Category Archive Home

Aibusu midomo atoaye jawabu la haki (Mithali 24:26)

SWALI: Nini maana ya huu mstari?

Mithali 24:26 “Aibusu midomo atoaye jawabu la haki”


JIBU: Kwa namna nyingine inasomeka hivi “ Atoaye jawabu la haki, ni sawa na mtu abusuye mdomo wa rafiki yake”

Kwa tamaduni za kale za kiyahudi, ishara ya kuonyesha upendo wa dhati kwa mtu ilikuwa ni kubusiana midomo, sio kama sasa inavyotumika kama ishara ya mahusiano ya kimwili.

Na ndio maana katika maandiko utaona mitume wanaagiza watakatifu wasalimiane kwa busu takatifu (Warumi 16:16), halikadhalika utaona Yuda alipomsaliti Bwana alimbusu.

Lakini kwa tamaduni zetu, sasa ishara ya upendo ni kupeana mikono, na mahali pengine kukumbatiana, lakini sio kubusiana.

Tukirudi katika mstari, anaposema, ‘atoaye jawabu la haki’ Yaani mtu ‘anapoamua kwa haki’  au ‘anapozungumza ukweli kwa mwenzake, au kwa jirani yake, bila unafiki au upendeleo, , rohoni anatafsirika kama ni mtu ambusuye rafiki yake, mtu ampendaye rafiki yake sana, kwa kumkumbatia au kumpa mkono.

Tofauti na inavyoeleweka. Na wengi, kwamba ukimweleza mwenzako ukweli, ni kuunda uadui. Lakini Bwana wetu hakulijali hilo, ndio maana japokuwa alichukiwa na viongozi wengi wakidini kwa kuwa kwake muwazi (Yohana 8:40-45), lakini leo hii tunauona upendo wa dhati aliokuwa nao kwetu kwa kufanya hivyo.

Nasi pia Bwana atusaidie tuwe na ‘jawabu la haki’ vinywani mwetu. Tudhihirishe upendo wa kweli.

Shalom

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Rafiki hupenda sikuzote; Na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.

SAUTI NYUMA YA ISHARA.

MAPEPO YANATAFUTA HIFADHI NDANI YAKO KWA BIDII SANA.

NINI TOFAUTI KATI YA MATENDO YA SHERIA NA MATENDO YA IMANI?

Ni nani aliyesema “Nitume mimi”? katika

MIMI SIOMBI KWAMBA UWATOE KATIKA ULIMWENGU.

UNYAKUO WA KANISA UMEPITA LEO!!

Rudi nyumbani

Print this post

MWIMBIE BWANA ZABURI KATIKA NYAKATI ZA FURAHA.

Biblia Inatufundisha kuomba pale tunapokuwa katika majaribu, au tunapokuwa katika hali ya kuhitaji jambo Fulani.

Mathayo 7:7 “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa;

8  kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa”.

Lakini pia haitufundishi tu kuomba bali pia inatufundisha KUIMBA NYIMBO WAKATI WA FURAHA!. (Hili ni jambo la muhimu kulijua).

Biblia inasema..

Yakobo 5:13 “Mtu wa kwenu amepatikana na mabaya? NA AOMBE. Ana moyo wa kuchangamka? NA AIMBE ZABURI”

Hapo anasema mtu wa kwenu akiwa amepatikana na mabaya basi aombe, labda kapatwa na maradhi, au kakumbana na majaribu mazito..katika hali hii, biblia imesema tuombe!! Na Mungu atatusikia na kutuokoa au kutuponya na misiba yetu..

Zaburi 107:

4 “Walitanga-tanga jangwani katika njia ya nyika; Hawakuona mji wa kukaa. 

5 Waliona njaa, waliona na kiu, Nafsi yao ilikuwa ikizimia ndani yao

 6 Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao”

Lakini pia biblia inasema ikiwa mtu ANA MOYO WA KUCHANGAMKA..Na AIMBE ZABURI..ambaye ana Maana yake kama mtu moyoni mwake anayo furaha, au kapata furaha…pengine kaona mkono wa Bwana ukimtetea, au Bwana kampa afya na kumwokoa na mabaya, Bwana  kampa amani, kampa utulivu n.k… mtu wa namna hii biblia imeshauri kuwa na “Aimbe zaburi” asikae tu kama alivyo!..

Sasa Zaburi ni nini?

Zaburi ni nyimbo maalumu za KUMTUKUZA MUNGU, KUMSIFU na KUMSHUKURU baada ya Bwana kututendea mema.. (Nyimbo hizi zinakuwa katika mfumo wa mashairi mazuri) mfano wa hizi ni zile Daudi alizokuwa anaziimba, kila baada ya kuuona wema wa Bwana!.

1Nyakati 16:7 “Ndipo siku hiyo Daudi alipoagiza kwanza kumshukuru Bwana, kwa mkono wa Asafu na nduguze.

 8 Mshukuruni Bwana, liitieni jina lake; Wajulisheni watu matendo yake.

 9 Mwimbieni, MWIMBIENI KWA ZABURI; Zitafakarini ajabu zake zote. 

10 Jisifuni kwa jina lake takatifu; Na ufurahi moyo wao wamtafutao Bwana”

Kila tunapomshukuru Bwana au tunapomsifu kwa Nyimbo hizi za Zaburi, tunajipandishia thamani zetu mbele za Mungu, na tunaithibitisha mioyo yetu mbele za Mungu.

Unajua ni kwanini Daudi alipata kibali sana Mbele za Mungu?.. Sababu mojawapo ni desturi yake hiyo ya kumwimbia Mungu Zaburi..(na ndio maana hata kitabu chake kikaitwa kitabu cha Zaburi).

Zaburi 57:7 “Ee Mungu, moyo wangu u thabiti, Moyo wangu u thabiti. NITAIMBA, NITAIMBA ZABURI, 

8 Amka, utukufu wangu. Amka, kinanda na kinubi, Nitaamka alfajiri.

 9 Ee Bwana, nitakushukuru kati ya watu, NITAKUIMBIA ZABURI KATI YA MATAIFA.

 10 Maana fadhili zako ni kubwa hata mbinguni, Na uaminifu wako hata mawinguni.

 11 Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, Na juu ya nchi yote uwe utukufu wako”

Kwahiyo ni muhimu kufahamu kuwa KUOMBA ni muhimu lakini pia KUIMBA ni muhimu sana (Hususani Zaburi)..Mambo haya mawili yanakwenda pamoja!.. haijalishi sauti yako ikoje, wewe mwimbie Mungu, kwasababu Mungu katuumba ili tumtukuze yeye na kumsifu, pasipo kujalisha sauti zetu.

1Wakorintho 14:15 “Imekuwaje, basi? Nitaomba kwa roho, tena nitaomba kwa akili pia; MTAIMBA kwa roho, TENA NITAIMBA kwa akili pia”

Lakini pia ni muhimu kujua kuwa Nyimbo za Zaburi lengo lake ni kumtukuza Mungu na kumshukuru, na kumwimbia na sio mipasho. Siku hizi za mwisho utaona mtu baada ya kufanyiwa wema na Mungu, ndio wakati wa yeye kuimba nyimbo ambazo anakuwa hana tofauti na watu wa kidunia ambao wanasemana kwa nyimbo!, huo ni udunia!. Na mtu wa namna hii asitegemee atapokea chochote kutoka kwa Bwana, haijalishi ananukuu zaburi kutoka kwenye biblia.

