Category Archive Sadaka

JE! KUNA UMUHIMU WOWOTE WA KULIPA ZAKA?

Jina la Bwana wetu Yesu Kristo libarikiwe, karibu tujifunze Neno la Mungu ambalo ndio mwanga wa njia zetu na taa ya miguu yetu. Zab 119:105..Leo tutajifunza kwa ufupi sana juu ya kulipa Zaka, Kimaandiko Zaka ni fungu la 10, yaani sehemu ya 10 ya mapato ya mtu anayatoa kwa Mungu. Kwahiyo zaka ni mojawapo ya aina ya sadaka.

Kabla hatujaenda kujifunza kuhusu umuhimu wa kulipa zaka, kama ina ulazima au la! Hebu tujifunze kidogo historia ya ZAKA.

Zaka kwa mara ya Kwanza ilianza kutolewa na mtu anayeitwa Ibrahimu, ambaye anajulikana kama Baba wa Imani.

Tunasoma hayo katika kitabu cha Mwanzo 14

Mwanzo 14:17 “Abramu aliporudi kutoka kumpiga Kedorlaoma na wale wafalme waliokuwa pamoja naye, mfalme wa Sodoma akatoka amlaki katika bonde la Shawe, nalo ni Bonde la Mfalme.

18 Na Melkizedeki mfalme wa Salemu akaleta mkate na divai, naye alikuwa kuhani wa Mungu Aliye juu sana.

19 Akambariki, akasema, Abramu na abarikiwe na Mungu Aliye juu sana, Muumba mbingu na nchi.

20 Ahimidiwe Mungu Aliye juu sana, aliyewatia adui zako mikononi mwako. ABRAMU AKAMPA FUNGU LA KUMI LA VITU VYOTE”.

Ibrahimu alimpa fungu la 10 huyu Melkizedeki, huyu Melkizedeki alikuwa ni Mungu aliyekuja katika Mwili wa kibinadamu… na pia anajulikana kama Kuhani Mkuu, mfano wa Mwana wa Mungu (Yesu Kristo) hana baba, wala mama, wala hana mwanzo wa siku wala mwisho wake. Kwahiyo alikuwa ni Mungu mwenyewe aliyekuja katika mwili wa kibinadamu.

Sasa wakati Abramu ametoka kumwokoa ndugu yake Lutu ambaye alikuwa ametekwa yeye pamoja na wanawe, njiani wakati anarudi akakutana na Huyu Melkizedeki, na huyu Melkizedeki alikuwa amebeba Divai na Mkate, akampatia Abramu na kwasababu Abramu alimpenda sana Mungu, hakuona vyema kupokea bure bila kutoa chochote…zaidi ya yote Mungu amemwonekania na kumfanikisha katikati ya maadui zake na kuwashinda! Hivyo ndani yake kuna kitu cha kipekee kikamgusa akaona si vyema kutomrudishia chochote Mungu wake, hivyo akaamua mwenyewe pasipo kuambiwa na mtu yeyote kumtolea Mungu wake sehemu ya 10 ya vitu vyake!!! O huo ni moyo wa namna gani? Kumbuka hakuambiwa hata na Mungu afanye vile, ni yeye mwenyewe tu kuna kitu ndani yake kilimfanya ajisikie vibaya endapo angemwona Mungu wake anaondoka mikono mitupu, na hicho si kingine zaidi ya Roho Mtakatifu.

Je! Sheria ilifanya kazi?

Sasa wakati huo kulikuwa hakuna sheria yoyote, wala amri 10 na Mungu hakuingia Agano na Ibrahimu kuhusu zaka, Miaka kama 400 hivi baadaye ndipo wana wa Israeli, walikuja kupewa sheria na Mungu! Na miongoni mwa hizo sheria ilikuwa ni pamoja na kulipa zaka!, ilikuwa ni lazima kulipa zaka, mtu asipolipa zaka ilikuwa inahesabika kwake kuwa ni dhambi!, na mbele za Mungu ni kama mwizi (Malaki 3:8-9).

