Category Archive Mafundisho

JINSI YA KUSIMAMA NA KUFUNDISHA/ KUHUBIRI

Ni kanuni gani ya kuzingatia wakati wa kuhubiri/kufundisha ili usimzimishe Roho?.

Kuna vita vikubwa sana vya kiroho vinavyoinuka muda mchache kabla ya kusimama kufundisha/kuhubiri ambavyo ni lazima mkristo avijue na ajue jinsi ya kuvishinda ili injili ya Bwana isizuilike.

Baada ya kuandaa somo kwa kuongozwa na Roho Mtakatifu, hatua inayofuata ni wewe kwenda kuwasilisha ujumbe ulioupokea mbele ya mtu au watu. Sasa ni muhimu kujua kanuni za kuwasilisha ujumbe ili usije ukamzimisha Roho, kwasababu Roho Mtakatifu pia anaweza kuzimishwa ndani ya mtu na mtu mwenyewe, na shetani ndicho anachokitafuta hicho, lengo lake Injili isiwafikie wengine.

(Kumbuka shetani mwenyewe hawezi kumzimisha Roho Mtakatifu, kwasababu Roho Mtakatifu ana nguvu kuliko yeye), anachokifanya shetani ni kuzikoroga hisia za mtu ili zisiruhusu Roho Mtakatifu kufanya kazi ndani yake. Na neno linatuambia kuwa “tusimzimishe Roho”

1Wathesalonike 5:19  “Msimzimishe Roho”.

Wengi huwa wanamzimisha Roho Mtakatifu wakati wa kusimama kufundisha/kuhubiri pasipo wao kujijua..unakuta wakati wanaandaa somo/mahubiri wanakuwa katika uwepo mkubwa sana lakini wakati wa kufundisha au kuhubiri ule uwepo au ile hali ya kutiririka inapotea, na hivyo kumfanya huyu mtu ajihisi Mungu hayupo naye au kamwacha.

Kiuhalisia huyu mtu hajaachwa na Roho Mtakatifu, isipokuwa hali yake ya ndani imezuia utendaji kazi wa Roho Mtakatifu.

Sasa yafuatayo ni mambo ya kuzingatia ili Roho asizime ndani yako, (kule kutiririka kusikome), na ule ujumbe wa Roho Mtakatifu ulioupokea ufike kwa walengwa kama Roho alivyokufunulia.

1.Usijipange kwa maneno mengi.

Epuka kujipanga kwa maneno mengi;  Maneno mengi yanazuia kutiririka kwa Roho Mtakatifu, wengi wanadhani kuwa na maneno mengi ndiko kueleweka, pasipo kujua kuwa anayewagusa watu na kuwafanya waelewe ni Roho Mtakatifu, hivyo ukifuata kanuni ya Roho Mtakatifu utaeleweka tu na utakuwa na matunda.

Unapojiandaa kwa maneno mengi, utajikuta unategemea yale maneno yako, na hivyo wakati Roho Mtakatifu anataka kuingiza mada nyingine katika akili yako wakati wa kufundisha ule ukuta wa maneno uliojiwekea unazuia kinywa cha Roho Mtakatifu kifanye kazi, na hivyo utajikuta unafundisha kwa akili zako, na yale maneno uliyoyaandaa yanapokwisha unajikuta na wewe umekauka, huna cha kusema Zaidi.

Kwahiyo jiandae kwa maneno machache tu!, hata kama unaona somo litakuwa ni fupi sana, Roho Mtakatifu ndio anataka iwe hivyo, ili hayo maneno mengine ayajazie yeye, ukiweka desturi hiyo siku zote utaona muda hautoshi, utaona daftari lako lina maneno machache uliyoyaandaa, lakini muda uliofundisha ni madakika mengi au masaa mengi, ukiona hiyo hali imekutokea jua sio wewe uliyekuwa unafundisha bali ni Roho Mtakatifu ndani yako.

2. Usifikiri fikiri.

Kufikikri fikiri ni nini utaenda kusema au kuhubiri, kunazima kinywa cha Roho Mtakatifu. Unapofika wakati wa kwenda kufundisha wengi huwa wanapaniki na kuwaza mara nyingi nyingi ni nini wataenda kusema, na hivyo kujikuta kulazimisha kupanga maneno ya kuzungumza kuanzia mwanzo hadi mwisho. Ukiona hiyo hali inakujua ndani yako dakika chache kabla ya kusimama kufundisha au kuhubiri ikatae!. Kwani ni adui anataka kutumia fikra zako kumzimisha Roho ndani yako.

Siku zote usijiangalie hali uliyonayo kifikra wakati wa kwenda kufundisha, hata kama hukumbuki chochote, wewe tulia mpaka wakati utakapofika wa kusimama, funga fikra zako kufikiri ni nini utaenda kufundisha au kuhubiri, ukiona mawazo hayo yanakujia hamisha fikra zako kwa kutafakari mambo mengine ya kiMungu au soma Neno, kwasababu wakati huo ndio wakati wa vita vikali, shetani anatumia nguvu kubwa sana kumshambulia mtu katika hii hatua.

Hivyo funga fikra zako na subiri ule wakati wa kufundisha Roho Mtakatifu atakupa cha kusema wakati ule ule utakaposimama kufundisha.

Kanuni kama hii Bwana Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wakati wakipelekwa mbele ya watu wa Mataifa, akawaambia wasifikiri fikiri watakavyojibu kwani watapewa kinywa saa ile ile watakaposimamishwa.

Mathayo 10:19 “ Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema

20  Kwa kuwa si ninyi msemao, bali ni Roho wa Baba yenu asemaye ndani yenu”.

Kwahiyo na wewe usiwe mtu wa kufikiri fikiri utakavyosema, subiri ule muda utakapofika utapewa kinywa cha kusema, ambacho hata wewe mwenyewe utajishangaa.

3. Usijiangalie udhaifu wako na Jiachilie

Usijipime kwa kujiangalia udhaifu wako, kama unajua kuhubiri au la!, kama una kigugumizi au la!, kama una uzoefu au la!..Kwani kinywa chochote kilichovuviwa na Roho Mtakatifu kina nguvu kwasababu kimebeba ujumbe wa Roho Mtakatifu.

Hivyo kabla ya kwenda kufundisha weka kando udhaifu wako, weka kando kumbukumbu za nyuma ambazo unahisi uliwahi kukosea, weka kando hisia kwamba husikilizwi au hueleweki, au unapotezea watu muda.

Zungumza kile kinachokuja kinywani mwako muda ule kwa ujasiri wote, (achilia moyo wako na fikra zako), wala usijilinganishe na yeyote wala usitafute kufundisha kama mtu Fulani unayemjua, hapo utaona Roho Mtakatifua atakavyokutumia na utakavyomhisi akitenda kazi ndani yako kwa viwango vingine.

