KAMA MKRISTO FAHAMU ZIPO HATUA UTAPIGISHWA NA MUNGU.

KAMA MKRISTO FAHAMU ZIPO HATUA UTAPIGISHWA NA MUNGU.

Wakati ule Mbingu inafungwa Israeli mvua isinyeshe miaka mitatu na nusu, tunaona Mungu alimwagiza Eliya aende akakae karibu na kijito cha Maji cha Kerithi, anywe maji ya mto ule, na pamoja na hayo, kunguru watatumwa kumletea chakula na nyama asubuhi na jioni.

Lakini tunasoma, upo wakati kijito kile kilikauka.. pengine yeye alidhani ataendelea kufaidika hivyo hivyo kwa muda wote mpaka Mungu atakapoileta tena mvua juu ya nchi, lakini haikuwa hivyo, Ni kweli yalikuwa ni maagizo ya Mungu yeye abaki pale, lakini Mungu hakukusudia abaki pale milele. Ingekuwa labda ni mimi wakati huo naona kijito ambacho Mungu alichoniagiza nikinywee kimekauka mawazo ya kuwa nimeashaachwa na Mungu yangeshaniingia.

Lakini baada ya tukio lile tunaona Mungu akampa maagizo mengine, ya kuelekea Sarepta akalishwe na mwanamke mjane, na sio tena kunguru.

1Wafalme 17: 2 “Neno la Bwana likamjia, kusema,

3 Ondoka hapa, geuka, uende upande wa mashariki, ujifiche karibu na kijito cha Kerithi kinachokabili Yordani.

4 Itakuwa utakunywa maji ya kile kijito; nami nimewaamuru kunguru wakulishe huko.

5 Basi akaenda akafanya kama alivyosema Bwana; kwa kuwa akaenda akakaa karibu na kijito cha Kerithi, kinachokabili Yordani.

6 Kunguru wakamletea mkate na nyama asubuhi, na mkate na nyama jioni, akanywa maji ya kile kijito.

7 Ikawa, baada ya siku kupita, kile kijito kikakatika, kwa sababu mvua haikunyesha katika nchi.

8 Neno la Bwana likamjia, kusema,

9 Ondoka, uende Sarepta, ulio mji wa Sidoni, ukae huko. Tazama, nimemwagiza mwanamke mjane wa huko akulishe.

10 Basi, akaondoka, akaenda Sarepta; hata alipofika langoni pa mji, kumbe! Mwanamke mjane alikuwako akiokota kuni; akamwita, akamwambia, Niletee, nakuomba, maji kidogo chomboni nipate kunywa.

Nachotaka tujifunze leo ni kuwa, ni tabia ya Mungu kutuvusha madarasa, si desturi yake sisi tuendelee katika darasa lile lile la ukristo kwa miaka yetu yote tuliyopo hapa duniani, ni lazima akikatishe kile kimoja, ili afungue mlango wa kutuletea kingine, na anafanya hivyo sio kutukomoa, bali ni kutukuza kiimani, tufikie utimilifu wa yeye anaoutaka kwetu.

Ikiwa wewe ni mkristo wa muda mrefu, utaelewa ninachokisema,ile  neema uliyokuwa unaipata kutoka kwa Mungu wakati unaokoka, sio neema ambayo unatembea nayo sasa hivi. Pengine siku za mwanzoni mwanzoni ulizookoka, ulihisi kama vile Mungu kakukumbatia kwa kila kitu, ni sawa na unalishwa na kunguru kama vile Eliya, lakini majira unafika unaona, kama neema hiyo imetoweka au imepungua kwako. Kile kijito kimekauka.

Sasa kama wewe ni mkristo ambaye umesimama, ukifikia katika hatua kama hiyo, usianze kufikiri kuwa Mungu amekuacha, kwasababu tu huoni yale mema uliyokuwa unayapata siku za mwanzoni. Badala yake fahamu kuwa, ni hatua nyingine Mungu anataka kukupigisha, ambayo hiyo itakufanya uwe imara zaidi kiimani kuliko ile uliyokuwa nayo hapo kabla.

Ukifikia hatua kama hiyo usikumbatie sana yale ya mwanzoni, kwasababu hata ukijaribu kuyaishi hutaweza tena, uvuli wake umeshapita, unachopaswa kufanya ni  kukaa katika utulivu mpya wa Mungu, omba, kisha pale Mungu anapokufungulia neema ya kuanzana napo, bila kukawia nenda napo..Wala usiogope, kwasababu Mungu atakuwa pamoja na wewe. Huku ukizingatia kuutunza tu utakatifu na Imani, viwango vyake vilevile vya kumcha Mungu.

Kwasababu ni Mungu Yule Yule aliyekuwa na wewe kukupigania, ndiye atakayekuwa na wewe, kukushindania katika darasa lingine jipya ambalo anakupeleka. Jambo unalopaswa kufanya ni wewe tu, kuongeza umakini wako kwa Mungu, na kutoruhusu kurudi nyuma kwa namna yoyote ile.

Kwamfano hapo nyuma ulikuwa katika mazingira tulivu sana ya kumtafakari Mungu, lakini unaona kama yamebadilika, mazingira mengine yamekuja, ambayo yanakulazimu kuwafundisha wengine zaidi, au kuwahubiria, ujue kuwa ni Mungu ndiye anayekuvusha darasa hilo, hawezi miaka yote, akufanye mtoto tu wa kulishwa, utafika wakati na wewe atakulazimisha uwalishe na wengine.

Pengine Mungu atakuhamisha hapo unapoishi na kukupelekea mahali pengine, Na kule unapata changamoto kidogo ya kukipata chakula cha kiroho, kama ilivyokuwa hapo mwanzoni, sasa  Unapoona hivyo, usifikiri kuwa Mungu amekuacha, bali ni wewe, kuishindania zaidi Imani, kutengeneza tena ratiba zako, Na Mungu atakufikisha mahali ambapo anataka ufike.

Hivyo ni jukumu letu kukumbuka kuwa tunapokuwa wakristo ni lazima Mungu atatupitisha  katika madarasa tofauti tofauti, atatuvikisha katika vipindi mbalimbali na katika madarasa hayo, tunapaswa tuwe wepesi wa kuyajua mapenzi yake ni nini, ili tuweze kuelewa ujumbe wa darasa hilo. Na faida yake ni kuwa yeye mwenyewe aliahidi kuwa hatatuacha, bali atakuwa pamoja nasi.

Eliya hakuachwa na Mungu alipoondolewa pale mtoni, na kupelekwa kwenye nyumba ya mjane, Baraka zile zile alizipata isipokuwa zilikuja tu katika maumbile tofauti. Huo ndio uzuri wa Mungu wetu.

Bwana akubariki.

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

Wale mamajusi walikuwa ni wakina nani?

JINSI ROHO MTAKATIFU ANAVYOWAFUNULIA WATU MAANDIKO.

RAHABU.

JE! JICHO LAKO LINAONA NINI KATIKATI YA MAJARIBU?

NI SAA KUMI NA MBILI (12) TU, ZA KRISTO KWAKO.

TAZAMA, NASIMAMA MLANGONI.

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
2 Comments
Newest
Oldest Most Voted
Inline Feedbacks
View all comments
Emmanuel
Emmanuel
2 years ago

Amen, kazi hii ni njema MUNGU awabariki sana,