Category Archive Home

MAANA HUFUMBA MACHO YAO WASIONE!

Karibu tunayatafakari maandiko…

2Petro 3:3 “Mkijua kwanza neno hili ya kwamba katika siku za mwisho watakuja na dhihaka zao watu wenye kudhihaki, wafuatao tamaa zao wenyewe,

4  na kusema, Iko wapi ahadi ile ya kuja kwake? Kwa maana, tangu hapo babu zetu walipolala, vitu vyote vinakaa hali iyo hiyo, tangu mwanzo wa kuumbwa.

MAANA HUFUMBA MACHO YAO WASIONE neno hili ya kuwa zilikuwako mbingu tangu zamani, na nchi pia, imefanyizwa kutoka katika maji, na ndani ya maji, kwa neno la Mungu;

6  kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia

7  Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu”.

Maandiko yanatuambia watu wa siku za mwisho watafumba macho yao WASIKUMBUKE KILICHOTOKEA WAKATI WA NUHU. Kwamba Mbingu zilikuwepo na nchi pia ilikuwepo, na watu walikuwa wanaendelea na mambo yao, wakidhihaki mahubiri ya Henoko na Nuhu kuhusiana na hukumu ya Mungu, na wakati ulipotimia wa kikombe cha ghadhabu ya Mungu kujaa, hakuna hata mmoja aliyesalia Zaidi ya Nuhu na wanawe na wake zao, jumla watu 8 kati ya dunia iliyokuwa imejaa mabilioni ya watu.

Sasa mambo hayo yalishawahi kutokea katika rekodi za wanadamu.. lakini watu WANAFUMBA MACHO YAO!, Wasione hilo, wala kulitafakari.. na hatimaye wanadhihaki wakisema mbona Yesu harudi!.. mbona tumesubiri na kusubiri!..

Lakini hao hao wanaelewa kilichotokea wakati wa Nuhu kuwa dunia iligharikishwa yote..na wanajua kabisa kuwa walikuwepo watu wenye dhihaka kama za kwao, wakisema hakuna Mungu, na hakuna mtakatifu duniani.. Lakini siku ilipofika ya kuokoka Nuhu peke yake na familia yako, ndipo walipoelewa kuwa walikuwepo wacha Mungu duniani, na tena Mungu haangalii wingi.

Ndugu usidanganyike!. KRISTO ANARUDI! Na wala hatakawia..

Waebrania 10:37 “Kwa kuwa bado kitambo kidogo sana, Yeye ajaye atakuja, wala hatakawia”.

Baada ya Kristo kuwachukua watu wake, kitakachofuata duniani ni gharika ya Moto wa ghadhabu ya MUNGU juu ya wote wasiomcha Mungu, kama tu ilivyokuwa nyakati za Nuhu.

2Petro 3:7 “Lakini mbingu za sasa na nchi zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu.

Hivyo kamwe usifikiri wala kuwaza, wala kutia wasiwasi juu ya ujio wa BWANA YESU KRISTO.. Kama ulishawahi kudanganywa, au kulaghaiwa basi ni wanadamu ndio waliokudanganya na kukulaghai, lakini MUNGU muumba wa mbingu na nchi, kamwe hajawahi kusema uongo, na hatakaa aseme uwongo..

Kizazi chetu kitahukumiwa zaidi kuliko kile cha Nuhu kwasababu laiti watu wa kipindi cha Nuhu, wangepata mfano wa wengine waligharikishwa kabla yao, huenda wangeyatii mahubiri ya Nuhu lakini hawakuwa na mifano kabla yao, lakini sisi tunao mfano, wa watu hao.. ni kitu gani kinatutia kiburi!.

Ni nini kinachotufumba macho, na kinachowafumba watu macho????

Unadhani ni shetani????... nataka nikuambie shetani anahusika kwa sehemu ndogo sana, (Na adui anapenda kila kitu asingiziwe yeye ili watu waendelee kujifariji namna hiyo)…..kinachowafanya watu KUFUMBA MACHO YAO, wasitafakari yaliyotokea nyakati za Nuhu na Sodoma na Ghomora ni KIBURI CHA UZIMA, na watu kwa mioyo yao wenyewe KUCHAGUA GIZA na KUIKATAA NURU.

Yohana 3:19 “Na hii ndiyo hukumu; ya kuwa nuru imekuja ulimwenguni, na watu wakapenda giza kuliko nuru; kwa maana matendo yao yalikuwa maovu”.

Siku hizi za Mwisho watu wameyafumba macho yao, wasione na wanajiaminisha ni shetani, kumbe si shetani bali ni wao…tupo! kizazi cha hatari sana..

Mathayo 13:15 “Maana mioyo ya watu hawa imekuwa mizito, Na kwa masikio yao hawasikii vema, Na macho yao wameyafumba; Wasije wakaona kwa macho yao, Wakasikia kwa masikio yao, Wakaelewa kwa mioyo yao, Wakaongoka, nikawaponya”

Kwa hitimisho usilisahau andiko lifuatalo…

2Petro 3:8 “Lakini, wapenzi, msilisahau neno hili, kwamba kwa Bwana siku moja ni kama miaka elfu, na miaka elfu ni kama siku moja.

9 Bwana hakawii kuitimiza ahadi yake, kama wengine wanavyokudhani kukawia, bali huvumilia kwenu, maana hapendi mtu ye yote apotee, bali wote wafikilie toba”.

Ikiwa bado hujampokea BWANA YESU, bali mlango wa wokovu sasa upo wazi, na tunaishi ukingoni kabisa mwa wakati. Hatuna muda mwingi KRISTO anarudi!. Ni wakati wa kutubu na kuishi maisha masafi yanayoendana na toba yetu.

Ufunuo 22:12 “Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.

13  Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho.

14  Heri wazifuao nguo zao, wawe na amri kuuendea huo mti wa uzima, na kuingia mjini kwa milango yake”

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

NUHU WA SASA.

UMEFUNULIWA AKILI?

KWANINI NI NUHU, AYUBU NA DANIELI?

Kuna tofauti gani kati ya uso wa Bwana na macho ya Bwana?

NI WAKATI UPI UTAUONA USO WA KRISTO?

Rudi nyumbani

Print this post

Anaposema zijapokuwa nyekundu kama bendera, ana maana gani?

SWALI: Mungu anaposema dhambi zetu zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu. Ana maana gani, kwenye hilo neno bendera?

Isaya 1:18 Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu.  19 Kama mkikubali na kutii mtakula mema ya nchi;


JIBU: Hapa ni Mungu anaeleza mambo mawili hayuhuso dhambi walizotenda watu wake.

