YAFAHAMU MAPENZI KAMILI YA MUNGU KWA MAADUI ZAKO.

YAFAHAMU MAPENZI KAMILI YA MUNGU KWA MAADUI ZAKO.

Haijalishi utaudhiwa na watu kiasi gani, haijalishi utakuwa na maadui wengi kiasi gani, lakini kamwe Mungu hawezi kuwachukia kama unavyowachukia wewe.

Jicho lako linavyowaona wewe ni tofauti na Mungu anavyowaona, wewe unatamani waangamizwe wapotee, lakini Mungu anatamani waokolewe. Wewe unatamani mabaya yawakute lakini Bwana Mungu anatamani watubu ili wasipatwe na mabaya. Ukiifahamu vyema tabia hiyo ya Mungu, utaacha kupoteza muda, kuwatakia shari maadui zako. Badala yake utawaombea Bwana azidi kuwapa neema watubu, na madhara yao yasikupate.

Lakini ukiwaombea kwa Mungu wafe!.utakuwa unapoteza muda, kwasababu kabla hawajawa maadui zako, Mungu alijua kuwa watakuja kuwa maadui zako na akawaumba hivyo hivyo.. angekuwa na hasira nao sana, kama ulizonazo wewe, angewaangamiza kitambo sana, au hata asingewaumba kabisa.

Kwahiyo mpaka unaona wameumbwa fahamu kuwa tayari ni mpango kamili wa Mungu wao wawepo duniani, na tena Mungu kawaumba kwasababu anawapenda.

Ni maneno magumu hayo lakini ndio ukweli.. Kama mtu fulani unamchukia kwasababu kakusengenya, na unatamani Mungu amwue, hayo maombi yako yatafika ukingoni!..kwasababu Mungu hatamwua kama unavyotaka wewe. Lakini ukitaka maombi yako yawe na nguvu ni heri uombe Bwana Mungu ampe roho ya kutubu, hapo utakuwa umeomba sawasawa na mapenzi yake.

Kama kuna mtu amekufanyia jambo baya, au anakufanyia mabaya yanayokuudhi sana. Na wewe ukaenda kuketi kuomba kwa Bwana Mungu kwamba amwue na kumpoteza kabisa, nataka nikuambie hayo maombi yako unapoteza muda. Kwasababu Bwana Mungu hakumuumba ili amwue, bali aifikilie toba na kubadilika… Ndio lengo lake!..kamwe huwezi kumfundisha Mungu ubaya.

Ezekieli 18: 23 “Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? Asema Bwana MUNGU; si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake, akaishi?”

2Petro 3:9b “….bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba”.

Mtu fulani kakuibia mali yako ambayo ni ya thamani, halafu unapiga magoti ukiomba kwamba Mungu amuue na kumuangamiza huko alipo, hayo maombi hayafiki popote. Maombi yenye tija na yanayompendeza Mungu, ni haya>>  “Bwana wasamehe kwa kuwa hawajui watendalo”.

Mtu fulani kakuendea kwa mganga ili upatikane na madhara fulani, na wewe unapiga magoti na kusema “Bwana waangamizwe na kufa kabisa, hata maiti zao zisionekane”..huku ukinukuu mstari huu katika agano la kale Kutoka 22: 18 “Usimwache mwanamke mchawi kuishi”. Mbona unapomfumania mkeo, au mumeo kwenye uzinzi hunukuu huu mstari wa Agano la kale na kuutumia??.

Kumbukumbu 22: 22 “Akifumaniwa mtu mume amelala na mwanamke aliyeolewa na mume, na wafe wote wawili, mtu mume aliyelala na mwanamke, na yule mwanamke naye; ndivyo utakavyoondoa uovu katika Israeli”.

Au sio Mungu mmoja aliyezungumza hayo maneno??… Kama ni Mungu mmoja aliyesema usimwache mwanamke mchawi kuishi, ndio huyo huyo aliyesema mtu akishikwa kwenye uzinzi awe mwanamke au mwanaume  sharti auawe, (tena amezungumza hayo kwa kinywa cha Nabii huyo huyo mmoja, Musa)..basi kwanini unachukua mstari mmoja na kuacha mwingine??.

