Title August 2021

Nini maana ya “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi”?

SWALI: Biblia inamaanisha nini inaposema “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi”?


JIBU: Tusome

Mithali 22:1 “Heri kuchagua jina jema kuliko mali nyingi; Na neema kuliko fedha na dhahabu”.

Inaposema kuchagua jina jema, inamaanisha Sifa njema, kwamfano labda kwenye jamii utasikia watu wanasema mtu Fulani ni mkarimu, au fulani ana upendo, au yule ana utu, hilo tayari ni jina jema, ambalo limezalika kutokana na tabia zake nzuri, Lakini ukisikia wanasema mtu yule ni muhuni, au kibaka, au tapeli, au fisadi, au jambazi, tayari hilo ni jina baya, ambalo halijazuka hivi hivi tu, bali limeonekana katika maisha ya yule mtu.

Sasa tukirudi katika mstari huo , hapo haimaanishi mtu kuwa na mali nyingi ni vibaya.. Hapana, bali anamaanisha kuchagua mali, Zaidi ya sifa njema hiyo ndio mbaya sana.

Kwamfano, utakuta mtu anachagua kufanya kazi ya bar/ casino, kisa tu inamlipa pesa nyingine kuliko zile nyingine za kawaida. Jiulize, mtu kama huyu atatafsiriwaje katika jamii, kama sio barmaid, au kahaba? Hiyo yote ni kwasababu kachagua pesa Zaidi ya jina zuri.

Au mkristo unapoacha kumwimbia Mungu wake, unakwenda moja kwa moja kuimba jimbo za kidunia, kisa tu atapata pesa za haraka. Hajui kuwa jina lake linabadilika kutoka katika kuwa mtumishi hadi muhuni.

Au kanisa la Kristo, linaposhiriki katika kampeni za kisiasa kisa tu limeahidiwa donge nono kutoka kwa wanasiasa. Jiulize ni nini kinajengeka katika macho ya jamii? Si wataliita chama cha kisiasa na sio kanisa tena sivyo? Japo ni kweli watapata pesa lakini tayari jina lao limeshabadilika. Hakuna mtu atakayewaamini.

Vivyo hivyo na sisi katika mambo yetu ya maisha ya kila siku, Ni heri tuchague jina jema, kwamfano sio kila huduma tutoze watu pesa, tukifanya hivyo hatuwezi kuitwa wakarimu, hatuwezi kuitwa wenye utu, au wenye upendo.

Tumuige Bwana wetu Yesu Kristo ambaye alitafuta, heshima, na jina jema katika huu ulimwengu Zaidi ya kitu kingine chochote.

Luka 2:52 “Naye Yesu akazidi kuendelea katika hekima na kimo, akimpendeza Mungu na wanadamu”.

Jina jema linatupa kibali kikubwa sana cha kukaribiwa au kutumiwa na Mungu, Mfano, Kornerio alitokewa na Mungu mpaka kupewa neema ya wokovu kutokana na sifa yake nzuri katika jamii.

Warumi 10:22 “Wakasema, Kornelio akida, mtu mwenye haki, mchaji wa Mungu, aliye na sifa njema kwa taifa lote la Wayahudi, alionywa na malaika mtakatifu kutuma watu kwako, uende nyumbani kwake, apate kusikiliza maneno kwako”

Na wengine wengi utawasoma katika biblia kama vile Anania (Matendo 22:12) na Stefano, (Matendo 6:3-5) wote hawa kutokana na sifa zao nzuri, Mungu aliwatumia sana. Vivyo hivyo na sisi tuthamini jina jema, kuliko mali, au mambo ya huu ulimwengu yanayopita.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

IFAHAMU HUZUNI NA FURAHA YA MALAIKA.

Pesa za bindoni ni nini?(Marko 6:8)

Maswali na Majibu

Nini maana ya Mungu amemfanya mwanadamu mnyofu?

Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa watoto wake wote.

Rudi nyumbani

Print this post

Biblia inamaanisha nini inaposema “Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake”?

 Mithali 12:10 “Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake; Bali huruma za mtu mwovu ni ukatili”.


JIBU: Hapa ni Mungu alikuwa anaonyesha tabia za mtu mwenye haki jinsi zilivyo kwamba huruma zake haziishi tu kwa wanadamu wenzake, bali pia zitadhihirika mpaka na kwa wanyama.

Kama vile Mungu sasa anavyowajali wanyama wake, kiasi kwamba hakuna hata mmoja anayekufa bila ya yeye kujua, na vivyo hivyo na sisi tunapaswa tuwe na tabia hizo, alisema ..

Mathayo 10:29 “Je! Mashomoro wawili hawauzwi kwa senti moja? Wala hata mmoja haanguki chini asipojua Baba yenu;”

Sehemu nyingine Bwana Yesu alisema maneno haya;

Luka 14:5 Akawaambia, Ni nani miongoni mwenu, ikiwa ng’ombe wake au punda wake ametumbukia kisimani, asiyemwopoa mara hiyo siku ya sabato?

 Akimaanisha kuwa, kumbe watu wengi walikuwa wanainajisi sabato pasipo wao kujua na Mungu asiwahesabie makosa, kwa tendo tu hilo la kuwaokoa wanyama wao.

Utaona pia sehemu nyingine, Balaamu Yule nabii wa uongo alipompigia Yule punda wake, mara tatu, Mungu alichukizwa sana na kitendo kile.. Na ndio maana swali la kwanza aliloulizwa na Yule malaika ni kwanini amempiga Yule punda kiasi kile? (Hesabu 22:32)

 Kuonyesha kuwa Mungu hapendezwi na kitendo cha utesaji wanyama.

Hivyo na sisi pia kama tulikuwa na tabia za kuwatesa wanyama, au kutoijali mifugo yetu, kiasi kwamba ukimkuta mbwa unamsindikiza na mawe,tuache hizo tabia, kama wanaishi na sisi pasipo madhara yoyote, hakuna sababu ya kuwapiga piga ovyo, au kuwafuga na kutowahudumia.

