Category Archive Uncategorized @sw-tz

JINSI MUNGU ATAKAVYOTOA THAWABU ZAKE, NA VIGEZO ATAKAVYOTUMIA. (Sehemu ya 3)

Shalom, huu ni mfululizo, wa Makala ambazo zinaeleza vigezo ambavyo Mungu, atavitumia kuwapa watu wake thawabu mbalimbali, au atakavyovitumia kuwakaribisha katika ufalme wake, hii ni sehemu ya tatu, ikiwa hukupitia sehemu zilizotangulia utatumia ujumbe inbox tukutumie chambuzi zake.

3) Biblia inatuonyesha kuna watu watu wataingizwa katika ufalme wa Mungu, bila kutambua sababu.

Inashangaza lipo kundi la watu ambalo litapewa neema ya kuungia ufalme wa Bwana wetu Yesu Kristo, bila lenyewe kutambua sababu mpaka litakapofunuliwa na Kristo mwenyewe siku ile.

Tunalisoma kundi hilo katika vifungu hivi.

Mathayo 25:31 “Hapo atakapokuja Mwana wa Adamu katika utukufu wake, na malaika watakatifu wote pamoja naye, ndipo atakapoketi katika kiti cha utukufu wake;

32 na mataifa yote watakusanyika mbele zake; naye atawabagua kama vile mchungaji abaguavyo kondoo na mbuzi;

33 atawaweka kondoo mkono wake wa kuume, na mbuzi mkono wake wa kushoto.

34 Kisha Mfalme atawaambia wale walioko mkono wake wa kuume, Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu;

35 kwa maana nalikuwa na njaa, mkanipa chakula; nalikuwa na kiu, mkaninywesha; nalikuwa mgeni, mkanikaribisha;

36 nalikuwa uchi, mkanivika nalikuwa mgonjwa, mkaja kunitazama; nalikuwa kifungoni, mkanijia.

37 Ndipo wenye haki watakapomjibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona una njaa, tukakulisha, au una kiu tukakunywesha?

38 Tena ni lini tulipokuona u mgeni, tukakukaribisha, au u uchi, tukakuvika?

39 Ni lini tena tulipokuona u mgonjwa, au kifungoni, tukakujia?

40 Na Mfalme atajibu, akiwaambia, Amin, nawaambia, kadiri mlivyomtendea mmojawapo wa hao ndugu zangu walio wadogo, mlinitendea mimi.

41 Kisha atawaambia na wale walioko mkono wake wa kushoto, Ondokeni kwangu, mliolaaniwa, mwende katika moto wa milele, aliowekewa tayari Ibilisi na malaika zake;

42 kwa maana nalikuwa na njaa, msinipe chakula; nalikuwa na kiu, msininyweshe;

43 nalikuwa mgeni, msinikaribishe; nalikuwa uchi, msinivike; nalikuwa mgonjwa, na kifungoni, msije kunitazama.

44 Ndipo hao pia watajibu, wakisema, Bwana, ni lini tulipokuona wewe una njaa, au una kiu, au u mgeni, au u uchi, au u mgonjwa, au u kifungoni, tusikuhudumie?

45 Naye atawajibu, akisema, Amin, nawaambia, Kadiri msivyomtendea mmojawapo wa hao walio wadogo, hamkunitendea mimi.

46 Na hao watakwenda zao kuingia katika adhabu ya milele; bali wenye haki watakwenda katika uzima wa milele”.

Kundi hili, ni lile, lilowahifadhi, watumishi wa Kristo, wakiwa hapa duniani, wasijue kuwa walikuwa wanamtendea Kristo mwenyewe, hapa hazungumzii maskini, na omba omba, au  mayatima hapana, wanaowahudumia hao wanayothawabu yao, ambayo tutaiona katika Makala inayofuata, bali wanaozungumziwa hapa ni watakatifu wa Bwana, ambao kutokana na maisha yao ya  utumishi, walipitia kupungukiwa, kuumwa, kukosa chakula, nguo, makazi n.k. Sasa wapo ambao waliwaona na kuwahifadhi, wasijue kuwa wanamtendea Kristo mwenyewe.

Sasa siku ile itakapofika, hawa watumishi wa Bwana watasimama na kuwataja mbele ya Kristo, na kwasababu hiyo Kristo atawapa neema ya kuuingia ufalme wake. Sawasawa na ule mfano wakili dhalimu tunaousoma katika Luka 16:1-12.

Mtume Paulo aliwaombea rehema ndugu wa mtu mmoja aliyeitwa Onesiforo, kwa jinsi walivyomtunza na kumuhudumia kwa mahitaji mbalimbali alipokuwa anahubiri.

2Timotheo 1:16 “Bwana awape rehema wale walio wa mlango wake Onesiforo; maana mara nyingi aliniburudisha, wala hakuuonea haya mnyororo wangu;

17 bali, alipokuwapo hapa Rumi, alinitafuta kwa bidii akanipata.

18 Bwana na ampe kuona rehema machoni pa Bwana siku ile. Na jinsi alivyonihudumia kwa mengi huko Efeso, wewe unajua sana”.

Vivyo hivyo, na wale ambao, wanawaona watu wanaomtafuta Mungu, ni kama mizigo kwao, wanawadhihaki, wanawatukana, wanawafukuza, hata wakiomba maji wanawaona ni wavivu. Watu ambao wanaposikia watumishi wa kweli wa Mungu ni kama kero kwa kwao, Watu kama hawa upo wakati Kristo naye atawakana.

Inatufundisha nini?, tukisema tunampenda Kristo, tunamaanisha kuwa tunawapenda na wale wampendao, kama unawachukia watakatifu, utampendaje Kristo?. Hivyo, wapo watu ambao Kristo atawakaribisha kwa namna hii,. Vilevile wapo watu ambao Kristo atawafukuza kwa namna hii. Kwasababu hawakumkaribisha Kristo kwao.

Shalom.

Usikose mwendelezo..

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

JINSI MUNGU ATAKAVYOTOA THAWABU ZAKE, NA VIGEZO ATAKAVYOTUMIA. (Sehemu ya 1)

JINSI MUNGU ATAKAVYOTOA THAWABU ZAKE, NA VIGEZO ATAKAVYOTUMIA. (Sehemu ya 2)

JINSI YA KUSOMA BIBLIA.

HUTATAMBUA LOLOTE, SIKU YA UNYAKUO IKIFIKA.

