JE KANISA LITAPITIA DHIKI KUU?

JE KANISA LITAPITIA DHIKI KUU?

Hili ni moja ya swali lenye mtafaruku mkubwa sana miongoni mwa wakristo, na wengi hata wameishia mpaka kugombana kabisa!..Wapo wanaoamini kanisa litapitia dhiki kuu ndipo linyakuliwe na wapo wanaoamini kanisa halitapita dhiki kuu, yaani utaanza kwanza unyakuo ndipo dhiki kuu ifuate.

Kuna kitu kimoja cha kimaandiko ambacho hakijulikani na wengi..nacho ni Mgawanyiko wa ujio wa Kristo;

Ujio huu umegawanyika katika vipengele vikuu 3, mtu akishindwa kuvielewa vipengele hivi basi biblia itamchanganya. Na vipengele hivyo ni kama ifuatavyo.

  1. UJIO WA KWANZA WA KRISTO:

Huu ni ule wakati Kristo alipozaliwa na Bikira Mariamu, na kuishi kwa miaka 33 na nusu na kisha kufa, na kufufuka na kupaa mbinguni alikotoka.

  1. UJIO WA PILI:

Huu utahusisha Kristo kuwapokea wateule wake mawinguni katika tendo maarufu lijulikanalo kama unyakuo. Wakati huo, wafu waliopo makaburini watafufuka wataungana na watakatifu walio hai na kwa pamoja watakwenda mawinguni kumlaki Bwana. Katika Ujio huu Kristo hatashuka duniani, atabaki mawinguni, watakaonyakuliwa ndio watakaokwenda mawinguni kumfuata na kwenda naye mbinguni kwenye makao waliyoandaliwa.

Katika hatua hii ndio litatimia lile neno.. la kwenye Luka 17:34

“Nawaambia, usiku huo watu wawili watakuwa katika kitanda kimoja; mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. 

35 Wanawake wawili watakuwa wakisaga pamoja; mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa. 

36 Watu wawili watakuwa shambani, mmoja atatwaliwa, mmoja ataachwa”.

Vilevile lile Neno “atakuja kama mwivi usiku”, ndio litatimia katika hatua hii..Pengine utakuwa umelala na mume wako/mke wako aliyeokoka  na ghafla! utapoamka asubuhi hutamkuta kitandani. n.k. 

Huu hautakuwa ujio wa kila jicho kumwona Yesu, kwasababu hatakuja kwa hukumu bali kwa ajili ya kuwachukua wateule wake na kwenda nao mbinguni kwenye karamu aliyowaandalia, ili kuwaepusha na dhiki ambayo itakwenda kuanza duniani muda sio mrefu. Dhiki ambayo inajulikana kwa jina lingine kama saa ya kuharibiwa ulimwengu!.

Ufunuo 3:10 “Kwa kuwa umelishika neno la subira yangu, mimi nami nitakulinda, utoke katika saa ya kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi”.

Sasa huo sio wakati wa kila jicho kumwona Yesu mawinguni, wakati wa kila jicho kumwona utakuwa ni wakati wa ujio wa tatu, ambao tutauona mbele kidogo.

Sasa kabla ya kwenda hatua ya mwisho ya Ujio wa tatu, hebu tujiulize maswali machache juu ya huu ujio wa pili.

  • Hebu jiulize kama Ujio huu wa pili wa Kristo (yaani unyakuo wa kanisa) utahusisha kila jicho kumwona Yesu, vipi kuhusu hao waliolala vitandani wakati wa kuja kwake?..Je wakati wa kuja kwake, watazinduka usingizini na kumwona Bwana mawinguni?..kama ndivyo basi sentensi hii itakuwa haina maana>> “wawili watakuwa wamelala mmoja atatwaliwa mmoja ataachwa”. 

Na wakati wa kila jicho kumwona Kristo, biblia inasema Mataifa yote wataomboleza..na milima itahama na visiwa, kutakuwa na tetemeko kubwa la nchi, na jua litazima na mwezi utakuwa mwekundu kama damu. Kwa ufupi mwisho wa dunia utakuwa umefika..Sasa kama mambo hayo yote yatatokea katika siku ile ya unyakuo, ni nani atakuwa amelala kitandani, au yupo shambani analima, katikati ya dhiki kubwa namna hiyo, huyo mpinga-Kristo atatokea wapi na atawapa watu chapa muda gani?.. 

Kwahiyo ni wazi kuwa siku ya unyakuo ni nyingine na siku ya Ujio wa Kristo ambao kila jicho litamwona nayo ni nyingine. Haiwezekani siku ya unyakuo ndio iwe siku hiyo hiyo ya kila jicho kumwona, na visiwa na milima kuhama.

