Category Archive maswali na majibu

Kuna tofauti gani kati ya uso wa Bwana na macho ya Bwana?

Zaburi 34:15 Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao.  16 Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani.

JIBU: Andiko hili lilinukuliwa tena na mtume Petro katika 1Petro 3:12-13  linasema;

 “12 Kwa kuwa macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake husikiliza maombi yao; Bali uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya. 13  Naye ni nani atakayewadhuru, mkiwa wenye juhudi katika mema?

Kama tunavyojua Macho kazi yake ni kutazama, lakini uso, ni kueleza taswira ya mtu/ kitu fulani.

Na  kimsingi macho huona vyote, vilivyo vyema na vilivyo vibaya. Isipokuwa jicho lolote hupendelea zaidi kutazama vilivyo vyema zaidi ya vile vibaya. Ndivyo ilivyo kwa Mungu wetu pia, anaona yote, maandiko yanasema hivyo katika;

Mithali 15:3 “Macho ya Bwana yako kila mahali; Yakimchunguza mbaya na mwema”.

 lakini zaidi anaelekeza macho yake zaidi kwa walio wema ili awape mema.

Na ndio maana ya hiyo sehemu ya kwanza ya andiko hilo inayosema ‘Macho ya Bwana huwaelekea wenye haki, Na masikio yake hukielekea kilio chao’ Lakini haimaanishi kuwa macho yake pia hayawaoni watenda mabaya.

Vivyo hivyo katika sehemu ya pili inayoeleza juu ya Uso wa Bwana. Kama tulivyoona Uso kazi yake ni kueleza taswira ya mtu. Kwa mfano mtu akifurahi, au akiwa na huzuni au akiwa na hasira ni rahisi kumtambua kwa kuutazama uso wake. Na Vivyo hivyo, kwa Mungu wetu ukiitambua tabia yake, basi ni sawa na umeuona uso wake.

Sasa uso wake pia upo katika pande mbili; 1) Wa Rehema, 2) na wa Hasira (Nahumu 1:2-3)

Maana yake ni kuwa ukimtafuta Bwana, na kumpenda, utaona uso wake mwema, utaona upendo wake, utaona fadhili zake, utaona ukarimu wake, huruma yake, na rehema zake sikuzote. Na ndio maana maandiko yanatuasa tupende kuutafuta Uso wa Bwana. Ili tuujue uzuri wake.

Zaburi 105:4 ‘Mtakeni Bwana na nguvu zake, Utafuteni uso wake sikuzote’.

Zaburi 143:7 “Ee Bwana, unijibu hima, roho yangu imelegea; Usinifiche uso wako, Nisifanane nao washukao shimoni’

Lakini pia kinyume chake ni kweli ukiwa mwovu, ukiwa mkaidi, ukiwa mbaya, unajiandaa kuuna uso wa Mungu wenye ghadhabu,na hasira, na mapigo na matokeo yake utakumbana na adhabu kali kutoka kwake. Ndio hapo, anasema.

‘Uso wa Bwana ni juu ya watenda mabaya, Aliondoe kumbukumbu lao duniani’.

Hivyo kwa ufupisho ni kwamba jicho la Mungu linaona wote, waovu na wema, vilevile uso wa Bwana unawaelekea wote waovu na wema. Lakini katika vifungu hivyo, na vingine baadhi, vinapozungumzia macho ya Bwana huwa vinalenga sana sana kwa wema. Na vinaposema Uso wa Bwana, huwa vinalenga sana sana kwa  upande wa waovu.

Kwahiyo usichanganyikiwe, bali fahamu muktadha, wa habari hiyo katika sehemu husika. Ili ujue alimaanisha nini hapo, kwa msaada wa Roho wa Mungu. Kwasababu hutumika kotekote

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255789001312 au +255693036618

Mada Nyinginezo:

UNAVYOZIDI KUWA MWENYE HAKI, NDIVYO KUJITAMBUA KWAKO KUNAVYOPUNGUA.

ANDALIZI LA MWISHO LA UJIO WA MPINGA KRISTO.

JIFUNZE KUDUMU UWEPONI MWA MUNGU.

Biblia inaposema Kaini akatoka mbele za uso wa Bwana, Inamaana gani?

Ni kweli hakuna mtu aliyewahi kuuona uso wa Mungu Zaidi ya Bwana Yesu?

Je Paulo na Petro walishindania nini? (Wagalatia 2:11).

TABIA ZA NJIA YA MUNGU KWA MKRISTO

Rudi nyumbani

Print this post

Maziara ni nini? Je! Na Tunaruhusiwa kuyajenga kwenye makaburi yetu?

Kwa utamaduni wa sasa mtu anapokufa, huwa anafukiwa chini ardhini, na juu huwekewa  kiashirio Fulani cha kawaida kuonesha eneo hilo lipo kaburi. Lakini  watu wengine hupenda kuyapa thamani makaburi ya watu wao, hivyo kwa juu hujengea, kichumba Fulani kinachopambwa kwa vito au mawe ya thamani , wengine wanaweka mnara Fulani n.k. Sasa vitu hivi vyote vinavyojengewa juu ndio huitwa Maziara.

Kwamfano katika picha hii, ni mfano wa Ziara ambalo lilijengwa na wenyeji wa Marekani kama kumuenzi raisi wao wa kwanza wa taifa hilo aliyeitwa George Washington.

Hata katika agano la kale, enzi za biblia, yapo makaburi yaliyokuwa ya kawaida, lakini pia yapo yaliyokuwa yamejengewa maziara. Na hayo yalikuwa hususani ya wafalme na manabii wakubwa waliotokea Israeli, ambao waliuliwa kikatili mfano wa hao  ni Zekaria, Hagai na Malaki.  Na waliohusika sana kutengeneza maziara haya walikuwa ni hawa waandishi na mafarisayo(Watu wa kidini). Wakidai kuwa wanawa-enzi manabii wao, lakini tunaona Yesu akiwakemea kwa dhambi ya unafki waliyokuwa wanaifanya kwa tendo hilo.

Tusome.