Siku zote ni lazima Nia zetu za kumwimbia Bwana ziwe takatifu mbele zake, na tusifanane na watu wa kidunia.. Hakuna mahali popote Daudi alimwimbia Sauli zaburi za kujionyesha kama yeye kakubaliwa mbele za Mungu zaidi ya Sauli, lakini kinyume chake utaona siku zote Daudi alimwombea rehema Sauli na zaidi sana alimheshimu hata kufikia hatua ya kumwita Sauli Masihi wa Bwana (yaani mpakwa mafuta wa Bwana), mtu ambaye usiku na mchana alikuwa anaitafuta roho yake.

Na sisi ni lazima tufanane na Daudi, tunamwimbia Mungu wetu Zaburi, huku fahamu zetu na akili zetu zikiwa zinamwelekea yeye(Bwana), na si zinawaelekea wale wanaotutesa, au kutuudhi, au kushindana nasi..huku tukiwaombea wote wanaopingana nasi kama Bwana Yesu, Mwalimu mkuu alivyotuelekeza katika…Mathayo 5:43

Mathayo 5:43 “ Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako;

44  lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi,

45  ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki?”

Bwana Yesu azidi kutubariki sote na kutusaidia.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

IFAHAMU HUZUNI NA FURAHA YA MALAIKA.

JE! NINAWEZA KUPOTEZA FURAHA YA WOKOVU?

Furaha ni nini?

Je ni kweli kila nafsi itaonja mauti kulingana na (Zaburi 89:48)?

OLE WAO WANAOJITAHIDI KUMFICHA BWANA MASHAURI YAO.

Rudi nyumbani

Print this post

Je! Ni Kristo au Kristu? Lipi ni neno sahihi?

JIBU: Neno Kristo limetoka katika lugha ya kigiriki (Khristos) ambalo likitafsiriwa katika Kiswahili linatamkika kama KRISTO.

Lakini Neno hili hili, kwa lugha ya kilatini  (Christus), likitafsiriwa katika Kiswahili linatamkika kama  KRISTU.

Swali ni Je! Ipi ni tafsiri sahihi?

Tufahamu kuwa biblia yetu  (husasani sehemu kubwa ya agano jipya) haikuandikwa katika lugha ya kilatini, au kiingereza, au kichina, au kifaransa.. Hapana bali iliandikwa katika lugha ya Kigiriki ya kale. Hivyo tafsiri ya biblia yetu ya Kiswahili tunaitolea moja kwa moja kutoka katika lugha hiyo ya kigiriki, na sio kiingereza au kilatino.

 Hivyo ni vizuri tukitumia lahaja ya lugha ya asili, iliyotumika kwenye biblia(Kigiriki) kuliko nyingine.

Japo wapo wanaotumia lahaja ya kilatino (Kristu), pia hawafanyi makosa, maadamu ni Kristo Yule Yule analengwa na sio mwingine. Ni sawa na anayesema ‘Sulemani’ au ‘Solomoni’. Ni Yule Yule mlengwa isipokuwa katika lahaja mbili tofauti.

Maana ya Kristo ni “Mtiwa-Mafuta” Ambapo kwa lugha ya kiyahudi anaitwa “MASIHI”. Hivyo tunaposema Yesu Kristo, tunamaanisha Yesu mtiwa mafuta.  Yaani Yesu aliyeteuliwa na Mungu mahususi kwa kazi ya kuwakomboa wanadamu. Ni yeye tu ndiye mwokozi wa ulimwengu wala hapana mwingine.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

JINA LA MUNGU NI LIPI?

Akida ni nani kibiblia, na kazi yake ni ipi? (Mathayo 8:5)

Nini maana ya ELOHIMU?

SEMA KWA LUGHA NYINGINE.

Babewatoto ni nani katika biblia?(Isaya 34:14).

Ni nani aliye kipofu, ila mtumishi wangu?

Mharabu ni nani katika biblia?

Rudi nyumbani

Print this post

Awanyimaye watu nafaka, watu watamlaani

SWALI: Nini maana ya huu mstari?

Mithali  11: 26 “Awanyimaye watu nafaka, watu watamlaani; Auzaye nafaka, baraka itakuwa kichwani pake”.


JIBU: Kuna wakati sukari ilikuwa adimu sana katika taifa letu, baadhi ya wafanyabiashara wakubwa walipoona janga hilo limetokea, wakanunua sukari nyingi, tani kwa matani, wakazificha, hivyo ikaifanya sukari (hata hiyo kidogo iliyokuwepo) kuwa adimu zaidi.. Lengo lao ni sukari izidi kupanda bei ili waiuze kwa bei ya juu sana wapate faida kubwa.

Lakini jambo hili liliwaathiri watu wengi, hususani wafanyabishara wadogo wanaotegemea sukari  kuzalisha bidhaa zao, pamoja na watu wa hali ya chini wasioweza kununua sukari kwa bei ya juu. Matokeo yake ikawa ni watu kulaumu na kuwakasirikia sana wanaofanya vitendo hivyo.

Au wakati ambapo maji ni adimu, baadhi ya watu hupadisha bei, kwa lengo la kujipatia faida kubwa zaidi, watakaa na maji yao kwenye visima mpaka atakapotekea mwenye bei kubwa. Watu wa namna hii ukichunguza utaona wanaishia kulaaniwa sana na watu wanaowazunguka.

Ndio maana ya huo mstari “Awanyimaye watu nafaka, watu watamlaani; Auzaye nafaka, baraka itakuwa kichwani pake”..

watu watampenda na kumbariki Yule ambaye atawauzia huduma yake kama ilivyo desturi ya sikuzote.

1Yohana 3:17  “Lakini mtu akiwa na riziki ya dunia, kisha akamwona ndugu yake ni mhitaji, akamzuilia huruma zake, je! Upendo wa Mungu wakaaje ndani yake huyo?”

Na rohoni pia ni vivyo hivyo,..Wakati tuliopo sasa maandiko yalitabiri ni wakati wa njaa kubwa sana ya kiroho, watu wakizunguka huko na kule kutafuta Neno la kweli la Mungu (Amosi 8:11-12). Lakini inasikitisha kuona baadhi ya watu wakificha maarifa, au huduma, kisa tu, hawalipwi vizuri..kumuona mtume/nabii ni sh. Laki moja. Kununua kitabu cha mhubiri Fulani ni sh.elfu themanini. Badala tuuze kwa bei nafuu, tunauza kibiashara, kisa tunafahamu ni lazima tu vitanunuliwa kwasababu sisi ni maarufu.

Bwana atusaidie. Tutoe nafaka tusiizuie

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Maana ya huu mstari ni ipi? Mithali 14:4 ‘Zizi ni safi ambapo hapana ngombe;bali nguvu za ngombe zaleta faida nyingi’.

Kusemethi ni nini katika biblia?

Uga ni nini? Na kazi yake ni ipi kibiblia?

KWA KUWA WASEMA MIMI NI TAJIRI.

