TUUTAFUTE UMOJA WA ROHO.

TUUTAFUTE UMOJA WA ROHO.

Umoja wa Roho Mtakatifu upo katika vifungo 7, ambavyo kama kanisa ni lazima tujifunge katika vifungo hivyo.

Lakini kabla ya kuvitazama hivi vifungo 7 vya Roho Mtakatifu, ni vizuri tuweke msingi kidogo kumhusu Roho Mtakatifu.

Biblia inatufundisha kuwa kuna Roho 7 za Mungu, ambazo ndizo zinazotajwa kama Macho 7 ya Mungu.

Ufunuo 5:6  “Nikaona katikati ya kile kiti cha enzi na wale wenye uhai wanne, na katikati ya wale wazee, Mwana-Kondoo amesimama, alikuwa kana kwamba amechinjwa, mwenye pembe saba na macho saba, AMBAZO NI ROHO SABA ZA MUNGU zilizotumwa katika dunia yote”

Vile vile inazitaja Roho hizi 7 kama TAA SABA ZA MUNGU, ikiwa na Maana kuwa hizo ndizo mwanga mbele ya kiti cha Enzi.

Ufunuo 4:5 “Na katika kile kiti cha enzi kunatoka umeme na sauti na ngurumo. NA TAA SABA ZA MOTO ZILIKIWAKA MBELE YA KILE KITI CHA ENZI, NDIZO ROHO SABA ZA MUNGU”.

Hii yote ikimaanisha kuwa Roho Mtakatifu anatenda kazi katika Nafasi zake 7, au hatua zake 7 katika kuwakamilisha watu wake, lakini haina maana kuwa Roho Mtakatifu wapo 7.

Kwa msingi huo basi twende tukazitazame jinsi anavyolikamilisha kanisa katika kifungo cha UMOJA katika hatua zake saba.

Tusome,

Waefeso 4:3 “ na kujitahidi kuuhifadhi UMOJA WA ROHO katika kifungo cha amani.

MWILI MMOJA, na ROHO MMOJA, kama na mlivyoitwa katika TUMAINI MOJA la wito wenu.

BWANA MMOJA, IMANI MOJA, UBATIZO MMOJA.

MUNGU MMOJA, naye ni Baba wa wote, aliye juu ya yote na katika yote na ndani ya yote”.

Tutazame moja baada ya nyingine:

1.MWILI MMOJA.

Mwili unaozungumziwa hapa ni Mwili wa Yesu, (Soma Waefeso 4:12 na Wakolosai 3:15), na Mwili huu unajengwa kupitia Vipawa na Karama ambazo Roho Mtakatifu ameziweka ndani yetu, ambapo kila mmoja ni kiungo ndani ya mwili huo.. Hivyo ili tuufikie umoja wa Roho kama kanisa ni lazima tuenende katika msingi huu kwamba kanisa linaongozwa katika karama za Roho Mtakatifu, na si itikadi, mapokeo au siasa.

1Wakorintho 12:13  “Kwa maana katika Roho mmoja sisi sote tulibatizwa kuwa mwili mmoja, kwamba tu Wayahudi, au kwamba tu Wayunani; ikiwa tu watumwa au ikiwa tu huru; nasi sote tulinyweshwa Roho mmoja.

14  Kwa maana mwili si kiungo kimoja, bali ni vingi”.

2. ROHO MMOJA.

Anaposema Roho mmoja, zipo roho nyingi, hata shetani naye ni roho.. ikiwa na maana kuwa ndani ya kanisa ni lazima tuwe na Roho mmoja anayezaa matunda yanayofanana kwa wote. Na matunda ya Roho ni yale yanayotajwa katika Wagalatia 5:22, kupitia hayo, tutakuwa tumekamilka katika kifungo cha pili cha Roho. Ndio maana biblia inatufundisha kuzichunguza roho, kwamaana zipo roho nyingi..

2Wakorintho 11:4 “Maana yeye ajaye akihubiri Yesu mwingine ambaye sisi hatukumhubiri, au mkipokea ROHO NYINGINE MSIYOIPOKEA, au injili nyingine msiyoikubali, mnatenda vema kuvumiliana naye”

3. TUMAINI MOJA

Tumaini linalozungumziwa hapa ni “Tumaini la Utukufu ujao”.. Kwamba kila aliyeokoka analo tumaini la kuingia katika utukufu wa Mungu ujao,(Mbingu mpya na nchi mpya). Hili ni tumaini ambalo Kanisa lazima liufikie, na si kila mmoja anaamini analoliamini, kwasababu wapo wengine wanaosema hakuna ufufuo, mtu akifa amekufa!, jambo ambalo ni kinyume kabisa na maandiko. Ufufuo upo, na watakatifu watafufuliwa na kuingia katika utukufu wa milele.

Wakolosai 1:26  “siri ile iliyofichwa tangu zamani zote na tangu vizazi vyote, bali sasa imefunuliwa kwa watakatifu wake;

27  ambao Mungu alipenda kuwajulisha jinsi ulivyo utajiri wa utukufu wa siri hii katika Mataifa, NAO NI KRISTO NDANI YENU, TUMAINI LA UTUKUFU”

4. BWANA MMOJA

Yupo Bwana mwingine (yesu mwingine), anayehubiriwa tofauti na yule wa kwenye maandiko matakatifu.

2Wakorintho 11:4 “Maana yeye AJAYE AKIHUBIRI YESU MWINGINE ambaye sisi hatukumhubiri, au mkipokea roho nyingine msiyoipokea, au injili nyingine msiyoikubali, mnatenda vema kuvumiliana naye”.

Yesu mwingine ni yule anayesema Mungu haangalii mwili anaangalia Roho, ni yule anayesema mchukie adui yako, n.k. Lakini yule halisi anasema Mwombee adui yako, waombeeni wale wanaowaudhi, na wasameheni wale wanaowaudhi (Mathayo 5:43).

5. IMANI MOJA

Imani moja ni sahihi ni ile inayosema mpatanishi kati ya Mungu na mwanadamu ni mmoja (naye ni YESU KRISTO), Lakini Imani nyingine inasema “watakatifu waliokufa pia wanaweza kuwa wapatanishi” hivyo wanaweza kutuombea…

1Timotheo 2:5  “Kwa sababu Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, Mwanadamu Kristo Yesu”.

Vile vile inasema, mwombezi wetu kwa Baba ni yeye mmoja Yesu Kristo ( 1Yohana 2:1) na wala hakuna mwingine, lakini Imani nyingine inasema waombezi wanaweza kuwa wengi mbinguni. Hivyo kanisa ni lazima lifikie umoja wa Imani ya kweli ya kwenye biblia, kwamba mpatanishi ni mmoja na mwombezi ni mmoja, ambaye ni Yesu Kristo, na wala hakuna mwingine wa kumsaidia.

6. UBATIZO MMOJA.

Ubatizo mmoja wa kimaandiko ni ule wa Maji mengi (Yohana 3:23) na kwa jina la Bwana Yesu Kristo (Matendo 2:38, Matendo 10:48, Matendo 19:5). Ni lazima kanisa lifikie huu umoja, na si kila mmoja kuamini ubatizo wake.