Mathayo 23:29  Ole wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnayajenga makaburi ya manabii, na kuyapamba maziara ya wenye haki, 30  na kusema, Kama sisi tungalikuwako zamani za baba zetu, hatungalishirikiana nao katika damu ya manabii. 31  Hivi mwajishuhudia wenyewe, ya kwamba ninyi ni wana wao waliowaua manabii. 32  Kijazeni basi kipimo cha baba zenu. 33  Enyi nyoka, wana wa majoka, mtaikimbiaje hukumu ya jehanum? 34  Kwa sababu hiyo, angalieni, mimi natuma kwenu manabii na wenye hekima na waandishi; na wengine wao ninyi mtawaua na kuwasulibisha, na wengine wao mtawapiga katika masinagogi yenu, na kuwafukuza mji kwa mji; 35  hivyo ije juu yenu damu yote ya haki iliyomwagika juu ya nchi, tangu damu ya Habili, yule mwenye haki, hata damu ya Zakaria bin Barakia, mliyemwua kati ya patakatifu na madhabahu. 36  Amin, nawaambieni, Mambo hayo yote yatakuja juu ya kizazi hiki.

Soma pia (Luka 11:47-48).

Swali ni je! Walikuwa wanafanya makosa kutenda jambo lile?

Jibu ni hapana, Bali walichokuwa wanakifanya nje, hakikuendana na kile kilichokuwa mioyoni mwao na ndio maana akawaita wanafiki. Kwasababu walikuwepo pia manabii wa Mungu na watu wenye haki wakati wao, mfano wa Yohana, pamoja na yeye mwenyewe lakini walikuwa wanataka kuwaua. Na ndivyo walivyokuja kufanya kwa Bwana, pamoja na mitume wako na watakatifu wa kanisa la kwanza kama vile wakina Stefano.

Je! Sisi tujengapo maziara kama heshima  kwa wafu wetu tunatenda dhambi?

Jibu ni la, Endapo tu hatutashirikisha ibada yoyote ya wafu mahali pale. Lakini kama ni kwa kumbukumbu, au kumu-enzi marehemu wako, hakuna shida kuweka ziara (kupamba kaburi lako kwa jinsi upendavyo). Lakini fahamu tu hilo halitakuongezea jambo lolote rohoni. Wala halimfaidii kwa lolote Yule marehemu kule alipo.

Je! Ni sawa kwa Mkristo kusafisha kaburi la mfiwa wako, na kufanya ibada mahali pale?

Kutunza kaburi lolote, yaani kulisafisha, kulirepea, kulipandia bustani, kulilinda.. Si kosa kibiblia, kwasababu tunaona katika biblia makaburi yalitunzwa kwa bustani, soma (Yohana 20:15), pia yalilindwa, Na zaidi yalihifadhiwa yasiharibiwe. Soma

2Wafalme 23:16 Naye Yosia alipogeuka, aliyaona makaburi yale yaliyokuwako huko, juu ya mlima; akatuma watu, akaitoa ile mifupa katika yale makaburi, akaiteketeza juu ya madhabahu, akainajisi, sawasawa na lile neno la Bwana, alilolinena yule mtu wa Mungu, aliyetamka mambo hayo.  17 Kisha akasema, Ni kumbukumbu la nani, hili ninaloliona? Na watu wa mji wakamwambia, Ni kaburi la yule mtu wa Mungu, aliyetoka Yuda, akayanena mambo hayo uliyoyatenda wewe juu ya madhabahu ya Betheli.  18 Akasema, Mwacheni; mtu awaye yote asiiondoe mifupa yake. Basi wakaiacha mifupa yake, pamoja na mifupa ya yule nabii aliyetoka Samaria.

Hivyo, upendapo kutunza kaburi la mpendwa wako, aliyefariki hufanyi kosa.

Vipi katika kufanya ibada?

Zipo ibada za wafu, ambazo ndizo zinazofanyika mara nyingi katika makaburi ya marehemu, ibadani hizo, zinahusianisha kuwaombea wafu hao, n.k. Ibada hizi ni za kipagani, na mkristo hapaswi kuzifanya ni  ibada za miungu. Au wengine wanakwenda kuzungumza na kaburi wakiamini Yule mtu yupo pale makaburini anawasikia. Huo ni uchawi.

Hivyo hakuna mahusiano yoyote ya kiibada katika makaburi. Endapo imetokea unakwenda kufanya maziara (yaani kukarabati au kupamba), basi unachofanya ni kufungua kwa maombi na kufunga kwa maombi, kisha mnaendelea na kazi yenu, ili kutimiza hili andiko

Wakolosai 3:17  “Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye”.

Na kama mmeguswa kutafakari maneno ya Mungu mahali pale, kama mfanyapo sehemu nyingine zozote, mfano kazini, shuleni, chini ya mwembe n.k..  Basi iwe ni kwa Mungu na sio kwasababu ya makaburi. Epuka Ibada za wafu.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Pango la Makpela ni lipi, je lina umuhimu wowote kwetu?

MAKABURI YAKAFUNUKA; IKAINUKA MIILI MINGI YA WATAKATIFU WALIOLALA;

MAUTI NA KUZIMU ZIKAWATOA WAFU WALIOKUWAMO NDANI YAKE.

Nini maana ya kuabudu?

Wenye kubatizwa kwa ajili ya wafu ni wakina nani?

Praitorio ni nini? Na Kwanini ilikuwa ni najisi kwa wayahudi kuingia humo? (Yohana 18:28)

Nini maana ya Ukuta uliopakwa chokaa (Matendo23:3)?

Makanda ni nini?

Rudi nyumbani

Print this post

Maana ya Mithali 29:21 “Amtunduiaye mtumwa wake tangu utoto, Mwisho wake atakuwa ni mwanawe”

Mithali 29:21 “Amtunduiaye mtumwa wake tangu utoto, Mwisho wake atakuwa ni mwanawe”.

Kutundua ni kujali mtu kupita kiasi, au kuonyesha wema uliopitiliza.

Hivyo hapo anaposema amtunduiaye mtumwa wake tangu utotoni, mwisho wake atakuwa ni mwanawe. Anamaanisha amjalie mtumwa wake, kupita kiasi, yaani kuishi naye kama sio mtumwa kwake, (kumdekeza), na kama mfano ikiendelea hivyo kwa kipindi kirefu, mwisho wake utakuwa ni kumfanya mwanawe, yaani mrithi.