Hivyo ni vyema kufahamu utendaji kazi wa Mungu katika agano la kale ni tofauti na utendaji kazi wake katika agano jipya..Katika agano la kale, kutokana na ugumu wa mioyo ya watu, watu walipewa ruhusa ya kuua wazinzi, kuua waabudu sanamu wote wanaoziabudu nje na kumwabudu Mungu wa Israeli, walipewa pia ruhusa ya kuwapiga kwa mawe wachawi, na watu wote wenye pepo waliokuwa wanaishi katika nchi, walipewa ruhusa ya kuua watu waliomlaani/kumtukana Mungu, walipewa ruhusa ya kuwatenga watu wenye ukoma n.k. Na hiyo yote ni kutokana na ugumu wa mioyo yao, na wala si kwasababu ulikuwa ni mpango kamili wa Mungu. Mpango kamili wa Mungu ulikuja kuletwa na Bwana Yesu pale aliposema..

Mathayo 5:21 “Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue, na mtu akiua, itampasa hukumu.

22 Bali mimi nawaambieni, Kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu; na mtu akimfyolea ndugu yake, itampasa baraza; na mtu akimwapiza, itampasa jehanum ya moto”.

Mathayo 5.38 “Mmesikia kwamba imenenwa, Jicho kwa jicho, na jino kwa jino;

39 Lakini mimi nawaambia, Msishindane na mtu mwovu; lakini mtu akupigaye shavu la kuume, mgeuzie na la pili.

40 Na mtu atakaye kukushitaki na kuitwaa kanzu yako, mwachie na joho pia.

41 Na mtu atakayekulazimisha mwendo wa maili moja, nenda naye mbili”.

Mathayo 5:43 “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako;

44 lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi,

45 ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki”.

Kwahiyo hakuna jino kwa jino katika Ukristo, wala hakuna kumpiga kwa mawe mtu yeyote anayefumaniwa katika uzinzi, wala hakuna kumuua mchawi yeyote, wala haturuhusiwi kuwachukia maadui zetu. Haja za mioyo yetu kwa Mungu, na sala zetu, ni kwamba Bwana atuepushe na madhara yote yanayoweza kufanywa na wao wanaotuchukia, na Bwana azifedheheshe kazi zao, ili mwisho wanapoona kuwa hazina madhara yoyote kwetu, watubu na kumfuata Mungu wetu sisi, hilo ndio lengo la kwanza la Mungu. Lakini si wafe katika dhambi zao hizo.

Kwahiyo huwezi kumfundisha Mungu uovu, yeye atabaki kuwa mkamilifu siku zote, anawaangazia jua lake waovu na wema, huwezi kumbadilisha yeye kuwa hivyo, hata uombe maombi ya namna gani, isipokuwa anachokitaka kwetu ni sisi kuwa kama yeye, tuwe na huruma kama yeye, tuwe wenye rehema kama yeye, tuwe wenye fadhili kama yeye, tuwe watakatifu kama yeye.

Mathayo 5:46 “Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?

47 Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo?

48 Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu”.

Bwana atubariki wote.

Kama hujampokea Yesu, jitafakari mara mbili unasubiri nini?. Injili si habari za kuburudisha kama tunazozisoma katika magazeti, bali ni ushuhuda, maana yake kila unapoisoma mahali au kuisikia mahali, inarekodiwa kuwa ulishawahi kuisikia, kwahiyo kama ukiipuuzia na kuiacha, na yule mwovu akaja kuchukua kile kilichopandwa ndani yako, kuna hatari kubwa sana itakayokukuta baada ya maisha haya.

Hivyo mpokee leo Kristo leo maishani mwako na wala usingoje kesho, kwasababu hujui yatakayozaliwa ndani ya siku moja, biblia inasema hivyo katika Mithali 27:1, na pia katafute ubatizo sahihi wa maji tele (Yohana 3:23) na kwa Jina la Yesu Kristo (Matendo 2:38),kama bado hujabatizwa ubatizo sahihi. Na Roho Mtakatifu atashuka juu yako kukuongoza katika kweli yote.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

VITA DHIDI YA MAADUI

MWANZO WA INJILI YA YESU KRISTO.

JE! UMEPOKEA KWELI ROHO MTAKATIFU?

CHUKIZO LA UHARIBIFU

Je! Kuna malaika wangapi mbinguni?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments