Category Archive Home

KWANINI NI NUHU, AYUBU NA DANIELI?

Jina la Bwana na mwokozi wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze biblia.. Maandiko yanasema..

Ezekieli 14:13 “Mwanadamu, nchi itakapofanya dhambi na kuniasi, kwa kukosa, nikaunyosha mkono wangu juu yake, na kulivunja tegemeo la chakula chake, na kuipelekea njaa, na kukatilia mbali mwanadamu na mnyama;

14 WAJAPOKUWA WATU HAWA WATATU, NUHU, NA DANIELI, NA AYUBU, kuwamo ndani yake, WANGEJIOKOA NAFSI ZAO WENYEWE TU KWA HAKI YAO, asema Bwana MUNGU”.

Hapo maandiko yamewataja watu watatu tu! Nuhu, Danieli pamoja na Ayubu. Unaweza kujiuliza ina maana ni hao tu ndio waliokuwa na haki kuliko manabii wengine wote na watakatifu wengine wote walioandikwa kwenye biblia (Agano la kale)?. Jibu ni la!..

Watakatifu wote wa kwenye biblia walikuwa na haki mbele za Mungu, na walimpendeza Mungu katika nafasi zao.. Lakini kulikuwa na jambo la kipekee katika hawa watu watatu, lililowafanya mpaka Bwana Mungu awataje hapa.. tutaenda kulitazama jambo hilo, ambapo litatusaidia na sisi kuenenda vyema katika ukristo wetu.

Sasa ili tuweze kuweka msingi wa kuelewa tabia waliyokuwa nayo hawa watu watatu, hebu tusome tena, maandiko mistari inayofuata ya mbele kidogo..

Ezekieli 14:19 “Au nikipeleka tauni katika nchi ile, na kumwaga ghadhabu yangu juu yake, kwa damu; ili kuwakatilia mbali nayo wanadamu na wanyama;

20 wajapokuwamo ndani yake Nuhu, na Danieli, na Ayubu, kama mimi niishivyo, asema Bwana MUNGU, HAWATAOKOA WANA WALA BINTI; watajiokoa nafsi zao tu kwa haki yao”.

Nataka tuone huo mstari wa 20, unaosema.. “Hawataokoa wana wala binti”. Maana yake ni kwamba watu hawa walikuwa wana tabia ya KUWAOKOA WATU NA GHADHABU YA MUNGU,  yaani Mungu alipotaka kuwaadhibu watu wote, hawa walisimama kuwaombea watu wao, au familia zao au wana wao, kitu kilichomfanya Mungu aghairi hasira yake kwa wale waliowaombea.

Kwa mfano utaona Nuhu, Mungu alipotaka kuigharikisha dunia, maandiko yanasema alionekana Nuhu peke yake ndiye mwenye haki,  wengine wote ikiwemo familia yake walikuwa miongoni mwa watu waliostahili adhabu ya gharika…. Lakini Nuhu alimwomba kwa ajili ya familia yake, na Mungu akamwambia atengeneze safina, sasa lengo la kutengeneza ile safina sio kujiokoa yeye peke yake bali yeye na nyumba yake, maandiko yanasema hivyo..

Waebrania 11:7 “Kwa imani Nuhu akiisha kuonywa na Mungu katika habari za mambo yasiyoonekana bado, kwa jinsi alivyomcha Mungu, ALIUNDA SAFINA, APATE KUOKOA NYUMBA YAKE. Na hivyo akauhukumu makosa ulimwengu, akawa mrithi wa haki ipatikanayo kwa imani”.

Hapo biblia inasema aliunda safina “APATE KUIOKOA NYUMBA YAKE”.. maana yake apate kuwaokoa wana wake na mke wake!.. Hivyo kitendo cha watoto wake kupata neema ya kuokoka ilikuwa ni kwasababu ya Nuhu Baba yao.

Vile vile tunamwona mtu kama Ayubu. Huyu naye alikuwa ni mtu wa kipekee sana, kwani kabla ya mambo yote alikuwa akiwaombea rehema watoto wake kwa Mungu kila siku.

Ayubu 1:4 “Nao wanawe huenda na kufanya karamu katika nyumba ya kila mmoja wao kwa siku yake; nao wakatuma na kuwaita maumbu yao watatu ili waje kula na kunywa pamoja nao.

5 Basi ilikuwa, hapo hizo siku za karamu zao zilipokuwa zimetimia, Ayubu hutuma kwao akawatakasa, kisha akaamka asubuhi na mapema, na kusongeza sadaka za kuteketezwa kama hesabu yao wote ilivyokuwa; kwani Ayubu alisema, YUMKINI KWAMBA HAWA WANANGU WAMEFANYA DHAMBI, NA KUMKUFURU MUNGU MIOYONI MWAO. NDIVYO ALIVYOFANYA AYUBU SIKUZOTE”.

Umeona tabia ya Ayubu?.. alikuwa ni mtu wa kuiombea nyumba yake rehema.. Inapokuja hatari hakutaka aokoke peke yake..alitaka kuokoka na familia yake..

Na mtu wa mwisho tunayeweza kumtazama ni Nabii Danieli, huyu maandiko hayajasema kama alioa au hakuoa!.. Lakini tabia ile ile ya kuwajali watu wa jamii yake, hata kuwaombea kwa Mungu, ndiyo iliyokuwa ndani yake..mpaka Mungu akaghairi mabaya juu ya watu wake Israeli kutokana na maombi ya Danieli. Na maandiko yanamtaja Danieli kama mtu aliyependwa sana na Mungu!..

Danieli 9:20 “Basi hapo nilipokuwa nikisema, na kuomba, na kuiungama dhambi yangu, NA DHAMBI YA WATU WANGU ISRAELI, na kuomba dua yangu mbele za Bwana, Mungu wangu, kwa ajili ya mlima mtakatifu wa Mungu wangu;

21 naam, nilipokuwa nikinena katika kuomba, mtu yule, Gabrieli, niliyemwona katika njozi hapo kwanza, akirushwa upesi, alinigusa panapo wakati wa dhabihu ya jioni.

22 Akaniagiza, akaongea nami, akasema, Ee Danielii, nimetokea sasa, ili nikupe akili upate kufahamu.

23 Mwanzo wa maombi yako ilitolewa amri, nami nimekuja kukupasha habari; maana wewe UNAPENDWA SANA; basi itafakari habari hii, na kuyafahamu maono haya.

24 Muda wa majuma sabini UMEAMRIWA JUU YA WATU WAKO, na juu ya mji wako mtakatifu, ili kukomesha makosa, na kuishiliza dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili ya uovu, na kuleta haki ya milele, na kutia muhuri maono na unabii, na kumtia mafuta yeye aliye mtakatifu”.

Kama ukisoma sala hiyo kuanzia juu kidogo (mstari wa kwanza), utaona jinsi Danieli alivyokuwa akiomba dua kwaajili ya watu wake(Yaani waisraeli wenzake walio katika hali ya utumwa huko Babeli). Na alipomaliza kuomba kwaajili yake na Watu wake, hapo katika mstari wa 24, maandiko yanasema Malaika Gabrieli alimjia na kumpa maneno ya faraja juu ya WATU WAKE ANAOWAOMBEA , ili kukomesha makosa, kuishiliza dhambi na kufanya upatatisho n.k

Ni jambo gani tunajifunza kwa watu hawa watatu?

Jambo kuu tunaloweza kujifunza kutoka kwa hawa watatu ni ile hali ya kujali wengine!… Wanaona itawafaidia nini wao kupata raha na kuokoka, na ilihali familia zao zinapotea?, ndugu zao wanapotea?..!.. wakaona hawana budi kutafuta njia yoyote ya watu wao kuwaokoa ndugu zao, haijalishi wanaonekana bado ni waovu mbele za Mungu!.. Ndio maana unaona Nuhu alijenga safina na akapona na wanawe watatu!, kadhalika Ayubu alikuwa anawaombea wanawe kila siku kwa kuwatolea dhabihu, kwasababu alihisi pengine wanawe wanaweza kuwa wamemuudhi Bwana mahali fulani katika maisha yao, hivyo aliuchukua mzigo wao.

Na wa mwisho ni Danieli, aliona hana sababu ya yeye kujifurahisha kwenye nyumba ya kifalme na ilihali watu wake wapo katika hali ya kukataliwa na Mungu, hivyo akachukua jukumu la kufunga na kuomba kwaajili ya watu wake.