Kwasababu kitendo cha kuwatendea mema, biblia inasema kinaongeza pia siku za kuishi duniani soma,

Kumbukumbu 22:6 “Kiota cha ndege kikitukia kuwa mbele yako njiani, katika mti wo wote, au chini, chenye makinda au mayai, naye koo ameatamia juu ya makinda, au juu ya mayai, usimtwae yule koo pamoja na makinda;

7 sharti umwache yule koo aende zake, lakini makinda waweza kuyatwaa uwe nayo; ili upate kufanikiwa, ufanye siku zako kuwa nyingi”.

Hiyo ndio maana ya huo mstari ..Mithali 12:10 “Mwenye haki huufikiri uhai wa mnyama wake; Bali huruma za mtu mwovu ni ukatili”.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Na hekima imejulikana kuwa ina haki kwa watoto wake wote.

HAKUNA MTU ANIONDOLEAYE, BALI MIMI NAUTOA MWENYEWE

USIRUDI NYUMA KWA KUITUMAINIA HAKI YAKO.

SINA PESA SASA, YESU ATANISAIDIA NINI?

Rudi nyumbani

Print this post

Kwanini Paulo, alihukumu wakati hukumu hairuhusiwi?

SWALI: Tukisoma katika Kitabu cha 1 Wakorintho Sura ile ya Tano, Tunaona Mtume Paulo Akizungumzia Habari Ya kutengwa Kwa Watu wenye kulichafua kanisa la Mungu,… sasa tukija katika Mstari wa 3, alisema hivi..

“ Kwa maana kweli, nisipokuwapo kwa mwili, lakini nikiwapo kwa roho, mimi mwenyewe nimekwisha KUMHUKUMU yeye aliyetenda jambo hilo, kana kwamba nikiwapo”.

Swali langu ni hili, Katika Huo mstari wa Tatu, naona Mtume Paulo anasema kwamba, mtu wa namna ile, Yaani aliye mzinzi, mlevi N.K.. yeye Amekwisha Kumuhukumu,… Sasa na Tukisoma katika kitabu cha Mathayo, 7:1, Bwana Yesu alituonya Kwamba tusihukumu, kwa maana tukihukumu mtu nasi tutahukimiwa….Sasa hapa imekaaje kaaje?


JIBU: Hukumu Mtume Paulo aliyomaanisha hapo si kuhukumu ile inayozungumziwa katika Mathayo 7..Kwamba msihukumu msije mkahukumiwa,.. Ile inayozungumziwa inakuja pale mtu anapotoa maneno yanatoa hatma ya maisha ya mtu mwingine, kana kwamba ni Mungu , kwamfano,kumwambia mwenzako wewe ni wa motoni tu, hata iweje huwezi kuokoka.  Hapo umeshahukumu. Au unapowaona wenye dhambi, kama vile mashoga, na unaanza kusema wale makafiri Mungu hawezi kuwakubali milele, dhambi zao hazifutiki,..Hapo tayari umeshahukumu.

Lakini mtume alichokimaanisha hapo sio hicho, bali alimaanisha hukumu ya ADHABU. Yaani kuadhibiwa kwa huyo mtu.

Na jambo kama hilo Mungu ameliruhusu wakati mwingine katika kanisa kufanyika.. Kwamfano katika habari hiyo ukiendelea kusoma mistari inayofuata utaona, mtume Paulo alisikia wakorintho wamejihusisha na zinaa mbaya, iliyokithiri ambayo haipo hata kwa watu wenye dhambi, yaani mtu anazini na mama yake halafu bado yupo katika kanisa. Sasa kwa kosa kama hilo Paulo akawaambia wakorintho, hata kabla hajafika tayari ameshamuhukumia adhabu mtu kama huyo. Na adhabu yenyewe ni kumkabidhisha shetani amuue, mwili aungamie ili roho ipone siku ile ya hukumu.

Hata sasa, matendo kama haya, yanaendelea katika kanisa la Kristo, leo hii limekuwa ni jambo la kawaida kusikia wachungaji wanazini na washirika wao, wengine wanavuka mipaka hadi na watoto wadogo, utasikia askofu anazini na muumini pamoja na mama yake, jambo ambalo huwezi kuliona hata kwa watu wenye dhambi. Na wenyewe wanaona ni sawa kwasababu hakuna mtu wa kuwakabidhisha kwa shetani.

Paulo anasema, ni heri ukabidhiwe kwa shetani uuawe, walau hasira ya Mungu utapoa juu yako, na siku  ile ya hukumu unusurike, kuliko kuendelea kuishi, katika hali hiyo hiyo mpaka kufa kwako, kwani adhabu yako itakuwa kubwa sana siku ile.

Luka 12:47 “Na mtumwa yule aliyejua mapenzi ya bwana wake, asijiweke tayari, wala kuyatenda mapenzi yake, atapigwa sana”.

Hivyo hiyo inatukumbusha  tuwe makini sana, katika ukristo wetu, vilevile  na katika wito wetu.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

Nini maana ya msiwe waalimu wengi (Yakobo 1:3)?

Tofauti ya kazi ya Damu ya Yesu na Jina la Yesu ni ipi?

Tofauti kati ya mtume na mwanafunzi ni ipi kibiblia?

KAMA SI YESU, HABARI YETU INGEKUWA IMEISHA ZAMANI SANA.

Mungu anaposema “nitaliweka jina langu” ana maana gani?

Rudi nyumbani

Print this post

Je mbinguni itakuwa ni kuimba tu wakati wote?.

Jibu: Hakuna andiko lolote katika biblia linalosema mbinguni ni mahali pa kuimba tu wakati wote!. Bwana Yesu alisema anakwenda kutuandalia makao..

Yohana 14:1 “Msifadhaike mioyoni mwenu; mnamwamini Mungu, niaminini na mimi.

2  Nyumbani mwa Baba yangu mna makao mengi; kama sivyo, ningaliwaambia; maana naenda kuwaandalia mahali.

3  Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali, nitakuja tena niwakaribishe kwangu; ili nilipo mimi, nanyi mwepo”.