Lakini sasa hatuishi kwa sheria bali kwa Imani, na Imani tunayoizungumzia ni Imani ile ile ya kwanza kama ya Ibrahimu, yaani Imani ya kufanya mambo bila ya kusukumwa sukumwa, na Imani hiyo ndio kama hiyo ya Ibrahimu, ya kumtolea Mungu fungu la 10 pasipo masharti!..Ibrahimu alitoa pasipo masharti, wala sheria, wala torati kwasababu Torati hata bado ilikuwa haijaja, wala kulazimishwa, wala kusukumwa wala kuombwa, wala kumwuliza Mungu, wala kuhubiriwa na mtu yeyote bali alitoa kwa Imani na kwa moyo, akitafakari kwamba vyote vimetoka kwa Mungu, na Mungu ndiye mpaji wangu (Yehova-YIRE), hivyo kama yeye amenipa sehemu kubwa ya vitu hivi, basi mimi nitamrudishia walau sehemu ya 10 ya vitu alivyonipa. Na akajiwekea hiyo kuwa ndio sheria yake daima! Kila sehemu ya 10 anayopata anamrudishia Mungu.

Ndugu, Ibrahimu alikutana na Melkizedeki, na hata sasa huyu Melkizedeki yupo naye si mwingine bali ni Bwana wetu Yesu Kristo, maandiko yanalithibitisha hilo katika…

Waebrania 6:20 “alimoingia Yesu kwa ajili yetu, mtangulizi wetu, amekuwa kuhani mkuu hata milele kwa mfano wa Melkizedeki”.

Waebrania 7:1 “Kwa maana Melkizedeki huyo, mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu aliye juu, aliyekutana na Ibrahimu alipokuwa akirudi katika kuwapiga hao wafalme, akambariki;

2 ambaye Ibrahimu alimgawia sehemu ya kumi ya vitu vyote; (tafsiri ya jina lake kwanza ni mfalme wa haki, tena, mfalme wa Salemu, maana yake, mfalme wa amani;

3 hana baba, hana mama, hana wazazi, hana mwanzo wa siku zake, wala mwisho wa uhai wake, bali amefananishwa na Mwana wa Mungu); huyo adumu kuhani milele.

4 Basi, angalieni jinsi mtu huyo alivyokuwa mkuu, ambaye Ibrahimu, baba yetu mkuu, alimpa sehemu ya kumi ya nyara”.

Waebrania 5:5 “Vivyo hivyo Kristo naye hakujitukuza nafsi yake kufanywa kuhani mkuu, lakini yeye aliyemwambia, Ndiwe mwanangu, Mimi leo nimekuzaa.

6 kama asemavyo mahali pengine, Ndiwe kuhani wa milele Kwa mfano wa Melkizedeki”.

Umeona Kristo amefananishwa na Melkizedeki, na kama Melkizedeki alipewa sehemu ya 10 na Ibrahimu, kadhalika Kristo naye anastahili sehemu ya 10, kwasababu yeye ndiye Melkizedeki wa Agano letu, na kama Melkizedekia alivyompigania Ibrahimu ndivyo Kristo anavyotupigania sisi sasa hivi,

Na kama Ibrahimu alimpa Melkizedeki fungu la 10 pasipo masharti, wala pasipo torati, wala pasipo sheria yoyote, wala pasipo kuhubiriwa na mtu, wala pasipo kushauriwa na mtu, wala pasipo kusukumwa na mtu yeyote ndivyo hivyo hivyo leo hii tunapaswa tumtolee YESU KRISTO fungu la 10 pasipo sheria yoyote, wala pasipo masharti yoyote, wala pasipo mahubiri yoyote, wala pasipo kusukumwa na mtu..Linapaswa liwe ni jambo linalotoka moyoni kwamba tunatambua uwepo wa Yesu Kristo katika maisha yetu na hivyo tunamheshimu kwa kumtolea fungu la 10, yeye hana shida na fedha! Lakini anaitazama mioyo yetu!. Na Bwana Yesu mwenyewe aliruhusu hilo katika (Mathayo 23:23).