7. MUNGU MMOJA.

Mungu mmoja wa kweli  ni yule aliyeumba mbingu na nchi, ambaye ni Baba wa yote, aliyeko juu mbinguni na si sanamu, wala miti, wala wanadamu. Hivyo ni lazima ndani ya mwili wa Kristo wote tufikie umoja huu wa kumwamini na kumwabudu Mungu mmoja, na kuchanganya ibada na miungu mingine au sanamu.

Adui anafanya kazi kwa nguvu, kuuvunja UMOJA HUU WA ROHO, kwasababu anajua ndio NGUVU YA KANISA, anataka kuweka umoja wake mwingine wa kidunia ndani ya kanisa, na kuutafsiri kama ndio umoja wa roho. Hivyo hatuna budi kuwa makini na kuyaishi maandiko.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mada Nyinginezo:

JE UNAMHUBIRI KRISTO KATIKA KWELI YOTE?.

Roho Mtakatifu ni nani?.

NI KWASABABU YA YESU KRISTO.

TUMAINI NI NINI?

Dinari ni nini na Rupia ni nini (Mathayo 20:2,Ufunuo 6:6)

Rudi nyumbani

Print this post

JE NI KIKOMBE KIPI UTAKINYWEA SIKU ILE?

Rohoni vipo vikombe viwili ambavyo Mungu ameviandaa kwa wanadamu.

  1. Kikombe Cha kwanza kinajulikana kama kikombe Cha ghadhabu ya Mungu.
  2. Na kikombe Cha pili kama kikombe Cha baraka/ wokovu.

KIKOMBE CHA GHADHABU

Kama hufahamu, Mungu Huwa anajiwekea “akiba” ya hasira yake. Ikiwa na maana si mwepesi kutimiliza hasira yake Kwa haraka, Huwa anaikusanya na siku ikifika kipimo chake Kisha akaimimina hapo huwa hapana Rehema Tena. Ni kilio na kusaga meno!.

Soma

Nahumu 1:2-3

[2]BWANA ni Mungu mwenye wivu, naye hujilipiza kisasi; BWANA hujilipiza kisasi, naye ni mwingi wa hasira; BWANA hujilipiza kisasi juu ya adui zake, huwawekea adui zake akiba ya hasira.

[3]BWANA si mwepesi wa hasira, ana uweza mwingi, wala hatamhesabia mtu mwovu kuwa hana hatia kamwe; BWANA ana njia yake katika kisulisuli na tufani, na mawingu ni mavumbi ya miguu yake.

Mifano halisi ya hasira ya Mungu tunaiona kipindi Cha gharika, kipindi Cha sodoma na Gomora. Na ameahidi pia katika siku za mwisho ataleta hukumu hiyo Kwa ulimwengu mzima, na itatimilika yote katika lile ziwa la moto.(2Petro 3:7-5)

Utapata majibu Kwanini Leo,  Mungu anaonekana kama vile yupo kimya Kwanini uovu unaendelea hachukui hatua stahiki duniani, fahamu ni kwamba anangoja kipimo chake kijae, kikombe kijae ili waovu wanywe ghadhabu yake yote. Ndivyo alivyowaambia Ibrahimu kuhusu kuangamia Kwa wakaanani, alikuwa anasubiria uovu wao utumie (Mwanzo 15:16), na siku ilipofika Yoshua aliwaangamiza wote.

Hivyo mtu unapokuwa mwovu unakijaza kikombe Cha ghadhabu ya Mungu, Na kama dhiki kuu itakupita basi utakatana na kikombe hicho siku Ile ya hukumu, utakinywa Kwa kutupwa kwenye lile ziwa la moto.

Ufunuo wa Yohana 14:10

[10]yeye naye atakunywa katika mvinyo ya ghadhabu ya Mungu iliyotengenezwa, pasipo kuchanganywa na maji, katika kikombe cha hasira yake; naye atateswa kwa moto na kiberiti mbele ya malaika watakatifu, na mbele za Mwana-Kondoo.

KIKOMBE CHA BARAKA.

Lakini pia watakatifu nao Bwana anawawekea akiba ya Baraka na mema. Kwa maisha ya haki wanayoishi sasa hapa duniani, usidhani kuwa hayo mema unayotendewa ndio malipo stahiki Kutoka Kwa Mungu wako,hapana..Bwana anakijaliza kikombe Cha watakatifu na siku Ile tutakinywea na Yesu Kristo kule mbinguni kwenye Karamu ya Mwana kondoo. Haleluya.

Mathayo 26:27-29

[27]Akakitwaa kikombe, akashukuru, akawapa, akisema, Nyweni nyote katika hiki;

[28]kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.

[29]Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.

Hapo ndipo tutakapoona wema wote wa Mungu maishani mwetu. Tutakinywea kikombe hicho, tutamiminiwa thawabu na Raha isiyo na kifani. Hapo ndipo tutakapojua ni jinsi gani Mungu anavyotujali. Usikose mbingu ndugu, kosa vyote lakini Unyakuo usikupite.

Ndugu ukiona unamtumikia Mungu Leo huoni faida yoyote, kama vile huoni malipo yoyote, ,tambua kuwa Bwana anaona..anaweka tu akiba, utaipokea Raha siku Ile itakapofika.

Unapojitesa kuishi maisha ya haki, halafu unaona kama vile Mungu hakujali..usijidanganye kikombe unakijazilisha tu. Wakati wa kukinywea utafika.

Soma haya maneno ya faraja Mungu aliyoyatamka Kwa watu wake..

Malaki 3:13-18

[13]Maneno yenu yamekuwa magumu juu yangu, asema BWANA. Lakini ninyi mwasema, Tumesema maneno juu yako kwa namna gani?

[14]Mmesema, Kumtumikia Mungu hakuna faida; na, Tumepata faida gani kwa kuyashika maagizo yake, na kwa kwenda kwa huzuni mbele za BWANA wa majeshi?

[15]Na sasa twasema ya kwamba wenye kiburi ndio walio heri; naam, watendao uovu ndio wajengwao; naam, wamjaribuo Mungu ndio waponywao.

[16]Ndipo wale waliomcha BWANA waliposemezana wao kwa wao. Naye BWANA akasikiliza, akasikia; na kitabu cha ukumbusho kikaandikwa mbele zake, kwa ajili ya hao waliomcha BWANA, na kulitafakari jina lake.

[17]Nao watakuwa wangu, asema BWANA wa majeshi, katika siku ile niifanyayo; naam, watakuwa hazina yangu hasa; nami nitawaachilia, kama vile mtu amwachiliavyo mwanawe mwenyewe amtumikiaye.

[18]Ndipo mtakaporudi, nanyi mtapambanua kati ya wenye haki na waovu, na kati ya yeye amtumikiaye Mungu na yeye asiyemtumikia.

Bwana atupe macho ya kumwelewa yeye. Kijazilishe kikombe Cha wokovu wako. Ili siku Ile ushiriki mema yote.

