Je aliyezungumza na Musa kule jangwani ni Mungu mwenyewe au malaika wake?

Je aliyezungumza na Musa kule jangwani ni Mungu mwenyewe au malaika wake?

Katika kitabu cha Kutoka 3:2, tunasoma ni Malaika wa Mungu ndiye aliyemtokea Musa, lakini tukiendelea mbele katika Mstari wa 4, tunaona ni Mungu ndiye anayezungumza na Musa, na si Yule malaika tena, hapo imekaaje?

Jibu: Tuisome habari hiyo…

Kutoka 3: 2 “Malaika wa Bwana akamtokea, katika mwali wa moto uliotoka katikati ya kijiti; akatazama, na kumbe! Kile kijiti kiliwaka moto, nacho kijiti hakikuteketea

3 Musa akasema, Nitageuka sasa, niyaone maono haya makubwa, na sababu kijiti hiki hakiteketei.

4 Bwana alipoona ya kuwa amegeuka ili atazame, Mungu akamwita kutoka katikati ya kile kijiti, akasema, Musa! Musa! Akasema, Mimi hapa.

5 Naye akasema, Usikaribie hapa; vua viatu vyako miguuni mwako; maana mahali hapo unaposimama ni nchi takatifu.

 6 Tena akasema, Mimi ni Mungu wa baba yako, Mungu wa Ibrahimu, Mungu wa Isaka, na Mungu wa Yakobo. Musa akaficha uso wake; kwa maana aliogopa kumwangalia Mungu”.

Aliyemtokea Musa ni Malaika wa Mungu, na si Mungu mwenyewe… na malaika huyo alimtokea katika mwonekano wa Moto.. (kumbuka malaika wanaweza kuchukua mfano wa umbile lolote, wanaweza kuchukua umbile la mtu, au moto, au mwanga), wanapochukua umbile la kibinadamu wanaonekana kama wanadamu, mfano wa yule aliyemtokea Yoshua katika kitabu cha Yoshua 5:14, wanapokuja katika maumbile haya wanakuwa kama watu kabisa, wanaweza kuonekana na kuzungumza. Kadhalika wanaweza kuja katika maumbile kama ya mwanga au moto..katika maumbile haya, unaweza kusikia sauti tu na usione mtu..ukaona tu huo mwanga au moto!. N.k

Sasa Malaika huyu alitumwa na Mungu kwa Musa akiwa amebeba ujumbe wa Mungu, na alimtokea Musa katika umbile la Moto, maana yake Musa aliona moto tu kwenye kile kijiti na kusikia sauti lakini hakuwa anaona mtu.

Sasa jambo moja la kujifunza ni kwamba, Malaika wanapobeba ujumbe wa Mungu, na Mungu anapoweka jina lake ndani yako,na kuwatuma, wanaweza kutoa ujumbe kana kwamba ni Mungu mwenyewe ndiye anasema ndani yao..Sasa katika huyu Malaika aliyezungumza na Musa, Mungu alikuwa ameweka neno lake ndani yake, kiasi kwamba lolote atakalozungumza ni Mungu ndio kazungumza…(Sasa sio kwamba ni lolote atakalojiamulia tu yeye kusema!..hapana..bali ni lile ambalo Mungu atakalomwambia alifanye na kulisema ndilo atakalolisema).. Tunaweza kusoma hilo vizuri…

Kutoka 23:20 “Tazama, mimi namtuma malaika aende mbele yako, ili akulinde njiani na kukupeleka mpaka mahali pale nilipokutengezea.

 21 Jitunzeni mbele yake, MWISIKIZE SAUTI YAKE; wala msimtie kasirani; maana, hatawasamehe makosa yenu; kwa kuwa JINA LANGU LIMO NDANI YAKE.

22 LAKINI UKIISIKIZA SAUTI YAKE KWELI, NA KUYATENDA YOTE NINENAYO MIMI; ndipo mimi nitakuwa ni adui wa adui zako, na mtesi wa hao wakutesao”.

Hapo mstari wa 22, anasema “lakini ukiisikiza sauti yake kweli, na kuyatenda yote ninenayo mimi”..Maana yake “Bwana atanena kupitia yule malaika, chochote Yule malaika atakachokisema ni Bwana kakisema”. Jambo hilo liliwezekana kwa malaika tu! ila kwa sehemu ndogo! (si wakati wote Mungu alizungumza na watu kupitia malaika wake kama alivyofanya kwa Musa hapo)..…

Lakini zamani hizi limewezekana kwa asilimia zote kupitia mmoja tu YESU KRISTO!! MKUU WA UZIMA.. Huyo amefanyika bora kupita malaika, akisema ni Mungu kasema asilimia 100!, Maneno yake ni Maneno ya Mungu,..kwasababu amefanyika Bora kupita malaika haleluya!!! (Tutakuja kuliona hilo vizuri mbeleni kidogo!!).

Lakini tukirudi katika upande wa Malaika aliyezungumza na Musa, tunaona baadaye, mbeleni kabisa wana wa Israeli walipoanza kuzembea kuwafukuza wale wenyeji wa miji ile, tunaona Yule malaika aliyepewa maneno ya Bwana kinywani mwake, akitokea na kuanza kuzungumza, kana kwamba ni Bwana mwenyewe ndiye anayezungumza…

Waamuzi 2:1 “Kisha malaika wa Bwana alikwea juu kutoka Gilgali kwenda Bokimu. Akasema, Mimi nimewaleta ninyi mkwee juu kutoka nchi ya Misri, nami nimewaleta hata nchi niliyowaapia baba zenu; nami nilisema, Mimi milele sitalivunja hilo agano langu nililoagana nanyi;

2 nanyi msifanye agano lo lote na hawa wenyeji wa nchi hii; zipomosheni nchi madhabahu zao; lakini hamkuisikia sauti yangu; je! Mmefanya haya kwa sababu gani?