Rudi nyumbani

Print this post

JINSI MUNGU ATAKAVYOTOA THAWABU ZAKE, NA VIGEZO ATAKAVYOTUMIA. (Sehemu ya 1)

Bwana Yesu asifiwe, katika Makala hizi, tutazama vigezo ambavyo Mungu atavitumia kutoa thawabu zake, tutakapofika kule ng’ambo, Hii itatusaidia kuzidisha hamasa zetu katika kumtumikia Mungu, kama vile mtume Paulo, alivyoliona hilo, mpaka akasema..

Wafilipi 3:14 “nakaza mwendo, niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu”.

 Tutapitia baada ya vifungu, ambavyo vitatupa picha jinsi thawabu hizo Mungu atakavyozigawa; Kigezo cha thawabu ya kwanza tunakisoma katika Mathayo 20:1-16

  1. Wapo watu watafanya kazi kidogo, lakini watalipwa sawasawa na wale waliofanya kazi nyingi.

Unaweza ukasema ni kwanini Mungu afanye hivyo? Embu tupitie Habari hii, tutapata majibu yote.

Mathayo 20 : 1-16

“1 Kwa maana ufalme wa mbinguni umefanana na mtu mwenye nyumba aliyetoka alfajiri kwenda kuajiri wakulima awapeleke katika shamba lake la mizabibu.

2 Naye alipokwisha kupatana na wakulima kuwapa kutwa dinari, aliwapeleka katika shamba lake la mizabibu.

3 Akatoka mnamo saa tatu, akaona wengine wamesimama sokoni wasiokuwa na kazi;

4 na hao nao akawaambia, Enendeni nanyi katika shamba langu la mizabibu, na iliyo haki nitawapa. Wakaenda.

5 Akatoka tena mnamo saa sita na saa kenda, akafanya vile vile.

6 Hata kama saa kumi na moja akatoka, akakuta wengine wamesimama, akawaambia, Mbona mmesimama hapa mchana kutwa bila kazi?

7 Wakamwambia, Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri. Akawaambia, enendeni nanyi katika shamba la mizabibu.

8 Kulipokuchwa, yule bwana wa shamba akamwambia msimamizi wake, Waite wakulima, uwalipe ujira wao, ukianzia wa mwisho hata wa kwanza.

9 Na walipokuja wale wa saa kumi na moja, walipokea kila mtu dinari.

10 Na wale wa kwanza walipokuja, walidhani kwamba watapokea zaidi; na hao pia wakapokea kila mtu dinari.

11 Basi wakiisha kuipokea, wakamnung’unikia mwenye nyumba,

12 wakisema, Hao wa mwisho wametenda kazi saa moja tu, nawe umewasawazisha na sisi tuliostahimili taabu na hari za mchana kutwa.

13 Naye akamjibu mmoja wao, akamwambia, Rafiki, sikudhulumu; hukupatana nami kwa dinari?

14 Chukua iliyo yako, uende zako; napenda kumpa huyu wa mwisho sawa na wewe.

15 Si halali yangu kutumia vilivyo vyangu kama nipendavyo? Au jicho lako limekuwa ovu kwa sababu ya mimi kuwa mwema?

16 Vivyo hivyo wa mwisho watakuwa wa kwanza, na wa kwanza watakuwa wa mwisho”.

Lakini ni wakina nani hawa, ambao, watakuja kulipwa sawasawa na wale waliotaabika katika kazi ya Mungu kwa muda mrefu.

Ukitazama, utaona, wale wa mwisho, hawakuwa wanashughulika mahali popote hapo kabla.. Bali mwenye shamba alipowafuata na kuwauliza kwanini mmesimama hapa mchana kutwa wakasema “Kwa sababu hakuna mtu aliyetuajiri”.. Hii ikiwa na maana kama wangebahatika kufuatwa na mwenye shamba tangu asubuhi nao pia wangefanya kazi kubwa tu kama wale wengine, lakini hakutokea mtu wa kuwaajiri mpaka jioni.

Ikifunua kuwa, kuna watu mpaka sasa bado hawajafikiwa na neema ya wokovu, na pengine umri umeenda, labda tuseme mpagani Fulani mwabudu ng’ombe, lakini akiwa na miaka 80, ndio anahubiriwa injili na kuokoka kwa kumaanisha, na baada ya hapo anakuwa tayari kumtumikia Mungu kwa moyo wake wote, pengine akamtumikia Mungu kwa uaminifu kwa mwaka 1 tu akafa.

Au mwingine, neema imemkuta katika ujana wake, labda miaka 20 tu, lakini akatumika miaka 2 tu, alipofikisha miaka 22 akafariki.

Sasa watu kama hawa, kama walitumika kwa uaminifu kwa muda huo mfupi tu. Usishangae kuwakuta kule ng’ambo wamepewa thawabu sawa mitume. Ni kwanini? Ni kwasababu wakati neema inawafikia, na muda wao wa kutumika ulipokuja, waliandikiwa muda mchache sana. Hivyo kama wangekutwa tangu zamani ni wazi kuwa wangemtumikia Mungu kwa uaminifu.

Lakini,ikiwa wewe leo hii unaisikia neema, unaichezea, leo upo na Kristo, kesho upo na shetani, yaani hueleweki, usitazamie, Kristo atakupa thawabu yoyote, ikiwa utakufa leo katika hali kama hiyo, yaani umezaliwa katika familia ya kikristo, unajua kabisa misingi ya kiimani kwamba, pasipo wokovu huwezi kwenda popote, usitazamie, utalingana na yule mpagani au mtu wa dini nyingine ambaye kaokoa hivi karibuni, halafu akafa.

Bwana alisema wamwisho watakuwa wa kwanza, na kwanza watakuwa wamwisho. Ithamini neema uliyopewa , hizi ni siku za mwisho.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Ni muda gani Bwana Yesu alisulibiwa. Je! Ni saa 3 au saa 6?

KWANINI MTINI KATIKATI YA MIZABIBU?

NI NANI ATAKAYEUCHUKUA MSALABA WA YESU?

AINA TATU ZA WAKRISTO.

Bwana Yesu alimaanisha nini kusema “Saa yangu haijawadia?”

Rudi nyumbani

Print this post

KWANINI MTINI KATIKATI YA MIZABIBU?

Kuna baadhi ya watu Mungu anawapanda katika kanisa, kwa namna ya kitofauti na kipekee sana..

Na pengine wenyewe hawalijui hilo..hivyo wanaishi maisha ya kimaficho ficho tu..au ya juu juu tu, kwa kisingizio kuwa wao si kama wengine.. wakidhani kuwa Kristo, amewaweka hapo bure, kwasababu hiyo..