  • Jambo la kwanza ni ukubwa/wingi wa dhambi walizonazo. Ndio hapo anafananisha rangi nyekundu sana, ukilinganisha na kitu kilicho cheupe sana mfano wa theluji.

Tunajua theluji inang’aa sana mfano wa jua, Kuonyesha ni jinsi gani hawa watu walivyokuwa mbali sana na ukamilifu, yaani jinsi gani walivyokuwa hawakaribii hata kidogo kuwa wema mbele za Mungu, walau wangeonekana wa rangu ya kijani, basi wangekuwa na afadhali, lakini ni mbali sana, wana rangi ya damu. Ndivyo ilivyokuwa Israeli yake.

  • Jambo la pili ni usugu wa dhambi uliokuwa ndani yao.Ndio hapo anafananisha na Bendera, ukilinganisha ni sufu nyeupe.

Zamani bendera nyingi zilichovywa katika rangi nzito nyekundu, inayodumu sana, kwasababu ni kitu cha kudumu muda mrefu, hivyo haikuhitajika rangi inayofubaa haraka. Sio tu bendera, lakini mpaka mavazi ya kifalme, au nguo za thamani za sufu.

Hivyo unaposoma habari za bendera hapo, si bendera ya kila rangi, mfano wa bendera tulizonazo sikuhizi zina rangi mbalimbali, zamani nyingi zilichovya kwa rangi  nyekundu. Hivyo Mungu anawaambia ijapokuwa ni nyekundu kama bendera, basi zitageuzwa na kuwa nyeupe kama Sufu, (akiwa na maana ambayo haijachovywa), Yaani Mungu anaweza kuiondoa hiyo rangi sugu, kwenye hicho kitambaa kana kwamba hakijachovywa kabisa.

Kufunua nini,

Yesu Kristo mwokozi wetu ndiye aliyetimiza huo unabii. Kuonyesha kuwa dhambi zote tulizotenda haijalisha ni nyingi kiasi gani, haijalishi ni mbaya namna gani yeye kwa damu yake anaweza kuzifuta kabisa kabisa. Dhambi tulizotenda haijalishi hazisameheki namna gani, hazineneki, ni sugu namna gani, yeye anao uwezo wa kuziondoa, kwa neema yake.

Swali ni je! Umesamehewa dhambi zako? Kama ni la! Unangoja nini kuipokea neema hii, ya WOKOVU mkuu namna hii? Pokea sasa msamaha wa dhambi kwa kutubu dhambi zako, na kumaanisha kuishi maisha mapya ya wokovu. Kisha moja kwa moja atakupokea na kukupa ondoleo la dhambi zako. Na baada ya hapo unahesabiwa kuwa huna dhambi yoyote, umestahili uzima wa milele, bure.

Ikiwa upo tayari kufanya hivyo leo basi, fungua hapa kwa ajili ya mwongozo wa maombi mafupi, na kwa kupitia sala hiyo kwa imani utakuwa umeshampokea Yesu Kristo, na amekusamehe dhambi zako zote.>>>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

Wale Nyoka wa Moto jangwani, walikuwa ni wa namna gani?

ALAMA ZA BENDERA YA ISRAELI ZINAWAKILISHA NINI?

MAANA YA RANGI KIBIBLIA.

Maana Ya Maneno Katika Biblia.

Rudi nyumbani

Print this post

USIWE MKRISTO WA KUKAA TU GHALANI,

Nakusalimu katika jina la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu tujifunze maneno ya uzima ya mwokozi.

Watu waliomwamini Yesu Kristo, yaani waliopokea ondoleo la dhambi zao. Hutambulika kama NGANO, lakini watu ambao bado wapo kwenye dhambi, hujulikana kama MAKAPI.

Sasa kazi ya kwanza ambayo Yesu anaifanya kwa mwamini, ni kumtenganisha yeye na makapi, kisha humweka katika ghala lake.

Mathayo 3:12  Ambaye pepeto lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake; na kuikusanya ngano yake ghalani, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika.

Ghalani ni uweponi mwa Mungu, yaani kutengwa na udunia.

Soma pia..Mathayo 13:29-30.

Sasa kama wewe unafahamu ukulima, unajua kabisa si mbegu zote zinawekwa ghalani kwa matumizi ya chakula, zipo nyingine, zinachukuliwa na kurudishwa shambani ili kwenda kuzalisha nyingine. Na baadaye huongeza ghala la mkulima.

Tofauti kabisa na ile inayobakia pale ghalani, itaendelea kubakia vilevile hata miaka 10, lakini ile inayokwenda shambani, ndani ya hicho kipindi cha miaka 10, yaweza kuongeza magunia mengi sana ya ngano nyingine.

Ndio maana Bwana Yesu alisema maneno haya;

Yohana 12:24  Amin, amin, nawaambia, CHEMBE YA NGANO ISIPOANGUKA KATIKA NCHI, IKAFA, HUKAA HALI IYO HIYO PEKE YAKE; BALI IKIFA, HUTOA MAZAO MENGI. 25  Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele. 26  Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu.

Umeona hapo? Kumbe isipoanguka na kuoza basi itaendelea kubakia katika hali ile ile. Lakini ikikubali kuanguka na kuoza, ardhini, basi itachipuka kama shina, na mwisho wa siku itazaa sana.

Na hapa ndipo waamini wengi, hawataki kuingia gharama. Wanatamani wamzalie Mungu matunda, lakini hawawezi, kwasababu hawajakubali “kufa na kuoza” kwa habari ya huu ulimwengu.

Hawajakubali kuziangamiza  nafsi zao kwa ajili ya Kristo. Sasa hiyo ndio inayopelekea wabakie tu kama wakristo wa ghalani,wasioweza kuzalisha chochote.

Yesu alitoa sifa za mbegu yenye kuzaa katika ule mfano wa mpanzi,  akasema nyingine ziliangukia njiani, nyingine kwenye miamba, nyingine kwenye miiba, na nyingine kwenye udongo mzuri. Akasema vilizoangukia kwenye udongo mzuri ziliweza kuzaa kwa tendo moja tu la “kuvumilia”

Kuvumilia nini?

Kuvumilia dhiki, na udhia kwasababu ya Kristo, kuvumilia vishawishi vya anasa, udanganyifu wa mali, na shughuli za ulimwengu huu zilizopitiliza, lakini pia kwa unyofu wa moyo walikuwa wanalitendea kazi Neno ili walilolisikia lisiwe bure adui akaliiba ndani yao. (Luka 8:11-15). Hao ndio wakristo wasio wa ghalani, ni wakristo waliokubali kutoka nje, kumletea Bwana matunda.