Njia zote za mtu ni safi machoni pake mwenyewe;(Mithali 16:2)

Gengeni ni wapi, wale nguruwe walipoteremkia? (Marko 5:13)

KWA WINGI WA WASHAURI HUJA WOKOVU.

Rudi nyumbani

Print this post

HUNA SHIRIKA NAMI.

Jina la Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo lihimidiwe, karibu tujifunze Biblia, Neno la Mungu wetu lililo mwanga wa njia yetu na taa iongozayo miguu yetu.

Kuna mambo ambayo mbele ya macho yetu ni madogo, na huenda yakaonekana hayana maana sana au umuhimu sana, lakini kwa Mungu ni ya maana sana, kiasi kwamba usipoyafanya baada ya kuyajua yanaweza kukuweka mbali na Mungu maili nyingi sana sana pasipo hata kutegemea.

Na kuna mambo ambayo mbele ya macho yetu tunayaona ni ya muhimu sana lakini mbele za Mungu yakawa ni madogo sana. Sasa ni muhimu sana kujua yale ya muhimu na yale ambayo si ya muhimu. Na kawaida ya shetani ni kuyafanya yale ambayo si ya muhimu sana kuwa ya Muhimu na yale ya Muhimu sana kuwa ya kawaida.

Kwamfano kuna mahali Bwana Yesu aliwaambia Mafarisayo kuwa wameacha mambo ya msingi na muhimu kama Adili, rehema na imani na badala yake wanakesha kuzitukuza zaka wanazozitoa..Wakidhani kuwa Mungu anapendezwa na Zaka zao zaidi ya wao kuwa na rehema, kwasababu yeye mwenyewe alisema kuwa anataka rehema na si sadaka! (Mathayo 9:13). Maana yake cha msingi kwanza ni rehema na ndipo sadaka zifuate..

Mathayo 23:23  “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache.

24  Viongozi vipofu, wenye kuchuja mbu na kumeza ngamia”.

Vile vile kuna maagizo mengine manne (4) ambayo ni ya Muhimu lakini shetani kayafanya yaonekane kama sio ya muhimu machoni pa watu.

1.Ubatizo.

Ubatizo ni agizo la muhimu sana kwa kila mtu baada tu ya kuamini, na ubatizo ulio sahihi na wa kimaandiko ni ule wa kuzama katika maji mengi na kwa jina la Bwana Yesu Kristo (Soma Yohana 3:23, Matendo 2:38, na Matendo 19:5), shetani ameurahisisha ubatizo machoni pa watu wengi kwasababu anaujua umuhimu wake, na kaelekeza nguvu kubwa sana hapo kuzuia watu wasibatizwe kwasababu anaelewa uthamani wa ubatizo.

Ndio maana leo hii utaona mtu yupo tayari kwenda kuogelea katika fukwe za bahari, au katika mabwawa maalumu (swimming pools) hata masaa 6 na asichoke, lakini kitendo cha kutii tu agizo la kuzamishwa kwenye maji mara moja na kuibuka kwa jina la Yesu hataki, hapo ndio utaona jinsi shetani alivyowekeza nguvu zake nyingi, kuzuia jambo hilo.

2. Wanawake kufunika vichwa (wawapo ibadani).

Biblia imeagiza wanawake wafunike vichwa wawapo ibadani kwasababu ya malaika (1Wakorintho 11:10). Sasa ukitaka kujua malaika wana umuhimu gani kasome safari ya wana wa Israeli, ujue waliwekwa chini ya nani.

Kutoka 23:20 “Tazama, mimi namtuma malaika aende mbele yako, ili akulinde njiani na kukupeleka mpaka mahali pale nilipokutengezea. 

21 Jitunzeni mbele yake, mwisikize sauti yake; wala msimtie kasirani; maana, hatawasamehe makosa yenu; kwa kuwa jina langu limo ndani yake”.

Mwanamke asiyefunika kichwa chake awapo ibadani baada ya kuujua ukweli, anaharibu uwepo wa Mungu na kujipunguzia Baraka za rohoni (haya ni mambo madogo machoni petu lakini mbele za Mungu ni makubwa na ya muhimu).

3. Kushiriki meza ya Bwana.

Bwana Yesu alisema tushiriki meza yake mara kwa mara, kwaajili ya ukumbusho wake.. Bwana Yesu kaitukuza meza yake hiyo zaidi hata ya siku yake ya kuzaliwa.. Hakuna mahali popote kaagiza tufanye ukumbusho wa siku yake ya kuzaliwa, lakini hapa kaagiza tushiriki meza yake kama ukumbusho wa siku yake ya kufa

1Wakorintho 11:24  “naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwa ajili yenu; FANYENI HIVI KWA UKUMBUSHO WANGU.

25  Na vivi hivi baada ya kula akakitwaa kikombe, akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu; fanyeni hivi kila mnywapo, KWA UKUMBUSHO WANGU.

26  Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo”.

Sasa sisi tukilipuuzia agizo hili la kushiriki meza ya Bwana na kuona kama ni dogo tu!, na lisilo na maana.. Basi tufahamu kuwa tumekaidi Agizo kuu la muhimu kwa faida yetu wenyewe.. Kama upo mahali ambapo hupati nafasi ya kushiriki meza ya Bwana basi harakisha sana kutafuta kufanya hivyo.

4. Kutawadhana miguu.

Moja ya Agizo ambalo shetani kalifanya lionekane halina maana kabisa ni hili la kuoshana miguu, lakini ni agizo kuu sana, na la Muhimu sana.. Hebu turejee biblia tuone kama agizo hili lina umuhimu wowote.

Yohana 13:5  “Kisha akatia maji katika bakuli, akaanza kuwatawadha wanafunzi miguu, na kuifuta kwa kile kitambaa alichojifunga.

6  Hivyo yuaja kwa Simoni Petro. Huyo akamwambia, Bwana! Wewe wanitawadha miguu mimi?

7  Yesu akajibu, akamwambia, Nifanyalo wewe hujui sasa; lakini utalifahamu baadaye.

8  Petro akamwambia, Wewe hutanitawadha miguu kamwe. YESU AKAMWAMBIA, KAMA NISIPOKUTAWADHA, HUNA SHIRIKA NAMI.

9  Simoni Petro akamwambia, Bwana, si miguu yangu tu, hata na mikono yangu na kichwa changu pia.

10  Yesu akamwambia, Yeye aliyekwisha kuoga hana haja ila ya kutawadha miguu, bali yu safi mwili wote; nanyi mmekuwa safi, lakini si nyote”

Hebu rudia kuusoma huo mstari wa 8, majibu Bwana Yesu aliyompa Petro.. alimwambia “KAMA NISIPOKUTAWADHA, HUNA SHIRIKA NAMI”.  Kumbe kitendo cha kudharau au kukataa kuoshana miguu kinaweza kusababisha sisi kupoteza ushirika na Mungu moja kwa moja!!… ni jambo la kuogopesha sana!, na la kulitafakari sana..

Hebu tuendelee kusoma mistari inayofuata, tuone kama agizo hilo lilikuwa ni lazima kwetu..

1Wakorintho 13:12  “Basi alipokwisha kuwatawadha miguu, na kuyatwaa mavazi yake, na kuketi tena, akawaambia, Je! Mmeelewa na hayo niliyowatendea?