Zamani enzi za biblia, watu walikuwa aidha wananunua watumwa, au wanawazalisha majumbani kwao, ikiwa na maana kama mtu huyo alikuwa na mtumwa, kisha mtumwa Yule akazaa, sasa wale watoto wanakuwa pia ni watumwa wa Yule bwana.

Na kulikuwa na sheria kwamba kila baada ya miaka 7, mbiu ilipigwa ya kuwafanya watumwa wote huru, hivyo waliotaka kuondoka waliondoka, lakini waliotaka kuendelea, basi waliendelea kwa mkataba mwingine wa miaka saba. Na hivyo mtumwa huyo aliwajibika kutumika ipasavyo muda wote huo wa mkataba wake (Kumbukumbu 15:1-18).

Sasa hapa, biblia inaeleza tabia ya bwana ambaye moyo wake ni wa kitofauti. Bwana ambaye, anatabia ya kumjali sana mtumwa wake kuliko uhalisia, huwenda anamuhurumia, kumwona anafanya kazi nyingi, hivyo anampa kidogo tu, au anapokwenda kwenye sherehe hamwachi nyumbani anakwenda naye pia, hata akiwa nyumbani majukumu anapewa machache sana, anakaa naye mezani pamoja wanacheka n.k… Sasa katika hali kama hiyo, ikiwa mtumwa huyo, atadumu kubaki kwa bwana wake, kwa kipindi kirefu, Yule bwana, atamfanya tu kuwa kama mmojawapo wa mwanawe, maana yake siku atakapotoa urithi, na huyu lazima apewe, kwasababu ameishi kama mtoto wake kwa kipindi kirefu.

Na hii ni kweli, hata katika kipindi hichi, labda mfanyakazi kaajiriwa kwenye nyumba fulani, kisha mwenye nyumba akampenda, akawa naye kwa kipindi cha miaka mingi, mwishowe, atamfanya tu kama mwanafamilia, na hatimaye atapata kitu kama mmojawapo wa watoto wake.

Ni kufunua nini rohoni?

Hii ni Tabia aliyokuwa nayo Mungu kwetu sisi watu wa mataifa.

Tulipokwenda kwake, hatukuwa wana wake, au warithi, bali warithi walikuwa ni wayahudi tu, lakini kwa ukarimu wake, akatutoa katika utumwa na kutufanya WANA, jambo ambalo si kawaida kwa bwana yoyote, kutenda kwa kijakazi aliyezaliwa kusikojulikana. Ndicho alichokuja kukifanya Yesu;

Yohana 15:15  Siwaiti tena watumwa; kwa maana mtumwa hajui atendalo bwana wake; lakini ninyi nimewaita rafiki; kwa kuwa yote niliyoyasikia kwa Baba yangu nimewaarifu.

Yohana 8:35  “Wala mtumwa hakai nyumbani sikuzote; mwana hukaa sikuzote. 36  Basi Mwana akiwaweka huru, mtakuwa huru kweli kweli”.

Hivyo mimi na wewe tunafanyika, WANA na WARITHI, wa Mungu kwa njia ya Bwana Yesu. Haleluya. Utukufu na heshima ni kwa Bwana wetu Yesu!! milele na milele.

Lakini ni nini tunapaswa kukifanya?

Ni kukubali tu kudumu katika nyumba yake. Kama vile mtumwa Yule ambaye aliamua kudumu tangu UTOTONI. Hivyo na wewe umepewa neema, dumu katika neema, dumu katika wokovu, acha kutanga tanga huku na kule. Mungu akaghahiri mema kwako. Ulimwengu hauwezi kukupa unafuu wowote, ni kwa Kristo tu ndio utapata raha nafsini, Hakuna mateso kwa Kristo, Utumwa wake ni mwepesi sana alisema hivyo. Soma (Mathayo 11:28-30).

Ikiwa hujaokoka unasubiri nini sasa? Embu fanya uamuzi wa haraka sana umgeukie Kristo akuokoe. Hizi ni siku za mwisho, anakaribia kurudi kuwanyakua wateule wake. Kama upo tayari kutubu leo dhambi zako, basi fungua hapa kwa  ajili ya mwongozo wa sala ya toba.>>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Nini tofauti ya Mtumwa, Mjakazi na kijakazi?

Maana ya Mithali 9:17 “Maji yaliyoibiwa ni matamu, Na mkate ulioliwa kwa siri hupendeza”

Miimo ni nini na kizingiti ni nini?

Ni kwa namna gani haki huinua taifa? (Mithali 14:34)

AKAPITA KATIKA LILE SHAMBA AMBALO YAKOBO ALIMPA YUSUFU MWANAWE

Nini maana ya Mithali 27:6 “Jeraha utiwazo na rafiki ni amini;

Nini maana ya kukunguwazwa (Marko 14:27)

Rudi nyumbani

Print this post

Kutoka 21:10 ina maana gani?.

Jibu: Tuanze kusoma  kuanzia mstari wa 7..

Kutoka 21:7 “Mtu akimwuza binti yake awe kijakazi, hatatoka yeye kama watumwa wa kiume watokavyo. 

8 Kwamba bwana wake hakupendezewa naye, akiwa amemposa, ndipo atakubali akombolewe; hana amri yeye kumwuza aende kwa watu wageni maana amemtenda kwa udanganyifu. 

9 Kwamba amposa mwanawe, atamtendea kama desturi zipasazo binti zake. 

10 Kwamba ajitwalia mke mwingine, chakula chake huyo, na nguo zake, na ngono yake, hatampunguzia.  11 Kwamba hamfanyii mambo haya matatu, ndipo atatoka aende bure, pasipo kutolewa mali”.

Jibu: Kwa desturi za kiyahudi mtumwa wa kiume au wa kike anapaswa amtumikie bwana wake kwa muda wa miaka 6 tu, ukifika mwaka wa 7 anakuwa yupo huru kuondoka.,

Kumbukumbu 15:12 “Ikiwa nduguyo, mume wa Kiebrania, au mwanamke wa Kiebrania, akiuzwa kwako, naye amekutumikia miaka sita; basi mwaka wa saba mwache huru aondoke kwako.