Ndugu tabia ya kujali uzima wa wengine, inaweza kudharaulika leo lakini ni jambo la heshima kubwa sana mbele za Mungu, Mungu ameweka kumbumbu la hawa watatu zaidi ya manabii wengine wote kutokana na tabia yao hiyo, kwa tabia hiyo ndio iliyomfanya Bwana awatukuze watu hawa watatu zaidi ya wengine wote.

Inawezekana leo umempokea Yesu, lakini ndani ya moyo wako, huna mzigo wa wengine kuwa kama wewe!.. Ni jambo baya sana…Inawezekana umeokoka, lakini moyoni mwako huna mzigo na Baba yako au mama yako ambaye bado hajaokoka kama wewe, Au huna mzigo na rafiki yako au ndugu yako ambaye bado yupo katika ulimwengu, au unaserebuka mtu fulani anapokufa bila kuokoka!

Fahamu kuwa tuna wajibu wa kuokoka sisi na vile vile kuwafikishia wengine wokovu.. kama sisi tulivyoupokea..ni lazima tuwe sababu ya wokovu kwa watu wengine..Ndivyo tutakavyompendeza Bwana na kukaa katika kumbukumbu lake daima.

Bwana atujalie tuweze kuyatenda mapenzi yake.

Maran atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

VITABU VYA BIBLIA: Sehemu ya 9 (Kitabu cha Ayubu).

HUTATAMBUA LOLOTE, SIKU YA UNYAKUO IKIFIKA.

NI LIPI KATI YA MAKUNDI HAYA, WEWE UPO?

KWANINI MIMI?

Neno “Via” linamaanisha nini katika biblia?

Nyumbani:

Print this post

IEPUKE GHADHABU YA MUNGU.

Tofauti na inavyoaminika na wengi kuwa hasira ya Mungu au ghadhabu ya Mungu, inakuja au inachochewa sana na watu waliomwacha Mungu, wa ulimwengu huu, yaani watu ambao hawajamwamini Mwokozi Yesu.

Hiyo ni kweli kabisa, lakini nataka nikuambia kuwa hiyo haichangii pakubwa kuimwaga ghadhabu ya Mungu ulimwenguni.

Jambo kubwa linaloleta ghadhabu ya Mungu ulimwenguni ni maovu katikati ya watu wa Mungu, pamoja na ndani ya nyumba ya Mungu. Kikawaida mtu asiyekujua akikutusi, au akikudhalilisha jambo lile haliwezi kuugusa moyo wako sana, kama ukitukanwa au kudhalilishwa na mtu unayemjua, au uliye na mahusiano naye ya karibu sana.

Yule uliye na mahusiano naye ya karibu ndiye anayeweza kukuudhi sana na kukufurahisha sana, tofauti na mtu mwingine ambaye hamna mahusiano yoyote au hata hamjuani.

Ndivyo hivyo hivyo na Mungu wetu, watu wanaompendeza sana ni watu wale alio na mahusiani nao maana yake watu waliookoka, na wala si watu wa ulimwengu huu ambao hawamjui Mungu.. kadhalika watu wanaomuudhi sana, ni watu waliookoka ambao hawajasimama sawasawa. Hao ndio wanaomhuzunisha sana na wanaougusa moyo wake kwa maovu yao zaidi ya watu wale ambao hawajaokoka kabisa na wanatenda mabaya.

Maana yake ni kwamba mtu anayesema ameokoka na huku ni mzinzi, au mtukanaji, au muuaji.. Huyo anamhuzunisha Mungu na kumuudhi mara nyingi zaidi ya Yule ambaye hamjui Mungu kabisa na ambaye hajaokoka. Mtu ambaye hajaokoka kabisa na yupo katika ulimwengu, na anafanya maasi, ni kweli anamhuzunisha Mungu lakini si kwa kiwango kile cha mtu aliye katika mahusiano na Mungu, na wakati huo huo anafanya maasi.

Ni muhimu sana kulijua hili ili tuweze kuchukua tahadhari, na kuacha kunyoosha vidole kwa watu waovu wasiomjua Mungu, ilihali sisi wenyewe tuliomjua Mungu hatujajiweka sawa ipasavyo.

Wewe uliyeokoka utasema unazini mara moja tu kwa mwezi au kwa mwaka, na kufikiri moyoni mwako kuwa una heri sana kuliko Yule kahaba unayeona anajiuza kila siku ambaye hamtaki Mungu na hajaokoka kabisa.

Nataka nikuambie wewe uliyeokoka unayezini mara moja kwa mwezi au mara moja kwa mwaka ndiye mwenye dhambi kubwa kuliko Yule kahaba anayezini kila siku ambaye hajaokoka!.. Wewe ndiye unayemhuzunisha Mungu sana kuliko Yule kahaba..

Wewe unayesema umeokoka na kulewa mara moja kwa mwezi, ndiye unayeichochea ghadhabu ya Mungu kuja ulimwenguni zaidi hata ya Yule mlevi, anayeshinda bar kila siku na huku hajaokoka kabisa.

Wewe unayejiita umeokoka na huku unatazama picha za utupu mitandaoni na unajichua, mara moja kwa mwezi ndiye unayefanya dhambi kubwa kuliko Yule ambaye hajamjui Mungu kabisa na anafanya mambo hayo kila siku.

Sasa hivi utatazama mataifa mengine, watu wanatembea uchi barabarani, watu wanamtukana Mungu.. na moyoni ukadhani una heri wewe ambaye humtukani Mungu lakini unatukana mara moja moja.. Nataka nikuambie ndugu, hao wamemkataa Mungu tangu zamani, na Mungu alishawaacha sawasawa na (wafuate tamaa zao), hivyo wanayo hukumu yao inayokuja kama hawatatubu..Lakini wewe unayejua kila kitu, ambaye umeshaanza mahusiano na Mungu, na unafanya mambo kama hayo, hata kama ni siku moja moja.. jua kuwa wewe ndiye unayeichochoa hasira ya Mungu.

Hivyo ndugu kumbuka siku zote, Maasi katikati ya  watu wa Mungu ndio yanayoleta ghadhabu ya Mungu zaidi ya wale walio nje ya Imani.

Hivyo ni wajibu wetu, kujitakasa zaidi, nyakati hizi za siku za mwisho.. wala tusijilinganishe na watu walio nje!.. na kufikiri kuwa makosa yao Mungu anayafananisha na yetu. Ni wakati wa kuukataa uvuguvugu wote na kutafuta kuwa moto katika Imani.

Ufunuo 3:14 “Haya ndiyo anenayo yeye aliye Amina, Shahidi aliye mwaminifu na wa kweli, mwanzo wa kuumba kwa Mungu.

15 Nayajua matendo yako, ya kuwa hu baridi wala hu moto; ingekuwa heri kama ungekuwa baridi au moto.

16 Basi, kwa sababu una uvuguvugu, wala hu baridi wala moto, nitakutapika utoke katika kinywa changu”.

Bwana akubariki.

Kumbuka pia ule mwisho umekaribia sana, na parapanda ya mwisho ipo karibuni kulia.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

“Shinikizo” ni nini kibiblia, Na maana yake rohoni ni ipi?

Je watu ambao hawajasikia kabisa injili watahukumiwa?

MATARAJIO YA KILA MWANADAMU DUNIANI NI YAPI?

INJILI YA MANENO LAINI ITAKUGHARIMU.

Rudi nyumbani

Print this post

KIFAHAMU KIGEZO  CHA KUSAMEHEWA NA MUNGU.

Shalom nakusalimu katika jina kuu la Bwana wetu Yesu Kristo. Leo nataka tujifunze jambo la muhimu sana ambalo Bwana anataka tufahamu tunapokwenda mbele zake hususani katika kumwomba msamaha au rehema..hili ni jambo la muhimu sana..naomba usome hadi mwisho.

Kwa kawaida hakuna mtu asiyemkosea Mungu..hata kama hutamkosea kwa dhambi ya moja kwa moja zipo dhambi nyingine ndogo ndogo  ambazo si rahisi kuzitambua kwa haraka..kwamfano unaweza kumkwaza jirani yako kwa kauli fulani.ambayo pengine wewe uliiona ni sawa tu, lakini kumbe hujui tayari ulishatenda dhambi mbele za Mungu, kumfanya mwenzako ajisikie vibaya…na ndio maana maisha ya toba ni ya muhimu sana kwa mkristo yeyote..

Sasa jambo ambalo wengi hatujui ni kuwa msamaha wa Mungu unayo masharti yake..huwa hauji hivi hivi tu kama unavyodhani..Na leo tutaona ni kwanini..