13  Ninyi mwaniita, Mwalimu, na, Bwana; nanyi mwanena vema, maana ndivyo nilivyo.

14  Basi ikiwa mimi, niliye Bwana na Mwalimu, nimewatawadha miguu, imewapasa vivyo kutawadhana miguu ninyi kwa ninyi.

15  Kwa kuwa nimewapa kielelezo; ili kama mimi nilivyowatendea, nanyi mtende vivyo.

16  Amin, amin, nawaambia ninyi, Mtumwa si mkuu kuliko bwana wake; wala mtume si mkuu kuliko yeye aliyempeleka.

17  Mkiyajua hayo, heri ninyi mkiyatenda”

Hapo Bwana Yesu kasema wazi kabisa wala hatuhitaji ufunuo wowote kuelewa… Ni lazima kuoshana miguu sisi wakristo kwa wakristo..na ndio ulikuwa utaratibu wa kanisa la kwanza (soma 1Timotheo 5:9-10). Kwahiyo na sisi ni lazima tutii agizo hilo vinginevyo tutapoteza ushirika na Bwana.

Shetani atakuhubiria leo kupitia watumishi wake kuwa “agizo hilo si la msingi” ndugu usidanganyike!..hata Petro alidhani hivyo, lakini saa alipoujua ukweli, alitamani hata Bwana Yesu amwoshe mwili mzima!..

Bwana Yesu atusaidie.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

LISHIKILIE SANA LILE AGIZO LA KWANZA.

Ni maneno gani Bwana Yesu aliyokuwa anayaandika ardhini? (Yohana 8:7).

TENDA AGIZO LA YESU, HILO NDIO LITAKALOKULINDA.

MWANAMKE, BINTI, MAMA.( Sehemu ya 1)

JE NI KUTII AU KUPATA KWANZA MAARIFA?

Rudi nyumbani

Print this post

KONDE LA DAMU (Akeldama).

Shalom, karibu tujifunze biblia.

Leo napenda tujifunze juu ya lile Konde Yuda alilolinunua.. Biblia inaliita kuwa ni “konde la Damu”. Tafsiri na konde ni “shamba/kiwanja”.. Hivyo Konde lolote lililopatikana au kununuliwa kwa fedha za mauaji lilijulikana kama “konde la damu”.

Na maandiko yanaonyesha kuwa Yuda alilinunua shamba kwa fedha/kima cha mauaji.. Na hakulinunua kwa matakwa yake, bali Maukuhani ndio waliokwenda kulinunua, lakini hati ya kile kiwanja ikaandikwa kwa jina la YUDA!.. kwasababu ni fedha zake ndizo zilizonunulia kiwanja hicho..

Sasa tendo walilolifanya makuhani kwenda kununua mahali pa kuzika wageni lilikuwa ni tendo la heshima na lenye kugusa hisia za wengi, kwani katika desturi za wayahudi ilikuwa wageni na Wayahudi hawazikwi mahali pamoja, sasa ilikuwepo changamoto ya wageni kutoka mbali wanaokuja Yerusalemu na kufia huko, changamoto ya mahali pa kuwazika ilikuwa kubwa, kwahiyo hawa makuhani kitu walichofanya kilikuwa ni cha kiungwana.. Hivyo wakaenda kununua sehemu ya gharama ya juu, katikati ya Yerusalemu karibu na bonde la mwana wa Hinomu.

Lakini sasa watu walipoulizia ni nani kanunua konde lile na kiasi kilichotolewa, siri ikajulikana kuwa kiwanja kile kilinunuliwa na mtu mmoja (marehemu) aliyeitwa Yuda kwa fedha iliyotokana na kumsaliti Bwana Yesu. Kwahiyo kila aliyepita karibu na kiwanja hicho na kuulizia habari za kiwanja hicho na mmiliki, basi alisimuliwa habari ya Yuda.. Hivyo kiwanja kile kikawa na sifa mbaya kutokana na tukio la Yuda.

Ni sawa sasahivi upite mahali uone jengo limejengwa na linatoa huduma Fulani nzuri…halafu unaambiwa jengo lile limejengwa kwa fedha za ujambazi/mauaji yaani mmiliki wa jengo aliua watu Fulani ili kupata fedha za kujenga hilo jengo. Bila shaka, hata kama lile jengo linafanya kazi nzuri kiasi gani, bado sifa yake itabaki kuwa mbaya. Ndivyo na konde alilolinunua Yuda.

Mathayo 27:3 “Kisha Yuda, yule mwenye kumsaliti, alipoona ya kuwa amekwisha kuhukumiwa, alijuta, akawarudishia wakuu wa makuhani na wazee vile vipande thelathini vya fedha, akasema, Nalikosa nilipoisaliti damu isiyo na hatia.

4  Wakasema, Basi, haya yatupasani sisi? Yaangalie haya wewe mwenyewe.

5  Akavitupa vile vipande vya fedha katika hekalu, akaondoka; akaenda, akajinyonga.

6  Wakuu wa makuhani wakavitwaa vile vipande vya fedha, wakasema, Si halali kuviweka katika sanduku ya sadaka, kwa kuwa ni kima cha damu.

7  Wakafanya shauri, wakavitumia kwa kununua konde la mfinyanzi liwe mahali pa kuzika wageni.

8  Kwa hiyo konde lile huitwa konde la damu hata leo”.

Habari hii tunaweza kuisoma tena vizuri katika Matendo 1:16-19.

Matendo 1:16 “ Ndugu, ilipasa andiko litimizwe, alilolinena Roho Mtakatifu zamani kwa kinywa cha Daudi, katika habari za Yuda aliyewaongoza wao waliomkamata Yesu;

17  kwa sababu alikuwa amehesabiwa pamoja na sisi, akapata sehemu ya huduma hii.

18  (Basi mtu huyu alinunua konde kwa ijara ya udhalimu; akaanguka kwa kasi akapasuka matumbo yake yote yakatoka.

19  Ikajulikana na watu wote wakaao Yerusalemu; hata konde lile likaitwa kwa lugha yao Akeldama, maana yake, konde la damu.)”

Ni nini tunajifunza katika habari hii?

1. Ukifanya jambo baya litakuja kujulikana tu hata baada ya kufa kwako!.

Yuda alimsaliti Bwana mbele ya wanafunzi wake 12 tu!, pengine wale wanafunzi wangeshuhudia kuwa Yuda ni msaliti wasingeaminika, lakini LILE KONDE lilikuja kumtangaza Yuda kwa watu wote, hata ambao walikuwa hawamjui walimjua kupitia konde lile. Vile vile Daudi alimfanyia ubaya Uria, kwa kumwua na kumchukua mke wake, jambo lile alilifanya kwa siri, lakini Mungu alikuja kulitangaza mbele ya jua, mpaka leo tunalisoma tukio lile.

2. Mali ya dhuluma ni lazima iishie kuwa na sifa mbaya.

Haijalishi mali ya dhuluma itadumu kuwa na heshima kwa muda gani, utafika wakati heshima yake itapotea na itabaki aibu!!.. Kama umepata nyumba kwa dhuluma mwisho wake utakuwa ni aibu, kama umepata shamba kwa dhuluma mwisho wake utakuwa ni aibu, na kitu kingine chochote kama ni cha dhuluma mwisho wake ni aibu.