Ulishawahi kuitafakari vizuri hii habari..

Luka 13:6-9
[6]Akanena mfano huu; Mtu mmoja alikuwa na mtini umepandwa katika shamba lake la mizabibu; akaenda akitafuta matunda juu yake, asipate.
[7]Akamwambia mtunzaji wa shamba la mizabibu, Tazama, miaka mitatu hii naja nikitafuta matunda juu ya mtini huu, nisipate kitu; uukate, mbona hata nchi unaiharibu?
[8]Akajibu akamwambia, Bwana, uuache mwaka huu nao, hata niupalilie, niutilie samadi;
[9]nao ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate.

Fikiria hilo ni shamba la Mizabibu..pengine ekari elfu moja, limeandaliwa mahususi kwa ajili ya kutoa zabibu za kibishara..lakini mwenye shamba tunaona bado katikati ya shamba hilo kubwa alipanda mti mwingine wa matunda ujulikanao kama “mtini”..

Kumbuka lengo lake halikuwa apate matunda ya biashara kutoka katika mti huo..bali pengine ya kula tu, na ndio maana mtini wenyewe ulikuwa ni mmoja tu. Lakini bado hakutaka ukae bila matunda..akaupa muda ili uzae..

Kuna watu Mungu kawapanda katika kanisa lake, ambao wanaweza kuonekana ni tofauti sana na watakatifu wengine pengine kilugha, labda hawajui kiswahili vizuri, au kimazingira, labda wapo mbali, au kinafasi, ni viongozi wakubwa n.k.na hivyo hawawezi moja kwa moja kutumika kama hawa wengine..kwa vikwazo hivyo.

Lakini wengi wa hawa huwa wanaishi maisha ya kujificha, wakidhani pengine sio sehemu ya kanisa la Kristo.

Nataka nikuambie, vyovyote vile ujionavyo..Kristo anatazamia matunda kutoka kwako. Anataka aone ukristo wako ukiangaza kwa wengine..anataka kuona unafanya kitu kwa ajili ya ufalme wa mbinguni..anataka kuona shamba lake alilokuweka wewe ndani yake pamoja na hao wengine hulikalii bure…na wewe pia kwa nafasi yako uhakikishe unazaa matunda..

Hizi ni siku za mwisho ndugu yangu..Kristo anasema Naja upesi, na ujira wangu, upo mkononi mwangu kumlipa kila mtu..sawasawa na kazi yake ilivyo..

Ufunuo wa Yohana 22:12
[12]Tazama, naja upesi, na ujira wangu u pamoja nami, kumlipa kila mtu kama kazi yake ilivyo.

Utalipwa nini siku ile..ikiwa miaka nenda rudi, wewe ni msikiaji tu wa injili, miaka nenda rudi upo tu mafichoni, hutaki ijulikane..jiulize Ni nini umemfanyia Bwana basi..mpaka akupe ufalme siku ile?

Bwana atutie nguvu, tutambue kuwa sote tupo shambani mwake..na sio jukumu la askofu fulani au shemasi. Na kwamba Bwana atamvumilia mtakatifu yoyote katika shamba lake asiyemzalia matunda.

Tafadhali shea na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

Jiunge na kundi letu la mafundisho ya Biblia whatsapp kwa kubofya hapa > Group-whatsapp

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post

Na alaaniwe ampigaye mwenzake kwa siri.

SWALI: Nini maana ya huu mstari

Kumbukumbu 27: 24 “Na alaaniwe ampigaye mwenzake kwa siri. Na watu wote waseme Amina”.


SWALI: Kulingana na sheria ya wayahudi, kosa lolotela kumdhuru mwenzako, liwe ni dogo au kubwa, lilipoonekana, adhabu yake ilitolewa palepale kulingana na kosa lenyewe.. kwamfano ukimng’oa mwenzako jino, na wewe pia uling’olewa la kwako, ukimtoa jicho, na lako pia linatolewa, ukiua na wewe pia uliuliwa,..hapo ndipo uovu ulipoweza kuondoka juu ya mtu.

Lakini kulikuwa na makosa mengine watu waliyafanya kwa siri, ambayo hayakuwa rahisi kugundulika kwa wazi, wanashangaa tu labda mtu kafa, wakidhani ni siku yake tu imefika, kumbe aliwekewa sumu siku nyingi ambayo ilikuwa inamuua kwa taratibu..

Sasa watu kama hawa, biblia inasema, wamelaaniwa, kwasababu wanawapiga wenzao kwa siri, wakidhani kuwa hata mbele za Mungu hawataonekana.

Mfano wa watu kama hawa katika biblia ni Yezebeli. Yeye alikwenda kumuua Nabothi Myezreeli, ili tu alipate shamba lake, akawaajiri watu wa kushuhudia uwongo waseme wamemsikia Nabothi amemtukana Mungu na mfalme, ili watu wampige mawe afe, na kweli akafanikiwa adhma yake, na watu hawakujua lolote.

Lakini Mungu alijua, ndipo akamtuma nabii Eliya kumtolea hukumu yake. Na kumwambia mbwa watamla maiti yake. Na kweli ndivyo ilivyokuja kuwa (1Wafalme 21).

Mwingine ni mfalme wa Daudi, yeye alimuua askari wake aliyeitwa Uria kwa siri akidhani kuwa Mungu hatamwona. Alichofanya ni kumwambia mkuu wake wa majeshi amweke, Uria mahali penye vita vikali, kisha wamuache mwenyewe, ili azidiwe na majeshi ya adui auliwe, na kweli, njama zake zilifanikiwa, lakini Mungu akamrudia Daudi na kumpa adhabu kali sana, na doa ambalo mpaka leo hii sisi tunalisoma (2Samweli 11).

Hata leo, watu wanawapiga wenzao kwa siri, kwa kuwawekea vikwazo mbalimbali, lakini kwa nje wanajifanya wapo Pamoja na wao kuwasaidia, tukiwa watu wa hivi Mungu atatulaani. Halikadhalika Wachawi wote wapo chini ya hii laana, kwasababu mchana wanacheka na wenzao kinafki, lakini usiku wanazunguka huku na huko kuwanga, na kuwasababishia wenzao madhara, na kuvuruga mipango ya watu wanaotaka kumtafuta Mungu.

Hivyo tuwe makini sana, ni heri uadhibiwe na mwanadamu, kuliko kuangukia katika laana za Mungu mwenyewe. Kwasababu yeye ndiye anayeichunguza mioyo ya watu. Ili tuweze kuishinda hii hali, hatuna budi kumaanisha kumfuata Kristo kweli kweli katika Maisha yetu. Hapo ndipo tutakapoweza kuishi Maisha ya upendo na wengine.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Mlima Gerizimu na Ebali ni ipi, na umuhimu wao rohoni ni upi?