 13 Nawe utakapomwacha huru aondoke kwako, usimwache aende zake mikono mitupu”

Ikiwa mtumwa wa kiume aliingia na mke wake basi utakapofika mwaka wa 7 ataondoka na mke wake huyo, (Kutoka 21:1-3) lakini kama aliingia bila mke na akaozwa mke kutoka katika familia ya bwana wake, basi utakapofika mwaka wa 7 atatoka yeye kama yeye, lakini mke na watoto watabaki kwa baba wa mke wake, hana amri ya kuondoka nao, lakini kama hataki kumwacha mke wake na watoto wake basi atamtumikie bwana wake huyo daima kwa agano la kutobolewa sikio kwa uma.

Kutoka 21:5 “Lakini huyo mtumwa akisema waziwazi, Mimi nampenda bwana wangu, na mke wangu na watoto wangu; sitaki mimi kutoka niwe huru; 

6 ndipo hapo huyo bwana wake atamleta mbele ya Mungu na kumleta mlangoni, au penye mwimo wa mlango; na bwana wake ATALITOBOA SIKIO LAKE KWA UMA; ndipo atamtumikia sikuzote”.

Hivyo ishara ya kutobolewa sikio ilikuwa ni ishara ya mtumwa kukataa uhuru wake.

Lakini kwa upande wa mtumwa wa kike (yaani kijakazi) ilikuwa ni tofauti kidogo. Kama kijakazi aliingia bila kuolewa na baadaye kijana wa bwana wake akampenda na kumwoa, kama mke wa kwanza basi famila ya kijana inapaswa kumfanya kama binti yao.

Lakini kama ameolewa kama mke wa pili, na bado ni kijakazi, na bwana wake hamtaki tena awe mke wake au suria wake, basi utakapofika mwaka wa 7, wakati wa maachilio, yeye hatamwachilia kama mabinti wengine wajakazi wanaoachiwa huru, bali kinyume chake ataachiliwa kwa gharama (maana yake atakombolewa).

Hivyo yule baba wa mtoto wa kiume aliyemwoa huyo binti, atamwuza kwa mojawapo wa ndugu aliye karibu, na si kwa mgeni (yaani mtu kutoka taifa lingine tofauti na Israeli), na asipopatikana wa kumnunua ndipo yule kijana ataendelea kuishi naye huku akimtimizia haki yote ya ndoa, ikiwemo CHAKULA, MAVAZI NA HAKI YA NDOA (Ngono).

Vitu hivyo vitatu ni sheria avitimize, si kwasababu hamtaki tena na kakosa mtu wa kumnunua basi aanze kumnyanyasa kwa kumnyima chakula chake na mavazi pamoja na haki ya ndoa ambayo imenenenwa na mtume Paulo kwa uongozo wa Roho katika 1Wakorintho 7:5. Na ikitokea kashindwa kumtimizia hayo mambo matatu basi atamwacha aende zake huru, bila gharama zozote za kumkomboa.

Kutoka 21: 10 “Kwamba ajitwalia mke mwingine, chakula chake huyo, na nguo zake, na ngono yake, hatampunguzia. 

11 Kwamba hamfanyii mambo haya matatu, ndipo atatoka aende bure, pasipo kutolewa mali”.

Mambo gani tunajifunza?

1.Kutoboa masikio si ishara nzuri.

Asili ya kutoboa sikio na kuweka hereni haikuwa nzuri, watu waliotobolewa masikio enzi za zamani ni watu waliokataa uhuru wao, hali kadhalika roho hiyo hiyo inatembea mpaka leo, kibiblia mwanamke au mwanaume hapaswi kutoboa masiko yake. Huenda ulitobolewa enzi hujaokoka, sasa umeshaokoka usiweke hereni baki katika uhalisia wako.

Wengi wanaosumbuliwa na nguvu za giza ni kutokana na vitu wanavyoviweka katika miili yao, na hawajui kuwa hivyo ndio vyanzo vya roho zinazowasumbua.

2. Ni lazima kutimiza haki ya Ndoa

Mtu aliyeoa au aliyeolewa ni sharti amtimizie mwenzie haki zote za ndoa ikiwemo upendo, na ukaribu wakati wowote unapohitajika. Maandiko yanasema mume hana amri juu ya mwili wake kadhalika mke.

1Wakorintho 7:2  “Lakini kwa sababu ya zinaa kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe, na kila mwanamke na awe na mume wake mwenyewe.

3  Mume na ampe mkewe haki yake, na vivyo hivyo mke na ampe mumewe haki yake.

4  Mke hana amri juu ya mwili wake, bali mumewe; vivyo hivyo mume hana amri juu ya mwili wake, bali mkewe.

5  Msinyimane isipokuwa mmepatana kwa muda, ili mpate faragha kwa kusali; mkajiane tena, Shetani asije akawajaribu kwa kutokuwa na kiasi kwenu”.

Maran atha!

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

EPUKA MUHURI WA SHETANI

USIMPE NGUVU SHETANI.

MISTARI YA BIBLIA KUHUSU NDOA.

TUNAHESABIWA HAKI BURE KWA NJIA YA IMANI.

Tu uzao wake Ibrahimu, wala hatujawa watumwa wa mtu.

Rudi nyumbani

Print this post

Je Bwana Yesu alikuwa na nywele ndefu?

JIBU: Picha nyingi zinazochorwa kumweleza Yesu, takribani nyingi ya hizo  zinamwonyesha ni mtu mwenye nywele ndefu. Lakini Je uhalisia wake ni upi, ni kweli alikuwa na nywele ndefu au fupi?

Maandiko yanaeleza utamaduni wa wayahudi, kwa wanaume ilikuwa kuacha nywele zirefuke kama zile za mwanamke ni aibu kwa mtu huyo. Anajivunjia heshima kubwa.

1Wakorintho 11:14  “Je! Hayo maumbile yenyewe hayawafundishi ya kwamba mwanamume akiwa na nywele ndefu ni aibu kwake? 15  Lakini mwanamke akiwa na nywele ndefu ni fahari kwake. Kwa sababu amepewa zile nywele ndefu ili ziwe badala ya mavazi”

Hivyo hakukuwa na mtu aliyekuwa na nywele ndefu isipokuwa tu mtu aliyeitwa mnadhiri wa Mungu.