Ubarikiwe.

Je umeokoka? Kama bado unasubiri Nini Leo usifanye hivyo. Ikiwa upo tayari kumgeukia Yesu na kumfanya mwokozi wa maisha Yako, akusamehe dhambi zako. Basi ni wewe tu kufungua moyo wako na kuikubali msamaha huo.Ikiwa upo tayari kufanya.hivyo basi fungua hapa Kwa mwongozo huo.

Bwana akubariki..

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mada Nyinginezo:

SIKU YA MAONYESHO MAKUU YA BWANA YESU, IPO KARIBU.

NIMEAZIMIA KUWAKUSANYA MATAIFA. NIPATE KUWAMWAGIA GHADHABU YANGU

UUNGU NI NINI? (1Petro 1:3-4)

KIKOMBE CHA GHADHABU YA MUNGU KINAJAA.

Kwanini Mungu aliwaagiza wana wa Israeli wasikisaze chakula?

IEPUKE GHADHABU YA MUNGU.

USIIHARIBU TABIA YAKO KWA MAZUNGUMZO YAKO.

Rudi nyumbani

Print this post

IFAHAMU FAIDA YA KUMKIRI KRISTO UKIWA HAPA DUNIANI.

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze biblia,

Bwana wetu Yesu alisema maneno yafuatayo…

Mathayo 10:32  “BASI, KILA MTU ATAKAYENIKIRI MBELE YA WATU, nami nitamkiri mbele za Baba yangu aliye mbinguni..”

Tunapomkiri Bwana Yesu hapa duniani tuna ahadi ya yeye kwenda kutukiri mbinguni mbele za Baba na Malaika lakini pia kuna faida ambayo tutaipata tukiwa hapa duniani kabla hatujafika kule mbinguni. Na moja ya faida hiyo ni ndio kama ile aliyoipata Mtume Petro, alipomkiri Bwana YESU katika usahihi wote mbele ya wote.

Tusome,

Mathayo 16:15  “Akawaambia, NANYI MWANINENA MIMI KUWA NI NANI?

16 Simoni Petro akajibu akasema, WEWE NDIWE KRISTO, MWANA WA MUNGU ALIYE HAI.

17 Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simoni Bar-yona; kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili, bali Baba yangu aliye mbinguni.

18 Nami nakuambia, WEWE NDIWE PETRO, NA JUU YA MWAMBA HUU NITALIJENGA KANISA LANGU; WALA MILANGO YA KUZIMU HAITALISHINDA.

19 Nami nitakupa WEWE FUNGUO ZA UFALME WA MBINGUNI; na lo lote utakalolifunga duniani, litakuwa limefungwa mbinguni; na lo lote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni”.

Umeona?.. Kabla tu ya Bwana Yesu kwenda kumkiri Petro mbele za Malaika watakatifu mbinguni, tayari alianza kumkiri akiwa hapa hapa duniani kabla ya kufika kule, kwamba..“YEYE NDIYE PETRO,… NA AKAMPA FUNGUO ZA UFALME WA MUNGU”…kila atakalolifunga duniani litakuwa limefungwa mbinguni na atakalolifungua duniani litakuwa limefunguliwa mbinguni.

Na sisi tunapomkiri Yesu kisahihi mbele za watu, tunaanza kuvuna matunda yake tukiwa hapa hapa duniani,….vile vile tunaposhuhudia habari zake kisahihi mbele za watu, na kumtangaza kama jinsi anavyotaka, faida yake tunaanza kuipata tukiwa hapa hapa duniani kabla ya kufika kule mbinguni,.. majina yetu yanabadilishwa katika ulimwengu wa roho tukiwa hapa hapa duniani, tunapewa mamlaka nyingine ya kipekee, na funguo za mambo mengi.

Je! Umemkiri Yesu katika maisha yako? (Kumbuka Kristo hatumkiri kwa moyo, bali kwa Kinywa).. Ikiwa na maana kuwa ni lazima tuhusishe vinywa vyetu na sauti zetu katika kumkiri yeye.

Warumi 10:10 “Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na KWA KINYWA HUKIRI HATA KUPATA WOKOVU”.

Je unamtangaza Bwana Yesu mbele za watu?..

Kama bado hujafanya hayo yote, ni vizuri ukafanya maamuzi leo, kwa faida yako mwenyewe ya hapa duniani na katika ulimwengu ujao…Lakini ukimwonea haya naye pia atakuonea haya kuanzia hapa hapa duniani, kabla ya kufika kule mbinguni.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mada Nyinginezo:

USIISHIE TU KUPATA HAKI, BALI PATA NA WOKOVU.

MFALME ANAKUJA.

BADO UPO YERUSALEMU TU..GALILAYA HUTAKI KWENDA?

NJIA YA WOKOVU NDANI YA KITABU CHA WARUMI.

Biblia inaposema “Wote tumetenda dhambi” si inamaanisha hakuna mtakatifu duniani?

Rudi nyumbani

Print this post

Chetezo ni nini katika biblia? (Walawi 10:1)

Chetezo ni kifaa/chombo kidogo kilichotumika katika tendo la kuvukiza uvumba ndani ya Hema ya Mungu au katika hekalu la Mungu. (Tazama picha juu).

Wakati kuhani alipotaka kufanya kazi za kikuhani ndani ya hema/hekalu la Mungu. Kabla ya mambo yote ilikuwa ni lazima avukize uvumba ndani ya hema/hekalu, lengo la kufanya vile ni kukijaza chumba chote moshi wa ule uvumba.

Hivyo alitwaa kozi mbili za makaa ya moto ambayo yalikuwa yanapatikana katika madhabahu ndogo (ijulikanayo kama madhabahu ya uvumba), iliyokuwa inapatikana upande wa kushoto wa patakatifu pa patakatifu.

Na akiisha kuyachukua yale makaa, ndipo anayatia ndani ya hiko chetezo pamoja na manukato yenye kutoa harufu nzuri yaliyotengenezwa kwa viungo maalumu alivyoviagiza Mungu mwenyewe…

Kutoka 30:34 “BWANA akamwambia Musa, Jitwalie manukato mazuri, yaani, NATAFI, NA SHEKELETHI, NA KELBENA; VIUNGO VYA MANUKATO VIZURI PAMOJA NA UBANI SAFI; vitu hivyo vyote na viwe vya kipimo kimoja;

35 nawe utafanya uvumba wa vitu hivyo, manukato ya kazi ya ustadi wa mtengenezaji manukato, yatakuwa yamekolea, safi, matakatifu”.

Na baada ya kuhani, kuvichoma viungo hivyo (manukato) pamoja na yale makaa ndipo moshi huo huo wenye harufu nzuri hupanda juu na kukijaza chumba chote, na hivyo Mungu hushuka kuipokea ibada hiyo. (Tendo hilo ndilo linaloitwa kuvukiza uvumba).