Nini maana ya mstari huu: (Mtu ambarikiye mwenzake kwa sauti kuu asubuhi na mapema; Itahesabiwa kuwa ni laana kwake.Mithali 27:14 )?

MAAGIZO AMBAYO HAYAJAAGIZWA!

Ni SIRI gani Paulo aliyokuwa anaimaanisha katika Waefeso 5:32?

Kuwaogopa wanadamu huleta mtego,(Mithali 29:25)

Rudi nyumbani

Print this post

UDHURU NI NINI KIBIBLIA?

Shalom, karibu tujifunze na tujikumbushe wajibu wetu sisi kama watakatifu katika safari yetu ya Imani hapa duniani.

Kuna mambo ambayo tunaweza tukashindwa kumfanyia Mungu, tukadhani kuwa “Mungu anaelewa”, kumbe yanatafsirika kama Ni UDHURU mbele zake.

Tofauti na sisi tunavyoweza kutafsiri Neno udhuru. Kwamba ni kutoa sababu za uongo, ili tu kuepuka jukumu au wajibu Fulani, kwamfano, labda mtu kakuambia naomba ukanipakilie mzigo wangu kwenye gari pale stendi unitumie.. Sasa pengine wewe hutaki kwenda, ili kupindua hiyo safari, saa hiyo hiyo unaunda safari yako ya uongo na kumwambia, hapana sitaweza kwenda, kwani ninamgeni wangu natarajia baadaye, nikamchukue hotelini sijui atatoka muda gani..Lakini unajua kabisa, jambo kama hilo hukuwa na mpango nalo, huo ndio udhuru tunaoufahamu sisi.

Lakini kwa Mungu udhuru, ni kutoa sababu za kweli tena  zenye maana na mashiko kabisa.. ambazo wakati mwingine ni kweli kabisa zinastahili kufanywa.. Ili kuelewa vizuri Embu tusome tena Habari hii kwa utulivu, naamini umeshaipitia mara kadhaa, lakini isome tena, na tena, uone ni nini Mungu analenga, na ujiangalie na wewe katika nafasi yako, Je! Mambo kama hayo yapo?,,Tusome..

Luka 14:16 “Akamwambia, Mtu mmoja alifanya karamu kubwa akaalika watu wengi,

17 akamtuma mtumwa wake saa ya chakula awaambie wale walioalikwa, Njoni, kwa kuwa vitu vyote vimekwisha kuwekwa tayari.

18 Wakaanza wote kutoa udhuru kwa nia moja. Wa kwanza alimwambia, Nimenunua shamba, sharti niende nikalitazame; tafadhali unisamehe.

19 Mwingine akasema, Nimenunua ng’ombe jozi tano, ninakwenda kuwajaribu; tafadhali unisamehe.

20 Mwingine akasema, Nimeoa mke, na kwa sababu hiyo siwezi kuja.

21 Yule mtumwa akaenda, akampa bwana wake habari ya mambo hayo. Basi, yule mwenye nyumba akakasirika, akamwambia mtumwa wake, Toka upesi, uende katika njia kuu na vichochoro vya mji, ukawalete hapa maskini, na vilema, na vipofu, na viwete.

22 Mtumwa akasema, Bwana, hayo uliyoagiza yamekwisha tendeka, na hata sasa ingaliko nafasi.

23 Bwana akamwambia mtumwa, Toka nje uende barabarani na mipakani, ukawashurutishe kuingia ndani, nyumba yangu ipate kujaa.

24 Maana nawaambia ya kwamba katika wale walioalikwa, hapana hata mmoja atakayeionja karamu yangu.

Embu zitafakari hizo sababu, uone kama hakuna hata moja isiyo na mashiko, ni kweli, sherehe tu, huwezi ifananisha na mke mpya..mwingine kanunua ng’ombe, wengi, hivyo ni lazima siku hiyo akawajaribu kwanza, vinginevyo wakiwa sio bora na siku imeshapita hawezi tena kuwarudisha,tayari ni hasara, mwingine kanunua shamba tayari, lakini bado hajaliona, hivyo ni lazima akalihakiki, kama ni lenyewe au kama ameuziwa dimbwi, na siku yenyewe ndio hiyo hiyo ya karamu aliyoalikwa hawezi kuacha kwenda?

Umeona, zote hizo zilikuwa ni sababu, lakini mwenye karamu anazitafsiri kama ni Udhuru. Kwasababu gani? Kwasababu wameyathamini mambo yao, Zaidi ya ile karamu yake kubwa.

Leo hii,watu wengi hata jumapili wameacha kwenda kanisani kabisa, wanasema, boss wangu hataki, wanazitetea kazi zao, ili wasifukuzwe..halafu kwenye vichwa vyao wanasema BWANA ANAELEWA!…Kama ingekuwa sio huyu boss wangu kunizuia, mimi nisingekosa kanisani hata siku moja..

Ndugu kwa Mungu huo ni udhuru..Kama unaweza kuitumikia kampuni yako, kwa siku 6 za wiki, hadi siku ya Mungu unaiiba, fahamu tu, Mungu hawezi kukuelewa, anautafsiri kama Udhuru. Haiwezekani wiki nzima, usijiwekee ratiba kwa Mungu wako ya kumwabudu yeye, hata siku moja.

Danieli hakuruhusu udhuru, hata alipokatazwa na mfalme wa dunia yote,(kumbuka Sio boss wa ka-kampuni fulani) kuabudu Mungu wake, na vitisho vyao vya kuwatupa katika tundu la simba wote watakaokaidi. kinyume chake Danieli ndio alifungua madirisha yake, akawa anamwabudu Mungu, wakati wengine, wanasema Mungu anaelewa, hali halisi ya sasa, tumekatazwa na mfalme, sisi ni nani tupinge..

Na walipomkamata na kumtupa katika tundu la Simba, Tunaona Mungu alikuwa naye..

Vivyo hivyo na akina Shedraka, Meshaki, na Abednego, walikataa udhuru wa Nebukadreza wa kuabudu sanamu, wakati wengine wanasema, Mungu anaelewa..wenyewe wakakataa kumvunjia Mungu heshima, ndipo walipotupwa katika tanuru la moto..Bwana aliwapigania na kuwaokoa.