Ukiona mtu anapinga kulipa ZAKA!(Na huku ameshaujua ukweli) Na anapinga kumtolea Mungu, Huo ni uthibitisho kuwa hana ROHO MTAKATIFU ndani yake! Ni moja ya uthibitisho wa mtu aliyekosa Roho Mtakatifu ndani yake!..Kwasababu ni wazi kuwa hampendi Mungu, kwasababu hawezi kumshukuru kwa kutoa hata sehemu ya 10 ya mali zake na kumrudishia yeye, ingawa anavuta pumzi bure, anakanyaga ardhi ambayo sio yake bure, anakula chakula ambacho hajui kimetengenezwaje tengenezwaje! Hathamini hata Kristo aliyeotoa uhai kwa ajili yake bure..Kwa ufupi ni mtu asiye na shukrani.

Na mtu wa namna hiyo atawezaye kumshukuru Mungu kwa kutoa sehemu ya 10 ya maisha yake kuhubiri Injili?, atawezaje kutoa kutoa hata uhai wake kwaajili ya Injili?, au atawezaje kuifia Imani? Kama tu sehemu ya 10 ya fedha yake hawezi kuitoa?. Huyo Mtu atawezaje hata kuacha vyote na kumfuata Kristo kama tu sehemu ya 10 kutoa ni vita?..Atawezaje kumtolea Mungu katika vyote alivyonavyo kama Yule mwanamke aliyetoa senti mbili na Bwana akamsifia? Tafakari tu!

Hivyo ZAKA sio kitu cha kukwepa kabisa! Hakitolewi kwa sheria wala kwa torati, wala kwa imeandikwa wapi kwenye biblia, bali kwa moyo kama vile Ibrahimu!..Kama huna kazi yoyote inayokupatia kipato hapo upo huru!, lakini chochote unachokipata tofauti na kazi kitolee sehemu ya 10 katika hicho na kumrudishia Mungu, huna kazi lakini umepewa zawadi kiasi Fulani cha fedha kitolee sehemu ya 10, na utoe kwa moyo pasipo kulazimishwa, kwasababu Mungu sio mkusanyaji mapato! Anataka tumtolee kwa Moyo na kwa furaha, huku tukielewa umuhimu wa kumtolea yeye kama Ibrahimu alivyofanya.

Sasa swali ni je! Usipotoa Zaka utakwenda kuzimu?

Kitakachompeleka mtu kuzimu sio kitendo cha kukiuka kulipa zaka au kuzini, au kuiba, au kutukana hapana kitakachompeleka mtu kuzimu ni kutokuwa na Roho Mtakatifu ndani yake, ambapo sasa matokeo ya kutokuwa na Roho Mtakatifu ndio hayo sasa atakuwa mwizi, mwasherati, mtukanaji, atakuwa ni mtu asiyekuwa na Moyo wa Utoaji kabisa, likija suala la utoaji ni vita, anakuwa hawezi kuwasaidia wengine, na pia hawezi kuchangia chochote katika ufalme wa mbinguni katika utoaji wake, pia anakuwa mtu asiyesamehe Kwasababu Mtu aliye na Roho Mtakatifu hawezi kufanya mojawapo ya hayo mambo kwasababu Roho Mtakatifu atakuwa anaugua ndani yake kuhusu dhambi na atakuwa anaugua pia kuhusu ni kwanini hamtolei Mungu, hivyo hawezi kukwepa kulipa zaka kama vile asivyoweza kukwepa kuwasaidia wengine au kusali.

Upo usemi unaosema kwamba, mimi ni mkamilifu katika kila kitu! Isipokuwa ni zaka tu ndio sitoi!