 3 Basi kwa ajili ya hayo mimi nilisema zaidi, Mimi sitawafukuza watoke mbele zenu; lakini watakuwa kama miiba mbavuni mwenu, na miungu yao itakuwa ni tanzi kwenu.

4 Ikawa, hapo huyo malaika wa Bwana alipoyanena maneno haya, kuwaambia wana wa Israeli wote, ndipo hao watu wakainua sauti zao na kulia

5 Nao wakaliita jina la mahali pale Bokimu; nao wakamchinjia Bwana sadaka huko”.

Umeona hapo?..aliyewatoa wana wa Israeli Misri kuwapeleka Kaanani ni Bwana, na si malaika, lakini Bwana alimpa Malaika wake jukumu zima, na vile vile, aliweka maneno yake ndani ya Yule malaika, kiasi kwamba atakachokinena Malaika yule, ni Bwana kakinena, na atakachokifanya malaika Yule ni Bwana kakifanya, vile vile Agano lake aliliweka ndani ya Yule malaika, kiasi kwamba atakayevunja agano lile la Yule malaika, ni sawa kalivunja agano la Mungu..kwasababu Neno lake limejaa ndani ya Malaika yule, anakuwa si yeye tena, bali ni Mungu anazungumza ndani yake.

Sasa katika agano hilo la kwanza, Mungu alizungumza ndani ya Malaika, lakini si wakati wote,(wakati mwingine Bwana alisema pasipo kuwatumia hao malaika).. lakini katika agano jipya, Mungu amejitwalia chombo chake, ambacho ametia maneno yake yote ndani yake, na agano lake lote ndani yake, zaidi ya alivyofanya kwa malaika…Chombo hicho hakina pumziko, wakati wote kikinena ni Mungu kanena..na chombo hicho si kingine zaidi ya Bwana Yesu…Huyu kafanyika bora kuliko malaika!!..

Waebrania 1:1  “Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa sehemu nyingi na kwa njia nyingi,

2  mwisho wa siku hizi AMESEMA NA SISI KATIKA MWANA, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu.

3  Yeye kwa kuwa ni mng’ao wa utukufu wake na chapa ya nafsi yake, akivichukua vyote kwa amri ya uweza wake, akiisha kufanya utakaso wa dhambi, aliketi mkono wa kuume wa Ukuu huko juu;

4  AMEFANYIKA BORA KUPITA MALAIKA, KWA KADIRI JINA ALILOLIRITHI LILIVYO TUKUFU KULIKO LAO”

Umeona sauti ya Mungu leo ipo wapi?..umeona agano la Mungu leo lipo wapi?..si kwa mwingine zaidi ya kwa YESU!.. Huyo ni zaidi ya Yule malaika aliyezungumza na Musa pale kwenye ule mwali wa Moto.. Na kama agano la kwanza ambalo Bwana alinena kupitia malaika lilikuwa na utukufu mkubwa vile, kiasi kwamba yeyote atakayelivunja neno la malaika Yule alikufa,. hili la pili ni mara nyingi zaidi..biblia inasema hivyo..

Waebrania 2:1 “Kwa hiyo imetupasa kuyaangalia zaidi hayo yaliyosikiwa tusije tukayakosa.

2  Kwa maana, IKIWA LILE NENO LILILONENWA NA MALAIKA LILIKUWA IMARA, na kila kosa na uasi ULIPATA UJIRA WA HAKI,

3  sisi je! Tutapataje kupona, tusipojali wokovu mkuu namna hii? AMBAO KWANZA ULINENWA NA BWANA, kisha ukathibitika kwetu na wale waliosikia”.

Je umempokea Yesu?.. Je! Umeyakabidhi maisha yako yote kwake?..fahamu kuwa Mamlaka yote ya mbinguni na duniani kapewa yeye..na yeye ndiye sauti ya Mungu kwetu!, ukimkataa yeye umemkataa Mungu, ukimkubali yeye umemkubali Mungu..

Kama bado hujamwamini, nafasi yako ya kumpokea ndio sasa, unachopaswa kufanya hapo ulipo ni kujitenga kwa muda, kisha kupiga magoti binafsi na kumkiri Yesu kwa kinywa chako kuwa ndiye Bwana na mwokozi wa ulimwengu, na kisha kukiri makosa yako kwa kutubu, huku umedhamiria kutofanya tena dhambi hizo, na baada ya hapo haraka sana bila kuchelewa tafuta ubatizo sahihi kama bado hujabatizwa ubatizo sahihi, kumbuka ubatizo ulioagizwa na Bwana Yesu ni ule wa maji mengi na kwa jina la YESU (Matendo 2:38), na baada ya hapo, Roho Mtakatifu atakuongoza katika yote yaliyosalia, ikiwemo kukupa uwezo wa kushinda dhambi.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

Naomba kufahamu maana ya “sura ya kijiti” katika Marko 12:26.

Ni kweli Waliolala Katika Kristo Wamepotea?(1Wakor 15:18)

NATAKA REHEMA, WALA SI SADAKA!

Tofauti ya kazi ya Damu ya Yesu na Jina la Yesu ni ipi?

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments