SI KILA KILICHO HALALI KINAFAA.

SI KILA KILICHO HALALI KINAFAA.

(Jihadhari na Marashi)

Si mambo yote yanayokubalika katika jamii basi yanafaa kwa mkristo.. Si mambo yote yanayokubaliwa na wengi basi yanafaa..ni muhimu kuchuja kila tunaloambiwa au tunayokutana nalo, kabla ya kulikubali, ndivyo biblia inavyotufundisha.

1Wakorintho 10:23  “Vitu vyote ni halali; bali si vitu vyote vifaavyo. Vitu vyote ni halali; bali si vitu vyote vijengavyo”.

Mojawapo ya jambo ambalo ni muhimu kuchukua nalo tahadhari ni “Matumizi makali ya marashi”. Unapojipulizia marashi ambayo mtu aliye mita 10 mbali nawe anayasikia, basi fahamu kuwa upo katika hatari kubwa sana.

Utauliza kivipi au kwa namna gani? Hebu turejee katika maandiko kidogo..

Utakumbuka ile habari ya yule mwanamke aliyemmiminia Bwana marhamu ya thamani nyingi mwilini mwake, na maneno Bwana Yesu aliyoyasema kuhusu kazi ya ile marhamu aliyomiminiwa?. Biblia inasema marhamu ile ilikuwa ni ya thamani kubwa, maana yake yenye kunukia sana na kwa eneo kubwa, kiasi kwamba mtu aliye mbali anaweza kuisikia harufu ya marhamu ile.

Tusome

Marko 14:3 “Naye alipokuwapo Bethania, nyumbani mwa Simoni mkoma, ameketi chakulani, alikuja mwanamke mwenye KIBWETA CHA MARHAMU YA NARDO SAFI YA THAMANI NYINGI; akakivunja kibweta akaimimina kichwani pake.

4  Palikuwa na watu waliochukizwa katika nafsi zao wakisema, Kwani kupoteza marhamu namna hii?

5  Maana marhamu hii ingaliweza kuuzwa kwa dinari mia tatu na kuzidi, wakapewa maskini. Wakamnung’unikia sana yule mwanamke.

6  Yesu akasema, Mwacheni; mbona mnamtaabisha? Amenitendea kazi njema;

7  maana sikuzote mnao maskini pamoja nanyi, na kila mpendapo mwaweza kuwatendea mema; lakini mimi hamnami sikuzote.

8  Ametenda alivyoweza; ametangulia kuupaka mwili wangu MARHAMU KWA AJILI YA MAZIKO”.

Umeona hapo?.. wakati huyu mwanamke anadhani Marhamu ile ingeweza kumfanya Bwana anukie vizuri mbele za watu na aonekane mtanashati.. lakini Bwana aliyaona yale manukato tofauti na mwanamke alivyoyaona, Bwana Yesu aliona hayafai kwa utanashati, bali kwa MAZIKO!.

Lakini kwasababu mwanamke alikuwa na nia njema ya kutubu na kumthaminisha Bwana ndio maana akapata kibali kwa muda ule, lakini Ujumbe tayari tumeachiwa, “kuwa marhamu kama hizo ni kwaajili ya maziko” so kwaajili ya utanashati.

Hiyo ikimaanisha kuwa kumbe kuna vitu tunaweza kuvipaka mwilini, au kuvivaa, na kumbe ni malighafi za MAUTI, Na KIFO!!. Ijapokuwa kwa nje tunaweza kuonekana watanashati na tunaovutia, lakini kumbe tumejipaka au tumekivaa kifo!.

Bwana Yesu angeweza kuwaambia wale watu kuwa marhamu ile amepakwa kwa kuwekwa tayari kukutana na mkutano ili kwamba wasikie harufu nzuri itokayo mwilini mwake, kwani bado alikuwa na siku kadhaa za kuhubiri mbele za watu kabla ya kufa, lakini wala yeye hakuziona hizo siku bali aliona marhamu ile inafaa kwa matumizi ya MAZIKO! Na si utanashati kama wengine wote walivyotazamia.

Mama/dada jiulize hayo marashi unayojipulizia mwilini mwako je unajiweka tayari kwa nini?..je kwaajili ya maziko yako??..

Na asilimia kubwa ya watu wanaotumia marashi makali ni lazima wanakuwa wanasumbuliwa na roho za mauti au uasherati… hivyo ni muhimu kuchukua tahadhari ya kiroho! Na si kila kitu kuiga kwasababu tu, tumeona ni kitu chenye kukubalika kila mahali.

Mama/dada Kama unatamani kujipamba basi jipambe kwa mapambo ya kibiblia, ambayo ndiyo yale yanayotajwa katika 1Timotheo 2:9 na 1Petro 3:3.

1Petro 3:3 “Kujipamba kwenu, kusiwe kujipamba kwa nje, yaani, kusuka nywele; na kujitia dhahabu, na kuvalia mavazi;

4  bali kuwe utu wa moyoni usioonekana, katika mapambo yasiyoharibika; YAANI, ROHO YA UPOLE NA UTULIVU, ILIYO YA THAMANI KUU MBELE ZA MUNGU.

5  Maana hivyo ndivyo walivyojipamba wanawake watakatifu wa zamani, waliomtumaini Mungu, na kuwatii waume zao.

6  Kama vile Sara alivyomtii Ibrahimu, akamwita Bwana; nanyi ni watoto wake, mfanyapo mema, wala hamkutishwa kwa hofu yo yote”.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Mada zinazoendana:

Mafundisho mengine:

Marhamu ni nini? Na Manukato ni nini?

JE NI HALALI KUOA WAKE WENGI, AU KUTOA TALAKA?

SISI TU MANUKATO YA KRISTO.

Mawaa ni nini? Kama tunavyosoma katika biblia?

EPUKA KUCHELEWA IBADA.

Rudi nyumbani

Print this post

JINSI YA KUISHINDA HALI YA MSONGO WA MAWAZO.

Msongo wa mawazo ni nini? Ni shinikizo au mfadhaiko wa kiakili, unaomkumba mwanadamu, pale anapokutana na matatizo, au taabu, au dhiki au shida Fulani. Hivyo inapotokea mtu huyu anashindwa kuzitatua changamoto hizo, ndipo msongo huo huja.

Kwamfano labda mtu amegundulika, ana ugonjwa usiotibika, na kaambiwa na daktari hawezi kupona, mtu kama huyu ni rahisi kukumbwa na msongo wa mawazo,

Au labda mwingine hana kazi na akiangalia familia inamtegemea, na bado hajafikia malengo yake kulinganisha na umri alionao, moja kwa moja mtu kama huyu ni rahisi kukumbwa pia na msongo wa mawazo. N.k.

Na kama tiba isipopatikana matokeo yake yanaweza kuwa mtu huyo, kupata matatizo ya kiafya, wengine kuchanganyikiwa, wengine kujitenga na watu, wengine kujifungia ndani kulia tu usiku kucha, wengine kutenda vitendo viovu, hata kujiua.

Je! Mkristo anaweza kuwa na msongo wa kimawazo? Jibu ni ndio anaweza kuwa nao. Lakini tiba imeshatolewa. Tutaona katika somo hili kwa namna gani, kwasababu yawezekana wewe ni mmoja wapo ambaye unakutana na hali hii na hujui cha kufanya.

Embu tuone kwanza baadhi ya watu katika maandiko ambao walipitia misongo ya mawazo

1) Eliya:

Eliya wakati amemaliza kuwaua manabii wa Baali, akatazama huku na huku na kujiona kama ni yeye peke yake ndiye nabii wa Mungu aliyebaki, hivyo ikampelekea ajitenge, na kukimbilia jangwani, akae huko mpaka afe.  Lakini Mungu alikuja kumtokea baada ya siku 40, akampa majibu ya faraja, kwamba asidhani yupo peke yake kuna wengine 7,000 amejisazia, rudi Israeli, kanitumikie. (1Wafalme 18-19)

2) Mfalme Daudi.