Umeona hapo anasema anaenda kutuandalia Makao, maana yake makazi..Na tena anasema yapo makao Mengi! (Si machache)…Na sehemu yoyote yenye makao/ makazi maana yake kuna shughuli nyingi, sio kuimba tu!. Kwa ufupi mbinguni itakuwa ni sehemu yenye upeo mkubwa kuliko duniani, vinginevyo basi duniani pangekuwa bora kuliko mbinguni.

Kama duniani tu! Vipo vitu vingi ambavyo vinavyowapa wanadamu raha, (ambavyo kimojawapo ndio hiyo kuimba) basi mbinguni hapawezi kuwa panyonge kuliko duniani, maana yake kule ni mara elfu elfu ya hapa.. zitakuwepo shughuli nyingi, na mambo mengi yatakayotupa raha na furaha, na sio kuimba tu!..kuimba itakuwa ni sehemu ya vitu hivyo!..Ndio maana mpaka sasa Bwana anatuandalia makao hayo, tukifika huko tutamfurahia Mungu katika viwango ambavyo hatujawahi kumfurahia.

Hivyo kwa hitimisho ni kwamba mbinguni hapatakuwa ni mahali pa kuimba tu usiku na mchana, bali kutakuwepo na mambo mengine mengi, ambayo biblia inasema jicho halijawahi kuona wala sikio kusikia.

1Wakorintho 2:9 “ lakini, kama ilivyoandikwa, Mambo ambayo jicho halikuyaona wala sikio halikuyasikia, (Wala hayakuingia katika moyo wa mwanadamu,) Mambo ambayo Mungu aliwaandalia wampendao”

Kwahiyo hatuna budi kutafuta kuingia mbinguni kwa gharama zozote zile, ili tusiyakose hayo mambo mazuri tuliyoahidiwa na Baba. Na lango la kuingia mbinguni ni moja tu!, nalo ni YESU KRISTO, alisema..

Yohana 14:5 “Tomaso akamwambia, Bwana, sisi hatujui uendako; nasi twaijuaje njia?

6  Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi”

Kwa kumwamini Yesu, na kuungama dhambi zetu zote, na kubatizwa katika ubatizo sahihi, na kupokea Roho Mtakatifu, hapo tayari tutakuwa tumeshaanza safari ya kwenda mbinguni. Tutakuwa tumeshaiona njia.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

YANAYOENDELEA SASA KATIKA MADHABAHU YA MUNGU ROHONI.

TABIA ZITAKAZOMTAMBULISHA MPINGA-KRISTO AJAYE.

BASI TUENDELEE KUMJUA MUNGU,NAYE ATATUJILIA KAMA MVUA YA VULI.

Jiepushe na tamaa ya Mali/kupenda fedha.

Rudi nyumbani

Print this post

Je! Watu ambao hawajawahi kusikia injili kabisa siku ya mwisho watahukumiwa?

JIBU: Kumbuka Mungu ameiandika injili yake katika sehemu kuu mbili. Sehemu ya kwanza ni katika kitabu, na sehemu ya pili ni katika moyo wa mwanadamu.

Watu wengi tunadhani, ni mpaka tusikie ndio tutahukumiwa hapana, hiyo ni sehemu ya kwanza, lakini kuna sheria ambayo Mungu tayari kashiweka katika moyo wa kila mwanadamu ajapo hapa duniani, ambayo hiyo inathibitishwa na kutetewa na “dhamiri na mawazo” ya mtu mwenyewe.

Biblia inasema..

Warumi 2:14 “Kwa maana watu wa Mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe.

15 Hao waionyesha KAZI YA TORATI ILIYOANDIKWA MIOYONI MWAO, dhamiri yao ikiwashuhudia, na mawazo yao, yenyewe kwa yenyewe, yakiwashitaki au kuwatetea;”

Umeona? Ikiwa na maana kuwa, hata ukienda katika jamii za watu ambao wamejitenga kabisa huko maporini, hawajui chochote kinachoendelea ulimwenguni, kazi yao ni kuwinda na kukusanya tu..bado utawakuta na tabia ambazo zinaendana kabisa na sheria za Mungu, kana kwamba wanaijui torati. Kwamfano utakuta wanapinga vitendo vya uuaji, wizi, au uzinzi n.k.

Mambo kama hayo, hawakuyasoma kwanza kwenye biblia, bali tayari yalishaandikwa mioyoni mwao kana kwamba walikuwa wanaijua biblia. Na ndio katika hayo Mungu atawahukumu. Kwasababu kama tulivyosoma hapo, kwamba kama mtu atafanya yaliyo ndani ya sheria, hata kama hajaisikia, basi tayari anaitenda sheria hiyo ndani ya moyo wake.

Lakini wakati wasasa tunaoishi, injili ya Kristo imeshasambaa ulimwenguni kote, Tumesikia, na bado mioyo yetu inatushuhudia. Haijalishi utaiamini, au huiamini,  Hivyo tujue kuwa tusipoitii hatutakuwa na udhuru siku ile ya hukumu.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

JE! WATOTO WACHANGA WANAWEZA KUHUKUMIWA NA KUTUPWA MOTONI.

Je Eliya aliandika waraka baada ya kupaa mbinguni?

HUTATAMBUA LOLOTE, SIKU YA UNYAKUO IKIFIKA.

NI LIPI KATI YA MAKUNDI HAYA, WEWE UPO?

Rudi nyumbani

Print this post

WAPENZI, MSIIAMINI KILA ROHO.

Wakati tunaoishi ni wakati ambao kuna machafuko mkubwa sana ya rohoni kuliko hata nyakati nyingine zilizowahi kupita huko nyuma,. Na muasisi wa hayo  ni shetani kwasababu anajua katika agano letu jipya kiini cha Kanisa ni ROHO MTAKATIFU. Hivyo anajua akiruhusu Roho wa Mungu peke yake alitawale kanisa, atawakosa watu wengi sana.

Hivyo tangu ule wakati wa mitume, alibadilisha mbinu zake za kivita, akitaka kulishambulia kanisa, haji tena mwilini, bali, ni anakuja na roho za udanganyifu zinazofanana sana na Roho Mtakatifu wa kweli kumbe sio.

