Title November 2020

Bisi ni nini? (Walawi 23:14, Ruthu 2:14)

Bisi ni nini?


Kama wengi tunavyofahamu bisi kwa mazingira yetu ni yale mahindi yanayokaangwa na kufutuka na pale yanapobadilika na kuwa na mwonekano mwingine (mweupe mweupe ) huliwa. Kwa wengine wamezoea kuyaita Popcorn lugha ya kigheni. Tazama picha kushoto.

Lakini kwa wayahudi, na jamii nyingi za watu wa mashariki ya kati, bisi zao haziwi kama hizi zetu za mahindi bali zao zinakuwa za ngano, na zinakaangwa vile vile kama zinavyokaangwa za mahindi isipokuwa tu  mwonekano wake haubadilika sana, kama ulivyo  wa mahindi.

Kuona jinsi inavyoandaliwa na mwonekano wake, tazama video hii >>>

https://www.youtube.com/watch?v=5fSY4YCVSoM

bisi za nganoHivyo mahali popote unapokutana na neno hili Bisi kwenye biblia basi ujue ni hii inayotengenezwa kwa ngano, na sio mahindi.

Kwamfano ukisoma biblia, utaona, Mungu anawapa wana wa Israeli maagizo kuwa pindi watakapovuna mavuno yao ya kwanza, wasile kwanza chochote katika walichokivuna, ikiwemo bisi, au masuke, mpaka watakapoleta kwanza kile kinachomstahili Mungu.

Walawi 23:14 “Nanyi msile mkate, wala bisi, wala masuke machanga, hata siku iyo hiyo, hata mtakapokuwa mmekwisha kuleta sadaka ya Mungu wenu; hii ni amri ya milele katika vizazi vyenu katika makao yenu yote”.

Utalisoma Neno hilo tena katika vifungu hivi;

Ruthu 2:14 “Tena wakati wa chakula huyo Boazi akamwambia, Karibu kwetu, ule katika mkate wetu, na ulichovye tonge lako katika siki yetu. Basi akaketi pamoja na wavunaji, nao wakampitishia bisi, naye akala akashiba, hata akasaza”.

1Samweli 17:17 “Ndipo Yese akamwambia Daudi mwanawe, Haya! Sasa uwachukulie ndugu zako efa ya bisi, na mikate hii kumi, ipeleke upesi kambini kwa ndugu zako;

18 ukampelekee akida wa elfu yao jibini hizi kumi, ukawaangalie, wa hali gani, kisha uniletee jawabu yao.

1Samweli 25:18 “Ndipo Abigaili akafanya haraka, akatwaa mikate mia mbili, na viriba viwili vya divai, na kondoo watano waliofanyizwa tayari, na vipimo vitano vya bisi, na vishada mia vya zabibu, na mikate ya tini mia mbili; akavipakia vitu hivi juu ya punda.

19 Akawaambia vijana wake, Haya! Tangulieni mbele yangu; angalieni, mimi nawafuata. Ila hakumwambia mumewe, Nabali.

Yoshua 5:10 “Basi wana wa Israeli wakapanga hema zao huko Gilgali; nao wakala sikukuu ya pasaka siku ya kumi na nne ya mwezi, jioni, katika nchi tambarare za Yeriko.

11 Nao wakala katika mazao ya nchi siku ya pili ya kuiandama hiyo sikukuu ya pasaka, mikate isiyotiwa chachu, na bisi, siku iyo hiyo”.

Soma pia, 2Samweli 17:28,

Je! Tunapaswa tukumbuke nini, kila tunapolisoma hili Neno?

Ni kwamba hata sisi, kwa kila Mungu anachotubariki, tusifikirie kula kwanza, mpaka tutakapohakikisha fungu la Mungu tumelitenga na kulitoa. Biblia imetumia neno bisi,  kwasababu ni chakula chepesi sana kukipika, ni kitendo cha kuweka kwenye sufuria na kukikaanga na kula, jambo ambalo halihitaji maandalizi mengi kuandaa, tofauti na vyakula vingine vya ngano, hii ikiwa na maana kuwa mtu anaweza kuvuna shamba lake, na hapo hapo akaenda kuchukua ngano hiyo na kukaanga mara moja na kula. Lakini hata hivyo Mungu kakataza. .. Hivyo na sisi, hatupaswi kufikiria kutumia hata  kwa vocha au kwa chipsi kile Mungu anachotubariki, kabla hatujalitenga fungu lake pembeni.

Hivyo ndio Mungu atakavyotubariki.

Shalom.

Tazama maana ya maneno mengine ya biblia chini.

 Pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

Masuke ni nini? (Luka 6:1, Marko 4:28)

Kuwiwa maana yake nini katika biblia?

Choyo ni nini kibiblia? (Luka 12:15, Zaburi 10:3)

USITAFUTE KUKANWA NA BWANA SIKU ILE.

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita..

Rudi Nyumbani:

Print this post

Jaa ni nini katika biblia?

“Jaa” ni nini katika biblia?

Jaa ni mahali ambapo uchafu unalundikwa, na uchafu huo unaweza kuwa ni kinyesi cha wanyama (yaani mbolea), au uchafu unaotokana na shughuli za kibinadamu (matakataka). Hivyo Jaa ni kama kifupi cha jalala tu.

Katika biblia tunaona neno hili likitumika..

Zaburi 133: 7 “Humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Na kumpandisha maskini kutoka jaani”.

Maana yake Bwana anaweza kumpandisha mtu kutoka majalalani na kumpandisha juu.

Ezra 6: 11 “Pia nimetoa amri kwamba, mtu awaye yote atakayelibadili neno hili, boriti na itolewe katika nyumba yake, akainuliwe na kutungikwa juu yake; tena nyumba yake ikafanywe jaa kwa ajili ya neno hili”.

Isaya 25: 10 “Kwa maana mkono wa Bwana utatulia katika mlima huu, na Moabu atakanyagwa chini huko aliko, kama vile majani makavu yakanyagwavyo katika MAJI YA JAA

Pia unaweza kusoma Danieli 2:5, Danieli 3:39, Maombolezo 4:5 na 1Samweli 2:8.