Vile vile kama umemwibia Bwana kwa matoleo yako, na ukatumia matoleo yale kufanya mambo yako ikiwemo kununua shamba kama Yuda, basi utaishi kuwa kama Yuda.

Vile vile kama unamsaliti Bwana na injili yake kwa kazi yako, au uzuri wako, au hadhi yako, au fedha zako au kwa chochote kile, basi fahamu kuwa unaelekea mahali pabaya.

Bwana Yesu atusaidie tuishi maisha ya uangalifu.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

UNAWAZA NINI SASA, JUU YA UFALME WA MBINGUNI?

LISHIKILIE SANA LILE AGIZO LA KWANZA.

KITABU CHA YUDA: SEHEMU YA 1

Je Mtu anaweza kusema uongo, Na Mungu akambariki?

Paulo alikuwa na maana gani aliposema “nimeaminiwa uwakili”

Rudi nyumbani

Print this post

KAZI YA MALAIKA MIKAELI KWA WATU WA MUNGU.

Jina la Bwana Yesu Kristo libarikiwe, karibu tuongeze maarifa ya Neno la Mungu.

Leo tutajifunza juu ya Malaika Mikaeli.

Mbinguni kuna aina kuu tatu za Malaika. Wapo malaika wa sifa ambao ndio wale Maserafi na Makerubi, pia wapo malaika wa Ujumbe ambaye ndio kundi la Gabrieli (aliyemletea Mariamu taarifa za kumzaa Bwana Yesu na pia aliyemletea ujumbe Danieli)

Pia wapo malaika wa Vita, ambao kazi yao ni kupambana na nguvu zote za adui zinazoshindana na watu wa Mungu, na hapa ndipo kundi la Mikaeli na wenzake linapotokea.

Sasa inaaminika na baadhi ya watu kuwa Mikaeli ni jina lingine linalomwakilisha Bwana Yesu..lakini kulingana na maandiko hilo jambo si kweli..

Sasa ni kwa namna gani Mikaeli sio Bwana Yesu kulingana na maandiko unaweza kufungua hapa na kusoma >>>Je Malaika Mikaeli ndiye Yesu mwenyewe?

Sasa maswali mawili ya kujiuliza ni je Mikaeli anampigania nani, na anapiganaje?

1. Anampigania nani?

Mikaeli ni malaika wa vita aliyewekwa na Mungu kulipigania Taifa la Israeli na kanisa la Mungu.

Tunalithibitisha hilo kipindi kile ambacho Danieli analetewa ujumbe na Malaika Gabrieli, na kumtaja Mikaeli kuwa amewekwa kusimama upande watu wa Danieli (yaani waisraeli)”.

Danieli12:1 “Wakati huo Mikaeli atasimama, jemadari mkuu, asimamaye upande wa wana wa watu wako…”

Pia unaweza kusoma Danieli 10:21,utaona Mikaeli anatajwa kama Mkuu wa watu wa Danieli

Hivyo Mikaeli ni malaika wa vita kwa ajili ya Taifa la Israeli kwa jinsi ya mwili, na Israeli ya roho ambayo ni kanisa (yaani sisi tuliompokea Yesu).

2. Mikaeli anapiganaje?

Vita vya Mikaeli dhidi ya roho zitufuatiliazo si za kurusha mikuki au mapanga..bali ni za hoja.

Maandiko yanasema shetani anatushitaki usiku na mchana mbele za Mungu (Ufunuo 12:10)..na zaidi sana tafsiri ya jina shetani ni “mshitaki / mchongezi”..hiyo ndio tafsiri ya jina shetani.

Kwahiyo shetani anachokifanya usiku na mchana na kuchukua taarifa zetu mbaya na kuzifikisha mbele za Mungu kama mashitaka, hata kama hataona dosari katika maisha yetu bado tu atafika Kwa Mungu kutuchongea kama alivyofanya kwa Ayubu.

Lakini sasa Mikaeli pamoja na wenzake wanachokifanya ni kupeleka hoja zetu nzuri mbele za Mungu, kamwe hawapeleki mashitaka..Na hoja za Mikaeli zikishinda dhidi ya hoja za shetani juu yetu ndipo hapo tunapata yale yote tuliyomwomba Mungu.

Lakini hoja za shetani zikishinda dhidi ya zile za Mikaeli bali tunakabidhiwa shetani, na hivyo tunawekwa katika mikono ya shetani na kupata madhara…kwasababu Mungu ni Mungu wa haki na hana upendeleo!…Ndio maana Adamu alipoasi Mungu hakumpendelea Adamu na bali aliruhusu shetani ayachukue mamlaka yake, kwasababu ni kweli kayapata kihalali kutoka kwa Adamu.

Kwahiyo vita kati ya shetani na malaika watakatifu si vingine zaidi ya hivyo vya hoja, kila upande unapamba kuvuna watu.

Tunaweza kupata picha zaidi tunaposoma ufunuo alioonyeshwa Yuda ambao alioonyesha kuhusu mwili wa Musa.

Yuda (sio yule aliyemsaliti Bwana) alifunuliwa katika roho jambo ambalo shetani alikuwa analifanya baada tu ya Musa kufa.

Alionyeshwa baada ya Musa kufa kumbe shetani alimfuata Mungu na kuutaka mwili wake, na lengo la kuutaka mwili wake ni wazi kuwa si lingine zaidi ya kutaka kuuweka uabudiwe na watu.

Na alipofika mbele za Mungu, alikuwa na hoja kwanini anautaka ule mwili, na pengine hoja ambayo alikuwa nayo ni lile kosa Musa alilolifanya lililompelekea yeye kufa (la kutompa Mungu utukufu).

Hivyo shetani alikuwa na kila sababu za yeye kuumiliki mwili wa Musa, lakini tunaona kitu cha kipekee ni kwamba wakati anapeleka hayo mashitaka Mikaeli aliyewekwa kwaajili ya kuwatetea Israeli alisimama kumpinga hoja zake hizo, na Mikaeli akatoa hoja zenye nguvu juu ya Musa, na hivyo Mikaeli akashinda na shetani hakukabidhiwa mwili wa Musa, ndio maana mpaka leo hakuna mtu anajua mifupa ya Musa ilipo.(Ni Mungu mwenyewe ndiye  aliyemzika).

Lakini endapo shetani angeshinda hoja mbele ya Mikaeli basi huenda Musa angekufa hemani na watu wangeikusanya mifupa yake na kuiabudu na ufalme wa giza ungestawi zaidi.

Yuda 1:9 “Lakini Mikaeli, malaika mkuu, aliposhindana na Ibilisi, na kuhojiana naye kwa ajili ya mwili wa Musa, hakuthubutu kumshitaki kwa kumlaumu, bali alisema, Bwana na akukemee”.

Ndugu mpendwa Ikiwa unasema umeshampokea Yesu halafu bado unafanya uzinzi, basi fahamu kuwa shetani anapeleka mashaka hayo mbele za Mungu mchana na usiku…akidai haki ya kukumiliki wewe.