Hivyo kuanzia ule wakati alianza kutoa matoleo mengi sana ya roho hizo. Mpaka sasa matoleo aliyonayo ni ya hali ya juu sana, kiasi kwamba usipokuwa makini utaweza ukavamiwa na roho za udanganyifu ukadhani ni Roho Mtakatifu kumbe ni uongo. Tupo katika wakati ambao si wa kiziamini kila roho zinazohubiriwa na watu.

Na ndio maana mitume walituonya na kusema..

1 Yohana 4:1 “Wapenzi, msiiamini kila roho, bali zijaribuni hizo roho, kwamba zimetokana na Mungu; kwa sababu manabii wa uongo wengi wametokea duniani”.

Sasa ili tuwe salama ni vizuri tukajua tabia za kweli za  Roho Mtakatifu zipoje, ili tuwe na amani na tulichokipokea.

  1. Tabia ya kwanza ni kuwa Atakufanya uwe Mtakatifu: 

Kama jina lake lilivyo, “Roho Mtakatifu”, ndicho anachokifanya ndani ya mtu pale anapokuja juu yake rasmi, Atamfanya awe mtakatifu. Kama alivyosema katika 1Wakorintho 3:16, kuwa miili yetu ni lazima iwe mitakatifu kwasababu huyo Roho anayekaa ndani yetu ni Mtakatifu. Hivyo Ni lazima ahakikishe kuwa yale matunda yote ya roho yapo ndani yako sawasawa (Wagalatia 5:22-23)

Hivyo ukiona umepokea Roho, ambayo ndani yako haikupi kiu ya kuwa mtakatifu, yaani kuacha anasa, kuacha uvaaji mbovu, kuacha, miziki ya kidunia, kuacha vimini, na milegezo, kuwa na upendo, na kiasi, basi ujue hiyo sio Roho ya Mungu, haijalishi utanena kwa lugha muda mrefu kiasi gani.. Kimbia hapo, haraka sana.

2) Atakuongoza katika kuijua kweli yote(Yohana 16:13): 

Kazi nyingine ya Roho wa kweli wa Mungu, ni kuwa hatakuacha katika hali hiyo hiyo,ya ujinga wa kiroho uliokuwa nao sikuzote, ni lazima akupigishe hatua za kiufahamu mpaka kufikia kusimama imara katika maandiko. Lakini ukiona umeokoka na miaka nenda rudi, hujui chochote kuhusiana na Neno la Mungu, wewe unachojua ni habari za wachawi na mapepo, ujue kuwa Huyo sio Roho Mtakatifu uliyempokea bali ni roho nyingine ya adui ipo ndani yako.

3) Atamshuhudia Kristo ndani yako : 

Roho Mtakatifu kazi yake ni kutoa ushuhuda wa Kristo katikati ya kanisa lake, na sio wa mwanadamu yoyote. Ikiwa na maana kiini cha kanisa ulilopo, au huduma, unayoitumikia msingi wa hapo ni lazima awe Bwana Yesu Kristo. Na sio mwanadamu Fulani, au mtakatifu Fulani. Ukiona Kristo hapewi kipaumbele chochote, au anachukuliwa kama mtu wa ziada tu, ujue roho ya mpingakristo ipo hapo.

1Yohana 4:2 “Katika hili mwamjua Roho wa Mungu; kila roho ikiriyo kwamba Yesu Kristo amekuja katika mwili yatokana na Mungu.

3 Na kila roho isiyomkiri Yesu haitokani na Mungu. Na hii ndiyo roho ya mpinga Kristo ambayo mmesikia kwamba yaja; na sasa imekwisha kuwako duniani”.

4) Ataweka karama au huduma ndani yako (1Wakorintho 12):

Karama hiyo/ huduma hiyo Roho Mtakatifu anaiweka kwa lengo la kulijenga kanisa la Mungu. Haiwezekani, ukawa umeokoka muda mrefu na miaka mingi, na umesema umepokea Roho Mtakatifu lakini kazi yako katika ufalme wa mbinguni haionekani. Wakati mojawapo ya kazi ya Roho Mtakatifu ni kuweka vipawa ndani yetu.

Hivyo kama hutakuwa mchungaji, au nabii, au mwinjilisti, au shemasi, au mwenye karama ya lugha, n.k basi utakuwa ni nyingine yenye faida katika kanisa kama kukirimu, kuimba, kufadhili n.k. Lakini haiwezekani kiungo kikawa hakina kazi kabisa katika mwili wa Kristo, kama mshirika anayekuja na kuondoka, miaka yote, ukiona hivyo ujue kuwa Roho uliyempokea si wa Mungu, bali ni wa adui.

5) Atachochea kuomba ndani yako. (Warumi 8:6)

Maandiko yanasema Roho Mtakatifu anaugua ndani yetu, kwa namna isiyoweza kutamkwa. Ikiwa na maana Mkristo wa kweli aliyepokea Roho, hataona amani kukaa wiki, miezi, miaka bila kuomba. Ile furaha ya wokovu itaondoka tu ndani yake, Hivyo atalazimika, kuwa mwombaji mzuri, kuhudhuria mikesha, na kufunga wakati mwingine.

Lakini ukiona unayo amani, kukaa mwezi mzima bila kuomba, na ndani yako husikii chochote, au mzigo wowote, hapo umepokea Roho nyingine ya adui. Jitathimini tena.

Tabia hizi tano (5), ukiziona ndani yako. Basi ujue Roho uliyempokea ni kweli Roho Mtakatifu, uwe na amani. Lakini kama hivyo vyote havipo ndani yako, Roho uliyepokea ni ya adui ibilisi. Unachopaswa ufanye ni umaanishe kuokoka katika maisha yako.

Maana yake, utubu dhambi zako kweli kweli, kisha ukabatizwe katika ubatizo sahihi wa kuzamishwa katika maji mengi na kwa jina la YESU KRISTO (Matendo 2:38). Kisha baada ya hapo, Roho wa kweli ataingia ndani yako, kuanza kukupigisha hizo hatua.

Kumbuka hizi ni siku za mwisho, na tumeaswa sana tuzijaribu hizo roho, usiridhike, na tabia mojawapo tu, jiulize je! Zote hizo zinaonekana ndani yako?