Embu kaa chini uitafakari kwa makini ile sala ya Bwana..ukisoma pale vizuri utaona wanafunzi wake walipomwomba awafundishe kuomba hakusita kuwafundisha, mwanzoni alianza kwa kuwaambia vipengele vya kuombea, bila masharti au vigezo vyovyote ..kwamfano aliposema “utupe leo riziki zetu hakutoa” sababu yake mbele kwanini iwe hivyo..hakusema kwa kuwa na sisi tunawapa wengine riziki zetu..hapana..bali alisema tuombe tu hivyo hivyo na Mungu atatugawia..vilevile aliposema “usitutie majaribu” hakusema kwasababu na sisi hatuwatii watu wengine majaribuni hapana..alisema tuombe tu hivyo hivyo inatosha na yeye mwenyewe atatuepusha na majaribu yote…

Lakini alipofikia kipengele cha Utusamehe makosa yetu..utaona hapo hapo alitoa na sababu ya kwanini sisi tusamehewe..na sababu yenyewe ni kwasababu na sisi tunawasamehe waliotukosea makosa yetu..

Hapo ndipo Mungu anapataka kila mmoja wetu ajue na aliweke hilo akilini kwamba hayo mawili yanakwenda sambamba..hapo hamvumilii mtu yeyote..na ndio maana kayaambatanisha yote mawili  kwa pamoja.

Tusome..

Mathayo 6:9 “Basi ninyi salini hivi; Baba yetu uliye mbinguni, Jina lako litukuzwe, Ufalme wako uje,

10 Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.

11 Utupe leo riziki yetu.

12 Utusamehe deni zetu, kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu.

13 Na usitutie majaribuni, lakini utuokoe na yule mwovu. [Kwa kuwa ufalme ni wako, na nguvu, na utukufu, hata milele. Amina.]

14 Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi.

15 Bali msipowasamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu”.

Umeona bado huko mwishoni kabisa Kristo analiwekea tena msisitizo neno lile lile alilolisema katika hiyo sala..kwamba Mungu anasamehe tu pale tunaposamehe..ndugu Mungu anaweza kukupa kila kitu unachomwomba hata kama wewe huwapi  wengine hivyo vitu…anaweza kukufanyia jambo lolote lile utakalo hata kama huwafanyii wengine hayo..unaweza ukawa mchoyo wa kupindukia na mbinafsi kwelikweli hutaki kuwapa watu vyakula vyako vinaozea huko ghalani..lakini ukamwomba Mungu akupe nafaka nyingi zaidi na akakupa tena tele mpaka ukakosa pa kuweka.

Lakini kwenye suala la kumwomba msamaha kama hutamsamehe ndugu yako aliyekukosea..hutamsamehe mke wako/mume wako aliyekuvunja moyo au kukusaliti ..sahau Mungu kukusamehe na wewe makosa yako..hiyo ondoa akilini kumbuka Mungu yupo makini (STRICT) sana na neno lake…akisema amesema..usijidanganye wala usidanganywe na mtu..huna msamaha wowote wa dhambi zako zote zilizokutangulia wala unazozitenda leo hii..

Ukifa leo ni moja kwa moja kuzimu..hakuna mzaha hapo..Na ndio maana jambo la KUSAMEHE linapaswa liwe ni sehemu ya maisha yetu ya kila siku. Haijalishi amekuudhi kiasi gani, amekutukana mara ngapi..kama bado una vinyongo vya tokea mwaka juzi, hutaki kuachilia na bado unaona okay..utakufa vibaya sana Ndugu ukiendelea hivyo, haijalishi utasema umeokoka. Dhambi hii imewashusha wengi kuzimu. Ni wengi kweli kweli kwasababu neno msahama kwao ni gumu lakini bado wanawataka na wenyewe wasamehewe na Mungu.

Bwana atutie nguvu. Tujifunze kusamehe Tutembee katika kanuni zake.Ili tuishi kwa amani hapa duniani, tuikwepe hukumu ya Mungu.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

SAMEHE KUTOKA NDANI YA MOYO WAKO.

Je! Kuna dhambi kubwa na ndogo, na kama hakuna je! Mtu aliyeua na aliyetukana je watapata adhabu sawa?

NI KIPI KINAMZUIA MUNGU KUZUNGUMZA NA SISI?

SISI NI WINDO BORA SANA, LA DHAMBI.

Kama Mungu ndiye kaumba kila kitu, je ni yeye huyo huyo ndiye aliyeumba dhambi pia?

Rudi nyumbani

Print this post

NI KIPI KINAMZUIA MUNGU KUZUNGUMZA NA SISI?

Jina la Bwana na mwokozi wetu Yesu Kristo libarikiwe, yapo mambo mengi yanayozuia Mungu kuzungumza na sisi katika maisha yetu, lakini leo tutalizungumzia jambo moja kuu linalosababisha Bwana apunguze kusema na sisi, au aache kusema na sisi kabisa.

Na jambo lenyewe ni tabia ya “KUJIFANYA HUJUI NA WAKATI UNAJUA”. Hii ni tabia moja iliyo ya hatari sana ambayo ina madhara makubwa sana kwa mtu. Unapojua jambo Fulani halafu unajifanya hujui, na wakati huo huo unakwenda kumuuliza Mungu, au kumwomba!, ni jambo linalosababisha Mungu kukaa kimya mbele yako.

Hebu tusome kisa kimoja katika biblia ambacho kitatusaidia kuelewa vyema..

Marko 11:27  “Wakafika Yerusalemu tena; hata alipokuwa akitembea hekaluni, walimwendea wakuu wa makuhani, na waandishi, na wazee,

28  wakamwambia, Ni kwa mamlaka gani unatenda mambo haya? Naye ni nani aliyekupa mamlaka hii uyatende haya?

29  Yesu akawaambia, Nitawauliza neno moja, nanyi mnijibu, kisha nitawaambia ni kwa mamlaka gani nayatenda haya.

30  Ubatizo wa Yohana ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu? Nijibuni.

31  Wakasemezana wao kwa wao, wakisema, Kama tukisema, Ulitoka mbinguni, atasema, Mbona, basi, hamkumwamini?

32  Ila tukisema, Ulitoka kwa wanadamu, waliogopa watu; maana watu wote walimwona Yohana kuwa nabii halisi.

33  Wakamjibu Yesu, wakasema, Hatujui. Yesu akawaambia, WALA MIMI SIWAAMBII NINYI NI KWA MAMLAKA GANI NAYATENDA HAYA”

Nataka tuangalie hicho kipengele cha mwisho, Bwana anakataa kuwaambia ni kwa mamlaka gani anatenda hayo.

Sasa swali la kujiuliza ni kwanini alikataa kuwaambia?.. Jibu ni rahisi, ni kwasababu walikuwa wanaujua ukweli lakini wakawa wanajifanya hawajui!.. Walikuwa wanajua kabisa Yohana alitumwa na Mungu, lakini wanajifanya hawajui katumwa na nani?. Hiyo ni tabia moja mbaya sana, ambayo hata sasa inaendelea katika roho.

Watu wengi wanayajua maandiko na ukweli wote, lakini hawataki kufanya au kutenda kama maandiko yanavyosema, na wakati huo huo wanakwenda kumwuliza Bwana na kumwomba katika maombi!..pasipo kujua kuwa wapo katika hatari ya kutokujibiwa chochote!..

Wanajua kabisa miili yao ni hekalu la Roho Mtakatifu, na kwamba hawapaswi kuiharibu wala kuichafua kwa vyovyote vile, lakini bado wanaiharibu kwa uzinzi, kwa uvaaji mbaya, kwa ulevi,  kwa uchoraji tattoo n.k.. Na wakati huo huo wanakwenda mbele za Bwana kuuliza, au kuomba uthibitisho!..Mwisho wa siku, kunakuwa hakuna majibu yoyote kwa walichokitazamia.

Ndugu dada au kaka, kama kuna kitu kimeandikwa katika maandiko, ambacho kipo wazi kabisa na ni cha moja kwa moja, huna haja ya kwenda kutafuta uthibitisho wa jambo hilo kwa maombi..hutajibiwa chochote!, utaishia kuomba kila siku na kurudia na kurudia, hutapata majibu yoyote!.. zaidi sana unaweza kujikuta unafungua mlango wa kuvamiwa na maroho yadanganyayo! Kwasababu umelikataa Neno la Mungu lililo wazi unakwenda kutafuta maono.. Siku zote fahamu kuwa Neno la Mungu(yaani biblia takatifu) ndio sauti ya Mungu, iliyo dhahiri na iliyowazi mbele yetu..

Kwamfano maandiko yanaposema..