Alikumbwa mara nyingi na msongo wa mawazo katika maficho yake alipokuwa anawindwa na mfalme Sauli. Mara nyingi alifikia hatua ya kukata tamaa ya maisha. Embu tafakari haya maneno aliyoyasema Daudi.

Zaburi 69:1 Ee Mungu, uniokoe, Maana maji yamefika mpaka nafsini mwangu.  2 Ninazama katika matope mengi, Pasipowezekana kusimama. Nimefika penye maji ya vilindi, Mkondo wa maji unanigharikisha.  3 Nimechoka kwa kulia kwangu, Koo yangu imekauka. Macho yangu yamedhoofu Kwa kumngoja Mungu wangu.  4 Wanaonichukia bure ni wengi Kuliko nywele za kichwa changu. Watakao kunikatilia mbali wamekuwa hodari, Adui zangu kwa sababu isiyo kweli. Hata mimi nalilipishwa kwa nguvu Vitu nisivyovichukua.  5 Ee Mungu, unajua upumbavu wangu, Wala hukufichwa dhambi yangu

3) Ayubu

Baada ya kupotelewa na mali zake, na watoto wake, hadi mwili wake kubaki mifupa tu. Mkandamizo ulimjia. Ayubu anasema;

Ayubu6:2 Laiti uchungu wangu ungepimwa, Na msiba wangu kutiwa katika mizani pamoja!  3 Kwa kuwa sasa ungekuwa mzito kuliko mchanga wa bahari; Kwa hiyo maneno yangu yamekuwa ya haraka

 Mpaka akanza kusema maneno magumu, ya kulaani siku aliyozaliwa. Mtu kama huyu alikuwa katika hali mbaya sana kifikra na kiakili.

4) Petro

Petro na Yuda walipitia jambo moja, kukana na kusaliti, ni dhambi pacha. Isipokuwa Yuda alikwenda kujinyonga kwasababu msongo wa mawazo ulimshinda, lakini Petro hakujinyonga. Yeye alikwenda kujificha na kulia sana kwa “majonzi”.  Tengeneza picha ni wewe unamkana Mungu wako, tena kwa maneno ya dhihaka mbele za watu. Hali hiyo unadhani itakufanya ujionaje kama sio mateso ya kiakili baada ya hapo?. Wengine wanapitia hali kama hizi, wanapojiona wamemtenda Mungu dhambi kubwa sana, isiyosameheka, wakidhani kuwa Mungu hawajali tena, hawathamini.(Mathayo 26:75)

5) Mitume 11.

Baada ya Bwana Yesu kufa, hofu ya wayahudi ikawavaa mitume, wakiona kuwa wao ndio wanaofuata kuuliwa baada ya kiongozi wao kufa.. Hivyo hiyo ikawapelekea kujifungia ndani, wasitoke. Msongo mkubwa sana wa mawazo uliwavaa, kutoka kwa wayahudi.(Yohana 20:19-29)

Itoshe tu kutumia mifano hiyo michache, kwani wapo wengine wengi sana katika biblia waliopitia hali kama hizi, mfano ni Musa, Yusufu, Yeremia, Nebukadreza, Hana (mamaye Samweli),  Danieli, Mtume Paulo wote hawa ukisoma habari zao katika biblia utayathibitisha hayo.

Lakini Je! Waliwezaje kuzishinda hizo hali.

Utagundua, walipopitia taabu zao, walilikumbuka TUMANI la Mungu. Ndilo lililowapa nguvu ya kuweza kuvuka nyakati hizo mbaya walizozipitia.  Waliyazingatia haya maneno;

1Petro 5:6  Basi nyenyekeeni chini ya mkono wa Mungu ulio hodari, ili awakweze kwa wakati wake; 7  HUKU MKIMTWIKA YEYE FADHAA ZENU ZOTE, kwa maana yeye hujishughulisha sana kwa mambo yenu.

Na lile alolisema Yesu..

Mathayo 11:28  Njoni kwangu, ninyi nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha

Pale akili zilipogoma, fikra kuzima, moyo kuwa baridi, walijifunza kumtwika Mungu, huzuni zao, mateso yao, shida zao. Hata pale ambapo hazikutatulika kwa wakati walioutarajia, lakini waliendelea na mwisho wa siku Bwana alikuja kuyaweka yote sawa. Kwasababu yeye mwenyewe alisema.

Yeremia 29:11 Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi TUMAINI siku zenu za mwisho

Hivyo ndugu, ikiwa na wewe upo katika hali hii ya msongo wa kimawazo, katika eneo lolote lile, iwe la kiroho, kihuduma, kifamilia, kikazi, kiafya, kimaendeleo. Umeshindwa kuendelea mbele, Usiogope. Kwa Mungu lipo TUMAINI, zaidi ya Matumaini yote ya kibinadamu.

Haijalishi msongo huo, umekupata kutokana na dhambi zako, au kutokana na hali zilizo nje ya uwezo wako. Usiogope. Mponyaji, mfajiri, mtatuaji wa matatizo yupo. Huyu si mwingine zaidi ya YESU KRISTO mwokozi.

Mungu akikupa tumaini, ujue ni lazima litokee, lakini mwanadamu akikupa tumaini, ni kusudi tu kukufariji, lakini tatizo linaweza kubaki palepale.  Yesu hayupo hivyo. Mtazame tu yeye. Wakati wa shida, ndio wakati wa kukimbilia chini ya mbawa zake, sio kuwakimbilia wanadamu.

JE! UFANYEJE?

  1. Katika hali hiyo, Usiache kuomba sana  & Kumsifu Mungu & Kushukuru, siku zote za maisha yako. Ongeza kiwango chako katika eneo hili.
  2. Soma sana Biblia: Utapata faraja ya Roho katika uwezo wa Mungu aliowatendea wengine.
  3. Usiwe mtu wa kutanga-tanga sana. Tuliza akili zako, si lazima utafute ushauri kwa kila mtu, jiachie kama vile huna tatizo lolote, ukimkabidhi Bwana yote, ukijua yeye yupo kazini.
  4. Kila wakati Jiambie, “Mungu wangu atayaweka yote sawa mwisho wa siku”.
  5. Mawazo ya kushindwa/kujihukumu yanapokuja yapinge.  Sema “Bwana ndiye boma langu na ngome yangu, na mwamba wangu sitatikisika”.

Na hakika, katika muda fulani, utaona Mungu anakuvusha, anakuponya, anakufariji, anakuondolea huo mzigo. Huo ni uhakika sio makisio. Usiache tu kuendelea na Bwana..

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Mafundisho Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618. Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

TUMAINI NI NINI?

UKIOKOKA,HIZI FIKRA ZIKIJA NDANI YAKO, ZIKATAE.

VITA VYA KIFIKRA BAADA YA KUZALIWA MARA YA PILI

TUUTAFUTE UMOJA WA ROHO.

Je shetani ana uwezo wa kujua mawazo ya mtu?

Tofauti kati ya ndoto na Maono ni ipi?

Rudi nyumbani

Print this post

Mwanamke aliyepotelewa na sarafu yake.

Huu ni mwendelezo wa Mafundisho maalumu yawahusuyo wanawake.

Mwanamke aliyepoteza shilingi moja.

Luka 15:8  Au kuna mwanamke gani mwenye shilingi kumi, akipotewa na moja, asiyewasha taa na kufagia nyumba, na kutafuta kwa bidii hata aione? 9  Na akiisha kuiona, huwaita rafiki zake na jirani zake, akawaambia, Furahini pamoja nami, kwa kuwa nimeipata tena shilingi ile iliyonipotea.