Je! Na sisi tunaweza kupiga hatua nyingine? Umeokoka ndio, lakini ni lazima wokovu wako uwe na matokeo kwa wengine, uwavute na wengine kwa Kristo, kama wewe ulivyovutwa. Hivyo kubali kumaanisha kumfuata Yesu na kukaa mbali na udunia kwa kadiri uwezavyo.

Jitoe pia kwa Bwana, mali zako, zitumike kuhubiri injili, tenga fungu lako kwa Bwana, penda kusapoti kazi za Mungu, usiwe msomaji tu na kusema Amen!. Onyesha kuwa na wewe ni mtendaji kazi ili thawabu yenu iwe ni  moja, na yule mtendaji kazi mwingine.

Bwana atusaidie, tutoke ghalani.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

NI YESU YUPI UMEMPOKEA?, NI ROHO IPI UMEIPOKEA? NA INJILI IPI UMEIPOKEA?

ANGALIA JINSI USIKIAVYO:

SEMA KWA LUGHA NYINGINE.

Je Mungu ana njia ngapi za kuzungumza?

Rudi nyumbani

Print this post

TENDA JAMBO LA ZIADA.

(Masomo maalumu yahusuyo kazi na uchumi).


Tunahitaji kujua kanuni chache ili tuweze kufungua milango yetu ya kiuchumi. Leo tutaangalia kanuni nyingine ambayo mkristo akiitumia basi anaweza kupata kibali mahali pale afanyiapo kazi.

Si wakati wote maombi tu pekee yanatosha kukuletea kibali katika maisha ya kazi/kuwajibika. Ni lazima pia uongeze na maarifa ili uweze kufungua milango hiyo ya Baraka.

Sasa ukitaka upate kibali kazini au kwa aliye juu yako, basi FANYA JAMBO LA ZIADA HAPO UFANYIAPO KAZI.

Kwa mfano Mshahara wako unaoupokea kwa siku, wiki au mwezi, ni kiasi Fulani…. baada ya kutoa sehemu ya Mungu (yaani sadaka pamoja na Zaka) kiasi kilichosalia  usikitumia chote katika mahitaji yako..bali toa sehemu kidogo ya hicho na ufanye jambo jipya na la kipekee hapo ufanyiapo kazi!.

Kwa mfano kama umeajiriwa na unafanya kazi ya usafi hapo kazini, badala ya kusubiri mwajiri wako akupe fedha ya kwenda kununua kifaa cha usafi, hebu wewe TENDA JAMBO LA ZIADA… toa kiasi kidogo cha pesa yako na nenda kununua kifaa hicho.

Kwa kufanya hivyo utaonekana mjinga mbele ya wafanyakazi wenzako na watu wengine walio karibu nawe pengine hata kwa mke wako/mume wako… lakini si kwa Mwajiri wako!, yeye atakusifu kama si kwa kinywa chake basi katika moyo wake, na hiyo itakuongezea kibali kikubwa sana katika maisha yako ya kazi… Utakuwa umepata nafasi katika moyo wake, na kiwango cha kukuamini na kukupenda kitaongezeka..

Au labda umeajiriwa katika mgahawa, hebu TENDA JAMBO LA ZIADA…badala ya kusubiri boss wako akupe fedha za kwenda kununua sahani za biashara, au akupe fedha za kwenda kununua sufuria, au sabuni.. hebu mara moja moja wewe toa kiasi chako kidogo cha mshahara kanunue zile sahani, au sufuria au kitu kingine chochote cha muhimu kinachohitajika pale..

Wala usianze kuangalia mahitaji uliyonayo (hayo yataendelea kuwepo tu)… wewe fanya hivyo kwasababu  unajua ni mbegu gani unayoipanda wakati huo!… wengine watakuona huna akili, au umechanganyikiwa, wewe usiangalie hayo bali angalia yanayokuja..

Pengine umeajiriwa kama mhasibu katika ofisi fulani, hebu TENDA JAMBO LA ZIADA, Toa kidogo katika mshahara wako kanunue kiti kingine cha ofisi au saa ya ofisi nzuri, au pamba kwa chochote kile pale ufanyiapo kazi.. weka mbali matatizo yako kwa muda, na mahitaji yako na ufanye hayo.. nakuhakikishia matokeo yake utakuja kuyaona baadaye.. Utapata kibali ambacho utakishangaa.

Wakati unafanya hayo, wengine watakuona ni mjinga, kwasababu hayo unayoyafanya yangepaswa kutekelezwa na boss wako au kampuni, na sio wewe…ndio maana watakuona umerukwa na akili, lakini Mwajiri wako atakuona ni shujaa..

Katika biblia Bwana YESU alitoa mfano wa wakili dhalimu, ambaye alitoa mali zake za wizi na kuwalipa wadeni wa Boss wake, na kupitia mali ile ya udhalimu alijipatanisha na boss wake pamoja na wadeni wa boss wake…na hivyo akasifiwa hata na yule yule aliyemwibia (yaani bosi wake). Soma Luka 16:1-12

Sasa huyu alijipatia kibali kwa mali ya udhalimu (maana yake mali ya wizi).. vipi wewe ambaye una mali ambayo sio ya wizi (halali), halafu ukaitumia katika kutafuta kibali?.. unadhani hutakipata??.

Lakini ukisema mimi nitaomba tu!, na kutumia kiasi chako kwa mahitaji yako tu…na huku hutaki kutenda jambo la ziada,  hapo unapofanyia kazi, utakuwa unajiwikwamishia Baraka zako tu!… kwasababu hayo uyafanyayo ni kila mtu anayafanya, na yameshazoeleka…lakini ukitenda TENDA TENDO LINGINE ZA ZIADA ambayo halifanywi na wengine wote, hapo utajipatia kibali.

Hata katika kumtumikia MUNGU, Bwana YESU alitufundisha kuwa ni lazima tujifunze kutenda tendo lingine la ziada ili tupokee kibali.

Mathayo 5:46 “Maana mkiwapenda wanaowapenda ninyi mwapata thawabu gani? Hata watoza ushuru, je! Nao hawafanyi yayo hayo?

47  Tena mkiwaamkia ndugu zenu tu, mnatenda tendo gani la ziada? Hata watu wa mataifa, je! Nao hawafanyi kama hayo?”

Hivyo pata maarifa na TENDA TENDO LA ZIADA, na utaona jinsi utakavyopokea kibali katika yote uyafanyayo!.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

TENDA HAKI KWA FAIDA YAKO MWENYEWE.