Sasa twende hatua ya mwisho ya tatu.

UJIO WA TATU:

Baada ya unyakuo kupita katika ujio wa pili, baadhi ya watu watatoweka, na dunia haitaelewa chochote, wengi watahisi watu wamepotea tu, kama ilivyo kawaida ya watu kupotea potea na kupatikana, na wengine wengi watajua ni habari za kuzusha tu!..taarifa chache zitafika vituoni, lakini mwisho zitaishia kupuuziwa… Kama baadhi ya taarifa za watu kupotea zinavyopuuzwa leo. Pasipo kujua kuwa Kristo tayari kashalinyakua kanisa lake (kundi dogo). Na siku hiyo hakutakuwa na ishara yoyote angani, wala jua halitazima..kutakuwa na ukimya tu kama wa siku zote.

Sasa katikati ya hicho kipindi, ndio utakuwa wakati wa mpinga-kristo kunyanyuka…Ndani ya miaka mitatu na nusu ya kwanza (yaani miezi 42), utakuwa ni wakati wa mpinga-kristo kuwadanganya watu waipokee chapa yake..wengi wataipokea chapa pasipo kujua, wakidhani ni mfumo mpya tu! Wa kimaendeleo umezuka, ambao utasaidia watu kutambulika kirahisi..Utakubalika duniani kwa muda mfupi sana, kiasi kwamba mtu atakayeukataa atakuwa anaenda kinyume na serikali, hivyo atatafutwa na kusingiziwa mambo yasiyofaa.

 Wachache sana wataipokea kwa kujua, kwa kujua kabisa kwamba hii ni chapa, lakini wengi hawatajua..kwasababu mpinga-kristo hatakuwa mtu mwenye mapembe kama watu wanavyofikiri, bali atakuwa ni mtu mwenye ushawishi mkubwa sana wa kisiasa, kidini, kiuchumi na kijeshi, na anatakua ni mtu anayeshika biblia!. Hivyo hatajulikana na wengi kuwa ndiye mpinga-kristo mwenyewe, kwasababu ataheshimika kama kiongozi wa dini, atakayeleta amani..hivyo atapewa nguvu na dunia nzima.

Baada ya miaka mitatu na nusu  ya kwanza kuisha, wale wachache ambao wataikataa chapa  yake hiyo ndio watakaoanza kuipitia DHIKI KUU, wengine hawataguswa!..wataendelea na shughuli zao za KUUZA NA KUNUNUA bila usumbufu!…Lakini walioikataa  watajaribu kujificha lakini watakamatwa na kupewa shutuma za uongo na hivyo kukusanywa katika magereza maalumu ya mateso…wakiwa humo watateswa mateso ambayo hayajawahi kutokea tangu dunia kuumbwa…na watamani kufa lakini wale waliowafunga hawatawaua mapema!!…

Lakini mwisho wa siku watakufa wote….na karibia na mwisho  ya hiyo miaka mitatu na nusu ya mwisho, wataisha wote…Ndipo Mungu ataanza kuwapiga wanadamu wote waliopokea hiyo chapa ya mnyama kwa yale mapigo ya VITASA SABA, tunayoyasoma katika ufunuo 16. Kwahiyo DHIKI KUU, itaongezewa juu yake vitasa saba..Na Mwisho kabisa, miaka hiyo ya dhiki na vitasa itakapoisha, biblia inasema Jua litatiwa giza, na mwezi utakuwa mwekundu kama damu, Ishara ya mwana wa Adamu itaanza kuonekana mbinguni..

Bwana Yesu mwenyewe Mfalme wa wafalme  atatokea mawinguni pamoja na jeshi kubwa na watakatifu walionyakuliwa…Atashuka kwa ajili ya vita vya Harmagedoni, na kwaajili ya utawala wa miaka elfu duniani.

Sasa siku hii kwa wale wachache ambao watakuwa wamesalia duniani, ambao waliipokea chapa lakini hawakufa katika mapigo ya vitasa saba..Wataona umeme ukimulika kutoka mashariki hata magharibi!..na dunia yote itakuwa giza ghafla (jua litazimwa)!…Na watamwona Kristo mawinguni, uso wake uking’aa kuliko jua…Hofu kuu itawaangukia wataomboleza kwa hofu, biblia inasema watatamani milima iwaangukie..