Bwana Yesu alipenda kutumia mifano halisi ya kimaisha kutufundisha habari za rohoni. Kwamfano katika habari hiyo tunafahamu mfano huo ulikuwa analenga mambo ya ufalme wa mbinguni, jinsi Mungu anavyomthamini mtu wake mmoja aliyepotea katika dhambi, pindi atubupo na kurejea. Kwamba tendo  hilo linamfanya yeye pamoja na malaika zake mbinguni kufurahi sana.

Lakini leo nataka tujifunze kuhusu mfano huo katika uhalisia wake wa kimaisha kama ulivyoandikwa. Kuna maswali lazima ujiulize kwanini amtaje mwanamke na sio mwanaume. Kisha aipoteze shilingi yake pale NYUMBANI kwake, na sio sehemu nyingine, labda barabarani au sokoni? Tofauti na mfano uliotangulia ambao unamzungumzia Yule mtu aliyepotelewa na kondoo mmoja akawaacha wale 99 akaenda kumtafuta Yule mmoja huko maporini.

Na hatua ambazo alitumia kuitafuta shilingi ile hadi kuipata, kuna funzo gani pia?.

Kumbuka kimaandiko aliyekabidhiwa nyumba aisimamie ni mwanamke, ndio maana biblia inasema,

Mithali 14:1 Kila mwanamke aliye na hekima hujenga nyumba yake; Bali aliye mpumbavu huibomoa kwa mikono yake mwenyewe.

Na hazina yake inapatikana humo, lakini pia ikipotea, basi hupotelea humo humo.

Tukisema nyumba hatumaanishi, gorofa, na sebule na jiko. Hapana, bali tunamaanisha wale waliomo mule. Hao ndio hazina yake hasaa.

Sasa katika mfano huo mwanamke huyu alikuwa na shilingi 10, labda tuseme hao ni watoto 10, au ndugu 10, lakini mmoja akapotea, huwenda akawa mtundu, au mwizi, au kibaka, au shoga, au jambazi n.k.  Lakini Mwanamke huyu hakukata tamaa na kukaa chini na kusema, Ahh! Ninao hawa 9, wenye kujitambua na wenye nidhani. Embu ngoja niachane na Yule pasua kichwa mtukutu, mwenye kiburi, asinipe presha, nifarijiwe na hawa wanangu 9 wazuri. Hapana, bali alilazimika kufanya jambo ili kuhakikisha amempata na Yule.

Hivyo kama tunavyosoma, hakukaa tu hivi hivi, na kuzungumza. Bali alichukua hatua fulani, na hatua zenyewe ndio hizi tatu.

  1. Kuwasha taa
  2. Kufagia nyumba
  3. Kuitafuta kwa bidii

Hii ikiwa na maana gani? mpaka anafikia hatua ya kuwasha tamaa, maana yake ni kuwa chumba hicho kilikuwa na giza, hivyo asingeweza kuipata shilingi yake katika mazingira yale. Tafsiri yake ni nini? Alimkaribisha Kristo. Ambaye ndio Nuru ya ulimwengu katika nyumba yake.

Hivyo hatua ya kwanza katika kutatua tatizo lake, alimtambua Kristo kwenye nyumba yake. Na sasa Nuru ilipomulika ndipo akatambua kuwa nyumba ilikuwa chafu. Kama asingewasha taa, kamwe asingeweza kugundua kuwa Vitu havipo katika mpangalio wake. Hivyo ikampasa aanze kwanza kuifagia nyumba ile, aipangilie vizuri. Makombo yaliyodondoka sakafuni ayafagie, vikombe na vijiko vilivyokaa hoe hae, aviweke mahali pake, nguo ambazo hazijakunjwa aziweke kabatini, uwazi uwepo. Hakukimbilia kuitafuta shilingi yake katika hatua hiyo. alijua hawezi kuipata katika mazingira yale, machafu, imejificha sana.

Hivyo ikamchukua muda Fulani mrefu kuisafisha nyumba yake, mpaka hatimaye, pengine baada ya saa 6, ikawa safi. Kila kitu kikawa katika mpangilio wake.

Ndipo sasa akaenda katika hatua ya mwisho ya “kuitafuta kwa bidii ile shilingi”.  Akaanza kupita eneo moja baada ya lingine, hakutoka nje ya nyumba kwenda kuitafuta barabarani, hapana bali pale pale ndani kwasababu alijua fedha zake hazijawahi kutoka nje ya nyumba.

Na hatimaye akaipata. Na mwisho wa siku akawaalika na marafiki zake, wakafurahi pamoja. Kwasababu ilimgharimu kuipata tena.

Hii ni kufunua nini?

Wanawake wengi wanapoona aidha ndugu zao nyumbani, au watoto wao, au ndoa zao zimeharibika,. Wengine wanakimbilia kwa waganga ili wasaidike, hapo umepotea, wengine wanakimbilia kwa washauri wa kijamii, bado hujapata suluhisho. Suluhisho pekee ni Nuru ya ulimwengu. Yesu Kristo, aimulikie kwanza nyumba yako.

Na Yesu anachokifanya ni kukuonyesha madhaifu uliyokuwa nayo, uchafu uliomo nyumbani mwako, ili urekebishe (ndio ufagie). Sasa wengine wanapofikia hatua hii, wanapoona wanahubiriwa waishi maisha ya utakatifu, wawe watu wa ibada majumbani mwao, wawe waombaji, wafungaji, wafukuze tabia zisiojenga majumbani  mwao, waweke mipaka Fulani kwenye familia zao. Wanaona kama wanatwikwa mzigo juu ya mzigo. Wanamkimbia Kristo, wanabakia kulia tu, na kuhuzunika..

Wanachofikiria tu, ni utatuzi wa tatizo, mume aache pombe (aokoke), watoto wawe wasikivu, nyuma iwe na amani, n.k.  lakini hawataki wao wenyewe kurekebisha baadhi ya mambo makwao. Hapo ndugu ukikwepa hatua hii, sahau kukipata unachokitafuta. Hata upewe bahari nzima ya mafuta ya upako, na pipa la chumvi. Unapoteza muda, hutatui jambo lolote.

Kristo anataka usafi kwanza, ndipo akupe jicho la kuiona shilingi yako iliyopotea. Sasa ikiwa utatimiza mambo hayo mawili yaani KRISTO ndani yako, na usafi wako. Kinachofuata ni kutafuta ulichokipoteza.

Hii ndio hatua sasa ya kumuhubiria, kumshauri, kumwonya, kumvuta kwa Bwana. Sasa ukiendelea hivyo hivyo, muda si mwingi utampata kiwepesi sana haijalishi alikuwa amepotea kiasi gani, au alikuwa sugu namna gani. Hakuna linaloweza kujificha mbele ya Nuru. Tatizo lolote sugu unalolijua wewe la kifamilia, kwa kufuata kanuni hizo litatatulika tu.

Hivyo wewe kama mwanamke, itambue huduma hii iliyopewa na Bwana, laiti kama wanawake wote, wangekuwa ni wa kujiwajibisha kwa namna hii, jamii zetu na familia zetu zisingekuwa na migogoro mingi,wala injili isingekuwa ngumu sana kuihubiri kwasababu tayari walishatangulia walioweka misingi bora nyuma. Hii ni huduma kubwa sana kwa mwanamke na Bwana anaithamini sana.

Simama katika nafasi yako wewe kama mama, wewe kama Dada, nyumba au familia itasimama, endapo wewe utasimama.