1Wakorintho 6:9  “Au hamjui ya kuwa wadhalimu hawataurithi ufalme wa Mungu? Msidanganyike; waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, wala waabudu sanamu, wala wazinzi, wala wafiraji, wala walawiti,

10  wala wevi, wala watamanio, wala walevi, wala watukanaji, wala wanyang’anyi”.

Hapo unahitaji ufunuo gani kuelewa hilo andiko??.. Inahitaji maombi gani ili uulewe!.. Unahitaji kufunga nini Mungu akufunulie kuwa ULEVI ni dhambi au uzinzi, au kuabudu sanamu?, na ilihali maandiko yanasema wazi kabisa hapo waabudu sanamu hawataurithi uzima wa milele?..Ukiwa na tabia hiyo kamwe hutamsikia Mungu akizungumza na wewe..

Bwana atusaidie tusiwe wanafiki mbele zake wala tusimjaribu.. Vile vile tulizingatie neno lake na kuliishi.

Maran atha!

Group la whatsapp jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Akawaambia Enendeni ulimwenguni mwote,MKAIHUBIRI INJILI KWA KILA KIUMBE.(Marko16:15.) Yesu Anamaanisha nini kusema MKAIHUBIRI INJILI KWA KILA KIUMBE?

TEGEMEA MUNGU KUZUNGUMZA NAWE KATIKA MAMBO MADOGO

Ni kwa namna gani malaika wa mbinguni wanaweza kutuhubiria sisi injili?

INJILI YA MANENO LAINI ITAKUGHARIMU.

Rudi nyumbani

Print this post

JE UMEJIANDAA KUTIMIZA UNABII UPI?

Kuna Nabii mbili zilizotabiriwa na Mungu zinazokuja mbele yetu,  Na nabii hizo ni KUOKOLEWA au KUHUKUMIWA. Wanadamu wote ni lazima waangukie katika mojawapo ya sehemu hizo mbili.

Lakini kabla ya yote kuna maswali machache ambayo tunaweza kujiuliza!,

Na maswali yenyewe ni haya; Je! Mungu anamchagua mtu kabla ya hata ya yeye kuzaliwa?, na je! Anajua kuwa huyo mtu hatma yake itakuwa ni ipi?, katika ziwa la moto au mbinguni?

Jibu ni kwamba Mungu anajua mambo yote, kwasababu ili awe Mungu ni lazima awe anajua kila kitu, na awe na upeo wa mbali sana kupita wetu na wa viumbe vyote, hivyo Mungu anamjua mtu kabla ya huyo mtu kuzaliwa, na anajua hatma yake kabla hata mtu huyo kuzaliwa..

Anajua kabisa  mwisho wake utakuwaje, kama ataokoka au atapotea!. Sisi wanadamu hatujui ni Mungu peke yake ndio anajua, na wala hakuna mtakatifu yoyote anayejua hatima ya mwanadamu mwenzake yeyote. Hiyo siri anajua yeye mwenyewe!.

Sasa swali sisi tutajijuaje kama tumekusudiwa uzima wa milele tangu asili (kwamba tutaokolewa), Tutakuja kuona mbeleni kidogo ni kwa namna gani tunaweza kujijua kama tutaokolewa au tutahukumiwa siku za mwisho..

Lakini kwanza hebu tutazame unabii wa watakaohukumiwa siku za mwisho…

Ufunuo 20:12 “Nikawaona wafu, wakubwa kwa wadogo, wamesimama mbele ya hicho kiti cha enzi; na vitabu vikafunguliwa; na kitabu kingine kikafunguliwa, ambacho ni cha uzima; na hao wafu wakahukumiwa katika mambo hayo yaliyoandikwa katika vile vitabu, sawasawa na matendo yao.

13  Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti na Kuzimu zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake. Wakahukumiwa kila mtu kwa kadiri ya matendo yake”.

Umeona hapo?.. Huo unabii ni lazima utimie kama ulivyo.. Mungu alishaliona kundi lote na anawajua wote watakaosimama hukumuni siku hiyo, na anawajua kwa majina kwamba watakuwa ni Fulani na fulani, na  Unabii huo ni lazima uje kutimia kama ulivyo.

Kadhalika upo unabii wa watakaookolewa siku za mwisho…

Ufunuo 7:9  “Baada ya hayo nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao”

Umeona na hapo pia? Wapo watu kutoka kila taifa, ambao wataokolewa, na Mungu anawajua wote watakaokolewa kwa majina na kwa sura… Lakini vile vile hajawataja!.. Maana yake hakuna mwanadamu yeyote aliyeambiwa na Mungu kuwa atakuwepo mbinguni siku za mwisho.

Sasa tutajijuaje kama tutakuwa miongoni mwa watakaokwenda mbinguni? Au watakaohukumiwa siku za mwisho..

Jibu ni rahisi, tutajua kama tutaokolewa siku ya mwisho kwa maisha tuanayoishi sasa… kama tunalitii Neno lake na kulifuata, maana yake kama tumetubu na kubatizwa na kumpokea Roho Mtakatifu na kuishi maisha ya utakatifu na ya kumpendeza yeye baada ya hapo, kama tutakaa na kuishikilia neema hiyo bila kuiachaia basi tuna uhakika wa kuwa miongoni mwa lile kundi kubwa la watakaokolewa.

Lakini kinyume chake kama tunaukataa wokovu leo, na kufa katika hali hii, basi tutakuwa miongoni mwa watakaotimiza unabii wa kuhukumiwa na kutupwa katika lile ziwa la moto siku za mwisho.

Hivyo uchaguzi ni wetu!.. kuchagua uzima wa milele au kuchagua mauti ya milele.

Yeremia 21:8 “Nawe waambie watu hawa, Bwana asema hivi, Tazama naweka MBELE YENU NJIA YA UZIMA, NA NJIA YA MAUTI”

Kumbukumbu 30: 15 “Angalia, nimekuwekea leo mbele yako uzima na mema, na mauti na mabaya”

Je! Umechagua unabii upi kuutimiza?

Bwana atubariki na kutujalia tuzidi kusogea kwake.

Group la whatsapp jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post

Ni kwa namna gani malaika wa mbinguni wanaweza kutuhubiria sisi injili?

SWALI: Naomba kufahamu Wagalatia 1:8 ina maana gani? Ni kwa namna gani malaika wa mbinguni wanaweza kutuhubiria sisi?


JIBU: Tusome,

Wagalatia 1:8 “Lakini ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe”.

Ni vizuri tukafahamu kwanza ni kwanini mtume Paulo alisema kauli kama hiyo. Alisema hivyo kutokana na kuzuka kwa makundi ya watu ambao walianza  kuhubiri injili nyingine tofauti na ile waliyokuwa wanaihubiri yenye kiini cha Yesu Kristo, na matokeo yake ikapelekea mpaka imani za watu wengi kupinduliwa, ambao tayari walikuwa wameshaijua njia ya kweli.

Na ndio maana mistari ya juu yake Paulo anasema..

Wagalatia 1:6 “Nastaajabu kwa kuwa mnamwacha upesi hivi yeye aliyewaita katika neema ya Kristo, na kugeukia injili ya namna nyingine.

7 Wala si nyingine; lakini wapo watu wawataabishao na kutaka kuigeuza injili ya Kristo”.

Unaona? na jambo la hatari zaidi ni kuwa watu hao waliowafundisha , walikuwa wanasema mambo hayo wamefunuliwa na Mungu mwenyewe, kwa kupitia maono ambayo waliletewa na malaika wa mbinguni.

Utalithibitisha pia  hilo katika.

Wakolosai 2:18 “Mtu asiwanyang’anye thawabu yenu, KWA KUNYENYEKEA KWA MAPENZI YAKE MWENYEWE TU, NA KUABUDU MALAIKA, AKIJITIA KATIKA MAONO YAKE NA KUJIVUNA BURE, KWA AKILI ZAKE ZA KIMWILI;

19 wala hakishiki Kichwa, ambacho kwa yeye mwili wote ukiruzukiwa na kuungamanishwa kwa viungo na mishipa, hukua kwa maongeo yatokayo kwa Mungu”.

Sasa kwa namna ya kawaida ni rahisi mtu kuamini pale anapoambiwa maono hayo au maagizo hayo, yameletwa na malaika. Ni rahisi kudhani agizo hilo ni la Mungu.

Mpaka baadaye taarifa hizo zikawafikia mitume, ndipo hapo sasa tunaona mtume Paulo, akitoa maneno makali kama hayo, na kusema, “ ijapokuwa sisi au malaika wa mbinguni atawahubiri ninyi injili yo yote isipokuwa hiyo tuliyowahubiri, na alaaniwe”.