Mathayo 24:29 “Lakini mara, baada ya dhiki ya siku zile, jua litatiwa giza, na mwezi hautatoa mwanga wake, na nyota zitaanguka mbinguni, na nguvu za mbinguni zitatikisika; 

30 ndipo itakapoonekana ishara yake Mwana wa Adamu mbinguni; ndipo mataifa yote ya ulimwengu watakapoomboleza, nao watamwona Mwana wa Adamu akija juu ya mawingu ya mbinguni pamoja na nguvu na utukufu mwingi 

31 Naye atawatuma malaika zake pamoja na sauti kuu ya parapanda, nao watawakusanya wateule wake toka pepo nne, toka mwisho huu wa mbingu mpaka mwisho huu.”.

Soma tena…

Ufunuo 6:12 “Nami nikaona, alipoifungua muhuri ya sita, palikuwa na tetemeko kuu la nchi; JUA LIKAWA JEUSI KAMA GUNIA LA SINGA, MWEZI WOTE UKAWA KAMA DAMU, 

13 na nyota zikaanguka juu ya nchi kama vile mtini upukutishavyo mapooza yake, utikiswapo na upepo mwingi. 

14 Mbingu zikaondolewa kama ukurasa ulivyokunjwa, na kila mlima na kisiwa kikahamishwa kutoka mahali pake. 

15 Na wafalme wa dunia, na wakuu, na majemadari, na matajiri, na wenye nguvu, na kila mtumwa, na mwungwana, wakajificha katika pango na chini ya miamba ya milima, 

16 WAKIIAMBIA MILIMA NA MIAMBA, TUANGUKIENI, TUSITIRINI, MBELE ZA USO WAKE YEYE AKETIYE JUU YA KITI CHA ENZI, NA HASIRA YA MWANA-KONDOO. 

17 Kwa maana siku iliyo kuu, ya hasira yao, imekuja; naye ni nani awezaye kusimama?.

Sasa utauliza hao wateule ambao Bwana atawakusanya wakati wa kutokea mawinguni kwa utukufu mwingi ni wakina nani?

Hao watakuwa ni Wayahudi 144,000, waliotiwa muhuri wa Mungu baada ya kuisikia ile injili ya manabii wawili wa kwenye Ufunuo 11, hivyo walifichwa mbali na mpinga-kristo na dhiki ya vitasa (Ufunuo 12:14-15). Kundi hili la wayahudi 144,000 ambao walifichwa mbali na yule joka…Ndio wanaoitwa wateule..

Hawa wakati Kristo atakaokuja ndio watakaokusanywa kutoka pepo nne, na kuletwa juu ya mlima Sayuni uliopo pale Israeli..(Ufunuo 14:1 “ Kisha nikaona, na tazama, huyo Mwana-Kondoo amesimama juu ya mlima Sayuni, na watu mia na arobaini na nne elfu pamoja naye, wenye jina lake na jina la Baba yake limeandikwa katika vipaji vya nyuso zao”). 

Kwahiyo sio kanisa ambalo litakusanywa kutoka pembe nne, bali ni wayahudi hao 144,000, ambao waliisikia ile injili iliyohubiriwa na wale manabii wawili katika Ufunuo 11, na kutiwa muhuri wa Mungu juu ya vipaji vya nyuso zao…Kanisa tayari lilikuwa utukufuni, na ndio linalorudi na Kristo hapa!.

Sasa upo utata mmoja maarufu katika Ufunuo 7:9-16..Tusome 

“ 9  Baada ya hayo nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi, na mbele za Mwana-Kondoo, wamevikwa mavazi meupe, wana matawi ya mitende mikononi mwao;

 10  wakilia kwa sauti kuu wakisema, Wokovu una Mungu wetu aketiye katika kiti cha enzi, na Mwana-Kondoo…………………………

13 Akajibu mmoja wa wale wazee akiniambia, Je! Watu hawa waliovikwa mavazi meupe ni akina nani? Na wametoka wapi? .

14  Nikamwambia, Bwana wangu, wajua wewe. Akaniambia, Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.

15  Kwa hiyo wako mbele ya kiti cha enzi cha Mungu, nao wanamtumikia mchana na usiku katika hekalu lake, na yeye aketiye katika kiti cha enzi atatanda hema yake juu yao. 

16  Hawataona njaa tena, wala hawataona kiu tena, wala jua halitawapiga, wala hari iliyo yote”

Mstari huu ndio unaowafanya wengi wahitimishe kwamba dhiki kuu itaanza ndipo tuende mbinguni…Lakini hebu soma vizuri mstari huo wa 9 unasema “nikaona, na tazama, mkutano mkubwa sana ambao hapana mtu awezaye kuuhesabu, watu wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha, wamesimama mbele ya kile kiti cha enzi”.