Mfano wa wanawali kumi(Mathayo 25), unaelewekaje?

Mistari ya biblia kuhusu kibali.

NJIA NYINGINE YA KUPATA REHEMA NA KIBALI KUTOKA KWA MUNGU.

MAPAMBO YA WANAWAKE WALIOUKIRI UCHAJI WA MUNGU.

Rudi nyumbani

Print this post

Chrislam ni nini?

Ni muungamaniko wa maneno makuu mawili. (Yaani Christian na Islamic). Likachukuliwa Neno la kwanza Chris katika Christian, likaunganishwa na Neno la katikati “slam” kutoka katika Islamic. Kuunda Christlam

Hii ni imani iliyozuka, katika taifa la Nigeria miaka ya 1970.  Kufuatana ni migongano ya kiimani baina ya makundi haya mawili ya dini, ikizingatiwa kuwa Taifa La Nigeria ndio lenye watu wengi barani Africa, na takribani Nusu kwa Nusu, dini hizi mbili ndio zimechukua jamii kubwa ya watu.

Hivyo waasisi ya umoja huu walikuwa na madhumuni ya kuondoa tofauti za kidini, husani zilizo katika mataifa ya magharibu na ya mashariki ya kati, Lakini pia kwasababu hizi ndio dini kubwa duniani, basi pia zikiungana zinaweza kusaidia kuushinda upagani kwa sehemu kubwa.Na ukweli ni kwamba imani hii imepata umaarufu mkubwa duniani, hususani kwa kipindi cha sasa.

Waanzilishi walisukumwa kuunda umoja huu, wakiamini kuwa, sehemu kubwa ya dini ya kikristo inatajwa katika Quran, wakimrejea Yesu mwenyewe pamoja na manabii wa kale, kama Ibrahimu na wengineo. Lakini pia uislamu unamwingiliano mkubwa wa kitamaduni ambao hata katika ukristo upo. Hivyo kwa mujibu wa hoja zao hakuna sababu ya kuwa na utofauti wowote katika mashindano ya kidini.

Lakini je! Umoja huu, mbele za Bwana unakubalika?

Imani ya Kikristo na dini ya kiislamu haviwezi kuchangamana, ni sawa na chuma na udongo. Kwasababu kiini cha imani ya ukristo ni KRISTO mwenyewe, na kwamba mtu hawezi kwenda mbinguni pasipo kumwamini YESU kama mwokozi PEKEE anayewaokoa wanadamu. Jambo ambalo linakinzana na dini ya Kiislam, katika imani ya kufika mbinguni, ambapo kwa waislam Kristo ni kama mmojawapo wa manabii tu wengine. Na hivyo mbingu si kupitia Kristo, bali ni kupitia matendo mazuri kama vile kukaa mbali na uovu n.k.

Uislamu haumtambui Kristo kama Mungu, huamini kuwa yoyote anaye amini kuwa Yesu ni Mungu, ni makufuru, kwasababu Mungu hajazaa, wala hana mshirika. Hivyo aaminiye uungu wa Yesu, pepo haimuhusu.

Kwa vigezo hivyo, uislamu na ukristo ni imani mbili tofauti kabisa, ijapokuwa zitaonekana kushea baadhi ya desturi, lakini bado haziwezi kuletwa pamoja kuwa kitu kimoja.

Je! Hatupaswi kuwa waamini wa Chrislam

Ndio wewe kama Mkristo,, imani yako haipaswi kuchanganywa na nyingine yoyote, ukifanya hivyo ni Kosa kiimani. Sisi tunaamini, wokovu ni kwa kupitia Yesu Kristo anaotupa BURE kwa neema katika kumwamini Yeye, kwa kifo chake pale msalabani.

Tunamtegemea Kristo kutuokoa, kutupa nguvu ya kuishi maisha makamilifu, kutuongoza, kwa asilimia zote. Hivyo hatuna msingi au tegemeo lingine nje yake yeye. Na hata hivyo kibiblia, yoyote asiyekubaliana na Kristo Yesu, kama ndiye mwokozi pekee. Huyo ni mpinga-Kristo.

Hivyo kwa hitimisho ni kuwa wewe kama mwana wa Mungu, usijihusishe ni imani yoyote nje ya Kristo Yesu mwokozi wako.

Matendo 4:12  Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

Dini ni nini, na Imani ya kweli ni ipi?

Praitorio ni nini? Na Kwanini ilikuwa ni najisi kwa wayahudi kuingia humo? (Yohana 18:28)

Uadilifu ni nini kibiblia?

Rudi nyumbani

Print this post

Merikebu ya Iskanderia kwanini itajwe jina lake ‘Ndugu Pacha’?

SWALI: Je kulikuwa na umuhimu wowote wa ile merikebu ya Iskanderia  walioipanda Paulo na wafungwa wengine kutajwa jina lake ‘ndugu Pacha’,?

Matendo 28:11  Baada ya miezi mitatu tukasafiri katika merikebu ya Iskanderia iliyokuwa imekaa pale kisiwani wakati wa baridi; na alama yake ni Ndugu Pacha. 12  Tukafika Sirakusa, tukakaa siku tatu. 13  Kutoka huko tukazunguka tukafikia Regio; baada ya siku moja upepo wa kusi ukavuma, na siku ya pili tukawasili Puteoli. 14  Huko tukakuta ndugu, wakatusihi tukae nao siku saba; na hivi tukafika Rumi.


JIBU: Safari ya mtume Paulo kama mfungwa, kutoka Kaisaria kwenda Rumi kuhukumiwa, haikuwa rahisi, iligubikwa na misuko suko mikubwa ambayo ilihatarisha maisha yao ukisoma Matendo 27, utaona mtume Paulo alionywa na Roho Mtakatifu kuhusu hatari hiyo lakini alipomwambia akida na manahodha, walipuuzia agizo lake, kwasababu watu wale hawakuamini habari za “miungu kabisa”. Maandiko yanasema walipoona upepo wa kusi umevuma kidogo tu, unaoruhusu kusafiri, wakadhani itakuwa hivyo mbeleni.

Lakini tunaona walipofika katikati, ghafla ile bahari iliwachafukia sana, upepo wa nguvu ukavuma merikebu yao ikawa karibu na kuzama, baadaye ilivunjika kabisa, na wakaokoka kwa shida kwasababu Mungu alimuhakikishia Mtume Paulo kuwa hakuna hata mmoja wao atakayeangamia.

