7]Nayo mavumbi kuirudia nchi kama yalivyokuwa, 

Nayo roho kumrudia Mungu aliyeitoa. 

Hivyo Ayubu aliposema nami nitarudi tena huko huko hakumaanisha mama yake mzazi, bali mama wa ulimwengu wote yaani ardhi.

Na ndivyo ilivyo kwa kila mmoja wetu, hukuja na kitu, utaondoka bila kitu chochote. Ukiwa uchi vilevile.

lakini jambo lingine la kufahamu kuwa, wale walio ndani ya Kristo, wafikapo kule ng’ambo hawataonekana uchi, bali watapewa vazi jipya la rohoni la Kristo Yesu, ndio ile miili mipya ya utukufu isiyoona uharibifu idumuyo milele.

2 Wakorintho 5:1-3

[1]Kwa maana twajua ya kuwa nyumba ya maskani yetu iliyo ya dunia hii ikiharibiwa, tunalo jengo litokalo kwa Mungu, nyumba isiyofanywa kwa mikono, iliyo ya milele mbinguni. 

[2]Maana katika nyumba hii twaugua, tukitamani sana kuvikwa kao letu litokalo mbinguni; 

[3]ikiwa tukiisha kuvikwa hatutaonekana tu uchi. 

Swali ni je! Umeandaliwa vazi lako baada ya kuondoka?

Kumbuka unalipokea kwa kumwamini Yesu Kristo leo, okoka tubu dhambi zako, ubatizwe, kisha upokee kipawa cha Roho Mtakatifu. vazi lako liwe limekamilika., ili siku ile usionekane uchi.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >>

https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

MAVAZI YA NDANI NA YA NJE.

SIFA ZA MAMBA YULE MKUBWA WA AYUBU.

MAMBO YA KUZINGATIA WAKATI WA MFUNGO.

Rudi Nyumbani

Print this post

Je Daudi aliwachukia viwete na vipofu? (2Samweli 5:6-9)

SWALI: Je Daudi aliwachukia viwete na vipofu? Kama tunavyosoma katika 2Samweli 5:6-9. Je! habari hiyo tunaielewaje?


JIBU:

2 Samweli 5:6-9

[6]Kisha mfalme na watu wake wakaenda Yerusalemu ili kupigana na Wayebusi, wenyeji wa nchi ile; hao ndio waliomwambia Daudi, wakisema, Usipowaondoa vipofu, na viwete, hutaingia humu kamwe; huku wakidhania ya kuwa Daudi hawezi kuingia humo.

[7]Lakini Daudi aliipiga ngome ya Sayuni; huu ndio mji wa Daudi.

[8]Naye Daudi alisema siku hiyo, Yeye atakayewapiga Wayebusi, na apande kwenye mfereji wa maji, na kuwapiga viwete, na hao vipofu, ambao roho yake Daudi inawachukia. Kwa sababu hii watu husema, Wako vipofu na viwete hawawezi kuingia nyumbani.

[9]Basi Daudi akakaa ndani ya ngome hiyo, akaiita mji wa Daudi. Kisha Daudi akajenga toka Milo na pande za ndani.

Habari hii inazungumzia wakati ule ambao Daudi alikwenda kuiteka Yerusalemu na kuufanya kuwa mji wa Mungu.

Alipofika na kukutana na wenyeji wa mji huo, walimdharau na kumsema kimafumbo kwa kauli ya mzaha kumwambia “Usipowaondoa vipofu, na viwete, hutaingia humu kamwe;”

Wakiwa na maana vita yake ni ya kupambanishwa na watu dhaifu kabisa wa mji, mfano wa vipofu na viwete, hao ndio apambane nao, lakini sio majemedari wa nchi ile. Akiweza hao walau ndio aingie sasa kujaribu kuuteka, huku wakijua kuwa hata hilo Daudi hataweza kwasababu walimwona ni dhaifu.