Lakini Je! Yesu alikuwa ni Mnadhiri ?

Kabla ya kufahamu kama Yesu alikuwa mnadhiri au la! Tufahamu kwanza mnadhiri alikuwa ni nani, na sheria ya mnadhiri ilikuwaje

Mnadhiri ni mtu aliyetengwa au aliyejitenga mwenyewe/ aliyejitoa wakfu kwa Mungu, kufuata na sababu binafsi, aidha kwa sababu ya shukrani yake ya kutendewa jambo Fulani kama vile kuponywa ugonjwa, au  kupatiwa mtoto, au kupata kitu Fulani kwa Mungu alichokuwa anamwomba. Hivyo katika agano la kale, kulikuwa na sheria ya mnadhiri. Na mnadhiri alikuwa yoyote Yule aidha mwanamke au mwanaume.

Sheria za mnadhiri ni zipi?

Kulingana na Hesabu 6:1-8

  1. Hakuruhusiwa kunywa divai, wala zabibu, wala juisi ya zabibu,  wala mbegu zake. Yaani kwa ufupi kitu chochote kilichomzao wa zabibu hakuruhusiwa kunywa
  2. Hakuruhusiwa kukata nywele zake, tangu siku hiyo aliyomwekea Mungu nadhiri mpaka atakapoitoa
  3. Hakuruhusiwa kugusa maiti. Hata kama ni ndugu yake wa karibu amekufa, baba yake au dada yake. Hakuruhisiwa  kufanya hivyo
  4. Ni lazima awe mtakatifu kwa Bwana; Maana yake ajitenge na mambo yote yaliyo najisi kipindi chote awapo katika kiapo chake.

Katika biblia, kulikuwa na makundi mawili ya wanadhiri

  1. Wanadhiri wa daima: Hawa ni waliotengwa tangu tumboni mwa mama zao: Mfano wao alikuwa  ni Samsoni, Samweli, Yohana Mbatizaji.. Hawakukatwa nywele zao, lakini pia hawakunywa divai maisha yao yote.
  2. Wanadhiri wa muda: Hawa ni aidha waliamua wenyewe katika kipindi Fulani katika maisha yao waingie kwenye viapo hivyo kwa Mungu, yaani wamtumikie yeye daima mpaka kufa kwao, au waliokuwa na nadhiri za muda, ambapo pengine baada ya miezi miwili, au mwaka mmoja wanaiondoa na kwenda kunyoa nywele zao, na kuendelea kutumia mizabibu nk. Mfano wa Hawa alikuwa ni mtume Paulo, ambaye kipindi Fulani anashuhudia naye alikuwa na nadhiri hiyo.

Matendo 18:18  “Baada ya hayo Paulo akazidi kukaa huko siku nyingi, kisha akaagana na ndugu akaabiri kwenda Shamu; na Prisila na Akila wakaenda pamoja naye, alipokwisha kunyoa kichwa chake huko Kenkrea; maana alikuwa ana nadhiri”

Sasa tukirudi kwa Bwana Yesu.

Je! Na Yeye alikuwa ni mnadhiri?

Jibu ni hapana, kwasababu Bwana alikunywa mzao wa mzabibu.

Mathayo 26:29  Lakini nawaambieni, Sitakunywa kabisa tangu sasa uzao huu wa mzabibu, hata siku ile nitakapokunywa mpya pamoja nanyi katika ufalme wa Baba yangu.

Kuonyesha kuwa hapo kabla alikuwa anakunywa.

Soma pia  Mathayo 11:19, Na Yohana 2:1-12, inatupa picha alitumia mzao wa mzabibu. Halikadhalika aligusa maiti, (Marko 5:41), na zaidi ya yote Bwana hakufungwa na sheria za torati.

Hivyo kwa kifupisho ni kwamba Bwana Yesu hakuwa na nywele ndefu, yawezekana alikuwa na nywele nyingi lakini hazikuwa ndefu kama za mwanamke, mfano wa aonekanavyo kwenye baadhi ya picha zinazochorwa.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

JE! NYWELE ZAKO ZINAOTA AU ZIMESIMAMA?

WINGU KUBWA LA MASHAHIDI.

Je! sheria ilikuwaje dhaifu kwasababu ya mwili? (Warumi 8:3)

NGUVU YA MNADHIRI WA BWANA.

MAUTI NA KUZIMU ZIKAWATOA WAFU WALIOKUWAMO NDANI YAKE.

Nini maana ya Kucheka kwenu na kugeuzwe kuwa kuomboleza (Yakobo 4:9)

Fahamu maana ya Mithali 29:4 “Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua.

Rudi nyumbani

Print this post

Je ni nyaraka zipi mtume Paulo aliziandikia gerezani?

Kati ya nyaraka kumi na tatu (13) alizoziandika mtume Paulo, Nne (4) kati ya hizo, aliziandika akiwa gerezani. Alipokuwa Rumi, ambapo maandiko yanatuonyesha  alipelekwa na kuwekwa chini ya kifungo maalumu ambacho aliruhusiwa watu kumtembelea lakini pia kuwahubiria injili akiwa katika kifungo hicho cha nyumba.

Matendo 28:16  “Tulipoingia Rumi Paulo alipewa ruhusa kukaa kwake mwenyewe pamoja na askari aliyemlinda…. 30  Akakaa muda wa miaka miwili mizima katika nyumba yake aliyokuwa ameipanga, akawakaribisha watu wote waliokuwa wakimwendea, 28.31  akihubiri habari za ufalme wa Mungu, na kuyafundisha mambo ya Bwana Yesu Kristo, kwa ujasiri mwingi, asikatazwe na mtu”.

Hivyo huko ndipo panaaminika aliandika nyaraka hizi nne. Ambazo ni

  1. Waefeso,
  2. Wafilipi,
  3. Wakolosai,
  4. Filemoni.

Sasa ni kwanini Nyaraka hizi na si nyingine?