Bwana akubariki

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

MAFUNDISHO KWA WANAWAKE

MWANAMKE ABIGAILI ANAFUNZO GANI KWA WANAWAKE?

Je mwanamke Fibi, alikuwa ni askofu wa makanisa, kama mitume?

BADO TUTAHITAJI TU KUSAIDIANA.

Je Mungu anaketi katika giza? (1Wafalme 8:12)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

Rudi nyumbani

Print this post

UTAJUAJE KAMA WEWE NI MTUMISHI WA MUNGU NA KRISTO YU PAMOJA NAWE?.

(Masomo maalumu kwa watumishi).

Jina la Mwokozi YESU KRISTO Lihimidiwe daima.

Je unajua namna yakujipima kama kweli wewe ni mtumishi wa Mungu na Kristo yu pamoja nawe?

Je unadhani ni ishara na miujiza ndio utambulisho pekee ya kwamba Kristo yu pamoja nawe?

Nataka nikuambie La!..Ishara na miujiza si uthibitisho wa kwanza wa Kristo kuwa pamoja nawe, kwasababu biblia inasema Yohana Mbatizaji hakufanya ishara hata moja lakini bado alikuwa mkuu kuliko manabii wote waliotangulia.

Yohana 10:41 “Na watu wengi wakamwendea, wakasema, Yohana kweli hakufanya ishara yo yote, lakini yote aliyoyasema Yohana katika habari zake huyu yalikuwa kweli”.

Na pia wapo watakaofanya ishara lakini atawakana kuwa hawajui…

Mathayo 7:22 “Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?

23 Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu”.

Umeona kumbe kufanya ishara au kutofanya si tija!..Si uthibitisho wa kwanza kuwa Kristo yu nawe!.

Sasa ni kipi kinachotupa uthibitsho kuwa tunatembea na YESU katika utumishi tunaoufanya?.

Jibu tutalipata katika maandiko yafuatayo..

Yohana 12:26 “Mtu akinitumikia, na anifuate; nami nilipo, ndipo na mtumishi wangu atakapokuwapo. Tena mtu akinitumikia, Baba atamheshimu”.

Hapo Bwana anasema mtu akitaka kumtumikia, yani kuwa mtumishi wake BASI AMFUATE!!… Na yeye alipo ndipo na mtumishi wake alipo, au kwa lugha nyepesi “Yeye yupo pamoja na wale waliomfuata”.

Sasa tunamfuata vipi YESU?.

Tusome tena maandiko yafuatayo..

Luka 9:23 “Akawaambia wote, Mtu ye yote AKITAKA KUNIFUATA, na ajikane mwenyewe, ajitwike msalaba wake kila siku, anifuate.

24 Kwa kuwa mtu atakaye kuiponya nafsi yake ataiangamiza, na mtu atakayeiangamiza nafsi yake kwa ajili yangu ndiye atakayeisalimisha”.

Kumbe ili tuwe watumishi wa kweli wa Mungu, ambao Kristo atakuwa nasi muda wote ni lazima TUJIKANE NAFSI KILA SIKU??.

Sasa swali ni je tumejikana nafsi zetu? au tunazipenda nafsi zetu na kuzishibisha kwa kila tunachokitaka.

Huwezi kumtumikia Mungu na huku hutaki kuacha mila, huwezi kumtumikia Mungu na huku unaupenda ulimwengu.
Huwezi kuwa mtumishi wa Mungu na huku hutaki kuacha mizaha, na wala dhambi.

Huwezi kumtumikia Mungu na bado unaishi na mke/mume asiye wako. Fahamu kuwa Kristo hayupo na wewe hata kama unaona ishara na miujiza katika maisha yako..hiyo ni kulingana na maneno ya Kristo mwenyewe.

Kanuni ya kutembea na Kristo, itabaki kuwa ile ile MILELE! Nayo ni KUJIKANA NAFSI, KUBEBA MSALABA NA KUMFUATA YEYE!. Kwasababu Kristo ni yeye yule, jana na leo na hata milele (Waebrania 13:8).

Na hiyo ni kwa faida yetu na si yake! (Ayubu 35:7).

Huenda umeshamwamini Kristo kuwa ni Bwana na Mwokozi wa maisha yako!.. Hiyo ni nzuri sana, lakini bado haitoshi, ni lazima uongezee hapo “KUJIKANA NAFSI!”. Na baada ya kufanya hivyo pia ujiandae kwa dhiki kwaajili yake.

Jiandae kuchekwa, kudharaulika, kuonekana mshamba, mjinga na usiyejielewa. Usiogope maana hizo ndizo chapa zake Yesu, (Wagalatia 6:17), na wewe sio wa kwanza, zilianza kwa Kristo BWANA WETU NA AKAZISHINDA.

Yohana 16:33 “Hayo nimewaambieni mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu”

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

REKEBISHA YAFUATAYO ILI UCHUMI WAKO UKAE SAWA.

KAMA MTUMISHI WA MUNGU, TAFUTA MAARIFA KWA BIDII.

“Amdhaminiye mgeni hakosi ataumia;Achukiaye mambo ya dhamana yu salama

Roho, Nafsi, na Mwili vina utofauti gani?

MAHANAIMU (Jeshi la Mungu)!.

Rudi nyumbani

Print this post

MWONGOZO WA MAOMBI YA WAHUDUMU/ WASIMAMAO MADHABAHUNI.

Ikiwa wewe una kazi ya kusimama madhabahuni/Mimbarani mara kwa mara kuwahudumia watu wa Mungu, basi ujue umewekwa mahali pa heshima sana, lakini pia pa kuwa makini sana. Kwa namna gani? Mahali pa heshima kwasababu ndio sehemu Mungu hushukia kuwahudumia watu wake, Hivyo wewe unakuwa kama lango la kwanza la Mungu, kusema au kutenda kazi kwa watu wake. Lakini pia usipopatumia ipasavyo una hatari kubwa sana ya kuuharibu utukufu wa Mungu. Na matokeo yake ni kuliathiri kundi zima kabisa, au ibada yote kutokuwa na maana.

Mara nyingine ibada kutofikia kilele cha Roho Mtakatifu, sio wale watu wasikiao kutokuwa makini, hapana ni kutokana na wahudumu kutokuwa na maandalizi ya kutosha ya kiroho na ki-mwili pindi haudumupo.  Kwa mfano ikiwa wewe ni mhubiri/Mchungaji, na unajua unaingia katika semina, au  jumapili utahudumu, halafu inafika asubuhi ya jumapili ndio uwaza ni nini cha kwenda kufundisha. Unaanda somo dakika 15tu, kisha unakwenda kusimama kuwahudumia watu wa Mungu, ambao wanatazamia walishwe Neno litakalowageuza maisha yao. Hapo ndugu usijidanganye, kuhudumu kwa namna hiyo sio kama Bwana anavyotaka.

Kumbuka kuwa machachari madhabahuni, kuwa na sauti kubwa, kuwa na uwezo wa kutoa vionjo mbalimbali, na watu kushangilia na kuruka-ruka, wakasema AMEEEN! Kubwa, ukadhani hiyo ndio ibada iliyowabariki watu. Hapo umejidanganya. Ibada isiyo na maandalizi haijalishi, imewarukisha watu kiasi gani. Hakuna uvuvio wa Roho!.

Ibada inaweza isiwe na makelele yoyote, mhubiri akawa ni mwenye kigugumizi, lakini ikiwa imeandaliwa vema kiroho. Maneno machache yanaweza yakawa na maana zaidi ya maneno elfu, na ya milio ya vinanda na gitaa. Watu wakajengwa, wakaguswa, wakafarijiwa, roho zao kwa namna ambayo wewe mhubiri unaweza ukadhani hujafanya jambo lolote. Isipokuwa wao wenyewe ndio wanaelewa mioyoni mwao.