Lakini matendo yako yakiwa sawasawa na biblia, basi shetani anakosa alama za kukushitaki mbele za Mungu, na kinyume chake Malaika wa Bwana, Mikaeli na kundi lake wanasimama kuyataja mambo yako mazuri mbele za Mungu, wanautazama uso wa Baba na kutaja mema yako kama maandiko yasemavyo..

Mathayo 18:10 “Angalieni msidharau mmojawapo wadogo hawa; kwa maana nawaambia ya kwamba malaika wao mbinguni siku zote huutazama uso wa Baba yangu aliye mbinguni”

Na kamwe malaika hawapeleki mashtaka mabaya mbele za Mungu kwaajili yetu.

2 Petro 2:11 “Wenye ushupavu, wenye kujikinai, hawatetemeki wakiyatukana matukufu; ijapokuwa malaika ambao ni wakuu zaidi kwa uwezo na nguvu, hawaleti mashitaka mabaya juu yao mbele za Bwana”.

Je umetubu kwa kumaanisha kuacha dhambi?..umeacha wizi?, umeacha usengenyaji?, umeacha ulevi, umeacha uasherati?, umeacha uuaji na hasira?.

Kama bado hujaacha hivyo vyote basi fahamu kuwa ndivyo vinavyokushitaki mbele za Mungu.

Marana tha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Je Malaika Mikaeli ndiye Yesu mwenyewe?

AMEFANYIKA BORA KUPITA MALAIKA!

Je Musa yupo anawashitaki watu..kulingana na Yohana 5:45?

WALA MSIUANGALIE MWILI, HATA KUWASHA TAMAA ZAKE.

UFUNUO: Mlango wa 14

Rudi nyumbani

Print this post

MAUMIVU  NYUMA-YA-HUDUMA.

Mtu yeyote aliyeokoka (Kwa kumaanisha kabisa), ni lazima Bwana ataweka huduma ndani yake, anaweza akawa mchungaji, au mwinjilisti, au mwalimu, au mwimbaji, shemasi, lakini pia anaweza akawa  mwandishi, mtunza bustani, mratibu wa vipindi, mwasibu wa kanisa,  n.k. maadamu tu zinafanya kazi ya kulihudumia kanisa  la Mungu, na si vinginevyo.

Licha ya kuwa utaifurahia kazi yako na kupata thawabu, lakini uhalisia wake ni kwamba, huduma yoyote Mungu anayokupa haitakuwa nyepesi kama wewe unavyoweza kudhani, yaliyowakuta mitume wakati fulani, yatakukuta na wewe, lakini yatamkuta hata na Yule ambaye atakuja kutumika baadaye.

Haya ni baadhi ya maumivu utakayokutana nayo;

KUACHWA:

2Timotheo 4:10  “Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia”

Tengeneza picha, Wakati ambapo mtume Paulo yupo katika kilele cha utumishi, halafu mtendakazi mwenzake mpendwa, anageuka ghafla, na kumwachwa alijisikiaje. Ni heri angemwacha na kwenda kutumika mahali pengine, lakini anamwacha na kuurudia ulimwengu. Ni maumivu makali  kiasi gani? Ni kuvunjwa moyo kiasi gani?

Mwaka 2016-2018, tulikuwa na rafiki yetu mmoja, hatukudhani kama siku moja tungekaa tutengane, kwasababu tulikuwa tumeshajiwekea malengo mengi makubwa ya kumtumikia Mungu, tuliishi kama Daudi na Yonathani, lakini tulipoanza kupiga hatua tu ya kutekeleza malengo yetu, ghafla alikatisha mawasiliano na sisi, akawa hapokei simu zetu, na baadaye kutu-block kabisa, akaurudia ulimwengu, hadi leo.

Tuyahifadhi haya ili yatakapotokea tusivunjike moyo tukaacha utumishi. Wakina Dema unaweza kupishana nao katika huduma Mungu aliyoweka ndani yako, ila usivunjike moyo.

UPWEKE:

Pale pale Mtume Paulo anamsihi Timotheo asikawie kumfuata, kwasababu Kreske, amekwenda Galatia, Tito, Dalmatia..

2Timotheo 4:9  “Jitahidi kuja kwangu upesi. 10  Maana Dema aliniacha, akiupenda ulimwengu huu wa sasa, akasafiri kwenda Thesalonike; Kreske amekwenda Galatia; Tito amekwenda Dalmatia. 11  Luka peke yake yupo hapa pamoja nami. Umtwae Marko, umlete pamoja nawe, maana anifaa kwa utumishi. 12  Lakini Tikiko nalimpeleka Efeso.

Kundi hili halikuondoka, kwasababu ya kuupenda ulimwengu kama Dema, hapana bali kwasababu ya huduma, hivyo mtume Paulo akabaki peke yake. Kuna wakati alikuwa na kundi kubwa la watenda kazi pamoja naye, lakini upo wakati alibaki peke na Luka tu.. Anamhizi Timotheo afike  pamoja na Marko, ili afarijike katika huduma, hali ya upweke imwache.

Kama mhudumu wa Kristo, zipo nyakati utakuwa peke yako, Hivyo usife moyo, ni vipindi tu vya Muda.

KUACHANA:

Moja ya ziara za mtume Paulo iliyokuwa na mafanikio makubwa sana, basi ni ile ziara ya kwanza. Ni kwasababu gani? Ni kwasababu alikuwa na Barnaba. Wote wawili walikuwa na nia ya Kristo, hawakuwa na fikra za kiulimwengu au kimaisha. Lakini cha kusikitisha hilo halikuendelea sana.. Walipishana kauli, kutokana na kwamba kila mmoja aliona uchaguzi wake ni bora kuliko wa mwingine.. Paulo alitaka kwenda Sila, lakini Barnaba kwenda na Marko. Lakini kama wangetoa tofauti zao, na kuwachukua wote, naamini huduma ingekuwa na mafanikio makubwa zaidi, lakini hilo lilikuwa halina budi kutokea.

Matendo 15:36 “ Baada ya siku kadha wa kadha Paulo akamwambia Barnaba, Haya! Mrejee sasa tukawaangalie hao ndugu katika kila mji tulipolihubiri neno la Bwana, wa hali gani.

37  Barnaba akaazimu kumchukua Yohana aliyeitwa Marko pamoja nao.

38  Bali Paulo hakuona vema kumchukua huyo aliyewaacha huko Pamfilia, asiende nao kazini.

39  Basi palitokea mashindano baina yao hata wakatengana. Barnaba akamchukua Marko akatweka kwenda Kipro”.

Nyakati za kupoteza kiungo chako muhimu katika huduma utapishana nacho.

KUFANYIWA UBAYA:

2Timotheo 4:13  “Lile joho nililoliacha kwa Karpo huko Troa, ujapo ulilete, na vile vitabu, hasa vile vya ngozi. 14  Iskanda, mfua shaba, alionyesha ubaya mwingi kwangu; Bwana atamlipa sawasawa na matendo yake. 15  Nawe ujihadhari na huyo, kwa sababu aliyapinga sana maneno yetu”.

Haijalishi, utampendeza mtu kiasi gani, utafanya wema mwingi namna gani, bado wapo watakaokupinga tu utumishi wako, na zaidi watakuwa ni kama maadui zako. Ni jambo ambalo mtume Paulo hakulitarajia lakini alikumbana nalo baadaye, kutoka kwa Iskanda.. Yaliyomkuta Kristo Bwana wetu kutoka kwa mafarisayo yakamakuta na yeye. Na huwenda yatakukuta na wewe wakati Fulani mbele. Usirudi nyuma.