Ndugu huo ni uongo wa shetani! haiwezekani mtu akawa mkamilifu katika mambo yote halafu akakosa tu kitu kimoja kwamba halipi zaka! Hakuna kitu kama hicho! Kama mtu halipi zaka kwa makusudi, na kashaujua ukweli, basi ni lazima atakuwa pia ni mwovu katika mambo mengine, ni sawa na kusema huyu mtu ni mtakatifu katika kila kitu lakini kasoro tu ni mwasherati! Huo ni uongo…

Dhambi moja inashirikiana na nyingine, aliye mwasherati ni lazima atakuwa na tamaa, kinyongo, mwongo na msaliti, mwenye wivu, mshindanaji hata kama kwa nje hatakuwa haonekani lakini moyoni mwake hivyo vyote anavyo. Kwahiyo kukwepa kulipa zaka ni uthibitisho wa kukosa Roho, na wote wasio na Roho wa Mungu biblia imesema hao sio wake (soma Warumi 8:9), na kama sio wake maana yake watakwenda kuzimu!.

Bwana akubariki.

Mada Nyinginezo:

JE! UNAYO NAFASI MBINGUNI?

KUWA MAKINI NA MITANDAO, NI SHIMO REFU.

JISHUSHE ILI MUNGU AKUHUDUMIE.

UNATAKA KUBARIKIWA? BASI USIKWEPE GHARAMA ZAKE.

Rudi Nyumbani:

 

Print this post

SADAKA YA MALIMBUKO.

Malimbuko ni nini?

Malimbuko maana yake “kitu cha kwanza kuja au kuzaliwa au zao la kwanza”, kwa lugha ya kiingereza “first fruits”…Katika Biblia agano la kale mtoto wa kwanza wa kiume kuzaliwa alikuwa ni malimbuko. Na huyo ni lazima awe malimbuko kwa Bwana.

Mwanzo 49:3 “Reubeni, u mzaliwa wangu wa kwanza, Nguvu zangu, na malimbuko ya uwezo wangu. Umewapita wengine kwa ukuu na kwa nguvu”.

Na sio tu watoto wa kwanza wa kiume, Bali hata wanyama wa kwanza na mazao ya kwanza ya nchi yote hayo yaliitwa malimbuko, na yalipaswa yatolewe pia kwa Bwana.

Mambo ya Walawi 23:9 “Kisha Bwana akanena na Musa, na kumwambia,Nena na wana wa Israeli, uwaambie, Hapo mtakapokuwa mmekwisha ingia hiyo nchi niwapayo, na kuyavuna mavuno yake, ndipo mtakapomletea kuhani mganda wa malimbuko ya mavuno yenu;”

Bwana alituoa maagizo kwa wana wa Israeli wote kutoa malimbuko katika mazao yao, yaani kupeleka sehemu ya kwanza ya mavuno yao nyumbani kwa Mungu, kuonesha shukrani zao mbele za Mungu kwa kupewa mazao..

Kama Bwana asingewapa mvua basi wasingepata hata hicho kidogo, kwahiyo “walimrudishia Bwana sehemu ya kwanza kabisa ya mazao yao”, kuonesha kuwa Mungu ni wa Kwanza na mengine yatafuata.

JE SADAKA YA MALIMBUKO ILIKUWA NA BARAKA YOYOTE?

Jibu ni ndio! ilikuwa na Baraka nyingi, kwasababu siku zote kitu cha Kwanza kumtolea Mungu kina nguvu kuliko cha Pili. Nguo mpya ambayo haijavaliwa na mtu ina thamani zaidi, na heshima zaidi kuliko ile ya Mtumba.

Raisi wa kwanza wa nchi, huwa anayoheshima kubwa Zaidi kuliko maraisi wengine wanaofuata. Kadhalika sadaka ya kwanza kabisa inayofika mbele za Mungu ina nguvu kubwa zaidi kuliko zinazofuata..Na sadaka hiyo ni ya “malimbuko”.

Kadhalika sadaka ya malimbuko ndiyo inayobariki kazi yote inayofuata, mshahara wa malimbuko ndio unaobariki mishahara mingine yote inayofuata. Tutakuja kuona hapo chini kidogo, ni kwa namna gani Kristo aliitwa limbuko lao waliolala, ikasababisha baraka kwa wote watakaolala kama yeye.

JE NI LAZIMA KUTOA MALIMBUKO KATIKA AGANO JIPYA?