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

JE! UMEPOKEA KWELI ROHO MTAKATIFU?

TUJIFUNZE JAMBO KWA WANAWAKE HAWA WAWILI:

Je aliyezungumza na Musa kule jangwani ni Mungu mwenyewe au malaika wake?

ZIFAHAMU KAZI TATU ZA ROHO MTAKATIFU KATIKA ULIMWENGU.

AHADI YA ROHO ILIYOSALIA SASA KWA KIPINDI CHETU.

Rudi nyumbani

Print this post

Je Eliya aliandika waraka baada ya kupaa mbinguni?

SWALI: Tunajua kuwa Nabii Eliya alipaa mbinguni katika upepo wa kisulisuli, lakini tunakuja kuona miaka mingi baadaye akituma waraka kwa mfalme mfalme Yehoramu juu ya ugonjwa wake (2Nyakati 21:12). Jambo hilo linawezekanikaje?


Jibu: Labda tusome,

2Nyakati 21:11 “Tena ndiye aliyefanya mahali pa juu milimani pa Yuda, na kuwaendesha katika uasherati wenyeji wa Yerusalemu, na kuwakosesha Yuda.

12 LIKAMJIA ANDIKO KUTOKA KWA ELIYA NABII, kusema, Bwana, Mungu wa Daudi baba yako, asema hivi, Kwa sababu hukuziendea njia za Yehoshafati baba yako, wala njia za Asa mfalme wa Yuda;

13 lakini umeiendea njia ya wafalme wa Israeli, ukawaendesha katika uasherati Yuda na wenyeji wa Yerusalemu, kama walivyofanya nyumba ya Ahabu; tena umewaua ndugu zako wa nyumba ya baba yako, waliokuwa wema kuliko wewe;

14 tazama, Bwana atawapiga pigo kubwa watu wako, na watoto wako, na wake zako, na mali yako yote;

15 nawe utakuwa na ugonjwa mkuu kwa maradhi ya matumbo, yatakapotokea matumbo yako kwa sababu ya ugonjwa huo siku kwa siku”

Ni kweli kabisa unabii huo ni wa kipindi cha mbele kabisa, wakati ambao Nabii Eliya ameshachukuliwa juu… Lakini swali la msingi hapo ni kwanini Eliya aonekane tena hapa akimtolea unabii huyu mfalme, je alituma huo waraka kutoka mbinguni huko alikokuweko au?

Jibu ni la! Hakutuma waraka kutoka mbinguni, bali ulikuwa ni waraka ambao aliuandika kabla ya kunyakuliwa juu. Alipewa unabii wa mbeleni, kwamba atatokea mfalme anaitwa Yehoramu ambaye atafanya mambo yasiyompendeza Mungu, na Bwana Mungu akampa maagizo aandike habari ya mambo yake pamoja na adhabu atakayoipata, hivyo Nabii Eliya akaandika katika waraka, na baada ya hapo pengine alimpa Eliya au mtumishi mwingine chini yake ili baada ya yeye kuondoka na huyo mfalme atakapotokea basi apewe ujumbe wake.

Na kweli baada ya hapo waraka ule ulihifadhiwa mpaka Mfalme Yohoramu alipotokea, na kufanya mabaya sawasawa na unabii huo wa Eliya, na mwisho akapatwa na mabaya kama Eliya alivyoandika..Kwani maandiko yanasema Yehoramu alipata ugonjwa wa matumbo, utumbo ukawa unatoka nje, huku unaoza!, na alikufa kifo cha kutokutamanika.

2Nyakati 21:18 “Na baada ya hayo yote Bwana akampiga matumbo kwa ugonjwa usioponyeka.

 19 Ikawa baada ya siku, ikiisha miaka miwili, matumbo yake yakatokea kwa sababu ya ugonjwa wake, akafa akiugua vibaya. Wala watu wake hawakumfukizia mafukizo kama ya baba zake”.

Hivyo sio kwamba Nabii Eliya alirudi kumtabiria wala kutuma wakara kutoka mbinguni, hapana bali aliuandika kabla ya kuondoka kwake.

Jambo kama hilo hilo pia tunaliona kwa Nabii mmoja ambaye alipewa unabii wa kuzaliwa mfalme atakayeitwa Yosia, ambaye atazibomoa bomoa madhabahu zote za baali katika Israeli..

1Wafalme 13:1 “Na tazama, akatoka mtu wa Mungu katika Yuda kwa neno la Bwana, akafika Betheli. Naye Yeroboamu alikuwa akisimama penye madhabahu, afukize uvumba.

 2 Basi mtu huyo akapiga kelele juu ya madhabahu, kwa neno la Bwana akasema, Ee madhabahu, madhabahu, Bwana asema hivi, Angalia, mtoto atazaliwa katika nyumba ya Daudi, jina lake Yosia; na juu yako atawachinja makuhani wa mahali pa juu, wanaofukiza uvumba juu yako, na mifupa ya watu itateketezwa juu yako”

Baada ya unabii huu kutoka kwamba atazaliwa mtoto anayeitwa Yosia, uliandikwa chini, na kisha kuhifadhiwa, ilipita miaka zaidi ya 100 ndipo mtoto huyo alipokuja kuzaliwa.. na akafanya yote sawasawa na yaliyotabiriwa kuhusu yeye.. Unaweza kusoma habari hiyo katika kitabu cha 2Wafalme 23:16-20.

Sio hao tu!, hata Nabii Isaya alishatabiri habari za kutokea Mfalme anayeitwa Koreshi ambaye atamjengea Mungu nyumba katika Israeli, na akamwandikia waraka huo, na ukahifadhiwa na wakati ulipofika miaka mingi baadaye, mfalme huyo alitokea kweli na akapewa ujumbe wake huo. Unaweza kusoma unabii huo katika Isaya 44:28, Isaya 45:1 na kutimia kwa unabii huo unaweza kusoma Ezra 1:2

Hivyo tunachoweza kujifunza ni kuwa Mungu anayajua yote yanayokuja, na kwamba Neno la Mungu halipiti, kama aliweza kuandika habari za Yehoramu miaka mingi kabla hajaja, na habari zake zikatimia kama zilivyo, vile vile kama aliweza kuziandika habari za Koreshi mfalme wa Uajemi na zikatimia kama zilivyo…  Basi tujue kuwa maneno yake aliyosema kuwa walevi, waasherati, waabuduo sanamu, wezi, n.k hawataurithi uzima wa milele  sawasawa na Wagalatia 5:21, basi tutambue kuwa Neno lake sio uongo, ni lazima litimie tu!, kwasababu Mungu ni yeye Yule jana, leo na hata milele habadiliki.

Wagalatia 5:19 “Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya, uasherati, uchafu, ufisadi,

20  ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi,

21  husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo, katika hayo nawaambia mapema, KAMA NILIVYOKWISHA KUWAAMBIA, YA KWAMBA WATU WATENDAO MAMBO YA JINSI HIYO HAWATAURITHI UFALME WA MUNGU”

Hivyo kama bado hatujamkabidhi Bwana maisha yetu, huu ni wakati wa kufanya hivyo.. Kama bado hujaokoka, ni  vizuri kufanya sasa kama mambo hayajaharibika, na ikashindikana kuyafanya upya tena. Hivyo hapo ulipo usipoteze muda, jigenge dakika chache na kisha tubu dhambi zako zote ukimaanisha kuziacha, na kisha tafuta ubatizo sahihi ambao ni wa maji mengi na kwa jina la Yesu ili ubatizwe upate ondoleo la dhambi zako, na hatimaye utapokea kipawa cha Roho Mtakatifu, ambaye atakuongoza na kukutia katika kweli yote ya maandiko.

Maran atha!

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.


Mada Nyinginezo:

NI VIZURI SISI KUWAPO HAPA.

KAMA MKRISTO FAHAMU ZIPO HATUA UTAPIGISHWA NA MUNGU.

JINSI MTUME PAULO ALIVYOUTHAMINI WITO WAKE, JUU YA WENYE VYEO.

WALA MSIUANGALIE MWILI, HATA KUWASHA TAMAA ZAKE.

KUJIFUNUA KWA YESU KWA PILI.

Rudi nyumbani

Print this post

NI LIPI KATI YA MAKUNDI HAYA, WEWE UPO?

Ikiwa Bwana Yesu atarudi leo, atakutana na makundi matatu ya watu wanaomsubiria yeye.

  • Kundi la kwanza ni kundi la HENOKO,
  • kundi la pili ni kundi la NUHU,
  • Na kundi la tatu ni kundi la LUTU.

Sasa ni vizuri ukafahamu wewe upo katika kundi lipi, kuanzia sasa, kabla ya wakati huo kufika. Kwasababu wakristo wengi wanadhani ukishamkiri tu YESU basi, inatosha wewe ni tiketi ya moja kwa moja, kwenda katika unyakuo.

Ndugu yangu, hizi ni siku za mwisho, hatuna muda mrefu wa kuishi hapa duniani, kama hulijui hilo ndio ulifahamu sasa, ni wajibu wetu sisi, tunaosema tumeokoka, kuyatathimini maisha yetu ya wokovu, ili tujue tupo upande upi.

1) Tukianzana na kundi la kwanza la HENOKO.

Kama sote tunavyojua Henoko alikuwa ni mtu wa saba tangu Adamu, na mtu pekee aliyenyakuliwa kutoka ulimwenguni pasipo kuonja mauti kwenye dunia ya wakati ule. Na biblia inatueleza sababu ya kuhamishwa kwake ni kwasababu alishuhudiwa kuwa alimpendeza Mungu,

Waebrania 11:5 “Kwa imani Henoko alihamishwa, asije akaona mauti, wala hakuonekana, kwa sababu Mungu alimhamisha; maana kabla ya kuhamishwa alikuwa ameshuhudiwa kwamba amempendeza Mungu”.

Biblia inasema alitembea na Mungu kwa muda wa miaka 300. Hivyo Mungu hakuona vema awepo katika uharibifu  wa gharika uliokuwa unakuja ulimwenguni kote.

Vivyo hivyo wakati tunaoishi sasa ni wakati wa nyakati ya SABA ya kanisa kwa mujibu wa kalenda ya Mungu kama tunavyosoma katika kitabu cha Ufunuo sura ya 2&3. Hivyo hadi sasa lipo kundi dogo sana la watakatifu linalofananishwa na Henoko, litakalotembea na Kristo hadi wakati wa kuja kwake, Watu hawa katika biblia wanajulikana kama Wanawali werevu na Bibi-arusi wa Kristo (Ufu 21). Ndio watakatifu watakaokwenda katika unyakuo ikiwa parapanda ya mwisho italia leo.

Hawa Mungu atawaepusha na dhiki kuu, na adha zitakazokuja huko mbeleni, kwa tukio linaloitwa UNYAKUO, kwasababu ni vipenzi wa Mungu.

Ufunuo 3:10 “Kwa kuwa umelishika neno la subira yangu, mimi nami nitakulinda, utoke katika saa ya kuharibiwa iliyo tayari kuujilia ulimwengu wote, kuwajaribu wakaao juu ya nchi”.

Ni watu ambao thawabu yao mbinguni ni kubwa sana.. ndio wale ambao watatawala na Kristo kama Wafalme, mabwana na makuhani. Na makao yao itakuwa ni katika ile Yerusalemu mpya ishukayo kutoka mbinguni kwa Baba.

Kundi la Pili, ni NUHU.

Hili kundi halituhusu sisi watu wa mataifa, Bali linawahusu Wayahudi. wayahudi tu peke yao ndio watakaokuwa katika kundi hili na Nuhu, Kristo atakaporudi. Ikiwa na maana kuwa, Unyakuo utakapopita hawatakwenda popote, kwasababu hawakuwa ndani ya Kristo. Na Mungu alifanya hivyo kwa makusudi, kuwapiga upofu ili sisi tuipokee hii neema. Lakini wakati utafika, hii neema Kristo atairudisha kwao, (Soma Warumi 11)  na baadhi yao wataiamini. Sasa hao, ndio wataingizwa katika Safina(mafichoni) ambayo Mungu ataindaa wakati huo, ili kuwalinda na hiyo dhiki kuu ya mpinga-Kristo, pamoja na ghadhabu ya Mungu itakayokuja ulimwenguni wakati huo. Soma (Ufu 7:1-8, 14:1)

Ufunuo 12:14 “Mwanamke yule akapewa mabawa mawili ya tai yule mkubwa, ili aruke, aende zake nyikani hata mahali pake, hapo alishwapo kwa wakati na nyakati na nusu ya wakati, mbali na nyoka huyo”.