Walipookoka na kufika kisiwa kile kilichoitwa Melita, walikaa miezi mitatu pale, kuruhusu hali ya hewa kutulia, kabla ya kuondoka. Lakini tunaona walipotaka kuondoka, safari hii wale mabaharia pamoja na maakida, hawakuichukulia safari yao kirahisi rahisi, yaani hivi hivi tu bila uongozo wowote. Ndipo walipojifunza kuchagua merikebu yenye “ulinzi wa kiroho”. Wakaipata hiyo ya Iskanderia iliyokuwa na nembo ya “Ndugu Pacha” kwa mbele.

Ndugu Pacha ni miungu ya kipagani ya kiyunani, ukisoma tafsiri nyingine za biblia imewataja moja kwa moja miungu hiyo kama Castor na Pollux. Ni miungu ambayo waliamini inahusika na ulinzi wa  safari za majini. Hivyo kwa imani yao ya kipagani, wakachukua nembo yao kuonyesha tunaiabudu na kuiheshimu hii miungu, na kutaka iwaongoze  salama katika safari yao, hawategemei tena elimu zao na nadharia zao.

Sasa tukirudi kwenye swali, linalouliza, kulikuwa ni umuhimu gani, hiyo merikebu ya Iskanderia kutajwa hadi nembo yake ya ndugu Pacha. Sababu ndio hiyo, Sio kwamba biblia inatufundisha, na sisi tukaweke miungu ya kipagani, kwenye vyombo vyetu vya usafiri kutuhakikishia ulinzi, hapana!

Bali inatufundisha Safari ya maisha hapa duniani. Kila mwanadamu anasafiri, lakini Je! Katika safari yako ni kitu gani kinakuongoza na kukulinda ili kukufikia ng’ambo yako salama?

Hakuna mwanadamu ambaye anaweza kujiongoza mwenyewe. Na ndio maana utaona hawa kwasababu hawakumjua Mungu wa kweli iliwabidi wakatafuta vinyago visivyoweza kuwasaidia kitu viwaongoze, na kama sio mtume Paulo kuwepo ndani ya Merikebu ile, safari yao ndio ingekuwa mbaya mara mbili zaidi. Hawakujua tu waliongozwa na Kristo Yesu pasipo wao kujua kwa neema tu!. Kwasababu watumishi wa Mungu walikuwa ndani.

Na sisi, hapa tulipo, fahamu kuwa maisha yako, bila KRISTO ni mauti mbele. Shetani hakuwazii mema, wala akili zako mwenyewe hazikusaidii ndugu, hiyo elimu ni kazi bure, huo uzoefu na ujuzi ulionao ni bure rafiki. Unamuhitaji Kristo, yeye ndio awe nembo  ya maisha yako. Mwamini leo akupe msamaha wa dhambi, mwamini leo akuokoe, safari yako iwe salama hapa duniani. Ukifa leo katika hali hiyo, fahamu ni jehanamu moja kwa moja. Umesikia injili ikihubiriwa mara ngapi, kwamba Yesu ni mwokozi lakini unapuuzia? Walio kuzimu wanatamani hata dakika moja, watubu hawawezi kwasababu kule hakuna maisha ya kuishi. Lakini wewe unaishi.

Usikiapo maneno haya, ugeuze moyo wako, umruhusu Kristo leo akuokoe, ikiwa upo tayari kumgeukia Bwana Yesu , na unatamani upate mwongozo wa kimaombi kwa ajili ya wokovu wako. Basi wasiliana nasi kwa namba uzionazo mwisho wa makala hii, bure.

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

NA UPEPO WA KUSI ULIPOANZA KUVUMA KIDOGO,

MAJARIBU MATANO (5) YA MKRISTO.

Kalafati ni nini? (Ezekieli 27:9)

KWANINI DANI ALIKAA KATIKA MERIKEBU.

Rudi nyumbani

Print this post

Nini maana ya “Mvinyo hudhihaki na kileo huleta ugomvi? (Mithali 20:1)

Jibu: Turejee.

Mithali 20:1 “Mvinyo hudhihaki, kileo huleta ugomvi; Na akosaye kwa vitu hivyo hana hekima”.

Hili ni andiko linaloelezea mambo makuu mawili yanayowakosesha watu waliopungukiwa na Hekima.. na Mambo hayo ni “Mvinyo” pamoja na “Kileo”. Na vitu vyote hivi viwili vina madhara kwa mtu anayevitumia..

Sasa ni ipi tofauti kati ya Mvinyo na Kileo? Na madhara yake ni yapi kwa mtumiaji?.

“Mvinyo” (kwa lugha ya kiingereza ni “wine”) ni kilevi kinachotengenezwa kwa “Matunda yaliyosagwa” kama Zabibu, mananasi, maembe n.k Mfano wa mvinyo unaotengenezwa kwa zabibu ni “Divai”.

Wakati “Kileo” (Kwa lugha ya kiingereza Beer/Bia) ni kilevi kinachotengenezwa kwa nafaka kama Ngano, mahindi, ulezi, mtama, mchele n.k

Kikawaida Mvinyo ndio wenye kilevi kingi kuliko Kileo. Na matokeo ya mtu anayetumia mvinyo au kileo yanakaribiana. Hebu tuangalia madhara ya kimoja baada ya kingine kibiblia.

   1. MVINYO

Biblia anasema “Mvinyo hudhihaki”.. maana yake ni kuwa mtu anayetumia mvivyo anakuwa ni mtu wa kudhihaki na kudhihakiwa!.. kwasababu ya wingi wa maneno yao yasiyo na maana yatokayo midomoni mwao.

Ndio maana utaona kile kipindi cha Pentekoste, walipowasikia wanafunzi wa Bwana YESU wakinena kwa lugha, walidhani wamelewa kwa mvinyo mpya na hivyo wakaanza kuwadhihaki..

Matendo 2:12 “Wakashangaa wote wakaingiwa na shaka, wakiambiana, Maana yake nini mambo haya? 13  WENGINE WALIDHIHAKI, WAKISEMA, WAMELEWA KWA MVINYO MPYA.

14  Lakini Petro akasimama pamoja na wale kumi na mmoja, akapaza sauti yake, akawaambia, Enyi watu wa Uyahudi, na ninyi nyote mkaao Yerusalemu, lijueni jambo hili, mkasikilize maneno yangu.

15  Sivyo mnavyodhani; watu hawa hawakulewa, kwa maana ni saa tatu ya mchana;

16  lakini jambo hili ni lile lililonenwa kwa kinywa cha nabii Yoeli”.