Jibu ni ndio! Kama tunalipa sadaka za Zaka, Malimbuko nayo ni lazima..Na baraka zake ni zile zile…Kwamba cha kwanza ni bora kuliko cha pili, haijalishi cha pili kitakuwa na wingi gani..lakini cha kwanza ni cha kwanza tu.

Na pia Roho Mtakatifu ndani yetu anatushuhudia, kwamba hiyo kazi kama Mungu asingeibariki basi tusingepata chochote, kwahiyo tunamheshimu Mungu na kumwonyesha kuwa yeye kwetu ni wa KWANZA kwa vitendo! kwahiyo tunampa Malimbuko yetu.

TUNATOAJE MALIMBUKO?

Kama umeajiriwa au umejiajiri, Mshahara wa Kwanza unaoupata unaupeleka kwa Bwana. Usiogope kupungukiwa, wala usiwaze waze utapata vipi fedha, yeye aliyekupa hiyo kazi anajua zaidi kuliko wewe, anasema maua haifanyi kazi na bado hayasokoti yanazidi kupendeza tu. kitu ambacho hata Sulemani katika fahari yake, hajawahi kuvikwa vizuri kama mojawapo ya hayo!. Kama Mungu anayavisha maua ya kondeni vizuri hivyo je si zaidi sisi?. (Mathayo 6:28)…hivyo usiangalie mazingira yanayokuzunguka mtolee Bwana sehemu ya kwanza.

Kadhalika Faida ya kwanza ya Biashara yoyote iliyo halali uliyojiajiri ni hivyo hivyo, sehemu ya kwanza ya mazao yako ya shambani, kama umevuna debe 10 mpelekee Bwana, mifugo yako imezaa wazaliwa wa kwanza mpelekee Bwana, au ibadilishe katika fedha, uipeleke nyumbani kwa Bwana.

Kumbuka kama umeshatoa mzaliwa wa kwanza wa mfugo wako, hao wengine hupaswi kutoa kama malimbuko. Hao utatoa tu kama sadaka na kwa jinsi Bwana atakavyokujalia. Na kwa jinsi utakavyopenda wewe kutoa, haina masharti!

Kumbuka pia kama umeacha kazi fulani na kwenda kuanza nyingine, ambayo inazalisha kwa namna nyingine, na ina mkataba mwingine wa kukuingizia kipato, hapo ni lazima utoe tena limbuko kwa hiyo kazi mpya ulioanza. Kwa ulinzi wa kazi yako.

YESU KRISTO LIMBUKO LAO WALIOLALA.

Mtu wa Kwanza kufufuliwa alikuwa ni Kristo! Lazaro alifufuliwa lakini alikufa tena…Hivyo ufufuo wake haukuwa na nguvu ya umilele, lakini Yesu alifufuliwa na hawezi kufa tena yupo mpaka leo, kwahiyo yeye ndiye mzaliwa wa kwanza wa walio kufa, (LIMBUKO).

Na kutokana na Mungu kumtoa kaburini na kumleta juu kama Limbuko, amesababisha hata sisi tuliomwamini tutakaofuata kufa kama yeye, nasi pia tupate hiyo ofa ya bure ya kufufuliwa katika siku ile! haleluya!

Hivyo kama sio Mungu kumtoa Yesu kuwa limbuko, baraka ya kufufuliwa sisi wengine tusingekuwa nayo.

1Wakorintho 15:20 “Lakini sasa Kristo amefufuka katika wafu, limbuko lao waliolala.

21 Maana kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na kiyama ya wafu ililetwa na mtu.

22 Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa.

23 Lakini kila mmoja mahali pake; limbuko ni Kristo; baadaye walio wake Kristo, atakapokuja”.

Na pia inasema..

Wakolosai 1:18 “Naye ndiye kichwa cha mwili, yaani, cha kanisa; naye ni mwanzo, ni mzaliwa wa kwanza katika wafu, ili kwamba awe mtangulizi katika yote”.