Ilikuwa ni kosa kubwa kufanya kazi ya kikuhani bila kuvukiza uvumba kwanza, vile vile ilikuwa ni kosa kubwa kuhani kutumia viungo vingine katika manukato au moto mwingine mgeni tofauti na ule wa madhabahuni katika zoezi la kuvukiza uvumba..(Soma Kutoka 30:9, Hesabu 3:4).

Kwa mapana zaidi kuhusu Kuvukiza uvumba fungua na ujumbe gani umebeba kiroho fungua hapa >>> KUFUKIZA UVUMBA NDIO KUFANYAJE?

Swali ni je katika agano jipya tuna amri/agizo la kufukiza uvumba katika nyumba za Ibada kama makuhani walivyofukiza katika nyumba ya Mungu katika agano la kale?

Jibu ni la!.. Katika agano jipya hatuna amri wala agizo hilo, kwasababu agano letu si tena la mwilini bali la rohoni, kama vile tusivyozitumia tena damu za wanyama katika ondoleo la dhambi bali damu ya YESU vile vile, hatuvukizi tena uvumba kwa namna yakimwili bali uvumba wetu sisi ni “maombi”.

Sasa CHETEZO kinawakilisha nini kiroho?.

“Chetezo” inawakilisha “moyo wa mtu” kama vile moto unavyowekwa ndani ya chetezo na uvumba kuvukizwa juu ndipo utukufu wa Bwana uonekane…Vivyo hivyo na sisi ni lazima Moto wa Roho Mtakatifu uwashwe ndani yetu na ndipo tuweze kumtumikia Mungu na kuomba sawasawa na mapenzi yake, kwa maana ule uvumba katika nyumba ya Mungu ni ufunuo wa maombi ya watakatifu katika agano jipya. (Ufunuo 8:3).

Je Moyo wako umeufanya safi?.. Biblia inasema tulinde mioyo yetu zaidi ya vyote tuwezavyo kuvilinda (Mithali 4:23).

Bwana atubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mada Nyinginezo:

SISI TU MANUKATO YA KRISTO.

MADHABAHU NI NINI?

USICHELEWE KUMPAKA BWANA MARHAMU!

MUNGU HATAZAMI MOTO WA KIGENI,KUWA MAKINI!

Marhamu ni nini? Na Manukato ni nini?

Rudi nyumbani

Print this post

UTAIKUZAJE IMANI NDANI YAKO?

Jina la Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo, lihimidiwe daima.

Karibu katika darasa hili fupi la biblia?

Je unajua imani inafananishwa na nini? Na je unajua ni kitu gani kinachoikuza Imani?.

Majibu ya maswali haya tutayapata ndani ya biblia…

Bwana Yesu aliifananisha imani na chembe ndogo ya Haradali, Chembe ya Haradali au kwa lugha nyingine punje ya Haradali ni mbegu inayotoa mmea unaoitwa Haradali.

Luka 17:6 “Bwana akasema, Kama mngekuwa na imani KIASI CHA CHEMBE YA HARADALI, mngeuambia mkuyu huu, Ng’oka, ukapandwe baharini, nao ungewatii”

Hapa Bwana anaifananisha imani na chembe ya Haradali, na anasema mtu akiwa nayo kwa kiasi hicho tu!, Tayari anaweza kufanya makubwa.

Sasa mtu anawezaje kufanya makubwa akiwa na chembe hiyo ya Haradali?. Hilo ndio swali la kujiuliza.

Wengi tunaishia kuitafakari tu ile chembe ya Haradali kwa udogo wake basi na si kwa upana wake,
Lakini hebu leo tutafakari kwa undani hii chembe ya Haradali na muujiza uliopo ndani yake.

Lakini awali ya yote tuweke msingi kwa kuutafakari mfano ufuatao…Tengeneza picha mkulima anakwambia ukiwa na punje moja ya indi, waweza kulisha watu mia.. Je kwa kusema hivyo atakuwa amemaanisha lile indi moja laweza kushibisha watu wote hao?.

Jibu ni la! Ni wazi kuwa indi moja haliwezi kushibisha umati wa watu mia, bali atakua amemaanisha kuwa endapo ukiichukua ile mbegu moja ya indi, ukaipanda yaweza kuzaa mahindi mengi ambayo yaweza kushibisha umati mkubwa wa watu.

Vivyo hivyo Bwana Yesu aliposema “Imani kama chembe ya Haradali yaweza kuhamisha milima na mikuyu” ..hakumaanisha ile mbegu kama mbegu bali matokeo ya ile mbegu, ndio maana hakuifananisha imani na chembe ya mchanga isiyozaa bali chembe ya Haradali iliyo hai na inayozaa..

Sasa ili tuelewe vizuri, tusome maandiko yafuatayo…

Marko 4:30 “Akasema, Tuulinganishe na nini ufalme wa Mungu? Au tuutie katika mfano gani?

31 NI KAMA PUNJE YA HARADALI, ambayo ipandwapo katika nchi, ingawa ni ndogo kuliko mbegu zote zilizo katika nchi,

32 lakini ikiisha kupandwa hukua, ikawa kubwa kuliko miti yote ya mboga, ikafanya matawi makubwa; hata ndege wa angani waweza kukaa chini ya uvuli wake”.

Umeona muujiza uliopo ndani ya punje ya Haradali?…kwamba inaanza kama mbegu ndogo tena dhaifu na kisha inapokua kubwa huzidi mboga zote na miti yote na kufanya matawi makubwa ambayo ndege waweza kukaa chini yake.

Kwahiyo kumbe Imani inayofananishwa na chembe ya Haradali, inahitajika kupandwa kwanza katika nchi, na kupaliliwa na kumwagiwa maji, ili iweze kuwa mti mkubwa utakaoweza kutoa matunda na hata kuwa tegemezi kwa viumbe wengine, lakini ikibaki katika hali ile ile haizai kitu, ni sawa na imekufa..kama maandiko yanavyosema…

Yakobo 2:17 “Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake”.

Sasa swali Imani inapaliliwaje na inamwagiwaje maji, ili ikue na kuleta matokeo makubwa.

Tusome Mathayo 17:20-21.

Mathayo 17:20 ” Yesu akawaambia, Kwa sababu ya upungufu wa imani yenu. Kwa maana, amin, nawaambia, Mkiwa na imani kiasi cha punje ya haradali mtauambia mlima huu, Ondoka hapa uende kule; nao utaondoka; wala halitakuwako neno lisilowezekana kwenu.

21 [LAKINI NAMNA HII HAITOKI ILA KWA KUSALI NA KUFUNGA.]

Umeona mwisho hapo?.. anasema, namna hii haitoki isipokuwa kwa KUSALI na KUFUNGA.

Kumbe KUSALI na KUFUNGA ndio kanuni ya kukuza Imani,…..kumbe Kufunga na kusali ndiko kuipalilia na kuinyeshea Imani ili Ikue, na mtu akiendelea kwa kanuni hiyo, kwa kitambo fulani basi ile imani ndani yake itakua yenyewe na baadaye atatoa matokeo makubwa kwa kila anachokihitaji.

Mtu aliyeipalilia imani yake hatatumia nguvu nyingi kupata jambo, kwa maana Imani yake ni imara na thabiti.. Ile punje ya Haradali ndani yake imegeuka kuwa mti mkubwa usiotikisika.