Hivyo epuka njia za kisiasa na za kijamii, katika habari za kiroho. Mungu anataka amwachie Roho wake Mtakatifu kushughulika na hali za mioyo ya watu. Hivyo ni lazima ujue namna ya kumwandalia mazingira hayo Roho wake, ili afanye kazi kama apendavyo.

Kama wewe ni mhudumu yoyote, aidha mhubiri/ mwana-kwaya. Jifunze kuwa na maandalizi marefu. Andaa somo lako, ukianza siku kadhaa kabla, au kama umetingwa sana, siku moja kabla, ukitenga saa za kutosha za kukaa uweponi kwenye utulivu walau SAA 4-5, tena ikizidi  hapo inakuwa ni vizuri zaidi. Katika hizo, Tumia saa 2 na nusu Kuombea Somo na ibada, tena Tumia Saa 2 na nusu kuandaa somo lako. Ikiwa mchana kuna usumbufu, Muda wa usiku ni mzuri zaidi.

Sasa katika maombi yako omba Roho Mtakatifu akufanyie mambo yafuatayo;

1) Omba Mungu akupe Somo la Kufundisha: (Dk 15)

Wakati mwingine unaweza ukawa na somo lako kichwani, hiyo ni vema. Lakini liondoe hilo kwanza, msihi Roho Mtakatifu akufunulie alilolikusudia kuwafikia watu wake siku hiyo. Na kwa kufanya hivyo aidha atakupa jipya kabisa pale utakapokuwa unatafakari, au ataliboresha hilo ulilokuwa umeliwaza, au siku ile ile atayazungumza maneno mapya kwa kinywa chako. Hivyo usikimbilie moja kwa moja kuhitimisha na kile ulichokipanga kukisema. (Yohana 16:13)

2) Omba Bwana akujalie kuihubiri kweli yote ya Neno lake na kwa ujasiri.(Dk 15)

Ni rahisi kama mwanadamu, kuhubiri mawazo yako, au injili nusu-nusu, aidha kwa kuwaogopa watu, au kuwapendeza watu, au kuwahurumia watu. Hivyo omba Bwana akusaidie hapo. Ili usilighoshi Neno lake na mawazo au hisia zako. Bwana Yesu alisimamia kweli katika mafundisho yake yote.

Yohana 8:40  Lakini sasa mnatafuta kuniua mimi, mtu ambaye nimewaambia iliyo kweli, niliyoisikia kwa Mungu. Ibrahimu hakufanya hivyo.

Yohana 7:7  Ulimwengu hauwezi kuwachukia ninyi; bali hunichukia mimi, kwa sababu mimi naushuhudia ya kuwa kazi zake ni mbovu

3) Omba Bwana aweke mifano kinywani mwako:(Dk 15)

Wakati mwingine lazima tuombe kuhubiri kama Bwana alivyohubiri. Yeye alitumia mifano mingi katika kuwasilisha Neno la Mungu. Na sisi pia hatuna budi kumwomba Roho Mtakatifu atujalie hekima hiyo. Husaidia sana watu kulielewa Neno kiurahisi na kulifurahia. Ukiomba Roho Mtakatifu anaweza kukufunulia wakati unaandaa somo, au wakati ule ule utakaokuwa unafundisha.

Marko 4:33  “Kwa mifano mingi ya namna hii alikuwa akisema nao neno lake, kwa kadiri walivyoweza kulisikia; 34  wala pasipo mfano hakusema nao;..”

4) Bwana ayajalie maneno yako yawe yenye uweza pindi uhudumupo:(Dk 15)

 Maneno yenye uweza, ni maneno yenye mamlaka. Bwana akitujalia karama hii ambayo ilikuwa ndani ya Yesu, tutaweza kuitiisha madhabahu, na watu kulisikiliza Neno la Mungu kwa hofu ya Mungu, na kwa nidhamu, na kwa bubujiko, mpaka watu Kuokoka na kuacha maovu.

Luka 4:32  “wakashangaa mno kwa mafundisho yake, kwa kuwa neno lake lilikuwa na uwezo”.

5) Omba jina la Mungu litukuzwe:(Dk 15)

Katika kuhubiri kwako ni muhimu sana, kuomba jina la Yesu litukuzwe. Wahubiri wengi wasimamapo hujijengea mazingira yao ili watukuzwe. Ili waonekane wanaupako, wanashuhuda n.k.. Lakini sio Kristo ainuliwe. Msihi Mungu akupe unyenyekevu madhahabuni pake, Ibada isiyo mtukuza Kristo, haijalishi itakuwa na uzuri kiasi gani, ni bure. Watu watoke wamemwona Kristo na sio mtu au vitu (Wakolosai 3:17).

6) Mungu akupe roho ya upambanuzi, (macho yako ya rohoni yafumbuliwe).(Dk 15)

Tuhudumupo hatuna budi kumwomba Mungu daima atupe upambanuzi, ni maombi ya daima, inaweza isiwe katika ibada zote, lakini pale ambapo anataka kufanya jambo basi atupe kuona rohoni. Ili tuweza kutembea katika wazo lake. Kwamfano labda mtu anatatizo Fulani, na Bwana anataka afunguliwe kwa wakati huo. Hivyo ni vema tumwombe Mungu karama hii. (Yohana 16:30)

7) Bwana akujalie usiathiriwe na mazingira:(Dk 15)

Mazingira huwaarithi wahudumu, kwamfano pale unapoona watu hawazingatii unachowafundisha, wengine wamelala, au mazingira ya sauti za mbali, au watu wanaozungumza, janga Fulani n.k.. Huweza kukutoa katika umakini wa Roho Mtakatifu. Hivyo Bwana akufanye kipofu katika eneo hilo ili usiuzimishe mtiririko bora wa Roho Mtakatifu. Adui hupenda kutumia mbinu hii, kukuvuruga. (Matendo 20:7-12)

8) Omba nguvu za Mungu ziwepo kuwahudumia watu:(Dk 15)

Omba Kwa kupitia mahubiri au mafundisho watu wafunguliwe, waponywe, wabarikiwe, wafarijiwe, ishara. Ibada isiwe baridi, au ya maneno matupu tu. Shuhuda zitokee, ili watu wamtukuze Mungu.

Luka 5:17  Ikawa siku zile mojawapo alikuwa akifundisha, na Mafarisayo na waalimu wa torati walikuwa wameketi hapo, waliotoka katika kila kijiji cha Galilaya, na Uyahudi, na Yerusalemu; na uweza wa Bwana ulikuwapo apate kuponya

9) Omba Bwana akulinde na mishale yote ya yule mwovu: (Dk 15)

Adui huwawinda sana wahudumu, na wahubiri na hivyo mishale mingi huwa inatumwa rohoni kukuvuruga, aidha kihisia, au kiafya, au kiakili. Omba Bwana akuzungushie wigo wake. Uchawi wowote, au roho zozote nyemelezi zisipate nafasi ya kupakaribia pale ulipo, au kuvuruga unachokifundisha. (Zaburi 127:1)

Kumbuka maombi haya sio kwa wahubiri tu, bali pia kwa wengine wote wahudumuo, kama vile Wana-kwaya, waalimu wa watoto, vijana, wakina-mama, wainjilisti, wamishionari.n.k. maadamu unahudumu hakikisha unakuwa na maandalizi, ili huduma yako isiwe bure. Zingatia sana maandalizi ya muda mrefu. Ukimaliza walau Dakika hizo zote 135 kwenye maombi. Sawa na SAA MBILI NA NUSU. Ukatumia tena muda kama huo kuandaa chakula chako cha kiroho. Utajiweka vizuri sana Roho Mtakatifu kufanya kazi vema kupitia wewe.