Lakini ikiwa sisi kila jambo tutazama, hali zetu, tusijidanganye kuwa Mungu anaelewa! Hizo zote ni udhuru. Usiruhusu kazi ile muda wa Mungu wako, usiruhusu, familia, mihangaiko, mali zitafune muda wa Mungu wako. Wengine wanasema jumapili ndio faida ninapata, ndugu ziache hizo faida zipite, Ni nani kakuambia Mungu hatakupa hizo siku nyingine? epuka udhuru..

Na ndio maana mwishoni kabisa mwa ile Habari, Bwana anasema…

“Maana nawaambia ya kwamba katika wale walioalikwa, hapana hata mmoja atakayeionja karamu yangu”.

Watu wanaotanguliza mambo yao mbele Zaidi ya Mungu katika kipindi hichi cha siku za mwisho, kwenye Unyakuo, kwenye karamu ya mwanakondoo mbinguni hawataenda. Swali je! Na wewe ni mtu wa udhuru kwa Bwana? Jibu unalo.

Maran atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Maswali na Majibu

UFUNUO: Mlango wa 19

KITABU CHA YUDA: SEHEMU YA 3

DHIKI KUU INAKUJA NA UNYAKUO UPO KARIBU.

KWASABABU MUDA TULIOBAKIWA NAO SI MWINGI.

Rudi nyumbani

Print this post

Hapo ndipo, atakapompa Mungu Baba ufalme wake.

SWALI: Kulingana na Danieli 7:14 inatabiri kuwa Ufalme wa Bwana Yesu utakuwa ni wa milele, Lakini tukirudi katika 1Wakorintho 15:24 anasema mwishoni atampa Baba yake ufalme wake,

Je hapo inamaana gani , Bwana Yesu ataurejesha ufalme kwa Baba yake au?


JIBU: Tusome vifungu vyote..

Danieli 7:13 “Nikaona katika njozi za usiku, na tazama, mmoja aliye mfano wa mwanadamu akaja pamoja na mawingu ya mbingu akamkaribia huyo mzee wa siku, wakamleta karibu naye.

14 Naye akapewa mamlaka, na utukufu, na ufalme, ili watu wa kabila zote, na taifa zote, na lugha zote, wamtumikie; mamlaka yake ni mamlaka ya milele, ambayo hayatapita kamwe, na ufalme wake ni ufalme usioweza kuangamizwa”.

Pia..

1Wakoritho 15:24 “Hapo ndipo mwisho, atakapompa Mungu Baba ufalme wake; atakapobatilisha utawala wote, na mamlaka yote, na nguvu.

25 Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake.

26 Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti”.

Ni vema tukumbuke kuwa Mungu na Yesu, sio watu wawili tofauti, wenye falme mbili tofauti.. Hapana, “SIRI ya uungu” ni kubwa sana, kama vile mtume Paulo alivyoandika katika 1Timotheo 3:16, Ikiwa na maana mtu usipofumbuliwa macho na kuielewa sehemu ya siri hii, anaweza kudhani Bwana Yesu na Baba yake, ni watu wawili tofauti kabisa…

Ukweli ni kwamba, ufalme Yesu, ndio ufalme wa Baba yake, na Ufalme wa Baba yake ndio ufalme wa Yesu, hivyo akimrudishia Baba ufalme, hakufanyi badiliko lolote, kwasababu yeye na Baba ni kitu kimoja. Ni kama anavyopenda tu yeye mwenyewe atawalie katika ofisi ipi!! Je ya Baba au ya Mwana.. hivyo tu..

Kwahiyo Ufalme huo, kwasasa unatawala rohoni, lakini utadhihirika rasmi, tunapoingia katika ule utawala wa miaka1000, ambapo Mungu (Ndani ya Kristo), atatawala kwa miaka hiyo elfu mpaka atakapohakikisha kila kitu kiovu kimefikia mwisho wake, Kisha baada ya hapo, atatawala sasa kama Baba (Yehova), milele na milele.

Na ndio maana ufalme wake ni wa milele na milele na milele.. Ambao hauwezi kuhasika na kwenda kwa adui, au kwa Malaika yoyote, au kwa kiumbe chochote, utabaki kwake milele na milele na milele. Utukufu na shukrani vimrudie yeye daima.

Amen.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

YESU NI NANI?

Tofauti kati ya ufalme wa mbinguni na ufalme wa Mungu ni ipi?

DANIELI: Mlango wa 11

TUMEFANYIKA KUWA WANA WA MUNGU!

UNYAKUO.

Rudi nyumbani

Print this post

MUME / MKE BORA KUTOKA KWA BWANA UTAMWONA UKIWA KATIKA MAZINGIRA GANI?

Nakusalimu katika jina kuu sana la Bwana wetu Yesu Kristo. Karibu tujifunze Neno la Mungu ili tupate maarifa sahihi ya kuishi hapa duniani.

Na leo tutaona mazingira ambayo ukikaa katika hayo basi Mungu atakujalia umwone mke/mume sahihi aliyekuchagulia toka mbali.

Tofauti na mazingira ya kiulimwengu ambayo yenyewe ili yakupe mke/mume wa kidunia ni sharti uwe katika mazingira ya kidunia..yaani uvae vimini, ujitembeze na suruali barabarani, unyoe viduku, uishi kama wasanii wa kidunia, uwepo disco na kwenye party party kila wakati n.k. ili uonekane.

Ukikaa katika mazingira kama hayo hakika dunia itakupatia unachokitafuta..

Lakini leo tutajifunza mazingira ya ki-Mungu… Ili Mungu akuonyeshe mke/mume sahihi tokea mbali je! Ukae katika mazingira gani.?

Tutamtazama Isaka mtoto wa Ibrahimu. Kama wewe ni msomaji wa biblia utakumbuka mpaka wakati mama yake anakufa hakuwa na mke bado.

Lakini siku moja Baba yake alipoona ni wakati sasa wa Isaka kuwa na mke alimtuma Kijakazi wake mmoja kwenda kumtafutia mke kutoka katika nchi ya mbali nchi sana ya baba zake. ..kwani hakutaka kumpatia mke kutoka katika miji ile waliyokuwepo.

Kuonyesha kuwa haijalishi utazungukwa na vijana wengi wazuri mahali ulipo, hiyo bado haikufanyi udhani mke/mume Mungu aliyekuchagulia ni lazima atoke hapo.

Sasa utaona mara baada ya yule kijakazi kutumwa kwenda kumtafutia Isaka mke na kumpata alipokuwa anarudi..Huku nyuma kuna tabia na desturi ambayo Isaka alikuwa nayo ambayo nataka leo tuione kwasababu hapa ndipo kiini cha somo letu kilipo.. Tusome..