Hapa ni mbinguni baada ya unyakuo…na sio kundi moja la watu Fulani tu! Bali ni la watu wote (sio tu walio hai) bali hata waliokufa katika Kristo katika vizazi vyote vya nyuma, wakina Petro waliokatwa vichwa, wakina Stephano waliopigwa mawe, wakina Perpetua waliopitia dhiki za kuwekwa kwenye maarena na kufunguliwa Wanyama wakali, wakina Polikapi waliochomwa moto, wakina Antipa na wengine wengi na hata wakristo wote wanaopitia dhiki za kiimani hata sasa ambao watakuwa hai mpaka ile siku ya kunyakuliwa….

Sasa wote hawa kwa pamoja ndio wanaolijenga hilo jeshi kubwa hapo juu la Ufunuo 7…Kwahiyo hilo sio kundi moja tu la watu Fulani tu wachache!..bali ni la watu wa vizazi vyote waliokufa katika Kristo(Na mbele za Mungu, ni washindi wa dhiki za ulimwengu, kama Bwana Yesu alivyosema “ulimwenguni mnayo dhiki”). Mbinguni hakutakuwa na makundi mawili; ya waliopitia dhiki na ambao hawajapitia dhiki, ndio maana unaona hapo hakuna makundi mawili, bali kundi moja tu!.

Huo ni ufupisho tu kwa yatakayotokea siku za mwisho…Hivyo kwa hitimisho ni kwamba kanisa halitapitia Dhiki kuu ya mpinga-kristo… “litaepushwa na saa ya kuharibiwa”..watakaopitia dhiki kuu ya mpinga-kristo ni wale watakaoachwa kwenye unyakuo..na watauawa na mpinga-kristo (na hawatakuwa miongoni mwa watakaokwenda mbinguni), wataikosa karamu ya Mungu mbinguni ingawa wakati wa Kristo kurudi na watakatifu, watafufuliwa na kuingia katika utawala wa miaka elfu hapa duniani.

Na siku ya unyakuo sio siku ya kila jicho kumwona Yesu mawinguni, sio siku ya mataifa yote kuomboleza.

Sasa ni kitu gani kinachowafanya watu wachanganyikiwe?

Ni kwasababu ya kutoelewa kalenda ya Neno la Mungu…Ni wachache sana wanalijua na kulielewa andiko la kwenye Warumi 11, linalozungumzia Upofu waliopigwa Wayahudi (yaani waisraeli). Upofu huo walipigwa wasimwamini Masihi, Yesu Kristo ili sisi watu wa mataifa tupate Neema (hebu tenga muda binafsi soma taratibu Warumi 11 yote).

Kutokana na upofu waliopigwa iliwafanya wasimwamini kabisa Yesu, na kujikuta wakimtazamia Masihi mwingine. Na sisi watu wa Mataifa ikawa ni nafasi kwetu kumwamini, kwani wale mitume ambao walipaswa watumwe kwa wayahudi walikuja kwetu na sisi tukamwamini Yesu, macho yetu yakafunguliwa..tukaipokea hiyo neema. Na tumekaa na hiyo neema sasa kwa Zaidi ya miaka 2,000, ndio maana huoni ugumu leo kuhubiri injili ya Yesu na watu wakamwamini kirahisi tu!..Neema hii haipo kwa Waisraeli unaowaona leo!..Ukienda Israeli ukiwaeleza Habari za Yesu, wanakuona ni mwendawazimu…wanakupinga kabisa!..ni wachache sana wanaomwamini, lakini Zaidi ya asilimia 90 ya waisraeli wanamkataa Yesu. Na hiyo ni kutokana na upofu waliopigwa..yaani neema waliyopokonywa ili tupewe sisi.

Lakini biblia inasema katika hiyo hiyo warumi 11…kwamba hawatakuwa katika hiyo hali ya kutomwamini Yesu milele. Itafika siku ambapo macho yao yatafumbuliwa..Siku hiyo itakuwa ni zamu ya watu wa mataifa kupitia ukame wa rohoni kama wanayoipitia sasa waisraeli.