Bwana akubariki. Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Pia tazama >>> JINSI YA KUSIMAMA NA KUFUNDISHA/ KUHUBIRI

Bwana

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mafundisho mengine:

Mimbari ni nini? Je tofauti kati ya Mimbari na madhabahu ni ipi?

Jinsi ya kuandaa Somo la kufundisha

NIFANYE NINI ILI MUNGU AYAJIBU MAOMBI YANGU?

Nini maana ya kuabudu?

EPUKA KUCHELEWA IBADA.

Nini maana ya kumwabudu Mungu katika Roho na kweli?

SABATO ILIFANYIKA KWAAJILI YA MWANADAMU NA SI MWANADAMU KWAAJILI YA SABATO!

Rudi nyumbani

Print this post

NI KIJIJI CHA AINA GANI UPO?

Yapo makazi ambayo si rafiki sana kwaajili ya uponyaji wa maisha yako!.

Kuna mahali/vijiji/mitaa ambayo ukikaa ni ngumu kupokea chochote kutoka kwa Mungu, isipokuwa Mungu mwenyewe amekuambia uishi hapo!. Lakini kama hakuna msukumo wowote wa KiMungu kuishi hapo, basi kuwa makini na mahali utakapopachagua!, kama ni mtaa, mji au kijiji.

Utauliza kwa namna gani?

Utakumbuka yule kipofu aliyepelekwa kwa Bwana ili aponywe!, biblia inasema “Bwana Yesu alimtoa nje ya kijiji kabla ya kumponya” na hata baada ya kumponya alimzuia asirudi kile kijiji alichokuwepo!.

Marko 8:22 “Wakafika Bethsaida, wakamletea kipofu, wakamsihi amguse.

23  Akamshika mkono yule kipofu, AKAMCHUKUA NJE YA KIJIJI, akamtemea mate ya macho, akamwekea mikono yake, akamwuliza, Waona kitu?

24  Akatazama juu, akasema, Naona watu kama miti, inakwenda.

25  Ndipo akaweka tena mikono yake juu ya macho yake, naye akatazama sana; akawa mzima, akaona vyote waziwazi.

26  Akampeleka nyumbani kwake, akisema, HATA KIJIJINI USIINGIE”

Umeona?..sababu ya Bwana kumtoa huyu kipofu nje ya kijiji si kwasababu ya ghasia ya watu!, hapana bali ni kutokana na hali ya kiroho ya mahali pale, maana yake mazingira ya kile kijiji yalikuwa ni magumu kwa yule mtu kupokea uponyaji! (Maana yake ukinzani uliokuwepo pale ulikuwa ni mkubwa sana), Ndio maana Bwana akamtoa kwanza nje ya kijiji kabla ya kumponya!

Hali kama hiyo inaendelea hata leo!, ipo mitaa ambayo ina vita vikali vya kiroho kuliko mingine, vipo vijiji vilivyo vizito kuliko vingine, na sisi kama wana wa Mungu ni lazima tuongozwe na roho mahali pa kwenda na mahali pa kuishi.

Aina ya vijiji/mitaa ifuatayo kuwa makini nayo!

1. Yenye watu wengi wasio na hofu ya Mungu.

Ukiona mtaa/kijiji hakuna hofu ya Mungu, maana yake watu wa mahali hapo ni watu wasiojali, na hata kuidharau injili, na kuipinga kazi ya Mungu, kuwa makini na huo mtaa au hicho kijiji. Kwasababu mitaa inayoikataa Injili mara nyingi inakuwa chini ya vifungo vya laana (Mathayo 10:14-15), na mwisho wake huwa inaharibiwa na Mungu aidha kwa mapigo ya magonjwa au majanga au hali za kiuchumi!.

2. Yenye kiwango kikubwa cha ushirikina na uasherati.

Uchawi na uasherati ni ibada kuu mbili za shetani. Mahali palipojaa kiwango kikubwa cha uasherati na ushirikina fahamu kuwa hiyo ni kambi ya adui asilimia zote. Kuwa makini na mahali hapo!. Kama Roho wa Bwana amekuongoza uishi, basi ishi hapo na utafanikiwa, maana ni mapenzi yake!..lakini kama sio, basi usiishi hapo, ili ubaki salama na familia yako!, (mara nyingi adui anatumia mitaa/vijiji kuharibu watoto au ndoa), hivyo kuwa makini!

Ufunuo 18:4 “Kisha nikasikia sauti nyingine kutoka mbinguni, ikisema, Tokeni kwake, enyi watu wangu, msishiriki dhambi zake, wala msipokee mapigo yake”

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

UPENDO NI NINI NA JE! KUNA AINA NGAPI ZA UPENDO?

KUNA AINA NGAPI  ZA MAOMBI?

AINA ZA MAJINI, MAJINA YAO, KAZI ZAO, NA TIBA ZAKE.

Aina za dhambi

UJUE UCHAWI WA MANABII WA UONGO?.

Rudi nyumbani

Print this post

MWONGOZO WA MAOMBI YA KUJIKUZA KIROHO.

Ikiwa wewe umeokoka, na una kiu kweli ya kumkaribia Mungu wako katika viwango vya juu. Basi fahamu huna budi ujikuze kiroho. Na ukuaji huo hutegemea mambo mawili makuu “Neno pamoja na maombi”. Katika tovuti hii yapo mafundisho mbalimbali yatakayokusaidia kupiga hatua hizo.

Makala hii imeegemea zaidi katika Maombi. Hivyo huu ni mwongozo wa Wiki kwa Wiki, mfululizo wa vipengele muhimu vya kuombea. Uwapo nyumbani, uwapo kanisani. Jiwekee ratiba Kisha kuwa mwombaji. Na hakika baada ya wakati fulani utaona matokeo makubwa sana ndani yako.

Wiki ya Kwanza:

Wiki ya pili:

Wiki ya Tatu:

Wiki ya Nne:

Wiki ya Tano:

Wiki ya Sita:

Wiki ya Saba:

Wiki ya Nane:

Mwendelezo utakuja…

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

MASOMO MBALIMBALI YA NENO LA MUNGU.

MAFUNDISHO MAALUMU KWA WAONGOFU WAPYA.

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 1

Orodha ya mafundisho yote.

KUONGOZWA SALA YA TOBA

Rudi nyumbani

Print this post

Makwazo ni nini kibiblia? Na madhara yake ni yapi?

Makwazo ni  mambo yanayozuia mwendelezo wa jambo Fulani lililokuwa limekwisha anza, au linalotaka kuanza. Kwamfano ulikuwa unasafiri lakini ghafla kwenye safari yako unakutana na mto mpana, unaokufanya ushindwe kuvuka, hicho kinaitwa kikwazo. Au ulikuwa unapika chakula chako, halafu ghafla gesi ikaishia katikati na chakula bado hakijaiva, hicho kinatiwa kikwazo.

Na rohoni pia vivyo hivyo yapo makwazo ambayo yanamzuia mtu asimalize mwendo wake wa imani, au asiendelee mbele tena katika kumtafuta Mungu. Na muhimu sana kuyajua na kujiepusha nayo.

Kibiblia makwazo yamegawanyika katika sehemu kuu tatu.

  1. Makwazo yanayowakumba watu wa Mungu kutoka kwa wapendwa wenzao
  2. Makwazo yanayowakumba watu wa Mungu kutoka kwa wapagani
  3. Makwazo yanayowakumba wapagani kutoka kwa watu wa Mungu.