Ndio maana watu waliojaa maombi na mifungo, wachawi hawawatesi wala hawana hofu na hatari yoyote, kwanini??..Kwasababu tayari imani yao imejengeka ndani yao.

Je na wewe unataka imani yako ikue?…basi usikwepe Mifungo, vile vile usikwepe maombi..Ikiwa utahitaji mwongozo wa maombi ya kukua kiroho ya kila wiki basi wasiliana nasi inbox na tutakusaidia kwa hilo, na vile vile kama utapenda kuungana nasi katika ratiba zetu za mifungo waweza kuwasiliana nasi inbox ili tuweze kukupa utaratibu.

Bwana akubariki.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mada Nyinginezo:

MSHAHARA WA DHAMBI:

UTAONA MAMBO MAKUBWA KULIKO HAYA.

MKAMCHUKUE SALAMA.

NINI TOFAUTI KATI YA MATENDO YA SHERIA NA MATENDO YA IMANI?

NGUVU YA UPENDO WA KRISTO.

Rudi nyumbani

Print this post

JE UNAMHUBIRI KRISTO KATIKA KWELI YOTE?.

(Masomo maalumu kwa watumishi wa Mungu).

Kama Mtumishi wa Mungu je unamhubiri Kristo katika Kweli yote?.

Ni rahisi kutamani na kutafuta Ishara kama njia KUU ya Kumhubiri Kristo, lakini nataka nikuambie kama utatafuta ishara halafu umeacha kumhubiri Yesu Kristo katika kweli yote, hiyo kwako ni hasara kubwa sana?

Hebu tumtazame mtu mmoja ambaye hakufanya ishara hata moja lakini alimzungumzia Kristo katika kweli yote na hiyo ikafanya kazi yake kuwa kubwa sana mbele za Mungu,…na mtu huyo si mwingine Zaidi ya Yohana Mbatizaji.

Yohana 10:40  “Akaenda zake tena ng’ambo ya Yordani, mpaka mahali pale alipokuwapo Yohana akibatiza hapo kwanza, akakaa huko.

41  Na watu wengi wakamwendea, wakasema, YOHANA KWELI HAKUFANYA ISHARA YO YOTE, LAKINI YOTE ALIYOYASEMA YOHANA KATIKA HABARI ZAKE HUYU YALIKUWA KWELI.

42  Nao wengi wakamwamini huko”

Umeona? Yohana hakufanya ishara hata moja, hakutoa pepo, hakuponya mtu kwa jina la Bwana, hakushusha moto kama Eliya ingawa roho ya Eliya ilikuwa juu yake,  wala hakutembea juu ya maji ili watu waone waamini…. lakini Yote aliyoyasema kumhusu Yesu na ujio wake yalikuwa kweli, wala hakudanganya!..  Hivyo hiyo ikamfanya awe Nabii mkuu Zaidi hata ya Musa na Eliya na manabii wengine wote waliotangulia.

Luka 7:26  “Lakini, mlitoka kwenda kuona nini? Nabii? NAAM, NAWAAMBIA, NA ALIYE ZAIDI YA NABII.

27  Huyo ndiye aliyeandikiwa haya, Tazama, namtuma mjumbe wangu Mbele ya uso wako, Atakayeitengeneza njia yako mbele yako.

28  Nami nawaambia, KATIKA WALE WALIOZALIWA NA WANAWAKE HAKUNA ALIYE MKUU KULIKO YOHANA; lakini aliye mdogo katika ufalme wa Mungu ni mkuu kuliko yeye”.

Huyo ni mtu ambaye hakufanya ishara yoyote! Lakini alimzungumzia Kristo katika KWELI YOTE!.. Kwahiyo kumbe kinachojalisha ni KWELI YOTE na si Miujiza wala ishara, wala umaridadi wala utashi!, bali KWELI YOTE!.

Je wewe kama Mtumishi wa Mungu, unahubiri madhara ya dhambi na hukumu ijayo?, au unahubiri tu mafanikio na kutoa pepo?.. Je unahubiri pia Ubatizo wa maji na wa Roho Mtakatifu au unahubiri tu upendo na faraja?.. Je unahubiri juu ya unyakuo na ziwa la moto, au unahubiri tu Amani?.. Ni Vyema kuhubiri yote pasipo kuacha hata moja, na hapo tutakuwa tumemhubiri Yesu katika kweli yote.

Epuka injili za kubembeleza na kuwastarehesha watu katika dhambi, Yohana Mbatizaji alihubiri na kusema…

Luka 3:7 “Basi, aliwaambia makutano ya wale waliomwendea ili awabatize, Enyi wazao wa nyoka, ni nani aliyewaonya ninyi kuikimbia hasira itakayokuja?

8  BASI, TOENI MATUNDA YAPATANAYO NA TOBA; WALA MSIANZE KUSEMA MIOYONI MWENU, TUNAYE BABA, NDIYE IBRAHIMU; KWA MAANA NAWAAMBIA YA KWAMBA KATIKA MAWE HAYA MUNGU AWEZA KUMWINULIA IBRAHIMU WATOTO.

9  NA SASA HIVI SHOKA LIMEKWISHA KUWEKWA PENYE MASHINA YA MITI; BASI KILA MTI USIOZAA MATUNDA MAZURI HUKATWA NA KUTUPWA MOTONI”.

Bwana Yesu atusaidie.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

NI INJILI GANI UNAHUBIRI?

MADHARA YA KUTAFUTA ISHARA.

TOFAUTI YA UBATIZO WA YOHANA NA UBATIZO WA BWANA YESU

SAUTI NYUMA YA ISHARA.

NI NINI BWANA ANATAKA KUTOKA KATIKA MUUJIZA ALIOKUFANYIA?

Rudi nyumbani

Print this post

Je! Habari iliyo katika 1Nyakati 21:25, na 2Samweli 24:24, ya Daudi kununua kiwanja  inajichanganya?

SWALI:  Ni ipi gharama sahihi ambayo Daudi aliilipia, kununulia shamba la Arauna, kwa ajili ya kumjengea Mungu hekalu. Je! Ni shekeli 600, au shekeli 50?. Je! Biblia inajichanganya.

JIBU:  Tusome,

2Samweli 24: 24 Lakini mfalme akamwambia Arauna, La, sivyo; lakini kweli nitavinunua kwako kwa thamani yake; wala sitamtolea Bwana, Mungu wangu, sadaka za kuteketezwa nisizozigharimia. Hivyo Daudi akakinunua hicho kiwanja cha kupuria na wale ng’ombe kwa shekeli hamsini za fedha.  25 Naye Daudi akamjengea Bwana madhabahu huko, akatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. Basi Bwana aliiridhia nchi, na tauni ikazuiliwa katika Israeli.