Yaani akiwa na maana kuwa maono yoyote yanayosadikika yametoka mbinguni aidha kwa mkono wa malaika, au wa nabii au mitume wowote, lakini ni nje na mafundisho ya msingi ya mitume, basi na ALAANIWE.

Lakini kumbuka kauli hiyo haimaanishi kuwa malaika watakatifu wanaweza kuleta maono ambayo hayatokani na Mungu hapana, ni mapepo ndio yanayoweza kufanya hivyo. Isipokuwa tu  mtume Paulo hapo alikuwa anaweka msisitizo wa uhakika wa injili yao. Kwamba ni ya kweli na haiwezi kupinduliwa na kiumbe chochote kilicho juu mbinguni au kilicho chini duniani, kwasababu ni injili ya kweli ya Mungu mwenyezi.

Hata sasa, ndugu yangu wapo watu wanaoishi kwa maono na ndoto, wamelitupa kapuni Neno la Mungu, wapo tayari kutii kila wanachoambiwa au kusikia hata kama kinakwenda kinyume na Neno la Mungu. Kipindi hichi roho za udanganyifu zipo nyingi, na ndio maana tumeambiwa tusiziamini kila roho bali tuzipime kama zimetokana na Mungu au la!,(1Yohana 4:1 ). Utasikia mtu anasema Mungu amenifunulia,nikamwoe mke wa fulani au nikaongeze mke wa pili, na yeye bila kutathimini hayo maagizo kama yanaendana na Neno la Mungu, yeye anakwenda kufanya vile. Kumbe hajui kuwa tayari ameshapotea, anaishi katika uzinzi na siku ya mwisho atahukumiwa.

Hivyo tuwe makini sana, suluhisho pekee ni tudumu katika mafundisho ya mitume (Neno la Mungu), ndio tutakuwa salama daima. Usitishwe na maneno ya mtu yeyote anayekuambia malaika kanitokea au nimeonyeshwa maono. Lithibitishe kwanza katika Neno la Mungu. Kama linakinzana litupe kapuni, ishi kwa Neno.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Hamjui ya kuwa mtawahukumu malaika? Ina maana gani?

Nini maana ya kuabudu malaika? (Wakolosai 2:18)

Je! Kuna malaika wangapi mbinguni?

Ni kweli Paulo alipuuzia maonyo aliyopewa ya kwenda Yerusalemu?

Je! Watu ambao hawajawahi kusikia injili kabisa siku ya mwisho watahukumiwa?

Rudi nyumbani

Print this post

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 3)

Sasa kumbuka kama tulivyoona katika malaka zilizotangulia, huko nyuma kote baada ya Mungu kuiumba dunia, alichokuwa anafanya ni UKARABATI TU, lakini sio uumbaji mwingine. Lakini hatua hii ambayo ndio ya mwisho Mungu atafanya uumbaji mwingine. Na uumbaji huu sio kwamba ataiondoa dunia yote, na kuitupa motoni, kama wengi wanavyodhani hapana, bali atafanya kama vile atakavyofanya kwenye miili yetu mipya ya kimbinguni.

Sasa kama bado hujasoma sehemu ya kwanza na ya pili, basi bofya hapa chini upitie kwanza, ndipo uendelee na sehemu hii ya tatu na ya mwisho>>

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

Siku ile tutakapoenda mbinguni, Mungu atatushushia miili mipya isiyokuwa ya udongo, bali imetengenezwa kwa matirio ya kimbinguni. Na itakaposhushwa , hii miili ya sasa tuliyonayo haitauliwa na kutupwa motoni, hapana bali itavaliwa au itamezwa na ile mipya ya kimbinguni, biblia inasema hivyo katika.

1Wakorintho 15.51 “Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika,

52 kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika.

53 Maana sharti huu uharibikao uvae kutokuharibika, nao huu wa kufa uvae kutokufa.

54 Basi huu uharibikao utakapovaa kutokuharibika, na huu wa kufa utakapovaa kutokufa, hapo ndipo litakapokuwa lile neno lililoandikwa, Mauti imemezwa kwa kushinda.

55 Ku wapi, Ewe mauti, kushinda kwako? U wapi, Ewe mauti, uchungu wako?”.

Umeona hapo, ndivyo itakavyokuwa pia juu ya mbingu mpya na nchi mpya. Sio kwamba dunia yetu, itaangamizwa kabisa iondolewe hapana, bali ITAGEUZWA, na kuwa DUNIA ya ajabu sana, ambayo mfano wake hauwezi kuelezeka, hauwezi kulinganishwa hata kwa chembe na ulimwengu huu wa sasa. Utukufu wake, utakuwa ni wa mbali sana sana sana, tena sana.

Vivyo hivyo na hizi mbingu zilizo juu yetu yaani (sayari, nyota, magimba n.k.) Vitakuwa na mwonekano mwingine tofauti kabisa, vitaanza kuwa na uhai navyo.

Ukisoma Ufunuo 21&22 yote Biblia inatoa tabia za hiyo mbingu mpya na nchi mpya jinsi zitakavyokuwa, nazo ni hizi;

  • Hakutakuwa na Bahari
  • Hakutakuwa na kilio
  • Hakutakuwa na maombolezo
  • Hakutakuwa na laana
  • Hakutakuwa na maumivu
  • Hakutakuwa na kifo
  • Hakutakuwa na Usiku.

Pia ile Yerusalemu mpya, (mji wa kimbinguni), ndio utashuka juu ya hii nchi mpya na mbingu mpya. Mji ambao utakuwa ni kitovu cha ulimwengu, ambao ni bibi-arusi tu na Kristo ndio watakaouingia.

Zaidi ya yote, ni kuwa Mungu atahamisha maskani yake, na kuileta duniani. Kwa mara ya kwanza mwanadamu ataishi na Mungu, na kuuona uso wake.

Ufunuo 21:3 “Nikasikia sauti kubwa kutoka katika kile kiti cha enzi ikisema, Tazama, maskani ya Mungu ni pamoja na wanadamu, naye atafanya maskani yake pamoja nao, nao watakuwa watu wake. Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao”.

Vilevile Muda utaondolewa, hakutakuwa tena na kitu kinachoitwa muda, kwani tutaishi Milele na milele na milele isiyokuwa na mwisho. Katika furaha na amani na vicheko daima.

Hakika ni mambo ambayo hayaelezeki, yaani tutamfurahia Mungu kila inapoitwa leo. Hizi sayari zote zisizohesabika mabilioni kwa mabilioni huko angani zitakuwa na kazi nyingi sana, hazikuumbwa ziwe ukiwa, hatuwezi kufahamu kila kitu lakini tukifika huko ndipo tutajua.

Bwana Yesu alimalizia na kusema maneno haya;

Ufunuo 22:12 “Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.

13 Mimi ni Alfa na Omega, mwanzo na mwisho, wa kwanza na wa mwisho.

14 Heri wazifuao nguo zao, wawe na amri kuuendea huo mti wa uzima, na kuingia mjini kwa milango yake”.

Ndugu yangu, kumbuka ili kufika huko, maandalizi yake yanaanza sasa. Inasikitisha kuona kuwa wapo watu ambao hawatafika huko, Ikiwa leo hii tunaishi maisha ya ukristo vuguvugu, tunasema tumeokoka lakini ulimwengu umejaa ndani yetu. Tunatazamia vipi, tuende mbinguni kwenye unyakuo?. Au tunatazamia vipi tuingie Yerusalemu mpya.

Hizi ni nyakati ambazo, si za kubembelezewa tena wokovu, ni wewe mwenyewe tu kuona, jinsi hali halisi ilivyo. Hakuna dalili ambayo haijatimia. Siku yoyote, unyakuo utapita, na dhiki kuu itaanza.

Ikiwa hujaokoka, embu leo fanya uamuzi sahihi, Tubu dhambi zako kwa kumaanisha kabisa kugeuka, kisha, nenda kabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO, sawasawa na Matendo 2:38, Kisha Bwana mwenyewe atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu, 

Ukikamilisha hizo hatua zote, basi ujue tayari wewe ni mwana wa ufalme, jukumu lako litakuwa ni kuutuzwa wokovu wako kwa maisha ya utakatifu na ya kumcha Mungu na ya ibada ya kweli utakayokuwa unayaishi. Ukisubiria unyakuo, na zaidi hiyo mbingu mpya na nchi mpya itakayokuja huko mbeleni.