Ni kwasababu ya habari za kufungwa kwake, alizozitaja katika nyaraka hizo; Ambazo zinaonyesha mazingira hayo alikuwa kifungoni.

Kwamfano ukisoma vifungu hivi, utaona,

Waefeso 3:1,4:1, Wafilipi 1:13, Wakolosai 4:3, Filemoni 1:10.

Je Ni nini cha kujifunza, katika vifungo vya mtume Paulo?

Yamkini Paulo alitamani awe huru kwa wakati ule ili aendelee kuihubiri injili kwa mataifa yote. Lakini hakujua mpango wa Mungu kwa nyaraka zake. Hakujua kuwa  Mungu atazihifadhi kwa mamia ya miaka, ili ziwe injili kwa vizazi vijavyo. Na matokeo yake ni kuwa nyaraka hizo zimehubiri injili kuliko hata wakati alipokuwa anazunguka mwenyewe kwenye mataifa akiwa huru.

Kwamfano mafunzo yaliyo katika kitabu cha Waefeso, yanatoa mwongozo mzuri kuanzia Viongozi wa kanisa, watakatifu hadi ngazi za kifamilia. Na jinsi gani mtakatifu anavyopaswa avae silaha za haki ili aweze kumpinga adui yake shetani (Waefeso 6:11-18)

Hii ni kuthibitisha maneno yale ya maandiko yanayosema kwamba injili  haifungiki.

2Timotheo 2:9  “Nami katika hiyo nimeteswa hata kufungwa kama mtenda mabaya; lakini neno la Mungu halifungwi

Na wewe pia ujionapo upo katika mazingira yanayokubana kuitangaza injili ya Bwana, usiwe na mawazo ya kukata tamaa, hapo hapo tazama upenyo wowote uutumie, kwasababu wewe umefungwa lakini sauti ya Mungu iliyo ndani yako, inauwezo wa kufika duniani kote, kwa vizazi vyote, hata kama umefungiwa kwenye chumba cha giza, namna gani, injili ya Kristo, inaangusha ngome popote.

Nyanyuka sasa, fanya jambo kwa Bwana, iamini nguvu ya msalaba.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Je! Mtume Paulo alikuwa ni Mrumi, Myahudi au raia wa Tarso?

Je Paulo na Petro walishindania nini? (Wagalatia 2:11).

Tarishi au Matarishi ni akina nani  kwenye biblia?

Je ni kweli Tumejengwa juu ya Mitume na Manabii? (Waefeso 2:20)

SIRI YA KUFANIKIWA KWA MTUME PAULO.

Paulo alikuwa na maana gani aliposema “nimeaminiwa uwakili”

Rudi nyumbani

Print this post

Je Paulo na Petro walishindania nini? (Wagalatia 2:11).

Swali: Kwanini Petro na Paulo walishindana na pia tunajifunza nini katika kushindana kwao?.

Jibu: Tusome,

Wagalatia 2:11 “Lakini Kefa alipokuja Antiokia, nalishindana naye uso kwa uso, kwa sababu alistahili hukumu”

Kushindana kunakozungumziwa hapo si kushindana kwa maneno ya dini kule kunakozungumziwa katika 1Timotheo 6:4, 2Timitheo 2:14 na Wafilipi 2:14, kwamba tutende mambo yote pasipo mashindano wala manung’uniko.

Wala si mashindano ya Imani, yale yanayozungumziwa katika Wafilipi 1:30 na Waebrania 12:1 ambayo tunapaswa tuwe nayo, (yaani kushindana dhidi ya nguvu za giza na kuishikilia imani).

Bali neno “mashindano” kama lilivyotumiwa hapo na Paulo lilimaanisha “kukabiliana”. Maana yake Paulo alipofika Antiokia na kukutana na Petro alikabiliana naye uso kwa uso na kumwonya kuhusiana na tabia aliyoonesha ya uvuguvugu juu ya desturi za wayahudi katika kula.

Maana yake Petro alipokuwa ameketi na wayahudi aliungana nao kwa kutokula vyakula vilivyo najisi kwa hofu ya wayahudi…lakini mahali alipoketi katika chakula pamoja na watu wa mataifa, alishirikiana nao katika vyakula hivyo vilivyo najisi kwa wayahudi.

Sasa tabia hiyo haikuwa sawa, ndipo Paulo alipoona na kumkabili na kumwambia dhahiri kuwa anachokifanya sio sawa.

Wagalatia 2:11 “Lakini Kefa alipokuja Antiokia, nalishindana naye uso kwa uso, kwa sababu alistahili hukumu

12 Kwa maana kabla hawajaja watu kadha wa kadha waliotoka kwa Yakobo, alikuwa akila pamoja na watu wa Mataifa; lakini walipokuja wao, akarudi nyuma akajitenga, huku akiwaogopa waliotahiriwa.

13 Na hao Wayahudi wengine wakajigeuza pamoja naye, hata na Barnaba pia akachukuliwa na unafiki wao.

14 Walakini, nilipoona ya kuwa njia yao haiendi sawasawa na ile kweli ya Injili, nalimwambia Kefa mbele ya wote, Ikiwa wewe uliye Myahudi wafuata desturi za Mataifa, wala si za Wayahudi, kwa nini unawashurutisha Mataifa kufuata desturi za Wayahudi?”.

Tunachoweza kujifunza kwa Paulo ni ujasiri wa kusimama kuitangaza kweli pasipo kujali cheo cha mtu wala heshima ya mtu, ikiwa na maana kwamba ikiwa yeyote ananyanyuka na kwenda kinyume na kweli basi anapaswa akabiliwe na kuonywa pasipo kujali cheo chake wala umaarufu wake lakini kwa nia ya upendo.

Vile vile tunachojifunza kwa Mtume Petro ni unyenyekevu, kwani baada ya kuonywa na Paulo alitubu na huoni popote akimkasirikia Paulo zaidi sana utaona anakuja kuwaelekeza watu kwenye nyaraka za Paulo kwamba wazisome..