1) Makwazo yanayowakumba watu wa Mungu kutoka kwa wapendwa wenzao

Tukianzana  na hilo kundi la kwanza, wapendwa tunaowazungumzia hapa ni wale ambao hawajasimama vema katika kweli. Ndio hawa ambayo Bwana Yesu anawazungumzia katika vifungu hivi;

Luka 17:1  Akawaambia wanafunzi wake, Makwazo hayana budi kuja, lakini ole wake mtu yule ambaye yaja kwa sababu yake! 2  Ingemfaa zaidi mtu huyo jiwe la kusagia lifungwe shingoni mwake, akatupwe baharini, kuliko kumkosesha mmojawapo wa wadogo hawa. 3  Jilindeni; kama ndugu yako akikosa, mwonye; akitubu msamehe. 4  Na kama akikukosa mara saba katika siku moja, na kurudi kwako mara saba, akisema, Nimetubu, msamehe.

Kwa namna gani hawa wanaweza kumkosesha ndugu. Kwamfano ni pale, Mpendwa mwezako anaposikia umemsengenya, Sasa Kama ni mdhaifu kiimani Hili linaweza kuwa ni kwazo kubwa sana kwake ambalo likamfanya hata nguvu yake ya kuendelea kudumu katika kusanyiko ikapoa. Zipo shuhuda nyingi sana za wapendwa ambao wamerudi nyuma kiwokovu kwasababu ya maisha haya. Hivyo kama mwanaminio hakikisha, kinywa chako, unakichunga. Jifunze kuwa na kiasi na uvumilivu. Jifunze kujiepusha na mambo mabaya Kwa wapendwa wenzio.

Kwazo hili linaweza pia kuwa katika ufahamu wa kiroho .

Utakumbuka Ayubu, alipopitia majaribu yake mazito, hakuna mahali popote alinena maneno yasiyo faa, lakini wale marafiki zake watatu, yaani Sofari, Elifazi na Bildadi, (ambao wanawawakilisha watumishi wa Mungu), walipofika, walitumia ujuzi wao wa kibinadamu kumuhukumu Ayubu, kwamba ni kwasababu alitenda dhambi,  hiyo ikampelekea Ayubu kunena hata maneno yasiyofaa.

Kama mtumishi wa Mungu, epuka hukumu ya macho,ukiletewa tatizo la mtu/ watu, usiangalie kwa jicho la nje, mwingine ni Mungu mwenyewe anampitisha katika madarasa yake, ukajikuta badala ya kutatua tatizo ndio unaongeza tatizo juu yake. Usianze kuhukumu matukio, bali kuwa katika Roho, tegemea zaidi uongozo wa Roho Mtakatifu. Hekima itakusaidia.

Pia lipo katika ujuzi.

Ukisoma Warumi 14, maandiko yanaeleza kwa upana jinsi ujuzi wetu unaweza kuwa kwazo kwa wengine wadhaifu was imani, kwamfano wewe ukipewa chakula ambacho umesikia kimepitishwa kwenye matambiko, ukashukuru, ukakila, ukijua kabisa chakula hakiwezi kukuondoa kwenye mpango wa Mungu. Lakini kwa ujuzi huo mwingine mwenye imani haba akakuona, na yeye akaanza kula vyakula vya kimatambiko na mila, akajikuta anashirikiana na uganga na mizimu, utakuwa umemsababishia kwazo kubwa kwa Mungu.

Lolote tunalolifanya, lazima tuangalie wengine wanaiga nini kwetu sisi wenye ujuzi. Uvaaji wako, wewe kama mkristo, unaweza ukajiona hauna shida kwako, lakini wengine wakaona ni sawa, hata kuvaa mavazi hayo ambayo hayana utukufu mbele za Mungu, utakuwa umefanyika kwazo kwao

2) Makwazo yanayowakumba watu wa Mungu kutoka kwa wapagani

Wapagani wanaweza kuzuia injili, isihubiriwe mahali, wakawapiga au wakawafunga watu wa Mungu n.k. Utaona Herode alimpinga Yohana akamweka gerezani hakuweza tena kuhubiri injili, wapagani waliwapinga watakatifu wengi. Hata mitume katika ziara zao walikutana na vikwazo vingi kutoka kwa watu wa mataifa, mahali pengine hawakuweza kuhubiri kwa utulivu (1Wakorintho 15:32, 1Wathesalonike 2:2).

3) Makwazo yanayowakumba wapagani kutoka kwa watu wa Mungu.

Watu ambao hawajakamilika katika imani. Kwamfano ni mpendwa lakini mzinzi, sasa wale watu wa nje, ambao walikuwa wanakaribia kuvutwa katika imani, wanapoona matendo ya watu kama hawa, wanasema kama ukristo wenyewe ndio huu ni heri niendelee kuwa mpagani. Hayo ni makwazo. Au unakuta mwingine ni tapeli, mwingine ni mtukanaji, mambo kama haya hufanyika kwazo kubwa sana kwa wapagani kuihubiri injili.

2Wakorintho 6:3  Tusiwe kwazo la namna yo yote katika jambo lo lote, ili utumishi wetu usilaumiwe; 4  bali katika kila neno tujipatie sifa njema, kama watumishi wa Mungu; katika saburi nyingi, katika dhiki, katika misiba, katika shida;

Hitimisho:

 Hivyo wewe kama ni mkristo jitahidi sana kuyaepuka makwazo kwa waaminio wenzako au kwa wapagani. Lakini pia kama ulikwazwa na ndugu yako, basi,  suluhisho sio kuvunjika moyo au kuuacha wokovu, bali ni kunyanyuka tena na kuendelea mbele. Biblia inasema;

Mithali 24:16 Kwa maana mwenye haki huanguka mara saba akaondoka tena; Bali wasio haki hukwazwa na mabaya.

Amka tena, mtumikie Bwana, kwasababu alishatujuza tangu mwanzo kwamba hayana budi kuja, hivyo hilo liwe ni jambo la kawaida kwako, jitie nguvu uendelee mbele.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

Mpagani ni nani?

USIMLAANI KIZIWI, WALA USITIE KWAZO MBELE YA KIPOFU.

Kutoka 21:10 ina maana gani?

Biblia inasema tusiwe kwazo kwa yeyote, je! inawezekanikaje kwa dunia hii ya sasa?(2Wakorintho 6:3).

MIMI SIOMBI KWAMBA UWATOE KATIKA ULIMWENGU.

HISIA YA MUNGU ILIYO MBAYA KULIKO ZOTE.

KIKWAZO CHA EUODIA NA SINTIKE.

Rudi nyumbani

Print this post

Nchi ya “Kabuli” ndio nchi gani kwasasa, na kwanini iliitwa hivyo? (1Wafalme 9:13).

Jibu: Tusome,

1 Wafalme 9:12 “Naye Hiramu akatoka Tiro kuitazama hiyo miji Sulemani aliyompa; wala haikumpendeza.

13 Akasema, Miji gani hii uliyonipa, ndugu yangu? Akaiita NCHI YA KABULI, hata leo”.

Nchi hiyo iliitwa “Nchi ya Kabuli” na sio “Nchi ya Kaburi”.Kuna tofauti ya “Kabuli” na “Kaburi”.

Maana ya “kaburi” ni shimo la kuzikia mtu aliyekufa, lakini “Kabuli” maana yake ni “isiyofaa kitu”. Kwahiyo hapo inaposema Nchi ya Kabuli, maana yake ni nchi isiyofaa kitu.

Sasa kwanini nchi hiyo iliitwa hivyo na huyu Hiramu?. Na ni funzo gani tunapata?.

Kipindi Sulemani anaijenga nyumba ya Mungu pamoja na nyumba yake mwenyewe, aliingia makubaliano na Mfalme wa Tiro kwamba Mfalme wa Tiro atampa Sulemani Malighafi za ujenzi (Miti ya Mierezi na mawe pamoja na malighafi nyingine baadhi, 1Wafalme 5:17-18), kwa makubaliano ya kwamba Mfalme Sulemani atampa Hirimu, mfalme wa Tiro ardhi kama malipo.