Lakini ikiwa utahitaji msaada wa kuokoka, au kubatizwa, au swali basi wasiliana nasi kwa namba zetu hizi kwa msaada zaidi. +255693036618/ +255789001312

Bwana akubariki sana.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

MKESHA WA KUINGIA MWAKA MPYA KILA MWAKA NI WA KUUTHAMINI SANA.

UNYAKUO.

UFUNUO: Mlango wa 1

Rudi nyumbani

Print this post

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

Sasa kama tulivyotangulia kuona katika sehemu ya kwanza kuwa hii dunia yetu ilipoumbwa, ilipitia uharibifu wa mara kwa mara, na baadaye kukarabatiwa  tena na sasa imesaliwa na uharibifu mmoja wa mwisho ambao  utakuja ulimwenguni hivi karibuni, na uharibifu wenyewe hautakuwa wa maji tena, bali wa moto. (2Petro 3:6-7)

Kwahiyo Mungu atakapomaliza kuuharibifu huu ulimwengu na kuwaondoa waovu wote, ataikarabati hii dunia na kuirejeshea utukufu wake kwa ilivyokuwa pale Edeni.  Na sababu ya Mungu kufanya hivyo, ili kuruhusu YESU KRISTO kuja kutawala hapa duniani pamoja na watakatifu wake, kama Mfalme wa Wafalme, na Bwana wa Mabwana kwa kipindi cha  miaka elfu moja (1000).

Wakati huo dunia itakuwa yenye amani tele, watu wataanza kuishi umri mrefu kama mwanzo, biblia inasema, mtu atakayekuwa na umri wa miaka 100 ataitwa bado mtoto mchanga,

Isaya 65:20 “Hatakuwapo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa”.

Watu watakuwa wakipanda na kujengwa wala hakuna atakayekuja kuharibu, au kuong’oa mazao yao. Wanyama wote watakuwa wapole, simba atakula majani, na mtoto atacheza kwenye tundu la nyoka na asidhuriwe kwa lolote (Isaya 65:21:25).

Lakini pamoja na hayo, biblia inarekodi pia watu waovu watakuwepo, ila dhambi haitatawala kwasababu shetani wakati huo atakuwa amefungwa, mtu akiasi kwa namna yoyote ile atauliwa,

Hivyo kwa ujumla ni kuwa utakuwa ni utawala wa amani nyingi sana, ni kipindi ambacho Mungu amewahifadhia watakatifu wake kuwafurahisha na kuwapa raha. Mimi na wewe tusikose hiyo sabato kuu ya Mungu ya utawala huo wa miaka 1000.

kwa urefu wa somo hilo la utawala wa miaka elfu, fungua hii link >>https://wingulamashahidi.org/2019/05/30/utawala-wa-miaka-1000/ 

Sasa mara baada ya utawala huo kupita, biblia inasema tena, shetani atafunguliwa kwa kipindi kifupi sana, kuwajaribifu wale waovu waliokuwa ndani ya dunia hiyo. Watakapo jaribu kuizunguka kambi ya watakatifu, wakati huo huo moto utashuka na kuwaangamiza wote. Kisha watahukumiwa na kutupwa katika lile ziwa la moto

Ufunuo 20:7 “Na hiyo miaka elfu itakapokwisha, Shetani atafunguliwa, atoke kifungoni mwake;

8 naye atatoka kuwadanganya mataifa walio katika pembe nne za nchi, Gogu na Magogu, kuwakusanya kwa vita, ambao hesabu yao ni kama mchanga wa bahari.

9 Wakapanda juu ya upana wa nchi, wakaizingira kambi ya watakatifu, na mji huo uliopendwa. Moto ukashuka kutoka mbinguni, ukawala.

10 Na yule Ibilisi, mwenye kuwadanganya, akatupwa katika ziwa la moto na kiberiti, alimo yule mnyama na yule nabii wa uongo. Nao watateswa mchana na usiku hata milele na milele”.

Baada ya hapo, mpango wote wa ukarabatiji wa ulimwengu utakuwa umeisha, kinachofuata sasa hiyo ni mbingu mpya na nchi mpya, ambayo Mungu aliikusudia tangu zamani wanadamu waishi ndani yake.

Jambo ambalo ndio shabaha yetu kuu sisi watakatifu. Hiyo mbingu mpya na nchi mpya. Kama vile mtume Petro alivyosema katika.

2Petro 3:13 “Lakini, kama ilivyo ahadi yake, mnatazamia mbingu mpya na nchi mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.

14 Kwa hiyo, wapenzi, kwa kuwa mnatazamia mambo hayo, fanyeni bidii ili mwonekane katika amani kuwa hamna mawaa wala aibu mbele yake”.

Mpaka hapo utakuwa umeona jinsi Mungu alivyoiumba dunia yake, na kila ilipoharibiwa, baadaye aliiponya kwa sehemu au aliikarabati na kuirudisha kama mwanzo. Lakini hakuwahi kufanya uumbaji mwingine mpya, wa ulimwengu.

Hivyo fuatana nami katika sehemu ya Tatu na ya mwisho, ambayo inaelezea sasa, jinsi hiyo mbingu mpya na nchi mpya itakavyokuja kuwa.

Bofya chini kwa sehemu ya kwanza na ya tatu >>>

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 3)

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

YANAYOENDELEA SASA KATIKA MADHABAHU YA MUNGU ROHONI.

NITAFANYA YERUSALEMU KUWA JIWE LA KUWALEMEA .

UTAWALA WA MIAKA 1000.

Rudi nyumbani

Print this post

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 1)

Nakusalimu katika jina kuu sana lipitalo majina yote la Bwana wetu Yesu Kristo, Nakukaribisha katika kujifunza maneno ya uzima.  Na leo tutajifunza juu ya mbingu mpya na nchi mpya.

Hili ni moja ya maswali yanayoulizwa na watu wengi, Je! Hiyo mbingu mpya na Nchi mpya inayozungumziwa katika maandiko itakuwa wapi? Je ni mbinguni au duniani?. Na Je! Itakuwa ni hii hii dunia yetu au italetwa dunia nyingine na Mungu?. Ili kufahamu fuatana nami mpaka mwisho wa makala hizi.

Historia ya mbingu na nchi:

Sasa kabla hatujaenda kutazama juu ya mbingu mpya na nchi mpya, ni vizuri tukafahamu historia ya “mbingu na nchi” ilianzia wapi. Tukisoma kile kitabu cha Mwanzo, biblia inasema

Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi ..(Mwanzo 1:1)

Inaposema “mbingu” inamaanisha anga lote, yaani sayari, na nyota na magimba yote yanayoonekana juu. Na “Nchi” inamaanisha hii dunia yetu tunayoishi sisi wanadamu na viumbe vyote.

Sasa Mungu alipoiumba, ilikuwa ni kamilifu sana, yenye kupendeza, lakini baada ya muda Fulani kupita,ambao biblia haijaeleza ni kipindi cha muda gani, ilikuja kuharibiwa na kuwa UKIWA.  Ikiwa na maana hakukuwa na kiumbe chochote kinachoishi, au uhai wowote unaoendelea, ikabakia kuwa kama mojawapo ya sayari nyingine, isipokuwa tu, hii yetu ilisalia na maji.

Mwanzo 1:2 “Nayo nchi ilikuwa ukiwa, tena utupu, na giza lilikuwa juu ya uso wa vilindi vya maji; Roho ya Mungu ikatulia juu ya uso wa maji”.

Najua pengine unaweza ukawa na swali, Je! Umejuaje, kuwa dunia yetu, hapo mwanzo ilikuwa ni nzuri na kamilifu kabla ya Mungu kuanza kutuumba sisi. Jibu ni kuwa maandiko yanatuambia Mungu hajawahi kuiumba nchi na kuiacha katika hali ya ukiwa. Soma.

Isaya 45:18 “Maana Bwana, aliyeziumba mbingu, asema hivi; Yeye ni Mungu; ndiye aliyeiumba dunia na kuifanya; ndiye aliyeifanya imara; HAKUIUMBA UKIWA, aliiumba ili ikaliwe na watu; Mimi ni Bwana, wala hapana mwingine”.

Unaona hapo? Anasema, hakuiumba ukiwa, ikiwa na maana kuwa Mungu haachi kazi nusu nusu anaumba kikamilifu. Hivyo hiyo inatuonyesha kuwa kabla ya sisi wanadamu kuumbwa, Mungu alikuwa tayari kashaiumba dunia kamilifu na yenye uhai ndani yake, Lakini kukatokea jambo Fulani la uharibifu, ikapelekea Mungu kuiharibu dunia ile, Na hatuwezi kushangaa jambo kama hilo kusababishwa na shetani, na mapepo yake, kwasababu hao ndio waliokuwepo kabla ya sisi wanadamu kuumbwa. Lakini siri hiyo Mungu kaificha ni yeye mwenyewe ndiye anayejua yaliyokuwa yanaendelea huko nyuma.