2 Petro 3:15 “Nanyi uhesabuni uvumilivu wa Bwana wetu kuwa ni wokovu, kama vile na ndugu yetu mpenzi Paulo alivyowaandikia kwa hekima aliyopewa

16 vile vile kama katika nyaraka zake zote pia, akitoa humo habari za mambo hayo; katika nyaraka hizo yamo mambo ambayo ni vigumu kuelewa nayo; na mambo hayo watu wasio na elimu, wasio imara, huyapotoa, kama vile wayapotoavyo na maandiko mengine, kwa uvunjifu wao wenyewe”.

Na sisi hatuna budi kuiga ujasiri wa Paulo na unyenyekevu wa Petro, huo ndio ukristo!!!..Lakini si kuona dhambi na kuzifumbia macho au kuambiwa ukweli na kukasirika badala ya kujifunza na kubadilika.

Bwana atusaidie katika hayo yote.

Maran atha.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post

Je! Yesu aliwezaje kuchukuliwa na shetani juu ya kinara cha hekalu kujaribiwa?

SWALI: Wakati shetani anamjaribu Yesu, biblia inasema alimchukua na kumpandisha kwenye kinara cha hekalu, swali ni je! Alikuwa anachukuliwaje mahali pale ni njia gani ilikuwa inatumika?


JIBU: Awali ya yote ni lazima tufahamu kuwa Bwana Yesu hakupelekwa sehemu nyingine yoyote ili kujaribiwa zaidi ya pale jangwani. Hii ikiwa na maana majaribu yake yote yalimtokea akiwa palepale jangwani.

Mathayo 4:1  “Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na Ibilisi,2  Akafunga siku arobaini mchana na usiku, mwisho akaona njaa”

Sasa kama ni hivyo iweje, shetani amtoe pale na kumpeleka kwenye kinara cha Hekalu na wakati huo huo amwonyeshe milki zote za ulimwenguni? Je! Aliondokaje pale? Au alichukuliwa kimazingara?

Mathayo 4:5  “Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mji mtakatifu, akamweka juu ya kinara cha hekalu 6  akamwambia, Ukiwa ndiwe Mwana wa Mungu jitupe chini; kwa maana imeandikwa, Atakuagizia malaika zake; Na mikononi mwao watakuchukua; Usije ukajikwaa mguu wako katika jiwe. 7  Yesu akamwambia, Tena imeandikwa, Usimjaribu Bwana Mungu wako. 8  Kisha Ibilisi akamchukua mpaka mlima mrefu mno, akamwonyesha milki zote za ulimwengu, na fahari yake, 9  akamwambia, Haya yote nitakupa, ukianguka kunisujudia. 10  Ndipo Yesu alipomwambia, Nenda zako, Shetani; kwa maana imeandikwa, Msujudie Bwana Mungu wako, umwabudu yeye peke yake. 11  Kisha Ibilisi akamwacha; na tazama, wakaja malaika wakamtumikia”

Jibu ni kwamba majaribu yale yalikuwa katika roho, na sio katika mwili, Kwa ufupi yalikuwa ni mfano wa maono. Na kikawaida maono yanapokuja ikiwa ni ya kukuonyesha tukio husika utashangaa waweza kujiona kama upo pale pale eneo lenyewe, lakini sio. Kama tu vile ndoto. Unaota upo kijijini kwenu, unashughulika, unaongea na ndugu, lakini kiuhalisia kumbe umelala palepale kitandani.

Ndivyo ilivyokuwa kwa Bwana Yesu, alikuwa palepale jangwani, wala hakutoka, isipokuwa alikuwa katika roho, akayaona hayo yote, aliyoonyeshwa na shetani.

Bwana akubariki.

Lakini pia ni vizuri, kutambua maana ya majaribu yale, Kwasababu hayo pia ndio shetani anayotumia kumjaribu kila mtakatifu aliyepo duniani. Kwa upana wa habari hiyo waweza fungua link hii >>> MAJARIBU MATATU YA YESU KRISTO

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

DAKIKA MOJA TU, INAKUFANYA UMWAMINI SHETANI?

Tofauti kati ya ufunuo, unabii na maono ni ipi?

NI KWA NAMNA GANI TUTASHINDA MAJARIBU?

JE! JICHO LAKO LINAONA NINI KATIKATI YA MAJARIBU?

UFUNUO: Mlango wa 11

DALILI TISA (9) ZA PEPO KUWEPO NDANI YA MTU.

KWA WINGI WA WASHAURI HUJA WOKOVU.

Rudi nyumbani

Print this post

Maana ya Mithali 9:17 “Maji yaliyoibiwa ni matamu, Na mkate ulioliwa kwa siri hupendeza”

SWALI: Je! mstari huu unaelewekaje? Mithali 9:17 “Maji yaliyoibiwa ni matamu, Na mkate ulioliwa kwa siri hupendeza”


JIBU: Mstari huo unamfunua mtu mwenye asili ya dhambi, jinsi vitu vilivyo kinyume na mapenzi ya Mungu vinavyoweza kupendeza mbele yake zaidi ya vile ambavyo ni sahihi kwake kuvifanya.

Kwamfano katika habari hiyo ukianzia vifungu vya juu utaona vinamweleza mwanamke kahaba, anavyowateka watu kuzini naye. Na mtu mjinga ataona ni sahihi kwenda kwake, lakini mwisho wake ni mbaya. Watu wengi wanaacha ndoa zao nakwenda kuzini nje! Kwasababu wanaona kile wanachokipata huko nje, kina uzuri kuliko kile walichokizoea ndani, wengine wanafanya uasherati, kwasababu wanaona wakingojea mpaka wakati wa ndoa, watakosa mambo mengi. Hao ndio wanaotembea katika usemi huo  “Maji yaliyoibiwa ni matamu, Na mkate ulioliwa kwa siri hupendeza”

Wengine wanaona wakitumia njia ya udanganyifu, ndio zitawafikisha katika malengo yao kwa haraka, kuliko njia za halali, hivyo hujiingiza katika wizi, na magendo.

Lakini ukizidi kusoma mstari unaofuata anasema..

.  Lakini huyo hajui ya kuwa wafu wamo humo; Ya kuwa wageni wake wamo chini kuzimuni.