4. Usiongozwe na  muda.

Ukiona hofu ya kuwahi kumaliza inaingia ndani yako, ikatae hiyo hali!.. Kwasababu ni mbinu nyingine ya shetani kumzimisha Roho Mtakatifu ndani yako (Kumbuka tena shetani mwenyewe hawezi kumzimisha Roho Mtakatifu, kwasababu Roho Mtakatifu ana nguvu kuliko yeye), anachokifanya shetani ni kuzikoroga hisia zako ili zisiruhusu Roho Mtakatifu kufanya kazi ndani yako.

Kwahiyo  hofu ya muda ikatae. Kama umepewa lisaa la kufundisha, usianze kuwaza utasema nini kwenye hilo lisaa lote (hiyo sio kazi yako) ni kazi ya Roho Mtakatifu, ukianza kuwaza utasema nini muda wote huo wakati utakapofika hofu iliyopo ndani yako itamzuia Roho Mtakatifu kusema kupitia wewe. Wewe anza kufundisha kana kwamba utamaliza dakika tano zijazo, na utaona Roho Mtakatifu atakachokifanya!.. Kama atapenda umalize ujumbe kwa dakika hizo hizo tano, wala usiogope!, ndivyo alivyotaka yeye, na kama atakusudia ufundishe kwa kwa lisaa au masaa mawili, atakupa maneno na utashangaa yametoka wapi.. Kwahiyo ondoa hofu ya muda!.

5. Wahusishe watu katika kufundisha kwako

Hii ni njia nyingine ya kuendeleza uwepo uwepo wa Roho Mtakatifu usikatike ndani yako, tumia muda kuwauliza maswali unaowafundisha kama unaweza kufanya hivyo, au kuwapa jukumu la kusoma mistari ya biblia n.k

Hizi ni baadhi ya njia chache utakazoweza kuzitumia ili Kile Roho Mtakatifu alichokufunulia kiweze kuwafikia walengwa.

Kwahiyo kwa hitimisho ni kwamba kabla ya kwenda kusimama kufundisha ZILINDE SANA FIKRA ZAKO!.. Kwasababu hizo ndizo shetani anashughulika nazo kuharibu mambo.

Bwana akubariki.

Ikiwa hukupata somo la “Jinsi ya kuandaa somo basi wasiliana nasi kwa njia ya inbox”

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Jinsi ya kuandaa Somo la kufundisha

Wanikolai ni watu gani? Katika biblia?

JE! UMEPOKEA KWELI ROHO MTAKATIFU?

Roho Mtakatifu ni nani?.

MASOMO MAALUMU KWA WANAWAKE.

Rudi nyumbani

Print this post

KAMA MKRISTO NI LAZIMA UWE NA DESTURI HII.

Je biblia inatufundisha wakristo kuwa na desturi?.

Jibu ni Ndio!, Biblia inatufundisha kuwa na desturi, ikiwa na maana kuwa desturi ina nyongeza kubwa sana katika Imani ya mkristo.

Sasa desturi ni nini?

Desturi ni kitu chochote mtu anachokifanya kwa kurudia rudia.(Ni Kanuni ya daima ya mtu)

Sasa si kila desturi ni nzuri lakini zipo chache zilizo nzuri, na leo tutaenda kutazama moja ambayo kila mkristo lazima awe nayo.

  1. KUKUSANYIKA

Hii ni desturi ya kwanza na ya msingi  tunayopaswa kuwa nayo, ambayo biblia imeihakiki!

Kukusanyika katika ibada, semina, na mikutano ni jambo ambalo linapaswa liwe desturi ya kila mkristo (maana yake mtu akilala akiamka anapaswa ajue kuwa kukusanyika ni sehemu ya maisha yake) na si jambo la kuamua leo kukusanyika na kesho kutokukusanyika. Biblia inatufundisha kuwa ni lazima liwe desturi kwetu,…sasa utauliza hilo tunalisoma wapi katika biblia..

Waebrania 10:25 “WALA TUSIACHE KUKUSANYIKA PAMOJA, kama ilivyo DESTURI YA WENGINE; bali tuonyane; na kuzidi kufanya hivyo, kwa kadiri mwonavyo siku ile kuwa inakaribia”.

Umeona?

Kumbe kukusanyika ilikuwa ni desturi ya kundi Fulani la watu wa Mungu, na hapa biblia inatufundisha hayo hayo, kwamba na sisi tusiache kukusanyika KAMA ILIVYO DESTURI YA WENGINE. Maana yake inapaswa iwe desturi yetu na sisi, liwe jambo endelevu.

Kukusanyika ibadani hakupaswi kuwa tendo la leo kuamua na kesho kutoamua, bali linapaswa liwe desturi, iwe unajisikia au hujisikii, kukusanyika ni lazima iwe desturi yako, shetani amewafumba watu macho wasione kama kukusanyika ni desturi badala yake waone kama ni tendo kujisikia au kutojisikia, na hivyo kuwanyonyea Baraka zao!

Hivyo atakachokifanya ni kuwatengenezea udhuru  na vijisababu kwenye vichwa vyao ili awafanye wasikusanyike na wengine.

Zifuatazo ni sababu kuu nne (4) za kuzikataa na kuzikimbia ambazo zitaharibu desturi yako njema ya kukusanyika na wengine.. kwasababu zinatoka kwa shetani.

1.Nimechoka:

Hii ni sababu ya kwanza ya kuikataa kwasababu hata siku nyingine za wiki unakuwa umechoka lakini huachi kwenda kwenye majukumu yako. Kwahiyo kama ilivyo desturi yako kwenda kazini, basi na kwenda kanisani kufanye kuwa desturi yako.

2.Naumwa:

Hii ni sababu ya pili yenye nguvu inayotoka kwa shetani, hata kama unasikia kuumwa kiasi gani usiache kukusanyika ibadani, kwasababu huko huendi kuongeza ugonjwa bali kuuondoa, kwasababu ugonjwa uliopata umetoka kwa shetani na kanisani shetani hayupo!.

Kama utakuwa na uwezo wa kuamka na kwenda hospitali pamoja na kwamba ni mgonjwa, kwanini usiamke na kwenda kanisani mahali penye uponyaji wa kiungu?

3.Mvua:

Hii ni sababu ya tatu ya shetani, ambayo inaharibu desturi ya wengi ya kwenda ibadani. Mvua isikuzuie kwenda ibadani.. bali nunua mwavuli na makoti ya mvua, na dhamiria kuwa iwe jua au mvua ni lazima ufike ibadani, kama mvua haiwezi kukuzuia kwenda kutafuta riziki za kimwili kwanini ikuzuie kwenda kutafuta riziki za kiroho?