Mwanzo 24:62-66

[62]Basi Isaka alikuwa amekuja kwa njia ya Beer-lahai-roi, maana alikaa katika nchi ya kusini.
[63]Isaka akatoka ili kutafakari kondeni wakati wa jioni; akainua macho yake, akaona, kuna ngamia wanakuja.
[64]Rebeka akainua macho, naye alipomwona Isaka, alishuka juu ya ngamia.
[65]Akamwambia mtumishi, Ni nani mtu huyu ajaye kondeni kutulaki? Mtumishi akasema, Huyu ndiye bwana wangu. Basi akatwaa shela yake akajifunika.
[66]Yule mtumishi akamwambia Isaka mambo yote aliyoyatenda.

Rudia tena Mstari wa 62 unasema…

‘Isaka akatoka ili kutafakari kondeni wakati wa jioni’.

Unaona, Pindi tu alipotoa mguu wake na kwenda kondeni kutafakari..alipojijengea desturi ya kwenda maporini mbali na makazi ya watu ili tu kupata utulivu na Mungu wake, kuutafakari ukuu wake na uweza wake na maajabu yake na ahadi zake..huko huko Mke wake alitokea..na akamwona tokea mbali..

Pengine yeye alidhani mjini alikoondoka ndipo wake wanapotokea lakini..alishangaa kule kule kondeni kwa mbali sana ngamia wanakuja wamembeba bibi arusi wake..

Hiyo ni kuonyesha Isaka haukuwa na hulka kama za vijana wengine walizokuwa nazo..alipendelea zaidi kumtafakari Mungu kuliko kuzurura zurura huko na huko.

Matokeo yake akampata Rebeka, mwanamke ambaye tunamsoma mpaka leo, licha ya kuwa alikuwa ni mwanamke anayemcha Mungu lakini bado alikuwa ni mzuri sana wa uso..Mwanzo 26:6-7

Ndugu, ikiwa unamuhitaji mke mzuri na anaye mcha Mungu basi kuwa kama Isaka..lakini ikiwa unamuhitaji Yezebeli basi ishi mfano wa hao vijana wa kidunia wanavyoishi leo hii..

Na hili pia lipo kwa upande wa pili wa mabinti..ikiwa unataka uolewe na mwanamume ilimradi tu mwanamume basi jiweke kama hao mabinti wa kidunia wanavyojiweka wanaotembea nusu uchi barabarani na kujipambapamba kama vile Yezebeli ili waonekane wanavutia..
Utampata unayemtafuta.

Lakini kinyume chake ni kuwa ukitulia katika kusudi la Mungu..unatumia muda mrefu kwa Mungu wako kuliko kutanga tanga..unamtakafakari tu yeye..nakwambia Mungu utakuongoza kwa Isaka wako tokea mbali..kama vile Rebeka alivyomwona Isaka akimfuta kutokea mbali..

Uhitaji kujionyesha onyesha ovyo..kwasababu anayekuletea mke/mume ni Mungu, si mwanadamu..wewe kaa katika kumtakafakari yeye maisha yako yote.

Kuoa utaoa, kuolewa utaolewa tu!..ukiishi maisha yanayopendeza Mungu si uongo utakutendea tu.

Daudi alisema..

Zaburi 37:25
[25]Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee,
Lakini sijamwona mwenye haki ameachwa
Wala mzao wake akiomba chakula.

Mungu hawezi kuacha kumpa mteule wake kitu kilicho chema, na kizuri.. Hawezi kuruhusu mke/mume pasua kichwa atokee mbele ya njia yake, mtu anayemcha yeye. Hilo haliwezekani..

Hivyo kama bado hujaokoka. Tubu leo anza maisha yako upya na Bwana Yesu kwa kumaanisha kabisa..Toba ya kweli inaambatana na kuucha ulimwenguni, mkatae shetani na kazi zake zote na vimini vyake vyote, na suruali zote na viduku vyote..kamtafakari Mungu huko makondeni, hata kama utaonekana mshamba..

Ishi maisha ya kumlingana Bwana..Na bila shaka wakati utafika atamtuma malaika wake kwenda kukuletea mwenzi sahihi..Kama Ibrahimu alivyomtuma kijakazi wake, kumletea Isaka Rebeka.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

KWANINI NDOA NYINGI ZINAVUNJIKA? (Sehemu ya 1: Upande wa wanaume)

Sadaka ya unga na sadaka ya kinywaji zilikuwaje?

Je! “Mke wa ujana wako” ni yupi kibiblia?

Rudi nyumbani

Print this post

Nini maana ya “Mpe kileo yeye aliye karibu na kupotea;?

SWALI: Nini maana ya huu mstari,

Mithali 31:6 “Mpe kileo yeye aliye karibu na kupotea; Kampe divai yeye aliye na uchungu nafsini.

7 Anywe akausahau umaskini wake; Asiikumbuke tena taabu yake”.

Je tunaruhusiwa kunywa pombe, tunapokuwa katika shida?


JIBU: Kumbuka agano la kale lilikuwa ni agano la mwilini, hivyo walitafuta kila mbinu za  mwilini ili kutatua matatizo ya mtu, kwamfano utaona ilikuwa ili kutatua tatizo la zinaa na migororo katika ndoa, waliruhusiwa kutoa talaka, au kuoa wake wengi. Lakini jambo kama hili haukuwa mpango wa Mungu tangu mwanzo.

Mathayo 19:7 “Wakamwambia, Jinsi gani basi Musa aliamuru kumpa hati ya talaka, na kumwacha?

8 Akawaambia, Musa, kwa sababu ya ugumu wa mioyo yenu, aliwapa ruhusa kuwaacha wake zenu; lakini tangu mwanzo haikuwa hivi”.

Na  ndio maana utaona, japokuwa waliruhusiwa kufanya hivyo, lakini bado tatizo la uzinzi halikutatuliwa lote, kwamfano Daudi alikuwa na wake wengi, pamoja na Masuria wengi, lakini bado hakuacha kwenda kutafuta wake za watu, na kuzini nao (Mke wa Uria). 2Samweli 11&12..Kwasababu kiu ya uzinzi haizimwi kwa kuoa wake wengi.