Katika Agano jipya neno hili limetumika mara moja tu, na Bwana Yesu Kristo katika kitabu cha Luka..

Tusome..

Luka 14:34  “Chumvi ni kitu chema; lakini chumvi ikiwa imeharibika, itiwe nini ikolee?

35  Haiifai nchi WALA JAA; watu huitupa nje. Mwenye masikio ya kusikilia, na asikie”

Kinyesi cha wanyama kikizidi kuharibika kinafaa katika mbolea, watu wanakikusanya na kukifunya mbolea baadaye, hali kadhalika takatata nyingine zote zinavyozidi kuharibika huwa hazikosi matumizi, zinaweza hata kutumika katika kuzalishe gasi ya asili, ambayo itatumika kama nishati..

Lakini chumvi ni kitu cha ajabu, ikishaharibika huwezi kuitumia kwa matumizi yoyote yale, huwezi kuitumia kwenye chakula, wala huwezi kuitumia kama mbolea, wala huwezi kuilundika pamoja na kutengeneza jalala na kuzalisha gesi, …Kwaufupi inakuwa kama mchanga tu..

Sasa Bwana Yesu alitufananisha sisi, tuliompokea yeye na chumvi..

Mathayo 5:13  “Ninyi ni chumvi ya dunia; lakini chumvi ikiwa imeharibika itatiwa nini hata ikolee? Haifai tena kabisa, ila kutupwa nje na kukanyagwa na watu.

14  Ninyi ni nuru ya ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika ukiwa juu ya mlima”.

Umeona? Bwana anatuonya, tujihadhari tunavyoenenda katika hii dunia, matendo yetu yasije yakatuharibia sifa zetu moja kwa moja, hata tusifae tena mbele za Mungu na wanadamu.

Kwa urefu juu ya somo hili la chumvi fungua hapa >> NYINYI NI CHUMVI

Je umempokea Yesu?..Kama bado, Kristo yupo mlangoni kurudi kulinyakua kanisa lake, biblia inasema atakuja kama mwivi usiku wa manane, maana yake ni hii, wakati watu na ulimwengu unahisi bado sana, kumbe huo ndio wakati wa kurudi Kristo kulichukua kanisa lake,

Swali ni je!..Bwana Yesu akija leo, una uhakika wa kwenda naye mawinguni?. Kama huna uhakika basi huo ni uthibitisho kwamba hutaenda naye atakapokuja. Hivyo tubu leo kwa dhati na amua kuanza maisha mapya na Kristo, naye atakupokea na kukupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

Nini tofauti kati ya Husuda, faraka na uchafu?

IMANI NI KUWA NA UHAKIKA WA MAMBO YATARAJIWAYO.

IJUE NGUVU YA IMANI.

KILA KIUNGO LAZIMA KISHUGHULIKE.

TUMEPEWA AMRI YA KUKANYAGA NGE NA NYOKA.

Rudi Nyumbani:

Print this post

NYAYO TUNAZOPASWA KUZIFUATA.

Shalom, Jina la Bwana Yesu libarikiwe, karibu tuyatafakari maandiko pamoja..

Ukifika mahali umepotea, na huoni mtu hata mmoja mbele yako wa kukupa msaada, lakini unapotazama chini, unaona nyayo za miguu zinaelekea upande fulani..bila shaka hatua inayofuata ni kuzifuata hizo nyayo, kwasababu unajua mwisho wa hizo nyayo ni kumfikia huyo mtu alipo.

Na Kristo sasa hayupo hapa duniani kwa namna ya mwili, yupo juu mbinguni..lakini katuachia nyayo…ambazo katika hizo tukizifuata tutamfikia yeye na kumwona macho kwa macho.

Sasa nyanyo hizo ni zipi?

Neno la Mungu linasema..

1Petro 2:20  “Kwa maana ni sifa gani kustahimili, mtendapo dhambi na kupigwa makofi? Lakini kustahimili, mtendapo mema na kupata mateso, huu ndio wema hasa mbele za Mungu.

21  Kwa sababu ndio mlioitiwa; maana Kristo naye aliteswa kwa ajili yenu, AKAWAACHIA KIELELEZO, MFUATE NYAYO ZAKE.

22  Yeye hakutenda dhambi, wala hila haikuonekana kinywani mwake.

23  YEYE ALIPOTUKANWA, HAKURUDISHA MATUKANO; alipoteswa, hakuogofya; bali alijikabidhi kwake yeye ahukumuye kwa haki”.

Tunapokuwa wapole kama Yesu alivyokuwa hapo tunaziendea nyayo zake, katika hii dunia iliyojaa upotofu, tunapostahimili mabaya, tunapotukanwa haturudishi majibu kama yeye, tunapoudhiwa ni lazima tusamehe..hapo tunazifuata nyanyo zake..na tutakapomaliza mwendo tukiwa tumezifuata nyayo hizo ni lazima tutamfikia hatutapotea.

Lakini sasa kuna nyayo nyingi duniani, kila mtu anatengeneza nyayo zake…mfano wa nyayo potofu ni hizi zinazosema… “mpende akupendaye, asiyekupenda mchukie”.. Hizi ni nyayo ambazo zinaonekana ni za faraja na za kujilinda, lakini ni nyayo potofu, mwisho wake ni upotevuni…Mwisho wake ni ziwa la moto.

Hivyo tusijifanye tunajua kumsahihisha Bwana Yesu Kristo na kufikiri, hakupaswa kuwa mpole vile… Siku zote fahamu kuwa Yesu alikuwa na uwezo wa kuwapoteza maadui zake pale kwa dakika moja tu, wala hakuna mtu ambaye angeweza kumgusa. Lakini hakuutumia huo uwezo kwasababu lengo lake ni hao watu watubu kwa wema wake..

Ndicho kitu Yesu anachotaka kwetu pia, kwamba kwa wema wetu, wengi wavutwe kwake…Lakini kama tukijiona kwamba sisi tuna ufunuo kuliko yeye, kwamba hatupaswi kuwa wapole, na wanyenyekevu, hatupaswi kuwa watu wa kusamehe wanaotuudhi,  hizo njia tunazoziendea tutajikuta kwenye ziwa la moto.