Na ukweli wakati huo Daudi hakuwa na nguvu yoyote, kwasababu ndio kwanza ametoka kuupokea ufalme. Hawakujua kuwa nguvu zake tangu zamani zina Mungu, ndio zile zilizomwangusha Goliathi ni silaha zake kwa jiwe moja.

Lakini Daudi aliipowafuatia na kuwapiga, na kuwaangamiza, naye alitumia pia jina hilo hilo la vipofu na viwete kimizaha akiwaita wayebusi waliomwonyeshea dharau..pamoja na hilo Daudi alionyesha kuwachia sana.

Lakini mistari hiyo hakumaanisha kuwa anawachukia viwete na vipofu. Hapana Kama ingekuwa hivyo asingemkaribisha Mefiboshethi mtoto wa Yonathani katika nyumba yake ya kifalme kuketi mezani pake daima..(2Samweli 9). Na ikumbukwe kuwa Daudi alikuwa anamcha Mungu na kuwakumbuka sana wanyonge.

Lakini pale inaposema….

“Kwa sababu hii watu husema, Wako vipofu na viwete hawawezi kuingia nyumbani”.

Ni kwamba kufuatana na Daudi kuwasema viwete na vipofu akiwarejea wayebusi, ukazuka msemo huo, ‘vipofu na viwete hawana ruhusu kuingia nyumbani mwa Mungu;. Lakini haikuwa hivyo’..

Misemo na namna hii ilikuwepo tangu zamani hata kuhusu ile habari ya mfalme Sauli, ya kutabiri (1Samweli 19:24), na kuhusu ike habari za mtume Yohana, pale wale mitume wengine waliposikia Kauli ya Bwana Yesu inayosema ikiwa nataka huyu awepo mpaka nijapo, wakadhani kuwa Yohana hata onja mauti kamwe, mpaka Yesu atakaporudi kumbe hawakumuelewa Bwana Yesu, hakumaanisha vile.(Yohana 21:22-23)

Na ndivyo ilivyodhaniwa kwa Daudi kwamba anawachukia vipofu na viwete, kumbe aliwamaanisha wayebusi.

Lakini ni nini hasaa tunaweza jifunza..katika tukio hilo?

Ni kawaida ya adui yetu anapokaribia kushindwa hunyanyua ujasiri wake kwa kiwango cha juu sana. Mji ambao uligeuzwa kuwa wa Bwana, na mwema kuliko yote, ulitanguliwa na dhihaka nyingi za kukatisha tamaa. Hata ukuta aliokuwa anaujenga Nehemia, ambao sehemu yake iliendelea kudumu kwa mamia ya miaka mbeleni ulitanguliwa na dhihaka nyingi za kuvunjishwa moyo. wakisema hata mbweha akipita juu yake utaanguka.

Silaha hiyo hiyo anaitumia adui leo, unapoona maono makubwa ya kuitenda kazi ya Bwana ndani yetu, vitisho vya adui huanzia hapo, aah wewe huna upako, wewe huwezi kuhubiri, huna pesa, huna elimu ya kukutosha, huna uzoefu, utafungwa..hizo zote ni dhihaka, Daudi alishazitambua toka kwa Goliathi, ndio maana akawashinda wayebusi.

Hivyo ni kusimama imara kuitetea injili, kwa imani tukijua hakuna linaloshindikana kwake yeye aaminiye. Na palipo na dhihaka nyingi ndipo palipo na mafanikio makubwa.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Wayebusi walikuwa ni watu gani?

Hanithi ni nini katika biblia? (kumbukumbu 23:17)

KWANINI YESU KRISTO NI MWANA WA DAUDI?

Rudi Nyumbani

Print this post

Kusanyiko la makini/ mkutano wa makini ni upi?