Na hawa vilevile hawatakuwa wengi, idadi yao itakuwa ni 144,000 tu Basi, hawa watahifadhiwa mbali na mpinga-Kristo, hivyo mpaka dunia inateketezwa kwa moto, hawa watakuwa mafichoni mahali ambapo Mungu amewaandalia wao tu. Hawakufa, mpaka utawala wa miaka 1000 utakapoanza, kama vile Nuhu alivyoishi hadi gharika ilipoisha.

Kundi la tatu ni LUTU.

Kundi hili ndio gumu zaidi, kwasababu halinyakuliwi, wala halitunzwi, bali linajiokoa lenyewe. Kama vile Lutu, wakati wa maangamizi ulipofika, hakunyakuliwa kama Henoko, wala hakuhifadhiwa kwenye safina, au handaki Fulani, kama Nuhu, bali aliambiwa na wale malaika, jiponye nafsi yako. (Mwanzo 19:17). Ikiwa na maana akiendelea kubaki pale, ni kifo.

Na utaona Lutu, alikuwa ni tajiri sana, lakini siku alipolazimika kuondoka, hakuondoka na kitu chochote pamoja naye hata kijiko, isipokuwa familia yake.

Ndivyo itakavyokuwa kwa kundi hili la wakristo vuguvugu watakaokosa unyakuo, ambao wanaojulikana kama wanawali wapumbavu. Siku hiyo watalazimika, kuingia katika dhiki kuu, ambayo kujiponya kwao ni lazima kuambatane na vifo na dhiki, na mateso mengi sana.

Na kwa bahati mbaya wengi sana hawataweza kustahili, wategeuka nyuma. Na matokeo yake ni kuwa jiwe la chumvi kama mke wa Lutu. Wengi wanadhani, kipindi cha dhiki kuu, kitakuwa ni chepesi, usidanganyike, mke wa Lutu, alidhani hivyo alipokuwa anatoka, lakini mbeleni aliona alipotoka ni heri kuliko alipokuwa anaelekea na ndio maana akagueka nyuma akawa jiwe la chumvi. Nataka nikuambia Siku hiyo ya dhiki kuu, na ya mapigo Mungu, mateso utakayokuwa unayapitia,  utaona ni heri upokee tu chapa,  kama sio  kumkufuru Mungu kabisa, kuliko kuvumilia dhiki hizo.

Kulithibitisha hilo soma.

Ufunuo 16:8 “Na huyo wa nne akakimimina kitasa chake juu ya jua, nalo likapewa kuwaunguza wanadamu kwa moto.

9 Wanadamu wakaunguzwa maunguzo makubwa, nao wakalitukana jina la Mungu aliye na mamlaka juu ya mapigo hayo; wala hawakutubu wala kumpa utukufu”.

Na kibaya zaidi, ni kuwa kundi hili hata kama litafanikiwa kustahimili dhiki(yaani kufa bila kuikana imani), kule litakapokwenda litakuwa la chini kabisa, halitakuwa na thawabu yoyote. Kwasababu halina chochote mkononi mwao, kama vile Lutu alivyopoteza vyote.

Ndugu, haya mambo yapo karibuni sana. Swali la kujiuliza Je! Wewe upo katika kundi lipi, Je! Ni la HENOKO au la LUTU. Jibu unalo moyoni mwako, ikiwa leo hii maisha yako yote ni kufikiria tu mambo ya ulimwenguni, hutaki kuishi maisha ya utakatifu yanayompendeza Mungu, Usitazamie kuwa Utakuwa katika kundi la Henoko. Ikiwa habari za siku za mwisho hazikuvutii, lakini habari za kutabiriwa biashara yako ni zenye kipaumbele, basi ujue hapa duniani utabaki tu kama paraparanda italia leo.

Tujifunze kwa Henoko, yeye alitembea na Mungu mpaka Mungu mwenyewe akamwonyesha Siku ya Kiama itakavyokuwa, unategemea vipi Mungu asimwepushe na ile gharika iliyokuwa mbele yake?

Yuda 1:14 “Na Henoko, mtu wa saba baada ya Adamu, alitoa maneno ya unabii juu ya hao, akisema, Angalia, Bwana alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu,

15 ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasiomcha Mungu wameyanena juu yake”.

Bwana atusaidie.

Maran Atha.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo.

Mada Nyinginezo:

MAJONZI YA MTUME PAULO KWA NDUGU ZAKE.

Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita..

SIKU YA UNYAKUO ITAKUKUTAJE?

KWA MIOYO YAO WAKAREJEA MISRI.

Rudi nyumbani

Print this post

Nini maana ya “Torati na manabii”?

SWALI: Tukisoma katika maandiko tunaona sehemu kadha wa kadha likitajwa neno “Torati na manabii”. Sasa hii torati na manabii maana yake ni nini? Kwamfano  Mathayo 7:12  inasema

“Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii”.

JIBU: Bwana Yesu aliposema Torati na manabii, alimaanisha Agano la kale, ambalo ndio limeundwa na vitabu vya Musa (Torati), ambavyo ni vitano (5), Mwanzo, Kutoka, Mambo ya Walawi, Hesabu na Kumbukumbu la Torati.  Pamoja na vitabu vyote vya manabii, kama vile, Yeremia, Isaya, Danieli, Ezekieli, Hababuki, Amosi, n.k. hapa ikijumuisha pia, vile vingine kama  Waamuzi, Zaburi, Ayubu, Wafalme,  Mithali, Ruthu n.k. Ambavyo sio moja kwa moja vya manabii, lakini vimebeba nabii za Mungu ndani yake.