KUDHANIWA VINGINE:

Watu wengi wanaweza kuchukizwa na wewe kwasababu matarajio yao kwako ni tofauti na walivyokutegemea, hili lilianza tangu wakati wa Bwana alipokuwa duniani. Watu wengi waliosikia habari zake, ikiwemo Yohana mbatizaji, walimtazamia Bwana angekuja kama mfalme Daudi, akipambana na utawala sugu wa kirumi, akivaa nguo za kifalme, akiogopwa na kila mtu. Lakini aliposikia analala kwenye milima ya mizeituni, anaongozana na wavuvi, anakaa na wenye dhambi..Imani ya Yohana ikatetereka kidogo na kutuma watu ili kuulizia kama yeye kweli ndiye, au wamtazamie mwingine..Lakini maneno ya Bwana Yesu yalikuwa ni haya;

“Naye heri awaye yote asiyechukizwa nami” (Mathayo 11:6).

Vivyo hivyo na mtume Paulo, alitarajiwa na wengi kuwa atakuwa ni mtu mkuu kimwonekano, mwenye mavazi ya kikuhani kama waandishi, kutoka na sifa zake, na nyaraka zake, kuvuma duniani kote..lakini walipokutana naye walimwona kama kituko Fulani hivi;

2Wakorintho 10:10  “Maana wasema, Nyaraka zake ni nzito, hodari; bali akiwapo mwenyewe mwilini ni dhaifu, na maneno yake si kitu.

11  Mtu kama huyo na afikiri hivi, ya kwamba jinsi tulivyo kwa maneno katika nyaraka tusipokuwapo, ndivyo tulivyo kwa matendo tukiwapo”

Hivyo si kila mtu atapendezwa na jinsi atakavyokukuta, wengine watakuacha au hawatakuamini kwasababu umekuja nje ya matarajio yao.

KUPUNGUKIWA:

Japokuwa vipo vipindi vyingi vya mafanikio, lakini pia vipo vipindi vya kupungukiwa kabisa. Paulo anamwagiza Timotheo pindi amfuatapo makedonia ambebe joho(Koti) lake, kwa ajili ya ule wakati wa baridi. Kama angekuwa na fedha ya kutosha wakati huo, kulikuwa hakuna haja ya kumwagiza, angenunua lingine tu alipokuwepo.

Mungu hawezi kukuacha, wala kukupungukia kabisa, atakupa, na kukufanikisha, lakini pia vipindi kama hivi utapishana navyo mara kwa mara na ni Mungu mwenyewe anaruhusu. Hivyo usitetereke.

Wafilipi 4:11  “Si kwamba nasema haya kwa kuwa nina mahitaji; maana nimejifunza kuwa radhi na hali yo yote niliyo nayo.

12  Najua kudhiliwa, tena najua kufanikiwa; katika hali yo yote, na katika mambo yo yote, nimefundishwa kushiba na kuona njaa, kuwa na vingi na kupungukiwa. 13  Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu”

KUUGUA:

Ukiwa mtumishi, haimaanishi wewe ni malaika, umejitenga na mateso ya hii dunia, Kazi hii itakufanya uumwe wakati mwingine, Timotheo alikuwa anaumwa mara kwa mara tumbo, kwasababu ya mifungo, kuhubiri sana, hivyo akashauriwa na Paulo atumie mvinyo kidogo kwa ajili ya kuweka tumbo lake sawa. Alikuwepo Epafrodito mtume, naye kwasababu ya injili, aliumwa sana, karibu na kufa lakini baadaye Bwana akamponya( Wafilipi 2:25). Elisha alikufa na ugonjwa wake.

Upitiapo vipindi vya magonjwa, usitetereke ukaacha utumishi bali jifariji kwa kupitia mashujaa hawa.

Hivyo, tukiyahifadhi haya moyoni, basi utumishi wetu hautakuwa wa manung’uniko au wa kuvunjika moyo, mara kwa mara. Kwasababu ndio njia ya wote. Hivyo tukaze mwendo katika kumtumikia Bwana, kwasababu malipo yake ni makubwa kuliko mateso tunayopishana nayo. Thawabu za utumishi ni nyingi sana,

Ufunuo 3:11  “Naja upesi. Shika sana ulicho nacho, asije mtu akaitwaa taji yako”.

Bwana akubariki.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

GHARAMA YA UFALME WA MBINGUNI.

Je Musa yupo anawashitaki watu..kulingana na Yohana 5:45?

Tofauti kati ya mtume na mwanafunzi ni ipi kibiblia?

Naye atawachunga kwa fimbo ya chuma.

Je mbinguni itakuwa ni kuimba tu wakati wote?

MAFUNDISHO MAALUMU KWA WAONGOFU WAPYA.

KAMA MHUBIRI USIWE MFANO WA DIOTREFE.

Rudi nyumbani

Print this post

Je! Siku ilihesabiwaje kabla ya jua na mwezi kuumbwa?

Swali: Katika kitabu cha Mwanzo tunasoma jua na mwezi viliumbwa katika siku ya 4 , sasa napenda kujua kabla ya hapo siku zilihesabiwaje, maana jua ndilo linalotenga mchana na usiku…na maandiko yanatuonyesha kuwa lilikuja kuumbwa siku ya 4?

Jibu: Ni kweli jua na mwezi viliumbwa siku ya 4, tena baada ya miti na miche ya kondeni kuumbwa (Mwanzo 1:14).

Lakini ukisoma kuanzia mstari wa pili katika kitabu hiko cha Mwanzo, utaona Mungu tayari alikuwa ameshaumba mchana na usiku na ameshatenga giza na nuru.

Mwanzo 1:1 “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.

2 Nayo nchi ilikuwa ukiwa, tena utupu, na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji; Roho ya Mungu ikatulia juu ya uso wa maji.

3 Mungu akasema, Iwe nuru; ikawa nuru.

4 Mungu akaiona nuru, ya kuwa ni njema; MUNGU AKATENGA NURU NA GIZA.

5 MUNGU AKAIITA NURU MCHANA, NA GIZA AKALIITA USIKU. IKAWA JIONI IKAWA ASUBUHI, SIKU MOJA”.

Umeona?..kumbe tayari Mungu alikuwa ameshaumba mchana na usiku kabla hata ya kuumba jua. Maana yake hata kama asingeumba jua bado majira na mchana na usiku yangekuwepo kwasababu yeye mwenyewe ndio Nuru ya ulimwengu (mwilini na rohoni).

Yohana 8:12 “Basi Yesu akawaambia tena akasema, Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima”.

Ndio maana katika ile mbingu mpya na nchi mpya hakutakuwepo  na jua na bado Nuru itakuwepo.

Ufunuo 21:23 “Na mji ule hauhitaji jua wala mwezi kuuangaza, kwa maana utukufu wa Mungu huutia nuru, na taa yake ni Mwana-Kondoo”.