Katika agano la kale, Israeli walikuwa na makusanyiko mengi, ambapo walikutanika kumfanyia Mungu ibada, na kuzishika sikukuu. Lakini pia yalichaguliwa makusanyiko mengine yaliyoitwa mikutano/makusanyiko ya makini. Makusanyiko haya yalifanyika  katika siku ya saba ya sikukuu ya Pasaka, na siku ya nane, baada ya sikukuu ya vibanda. Katika siku hiyo hawakuruhusiwa kufanya kazi yoyote. Bali ilitengwa kwa ajili ya kujitakasa, au kujisogeza karibu na Mungu,

Hivi ni vifungu baadhi vinavyoielezea siku hiyo;

Hesabu 29:35 Tena siku ya nane mtakuwa na kusanyiko la makini sana; hamtafanya kazi yo yote ya utumishi;

36 lakini mtasongeza sadaka ya kuteketezwa, sadaka ya kusongezwa kwa moto, harufu ya kupendeza kwa Bwana; ng’ombe mume mmoja, na kondoo mume mmoja, na wana-kondoo waume wa mwaka wa kwanza wakamilifu saba.

Walawi 23:34 Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Siku ya kumi na tano ya mwezi huo wa saba ni sikukuu ya vibanda muda wa siku saba kwa Bwana.

35 Siku ya kwanza kutakuwa na kusanyiko takatifu; msifanye kazi yo yote ya utumishi.

36 Mtamsongezea Bwana sadaka kwa moto siku saba; siku ya nane kutakuwa na kusanyiko takatifu kwenu; nanyi mtamsongezea Bwana sadaka kwa moto; ni mkutano wa makini huu; msifanye kazi yo yote ya utumishi

Kumbukumbu 16:8 Siku sita utakula mikate isiyotiwa chachu; na siku ya saba na uwe mkutano mtukufu kwa Bwana, Mungu wako, usifanye kazi yo yote.

Huo mkutano mtukufu ndio kusanyiko la makini.

Hekalu la kwanza pia lilipomalizika liliwekwa wakfu katika siku hii ya kusanyiko la makini

2Nyakati 7:9 Hata siku ya nane wakaita kusanyiko la makini; kwa maana walishika kuitakasa madhabahu siku saba, na sikukuu siku saba.

Sehemu  nyingine mikusanyiko hii iliitishwa rasmi, kwa lengo la kujimimina kwa Mungu kuomba, kwa ajili ya maovu na majanga ambayo yanaipata nchi. (Yoeli 1:14 – 2:15). Kusanyiko hili liliitwa pia kama kusanyiko  kuu.

Je! Ufunuo wake ni upi leo?

Kama vile tulivyo na mikusanyiko ya aina mbalimbali leo, mfano  ya shule ya jumapili, ya semina, ya injili n.k. Vivyo hivyo hatuna budi kuwa na makusanyiko ya makini. Ambayo ni mikusanyiko ya mifungo na maombi. Ambapo tunapata muda wa kujimimina kwa undani kabisa uweponi mwa Mungu, kumtaka aingilie kati mambo yetu.

Je! unaithamini? Mungu aliyesema tusiache kukusanyika pamoja (Waebrania 10:25). Hakumaanisha tu mikusanyiko ya jumapili, lakini pia ya mifungo na maombi.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Rudi Nyumbani

Print this post

Wakijifunza siku zote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.

SWALI: 2Timotheo 3:7, ina maana gani inaposema;

wakijifunza siku zote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.


JIBU: Katika kitabu cha 2Timotheo sura ya tatu(3), kuanzia mstari 1-9. Kinaeleza sifa za watu watakaozuka katika siku za mwisho.  Tabia ambazo hapo mwanzo hazikuwepo. Sasa ukisoma pale utaona zimeorodheshwa baadhi ikiwemo kutokea watu wenye kupenda fedha, watu wakali, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu,..na nyinginezo

Lakini ipo sifa nyingine inatajwa pale, kuwa litazuka kundi la watu wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake..ndio hao ambao anaeleza sasa mbeleni, wanajifunza sikuzote ila wasiweze kuufikia ujuzi wa kweli.