Vivyo hivyo, Na katika masuala ya kuondoa huzuni, au uchungu moyoni, walikuwa na desturi, kwamba mtu aliye katika hali hiyo, mfano kama kafiwa na watoto wake wote, au mke n.k. kama vile Ayubu Walikuwa wanawapa pombe, wanywe kwa kipindi hicho iwasahaulishe matatizo yao. Lakini hilo halikufanikiwa kwa wakati wote, kwasababu pombe ikiisha tu kichwani, huzuni yake inarudia tena pale pale..kwasababu kiu ya huzuni haiwezi kukatwa kwa pombe..Mungu aliruhusu tu iwe hivyo kwa muda, kwasababu ya mazingira waliyokuwa nayo kwa wakati ule, lakini halikuwa kusudi lake tangu mwanzo.

Na ndio maana sasa katika wakati wa agano jipya Mungu alileta suluhisho la moja kwa moja la mambo yote rohoni na suluhisho lenyewe ni ROHO MTAKATIFU.

Bwana Yesu  alisema..

Yohana 7:37 “Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe.

38 Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake.

39 Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa”

Roho Mtakatifu akishaingia ndani ya mtu, anafanya kazi ambayo pombe imeshindwa, madawa ya kulevya yameshindwa, anamwondolea mtu hofu yote, uchungu wote, tamaa yote, wasiwasi wote na mashaka yote, na kiu yote ya uovu milele. Na ndio maana mtu aliyejazwa na Roho Mtakatifu vizuri huwa anaonekana kama mlevi, mtu asiyejali ni nini anakipitia saa hiyo..Kama tunavyoona siku ile ya Pentekoste.

Matendo 2:15 “Sivyo mnavyodhani; watu hawa hawakulewa, kwa maana ni saa tatu ya mchana;

16 lakini jambo hili ni lile lililonenwa kwa kinywa cha nabii Yoeli,

17 Itakuwa siku za mwisho, asema Mungu, nitawamwagia watu wote Roho yangu, na wana wenu na binti zenu watatabiri; na vijana wenu wataona maono; na wazee wenu wataota ndoto”.

Hivyo, sisi hatuna ruhusu ya kunywa pombe, kwasababu ndani ya pombe, biblia inasema upo UZINZI, na matendo mabaya, lakini katika Roho Mtakatifu upo uhuru. Ukinywa pombe unatenda dhambi.

Waefeso 5:18 “Tena msilewe kwa mvinyo, ambamo mna ufisadi; bali mjazwe Roho;”

Kwahiyo mstari huo hauhalalishi ulevi, kama tu vile uoaji wa wake wengi usivyokuwa halali sasa, japokuwa uliruhusiwa katika agano la kale.

Tutambue ujumbe wa saa tunayoishi.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

JE! ULEVI NI DHAMBI?.

Nini maana ya msiwe waalimu wengi (Yakobo 1:3)?

Je Lutu alikwenda kuwahukumu watu wa Sodoma na Gomora? Kulingana na Mwanzo 19:9?

USIJITUMAINISHE JUU YA SIRA YAKO ANGALI UPO KATIKA DHAMBI.

Nini maana ya Usiwe mwovu kupita kiasi? (Mhubiri 7:17)

Rudi nyumbani

Print this post

Je! Ni kweli Yesu alirejesha kila kitu kama pale Edeni?

SWALI:Tunasema Yesu karejesha kila kitu Adamu alichopoteza pale Edeni, Lakini kiuhalisia mbona hajarejesha kila kila kitu, mbona tunaona kifo bado kipo, mbona waovu ndio wanaotawala dunia, mbona magonjwa na ajali vinakithiri duniani?


JIBU: Ni kweli kabisa Bwana wetu Yesu Kristo, amekabidhiwa umiliki wa vitu vyote, Kuanzia juu mbinguni, mpaka huku duniani, vyote vipo chini yake. Na kazi kuu aliyokuja kuifanya ni kuvirejesha vyote vilivyoharibiwa na adui, katika nafasi yake, na hata Zaidi yah apo.

Mathayo 11: 27a Akasema, Nimekabidhiwa vyote na baba yangu;..

Soma pia,

Waefeso 1:20 “…. akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho;

21 juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia;

22 akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo

23 ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote”.

Basi kama ni hivyo, utauliza ni kwanini basi, hatuoni mamlaka yake yote yakitimia ulimwenguni?

Jambo ambalo watu wengi hawajui ni  kuwa, Huduma ya Bwana wetu Yesu Kristo haijaishia pale tu alipopaa kwenda mbinguni..bali aliondoka kwa muda tu, akaahidi kurudi, Na ndio maana ujio wake,aliugawanya mara  mbili, ambapo mara ya kwanza alikuja kwa lengo la kuokoa roho za watu na mauti, ndipo hapo akalazimika kufa msalabani, ili damu ipatikane kwa ajili ya ondoleo la dhambi. Hivyo kipindi chote hicho hakuhangaika, na mambo yoyote ya mwilini, au ya kiutawala, au ya kijeografia japokuwa alikuwa amekabidhishwa vyote.

Lakini ujio wake wa pili, hautakuwa tena kama ule wa kwanza, wenye lengo la wokovu wa roho za watu..Hapana, bali atakuja mahususi kwa lengo la kuukomboa huu ulimwengu na mifumo yake yote mibovu, Hapo ndipo atakapokuja kama mtawala, yaani MFALME WA WAFALME na BWANA WA MABWANA. Katika ule utawala wa miaka 1000 (Ufunuo 19:16)

Sasa atakapokuja katika awamu hii,

1) jambo la kwanza atakalofanya ataleta Amani duniani. Kutimiza lile andiko kwamba siku ile Mbwa-mwitu atalala Pamoja na mwana-kondoo, mtoto anyonyaje atacheka kwenye tundu la nyoka. (Isaya 11:5-9, 65:25)

2) Pili atadhibiti uchungu; Watu hawatazaa t tena kwa uchungu (Isaya 65:23)

3) Tatu atabidhibiti, magonjwa na maajali: Hilo ndilo litakalowafanya watu waweze kuishi miaka mingi hata karibia na 1000. (Isaya 65:20). Biblia inasema kipindi hicho, mtu atayekufa na miaka mia ataitwa mtoto mchanga.

4) Nne atadhibiti uharibifu: Yaani Hutajenga, akakaa mwingine, wala hutapanda akala mwingine..(Isaya 65:22)

5) Tano atadhibiti dhambi: Kumbuka wakati huo shetani atakuwa amefungiwa, na mtu yeyote atakayeonyesha dalili za uvunjifu wa amani, fimbo ya chuma, itamlalia.(Ufunuo 12:5)

6) Na mwisho kabisa atamalizana na  MAUTI, huyu ndiye adui wa mwisho.