4.Dharura

Dharura ni kitu chochote kinachonyanyuka wakati wa wewe kwenda ibadani, na hizo zinaweza kuwa ni za kikazi, familia, na nyinginezo..  Utakuta mtu anapigiwa simu na kuombwa ahudhurie mahali Fulani, na pasipo aibu ya uso anakubali na ilihali anajua kabisa siku hiyo ni maalumu kwa Mungu wake kukusanyika na wengine, lakini mtu huyo huyo akipokea simu siku za kazi yupo radhi kukataa kuvunjiwa ratiba zake za kazini na kuiheshimu kazi yake, lakini Nyumbani kwa Mungu kwake si kitu, Ukatae huo udhuru utaharibu desturi yako iliyo njema.

Na zipo sababu nyingine nyingi, hizi ni chache tu, lakini katika hizo zote kataa visababu lakini jenga Desturi.. Huenda Desturi yako leo imeharibiwa na shetani, lakini Bwana Yupo kukusaidia ndio maana unayasikia haya leo.

Unachopaswa kufanya kuanzia leo ni kuomba rehema na kisha kutendea kazi hiki unachokisikia kuanzia leo, weka ratiba ambayo haibadiliki. Kwasababu desturi ya kwenda kanisani imehakikiwa na Roho Mtakatifu kuwa ni desturi njema. Hatuhitaji kuongozwa na Roho Mtakatifu au kupokea maono ya kwenda kanisani au la! Biblia tayari imeshatuelekeza kuwa inapaswa iwe desturi yetu.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Je ni kweli ilikuwa desturi ya Bwana kuishika sabato?(Luka 4:16)

TUSIIFUATISHE KAWAIDA YA ULIMWENGU HUU.

EPUKA KUCHELEWA IBADA.

KATAA KUWA EUTIKO, WA KUSINZIA IBADANI.

Uishi kwa furaha pamoja na mke umpendaye, siku zote

Rudi nyumbani

Print this post

Ni kwa namna gani haki huinua taifa? (Mithali 14:34)

Pia kwa kupokea mafundisho ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP, jiunge na channel yetu kwa kubofya link hii >> https://whatsapp.com/channel/0029VaBVhuA3WHTbKoz8jx10

Swali: Maandiko yanasema “Haki huinua Taifa”.. Je hii imekaaje kiundani zaidi?

Jibu: Tusome,

Mithali 14:34 “HAKI HUINUA TAIFA; Bali dhambi ni aibu ya watu wo wote”.

Kwa tafsiri ya kawaida mtu mwenye haki ni yoyote yule anayefanya matendo ya haki bila kujali kile anachokiamini, lakini kibiblia ni tofauti kidogo…Kibiblia  mtu “mwenye haki” ni yule anayemcha Mungu na “asiye haki” ni yule asiyemcha Mungu.

Kwahiyo hata kama mtu atajitahidi kufanya matendo mazuri na yenye kukubalika katika jamii yake yote, lakini kama moyoni mwake hamwamini Mungu, huyo kibiblia ni mtu asiye haki hata kama ana sifa njema.

Kwahiyo wanapoongezeka watu wanaomcha Mungu wengi katika Taifa maana yake “Haki na yenyewe inazidi kuongezeka”. Na matokeo ya kuwepo Wenye haki wengi juu ya nchi kuliko wasio haki ni kunyanyuka kwa Taifa, na kinyume chake wanapokuwepo wasio haki wengi katika nchi kuliko wenye haki basi Taifa linakuwa hatiani kuanguka. Sasa utauliza ni kwa namna gani?.. Hebu tujikumbushe kidogo ile habari ya Ibrahimu na Elohimu wakati ule wa Maangamizi ya Sodoma na Gomora

Mwanzo 18:22 “Basi wale watu wakatoka huko wakaelekea Sodoma; lakini Ibrahimu alikuwa akali akisimama mbele za Bwana.

23 Ibrahimu akakaribia, akasema, JE! UTAHARIBU MWENYE HAKI PAMOJA NA MWOVU? 

24 Huenda wakawapo wenye haki hamsini katika mji, utaharibu, WALA HUTAUACHA MJI KWA AJILI YA HAO HAMSINI WENYE HAKI WALIOMO? 

25 Hasha usifanye hivyo, ukamwue mwenye haki pamoja na mwovu, mwenye haki awe kama mwovu. Hasha; Mhukumu ulimwengu wote asitende haki? 

26 BWANA AKASEMA, NIKIONA KATIKA SODOMA WENYE HAKI HAMSINI MJINI, NITAPAACHA MAHALI POTE KWA AJILI YAO. 

27 Ibrahimu akajibu, akasema, Basi, nimeshika kusema na Bwana, nami ni mavumbi na majivu tu.

28 Huenda wakapunguka watano katika wale hamsini wenye haki, je! Utaharibu mji wote kwa kupungua watano? Akasema, Sitauharibu, nikiona humo arobaini na watano. 

29 Akazidi tena kusema naye, akinena, Huenda wakaonekana humo arobaini? Akasema, Sitafanya kwa ajili ya hao arobaini. 

30 Akasema, Bwana asiwe na hasira, nami nitasema, Huenda wakaonekana huko thelathini? Akasema, Sitafanya, nikiona humo thelathini. 

31 Akasema, Tazama, nimeshika kusema na Bwana, huenda wakaonekana huko ishirini? Akasema, Sitaharibu kwa ajili ya hao ishirini. 

32 Akasema, Bwana asiwe na hasira, nami nitasema mara hii tu, Huenda wakaonekana huko kumi? Akasema, Sitaharibu kwa ajili ya hao kumi.

 33 Basi Bwana alipokwisha kuzungumza na Ibrahimu, akaenda zake; Ibrahimu naye akarudi mahali pake”.

Umeona? Kumbe Miji ya Sodoma na Gomora iliteketea kwasababu ya kukosekana wenye haki ndani yake, kumbe wangeonekana tu wenye haki 10, basi miji ile yote ingepona!…lakini walipokosekana ndipo miji ile ikaanguka na kuangamia.

Ikiwa na maana kuwa Amani ya Miji na Mataifa ni kwasababu ya wenye haki ndani yake, ni kwasababu ya watu wa Mungu kuwepo ndani yake, hao wakiondolewa Taifa au mji unaanguka na kuangamia.

Ndio maana maandiko yanazidi kutufundisha kuwa dhiki kuu haitaanza mpaka Kanisa (wenye haki) watakapoondolewa, ikimaanisha kuwa uwepo wa watu wa Mungu katika dunia ndio unaozuia mambo kuharibika.. lakini hao watakapoondolewa ndipo Mataifa yataanguka, na ulimwengu mzima kwa ujumla.

2Wathesalonike 2:6  “Na sasa lizuialo mwalijua, yule apate kufunuliwa wakati wake.

7  Maana ile siri ya kuasi hivi sasa inatenda kazi; LAKINI YUKO AZUIAYE SASA, HATA ATAKAPOONDOLEWA.

8  Hapo ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake”

Je na wewe ni miongoni mwa wenye haki?