Siku hiyo itakuwa ni siku ya Neema ya wokovu kuondoka kwa watu wa Mataifa milele na kuhamia Israeli. Sasa Neema hiyo itahitimishwa na tukio la unyakuo. Kristo atakapolinyakua tu kanisa lake, na Mlango wa Neema siku hiyo hiyo utakuwa umefungwa kwa watu wa Mataifa na kubakia kwa waisraeli peke yao. Huku hata mtu aombe vipi, hakuna rehema. Roho Mtakatifu atahamia kwa Waisraeli, watahuzunika sana na kujilaumu ilikuwaje kuwaje mpaka wakamkataa Masihi kwa miaka yote hiyo…

Kwa kupitia injili ya wale manabii wawili, ndio watapatikana idadi ile 144,000 (Haijulikani kama ndio namba kamili,  au ni ya kuwakilishi tu, kwamba idadi inaweza kuwa kubwa Zaidi ya hiyo). Lakini hao tu ndio watakaosalimika, ndio wateule,  na watakusanywa katika Mlima Sayuni.

Warumi 11:25  “Kwa maana, ndugu zangu, sipendi msiijue siri hii, ili msijione kuwa wenye akili; ya kwamba kwa sehemu ugumu umewapata Israeli, mpaka utimilifu wa Mataifa uwasili. 

26  Hivyo Israeli wote wataokoka; kama ilivyoandikwa, Mwokozi atakuja kutoka Sayuni; Atamtenga Yakobo na maasia yake. 

27  Na hili ndilo agano langu nao, Nitakapowaondolea dhambi zao”.

Sasa hapa kwenye WAKATI WA MATAIFA na WAKATI WA WAYAHUDI, ndiko kunakowafanya watu washindwe kuuelewa ujio wa Bwana.  Asilimia kubwa ya watu hawajui kuwa kuna wakati wa Wayahudi kurudiwa na kumwamini  mwokozi…wengi wanajua tu! Kuna unyakuo basi!…kwamba baada ya unyakuo hakuna chochote kitakachoendelea, na wanaamini kuwa mbinguni tutakaa huko milele, wala hakuna wakati tutarudi tena huko..Hawajui kwamba kuna utawala wa miaka elfu wa kutawala na Kristo duniani unatungoja. N.k

Tukiyajua hayo..huu sio wakati wa kucheza na Neema tuliyopewa sisi watu wa mataifa hata kidogo…Sasahivi unaweza kusikia injili, ukaikataa kwa mdomo lakini moyoni mwako ukashuhudiwa kwamba ni kweli yanayozungumzwa…Hicho kinachokushuhudia ndani yako ni sauti ya wito wa Mungu (Ni neema ya Mungu bado inatuita)..Itafika kipindi itaondoka kabisa…itahamia Israeli.. na hiyo sauti ya Roho Mtakatifu itakapoondoka..Ndipo mpinga-kristo atafunuliwa.

2Wathesalonike 2:7  “Maana ile siri ya kuasi hivi sasa inatenda kazi; lakini yuko azuiaye sasa, hata atakapoondolewa. 

8  Hapo ndipo atakapofunuliwa yule asi, ambaye Bwana Yesu atamwua kwa pumzi ya kinywa chake, na kumwangamiza kwa ufunuo wa kuwapo kwake”

Bwana atubariki.                  

Group la whatsapp Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia masomo haya kwa njia ya email yako au Whatsapp tutumie ujumbe kwenye box la maoni chini au piga namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

MAJONZI YA MTUME PAULO KWA NDUGU ZAKE.

YONA: Mlango wa 3

NA YEYE ALIYEKETI JUU YA WINGU AKAUTUPA MUNDU WAKE JUU YA NCHI, NCHI IKAVUNWA.

Kile kinara cha Taa ndani ya Hekalu la Sulemani kilikuwa kinawakilisha nini?

YAKINI NA BOAZI.

NEEMA YA MZALIWA WA PILI.

MKUMBUKE MKE WA LUTU.

JINSI SODOMA NA GOMORA ILIVYOKUWA INAVUTIA SANA..

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
7 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
SAMWELI MSAFIRI
SAMWELI MSAFIRI
2 years ago

MUNGU AKUBARIKI SANA MTUMISHI WA MUMGU

Anonymous
Anonymous
2 years ago

amen

ELIBARIKI NELSON SHUKIA
ELIBARIKI NELSON SHUKIA
2 years ago

Naomba kutumiwa somo hili la dhiki kuu

0755680520.

Hongereni kwa somo zuri na lenye baraka

Anonymous
Anonymous
3 years ago

Bwana Yesu apewe sifa mtumishi wa MUNGU ubarikiwe Sana kwa SoMo zuri nimengi nimejifunza kiasi kwamba sitabaki Kama nilivyokuwa naweza hata kuwaelekeza wengine napenda, niendelee kujifunza kwakunitumia mafundishisho yako
Namna ya WhatsApp 0744004103
Imail sadicksteven59@mail.com