Maana yake ni kuwa wote wafanyao mambo kama hayo, mwisho wao unakuwa ni kifo, na kuishia kuzimu kabisa. Dumu katika ndoa yako, kataa vya wengine, epuka mambo ya sirini. Yusufu hakukubali kuzini na mke wa boss wake. Lakini Daudi alidanganyika akazini na mke wa kijakazi wake, matokeo yake yakawa na yeye kunajisiwa wake zake vilevile, mtoto wake kufa, na ufalme wake kutikiswa na mwana wake mwenyewe aliyeitwa Absalomu, lakini zaidi sana kupoteza furaha ya wokovu kwa miaka mingi sana. Daudi alijutia makosa yake kwa muda mrefu sana.

Hivyo usipumbazwe na vivutio vyovyote vya dhambi vitakugharimu sana.

Shalom.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Nini maana ya Mithali 27:21  inaposema “mtu hujaribiwa kwa sifa zake?”

Fahamu maana ya Mithali 29:4 “Mfalme huithibitisha nchi kwa hukumu; Bali yeye apokeaye rushwa huipindua.

Kuwaogopa wanadamu huleta mtego,(Mithali 29:25)

Jicho ni  nini (Yakobo 3:11)

NI NINI BWANA ANATAZAMIA KILA TUNAPOSHIRIKI MEZA YAKE.

KUWA MAKINI NA MITANDAO, NI SHIMO REFU.

Ni lini na wapi Ibrahimu aliioona siku ya Bwana akashangilia?

Rudi nyumbani

Print this post

Je ni lazima nibadili jina baada ya kuokoka?

SWALI: Je ni lazima nibadili jina baada ya kuokoka, na kama ni hivyo ni mazingira gani yaliyo sahihi kufanya hivyo?


JIBU: Nakusalimu katika jina la Bwana Yesu Kristo.

Unapookoka, ni vema kufahamu Kristo akishakukomboa umekombolewa kweli kweli, Huwezi kukosa mbingu kwasababu ya jina lako, hata kama lina maana mbaya, kwasababu wapo watu waliokuwa na majina mabaya, mmojawapo ni Yabesi ambaye jina lake lilimaanisha “huzuni”, kwasababu alizaliwa katika kipindi cha huzuni, na wazazi wake wakamwita hivyo lakini alimlingana na Mungu na Mungu akambariki na kumtukuza sana (1Nyakati 4:9-10).Lakini walikuwepo pia watu wenye majina mazuri mmojawapo Yuda, lakini tabia zake hazikuendana na jina lake.

Hivyo ikiwa jina lako si zuri sana, na huoni shida kuendelea nalo, huwezi kumkosa Mungu kwasababu ya hilo. Lakini pia, yapo mazingira ambayo, inampasa mkristo abadili jina endapo kuna ulazima wa kufanya hivyo. Na mazingira yenyewe ni kama haya;

  1. Umefunuliwa na Mungu mwenyewe: Wakati mwingine Mungu anaamua kumwambia mtu abadili jina, sio kwasababu jina lile ni baya, hapana, bali kwasababu ya kusudi alilowekewa mbele yake kulifanya. Kwamfano Mungu alimbadili jina Abramu, akamwita Ibrahimu, na tafsiri yake ni ‘Baba wa mataifa mengi’, hivyo huduma yake ya kuwa baba wa wengi, ilimpasa iendane na jina lake. Na ndivyo  ilivyokuwa kwa Sara na baadhi ya mitume.
  2. Jina lenye tafsiri ya imani nyingine/ au miungu: Yapo majina ambayo, ukiitwa mtu atatambua wewe ni wa dini nyingine, sasa hapa ni amani tu ya Kristo itawale ndani yako, ukiona ni vema ubadili, ni sawa, ili injili au ushuhuda wako usiwe na kikwazo kwa wengine mbeleni. Lakini bado hilo halikufanyi Mungu asikutumie, utatumiwa tu. Katika biblia tunaona Danieli, aliitwa jina la kipagani na Nebukadreza, Belteshaza (Danieli 1:7), Lakini hakuling’ang’ania hili jina, badala yake aliendelea kujiita Danieli, na mbingu pia ilimtambua hivyo. Japokuwa mfalme alimuita Belteshaza kufuatana na jina la miungu yake. Kwahiyo ikiwa jina lako halikaribiani na imani, ukiona vema kubadilisha hutendi dhambi.
  3. Maisha mapya:  Wakati mwingine historia yako ya nyuma, inaacha sifa mbaya katika jina lako. Kwamfano, ulikuwa ni mtu jambazi na mwizi, na unajulikana kwenye jamii kama ‘Yule Fulani kibaka’. Sasa wengi wanapookoka, wanasukumwa kabisa kubadilisha na majina yao, wawe wapya kote kote. Mfano mmojawapo wa hawa ni mtume Paulo, alikuwa mwuaji, na alikuwa anaitwa Sauli. Lakini alipomgeukia Mungu na jina lake pia akalibadili.
  4. Jina lisilo na tafsiri nzuri: Kumbuka pia wapo wengine wanakwazwa na tafsiri za majina yao. Labda anaitwa majuto, au shida, au msiba, au masumbuko. Hivyo anapookoka anapendelea ajiite majina ya ushindi au yenye Baraka. Hivyo anayechagua hili ni vizuri zaidi.

Kwahiyo hivyo ndio vigezo vya mtu kusukumwa abadili jina. Lakini usibadili kwasababu ya shinikizo la mtu, ikiwa huoni kikwazo chochote kuitwa jina hilo lako. Kwasababu wokovu wako, hauwezi kuzuiwa na jina. Hilo ulifahamu.

Bwana akubariki.

Tafadhali shea na wengine ujumbe huu;

Pia Kwa maombezi/ Ushauri/ Maswali/ Whatsapp:
Tuandikie katika BOXI la Maoni hapo chini au
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

JINA LAKO NI LA NANI?

MAANA YA MAJINA NA TAFSIRI ZAKE.

Kula uzao wa tumbo lako maana yake nini? (Kumbukumbu 28:53)

Majina mbalimbali ya Mungu na maana zake.

Huihesabu idadi ya nyota, Huzipa zote majina.

KWA WINGI WA WASHAURI HUJA WOKOVU.

UPEPO WA KUSI HULETA MVUA;

Rudi nyumbani

Print this post