Kumbuka katika zama hizi tunahesabiwa haki mbele za Mungu kwa njia ya kumwamini Yesu Kristo… Na si kwa matendo yetu yasiyo na Imani yoyote…

Wagalatia 2:16 “hali tukijua ya kuwa mwanadamu hahesabiwi haki kwa matendo ya sheria, bali kwa imani ya Kristo Yesu; sisi tulimwamini Kristo Yesu ili tuhesabiwe haki kwa imani ya Kristo, wala si kwa matendo ya sheria; maana kwa matendo ya sheria hakuna mwenye mwili atakayehesabiwa haki”.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Mataifa ni nini katika Biblia?

Ipi tofauti ya Falme, Mamlaka na Wakuu wa giza (Waefeso 6:12)

TUNA WAJIBU WA KUOMBEANA KWA KINA.

Rudi nyumbani

Print this post

Katika kila kazi mna faida; Bali maneno ya midomo huleta hasara tu.

SWALI: Nini maana ya huu mstari?

Mithali 14:23 “Katika kila kazi mna faida; Bali maneno ya midomo huleta hasara tu”


JIBU: Kitabu cha Mithali na Mhubiri ni vitabu vilivyobeba mafunzo mengi sio tu yale ya kiroho bali pia hata ya maisha ya kawaida. Mstari huo unaelezea uzito wa kitu kinachotendewa kazi zaidi ya kile kinachozungumzwa tu. Kwamfano hapo anaanza kwa kusema “katika KILA KAZI mna faida”.. Maana yake ni kuwa katika kazi yoyote (iliyonjema), inafaida nyuma yake,. Iwe ni ya kudharaulika au yenye heshima, iwe ni ngumu iwe ni rahisi, iwe ni ya kipato kikubwa au kidogo, maadamu kazi fulani inatendeka ni lazima faida tu itaonekana nyuma yake.

Lakini mtu akiwa ni wa mipango mikubwa, mikakati mingi, akili nyingi za kubuni namna ya kutenda kitu Fulani, vikao vingi,  halafu hakitendei kazi, Bwana anasema, badala ya faida kinyume chake ni hasara tu atapata..

Vivyo hivyo na katika roho. Bwana anataka tuwe watendaji wa Neno lake, Sio kusikia tu au kuomba tu peke yake. Unaweza ukaomba usiku kucha lakini kama sio mtendaji wa Neno lake uliombalo, ni unapoteza nguvu tu.

Kwamfano unaomba Bwana akusaidie uushinde uasherati, lakini bado unashikamana na vichocheo vyake vyote, una picha chafu kwenye simu yako, kinywa chako kinazungumza mambo ya kizinzi na vijana wenzako, unachati na watu wa jinsia tofauti muda wote, unatazama tamthilia zenye maudhui hayo, unasikiliza miziki ya kidunia, unaishi na boyfriend/girlfriend. Unategemea vipi tamaa zisikutawale? Utaomba usiku kucha na hutaona matokeo yoyote, kwasababu hukitendei kazi kile unachokiomba.

Bwana alisema kama vile mwili bila roho umekufa, vivyo hivyo imani bila matendo imekufa ndani yake.(Yakobo 2:17). Kukitendea kazi kile kimoja ukiombacho, kina nguvu sana kuliko maneno elfu unayoweza kumwomba Mungu mwaka mzima.

Yakobo 1:22  “Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu. 23  Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo. 24  Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo”.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Nini maana ya “katika wingi wa hekima mna wingi wa huzuni”.

Nini maana ya huu mstari? “Yeye mwenyewe ataokolewa lakini ni kama kwa moto”

Mithali 14:4 ‘Zizi ni safi ambapo hapana ngombe;

Marijani ni nini katika biblia(Ayubu 28:18,Mithali 8:11)?

Nini maana ya mhubiri 9:11? si wenye mbio washindao katika michezo?

BWANA UNIJULISHE MWISHO WANGU.

Rudi nyumbani

Print this post

HATA WAKATI WENU WA MVI NITAWACHUKUENI. (Isaya 46:3)

Isaya 46:3 “Nisikilizeni, enyi wa nyumba ya Yakobo, ninyi mlio mabaki ya nyumba ya Israeli, mliochukuliwa nami tangu tumboni, mlioinuliwa tangu mimbani; 

4 na hata uzee wenu mimi ndiye, na hata wakati wenu wa mvi nitawachukueni; nimefanya, nami nitachukua; naam, nitachukua na kuokoa”.

Mstari huu wa faraja unatuonyesha fadhili za Mungu jinsi zilivyo nyingi kwa watu wake, Anaonyesha jinsi asivyoweza kuwaacha watu wake, tangu wakiwa tumboni mwa mama zao hadi kufikia uzee wao. Kila hatua ya maisha yupo nao, kila pito liwe rahisi au liwe gumu yupo nao, wakiwa watoto, wakafikia ujana, kisha nguvu zikaisha wakiwa wazee, Mungu yupo nao. Haleluya.

Daudi alilitambua hilo pindi alipoishiwa nguvu zake, akaandika…

Zaburi 37:25 “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, Lakini sijamwona mwenye haki ameachwa Wala mzao wake akiomba chakula”.

Hivyo huna haja ya kuhofu kesho yako itakuwaje au uzee wako utaishaje, maadamu upo na Bwana, maadamu unamtumikia, siku hizo zikifika, atakuhifadhi Mungu wako. Mwingine anasema mpaka sasa sina mfuko wa mafao, na nguvu zangu zinakaribia kuisha, ni nani atakayenisaidia, ni nani atakayekuwa karibu na mimi? Jibu ni kuwa  Bwana ndiye atakayekuwa karibu na wewe. Kwasababu tangu zamani ulimtumainia. Lakini hata kama utakuwa na mali, huwezi kuwa na raha moyoni wakati huo endapo Kristo hayupo nafsini mwako sasa.

Hivyo wekeza maisha yako kwa Bwana sasa, ili kesho yako pia iwe na matumaini na raha tele. Ikiwa wewe ni kijana wakati huu uliopo, mtafute muumba wako, upokee WOKOVU kwa kumaanisha kabisa kuuacha ulimwengu, mtumikie Mungu, kimbia kweli kweli tamaa za ujanani, kabla zile nyakati mbaya za hatari hazijafika, Kwasababu maandiko yanasema kuna siku-mbaya mbeleni zitawakumba watu ambao hawakumcha Mungu tangu zamani.

Mhubiri 12:1 “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, Kabla hazijaja siku zilizo mbaya, Wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo”.

Ikiwa upo tayari kutubu dhambi zako leo , na kumkaribisha Bwana Yesu maishani mwako, basi bofya hapa kwa mwongozo wa sala hiyo ya toba >>>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

TUTAMKARIBIA MUNGU KWA IDADI YA MVI ZETU ROHONI.

Je! Wana wenu huwatoa kwa nani? maana yake ni nini?