Mathayo 26:51  “Na tazama, mmoja wao waliokuwa pamoja na Yesu akanyosha mkono wake, akaufuta upanga wake, akampiga mtumwa wa Kuhani Mkuu, akamkata sikio.

52  Ndipo Yesu akamwambia, Rudisha upanga wako mahali pake, maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.

53  Ama wadhani ya kuwa mimi siwezi kumsihi Baba yangu, naye ataniletea sasa hivi zaidi ya majeshi kumi na mawili ya malaika?”

Soma tena..

Luka 9:52  “akatuma wajumbe kutangulia mbele ya uso wake; wakaenda wakaingia katika kijiji cha Wasamaria, ili kumtengenezea mahali.

53  Lakini wenyeji hawakumkaribisha kwa vile alivyouelekeza uso wake kwenda Yerusalemu.

54  Wanafunzi wake Yakobo na Yohana walipoona hayo, walisema, Bwana, wataka tuagize moto ushuke kutoka mbinguni, uwaangamize; [kama Eliya naye alivyofanya]?

55  Akawageukia, akawakanya. [Akasema, Hamjui ni roho ya namna gani mliyo nayo.]

56  Kwa maana Mwana wa Adamu hakuja kuziangamiza roho za watu, bali kuziokoa. Wakaondoka wakaenda mpaka kijiji kingine”.

Bwana atupe macho ya kuona nyayo zake, na kuzifuatia katika Jina la Yesu.

Maran atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

kwanini yule kijana aliitupa ile nguo ya kitani chini na kukimbia uchi?

JIKANE NAFSI MTEULE WA MUNGU.

CHUKIZO LA UHARIBIFU

MZAZI, JALI MAISHA YA KIROHO YA MTOTO WAKO.

Rudi Nyumbani:

Print this post

Kuwiwa maana yake nini katika biblia?

Neno kuwiwa maana yake ni “kudaiwa”.  Mtu anaposema ninawiwa kiasi fulani cha fedha maana yake ni “anadaiwa kiasi fulani cha fedha”, Au mtu anaposema ninamuwia mtu fedha, maana yake ni “anamdai mtu kiasi fulani cha fedha”. Hivyo kuwiwa/kuwia ni neno la kiswahili cha zamani lenye maana ya kudai au kudaiwa.

Katika biblia tunaona mifano kadhaa ambapo neno hili lilitumika.

Mathayo 18: 22  “Yesu akamwambia, Sikuambii hata mara saba, bali hata saba mara sabini.

23  Kwa sababu hii ufalme wa mbinguni umefanana na mfalme mmoja aliyetaka kufanya hesabu na watumwa wake.

24  Alipoanza kuifanya, aliletewa mtu mmoja awiwaye talanta elfu kumi.

25  Naye alipokosa cha kulipa, bwana wake akaamuru auzwe, yeye na mkewe na watoto wake, na vitu vyote alivyo navyo, ikalipwe ile deni

26  Basi yule mtumwa akaanguka, akamsujudia akisema, Bwana, nivumilie, nami nitakulipa yote pia.

27  Bwana wa mtumwa yule akamhurumia, akamfungua, akamsamehe ile deni”.

Mistari mingine katika biblia yenye neno hilo “kuwiwa” ndani yake ni Luka 16:7 na Warumi 13:8.

Mbali na hilo, Biblia inatufundisha kuwa baada ya kuokoka na sisi pia tunakuwa na deni la kwenda kuwapelekea wengine habari za wokovu. Hivyo tunakuwa TUNAWIWA na watu wa ulimwengu habari za wokovu.

Hivyo hatuna budi kuipeleka injili kwa wengine, ambao wapo nje ya wokovu, kwa karama zetu, kwa  mali zetu na kwa nguvu zetu, kwasababu hilo ni deni kwetu.

Kama Mtume Paulo alivyosema mahali fulani kwamba ANAWIWA na watu wa aina mbali mbali, katika kuwapelekea injili..

Warumi 1:13  “Lakini, ndugu zangu, sipendi msiwe na habari, ya kuwa mara nyingi nalikusudia kuja kwenu, nikazuiliwa hata sasa, ili nipate kuwa na matunda kwenu ninyi pia kama nilivyo nayo katika Mataifa wengine.

14  NAWİWA NA WAYUNANİ na wasio Wayunani, NAWİWA na wenye hekima na wasio na hekima.

15  Kwa hiyo, kwa upande wangu, mimi ni tayari kuihubiri Injili hata na kwenu ninyi mnaokaa Rumi.

16  Kwa maana siionei haya Injili; kwa sababu ni uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa Myahudi kwanza, na kwa Myunani pia”.

Hivyo pia na sisi baada ya kuokoka ni wajibu wetu, kuipeleka injili kwa watu ambao hawajaokoka, roho zao ni deni kwetu, kwahiyo ni lazima kuwapelekea habari njema za wokovu pasipo kuionea haya injili, kwasababu injili ni uweza wa Mungu uletao wokovu.

Marko 16: 15  “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe.

16  Aaminiye na kubatizwa ataokoka; asiyeamini, atahukumiwa”.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

Kwanini Mungu hakumuua Nyoka, akamwacha Hawa ajaribiwe katika bustani ya Edeni?

Akawaambia Enendeni ulimwenguni mwote,MKAIHUBIRI INJILI KWA KILA KIUMBE.(Marko16:15.) Yesu Anamaanisha nini kusema MKAIHUBIRI INJILI KWA KILA KIUMBE?

EPUKA KUTOA UDHURU.

BWANA alimaanisha nini kwenye mstari huu Marko 2:21″ Hakuna mtu ashonaye kiraka cha nguo mpya katika vazi kukuu;?

Rudi Nyumbani:

Print this post

Hirimu ni nini kibiblia?(Wagalatia 1:14)

Hirimu ni nini?


Hirimu ni mtu aliye katika kundi la umri wako (rika). Kwamfano tukisema, Petro na Yohana ni hirimu moja, tunamaanisha Petro na Yohana ni watu wa umri mmoja.

 Lakini kibiblia hirimu linakwenda mbali kidogo  zaidi ya hapo, mahali pengine linamaanisha kijana mdogo.

Kwamfano mistari hii inazungumzia hirimu kama mtu wa umri mmoja naye.

Danieli 1:10 “Mkuu wa matowashi akamwambia Danieli, Mimi namwogopa bwana wangu, mfalme, aliyewaagizia ninyi chakula chenu na kinywaji chenu; kwa nini azione nyuso zenu kuwa hazipendezi kama nyuso za vijana hirimu zenu? Basi kwa kufanya hivyo mtahatirisha kichwa changu mbele ya mfalme”.

Hapo ni Yule mwangalizi wa Vijana, towashi akiwaeleza akini Danieli hofu yake juu kukunjamana sura zao, pale vijana wenzao wa rika lao watakapoitwa nyumbani kwa mfalme na kuonekana wananawiri kushinda wao, atauliwa yeye.

Soma tena..

Wagalatia 1:14 “Nami naliendelea katika dini ya Kiyahudi kuliko wengi walio hirimu zangu katika kabila yangu, nikajitahidi sana katika kuyashika mapokeo ya baba zangu.

15 Lakini Mungu, aliyenitenga tangu tumboni mwa mama yangu, akaniita kwa neema yake,”

Hapo mtume Paulo anazungumzia jinsi alivyofanya bidii ya kuzishika dini za kiyahudi kuliko hata watu waliokuwa wa rika lake, au umri wake, vijana wenzake.

Lakini katika vifungu hivi, vinalitaja neno hili, vikimaanisha kijana mdogo.

Waamuzi 8:14 Ndipo akamshika mtu mmoja hirimu katika watu wa Sukothi, akamwuliza; naye akamwandikia majina ya hao wakuu wa Sukothi, na wazee wa mji, watu sabini na saba.

Soma pia..Waamuzi 17:7,11, 18:3

Hivyo, ni nini tunaweza kujifunza kutokana na Neno hili?

Hata sisi tupo katika marika, tujiulize katika marika tuliyopo, ni mambo gani ya maana tunafanya kwa Mungu etu. Upo katika rika la miaka 12 angalia kwenye biblia waliokuwa na miaka hiyo walikuwa na bidii gani kwa Mungu. Yesu alipokuwa na umri huo, alikuwa hekaluni akijifunza sheria ya Mungu, je na wewe unafanya hivyo?

Upo katika rika la miaka 30, jiulize katika umri huo, unatenda jambo gani katika ufalme wa mbinguni? Bwana Yesu alipokuwa katika umri huo, alianza kuitenda kazi ya Mungu kwa nguvu akijua kuwa muda wake aliobakiwa nao kuishi duniani ni mchache.. Je, na wewe uliye katika rika hilo unalijua? Hirimu yetu Kristo Yesu alitendaje katika umri huo?

Vivyo hivyo upo katika miaka 40, au 50, au 70  au 80 jiulize ni nini unakiingiza katika ufalme wa mbinguni, Je ni kutwa kuchwa kusumbukia ya ulimwengu? Je, ni elimu tu, Je ni familia tu, au ni nini?. Musa alikuwa na miaka 80 alipoanza kumtumikia Mungu lakini utumishi wake aliuthamini, kana kwamba alikuwa na miaka 20, Je! Na wewe unafanya hivyo?

Kumbuka biblia inasema..

Mhubiri 12:1 “Mkumbuke Muumba wako siku za ujana wako, Kabla hazijaja siku zilizo mbaya, Wala haijakaribia miaka utakaposema, Mimi sina furaha katika hiyo”.

Heshimu umri wako, tambua ni nini unapaswa ufanye kwa wakati huo.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

Choyo ni nini kibiblia? (Luka 12:15, Zaburi 10:3)

Nini maana ya Dirii, Chepeo na Utayari?

Baadhi ya watu  na misemo ambayo haipo katika biblia.

IKO NJIA IONEKANAYO KUWA SAWA MACHONI PA MTU.

UNYAKUO.

Rudi Nyumbani:

Print this post

kwanini yule kijana aliitupa ile nguo ya kitani chini na kukimbia uchi?

SWALI: Naomba ufafanuzi kidogo hapa sijaelewa vizuri, kwanini wakati Bwana Yesu anakuja kukamatwa naona kijana waliyemkamata alikuwa na nguo ya kitani ila baadae tunaona anaitupa nguo na kukimbia uchi , Marko 14:51-52

JIBU: Tusome;

Marko 14:50 “Ndipo wakamwacha, wakakimbia wote.

51 Na kijana mmoja alimfuata, amejitanda mwili wake nguo ya kitani; wakamkamata;

52 naye akaiacha ile nguo ya kitani, akakimbia yu uchi”.

Biblia haielezi huyu kijana alikuwa ni nani, wengine wanasema alikuwa ni Marko mwenyewe aliyeandika kitabu hicho, au mwanafunzi mwengine mbali na wale

 12, kwasababu wale walikuwa yatari wameshakimbia, ukisoma mstari wa 51. Lakini kufahamu kama huyu kijana alikuwa ni miongoni mwa wale 12 au wengineo sio la muhimu sana kwenye habari hiyo . La muhimu ni kujua kwanini tukio kama lile lijitokeze.

Kwanini biblia inasema aina ya vazi alilovaa kwamba ni la kitani?. Kwanini aache vazi akimbie na sio kitu kingine? .Tukiweza kuyatafakari maswali hayo tutapata ujumbe mkubwa sana nyuma ya tukio lile.

Kama tukichunguza asili ya vazi hilo, kwa mazingira yaliyokuwa yanaendelea pale tunaweza kusema ni vazi linalomsitiri mtu mwili wote. Kiasi kwamba likivaliwa halihitaji kuvaliwa na kitu kingine ndani. Kiasi kwamba mtu akilivua ni rahisi kubakiwa uchi.

Pili, ni vazi ambalo ni rahisi kuvulika, halihitaji kufungwa au kushikizwa kwa vitu vingi. Na ndio maana utaona kijana huyo alipokamatwa tu na wale askari, ilikuwa ni rahisi kuwaachia lile vazi na kukimbia. Ingekuwa ni vazi lenye vifungo, au mikandani mingi, isingekuwa rahisi kujikwamua kwa wale askari.

Na jambo lingine unaweza kuona pale, ni kuwa wale askari waliona njia pekee ya kumkamata ni kwa kulishika vazi lake, na sio pengine mikono yake au kitu kingine,. Na ndio maana utaona kijana alitumia njia ya kuacha vazi ili akimbie.

Hiyo ni kutufundisha, kuwa lipo vazi la rohoni (Kitani ya rohoni). Ambalo linauwezo wa kuusitiri uchi wote wa mtu wa rohoni, lakini pia ni jepesi sana mtu kulivua. Na ndio Bwana Yesu alisema..

Ufunuo 16:15 “(Tazama, naja kama mwivi. Heri akeshaye, na KUYATUNZA MAVAZI YAKE, asiende uchi hata watu wakaione aibu yake.)”

Unaona hapo anasema heri “ayatunzaye” mavazi yake. Ni kuonyesha kuwa mavazi hayo yanapaswa yatunzwe sana..kwasababu ni rahisi kuvulika.. Tutaona mbele kidogo mavazi hayo ni nini..

Na adui yetu shetani, anachokiwinda kwetu, sio miili yetu, sio mionekano yetu, si madhehebu yetu, si dini zetu. Bali ni mavazi yetu ya rohoni..Hayo ndiyo anayokimbilia kuyashika, haya ndiyo anayotaka umuachie, kama alivyofanya kwa yule kijana, Na mavazi yenyewe si mengine zaidi ya “matendo yetu ya haki” (yaani, utakatifu). Biblia inasema hivyo katika.

Ufunuo 19:8 “Naye amepewa kuvikwa kitani nzuri, ing’arayo, safi; KWA MAANA KITANI NZURI HIYO NI MATENDO YA HAKI YA WATAKATIFU”.

Unaona? Mavazi ya kitani ni matendo ya haki ya watakatifu.  Mpaka hapo utakuwa unapata kufahamu ni picha gani Mungu alikuwa anatuonyesha kwa yaliyokuwa yanaendelea kwa Yule kijana rohoni. Hata sasa ni kawaida watu wanapopitia shida kidogo, au dhiki au wanapokutana na matatizo  kuuacha wokovu, wanaacha utakatifu, wanamwacha Mungu, wanaacha kutenda matendo mema tena, wanamwachia adui vazi lao la thawabu.

Hivyo Neno la Mungu linatufundisha, tukutanapo na udhia wowote, au dhiki, tusiwe wepesi wa kuuacha wokovu wetu na utakatifu wetu.

Swali ni je! VAZI hili unalo? Ikiwa huna

Bwana Yesu anakupa shauri katika Ufunuo 3:18 kuwa ukanunue kwake mavazi hayo meupe uvae ili aibu ya uchi wako isionekane.. Hivyo tubu kama bado hujafanya hivyo, ukabatizwe, upokee Roho Mtakatifu. Ukamilishwe kwa vazi hili

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

MAVAZI YA NDANI NA YA NJE.

JE! UNAYATUNZA MAVAZI YAKO?

MAVAZI YAPASAYO.

Nguo za magunia katika biblia ni zipi?

JE! PAKA KULIA USIKU NI ISHARA YA UCHAWI?

Rudi Nyumbani:

Print this post

Choyo ni nini kibiblia? (Luka 12:15, Zaburi 10:3)

Choyo ni nini kibiblia?


Choyo ni tamaa ya hali ya juu, aidha wa mali, uongozi, au chakula, ambayo inaambatana na uchoyo. Kwa namna nyingine ni Tabia ya ubinafsi, tabia ya umimi. Kukataa kwa makusudi kuwapa wengine kile ulichonacho, au wanachostahili kukipata, kwa maslahi yako mwenyewe.

Mithali 21:26 “Kuna atamaniye kwa choyo mchana kutwa; Bali mwenye haki hutoa wala hanyimi”.

Jambo ambalo Bwana Yesu alituonya sana tujiepushe nalo, alilizungumza hilo siku ile alipokutana na yule mtu ambaye alimwomba amwonye ndugu yake, juu ya urithi wao. Pengine ni urithi walioachiwa na baba yao alipokufa na huyu ndugu yao mmoja anataka kuwadhulumu hataki kuwapa, au ni mashamba ya ukoo, na hivyo anataka ayamiliki yeye mwenyewe, au ayauze na ndugu zake wasipate kitu n.k.. Vyovyote vile, lakini Bwana Yesu alimwambia hivi,

Luka 12:13 “Mtu mmoja katika mkutano akamwambia, Mwalimu, mwambie ndugu yangu anigawie urithi wetu.

14 Akamwambia, Mtu wewe, ni nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawanyi juu yenu?

 15 Akawaambia, ANGALIENI, JILINDENI NA CHOYO, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo.

16 Akawaambia mithali, akisema, Shamba la mtu mmoja tajiri lilikuwa limezaa sana;

17 akaanza kuwaza moyoni mwake, akisema, Nifanyeje? Maana sina pa kuyaweka akiba mavuno yangu.

18 Akasema, Nitafanya hivi; nitazivunja ghala zangu, nijenge nyingine kubwa zaidi, na humo nitaweka nafaka yangu yote na vitu vyangu.

19 Kisha, nitajiambia, Ee nafsi yangu, una vitu vyema vingi ulivyojiwekea akiba kwa miaka mingi; pumzika basi, ule, unywe, ufurahi.

20 Lakini Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani?

21 Ndivyo alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu”.

Tabia hii ya Choyo ilitabiriwa kukithiri sana katika siku za mwisho,(Ambazo ndio hizi tunazoishi) kuwa watu watakuwa ni wa kupenda fedha, na wa kujipenda wao wenyewe.(2Timotheo 3:2). Jambo ambalo ni baya sana.