Kwahiyo kwa hitimisho ni kuwa Mungu aliumba mchana na usiku, kabla ya kuliumba jua..na hiyo ni kuonyesha utukufu wake yeye, na pia kuonyesha kuwa yeye ndiye Nuru halisi Na ndio chanzo cha Nuru yote.

Je umempokea Bwana Yesu aliye Nuru ya kweli? Kama bado fahamu kuwa bado upo gizani ijapokuwa jua linakumulika…kwahiyo ni vyema ukafanya maamuzi thabiti leo ya kumpokea na kuokoka.

Yohana 12:46 “Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani”

Soma pia Yohana 9:5 na Yohana 11:9.

Bwana Yesu akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Je! mwanadamu wa kwanza kuumbwa ni yupi?

HAMA KUTOKA GIZANI

NI SAA KUMI NA MBILI (12) TU, ZA KRISTO KWAKO.

Biblia inamaanisha nini iliposema “wakidhania kuwa ulevi wakati wa mchana ni anasa;?

Je mke wa Musa alikuwa ni Mweusi?

Rudi nyumbani

Print this post

KWA WINGI WA WASHAURI HUJA WOKOVU.

Nakusalimu katika jina kuu lenye uweza la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu tujifunze maneno ya Mungu ambayo ndio uzima wetu.

Mungu ana njia nyingi za kuzungumza, anaweza kutumia ufunuo wa roho, anaweza kutumia Neno, anaweza kutumia maono anaweza kutumia mambo ya asili au matukio. Lakini si wakati wote Mungu ataleta majibu kwa kupitia njia hizo. Haijalishi utakuwa ni wa kiroho kiasi gani. Ipo njia nyingine ambayo Mungu huitumia na hiyo tusipoifahamu vema, tutapata hasara ya mambo mengi kama sio kupotea kabisa. Na njia yenyewe ni kupitia mashauri yetu sisi wenyewe tunapokuwa wengi pamoja..

Kwamfano embu tafakari hivi vifungu;

Mithali 11: 14 “Pasipo mashauri taifa huanguka; Bali kwa wingi wa washauri huja wokovu”

Maana yake ni nini? Kwamba taifa linapokataa maoni, mapendekezo, mawazo mbalimbali, kutoka kwa wananchi wake, kamwe taifa hilo haliwezi kufanikiwa,

Maandiko bado yanasema..

Mithali 15: 22 “Pasipo mashauri makusudi hubatilika; Bali kwa wingi wa washauri huthibithika”.

Mithali 24:6 “Maana kwa mashauri ya akili utafanya vita; Na kwa wingi wa washauri huja wokovu”.

Maana yake ni nini? Kwamba palipo na vita, ni lazima yawepo maono ya askari wengi, ni jinsi gani watapambana na adui yao, huyu anasema hivi, Yule vile, na mwisho wa siku linatoka jawabu moja madhubuti ambalo litaleta mafanikio makubwa, lakini ikiwa pendekezo linatoka kwa mmoja tu yaani yule mkuu wa kikosi, ni dhahiri kuwa jeshi, litakuwa dhaifu, na matokeo yake ni kupigwa..

Amen.

Hili ni jambo la muhimu sana kwa sisi tulio wakristo. Bwana Yesu aliposema tuwe na umoja, tunie mamoja, alijua kabisa atatumia njia hiyo kuleta majibu ya mambo mengi pasipo hata kusubiria mafunuo au maono.

Utauliza jambo hili lilifanyika wapi katika kanisa kwenye agano jipya.

Utakumbuka, Paulo na Barnaba walipokwenda kuhubiri injili kwa watu wa mataifa, walitokea wayahudi kadha wa kadha, wakaanza kuwaambia mataifa kuwa msipotahiriwa ninyi hamwezi kuokoka()..Hivyo jambo hilo likaleta mkanganyiko mkubwa sana, ikawabidi hadi Paulo na Barnaba warudi Yerusalemu wakasikilize mitume na wazee wanasema nini juu ya hilo.

Hivyo walipofika Yerusalemu, akina Petro na wazee, waliitisha baraza, na kuanza kulitathimini jambo hilo. Je ni sawa watahiriwe na kuishika torati ya Musa au sio sawa.. Sasa maandiko yanatuambia walihojiana sana, huyu anasema hivi, yule vile (Lakini katika amani na upendo, na sio katika mashindano).. na matokeo yake Roho wa hekima akaingia ndani yao, likapatikana shauri moja thabiti. Na kwa kupitia hilo kanisa la mataifa likathibitika sana kwa waraka waliowaandikia, likaenenda katika furaha ya Roho Mtakatifu daima.

Embu tusome pale kidogo, litusaidie…

Matendo 15:7  “NA BAADA YA HOJA nyingi Petro akasimama, akawaambia, Ndugu zangu, ninyi mnajua ya kuwa tangu siku za kwanza Mungu alichagua miongoni mwenu ya kwamba Mataifa walisikie neno la Injili kwa kinywa changu, na kuliamini.

8  Na Mungu, ajuaye mioyo ya watu, akawashuhudia, akiwapa Roho Mtakatifu vile vile kama alivyotupa sisi;

9  wala hakufanya tofauti kati yetu sisi na wao, akiwasafisha mioyo yao kwa imani…..

13  Na hao walipokwisha kunyamaza Yakobo akajibu, akisema, Ndugu zangu, nisikilizeni.

14  Simeoni ametueleza jinsi Mungu hapo kwanza alivyowaangalia Mataifa ili achague watu katika hao kwa ajili ya jina lake.

15  Na maneno ya manabii yapatana na hayo, kama ilivyoandikwa, 16  Baada ya mambo haya nitarejea, Nami nitaijenga tena nyumba ya Daudi iliyoanguka. Nitajenga tena maanguko yake, Nami nitaisimamisha;”

Kwa muda wako isome habari yote katika kitabu hicho cha Matendo ya mitume sura ya kumi na tano (15),

NINI BWANA ANATAKA SISI TUJUE  KAMA KANISA?

Lazima  tujifunze wakati mwingine tuwe watu wa Hoja nyingi, mapendekezo mengi, (lakini katika upendo na amani), ili kanisa lijengwe, ili injili ihubiriwe katika ufasaha wote. Kama tulivyosoma hapo juu inavyosema.. “kwa mashauri ya akili utafanya vita; Na kwa wingi wa washauri huja wokovu.” Hatutaweza kushindana na shetani kama tutakuwa hatuna mikakati, na mipango ya mara kwa mara,.

Kila kiungo katika mwili wa Kristo, kina nafasi ya kuchagia mashauri mema. Hivyo tujifunze njia hii, ili Mungu azungumze na sisi. Lakini tukikosa mapatano, “Taifa huangamia”..Sisi hatutaangamia kwa kutii agizo hili.

Bwana alibariki kanisa lake.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Kuwaogopa wanadamu huleta mtego,(Mithali 29:25)

Ni kwa namna gani, upendo husitiri wingi wa dhambi? (1Petro 4:8)

Na ulimi laini huvunja mfupa.(Mithali 25:15)

JE! NINAWEZA KUPOTEZA FURAHA YA WOKOVU?

NJIA YA KUPATA WOKOVU.

Kama tunaokolewa kwa neema kwanini wokovu tuupate kwa nguvu?

MITHALI AU METHALI ZA BIBLIA

Rudi nyumbani

Print this post