Sasa wakati ulipofika wa sisi kuumbwa Mungu akaanza kuikarabati dunia tena. ndipo hapo  tunaona akasema na iwe mwanga ikawa mwanga, n.k. Mpaka ikiwa sehemu nzuri sana tena ya kutuvutia, lakini tunajua maisha yalipokuja kuendelea mbele Adamu akaasi, dhambi ikaingia, baadaye hali ikaendelea kuwa mbaya kupitiliza, hadi Mungu akaghahiri kuwaumba wanadamu, baadaye akasema nitawaangamiza wanadamu wote, watoke katika uso wa nchi.

Ndipo hapo akaleta kitu kinachoitwa gharika duniani, akaigharikisha dunia nzima. Akasalia Nuhu tu, na familia yake, jumla watu 8, dunia ikabakia ukiwa kama ilivyokuwa pale mwanzo.

Isaya 24:1 “Tazama, Bwana ameifanya dunia kuwa tupu, aifanya ukiwa, aipindua, na kuwatawanya wakaao ndani yake”.

Hivyo, dunia ya wakati ule ilipogharikishwa, haikukarabatiwa tena na Mungu kama alivyofanya pale mwanzo, badala yake aliyakausha maji tu, lakini uzuri mwingi wa mbingu na nchi ulipotea, jua likawa kali kuliko pale mwanzo, kwasababu maji yaliyokuwa juu ya anga yalipunguzwa, umri wa watu kuishi ukapungua sana, kutoka miaka elfu hadi miaka 120, Kama Mungu alivyosema.

Basi, baada ya hapo maisha yakaendelea tena kama kawaida, watu wakaongezeka , wakaijaza dunia, maasi yakarudi na kuongeza, tena hata zaidi ya kipindi kile cha Nuhu, Mungu akaanza kuwaonya wanadamu kwa vinywa vya manabii wake, akawaambia huu ulimwengu utakwenda kuangamizwa , kama ilivyokuwa kipindi kile cha gharika, lakini kuangamziwa kwake hakutakuwa kwa maji tena, bali kwa moto, ili kuifanya kuwa UKIWA tena.

Unaweza kusoma hilo katika vifungu hivyo katika mistari hii;

Isaya 13:9 “Tazama, siku ya Bwana inakuja, siku kali, ya hasira na ghadhabu kuu, ILI IIFANYE NCHI KUWA UKIWA, na kuwaharibu watu wake, wenye dhambi, wasikae ndani yake.

10 Maana nyota za mbinguni na matangamano havitatoa nuru yake; jua litatiwa giza wakati wa kucha kwake, na mwezi utaacha nuru yake isiangaze.

11 Nami nitaadhibu ulimwengu kwa sababu ya ubaya wake, na wenye dhambi kwa sababu ya hatia yao; nami nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao walio wakali;

12 nitafanya wanadamu kuadimika kuliko dhahabu safi, na watu kuliko dhahabu ya Ofiri.

13 Kwa hiyo nitazitetemesha mbingu, na dunia itatikiswa itoke katika mahali pake, kwa sababu ya ghadhabu ya Bwana wa majeshi, na kwa sababu ya siku ya hasira yake kali”.

Soma pia,

2Petro 3:6 “kwa hayo dunia ile ya wakati ule iligharikishwa na maji, ikaangamia.

7 Lakini MBINGU ZA SASA NA NCHI zimewekwa akiba kwa moto, kwa neno lilo hilo, zikilindwa hata siku ya hukumu, na ya kuangamia kwao wanadamu wasiomcha Mungu”.

Unaona? Zoezi lile lile la Mungu kuiharibu nchi, linaendelea, lilianza kabla ya sisi kuumbwa, likatokea tena wakati wa Nuhu, na litamalizia, na wakati wetu sisi tunaoishi. Kwahiyo kinachongojewa sasa ni Mungu kuwanyakua tu watakatifu wake, baada ya hapo, kitakachofuata ni uharibifu mkubwa sana wa huu ulimwengu.Ambao utakuwa ni wa kutisha sana, kwasababu, dunia itatikiswa kwa namna ambayo haijawahi kutokea, jua litatiwa giza, visiwa vitahama, waovu wote watakufa, watakaosalia watakawa ni wachache sana pengine watu 10 tu, katika dunia nzima, kwasababu moto usiokuwa wa kawaida utaipika hii dunia tena, ili kuifanya kuwa ukiwa kama pale mwanzo.

Ufunuo 16:17 “Na huyo wa saba akakimimina kitasa chake juu ya anga. Sauti kuu ikatoka katika hekalu, katika kile kiti cha enzi, ikisema, Imekwisha kuwa.

18 Pakawa na umeme na sauti na radi; na palikuwa na tetemeko la nchi kubwa, ambalo tangu wanadamu kuwako juu ya nchi hapakuwa namna ile, jinsi lilivyokuwa kubwa tetemeko hilo. Hii ndio siku ya kiama inayofamika na wengi.

19 Na mji ule mkuu ukagawanyikana mafungu matatu, na miji ya mataifa ikaanguka; na Babeli ule mkuu ukakumbukwa mbele za Mungu, kupewa kikombe cha mvinyo ya ghadhabu ya hasira yake.

20 Kila kisiwa kikakimbia, wala milima haikuonekana tena.

21 Na mvua ya mawe kubwa sana, ya mawe mazito kama talanta, ikashuka kutoka mbinguni juu ya wanadamu. Wanadamu wakamtukana Mungu kwa sababu ya lile pigo la mvua ya mawe; kwa maana pigo lake ni kubwa mno”.

Huu wakati unatisha sana, hatuwezi kueleza mambo yote, lakini kama utataka somo linalohusiana na hii siku ya Bwana itakavyokuwa basi bofya link hii>>>> https://wingulamashahidi.org/2018/07/17/siku-ya-bwana-inayotisha-yaja/

Msingi huu utatusaidia kufahamu agenda ya Mungu juu ya hii dunia yetu, na mpaka mwisho wake utakavyokuja kuwa.

Mpaka hapo tunaweza kuendelea  katika sehemu ya pili ya mbingu mpya na nchi mpya.. Hivyo kwa mwendelezo unaweza kubofya chini>>

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 2)

MBINGU MPYA NA NCHI MPYA. (Sehemu ya 3)

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

Je ni kweli siku ya mwisho dunia itakunjwa kama karatasi na kutupwa motoni?

Je! tunapaswa kukiamini Kitabu cha Henoko?

UFUNUO: Mlango wa 17

Rudi nyumbani

Print this post

WEKA KUMBUKUMBU YA MAMBO BWANA ANAYOKUFANYIA KWASABABU YATAKUFAA MBELENI.

Jina la Bwana wetu Yesu, libarikiwe.

Kuna umuhimu mkubwa sana wa kuweka kumbukumbu za mambo Bwana anayoyafanya katika maisha yako, kwasababu aidha zitakusaidia wewe mbeleni au zitawasaidia wengine. Kila tendo la kimiujiza Bwana analokufanyia liandike chini. Kwasababu zitakuja nyakati ambazo utaishiwa nguvu, na kama utakuwa huna kumbukumbu yoyote kichwani kwako itakuwa ni ngumu kushinda majaribu hayo..

Nguvu ya Daudi kumshinda Goliathi, si upako aliokuwa nao, wala si maono aliyoona wala ndoto aliyoota, bali ni uwezo wa kukumbuka mambo Mungu aliyomtendea wakati alipokutana na simba na dubu, walipokuwa wanavizia kondoo, Bwana alivyomsaidia akawaua, na alipoliweka hilo moyoni, ulipokuja wakati wa jaribu kubwa kama hilo la Goliathi, aliweza kukumbuka jinsi Bwana alivyomsaidia kuwaua wale hayawani wakali, na akamchukulia Goliathi kuwa naye pia atamwua kama alivyowaua wale wanyama.

1 Samweli 17:32 “Daudi akamwambia Sauli, Asizimie moyo mtu ye yote kwa ajili ya huyu; mimi mtumishi wako nitakwenda kupigana na Mfilisti huyu.

33 Sauli akamwambia Daudi, Huwezi wewe kumwendea Mfilisti huyu upigane naye; maana wewe u kijana tu; na huyu ni mtu wa vita tangu ujana wake.