Hivyo, na sisi tunapaswa tujichunguze kama tabia hii ipo ndani yetu, Kristo ameshatuasa tujiepusha nayo, tuache ubinafsi, bali tuwe watu wa kuridhika, na watu wa kushea na wengine vile ambavyo Mungu anatubarikia navyo, kwasababu vya duniani vinapita, hatukuja na kitu na wala hatutaondoka na kitu.

Zaburi 10:3 “Maana mdhalimu hujisifia tamaa ya nafsi yake, Na mwenye choyo humkana Bwana na kumdharau”.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

KUNA UMUHIMU WA KUWA MTU WA KURIDHIKA.

Nini maana ya Dirii, Chepeo na Utayari?

Santuri ni nini? (Danieli 3:5,10)

Jabari ni nini, kama linavyotumika kwenye biblia?

Mkatale ni nini katika biblia? (Matendo 16:24)

NGUVU YA UPOTEVU.

NA UPEPO WA KUSI ULIPOANZA KUVUMA KIDOGO,

Rudi Nyumbani:

Print this post

Nini maana ya Dirii, Chapeo na Utayari?

Chapeo:

Chapeo ni kofia ngumu ya chuma waliyokuwa wanavaa watu waliokuwa wanakwenda vitani. Tazama picha chini.

chepeo ni nini

Kwa lugha ya kiingereza ni “Helmet” . Kwa nyakati hizi, shughuli nyingi na michezo mingi jamii ya kofia hizo zinatumika, kwamfano wanaondesha pikipiki ni lazima wavae helmet (yaani chepeo), kwa usalama wa safari yao hiyo, kwasababu kwa bahati mbaya ikitokea wakipata ajali, sehemu ya kichwa haitadhurika kutokana na kofia hiyo ngumu waliyoivaa. Kadhalika na sehemu nyingine nyingi, chepeo zinatumika. Na pia chepeo za askari wa zama hizi, sio sawa na za askari wa zamani, hizi za nyakati zetu zimetengenezwa kwa kwa utashi zaidi mara nyingi ya zile, ambapo hata askari akipitia mahali penye hewa ya sumu si rahisi kudhurika.

askari wa sasa

Na sisi wakristo katika roho ni maaskari wa Kristo, nasi pia hatuna budi kuzivaa chepeo vichwani mwetu, hiyo itatusaidia chochote kile kitakachorushwa na adui shetani katika roho, dhidi yetu, visiweze kuvidhuru vichwa vya roho zetu, na hata pia tukianguka kwa bahati mbaya katika vita hivi vya imani, tusiweze kudhurika, maana yake tusife moja kwa moja, bali tuweze kusimama tena, kwasababu vichwa vyetu vimehifadhiwa. Na pia vita vyetu sisi ni vikali zaidi ya watu wa vizazi vya nyuma hivyo hatuna budi, kuvaa chepeo zinazoenenda na vita vyetu..Na chepeo hizo ni “Wokovu ule wa kimaandiko kabisa ambao haujachanganywa na chochote”.

DIRII:

Dirii ni vazi la chuma wapiganaji wa zamani walilokuwa wanavikwa katika maeneo ya kifua, ambapo vazi hilo litamkinga mwanajeshi yule dhidi ya mikuki ambayo itarushwa kwa bahati mbaya, na kumfikia maeneo ya kifua au tumbo, hapo vazi hilo la chuma, litamkinga askari yule yule asijeruhiwe.

dirii ni nini

Katika zama zetu hizi, vita vya mikuki havipo tena, vipo vita vya kutumia risasi na bunduki, hivyo dirii za siku hizi, zinatengenezwa mahususi kwa kuzuia risasi zisipenye kwenye kifua au tumbo la mtu, kwa lugha ya kiingereza wanaziita “bullet proof vest”. Tazama picha chini..

bullet proof

Na sisi pia wakristo ni askari wa Bwana, na tupo vitani, Dirii tunayoivaa sisi sio vyuma vya damu na nyama bali ni Dirii ya Haki, ambayo tunaipata katika mistari ifuatayo..(Warumi 2:13, Warumi 3:21-22, Waebrania 10:38, Mathayo 6:33). Na kama vile jinsi vita vinavyobadilika kulingana na Nyakati, vivyo hivyo na vita vyetu sisi watu wa siku za mwisho, ni vikali zaidi kuliko vya watu wa kwanza, hivyo hatuna budi kila siku kuzihakiki dirii zetu kama zinatosha kuzuia silaha za Adui yetu shetani, kama hazitoshi basi hatuna budi kutafuta zinazotosha, na tunazitafuta kwa kulisoma Neno Sana na kulielewa.

UTAYARI:

Utayari unaozungumziwa hapo ni Aina ya vazi la chuma, linalovaliwa katika miguu…Dirii inavaliwa kifuani lakini Utayari unavaliwa miguuni…vazi hili linavikwa katika kila mguu, lengo lake ni kukinga upande wa mbele wa mguu usiweze kujeruhiwa..Kwasababu askari akishajeruhiwa miguu yake hataweza kupambana tena vita hata kama atakuwa na uzoefu mwingi kiasi gani. Tazama picha chini..

utayari

Na sisi kama Askari wa Kristo, ni lazima tuvae utayari miguuni mwetu, ambao tunaupata kwa njia ya injili ya amani.

Hizi ni silaha chache tu za kujikinga, lakini zipo pia silaha moja ya kushambulia ambayo ni UPANGA WA ROHO, Kwa urefu juu ya Silaha hizi kwa Mkristo na namna ya kuzitumia, unaweza kufungua hapa >> Mapambano dhini ya shetani

Na kama bado hujaokoka, na ungependa kufanya hivyo leo, basi usingoje kesho, hapo hapo ulipo Kristo yupo..Hivyo dhamiria kutubu kwa dhati leo, na Kristo atakukubali, kwasababu alisema wote wamjiao, hatawatupa nje kamwe. Hivyo kama utaweza kupiga magoti na kutubu wewe mwenyewe binafsi ni vizuri, lakini kama utahitaji msaada unaweza kufungua hapa >>> KUONGOZWA SALA YA TOBA

Au ukapiga namba hizo hapo chini..

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

MAPAMBANO DHIDI YA SHETANI.