NINYI AKINA BABA MSIWACHOKOZE WATOTO WENU

UFANYE WEMA WAKO KATIKA MAARIFA.

ANGALIENI MWITO WENU.

Praitorio ni nini? Na Kwanini ilikuwa ni najisi kwa wayahudi kuingia humo? (Yohana 18:28)

Afadhali mtu akutwe na dubu aliyenyang’anywa watoto wake.

Rudi nyumbani

Print this post

Maana ya ‘taabu haitoki mchangani, Wala mashaka hayachipuki katika nchi’ ni nini?

Ayubu 5:6 “Kwani taabu haitoki mchangani, Wala mashaka hayachipuki katika nchi;”

Watu wengi tumekuwa tukilaumu mazingira, tukilaumu wanyama, tukilaumu ardhi, na vitu vingine vya asili kuwa ndio chanzo cha matatizo yetu, chanzo ya shida zetu na mashaka yetu rohoni. Lakini maandiko yanatupa uhalisia kwamba taabu na mashaka havichupuki ardhini, kama vile mchicha umeavyo, bali vinatoka ndani yetu wenyewe.

Makosa  yetu ndio zao la kila aina ya matatizo yetu. Asili ya migogoro katika ndoa, sio ule m-buyu uliokaribu na nyumba zetu. Unaweza kuhama hata nchi ukakaa chini ya mizeituni na mizabibu mizuri, na maua, lakini bado ndoa yako ikaendelea kuwa na matatizo tena makubwa zaidi  hata yale ya mwanzo.

Sababu ya kuteswa na mapepo, sio Yule paka mweusi wa jirani anayekuja kulala batini kwako kila siku usiku. Bali ni kwasababu Kristo hayupo ndani yako.

Sababu ya kutokupiga hatua kiroho, sio hiyo ardhi unayoishi, au unayoimiliki, usihangaike na maombi ya kufungua/ kukomboa ardhi, hangaika na vifungo vilivyomo ndani yako. Ambavyo vinatokana na aidha kutolielewa Neno la Mungu, au kuwa nje ya wokovu.

Biblia inasema..

Yohana 8:36  Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli.

Na tena inasema…

Yohana 8:32  “tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru”.

Rekebisha mwenendo wako, pokea wokovu wa kweli, kisha liishi Neno la Kristo kila siku. Hakika utaona jinsi tatizo lako linavyotalika kirahisi, ndipo utaacha kuyalaumu mazingira ya nje.

Ayubu 5:6 “Kwani taabu haitoki mchangani, Wala mashaka hayachipuki katika nchi;”

Je! Umeokoka?  Kama bado unasubiri nini? Je! Unatambua kuwa hizi ni siku za mwisho, na Kristo yupo mlangoni kurudi, tunaishi katika muda wa nyongeza tu, siku yoyote unyakuo wa kanisa unapita, watakatifu kuchukuliwa mbinguni na wenye dhambi kwenda motoni?. Fanya uamuzi sahihi sasa, ikiwa upo tayari kuokoka leo, basi fungua hapa kwa mwongozo huo >>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

MTU MWENYE KUSITA-SITA KATIKA MAWAZO MAWILI.

LAKINI WAKATI WA TAABU WATASEMA, SIMAMA UKATUOKOE.

Rafiki hupenda sikuzote; Na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 9 (Kitabu cha Ayubu).

Uasherati wa Kiroho maana yake nini?

Rudi nyumbani

Print this post

JE! UPO KATIKA MAJI YA UTULIVU?

Shalom, nakusalimu katika jina la Yesu Kristo mwokozi wetu. Karibu tujifunze maneno ya uzima maadamu siku ile inakaribia.

Katika siku hizi za mwisho ni lazima uwe makini sana na mahali ulipo, kwasababu zama zimebadilika, si kila jambo la kuliamini, vilevile si kila jambo la kutoliamini. Unamuhitaji Roho Mtakatifu sana kukusaidia kuchagua kilicho sahihi.

Bwana anatufananisha sisi na kama kondoo, na yeye kama mchungaji. Na sikuzote, mchungaji mwema, huwa anawapeleka kondoo wake katika maji ya mito-salama. Na si kila mto ilimradi mto tu anawapeleka kondoo zake kunywea maji hapana, bali pale tu palipo na maji ya utulivu ndipo anapowapeleka kondoo zake.

Ndio maana katika Zaburi ya 23 Inasema;

Zaburi 23:1 ‘Bwana ndiye mchungaji wangu, Sitapungukiwa na kitu.  2 Katika malisho ya majani mabichi hunilaza, Kando ya maji ya utulivu huniongoza’.

Ni kwanini maji ya utulivu, kwasababu maji yenye mvurugano, au yaliyotibuliwa yana hatari nyingi, huwenda ni makao ya viboko na mamba na hivyo kutembea kwao huko ndio kunafanya maji Yale yawe na mvuragano, kwahiyo kondoo akinywa maji pale yupo hatarini kuvutwa na mamba, akafanyika kitoweo.

Au huwenda maji hayo ni mkondo wa mafuriko, hivyo kitu chochote kitakachotelezea kule mtoni, si rahisi kupona kinyume chake ni kitasombwa na kupotelea mbali.

Hivyo maji yasiyotulia, si salama kwa mifugo. Na mchungaji apendaye kondoo huwa hawapeleki mifugo yake hapo.

Ndivyo ilivyo kwa Kristo, anapotuokoa, anatuongoza kwa Roho wake malipo na maji ya utulivu tukae hapo tunywe. Lakini tatizo linakuja ni sisi kuyakataa maji ya utulivu, tunayatafuta maji ya mivurugano.

Ndugu usiangalie ukubwa wa mto, au ukubwa wa Bwawa, haikuhitaji wewe kunywa mto mzima ndio ukate kiu yao. Naamanisha usiangalie wingi wa watu, au ukubwa wa jengo na madhabahu iliyopambwa, au utajiri wa kanisa ndio ufikiri kuwa hapo ni salama kwa roho yako. Bali tazama palipo na utulivu wa kiroho. Hapo ndipo utulize nafsi yako. Kwasababu unaweza kwenda mahali kwa lengo la kuikata kweli kiu yako kwa Bwana lakini kinyume chake ukakutana na mamba wakali wakakumaliza kabisa.

Palipo na maji salama ni wapi?

Kwanza ni pale Palipo na fundisho la Yesu: Yesu ndio maji yenyewe tulivu ya uzima, na sio nabii au mtume au askofu, au kanisa, au pesa, au umaarufu.. Hivyo angalia kiini cha fundisho unalofundishwa mahali ulipo, je yote yanalenga kukukuza kumjua Yesu au linakupeleka katika mambo mengine? Fikiri Tangu umekaa hapo, ni nini umeongeza katika kulijua Neno la Kristo katika kweli yote. Lakini Kama umejazwa maarifa ya ki-mwili tu zaidi yale ya Kristo, yaani  ya ki-ndoa, ki-uchumi, uchawi, biashara,pesa, hiyo ni injili nyingine, ni mafuriko ya adui, hakuna maji tulivu hapo, utazombwa na kuangamia kabisa.