Tusome;

2 Timotheo 3:5-9

[5]wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao.

[6]Kwa maana katika hao wamo wale wajiingizao katika nyumba za watu, na kuchukua mateka wanawake wajinga wenye mizigo ya dhambi, waliochukuliwa na tamaa za namna nyingi;

[7]wakijifunza siku zote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.

[8]Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani.

[9]Lakini hawataendelea sana; maana upumbavu wao utakuwa dhahiri kwa watu wote, kama vile na upumbavu wa hao ulivyokuwa dhahiri.

Maana ya ujuzi;

Ujuzi maana yake ni ufanisi au kukifanya kitu kwa utashi wote. Mtu anaweza akafanya jambo lakini akiwa hana ujuzi nalo litakuwa ni kituko kama sio hasara kabisa. Kwamfano mtu atasema, mimi naweza kujenga (na hajasomea ujenzi). Hivyo akaenda kununua tofali na kuanza kupandisha, unajua ni nini kitamkuta? kwasababu hajui kanuni za ujenzi anaenda  kufanana na yule mtu aliyejenga nyumba yake juu ya machanga.

Ndivyo ilivyokuwa kwa hawa watu, hawakuufikia huo ujuzi wa kweli, kwasababu walikuwa na nia zao wenyewe za tofauti na sio ya Kristo, walilenga kuwakusanya wanawake waliokuwa na mizigo ya dhambi, kama daraja lao, na hifadhi yao ya kihuduma, ili watumize malengo yao. Sasa Kwa urefu wa tabia za wanawake hao bofya link hii  uwasome >>> Wanaowachukua wanawake wajinga mateka ni akina nani?

Lakini huo ujuzi wa kweli ni upi?

ujuzi wa kweli ni UTAUWA/ UTAKATIFU. Mtu anayefikia kilele cha kuifahamu kweli ya Kristo huishia katika utakatifu wa kweli. Tunalisoma hilo katika;

Tito 1:1

[1]Paulo, mtumwa wa Mungu, na mtume wa Yesu Kristo; kwa ajili ya imani ya wateule wa Mungu, na ‘ujuzi wa kweli’ ile iletayo utauwa;

Umeona ujuzi wa kweli, lazima ulete utauwa.

Lakini watu hawa walikuwa na mfano wa utauwa lakini walizikana nguvu zake kimatendo, ndio maana hawakufikia..waliitwa wakristo lakini wakristo jina, waliitwa mitume, wainjilisti, manabii, waalimu, watakatifu, lakini nia zao zipo penginepo. Walikuwa na elimu za vyuoni, wanajua kuyachambua maandiko, na vifungu vyote, lakini maisha ya utakatifu yapo mbali na wao.

Ndilo linalotendeka leo hii, maarifa tuliyonayo kuhusu Mungu ni mengi, zaidi hata watu wa kale, tuna wingi wa vyuo vya theolojia, na makanisa, na mafudisho mengi. Lakini maisha ya wengi hayamwakisi Kristo katika utakatifu wa kweli.

ndio hili neno linatimia,

wakijifunza siku zote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli

Ni swali la kujiuliza na sisi, je! wokovu wetu umefikia ujuzi wa kweli? Kumbuka hizi ni siku za mwisho, mafundisho uliyonayo yanakusukuma kwenye nini? FUATA UTAKATIFU.

Bwana akubariki

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >>https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Nini maana ya mhubiri 9:11? si wenye mbio washindao katika michezo?

MWE NA HASIRA, ILA MSITENDE DHAMBI.

NJIA KUU YA KUINGIA KATIKA ULE MJI.

Rudi Nyumbani

Print this post

Maana ya Mathayo 6:34 ‘Yatosha kwa siku maovu yake’ 

SWALI: Bwana Yesu alikuwa anamaanisha nini kusema.. “Yatosha kwa siku maovu yake”.

Mathayo 6:34

[34]Basi msisumbukie ya kesho; kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe. Yatosha kwa siku maovu yake.