Kiasi kwamba hakutakuwa na kifo tena ulimwenguni, wala machozi, wala maombolezo.

Hapo ndipo atakamporejeshea Baba mamlaka yote. Na kazi yake itakuwa imekwisha ya ukombozi. Na ndio hapo tutaingia katika ile mbingu mpya na nchi mpya, ambayo Jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia.

1Wakorintho 15:24 “Hapo ndipo mwisho, atakapompa Mungu Baba ufalme wake; atakapobatilisha utawala wote, na mamlaka yote, na nguvu.

25 Maana sharti amiliki yeye, hata awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake.

26 ADUI WA MWISHO ATAKAYEBATILISHWA NI MAUTI”.

Hivyo, kwa kipindi hichi tulichopewa hapa katikati, tangu siku alipopaa hadi sasa, ni kuhakikisha kila mmoja, anaupokeo huo ukombozi wa roho yake, kwa gharama yoyote ile. Na hiyo inakuja tu kwa kumwamini Yesu Kristo, na kumpokea Roho wake.

Lakini kama mtu atakutwa katika hali ya dhambi hadi siku anayorudi mara ya pili, ajue kuwa hakuna neema tena ya ukombozi juu yake kwasababu Kristo ameshabadili ofisi. Wakati huo, atawaangamiza waovu wote kwa kuwaua kwa pumzi yake (Ufunuo 19:21). Kisha kwenda kuwatupa katika ziwa la moto.

Hivyo, uovu unaouna leo hii duniani ni wa kitambo tu, vita unavyoviona, uchungu, magonjwa na vifo, vyote vina muda mfupi. Hivi karibu Bwana anarudi, kuja kutawala na sisi kwa muda wa miaka 1000. Ndani ya hichi kipindi kila kitu kitarejeshwa katika hali yake.

Na ndio maana huna sababu ya kukimbizana na huu ulimwengu mbovu, ambao tumezungukwa na hatari ya kila namna, ndugu jiwekee hazina mbinguni, kwenye huo ulimwengu ujao wa amani unaokuja.

Lakini kwa bahati mbaya si wote watapokea neema hii ya kutawala na Kristo. Ikiwa utakufa leo katika hali yako ya dhambi. Utabakia huko huko makaburini hadi siku ile ya ufufuo, kisha uhukumiwe na kutupwa motoni.

Je! Bado unaendelea katika dhambi zako? Bado unaichezea tu hii neema? Kisa Kristo ni mpole sasa kwako unadhani atakuvumilia hivyo katika hali yako ya dhambi milele ? Ndugu yangu. Bwana Yesu Kristo ni mkuu kuliko unavyoweza kufikiri, utalithibitisha hilo, siku ile atakaporudi mara ya pili. Ambapo biblia inasema kila kinywa kitakiri, na kila goti litapigwa. Na mataifa watamwombolezea.

Heri ukampa Yesu Kristo Maisha yako angali bado una muda mchache, hivi karibuni Parapanda italia, Na Kristo atabadili ofisi yake.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

KWANINI YESU NI ADAMU WA PILI?

Kwanini Mungu aliwaita Adamu na Hawa jina moja?

TAFAKARI SANA KABLA YA KUAMUA HATIMA YAKO.

Biblia inaposema “Wote tumetenda dhambi” si inamaanisha hakuna mtakatifu duniani?

HUTATAMBUA LOLOTE, SIKU YA UNYAKUO IKIFIKA.

Rudi nyumbani

Print this post

Hakitaingia kamwe cho chote kilicho kinyonge.(Ufu 21:27)

SWALI; Naomba kuuliza katika ufunuo 21:27 kwamba hakitaingia kilicho kinyonge hili neno kinyonge linamaanisha nini? Je ni watu dhaifu mfano vilema?


Ufunuo wa Yohana 21:27
[27]Na ndani yake hakitaingia kamwe cho chote kilicho kinyonge, wala yeye afanyaye machukizo na uongo, bali wale walioandikwa katika kitabu cha uzima cha Mwana-Kondoo.

JIBU: “Kinyonge” kinachozungumziwa hapo si mtu mlemavu, kama ingekuwa hivyo Bwana Yesu asingesema..kiungo chako kimoja kikikukosea king’oe ni heri uingie mbinguni mlemavu kuliko kuwa viungo vyako vyote na kuishia kuzimu.(Mathayo 5:29-30)

Lakini kinyonge kinachozungumziwa hapo ni kipi?

Kitu kinyonge sikuzote ni kitu kisichokuwa na nguvu ya kustahimili mtikisiko fulani aidha mapigano,ugonjwa,Dhoruba, mateso n.k.

Vivyo hivyo katika roho mtu asiyekuwa na nguvu ya kuushinda ulimwengu huyo ni sawa na mnyonge. Na ndio maana Bwana Yesu alisema maneno haya..

Mathayo 11:12
[12]Tangu siku za Yohana Mbatizaji hata sasa ufalme wa mbinguni hupatikana kwa nguvu, nao wenye nguvu wauteka.

Utajiuliza ni kwanini Bwana arejee siku za Yohana mbatizaji, na sio siku za labda, Isaya, au Musa, au Samweli? Bali Yohana Mbatizaji?

Alisema hivyo, ili kutupa picha na sisi tunapaswa tuishi Maisha ya kuukana ulimwengu, mfano wa Yohana mbatizaji..Ambaye biblia inasema Maisha yake yote, aliishi majangwani mbali na ulimwengu, na matokeo yake akawa akiongezeka nguvu rohoni kila siku (Luka 1:80).

Hivyo na sisi tunapaswa tuushinde ulimwengu, ili tuweza kuuteka ufalme wa Mungu, ikiwa uzinzi utatushinda, ikiwa anasa na tamaa za ujanani zitatushinda, basi sisi ni wanyonge, na hivyo, kamwe hatutakaa tuuingie ule mji mpya wa Yerusalemu, utakaoshuka kutoka mbinguni. Kwasababu watakaoingia kule ni watakatifu tu walioushinda ulimwengu, na si vinginevyo.

Huu si wakati wa kuikumbatia dhambi..na kusema kwamba mimi siwezi kuushinda ulimwengu, ni wajibu wako kushindana mpaka ushinde…hupaswi kuwa mnyonge. Kumbuka wewe ukishindwa haimaanishi kuwa mwingine kashindwa.

Lakini tutawezaje kufikia hapo?

Tutafika kwa njia moja tu nayo ni  kwa kumaanisha kabisa kuacha dhambi, na kujitwika misalaba yetu na kumfuata Yesu kwa gharama zozote zile.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post