Yohana 4:13  “Yesu akajibu, akamwambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena; 14  walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujikia uzima wa milele”

Palipo na Upendo: Hicho ni kigezo cha pili.

Yakobo 3:16  “Maana hapo palipo wivu na ugomvi ndipo palipo machafuko, na kila tendo baya”.

Katika mkusanyiko wowote, fundisho la tendo la upendo wa ki-ndugu linapuuziwa, au halihimizwi, ndani  kuna vita visivyokoma kati ya washirika, pengine huwenda na viongozi kwa viongozi, hiyo ni ishara kuwa utulivu wa Roho haupo hapo, hivyo ni hatari pia kwa maisha yako ya kiroho.

Tujitahidi sana kuwa na vipimo hivi vya kiroho katika kuchagua mahali tukusanyakapo kupata maji ya uzima, vitakusaidia sana, kwasababu hizi ni siku za mwisho, na manabii wengi na makristo wa uongo na madhehebu na dini za uongo  zimezuka kila pembe ili kuwatoa watu kwenye mstari.

Yajali maisha yako ya kiroho. Mpende Kristo na Agizo lake.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

MAFUNDISHO MAALUMU KWA WAONGOFU WAPYA.

JINSI YA KUMSIKIA MUNGU, NA KUPOKEA MAFUNUO AU JUMBE KUTOKA KWAKE.

MWENGE WAKO WA UHURU UPO WAPI?

MADHARA YA KUKOSA MAJI YA UZIMA BAADA YA KIFO.

WALIKUWA WAMECHOKA NA KUTAWANYIKA KAMA KONDOO WASIO NA MCHUNGAJI.

JE! UNAMPENDA BWANA?

Rudi nyumbani

Print this post

WENGINE WANAKESHA KWAAJILI YAKO.

Jina la Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze biblia.

Leo nataka tujifunze umuhimu wa kuchunguza mambo, kwani  tusipokuwa watu wa kuchunguza mambo basi tunaweza tusiuelewe uweza wa Mungu.

Asilimia kubwa ya watu wanaobarikiwa hawajui kuwa mafanikio yao ni kutokana na maombi ya watu wengine (ambao wanawaombea wao pasipo kujua), hivyo ni muhimu sana kufikiri wakati wa kufanikiwa.

Hebu tujifunze katika ile habari ya Kana ya Galilaya pale Bwana Yesu alipofanya muujiza wake wa kwanza wa kugeuza maji kuwa divai.

Maandiko yanasema baada ya Bwana Yesu kubadili yale maji kuwa divai, yule Mkuu wa meza, aliyeteuliwa kuandaa  vinywaji vya wageni wa kawaida na mgeni rasmi, hakujua kama ile divai mpya imetoka kwa Bwana, badala yake alidhani mwenye sherehe ndiye aliyeinunua, na ndipo akaenda kumfuata mwenye sherehe (Bwana harusi) na kumpongeza akidhani kuwa yeye ndiye kainunua ile divai mpya na kuwapa watu wote wanywe.

Na yule Bwana harusi naye akashangaa kupewa sifa ambazo si zake, huenda na yeye akadhani kuna mtu tu katikati ya sherehe kajitokeza na kujitolea kununua divai mpya ili kuimeza aibu.. kwamaana divai kuisha katikati ya sherehe na bado kuna watu wa muhimu hawajapata, ilikuwa ni aibu kubwa sana kwa wenye sherehe. Hivyo mpaka mwisho wa sherehe ni wachache sana ndio waliojua siri ya ile divai, kuwa na Bwana Yesu ndiye aliyeitoa.

Tusome,

Yohana 2:1 “Na siku ya tatu palikuwa na arusi huko Kana, mji wa Galilaya; naye mama yake Yesu alikuwapo.

2  Yesu naye alikuwa amealikwa arusini pamoja na wanafunzi wake.

3  Hata divai ilipowatindikia, mamaye Yesu akamwambia, Hawana divai.

4 Yesu akamwambia, Mama, tuna nini mimi nawe? Saa yangu haijawadia.

5  Mamaye akawaambia watumishi, Lo lote atakalowaambia, fanyeni.

6  Basi kulikuwako huko mabalasi sita ya mawe, nayo yamewekwa huko kwa desturi ya Wayahudi ya kutawadha, kila moja lapata kadiri ya nzio mbili tatu.

7  Yesu akawaambia, Jalizeni mabalasi maji. Nao wakayajaliza hata juu.

8  Akawaambia, Sasa tekeni, mkampelekee mkuu wa meza. Wakapeleka.

9  Naye mkuu wa meza alipoyaonja yale maji yaliyopata kuwa divai, (wala asijue ilikotoka, lakini watumishi walijua, wale walioyateka yale maji), yule mkuu wa meza alimwita bwana arusi,

10  akamwambia, Kila mtu kwanza huandaa divai iliyo njema; hata watu wakiisha kunywa sana ndipo huleta iliyo dhaifu; wewe umeiweka divai iliyo njema hata sasa”.

 Sasa nataka tuone nyuma ya Baraka hizo alikuwa nani?, Nyuma ya muujiza huo alikuwa nani, na nyuma ya aliyetoa aibu alikuwa ni nani?.. kisha na sisi tutapata akili wakati wa kufanikiwa.

MWOMBAJI/ WAOMBAJI.

Kulipoonekana tatizo, Marimu alienda kumwomba Bwana na kumsihi sana. Huyu ndiye aliyekuwa mwanzo wa muujiza wa divai. Kama sio Mariamu watu wangeabika kwenye sherehe hata kama sherehe hiyo Kristo alikuwepo ndani.

Vile vile hata leo, ukiona jambo Fulani la heri limetokea mbele yako lililoziba aibu yako, hebu tafakari sana, usijivune wala usikimbilie kusema wewe ni mwenye bahati, huna bahati yoyote, hayo ni matokeo ya wengine kuomba kwaajili yako..haijalishi Kristo yupo na wewe.. Hata katika ile harusi Kristo alikuwepo ndani, alikuwa ni mwalikwa, lakini bado kama pasingekuwepo mwombaji, hakuna kitu kingefanyika.

Ukiona umebarikiwa kwa jambo Fulani au mambo yako fulani fulani yameenda sawa usikimbilie kujisifu, wala kujivuna, kwamba una bahati!!…fahamu kuwa hayo ni matokeo ya wengine kuomba kwaajili yako, na hao huenda unawajua au huwajui.

Mtoto ukifanikiwa jua wakati mwingine ni matokeo ya maombi ya wazazi wako na si kwasababu wewe una akili sana au una ujanja mwingi, kijana ukifanikiwa jua ni matokeo ya maombi ya ndugu zako, au wapendwa wenzako wanaokesha kwaajili yako pasipo wewe kujua.