MAISHA ULIYOPITIA NYUMA NI USHUHUDA TOSHA WA WEWE KUMTUMIKIA MUNGU:

USIRUHUSU MUNGU AWEKE UADUI KATI YAKO NA WATU WAKO.

NEHUSHTANI (NYOKA WA SHABA).

JE! WEWE NI MWAKILISHI MWEMA?

Rudi Nyumbani:

Print this post

USITAFUTE KUKANWA NA BWANA SIKU ILE.

Kukanwa hakuna tofauti sana na kusalitiwa..Ni maneno pacha!.. Alichokifanya Yuda hakina tofauti sana na alichokifanya Petro. Tofauti ni kwamba mmoja “kamkataa Yesu” mwingine “kamuuza”..lakini wote wamemkana, na wote wamemsaliti.

Utauliza hata Petro alimsaliti Bwana?..Jibu ni ndio!.. kumkana mtu wakati wa mateso yake na dhiki yake, na siku zote mlikuwa mnatembea pamoja ni kumsaliti pia!.

Sasa kuna maneno Bwana Yesu aliyasema ambayo ndio kiini cha somo letu leo.

Tusome..

Mathayo 10:33  “Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu aliye mbinguni.

34  Msidhani ya kuwa nimekuja kuleta amani duniani; la! Sikuja kuleta amani, bali upanga. ”

Sasa kukana maana yake ni nini?..

Mnapokubaliana na mtu, na kuwekeana nadhiri ya kwamba mtakuwa pamoja katika shida na raha, na ukatembea na huyo ndugu yako ukiamini kwamba popote mtakuwa pamoja mkisaidiana na kuteteana, halafu ghafla mnaingia kwenye tatizo, yule ndugu yako anakukataa ghafla tu, anasema hakujui, wala hamjuani! pasipo kutegemea..huko ndiko kukanwa au kusalitiwa.

Ndicho Bwana alichomaanisha hapo kwamba siku ile atawakana baadhi ya watu. Ikiwa na maana kuwa, hapa duniani ataendelea kutembea na wewe kama rafiki wa kweli kwako, ukimwomba kitu atakupa, hata ukiumwa utakuponya, utaweza kwenda kukemea pepo kwa jina lake litatoka,  utajihisi kabisa kwamba unaye rafiki wa kweli maishani mwako, na utakuwa na uhakika kwamba huwezi kupotea kamwe, yeye yupo na wewe, ukimwita atakuitikia… Lakini siku ile utashangaa amekuwaje!!..utashangaa anakuwambia sikujui…Ndipo utaanza kusema… si ni juzi tu ulinitokea kwenye ndoto ukanionyesha maono, si ni juzi tu, nilitoa pepo kwa jina lako, si ni juzi tu ulinionyesha unabii..inakuwaje leo unasema hunijui??…Huko ndio kukanwa, ambako kunaumiza sana.

Na ndio maana alisema;

Luka 13:24  “Jitahidini kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi watataka kuingia, wasiweze.

25  Wakati mwenye nyumba atakaposimama na kuufunga mlango, nanyi mkaanza kusimama nje na kuubisha mlango, mkisema, Ee Bwana, tufungulie; yeye atajibu na kuwaambia, Siwajui mtokako;

26  ndipo mtakapoanza kusema, Tulikula na kunywa mbele yako, nawe ulifundisha katika njia zetu.

27  Naye atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa udhalimu.

28  Ndipo kutakapokuwa na kilio na kusaga meno, mtakapomwona Ibrahimu na Isaka na Yakobo na manabii wote katika ufalme wa Mungu, nanyi wenyewe mmetupwa nje”.

Na pia Bwana alizungumza maneno kama hayo hayo katika kitabu cha Mathayo…

Mathayo 7:21  “Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni.

22  Wengi wataniambia siku ile, Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi?

23  Ndipo nitawaambia dhahiri, SIKUWAJUA NINYI KAMWE; ONDOKENİ KWANGU, ninyi mtendao maovu”.

Leo hii watu wengi wanapumbazika na fadhili za Mungu..na huku mioyoni mwao wamemwacha Mungu, mioyoni mwao wamemkana na kumkataa, bado ni wazinzi kwa siri, bado ni wauaji, waizi, walevi, wachawi, waabudu sanamu, na watu wanaoupenda ulimwengu… Wamemkataa Yesu, na maishani mwao kwasababu wanaona Mungu anazidi kuwapa afya, wanadhani Kristo anapendezwa nao, wanaona bado wanabarikiwa katika biashara zao, wanadhani wapo mioyoni mwa Kristo, wanapomwomba Kristo, hiki au kile wanapatiwa wanajua wanatembea na mtu ambaye kamwe hawezi kuwakana…Oo inasikitisha sana siku ile ghafla yule aliyekuwa anawapa chakula, aliyekuwa anawashika mkono wakati wa shida, aliyekuwa anawaponya, aliyekuwa anawafaraji wakati wa shida, ghafla anawakana na kuwaambia SIWAJUI…Na haishii hapo, anaendelea na kusema ONDOKENI KWANGU….

Siku hiyo utasema, yule Yesu wa upendo leo hii ananifukuzaa!!!!.. Yule niliyekuwa kila siku namwona kwenye maisha yako leo hii ananifukuzaa…Hutaamini lakini ndivyo itakavyokuwa!!!

Tusitamani kukanwa siku ile. Je Kristo ameyatakasa maisha yako? Au bado unapumbazika na fadhili zake kwako?..Kumbuka yeye anasema anawanyeshea mvua waovu na wema…hivyo si jambo kubwa sana yeye kukupa wewe gari, kama anaweza kukupa nishati ya jua bure kwa miaka yote hiyo uliyoishi, na huku bado ni mlevi, hivyo ni gari atakupa pia, na nyumba (wala si shetani ambaye atakupa, ni yeye Yesu) lakini siku ile atakuambia dhahiri sikujui..Kama hujampokea Yesu, na kufanya uteule wako imara, huu ni wakati wako sasa. Tubu dhambi zako na pia tafuta ubatizo kama bado hujabatizwa, na Kristo atakupa kipawa cha Roho wake Mtakatifu, ambaye atakuongoza kukupeleka kule anakotaka yeye.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312

Mada Nyinginezo:

JE YESU AMEJIAMINISHA KWAKO?