JIBU: Bwana, hataki tuwe na hofu ya vitu vya huko mbeleni (ambavyo bado havijafikiwa), si mpango wa Mungu tubebe mizigo mingi kwa wakati mmoja, kwasababu hatujaumbiwa asili hiyo, ndio maana hata katika ile sala ya Bwana tunasema; utupe “siku kwa siku” rikizi yetu.

Hasemi utupe riziki ya “mwaka mzima” kana kwamba tukikosa vyote leo hatutaishi.. bali siku kwa siku..

Kwanini iwe hivyo?

Sasa katika hali yetu ya kibinadamu tunajua kabisa mihangaiko yetu, taabu zetu, shughuli zetu za kila siku, mara nyingi huwa haziwi safi kama tunavyotarajia, wakati mwingine kama sio kujikwaa, basi tunakutana na mambo mengi pia ya kukosesha yasiyompendeza Mungu. Hayo ndio maovu yake.

Tunakutana na watukanaji, na wazinzi, na waharibifu, wenye mizaha, wasumbufu, n.k. hivyo kiuhalisia katika mambo yetu mema, maovu pia hutokea. Hivyo kitendo cha kuyataabikia sana ya mbeleni, tafsiri yake ni kuwa tunayaleta na maovu yake pia leo. Na matokeo yake tutalemewa na maovu kichwani Na kujikuta tunamkosea Mungu.

Bwana anataka tupambane kwanza na yale ya leo, ya kesho tutapewa nguvu ya kushindana nayo. Kwa tafsiri nyingine ikiwa wewe ni wa kubeba mambo mengi ya mbeleni, dhambi itakulemea na kukushinda.

Yatosha kwa siku maovu yake.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Ni kwa jinsi gani Mungu anapatiliza maovu ya baba zetu sawasawa na Kutoka 20:5-6?

Nilikuwa naomba kujua utofauti kati ya DHAMBI, UOVU na KOSA kibiblia.asante!!

HAMJAFAHAMU BADO?

Rudi Nyumbani

Print this post

NYOSHA MKONO WAKO, UUGUSE MFUPA WAKE NA NYAMA YAKE.

Shetani huwa ana kauli zake, za uongo ambazo hupenda kuwaaminisha watu, kuwa kuna mambo mwanadamu hawezi kuyafanya akiwa hapa duniani hata iweje.

Tukisoma habari ya Ayubu wakati ule shetani alipokwenda kumshitaka kwa Mungu.

Mungu alipomuuliza kuhusu mwenendo wake, majibu ya shetani yalikuwa ni kwamba Mungu amemzungushia wigo, kutunza alivyonavyo, Na kama atapotezewa alivyonavyo, basi atamkufuru Mungu waziwazi. Hivyo Mungu akaruhusu shetani amjaribu Ayubu, amchukulie alivyo navyo vyote, lakini uongo wa kwanza, ukashindwa, alipoona Ayubu anamtukuza Bwana katika misiba yake. Hiyo ni kuonyesha kuwa mwanadamu yoyote anaweza  kuishi bila msukumo wa mali,wala mtu wala kitu chochote katika hii dunia.

Lakini baadaye tena, akaendelea mbele kuzungumza uongo mwingine, alipoona Ayubu bado yupo na Mungu, akamwambia Mungu, yote yanawezekana kwa mwanadamu kuvumilia, lakini hili la kuugusa mfupa wake,kumtesa, kamwe hawezi kuvumilia atakukufuru tu. Mimi ninawajua wanadamu uwezo huo hawana, nilishawafundisha pia huko duniani.

Ayubu 2:4 Shetani akamjibu Bwana, na kusema, Ngozi kwa ngozi, naam, yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake.

5 Lakini sasa nyosha mkono wako, uuguse mfupa wake na nyama yake, naye atakukufuru mbele za uso wako.

6 Bwana akamwambia Shetani, Tazama, yeye yumo mkononi mwako; lakini tunza tu uhai wake.  7 Basi Shetani akatoka mbele za uso wa Bwana, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa.