Unapoona unapiga hatua kimaisha au kiroho, fahamu kuwa ni matokeo ya wanaokuongoza kiroho kukuombea, wala usidhani ni kwa nguvu zako au una bahati..

Waebrania 13:17  “Watiini wenye kuwaongoza, na kuwanyenyekea; maana wao wanakesha kwa ajili ya roho zenu, kama watu watakaotoa hesabu, ili kwamba wafanye hivyo kwa furaha wala si kwa kuugua; maana isingewafaa ninyi”

Ukilifahamu hili siku zote utakuwa mnyenyekevu na kumshukuru Mungu kwa kila jambo na pia kufikiri sana kuwaheshimu wanaokuombea na hata wewe kutenga muda kuwaombea!.. Laiti yule mkuu wa Meza na yule Bwana arusi wangejua kitu Mariamu alichowafanyia, kwenda kuwaombea kwa Bwana wangeshangaa sana, na kunyenyekea sana.

Laiti ungejua mambo watu wanayomwambia Bwana kuhusu wewe, usingebaki kama ulivyo..

Amani ya familia yako, Amani ya jamii yako, Amani ya nchi yako, ni matokeo ya maombi ya watu wengine wa Mungu wanaolia mbele zake usiku na mchana.. wala si kwasababu nyingine?, kama si hao ni kitambo sana mambo ya ulimwengu yangeshaharibika..(2Thesalonike 2:7).

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

SABATO ILIFANYIKA KWAAJILI YA MWANADAMU NA SI MWANADAMU KWAAJILI YA SABATO!

Je! Siku ilihesabiwaje kabla ya jua na mwezi kuumbwa?

Je! Karamu za ‘Idi’ ndio zipo hizo tunazozisoma katika Hosea (12:9)

Ni lini na wapi Ibrahimu aliioona siku ya Bwana akashangilia?.

Je! Mwendo wa Sabato ulikuwaje kibiblia?(Matendo 1:12)

Rudi nyumbani

Print this post

SHUGHULIKA SANA NA DHAMBI YA KUSAHAU.

Nakusalimu katika jina kuu sana na lenye nguvu la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu tujifunze maneno ya uzima ya Mungu wetu.

Sisi kama Wanadamu Kila mmoja wetu haijalishi ameokoka au hajaokoka, ndani yake ameumbiwa kiwango cha “kusahau”. Hii ni karama ya Mungu na ni vizuri kumshukuru Mungu Kwa jambo hili, kwasababu kama tungeikosa wanadamu wote tusingeishi hivi tulivyo Leo.

Lakini kusahau kukisimama Mahali pasipo-papasa, inageuka kuwa hatari kubwa sana, Tena dhambi yenye matokeo mabaya sana rohoni.

Kuna aina ngapi za kusahau?

Sasa kusahau kunaweza kuwa aidha kupoteza kumbukumbu ya lile jambo au tukio, Moja Kwa Moja akilini mwako, uwe kana kwamba hujawahi kulipitia. 

Au kunaweza kuwa kulipoteza tu Kwa muda katika kumbukumbu lakini utakapokumbushwa unalikumbuka Tena.

Kusahau kwenye madhara ni kupi?.

Kabla ya kutazama ‘kusahau’ kwenye hasara tuone kusahau kwenye faida kukoje.

Kusahau kwenye faida kunatimia katika mambo yasiyo na maana, au yenye maudhui hasi kwako. Kwa mfano pale mtu unapotukanwa, au unapopigwa kikumbo barabarani na mtu usiyemjua, unaposikia miziki isiyokufaidia huko nje, unapofiwa, unapodhulumiwa, unaposemwa, unapovunjiwa heshima, unapoaibishwa, unaposingiziwa n.k… Mazingira kama haya ambayo ni hasi…kusahau Kunahitajika sana na ni lazima ujifunze kuruhusu jambo hili liumbike ndani Yako ili uponyeke kwa haraka,.maana ndio sehemu yake hiyo inapopaswa itumike.

Lakini kusahau kusikokujenga ni pale unaposahau Matendo mema, au mambo chanya yakupasayo kutenda. Kwamfano Sheria inasema ” usitupe taka hapa” Halafu inapita wiki Moja umesahau agizo hilo, unarudia tena kutupa taka pale pale ulipokatazwa..Hapo utakuwa hujitafutii jambo lingine zaidi matatizo?

Vivyo hivyo katika Neno la Mungu pale unaposahau sahau Neno la Mungu hapo ndio pabaya sana. Wakristo wengi hatujui kuwa Mungu “anayorudia kutuambia ni mengi kuliko Yale mapya anayotaka kusema nasi”..Ni Kwanini? ni kwasababu tumekuwa wepesi wa kusahau Sheria zake.

Mambo yamekuwa kinyume chake, badala tusahau yaliyo mabaya tukumbuke yaliyo mema, tunasahau mema tunakumbuka mabaya sikuzote.

Ni shambuliko kubwa sana ambalo ibilisi amelipanda mioyoni mwa wanadamu. Ndio sababu uchungu haukomi, masengenyo hayaishi, vita vinazuka Kila siku, fitna, unafki, na uongo havina mwisho ni kwasababu Hali Ile Ile tuliyokuwa nayo nyuma mpaka sasa tunairuhusu ikae kwenye akili zetu.

Wakati nguvu hiyo tungepaswa tuitumie kulihifadhi Neno la Mungu mioyoni mwetu ili Matendo chanya yaendelea kutokea ndani yetu, hatufanyi hivyo.. maandiko yanasema..

Yakobo 1:22-25

[22]Lakini iweni watendaji wa neno, wala si wasikiaji tu, hali mkijidanganya nafsi zenu.

[23]Kwa sababu mtu akiwa ni msikiaji wa neno tu, wala si mtendaji, mtu huyo ni kama mtu anayejiangalia uso wake katika kioo.

[24]Maana hujiangalia, kisha huenda zake, mara akasahau jinsi alivyo.

[25]Lakini aliyeitazama sheria kamilifu iliyo ya uhuru, na kukaa humo, asiwe msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, huyo atakuwa heri katika kutenda kwake.

Tuweke mfano, tunaweza kusoma kwenye biblia kwamba Upendo hauhesabu mabaya, Wala haujivuni, Wala hauoni uchungu n.k(1Kor 13).. Sasa wakati uliposoma hili  neno, moyoni mwako unasema nitaliishi hili Neno, lakini inapita siku mbili unashangaa umerudia kule kule, unaanza ishi maisha ya namna Ile ya kwanza,. Tatizo lipo hapo kwenye kusahau. Laiti.hilo Neno lingekuwa limeganda viizuri kwenye moyo wako, ingekuwa breki pale tu mambo mabaya yanapojaribu kuvuka mipaka.