34 Daudi akamwambia Sauli, Mtumishi wako alikuwa akichunga kondoo za baba yake, na alipokuwa akija simba, au dubu, akamkamata mwana-kondoo wa lile kundi,

35 mimi hutoka nikamfuata, nikampiga, nikampokonya kinywani mwake; na akinirukia, humshika ndevu zake, nikampiga, nikamwua.

36 Mtumishi wako alimwua simba na dubu pia; na huyu Mfilisti asiyetahiriwa atakuwa kama mmoja wao, kwa sababu amewatukana majeshi ya Mungu aliye hai.

37 Daudi akasema, Bwana aliyeniokoa na makucha ya simba, na makucha ya dubu, ataniokoa na mkono wa Mfilisti huyu. Sauli akamwambia Daudi, Enenda, na Bwana atakuwa pamoja nawe”

Umeona hapo?..Daudi alitumia tu USHUHUDA wa Dubu na Simba, kumwangusha Goliathi. Lakini hebu fikiri angekuwa ni mtu wa kusahau, matendo makuu ya Mungu, angepata wapi ujasiri wa kumsogelea Goliathi?.

Kwahiyo tunachoweza kujifunza ni kuwa Ushuhuda wa Daudi kuwaua Dubu na Simba, ulikuwa ni wa muhimu sana kwa nyakati zijazo.

Kadhalika yapo mambo mengi ya kimiujiza ujiza yanayoendelea kila siku katika maisha yetu, ambayo Bwana anayafanya, hatuna budi kuyahifadhi hayo, aidha kwa maandishi, au kama tunakumbukumbu nzuri basi tuyahifadhi mioyoni mwetu yasiweze kupotea.

Hebu tuangalie mfano mwingine wa mtu aliyetunza mambo makuu Mungu aliyoyafanya mbele ya macho yake, ambapo yakaja kuwa ya maana sana siku za mbeleni.

Na mtu huyo si mwingine zaidi ya Mariamu, mama yake YESU.

Asilimia kubwa ya habari tunazozisoma za kuzaliwa kwa Bwana Yesu, na matukio yaliyokuwa yanaendelea wakati wa kuzaliwa kwake, ni kutokana na Mariamu kuwasimulia watu, hakuna mwingine aliyekuwa na taarifa za kutosha kuhusu kuzaliwa kwa Yesu zaidi ya mama yake Mariamu.

Kwamfano habari za wale wachungaji makondeni tunazozisoma, Waandishi kama wakina Luka, Mathayo na Yohana hawakufunuliwa, bali walizipata kutoka kwa Mariamu, mama yake, kwani walikwenda kumuuliza ni nini kilikuwa kinaendelea wakati wa kuzaliwa kwake..Na Mariamu akawaeleza na ndio wakaandika habari hizo.. Hawakufunuliwa habari hizo na Roho Mtakatifu, wala hawakuona maono, hapana!, bali walihadithiwa na wakina Mariamu..

Luka mwenyewe anashuhudia hayo…

Luka 1:1 “Kwa kuwa watu wengi wametia mikono kutunga kwa taratibu habari za mambo yale yaliyotimizwa katikati yetu,

2  KAMA WALIVYOTUHADITHIA WALE WALIOKUWA MASHAHIDI WENYE KUYAONA, na watumishi wa lile neno tokea mwanzo,

3  nimeona vema mimi nami, kwa kuwa nimejitafutia usahihi wa mambo hayo yote tangu mwanzo, kukuandikia kwa taratibu, Theofilo mtukufu,”.

Umeona hapo?. Luka anasema “kama walivyotuhadithia”.. Maana yake ulipofika wakati wa kwenda kuandika habari za Bwana kiusahihi, waliwatafuta wakina Mariamu, na wengine wachache waliokuwepo wakati wa kuzaliwa kwake, wawasimulie yaliyokuwa yanajiri..

Sasa hebu tuchunguze zile habari za wachungaji makondeni Mwandishi Luka alizitolea wapi!..

Luka 2:8  “Na katika nchi ile ile walikuwako wachungaji wakikaa makondeni na kulinda kundi lao kwa zamu usiku.

9  Malaika wa Bwana akawatokea ghafula, utukufu wa Bwana ukawang’aria pande zote, wakaingiwa na hofu kuu.

10  Malaika akawaambia, Msiogope; kwa kuwa mimi ninawaletea habari njema ya furaha kuu itakayokuwa kwa watu wote;

11  maana leo katika mji wa Daudi amezaliwa, kwa ajili yenu, Mwokozi, ndiye Kristo Bwana.

12  Na hii ndiyo ishara kwenu; mtamkuta mtoto mchanga amevikwa nguo za kitoto, amelala katika hori ya kulia ng’ombe.

13  Mara walikuwapo pamoja na huyo malaika, wingi wa jeshi la mbinguni, wakimsifu Mungu, na kusema,

14  Atukuzwe Mungu juu mbinguni, Na duniani iwe amani kwa watu aliowaridhia.

15  Ikawa, malaika hao walipoondoka kwenda zao mbinguni, wale wachungaji waliambiana, Haya, na twendeni mpaka Bethlehemu, tukalione hilo lililofanyika, alilotujulisha Bwana.

16  Wakaenda kwa haraka wakamkuta Mariamu na Yusufu, na yule mtoto mchanga amelala horini.

17  Walipomwona wakatoa habari waliyoambiwa juu ya huyo mtoto.

18  wote waliosikia wakastaajabu kwa hayo waliyoambiwa na wachungaji.

19  LAKINI MARIAMU AKAYAWEKA MANENO HAYO YOTE, AKIYAFIKIRI MOYONI MWAKE.

20  Wale wachungaji wakarudi, huku wanamtukuza Mungu na kumsifu kwa mambo yote waliyosikia na kuyaona, kama walivyoambiwa”

Umeona hapo?, Mariamu aliyaweka hayo yote moyoni!, hakuyapuuzia tu na kuyaacha yapite!, bali aliyatunza, kwasababu alijua siku moja yatakuja kuwafaa wengine huko mbeleni, ambao ndio wakina Luka pamoja na sisi.

Kadhalika tuchunguze sehemu nyingine tena Mariamu, aliyoweka kumbukumbu ya maisha ya Mwokozi Yesu..

Luka 2:48 Na walipomwona walishangaa, na mama yake akamwambia, Mwanangu, mbona umetutenda hivi? Tazama, baba yako na mimi tulikuwa tukikutafuta kwa huzuni.

49  Akawaambia, Kwani kunitafuta? Hamkujua ya kuwa imenipasa kuwamo katika nyumba ya Baba yangu?

50  Nao hawakuelewa na neno hilo alilowaambia.

51  Akashuka pamoja nao mpaka Nazareti, naye alikuwa akiwatii; NA MAMAYE ALIYAWEKA HAYO YOTE MOYONI MWAKE.

52  Naye Yesu akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu”

Umeona na hapo?..Kama Mariamu asingeyaweka moyoni leo hii tusingejua kama Bwana alikuwa ni mtii kwa Mungu na kwa wanadamu. Na sio tu hayo bali na mengine yote tunayoyasoma yanayomhusu Bwana, ni kutokana na mtu, au watu Fulani kutunza kumbukumbu hizo.

Jambo ambalo limekuja kuwa Baraka kwetu sisi, watu wa vizazi vya baadaye..

Kadhalika na sisi hatuna budi kujifunza katika hayo, tutunze kumbukumbu za yote Bwana anayoyafanya kwetu, au kwa watoto wetu, au kwa jamii yetu, ili kumbukumbu hizo ziweze kuja kutusaidia katika nyakati za baadaye za majaribu, na ziweze pia kusaidia vizazi vingine vijavyo kama vitakuwepo.

Mithali 13:22 “Mtu mwema huwaachia wana wa wanawe urithi; Na mali ya mkosaji huwa akiba kwa mwenye haki”.

Bwana atubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Pia kama utapenda uwe unafikiwa na masomo ya kila siku kwa njia ya WHATSAPP basi bofya hapa ujiunge moja kwa moja  >>>> WHATSAPP


Mada Nyinginezo:

MAMA, TAZAMA, MWANAO.

Na ulimi laini huvunja mfupa.(Mithali 25:15)

SIKU YA HOFU YANGU NITAKUTUMAINI WEWE.

Hanithi ni nini katika biblia? (kumbukumbu 23:17)

Hapana hata mmoja aliyethubutu kuambatana nao;

HUYU MELKIZEDEKI NI NANI?

Rudi nyumbani

Print this post