Umeona hapo?.. walianza kuwadhihaki wakidhani wamelewa kwa MVINYO MPYA, ikimaanisha kuwa Mvinyo huleta dhihaka kwa anayekunywa. Na mtu anayelewa kwa mvinyo atapokea dhihaka nyingi katika maisha yake..

    2. KILEO

Biblia inaendelea kusema kileo huleta “UGOMVI”. Asilimia kubwa ya watu wanaogombana mpaka kufikia hatua ya kudhuriana ni walevi wa pombe, mafarakano mengi yanatoka kwa watu waliolewa..

Hivyo kwa hitimisho ni kwamba, Ulevi wa aina yoyote ile uwe wa “Mvinyo” au wa “Kileo” matokeo yake ni mabaya katika maisha ya ulimwengu huu na ule ujao…. Kulingana na biblia walevi wote hawataurithi uzima wa milele (soma 1Wakorintho 6:9-10 na Wagalatia 5:19-20)..

Warumi 13:13 “Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ULAFI NA ULEVI, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu.

14  Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake”.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

UPEPO WA KUSI HULETA MVUA;

“Si watu wa kutumia mvinyo sana”, je tunaruhusiwa kutumia mvingo kidogo?(1Timotheo 3:8).

Biblia ina maana gani inaposema akonyezaye kwa jicho huleta masikitiko?

Je! mwanadamu wa kwanza kuumbwa ni yupi?

JE! ULEVI NI DHAMBI?.

Rudi nyumbani

Print this post

 UNAUELEWA, HISOPO UMEAO UKUTANI?

1Wafalme 4:32 Naye akanena mifano elfu tatu, na nyimbo zake zilikuwa elfu moja na tano.  33 Akanena habari za miti tangu mwerezi ulioko Lebanoni hata HISOPO UMEAO UKUTANI; pia akanena habari za wanyama, na za ndege, na vitambaavyo, na samaki.

Salaam! karibu tujifunze na kutafakari bahari za mwokozi wetu Yesu Kristo na uzuri wake maishani mwetu.

Habari yetu itaanzia kwa mfalme Sulemani ambaye Mungu alimjalia hekima nyingi zaidi ya wanadamu wote waliokuwa duniani kwa wakati ule. Na moja ya mambo ambayo, aliyatafakari sana, hayawakuwa tu yanayowahusu wanyama na viumbe hai, lakini ni pamoja na mimea mbalimbali.

Hivyo kama tunavyosoma katika vifungu hivyo, aliweza kutambua hekima iliyokuwa imejificha nyuma ya miti mikubwa na yenye umaarifu kama mierezi, lakini, kilichomtafakarisha pia sio katika mimea mikubwa, lakini pia midogo  mfano wa Hisopo, na jinsi inavyomea. Na hapo tunaona anaeleza sifa yake, kwamba ni mmea unaomea ukutani.

Ikiwa na maana, mahali palipo na ardhi ngumu, au mwamba au jiwe, wenyewe unamea, na kukua na kuzaa bila shida yoyote. Tofauti na mimea mingine mingi yenye nguvu, itahitaji  udogo mlaini mwingi, tena tifutifu, lakini huu wa hisopo ni wa kipekee unahitaji mahali pagumu.

Kufunua nini?

Mmea huu unamfunua Bwana wetu Yesu Kristo,yeye  Hakuhitaji mahali palipoandaliwa pa kitajiri, ili kulitimiza kusudi la kifalme duniani,  hakuhitaji familia ya kidini maarufu, au kabila la kikuhani,  ili aishi maisha makamilifu, hakuhitaji kuishi mji mtakatifu Yerusalemu ili ampendeze Mungu. Bali alitokea mahali ambapo ni vijijini (Nazareti), familia maskini, tena nyakati za kipagani, ambazo imani ilikuwa imekongoroka sana, pia, kabila lisilojiuhusisha na mambo yoyote ya kikuhani kabisa. Hivyo Yesu aliishi katika jamii ya wapagani.

Wakati sisi katikati ya dhiki nyingi (yaani penye mwamba mgumu) tunanyauka. Yeye ndio alikuwa anasitawi. Aliweza kustahimili mapingamizi ya kila namna zaidi ya mwanadamu yoyote aliyewahi kutokea hapa duniani. Alichukiwa na ulimwengu, alisalitiwa, alikanwa, aliachwa peke yake, aliaibishwa, alipigwa mpaka kuuawa. Lakini hakuwahi kuanguka au kutenda dhambi yoyote. Haleluya! Anastahili hakika mwokozi wetu Yesu Kristo.

Ni hisopo umeao ukutani. Mahali ambapo mimea mingine imeshindwa, yeye ameweza.

Na ndio maana Neno linasema;

Waebrania 12:2  tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili msalaba na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu.

3  MAANA MTAFAKARINI SANA YEYE ALIYEYASTAHIMILI MAPINGAMIZI MAKUU NAMNA HII YA WATENDAO DHAMBI JUU YA NAFSI ZAO, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.

4  Hamjafanya vita hata kumwagika damu, mkishindana na dhambi;

Umeona ni kwa namna gani Yesu alivyokuwa mwamba imara wa kutegemea sana?

Na ndio maana maandiko sasa yanasema, kwa kuwa alijaribiwa kama sisi, basi anaweza kuchukuliana na sisi pia katika mambo yetu ya udhaifu.

Waebrania 4:14  Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu.

15  Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi.

16  Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji.

Hivyo ndugu, ni nini unachongoja, usiokoke leo?. Wewe peke yako hutaweza, kuushinda huu ulimwengu, unaihitaji neema ya Yesu Kristo ikusaidie. Mpokee leo, upate ondoleo la dhambi zako,  Akupe na Roho wake mtakatifu ili kukusaidia sasa kuishi maisha ya ushindi kama yeye alivyoishi.

Ukipita katika miamba lakini unaendelea kumea.  Hivyo chukua uamuzi huo leo. Ikiwa upo tayari kuokoka basi fungua hapa kwa mwongozo wa sala ya Toba. >>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

ALIFANYIKA SADAKA KWA AJILI YETU!

VITA BADO VINAENDELEA.

TUKAZE MWENDO KWA TULIYOANDALIWA.

TUNAHESABIWA HAKI BURE KWA NJIA YA IMANI.

Rudi nyumbani

Print this post

Je shauri la kuipepeleza Kanaani lilitoka kwa wana wa Israeli au kwa BWANA?