1Nyakati 21:25 “Basi Daudi akampimia Arauna thamani ya mahali pale shekeli mia sita za dhahabu kwa uzani  26 Kisha Daudi akamjengea Bwana madhabahu huko, akatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani, akamlingana Bwana; naye akamwitikia kutoka mbinguni kwa moto juu ya madhabahu hiyo ya sadaka ya kuteketezwa”

Vifungu hivyo havijichanganyi,  vyote vipo sahihi. Mwandishi wa kitabu cha Samweli anaeleza lile eneo ambalo lilikuwa ni la kupuria tu, pamoja na wale ng’ombe gharama zake jumla ndio shekeli hamsini, lakini sio eneo lote la kiwanja. Tukirudi kwenye 1Nyakati mwandishi anaeleza sasa eneo lote, anatumia neno “mahali pale”. Kwamba jumla yake yote ni shekeli mia sita. Gharama zote za mahali pale zilikuwa ni shekeli 600

Kwamfano wewe unaweza ukawa umelenga kupanunua mahali Fulani kwa ajili ya shughuli zako za kimaendeleo. Lakini ikakugharimu ununue sehemu yote ili uweze kupamiliki vizuri na pale. Hivyo kama eneo lile tu moja gharama yake ilikuwa milioni 1, Lakini kwasababu ya kulipia fidia kwa watu kando kando kuwahamisha, na kodi, na ukarabati n.k. unajikuta unaenda mpaka milioni 20.

Ndicho kilichomkuta Daudi.

Kwahitimisho ni kuwa vifungu hivyo vipo sahihi havijichanganyi.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

Swali: Je idadi ya askari waliohesabiwa katika 1Nyakati 21:5 na 2Samweli 24:9 inajichanganya?.

Biblia inamaana gani iliposema “Dhambi ilipozidi, Neema ilizidi kuwa nyingi Zaidi”.

KWANINI YESU KRISTO NI MWANA WA DAUDI?

NI KWANINI WATU WENGI WANASHINDWA KUMWELEWA MUNGU?

Je Kauli ya Mungu katika Warumi 11:4 na 1Wafalme 19:18 inajichanganya?.

Je! Wamwona mtu mwenye bidii katika kazi zake?

Novena ni nini? Na je ipo kibiblia?

Rudi nyumbani

Print this post

VUNJA AGANO LA MAUTI.

Mtu anaingiaje agano na mauti?

“Agano” kwa jina lingine ni “Mkataba”

Mtu anapoingia mkataba na mtu mwingine ni sawa na kaingia agano na mtu huyo.

Sasa mwanadamu pia anaweza kuingia Agano na Mauti, Ndivyo biblia inavyotufundisha kuwa mtu anaweza kuingia agano na Mauti na kuingia katika mapatano na kuzimu.

Isaya 28:18 “Na agano lenu mliloagana na mauti litabatilika, tena mapatano yenu mliyopatana na kuzimu hayatasimama; pigo lifurikalo litakapopita, ndipo ninyi mtakapokanyagwa nalo”.

Na kama mtu ameingia Agano na Mauti ni lazima mauti itakuwa na nguvu juu yake,itamwandama popote anapokwenda na itampata..hivyo ni lazima hilo agano livunjwe ili mtu huyo abaki huru, na uzima utawale ndani yake,

Sasa kinachomwingiza mtu katika agano la Mauti ni nini?..je ni ndoto anazoziota?, Au ni wachawi?, Au wanadamu?..

Jibu: Si wanadamu, wala wachawi, wala ndoto mtu anazoota bali ni “dhambi ndani ya mtu”…Biblia inasema “Mshahara wa dhambi ni Mauti”.

Warumi 6:23 “Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti; bali karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu”.

Sasa hapo hasemi “matokeo ya dhambi ni mauti” bali “mshahara wa dhambi ni mauti”.

Maana yake mtu anayefanya dhambi ni sawa na mtu anayefanya kazi za kumpatia mshahara..Kwamba ni lazima atakuwa na mkataba wa kazi (yaani agano la kazi) ili apokee mshahara.

Halikadhalika na mtu anayefanya dhambi, anakuwa kwanza ameingia agano na hiyo dhambi na ndipo anapokea mshahara wake baada ya kuitendea kazi, na mshahara wake ndio “Mauti”.

Kwahiyo kumbe Agano la Mauti ni “dhambi”..Ikiwa na maana kuwa mtu akiondoa dhambi katika maisha basi atakuwa amelivunja hilo agano la Mauti lililo ndani yake!.

Kumbe mtu anayeabudu sanamu tayari yupo katika agano na mauti, kumbe mtu anayezini tayari kashaingia agano/mkataba na mauti, Kumbe mtu anayeiba tayari yupo katika agano na mauti?, Na kwamba siku yeyote atakumbana na Mauti ya mwili na roho, na hatimaye kutupwa katika ziwa la moto ambako huko kuna mauti ya pili. (Ufunuo 20:14 na 21:8)

Sasa hili agano la Mauti tunalivunjaje?…je ni kwa kuwekewa mikono na watumishi?, Au kwa kunywa maji na mafuta yajulikanayo kuwa ya upako?, Au kwenda kukemea hayo maagano?

Jibu la swali hili hatulipati pengine popote isipokuwa kwenye biblia.

Matendo 2:38 “Petro akawaambia, TUBUNI MKABATIZWE KILA MMOJA KWA JINA LAKE YESU KRISTO, MPATE ONDOLEO LA DHAMBI ZENU, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu”.

Umeona kanuni ya Kuondoa dhambi?…si kwa kupakwa mafuta, au kuwekewa mikono kichwani…bali ni kwa KUTUBU NA KUBATIZWA.

Unapotubu kwa kumaanisha kabisa kuacha dhambi basi unapokea msamaha na papo hapo na lile agano la Mauti linavunjika!..sawasawa na maandiko hayo ya Isaya 28:18,

Isaya 28:18 “Na agano lenu mliloagana na mauti litabatilika, tena mapatano yenu mliyopatana na kuzimu hayatasimama; pigo lifurikalo litakapopita, ndipo ninyi mtakapokanyagwa nalo”.

Lakini kama hakuna toba halisi na ubatizo basi agano la mauti bado lipo palepale..halijavunjika! Haijalishi mtu huyo atawekewa mikono na watumishi wangapi, au ataombewa na watu wangapi, au anaabudu dhehebu kubwa kiasi gani..kama bado hataki kuacha dhambi, zinazotajwa katika Wagalatia 5:19…basi Mauti bado ipo pale pale.

Tubu leo na Agano la Mauti litabatilika juu yako, kile kifo ambacho ulikuwa umekiona kimekukaribia kitapelekwa mbali nawe.. Na hakikisha toba yako inaendana na matendo, kama umetubia wizi, au uzinzi, au uchawi au jambo lingine lolote hakikisha kuanzia siku hiyo hurudii tena hayo..(Unafanyika kiumbe kipya).

Bwana atusaidie.
Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

Je Adamu na Hawa, walikuwa hawafanyi mema kabla ya kula tunda?

Tofuati kati ya kifo na mauti ni ipi?

DHAMBI YA MAUTI

MSHAHARA WA DHAMBI

Wote wanaokumbwa na mauti sasa ni kutokana na dhambi zao?

Rudi nyumbani

Print this post

Novena ni nini? Na je ipo kibiblia?

Jibu: Neno “Novena” limetokana na neno la kilatini “Novem”… lenye maana ya “Tisa”(9). Madhehebu baadhi ikiwemo Katoliki na Orthodox yamelitoa neno hili na kulitumia katika aina Fulani ya mfululizo wa sala kwa kipindi cha siku 9.

Sala hizo zinahusisha kuomba kwaajili ya  jambo fulani au kushukuru, na zinahusisha ibada za kuomba Rozari kwa wakatoliki (jambo ambalo si sahihi kibiblia). Na kwanini kusali Rozari sio agizo la biblia?, fungua hapa kwa maelezo Zaidi >>>JE SALA YA ROZARI TAKATIFU NI YA KIMAANDIKO?

Sasa msukumo wa kuomba Novena, (yaani siku 9) mfululizo umetokana na matukio maalumu yanayotokea baada ya siku 9, au miezi 9 kumalizika. Kwamfano utaona kabla ya Pentekoste kutimia, walikusanyika Mitume na watu wengine baadhi mahali pamoja kuomba, na wakaomba kwa muda wa siku 9, baada ya Bwana Yesu kupaa na siku ya 10 ikawa ni Pentekoste.

Hivyo ushawishi huu wa kupokea Roho Mtakatifu baada ya maombi ya siku 9, ukaaminika na madhehebu hayo kubwa ni lazima uendelee ili kupokea kitu kingine mfano wa hicho kutoka kwa Mungu, vile vile mwanamke anajifungua mtoto baada ya miezi 9, hili nalo likawafanya viongozi wa madhehebu haya kuamini kuna kitu katika 9, (novena).

Sasa swali ni je! Biblia imetuagiza kutumia mfumo wa Novena, katika maombi ili kupokea jambo maalumu kutoka kwa Mungu? Kwamba tuwe na maombi maalumu ya kurudia rudia kwa muda wa siku 9 ili tupokee jambo kutoka kwa Mungu?.

Jibu ni la!.

Biblia haijaagiza mahali popote tusali “Novena” kwamba tuwe na kipindi Fulani maalumu cha siku 9 mara kwa mara ili Mungu aachilie kitu juu yetu. Utaratibu huu umetengenezwa na wanadamu, kufuatia ushawishi wa siku ya Pentekoste. Hivyo kama umetengenezwa na wanadamu, hauwezi kuwa Sharti, au Agizo la lazima kwa wakristo, kwamba usipofanya hivyo ni kosa kibiblia!.

Agizo hili linaweza kuwa la binafsi, kama tu vile mfungo usivyokuwa sharti, ni jinsi mtu atakavyosukumwa na kuongozwa kufunga!.

Lakini mbali na hilo hata kama Novena ingekuwa ni agizo la biblia, bado inavyofanyika na madhehebu baadhi ikiwemo Katoliki, bado haifanyiki sawasawa na maandiko.. Kwasababu katika biblia tunaona kabla ya Pentekoste walikuwa wamekusanyika mahali pamoja wakisali, wakimwomba Mungu na Mariamu mama yake Yesu alikuwemo miongoni mwao, naye pia akimwomba Mungu, na hawakuwa na sanamu ya mtakatifu Fulani aliyetangulia kufa!, bali walikuwa wakimwomba Mungu aliye juu, (Matendo 1:12-14)

Lakini leo hii katika sala hizo za Novena ni kinyume chake!, wanaoombwa ni watakatifu waliokufa ikiwemo Maria mwenyewe, jambo ambalo ni kinyume kabisa na maandiko!, hivyo badala ziwe sala za Baraka, zinageuka na kuwa ibada za sanamu! (Bwana Yesu atusaidie sana!!).

Kwahiyo kwa hitimisho ni kwamba Novena haipo kibiblia,..kama mtu atajiwekea utaratibu wake binafsi wa kusali Novena, na sala hiyo ikawa ni kulingana na Neno la Mungu, isiyohusisha sanamu wala desturi za kipagani basi hafanyi dhambi!, huenda ikawa bora kwake.

Lakini inapogeuka na kuwa sharti, na tena ikahusisha ibada za sanamu basi inakuwa ni machukizo makubwa mbele za Bwana kulingana na maandiko.

Bwana atusaidie!.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mada Nyinginezo:

SALA YA BWANA. (Namna ya kuiomba)

Ni lazima mtu aongozwe sala ya toba ili awe ameokoka?

SALA YA UPONYAJI/MAOMBI YA UPONYAJI.

Kuna tofauti gani kati ya SALA na DUA?

Ni lazima mtu aongozwe sala ya toba ili awe ameokoka?

Rudi nyumbani

Print this post

Kuomba katika roho ni kupi? na je nifanye nini ili niweze kuomba hivyo?

Neno hilo utalisoma katika vifungu hivi;

Waefeso 6:18  kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote

Yuda 1:20  Bali ninyi, wapenzi, mkijijenga juu ya imani yenu iliyo takatifu sana, na kuomba katika Roho Mtakatifu

Watu wengi wanaamini kuomba katika Roho ni kuomba kwa “kunena kwa lugha tu”. Nje ya hapo sio kuomba kwa Roho. Lakini tukiwa na mtazamo huo basi tutakuwa na uelewa finyu kuhusu Roho Mtakatifu.

Ukweli ni kwamba hiyo ni namna mojawapo kati ya nyingi ambazo Roho wa Mungu anamjalia mtu kuomba.

Maana ya ‘kuomba katika Roho’ Ni kuomba ‘ndani ya Roho ya Mtakatifu/ ndani ya utaratibu/ uwepo wa Roho Mtakatifu’. Na hiyo ni zaidi ya kunena kwa lugha, Hii ikiwa na maana Mtu anaweza kuomba lakini asiwe katika uwepo huo. Na matokeo ya hivyo ni maombi kuwa makavu sana, yasiyo na nguvu.

Sasa mstari mama unaotufundisha juu ya uombaji wa Roho Mtakatifu ni huu;

Warumi 8:26  “Kadhalika Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo, lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa KUUGUA KUSIKOWEZA KUTAMKWA”

Hapo anasema “kuugua kusikoweza kutamkwa” . Maana ya kuugua hapo ni kuweka uzito, au presha, au shauku  ya kuomba ndani ya mtu isiyokuwa ya kawaida. Tofauti na angejitahidi kwa nguvu zake yeye mwenyewe. Sasa mtu akifikia hatua hiyo, basi tayari kuanzia huo wakati anaomba katika Roho hata kama maneno yake ni ya kawaida anayoyatumia. Maombi hayo yana nguvu na yanasikika sana mbele za Mungu.

Kwamfano, ndio hapo utakuta mtu anaomba, lakini mara anasikia kububujika machozi ndani yake, mwingine anazidi kuona kiu ya kuendelea kuombea jambo lile lile kwa muda mrefu tofauti na sikuzote. Mfano wakati ule Bwana Yesu alipokuwa Gethsamane anaomba.

mwingine anajisikia wepesi usio wa kawaida, uchovu wote umeondoka ijapokuwa alikuwa amechoka sana, anaanza furahia maombi, anafurahia kuendelea kubaki palepale muda mwingi kuendelea kuomba,

Sasa hali kama hizi ukizifikia, ujue tayari umeshazama katika Roho, umeshawezeshwa na Roho, maombi yako yanakuwa na nguvu sana,

Mwingine anasikia raha Fulani moyoni, akiwa anaomba, mwingine ndio anazama katika kunena kwa lugha (kwa kusukumwa na Roho), na sio kwa akili. Mwingine anasindikizwa na kuusikia uwepo wa Mungu umemfunika, nguvu za Mungu zinashuka mwilini mwake, n.k. na unajikuta unafurahia sana maombi..

Kusudi la sisi kuomba sio kwenda kujitesa au kujiumiza, hapana bali ni mahusiano, tena ya kama mtu anazungumza na Baba yake. Kiasi kwamba ukitoka kwenye maombi unaona umetoka kweli kuwasiliana na mtu, sio umetoka kuusemesha ukuta, usiokuwa na mrejesho wowote, umeomba hewani hewani tu

Sasa ni mapenzi ya Mungu kwamba sisi watoto wake kila tuombapo tuombe katika Roho Mtakatifu. Tuzame, tuyafurahie maombi yetu. Sasa tunawezaje kufikia hatua hiyo?

Kabla ya kuona namna ya kufikia hicho kilele. Tuone kwanza vikwazo vinavyomzuia mtu asiombe kwa Roho.

VIKWAVYO VINAVYOPINGANA NA MTU KUOMBA KATIKA ROHO.

  1. Mwili
  2. Shetani

Hawa ndio maadui wawili wakubwa wa mtu kuzama. Ndio maana wewe kama mwombaji ni lazima uwafahamu, na ujue kabisa huna budi kushindana nao na ni lazima ukutane nao. Vinginevyo usipowatilia  maanani kila siku maombi yako yatakuwa ni ya “kawaida sana” na kila utakapofikiria  kitu kinachoitwa maombi utaona kama vile unapelekwa gerezani.

Ndugu Mungu hajakusudia tujihisi hivyo sisi watoto wake tunapomkaribia yeye, tuwe kama tunaliomba sanamu lisilonena, amekusudia kutupa mrejesho, na ndio hiyo zawadi ya Roho kuugua ndani yetu. Lazima atupe mrejesho wake kwamba yupo nasi.

Sasa uanzapo, hakikisha unaunyima mwili wako, raha zote, zinazokinzana na wewe kuomba. Kwamfano, ukijiona mwili unasinzia au unapoa wakati wa kuomba usipende kukakaa kwenye kiti, ni heri upige magoti, ukishindwa tembea-tembea. Tena ni vizuri ukanyoosha na mikono yako juu, huku umefunika macho. Kisha anza kuomba.

Usiogope adhabu hizo za mwanzoni hazitadumu muda mrefu sana utaingia katika Roho, ni mwili tu unakuambia wacha, kunitesa, wewe ulazimishe tu, ukikuambia leo siku nzima umefanya kazi legea-legea, pinga hayo mawazo. Hivyo ukiwa Sasa katika hali hiyo. Anza kuomba lakini pia tumia ahadi za Mungu zilizopo kwenye biblia ni muhimu sana, kulingana na jambo unaloliombea, mkumbushe Bwana, ulisema hivi, na hivi kwenye Neno lako,, Ulisema ni nani aliye Baba, mtoto wake akimwomba mkate atampa jiwe, mkumbushe mwambie ulisema, kama ungetazama dhambi zetu ni nani angesimama,..mwambie ulisema niite nami nitakuitikia, nami nitakuonyesha mambo makubwa na magumu usiyoyajua n.k..Tumia njia hiyo, kujimimina kwa Bwana

Omba huku umetilia umakini(concentrate), mawazo yako ukiyalazimisha yasiende nje ya Mungu. Tengeneza picha halisi Mungu amesimama mbele yako kukusikia, fumba macho. Usiruhusu kufikia mambo ya nje, kwasababu akili yako itakuwa shapu kukutoa, ukitoka rudi, endelea kuomba. Ndio ni kipindi kifupi utataabika , lakini hatimaye utazama tu.. Sasa ukiendelea kudumu kwa kung’ang’ania huko  kwenye maombi hayo kwa kipindi fulani. Hayo mazingira rafiki ya Roho Mtakatifu kuyaingilia maombi yako. Utashangaa tu, wepesi usio wa kawaida umezuka ndani yako. Tangu huo wakati endelea kuomba kwa jinsi usikiavyo rohoni, kwani hayo maneno unayoyaomba mengine hutaelewa unayatolea wapi, huyo ni Roho Mtakatifu anaomba na wewe.

Ndio maana akasema msifikiri-fikiri, kwasababu Roho mwenyewe atawajalia.  Wengine kabla ya kuomba wanasema sijui nitaomba nini? Ndio hujui kwasababu bado hujazama, ukishazama utaweza tu kuomba kwasababu ni yeye ndio anayekujalia. Wengine wanasukumwa kunena kwa lugha n.k.

Adui wa pili ni shetani. Huyu anapaswa apingwe kwa kukemewa. Kabla ya kuanza maombi, hakikisha unayateka mazingira yako ya kimaombi. Ukimwomba Mungu, afukuze uwepo wote wa mapepo, hapo ulipo.  Dalili ya shetani, ni pale unashangaa ukiwa unataka kuomba kichwa kinauma au tumbo, au hali Fulani isiyo ya kawaida inakuvaa katika mwili wako. Huyo ni shetani, mpinge kwa kukemea kisha endelea na maombi. Au mwingine anaona mazingira ya kusumbuliwa, mara kelele Fulani za nje, au simu zinaingia, ambazo si kawaida sikuzote kuwepo. Ndio maana ni vizuri katika kuomba kwako uzime simu. Ukae mbali na mazingira yenye mwingiliano, hiyo itakufanya umpe adui wakati mgumu kukusumbua.

Zingatia tu: Shetani haogopi sana maombi ilimradi maombi, anaogopa sana maombi yaliyo katika Roho, Hata kama ni ya muda mfupi, hayapendi, na ndio atakayoyapiga vita sana. Hivyo usiwe mwepesi mwepesi kupenda kuomba juu juu.

Kwahiyo ukizingatia mambo hayo mawili kutakufanya uzame rohoni katika maombi yako yote. Na utayafurahia na utaona matokeo pia.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika sanduku la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

KANUNI YA KUOMBA NA KUPOKEA.

HIZI NI NYAKATI ZA KUFUNGA NA KUOMBA.

KUNA AINA NGAPI  ZA MAOMBI?

SALA YA BWANA. (Namna ya kuiomba)

JE! TUNAPASWA TUOMBE MARA NGAPI KWA SIKU?

JINSI SHETANI ANAVYOZUIA MAJIBU YA MAOMBI YETU.

Rudi nyumbani

Print this post