8 Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni.  9 Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe.

10 Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo. Je! Tupate mema mkononi mwa Mungu, nasi tusipate na mabaya? Katika mambo hayo yote Ayubu hakufanya dhambi kwa midomo yake.

Hilo nalo likashindikana. Kumbe mtu, hata kuupoteza uhai wake kwa ajili ya Kristo, linawezekana.

Ni nini Bwana anatufundisha kwa mawazo ya adui kwetu sisi ?

Leo hii ni rahisi sana kusikia, kauli kama, hakuna mtakatifu duniani! Ni rahisi kuona mtu anaanguka ovyo katika dhambi, na kutumia kisingizio kuwa yeye sio malaika. Utasikia kauli kama haiwezekani mtu kuacha vyote alivyonacho kwa ajili ya Kristo. Ndugu tambua kuwa hizo ni kauli za ibilisi ndani ya moyo wako. Adui anapenda kumshusha thamani mtu, kumweka kama kiumbe ambaye hawezi kujisimamia, hafundishiki, haaminiki.

Ni kweli mwanadamu kuwa na ukamilifu wa Mungu haiwezekani (Ndio sababu Yesu akaja kutukomboa), lakini kuna viwango Fulani Mungu anajua tunaweza kuvifikia, akalithibitisha hilo kwa Ayubu. Kama Ayubu ameweza kwanini wewe ushindwe, usijishushe thamani.

Neema haijaja kutuambia kuwa sisi hatuwezi, bali  imekuja kutuwezesha zaidi kuwa wakamilifu mbele za Mungu, yaani pale Ayubu aliposhindwa sisi tunasaidiwa kwa hiyo, na kutufanya tupokelewe kikamilifu mbele za Mungu, hiyo ndio kazi ya Neema (Soma Tito 2:11-12).

Kamwe usiruhusu hayo maneno ya kushushwa thamani na ibilisi, kwamba wewe huwezi mpendeza Mungu, huwezi kuacha vyote kwa ajili yake. Yesu  alisema tutakuwa wakamilifu kama Baba yetu alivyomkamilifu. Tunachopaswa kufanya ni kuamini kuwa hilo linawezekana na kuonyesha bidii katika hilo kumpendeza yeye. Na neema ya Mungu itatusaidia kufikia kilele Hicho cha juu kabisa.

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >>https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 9 (Kitabu cha Ayubu).

ILI TUONEKANE WAKAMILIFU MBELE ZA MUNGU.

Kwanini Labani aseme Yakobo ni Mfupa wake na nyama yake?(Mwanzo 29:14)

Rudi Nyumbani

Print this post

IFAHAMU KANUNI YA KUTAKA NA KUPATA.

Warumi 7:18  “Kwa maana najua ya kuwa ndani yangu, yaani, ndani ya mwili wangu, halikai neno jema; kwa kuwa KUTAKA NATAKA, bali KUTENDA LILILO JEMA SIPATI.

19  Kwa maana lile jema nilipendalo, silitendi; bali lile baya nisilolipenda ndilo nilitendalo”.

Je na wewe ni miongoni mwa watu wanaosumbuliwa na utumwa wa namna hiyo?.. UNATAKA na kutamani lakini unajikuta HUPATI au HUWEZI au HUFANYI au HUPOKEI?.

> Unataka kumtumikia Mungu lakini unajikuta huwezi..

> Unataka kuwa msomaji wa Neno lakini unajikuta hufanikiwi.

> Unataka na kutamani kufanya mema na mazuri kwaajili ya Mungu wako lakini hufanikiwi n.k

Kama UMETAKA mambo mengi na huoni uelekeo wa kulipata, basi huwenda NJIA unayoitumia kutaka na kutafuta hayo mambo ina kasoro..

Hebu jaribu njia hii, ya kutaka mambo halafu uone kama hutapata uyatakayo,

Na njia hii si nyingine Zaidi ya ile aliyoitumia Danieli.

Danieli 9:3 “Nikamwelekezea Bwana Mungu uso wangu, ILI KUTAKA kwa MAOMBI, NA DUA, PAMOJA NA KUFUNGA, NA KUVAA NGUO ZA MAGUNIA NA MAJIVU. 

4 Nikamwomba Bwana, Mungu wangu, nikaungama, nikasema, Ee Bwana, Mungu mkuu, mwenye kutisha, ashikaye maagano na rehema kwao wampendao, na kuzishika amri zake”

Umeona kanuni Danieli aliyoitumia??… HAKUTAKA mambo kwa kupiga ramli, au kwenda kwa waganga wa kienyeji, wala kwa kwenda Kuwadhulumu watu au kukorofishana na watu au kula rushwa, au kujipendekeza kwa watu bali KWA MAOMBI, NA DUA NA KUFUNGA NA KUVAA NGUO ZA MAGUNIA NA MAJIVU, na matokeo yake alipata alichokuwa anakitafuta..

Na sisi tunajifunza mambo hayo hayo…

> Tukitaka Amani nyumbani.. kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Amani katika ndoa.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Amani kazini.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Akili darasani.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Ulinzi na afya.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

> Tukitaka Ujazo wa Roho Mtakatifu.. Kanuni ni hiyo > Kufunga na Kuomba.

Luka 11:13 “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao wamwombao?”

Kama Bwana YESU alivyosema kuwa “kuna mambo hayawezekaniki, isipokuwa kwa kufunga na kuomba”

Wafilipi 2:13 “Kwa maana ndiye Mungu atendaye kazi ndani yenu, KUTAKA KWENU na kutenda kwenu, kwa kulitimiza kusudi lake jema.

14  Yatendeni mambo yote pasipo manung’uniko wala mashindano”

Bwana atusaidie.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

KANUNI JUU YA KANUNI.

NJIA SAHIHI YA KUFUNGA.

MAMBO MENGINE HAYATOKI ISIPOKUWA KWA KUFUNGA.

Nini maana ya “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi”?

HIZI NI NYAKATI ZA KUFUNGA NA KUOMBA.

Rudi Nyumbani

Print this post

MAMBO YA KUZINGATIA WAKATI WA MFUNGO.

Yafuatayo ni mambo saba (7) ya kuzingatia wakati wa Mfungo.

1.MAOMBI

Mfungo wowote ili uwe ni mfungo ni lazima uambatane na Maombi.. Mfungo usiokuwa na maombi ni sawasawa na bunduki isiyo na risasi.

Marko 9:28 “Hata alipoingia nyumbani, wanafunzi wake wakamwuliza kwa faragha, Mbona sisi hatukuweza kumtoa?

29  Akawaambia, Namna hii haiwezi kutoka kwa neno lo lote, isipokuwa kwa kuomba”.

Mathayo 17:21  [Lakini namna hii haitoki ila kwa kusali na kufunga.]

Kila siku utakayofunga hakikisha unaomba, (tena maombi ya masafa marefu, tofauti na siku nyingine).

 2. KUWA MTULIVU.

Unapofunga usiwe mtu wa kuhangaika na kuzurura huku na kule, bali kuwa mtu wa faragha muda mwingi, wakati wa mfungo si wakati wa kuzurura kwenye makao ya watu, au vijiwe..kuwa mtulivu, tafuta maeneo tulivu na omba.

3. ZUIA KINYWA.

Mfungo sio tu kujizuia kula na kunywa, bali pia kujizuia kuzungumza kupita kiasi…. Unapofunga si wakati wa kusema na kila mtu, si wakati wa kujiachia (hususani kwa watu wasio wa kiroho) bali ni wakati wa faragha wewe na Mungu wako (kwa kutafuta sauti ya Mungu kupitia maneno yake)

4. EPUKA MATENDO YA MWILI.

Kama ni mwanandoa jizuie kwa kiwango kikubwa au chote kukutana kimwili na mwenzi wako..Vile vile Kama unafanya shughuli fulani inayohusisha mwili wako, ipunguze kwa kiwango kikubwa..

5. PUNGUZA KIWANGO CHA KULA.

Mfungo sio kuhamisha mlo wa asubuhi na mchana na kuupeleka jioni..La! bali ni  kuunyima mwili ili roho yako ije juu (inufaike).. Maana yake wakati wa kufungua (kufuturu) usile kiwango kikubwa cha chakula, kwa kufidia mlo wa asubuhi na mchana.. Ukifanya hivyo utakuwa hutendi dhambi, lakini mfungo wako unaweza usiwe na matokeo makubwa kama wa yule ajizuiaye kweli kweli.

6.USILE VYAKULA VITAMU-TAMU.

Wakati wa kufungua epuka kula vyakula vitamu tamu, hususani vile unavyovipenda sana, ambavyo vinakuburudisha sana.. “Kumbuka tena mfungo ni kuunyima mwili na si kuupendeza mwili”… Sasa unapoupa vile vitu ambavyo unavipenda sana, hapo bado kuna kaukasoro katika mfungo wako..

Danieli alikuwa ni mtu aliyejinyima vitu vitamu wakati wa mfungo… na hatimaye mfungo wake ukawa na matokeo makubwa.

Danieli 10:2 “Katika siku zile mimi, Danielii, nalikuwa nikiomboleza muda wa majuma matatu kamili.

3 Sikula chakula kitamu, wala nyama wala divai haikuingia kinywani mwangu, wala sikujipaka mafuta kabisa, hata majuma matatu kamili yalipotimia”.

7. USIWE MTU WA KUJITANGAZA.

Mathayo 6:16 “Tena mfungapo, msiwe kama wanafiki wenye uso wa kukunjamana; maana hujiumbua nyuso zao, ili waonekane na watu kuwa wanafunga. Amin, nawaambia, wamekwisha kupata thawabu yao.

17  Bali wewe ufungapo, jipake mafuta kichwani, unawe uso;

18  ili usionekane na watu kuwa unafunga, ila na Baba yako aliye sirini; na Baba yako aonaye sirini atakujazi”.

Mfungo unapaswa uwe siri hususani kwa watu walio wa nje (yaani wasiohusiana na wewe).. Kwa ndugu yako wa karibu sana, au mke au mume au watoto, mfungo wako ni ngumu kuwa siri kwao, kwasababu unaishi nao katika maisha ya kila siku (hata usipowaambia watafahamu tu)..Hivyo unaweza kuwashirikisha ikiwa lengo lako si upokee utukufu kutoka kwao.

Vile vile kiongozi wako wa kiroho, au mpendwa mwenzako (wa Imani moja na wewe) unaweza kumshirikisha mfungo wako (ikiwa lengo lako si kupata utukufu kutoka kwake) bali kupokea hamasa au kumhamasisha (Hilo ni jambo jema).

Lakini kama lengo lako ni wewe uonekane kwao ili utukuzwe, basi mfungo huo unaweza usizae matunda yale mtu anayoyategemea..

Bwana akubariki.

Washirikishe na wengine habari hizi njema kwa kushea

Ikiwa utapenda kupata msaada wa kumpokea Yesu maishani mwako bure, Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo chini ya makala hii.

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kupofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Kwa mawasiliano: +255789001312 au +255693036618

Bwana akubariki.

Mafundisho mengine:

Je unaruhusiwa kufanya tendo la ndoa ukiwa katika mfungo?

Kwanini tunafunga na kuomba?

KWARESMA IPO KIMAANDIKO?

JUMATANO YA MAJIVU NI TENDO LA KIMAANDIKO?

REKEBISHA YAFUATAYO ILI UCHUMI WAKO UKAE SAWA.

Rudi Nyumbani

Print this post