Swali: Je lile shauri la kupeleka wapelelezi Kanaani lilitoka kwa nani?..Maana sehemu moja katika biblia inasema lilitoka kwa Bwana (Hesabu 13:1-3) na sehemu nyingine inasema lilitoka kwa wana wa Israeli (Kumbukumbu 1:22-23). Je! lipi ni sahihi, na je biblia inajichanganya?.


Jibu: Turejee mistari hiyo, mmoja baada ya mwingine.

Hesabu 13:1 “Kisha Bwana akanena na Musa, akamwambia,

2 Tuma watu, ili waende wakaipeleleze nchi ya Kanaani, niwapayo wana wa Israeli; katika kabila ya baba zao mtamtuma mtu mmoja, kila mtu na awe mkuu kati yao.

3 Basi Musa akawatuma kutoka nyika ya Parani kama alivyoagizwa na Bwana; wote walikuwa ni watu walio vichwa vya wana wa Israeli”.

Hapa tunaona ni MUNGU ndiye anamwamuru Musa apeleke wapelelezi.

Kumbukumbu 1:22 “Nanyi mkanikaribia kila mmoja wenu, mkasema, Na tupeleke watu mbele yetu, ili watupelelezee nchi na kutuletea habari za njia itupasayo kuipandia, na za miji tutakayoifikia.

23 Neno hili likanipendeza sana; nikatwaa watu kumi na wawili, mtu mmoja wa kila kabila”

Na hapa tunasoma kuwa ni “Wana wa Israeli” ndio waliopendekeza kupeleka wapelelezi Kanaani. Sasa swali ni je!..biblia inajichanganga?.

Jibu ni La!.. Biblia haijichanganyi mahali popote, isipokuwa fahamu/pambanuzi zetu ndizo zinachojichanganya au kuchanganyikiwa.

Sasa ni kwanini hapo sehemu moja iseme ni Mungu na sehemu nyingine iseme wana wa Israeli? Ukweli ni upi?

Ukweli ni kwamba wazo la kupeleka wapelelezi wakaiepeleze Kanaani ni Wana wa Israeli ndio waliolitoa, kamwe Mungu asingeweza kuwaambia wana wa Israeli wapeleke wapelelezi kwasababu yeye ana nguvu nyingi na wala hahitaji utafiti wa wanadamu katika kuokoa au kuharibu!…Kama ndivyo angefanya kwanza kwa Farao, lakini tunasoma Farao alikuwa kama mnyoo tu mbele za Bwana, na Taifa la Misri kwa wakati huo lilikuwa na nguvu Zaidi hata ya Kanaani.

Hivyo kilichowasukuma wana wa Israeli kupeleka wapelelezi ni hali ya ugumu wa mioyo yao, ambayo baada ya kutoka Misri walianza kuusahau uweza wa Mungu na kumdharau Mungu, kiasi kwamba hawakuamini kwamba angeweza kuwashindania kama alivyowashindania walipotoka Misri, lakini kinyume chake wakaukataa uweza wa Mungu, mioyo yao ikawa migumu, wakajitwika silaha, na wakapanga mipango yao.

Hesabu 14:11 “Bwana akamwuliza Musa, Je! Watu hawa watanidharau hata lini? Wasiniamini hata lini? Nijapokuwa nimefanya ishara hizo zote kati yao”.

Sasa kwakuwa wana wa Israeli tayari walikuwa wameshamdharau Mungu na uweza wake, hivyo Mungu aliruhusu baadhi ya Mambo wayafanye, katika kiwango cha uweza walichompimia. Na mojawapo ya jambo ambalo aliliruhusu ni hilo la kwenda kupeleleza.

Hivyo Musa aliposikia mpango wa wana wa Israeli kwenda kuipeleleza, alienda kuuliza kwa Bwana, na Bwana akawapa ruhusa sawasawa na hiyo Hesabu 13:1-6. Na sio jambo hilo tu ambalo Mungu alitoa ruhusa bali yapo na mengine mengi ambayo wana wa Israeli walijiamulia na Mungu akaruhusu yaendelee katikati yao, lakini hayakuwa mapenzi makamilifu ya Mungu, baadhi ya mambo hayo ni yale ya wana wa Israeli kujitakia mfalme katika (1Samweli 8:5) na yale ya talaka ambayo Bwana YESU aliyasema katika Mathayo 19:3-8.

Mathayo 19:3 “Basi Mafarisayo wakamwendea, wakamjaribu, wakimwambia, Je! Ni halali mtu kumwacha mkewe kwa kila sababu?

4  Akajibu, akawaambia, Hamkusoma ya kwamba yeye aliyewaumba mwanzo, aliwaumba mtu mume na mtu mke,

5  akasema, Kwa sababu hiyo, mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja?

6  Hata wamekuwa si wawili tena, bali mwili mmoja. Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.

7  Wakamwambia, Jinsi gani basi Musa aliamuru kumpa hati ya talaka, na kumwacha?

8  Akawaambia, MUSA, KWA SABABU YA UGUMU WA MIOYO YENU, ALIWAPA RUHUSA KUWAACHA WAKE ZENU; LAKINI TANGU MWANZO HAIKUWA HIVI.

9  Nami nawaambia ninyi, Kila mtu atakayemwacha mkewe, isipokuwa ni kwa sababu ya uasherati, akaoa mwingine, azini; naye amwoaye yule aliyeachwa azini”

Hii ikitufundisha kuwa, kuna mambo ambayo Mungu anaweza kuyaruhusu katika maisha yetu yatokee lakini yakawa si mapenzi makamilifu ya Mungu. Hivyo ni muhimu sana kutafuta kuyajua na kuyafanya mapenzi makamilifu ya MUNGU, na ndivyo tutakavyompendeza Mungu, na kuishi kama atakavyo yeye.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

Kanaani ililaaniwa (Mwanzo 9:20-25,) kwanini Mungu awapeleke wana wa Israeli katika nchi iliyolaaniwa?

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

EPUKA KUPELELEZA KILA KITU MUNGU ANACHOKUAHIDIA.

NINI MAANA YA SISI KUWA WATOTO WA MUNGU?

Nini maana ya Mithali 19:21Mna hila nyingi moyoni mwa mtu; Lakini shauri la Bwana ndilo litakalosimama.

Rudi nyumbani

Print this post

Roho ya Malipizi/ roho za malipizi ni nini?

Swali: roho za Malipizi ni nini na mtu anawezaje kuzifunga?


Jibu: roho ya Malipizi au roho za malipizi ni roho zinazojilipiza kisasi baada ya kushindwa vita.

Maandiko yanasema vita vyetu sisi si juu ya damu na nyama, bali juu ya falme na mamlaka za giza katika ulimwengu wa roho.

Waefeso 6:12 “Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho”.

Sasa hizi roho za mapepo na za wakuu wa giza, zinaposhindwa vita dhidi ya mtu, au watu, au kanisa basi, huwa zina tabia ya kukimbilia kutafuta sehemu nyingine iliyo dhaifu ya huyo mtu, au watu au kanisa na kushambulia ili kumwumiza yule aliyekuwa anashindana nazo.

Tuchukue mfano, mtu mmoja aliyeokoka ameomba kwaajili ya familia yake (Labda kwajili ya Mke wake au Mume au watoto), na katika kuomba kwake, ameomba ulinzi, na neema ya kumjua Mungu, na Zaidi sana amezikemea roho zote zinazopambana na familia yake, (roho za kurudi nyuma, roho za magonjwa na matatizo mengine) na amezishinda kwa maombi na kuziadhibu sawasawa na 2Wakorintho 10:6.

Sasa roho hizo (za mapepo na wakuu wa giza) zinapoanguka na kushindwa namna hiyo, huwa zina tabia ya kulipiza kisasi…kwa wakati huo zinaondoka na kwenda kutafuta sehemu nyingine ya maisha ya huyo mtu zilizo dhaifu na kuzivamia au kufanya nazo vita kutokana na uchungu na hasira za kushindwa..

Ndio hapo zitaacha kushughulika na familia ya huyo mtu kwa muda, na kwenda kupiga marafiki wa karibu wa huyo mtu, au wazazi, au watu wengine wowote walio wa muhimu katika maisha ya huyo mtu, lengo ni ili kumwumiza huyo mtu au kumsumbua na zinaweza kwenda kupiga kwa magonjwa, hasara au hata mauti kabisa..

Hivyo ni muhimu sana kumalizia maombi kwa kuomba ulinzi kwa watu wote walio karibu nawe ili wazidhurike na ghadhabu za hizo roho.

Hiyo siku zote ndio tabia ya shetani na majeshi yake, “kujilipiza kisasi”

Sasa  pengine utauliza ni wapi katika biblia jambo kama hilo limetokea?..tusome maandiko yafuatayo..

Ufunuo 12:7 “Kulikuwa na vita mbinguni; Mikaeli na malaika zake wakapigana na yule joka, yule joka naye akapigana nao pamoja na malaika zake;

8  nao hawakushinda, wala mahali pao hapakuonekana tena mbinguni.

9  Yule joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani, audanganyaye ulimwengu wote; akatupwa hata nchi, na malaika zake wakatupwa pamoja naye.

10  Nikasikia sauti kuu mbinguni, ikisema, Sasa kumekuwa wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa maana ametupwa chini mshitaki wa ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za Mungu wetu, mchana na usiku.

11  Nao wakamshinda kwa damu ya Mwana-Kondoo, na kwa neno la ushuhuda wao; ambao hawakupenda maisha yao hata kufa.

12  Kwa hiyo shangilieni, enyi mbingu, nanyi mkaao humo. Ole wa nchi na bahari! KWA MAANA YULE IBILISI AMESHUKA KWENU MWENYE GHADHABU NYINGI, akijua ya kuwa ana wakati mchache tu”.

Umeona hapo mstari wa 12, maandiko yanasema yule ibilisi aliposhindwa alitupwa chini mwenye ghadhabu nyingi, na anashuka kujilipiza kisasi kwa kufanya vita na hao wakaao juu ya nchi na bahari kutokana na kushindwa kwake vita mbinguni. Na hapa tumeshapata jibu kwanini shetani anafanya vita na sisi wanadamu?.. sababu si nyingine Zaidi ya kisasi alichonacho, lakini ashukuriwe Kristo YESU Bwana wetu yupo katika mkono wa kuume akituombea (Warumi 8:34) .

Lakini tukizidi kusoma maandiko hayo mpaka ule mstari wa 17  bado tunaendelea kuona kisasi cha shetani baada ya kushidwa tena vita dhidi ya yule ya yule mtoto (YESU KRISTO) na dhidi ya yule mwanamke (Israeli).

Ufunuo 12:13 “Na joka yule alipoona ya kuwa ametupwa katika nchi, alimwudhi mwanamke yule aliyemzaa mtoto mwanamume.

14  Mwanamke yule akapewa mabawa mawili ya tai yule mkubwa, ili aruke, aende zake nyikani hata mahali pake, hapo alishwapo kwa wakati na nyakati na nusu ya wakati, mbali na nyoka huyo.

15  Nyoka akatoa katika kinywa chake, nyuma ya huyo mwanamke, maji kama mto, amfanye kuchukuliwa na mto ule.

16  Nchi ikamsaidia mwanamke; nchi ikafunua kinywa chake, ikaumeza mto ule alioutoa yule joka katika kinywa chake.

17  Joka akamkasirikia yule mwanamke, AKAENDA ZAKE AFANYE VITA JUU YA WAZAO WAKE WALIOSALIA, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu; naye akasimama juu ya mchanga wa bahari”.

Umeona tena hapo?.. baada ya Ibilisi kumshindwa “mtoto na yule mwanamke” anapanga tena malipizi juu ya uzao wake, hiyo yote ni kuonyesha roho mbaya ya kisasi aliyonayo adui.

Vivyo hivyo, mpaka leo hiyo roho anayo pamoja na mapepo yake, yakishindwa vita yanaenda kutafuta wengine kumalizia hasira zao, kwahiyo ni muhimu sana pia kuomba maombi ya kufunga na kuzuia hizo roho zisiende kuleta madhara sehemu nyingine ya maisha ya watu unaohusiana nao!.

Na huu ndio umuhimu wa kuwaombea wengine, na pia ndio umuhimu wa kuomba.. Usipokuwa mwombaji na kusubiri kuombewa tu mara kwa mara, upo katika hatari ya kuvamiwa na maroho ya malipizi kutoka katika kila kona (kutokana na maombi ya wengine) endapo hawatafunga hizo roho. Kwahiyo ni muhimu sana kuomba na kuwaombea wengine.

2Wakorintho 10:4 “(maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;)

5  tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo;

6  tena tukiwa tayari kupatiliza maasi yote, kutii kwenu kutakapotimia”

Bwana akubariki.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

HIZO NDIZO ROHO ZA MASHETANI.

USILIPIZE KISASI.

UFUNUO: Mlango wa 12

JINSI YA KUPIGANA MAOMBI YA VITA.

Nini maana ya Dirii, Chapeo na Utayari?

Rudi nyumbani

Print this post