Sasa baada ya Sulemani kukamilisha ujenzi wa nyumba hizo mbili, ambapo alitumia miaka 20 (1Wafalme 9:10), aliazimu kumlipa Hirimu malipo yake.

Hivyo Sulemani akaamua kumpa Mfalme wa Tiro miji 20, (maana yake kila mji mmoja kwa mwaka mmoja aliotumikiwa). Zaidi ya hayo Sulemani alimpa Hiramu mwaka kwa mwaka kori nyingi za mafuta na ngano.

1Wafalme 5:10 “Basi Hiramu akampa Sulemani miti ya mierezi na miti ya miberoshi kadiri alivyotaka. 

11 Sulemani akampa Hiramu kori ishirini elfu za ngano, chakula cha watu wake, na kori ishirini za mafuta safi. Ndizo Sulemani alizompa Hiramu mwaka kwa mwaka”.

Lakini tunasoma Hiramu, Mfalme wa Tiro hakupendezwa na miji hiyo 20 iliyokuwa kaskazini mwa Israeli (Galilaya, mpakani na Tiro), na biblia haijataja sababu za yeye kutopendezwa na miji hiyo, huenda pengine aliona si mizuri na yeye alitegemea kupewa miji mingine mizuri yenye kupendeza, ambayo huenda ipo katikati ya Israeli.

Na kwasababu hakupendezwa nayo, aliipokea tu hivyo hivyo, na kuiita “miji isiyo na faida” yaani “Kabuli”

Lakini yote katika yote biblia haijaelezea kwa kina sababu ya Sulemani kufanya vile, au sababu ya Hiramu, Mfalme wa Tiro kutopendezwa nayo na hata kuiita nchi ya Kabuli (Maana yake isiyofaa kitu).

Ni nini tujajifunza kupitia habari hiyo na miji hiyo?.

Tunachoweza kujifunza ni kuwa tunapotenda wema “tusitegemee malipo kutoka kwa wanadamu, bali kutoka kwa Mungu”. Malipo ya wanadamu siku zote yana mapungufu mengi.

Mfalme huyu wa Tiro, alikuwa ni mtu mwema sana kuliko wafalme wote waliowahi kutokea Tiro, na zaidi sana alikuwa ni rafiki yake Mfalme Daudi, baba yake Sulemani, na hata alivyosikia kuwa Sulemani anataka kumjengea Mungu nyumba alifurahi sana na kumtukuza Mungu wa Israeli, (1Wafalme 5:7) hivyo akamtia nguvu Sulemani kwa sehemu kubwa sana, lakini pamoja na hayo alitazamia kupewa thawabu nyingi (malipo mengi) kutoka kwa Sulemani, kwasababu alijua Sulemani alikuwa Tajiri sana, Zaidi ya wafalme wote duniani, lakini kinyume chake akapewa vichache tofauti na alivyotegemea, hivyo moyo wake ukauma!, lakini Laiti kama angetegemea vichache ni wazi kuwa asingeumia kwa vile alivyopewa badala yake angeshukuru na thawabu yake ingezidi kuwa kubwa mbele za Mungu.

Hivyo na sisi hatupaswi kutegemea malipo kutoka kwa watu, pale tunapotenda wema bali tunapaswa tuwe na nia ya kiasi, ili wakati wa Bwana ukifika tupate thawabu kulingana na kile tulichokitenda.

Bwana atubariki.

Maran atha.

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618 Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

Miji ya Tiro na Sidoni ni miji gani kwasasa?

Kwanini Herode aliwakasirikia watu wa Tiro na Sidoni? (Matendo 12:20)

Je! Sulemani alienda mbinguni?

Je Mungu anaketi katika giza? (1Wafalme 8:12)

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 14 (Yoeli, na Obadia).

Rudi nyumbani

Print this post

Sakafu ya mawe/ Gabatha ni nini?

Neno hilo utalisoma katika andiko hili;

Yohana 19:13  Basi Pilato, aliposikia maneno hayo, akamleta Yesu nje, akaketi juu ya kiti cha hukumu, mahali paitwapo Sakafu ya Mawe, au kwa Kiebrania, Gabatha

Maana ya Gabatha ni “eneo lililoinuka”. Ni sehemu iliyojengwa mbele ya jumba la kifalme la Pilato ambapo hukumu zake alizitolea hapo. Kama biblia inavyosema paliitwa sakafu ya mawe. Maana yake palikuwa ni eneo la sakafu iliyojengwa kwa mawe.  (Tazama picha juu).

Hapo ndipo hukumu ya Bwana wetu Yesu Kristo ilipotolewa ya yeye kusulibiwa.

Lakini jambo ambalo unapaswa utafakari kuhusiana na tukio hilo, ni kuwa Mungu, ambaye ndiye muhukumu wa wanadamu wote, anasimama mbele ya kiti cha hukumu cha wanadamu kuhukumiwa. Mungu kukubali kuhukumiwa  Ni ishara ya unyenyekevu usiokuwa wa kawaida. Na hapo tunathibitisha kuwa hukumu za wanadamu hazitendi haki. Lakini utafika wakati na yeye mhukumu mkuu ataketi katika kiti chake cha enzi kuwahukumu wanadamu wote. Ambapo kwa haki kila mtu atalipwa sawasawa na matendo yake.

Jiulize wakati huo utakuwa upande upi?. Kwake hakuna upendeleo wa kibinadamu kama alivyofanya Pilato kwa wayahudi, kwake hakuna rushwa, kwake hakuna siri, yote yatamulikwa na kuwekwa wazi, na kama jina lako halipo katika kitabu cha uzima, utatupwa katika lile ziwa la moto, ambapo utateketea huko usiku na mchana.

Ufunuo 20:11  Kisha nikaona kiti cha enzi, kikubwa, cheupe, na yeye aketiye juu yake; ambaye nchi na mbingu zikakimbia uso wake, na mahali pao hapakuonekana. 12  Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao. 13  Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na Kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake. 14  Mauti na Kuzimu zikatupwa katika lile ziwa la moto. Hii ndiyo mauti ya pili, yaani, hilo ziwa la moto. 15  Na iwapo mtu ye yote hakuonekana ameandikwa katika kitabu cha uzima, alitupwa katika lile ziwa la moto.

Je!  Umejiandaaje kukutana na mhukumu wa haki? Kumbuka huwezi kuokoka, ikiwa bado upo nje ya Kristo Yesu. Unachopaswa kufanya ni kutubu leo,  ili upate ondoleo la dhambi zako. Ndipo kuanzia huo wakati na kuendelea uwe na amani na Mungu wako,. Hakuna ukombozi kwa yoyote Yule zaidi ya Yesu Kristo.Huwezi kuokoka kwa nguvu zako mwenyewe. Yesu alikufa tayari kwa dhambi zako, ili aziondoe, akuhesabie sio mkosaji.

Ikiwa upo tayari leo kumkabidhi Bwana maisha yako ayaokoe na kuyaongoza, Basi fungua hapa kwa mwongozo wa sala ya Toba >>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618. Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mafundisho mengine:

Kiti cha Rehema kilikuwaje? (Kutoka 40:20)

Uga ni nini? Na kazi yake ni ipi kibiblia?

MAUTI NA KUZIMU ZIKAWATOA WAFU WALIOKUWAMO NDANI YAKE.

Wote wanaokumbwa na mauti sasa ni kutokana na dhambi zao?

Chetezo ni nini katika biblia? (Walawi 10:1)

“Shinikizo” ni nini kibiblia, Na maana yake rohoni ni ipi?

Rudi nyumbani

Print this post