Hiyo ndiyo faida ya “kutoa sadaka ya malimbuko”, Inakuwa inabariki mazao mengine yaliyosalia..Kama Bwana Yesu alivyotubariki sisi tutakaokufa katika yeye. Tunalotumaini la ufufuo, kwasababu yeye amefanyika kuwa mtangulizi wetu, Na wewe unalo tumaini la kufufuliwa kazi yako upya, au biashara yako, au kilimo chako endapo kitasuasua kama ulitoa limbuko(kama sadaka ya utangulizi)! siku ile ulipoianza hiyo kazi,

Lakini pamoja na hayo yote! haitakufaidia chochote, kama utatoa sadaka ya malimbuko na huku maisha yako yapo nje ya wokovu, huku bado ni mlevi, bado ni msengenyaji, bado ni mtukanaji, bado ni mfanyaji masturbation, na bado kahaba, bado mla rushwa..Mungu wetu hafanyi kazi ya ukusanyaji mapato kwetu,…Kwamba uwe mwovu au usiwe mwovu kodi ni lazima ulipe!.

Hapana Mungu wetu hayupo hivyo, yeye hakusanyi mapato kutoka kwetu kama wafanyavyo TRA kwasababu yeye ana kila kitu tayari, anataka tu! tujifunze kutoa kwa faida yetu wenyewe, kama yeye alivyo mtoaji, na hapendezwi na sadaka ya mtu mwovu, hivyo kama unatoa sadaka na bado mlevi, au kahaba..ni afadhali usitoe kabisa kwasababu ni machukizo mbele za Mungu. Hakuchukii wewe, bali unachotoa kinamchukiza, na anataka tufanye kilicho bora.

Biblia inasema

Kumbukumbu 23:18 “Usilete ujira wa kahaba, wala mshahara wa mbwa, katika nyumba ya Bwana, Mungu wako, kwa ajili ya nadhiri yo yote; kwani haya ni machukizo kwa Bwana, Mungu wako, yote mawili”.

Hivyo kama hujampa Kristo maisha yako umechelewa sana, ni afadhali ufanye hivyo sasa kabla mlango wa Neema haujafungwa, unachotakiwa kufanya ni kutubu kwa kukusudia kuacha kufanya dhambi tena!!, Unaamua kwa vitendo! kuacha ulevi, anasa, uvaaji mbaya, rushwa, na mambo yote machafu kisha unaenda kubatizwa tena! kwasababu kama ulibatizwa na umerudia machafu ya ulimwengu huu, kiasi hata cha kufanya uzinzi na uasherati unapaswa ukabatizwe tena katika maji tele, na kwa jina la Yesu kwa ajili ya ondoleo la dhambi zako kulingana na Matendo 2:38,

kisha baada ya kufanya hivyo Roho Mtakatatifu ataingia ndani yako, na kukupa uwezo wa kushinda dhambi kwa namna ya kipekee.

Baada ya kufanya hivyo, utakuwa umeokoka na kufanyika kuwa mwana wa Mungu, hivyo tafuta kusanyiko la kikristo linalomhubiri Kristo, na maneno yake ya kwenye biblia yenye vitabu 66 na sio vitabu 666, ujiunge hapo!, ili usizimike kiroho. Na Bwana mwenyewe atakusaidia kufanya yaliyosalia, kwasababu Neno lake ni mwanga wa njia zetu.

Ubarikiwe.


Mada Nyinginezo:

ROHO HUTUOMBEA KWA KUUGUA KUSIKOWEZA KUTAMKWA!

NILIMWONA SHETANI, AKIANGUKA KUTOKA MBINGUNI.

BARAGUMU NI NINI?

Je! ni vema kwa mkristo kwenda hospitali au kutumia miti shamba anapougua?

Rudi Nyumbani

Print this post

UTAPENDA KUCHANGIA HUDUMA HII?

Tutamshukuru Mungu kwa ajili yako, kwa mchango wako, ili kuifanya injili hii isonge mbele Tuma sadaka yako kwa namba hizi:
Airtel:+255789001312 -Devis Magembe
Mpesa: +255767992434-Denis Magembe