Kwahiyo torati na manabii kwa ufupi ni lile agano lote la kale. Hivyo Pale Bwana Yesu alipokuwa anawafundisha juu ya kanuni za kufuata, alirejea biblia yao, akiwaambia kuwa kiini cha biblia hiyo ni UPENDO. Wala hakuna siri nyingine nyuma yake, Torati yote, pamoja manabii wote, walichokuwa wanahubiri ni Upendo, (Ambao umegawanyika, wa Mungu na wanadamu)

Hata sisi wa leo tulio katika agano jipya, tunaposoma biblia yote tujue Ujumbe mkuu tunaoupata katika agano letu ni ule ule UPENDO. Na ndio maana Mtume Paulo alisema.

1Wakorintho 13:1 “Nijaposema kwa lugha za wanadamu na za malaika, kama sina upendo, nimekuwa shaba iliayo na upatu uvumao.

2 Tena nijapokuwa na unabii, na kujua siri zote na maarifa yote, nijapokuwa na imani timilifu kiasi cha kuweza kuhamisha milima, kama sina upendo, si kitu mimi.

3 Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu”.

Hivyo na sisi, tunapaswa tuutafute huu, kwa bidii zote, ili tuonekane kuwa wakamilifu mbele za Mungu.

Shalom

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312

pia kama utapenda uyapate mafundisho haya kwa njia ya Whatsapp au email basi tutumie ujumbe kwenye namba hizo hizo. Jiunge na magroup yetu ya whatsapp kwa kubofya hapa > WHATSAPP-Group

Mada Nyinginezo:

Rudi nyumbani

Print this post

Kwanini Yesu aliwaambia wale wakoma wakajionyeshe kwa makuhani?

SWALI: Kwanini Bwana Yesu aliwaambia wale watu wenye ukoma waende kujionyesha kwa makuhani?, kwanini asiwaponye tu hivyo hivyo na kuwaacha mpaka awaambie waende kwa makuhani.

Luka 17:12 “Na alipoingia katika kijiji kimoja, alikutana na watu kumi wenye ukoma; wakasimama mbali,13 wakapaza sauti wakisema, Ee Yesu, Bwana mkubwa, uturehemu!

14 Alipowaona aliwaambia, Enendeni, mkajionyeshe kwa makuhani. Ikawa walipokuwa wakienda walitakasika”.


JIBU: Kama vile Injili ya Kristo inavyowafikia watu katika namna mbili, wengine kuwaokoa na wengine kama ushuhuda kwao (Mathayo 24:14)

Vivyo hivyo na uponyaji wake alivyouachia, alikusudia uwafikie watu kwa namna mbili. Kuokoa na wakati huo huo kuwa Ushuhuda.Si kila uponyaji au muujiza Yesu aliokuwa anaufanya ulikuwa ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu. Hapana, bali ponyaji nyingine aliziruhusu mahususi kwa lengo la kuwa ushuhuda kwa wengine, ili siku ile ya hukumu wasije wakasema hatukuona, au hatukusikia.

Tunasoma jambo kama  hilo katika..

Mathayo 8:1 “Naye aliposhuka mlimani, makutano mengi walimfuata.

2 Na tazama, akaja mtu mwenye ukoma akamsujudia, akisema, Bwana, ukitaka, waweza kunitakasa.

3 Yesu akanyosha mkono, akamgusa, akisema Nataka; takasika. Na mara ukoma wake ukatakasika.

4 Yesu akamwambia, Angalia, usimwambie mtu; ila enenda zako, ukajionyeshe kwa kuhani, ukaitoe sadaka kama alivyoamuru Musa, IWE USHUHUDA KWAO”.

Ndicho kilichowakuta Makuhani, pamoja na mafarisayo na waandishi. Ni watu ambao walikuwa hawataki kusikia wala kuamini, Hivyo Bwana Yesu, alipowaponya baadhi ya watu hakuwaacha tu hivi hivi waende,kama alivyofanya sehemu nyingine, bali aliwaagiza waende kuwaeleza makuhani miujiza iliyowakuta,. Hivyo walikuwa wanapokea shuhuda nyingi sana kutoka kwa watu  mbalimbali walioponywa.. Pengine kwa siku  hata watu 100. Na kila walipoulizwa ni nani kawaponya wanasema YESU.

Hivyo hata sasa na sisi, tusifurahie tu miujiza ya Mungu anatuletea miujiza mingi, watu wanaponywa, wanafunguliwa, na huku maisha yetu yapo nje ya Kristo. tusifurahie kwasababu tujue ni hukumu tu tunajiandikia. Na ndio maana Bwana alisema maneno haya sehemu fulani;

Mathayo 11:21 “Ole wako, Korazini! Ole wako, Bethsaida! Kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwenu ingalifanyika katika Tiro na Sidoni, wangalitubu zamani kwa kuvaa magunia na majivu.

22 Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi Tiro na Sidoni kustahimili adhabu zao siku ya hukumu kuliko ninyi.

23 Nawe Kapernaumu, je! Utakuzwa mpaka mbinguni? Utashushwa mpaka kuzimu; kwa kuwa kama miujiza iliyofanyika kwako ingalifanyika katika Sodoma, ungalikuwapo mji huo hata leo.

24 Walakini nawaambieni, itakuwa rahisi nchi ya Sodoma kustahimili adhabu yake siku ya hukumu kuliko wewe”.

Hivyo hiyo ndio iliyokuwa sababu kwanini aliwaambia wakajionyeshe kwa makuhani, kwasababu wao ndio waliokuwa hawamwamini wala kuziamini kazi zake.

Shalom.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema,

Kwa maombezi/Ratiba za ibada/ Ushauri/ Maswali.
Piga namba hizi: +255693036618 au +255789001312 Pia unaweza ukapata mafundisho haya Kwa njia ya Whatsapp yako, jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP

Mada Nyinginezo:

Ukoma wa nyumba ulifunua nini zamani?

Nini maana ya msiwe waalimu wengi (Yakobo 1:3)?

Kwanini Bwana Yesu alitokea katika ukoo wa Yuda?

MIUJIZA YA KRISTO, HAITEGEMEI KANUNI ZA KIBINADAMU.

Rudi nyumbani

Print this post