Sasa tunawezaje kuishinda Hali hii ya kusahau sahau?

Ni kama vile mwanafunzi darasani, mara nyingi anakuwa ni mtu wa.kurudia rudia kusoma na kufanyia sana mazoezi kile alichofundishwa..lengo la kufanya vile ni kulazimisha akili yake inakili Yale mafundisho kwa muda mrefu ili atakapoingia kwenye mtihani asisahau chochote…Lakini kama akisema Mimi ni ‘genius’ sina muda wa kurudia nilivyofundishwa..ni wazi kuwa mambo mengi yatamruka, na atafeli.

Hivyo na sisi sote ni wanafunzi wa Biblia. Soma biblia Kila siku ifanye kuwa rafiki Yako, usiwe mtu wa kusoma Leo, Tena wiki ijayo au mwezi ujao, ndio unakuja kusoma tena..SoMo tafakari mambo uliyoagizwa mule na Mungu Kila siku..Ndivyo itakavyokuwa rahisi kuliishi Neno la Mungu, kinyume na hapo usijidanganye Utasahau…kwasababu mwisho wa siku yatatoka moyoni mwako, na hivyo dhambi yoyote itakayokatisha mbele Yako, utashindwa kukabiliana nayo mapema. Mungu hapendi tuwe na tabia hii ya kusahau sahau Neno lake.

Kumbukumbu la Torati 6:6-9

[6]Na maneno haya ninayokuamuru leo, yatakuwa katika moyo wako; [7]nawe uwafundishe watoto wako kwa bidii, na kuyanena uketipo katika nyumba yako, na utembeapo njiani, na ulalapo, na uondokapo. [8]Yafunge yawe dalili juu ya mkono wako, nayo yatakuwa kama utepe katikati ya macho yako. [9]Tena yaandike juu ya miimo ya nyumba yako, na juu ya malango yako.

Piga vita kusahau Neno la Mungu.

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Wivu ni nini na kuna aina ngapi za Wivu? Na je ni dhambi kuwa na Wivu?

Utii ni nini? na ni nani tunayepaswa kumtii au kutokumtii?

NINI MAANA YA SISI KUWA WATOTO WA MUNGU?

JE NI KUTII AU KUPATA KWANZA MAARIFA?

YESU ANA KIU NA WEWE.

DHAMBI YA MAUTI

PALE AHADI ZA MUNGU ZINAPOKUJARIBU.

Rudi nyumbani

Print this post

TAA YA MWILI NI JICHO,

Karibu tujifunze biblia,

Mathayo 6:22  “Taa ya mwili ni jicho; basi jicho lako likiwa safi, mwili wako wote utakuwa na nuru.

23  Lakini jicho lako likiwa bovu, mwili wako wote utakuwa na giza. Basi ile nuru iliyomo ndani yako ikiwa giza; si giza hilo”

Umewahi kujiuliza ni kwa namna gani “Jicho” limefananishwa na “Taa ya mwili”?

Siku zote taa ikiwa inaangaza basi nyumba yote inakuwa na Nuru na ndipo vitu vyote vilivyomo ndani vinaweza kuonekana, lakini ikizima nyumba yote inakuwa giza na hakuna kitakachoonekana.

Hali kadhalika na jicho likiwa halioni, au likiwa limefumbwa basi kinachoonekana ni giza, huwezi kuona chochote, huwezi kuona mikono yako, wala miguu yako, wala kiungo kingine chochote, huwezi kuona mbele wala nyuma wala kitu kingine chochote. Kwa ufupi unakuwa ni kipofu!. Hayo ni matokeo ya jicho kuharibika!.

Sasa Bwana Yesu analinganisha Nuru iliyopo ndani yetu na jicho.. Kwamba Nuru iliyopo ndani yetu, kazi yake ni kutuongoza njia, kama vile Jicho linaloona linavyoongoza njia na kuusaidia mwili wote kusonga mbele,  vile vile Nuru iliyopo ndani yetu kazi yake ni kuongoza maisha yetu katika njia sahihi.

Sasa Nuru iliyopo ndani yetu au inayopaswa iwe ndani yetu ni nini?.

Mathayo 5:16 “Vivyo hivyo NURU YENU NA IANGAZE mbele ya watu, wapate kuyaona MATENDO YENU MEMA, wamtukuze Baba yenu aliye mbinguni”.

Umeona hapo?.. kumbe Nuru ni “Matendo yetu mema” .. kwamba matendo yetu yanapokuwa mema, basi ni sawa na macho yanayoona!.. Kumbe matendo yetu yakiwa mabaya sisi ni sawa na vipofu!, wala hatujui tunapokwenda!…kama Bwana Yesu alivyosema katika…

Mathayo 15:14  “Waacheni; hao ni viongozi vipofu wa vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili”.

Je unataka kuona mambo yaliyopo mbele yako? na njia unayoielekea? kama ni salama?.. je! Unataka kuona hatari inayokuja na kuepukana nayo?.. Basi fanya matendo mema!!…usiende kwa waganga wala wasoma nyota wala manabii, wewe yasafishe matendo yako tu!, na utaona mambo yajayo!..

Hiyo ndio siri nyingine iliyopo nyuma ya “Matendo yetu mazuri”.. sio tu yanaupendeza moyo wa Mungu na kutupa baraka.. bali pia yanatuongoza na kutufanya tuone mambo yajayo (yaliyopo mbele yetu).

Na unayasafishaje matendo yako?.. Si kwa nguvu zako bali kwa Neema iliyopo ndani ya damu ya Yesu, ambayo hiyo inakuja kwa njia ya kutubu dhambi na kumaanisha kuziacha pamoja na kupata ubatizo sahihi..

Hapo Roho Mtakatifu ataingia ndani yako na kukupa uwezo wa wewe kufanya matendo yampendezayo Mungu, na hivyo macho yako ya kiroho yatakuwa angavu… Utakuwa na uwezo wa kuona hatari zilizopo mbele yako na kuepukana nazo, utakuwa na uwezo mkubwa wa kuona hasara zilizopo mbele yako na kuzikwepa, utakuwa unauwezo wa kuona mema yaliyopo mbele yako na kuyafuata na vile vile utakuwa na uwezo wa kuona hatari inayokufuata nyuma yako n.k

Lakini kanuni ni hiyo moja tu!..Ifanye Nuru yako (matendo yako) yaangaze!

Bwana akubariki.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

TWAENENDA KWA IMANI NA SI KWA KUONA.

Kama ulimwengu ujao utakuwa na watakatifu tu, sasa hao watakaotawaliwa watatoka wapi?

RUHUSU TOHARA IPITE JUU YA KARAMA YAKO.

ITII SAUTI ILIYOPO NYUMA YA KILA ISHARA YA MUNGU!

LAKINI MAKINDA WAWEZA KUYATWAA UWE NAYO.

Rudi nyumbani

Print this post