KWANINI KRISTO AFE?

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita..

JINSI SHETANI ANAVYOZUIA MAJIBU YA MAOMBI YETU.

Kitabu kifupi katika biblia ni kipi, na ujumbe wake ni upi?

Rudi Nyumbani:

Print this post

Baadhi ya watu  na misemo ambayo haipo katika biblia.

Ifuatayo ni baadhi ya misemo, ambayo ipo katika jamii yetu, ambayo inadhaniwa kuwa ipo kwenye biblia lakini kiuhalisia haipo kabisa, aidha imetungwa na watu tu au inapatikana kwenye vitabu vingine tofauti na biblia.

  1. Jisaidie nami nitakusaidia

Huu msemo haupo kabisa kwenye biblia takatifu, ingawa umekuwa ukitumika na hata wakristo wakiamini kuwa kuna mahali kwenye biblia Mungu alisema “jisaidie nami nitakusaidia”. Hivyo kama mkristo badala ya kuutumia huo msemo ni afadhali ukatumika huu  “….. imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake (Yakobo 2:17 )”.

  1. Mungu si Athumani.

Huu pia ni msemo wa methali za kiswahili, ambao ni umekuwa ukitumika na hata wakristo baadhi wakiamini ni aya fulani katika biblia, una huo msemo.. Lakini katika biblia nzima huo mstari haupo. Hivyo badala ya kuutumia huo ni afadhali ukatumika huu “Mungu si mtu, aseme uongo; Wala si mwanadamu, ajute; Iwapo amesema, hatalitenda? Iwapo amenena, hatalifikiliza?( Hesabu 23:19)”.

  1. Mungu hamtupi Mja wake.

Huu usemi pia haupo kwenye biblia takatifu, ingawa hauna tafsiri mbaya, lakini haupo kwenye maandiko… Hivyo badala ya kuutumia huo ni vizuri, ukajizoeza kuutumia huu ambao upo kwenye maandiko… “Kwa kuwa Bwana hatamtupa mtu Hata milele. Maana ajapomhuzunisha atamrehemu, Kwa kadiri ya wingi wa huruma zake Maombolezo 3: 31”

  1. Mpende akupendaye, asiyekupenda achana naye.

Msemo huu sio tu haupo kwenye biblia, lakini ni msemo wa uliotengenezwa na adui shetani asilimia mia..kwasababu ni kinyume cha maneno ya Bwana Yesu mwenyewe aliyoyasema katika..

Mathayo 5:43  “Mmesikia kwamba imenenwa, Umpende jirani yako, na, Umchukie adui yako;

44  lakini mimi nawaambia, Wapendeni adui zenu, waombeeni wanaowaudhi,

45  ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni; maana yeye huwaangazia jua lake waovu na wema, huwanyeshea mvua wenye haki na wasio haki”.

          5. Kila Nafsi itaonja mauti:

Huu ni msemo maarufu sana, lakini haupo kabisa kwenye biblia..Na zaidi ya yote ni kinyume cha Biblia. Kwasababu biblia ambalo ndio Neno la Mungu inasema.. watakuwepo watu ambao unyakuo utawakuta wakiwa hai, na hawa watakuwa miongoni mwa watu ambao hawataonja mauti kabisa.. Hivyo sio wote watakufa..

1Wakorintho 15:51 “Angalieni, nawaambia ninyi siri; hatutalala sote, lakini sote tutabadilika,

52 kwa dakika moja, kufumba na kufumbua, wakati wa parapanda ya mwisho; maana parapanda italia, na wafu watafufuliwa, wasiwe na uharibifu, nasi tutabadilika”

Yafuatayo ni majina ambayo hayapo katika katika biblia.

  1. Mohamed

Jina hili halipo kabisa kwenye biblia, wala hakuna mtu mwenye jina kama hili katika biblia nzima. Yapo majina kama Yohana, Yuda, Anania ambayo yameonekana katika biblia sehemu mbali mbali, kwa watu tofauti tofauti, yakijirudia lakini jina hili Mohamedi  halipo hata kwa mtu mmoja katika biblia nzima, aidha kwa watu wa Mataifa au katikati ya wana wa Israeli. Hivyo hadithi zozote zinazotaja uwepo wa mtu mwenye jina hili katika biblia ni hadithi za kutunga na zenye maudhui ya kupotosha.

  1. Israeli Mtoa roho

 Usemi huu ni maarufu, ukimlenga malaika yule anayehusika na kutoa roho za watu, yaani mtu anapokaribia kufa kuna malaika anakuja, almaarufu kama “Israeli Mtoa roho” ndiye anayehusika katika kuiondoa roho ya mtu. Usemi huu, na jina hilo, halipo kabisa katika biblia nzima, hivyo ni usemi uliotungwa na watu.

Yapo na mambo mengine mengi, ambayo yanaaminika na wengi kuwa yapo katika ndani ya Biblia lakini kiuhalisia hayapo. Hivyo ni wajibu wetu kuwa makini, na kujifunza kuyasoma maandiko wenyewe kuliko kusubiria tu kusimuliwa au kuhadithiwa, kwasababau adui yetu shetani hajalala usingizi, usiku na mchana anatunga mbinu mpya za kuweza kututoa katika mstari, na kuyageuza maandiko, hivyo tuwe macho.

Maran atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255 789001312


Mada Nyinginezo:

USIIGEUZE NYUMBA YA MUNGU KUWA PANGO LA WANYANG’ANYI.

Wapunga Pepo wanaozungumziwa kwenye biblia ni watu wa namna gani?

Katika Yakobo 1:13 Biblia inasema Mungu hamjaribu mtu, lakini tukirudi kwenye kitabu cha Mwanzo 22:1 tunaona Mungu alimjaribu Ibrahimu. Hapo naomba mwanga zaidi.

Je ni sahihi kumtenga mtu anapofanya dhambi kanisani?

Je! Kusoma biblia kwenye simu ukiwa kanisani ni dhambi?

Rudi Nyumbani:

Print this post