Wale manabii 400 waliomtabiria mfalme Ahabu wakati wa Mikaya walikuwa ni manabii wa Mungu au?

Wale manabii 400 waliomtabiria mfalme Ahabu wakati wa Mikaya walikuwa ni manabii wa Mungu au?

JIBU: Ndio wale manabii 400 waliomtabiria Ahabu (tunaowasoma katika 1wafalme 22 ) walikuwa ni manabii wa Mungu, na hapo kabla walikuwa wanapokea unabii sahihi kutoka kwa Mungu kwasababu manabii zamani ilikuwa ni lazima wajaribiwe kwanza kabla ya kuitwa mbele za wafalme,. Ni lazima nabii huyo ashuhudiwe kutoa unabii na kutimia vinginevyo hawezi hata kumkaribia Mfalme. kwahiyo ni dhahiri walikuwa wanatoa unabii na unatimia kabisa, japo mioyo yao haikuwa mikamilifu mbele za Mungu kama ilivyokuwa kwa nabii Mikaya…

walikuwa wanapenda utukufu wa wanadamu kuliko utukufu wa Mungu na ndio maana walikuwa wanakaa katika majumba ya kifalme, wakipenda kuwatabiria watu mambo mazuri tu ya faraja hata kama wapo katika dhambi zao, Hivyo tabia hiyo ikawapelekea kupata sifa nyingi kutoka kwa wafalme, lakini hawakujua kuwa Mungu alikuwa amewaacha. Bwana Yesu aliwaambia wanafunzi wake Luka 6: 26 ” Ole wenu ninyi watu wote watakapowasifu, kwa kuwa baba zao waliwatenda manabii wa uongo mambo kama hayo.”

 Mfano mwingine wa manabii kama hawa tunamwona nabii Balaamu (hesabu 22), aliyetaka kwenda kuwalaani Israeli kwa ujira wa udhalimu ili amridhishe tu mfalme Balaki.. 

Huu ni mfano pia wa manabii wengi tulionao sasa wanapenda kusifia pesa,umaarufu,ukubwa, vyeo, wanawatolea watu unabii ili wapate pesa, na kupendwa, sasa manabii kama hao ni rahisi kuingiwa na roho zidanganyazo, hivyo kuwafanya leo wasikie kutoka kwa Mungu kesho wasikie kutoka kwa shetani..lakini manabii kama Mikaya ambao ni wachache sana wao husimama katika Neno, huishi maisha matakatifu na kusema kile Mungu anachotaka tu waseme pasipo kujali cheo cha mtu,utajiri wa mtu, au hali ya mtu, hivyo Mungu anawaepusha na roho zidanganyazo na unabii wao unakuwa thabiti na hakika siku zote, lakini kwa hao wengine wanafungua milango kwa roho zidanganyazo kama ilivyowatokea wale manabii 400.(Mapepo yalivyowaingia wote na kutabiri uongo mbele za Mfalme) 

Hivyo ndugu ni kuwa makini na aina ya manabii waliopo leo hii. Mtu yeyote anayejiita nabii akija na kukutolea unabii ni vizuri kabla ya kuupokea huo unabii, uupime kwanza kwenye NENO, kisha ukilandana nalo ndipo uuchukue, kama haulandani hata kama alishakutolea unabii hapo kabla na ukatimia, usipokee. Kwamfano mtu alikutabiria na kukwambia Bwana kamwonyesha baada ya mwezi mmoja utabeba mimba ya mapacha na wewe wakati huo ni mgumba, na kweli huo wakati ulipofika ukapata mimba na kujifungua mapacha kama alivyokutabiria, lakini leo hii anakuja tena na kukwambia Bwana kamuonyesha umuache huyo mume uliyefunga naye ndoa uliye naye leo ukaolewe na mwingine Bwana aliyekukusudia..Sasa kiharakaharaka ni rahisi kumwamini kwasababu alishakutabiria mara ya kwanza na ikatimia lakini wewe hujui mahusiano yake na Mungu wake yalishaharibika hivyo kumfanya apokee maono mengine kutoka kwa shetani akidhani ni ya Mungu, kwasababu ulinzi ndani yake haupo, dhambi imemtawala amekuwa lango la shetani …Ndivyo walivyofanya wale manabii 400 wa Ahabu. 

Sasa unapokutana na unabii kama huo unakumbuka lile neno linalosema “mtu atakayemwacha mume/mume wake isipokuwa kwa habari ya uasherati na kwenda kuolewa na mwingine azini na anamfanya yule aliyemwacha kuwa mzinzi”…Hivyo hapo unauacha huo unabii na kulishikilia Neno. Soma mstari huu. 

Kumbukumbu 13: 1 “Kukizuka katikati yako nabii, au mwotaji wa ndoto, akikutolea ishara au ajabu,

2 ikatukia hiyo ishara au hiyo ajabu aliyokuambia akisema, Na tuifuate miungu mingine usiyoijua, tuitumikie hiyo;

3 wewe usiyasikize maneno ya nabii yule, au yule mwotaji wa ndoto, kwa kuwa Bwana, Mungu wenu, yuawajaribu, apate kujua kwamba mwampenda Bwana, Mungu wenu, kwa mioyo yenu yote na roho zenu zote.

4 Tembeeni kwa kumfuata Bwana, Mungu wenu; mcheni na kushika maagizo yake na kuisikia sauti yake, nanyi mtumikieni na kushikamana naye.

5 Na yule nabii, au yule mwotaji wa ndoto, na auawe, kwa kuwa amesema yaliyopotoka juu ya Bwana, Mungu wenu, aliyewatoa katika nchi ya Misri, akakukomboa katika nyumba ya utumwa, apate yule mtu kukupotoa katika njia aliyokuamuru Bwana, Mungu wako, uiendee. Ndivyo utakavyouondoa uovu utoke katikati yako”. 

Ubarikiwe sana. jiunge na channel yetu Kwa kubofya hapa >> WHATSAPP


Mada zinazoendana:

NITAMJUAJE NABII WA UONGO?

TABIA YA WAZI INAYOWATOFAUTISHA MANABII WA UONGO NA WALE WA UKWELI.

MPINGA-KRISTO

ROHO YA MPINGA KRISTO IKITENDA KAZI SIKU HIZI ZA MWISHO

KUCHEZA KARATA NI SAHIHI KWA MTU ALIYE MKRITO?

SEHEMU ISIYO NA MAJI.


 

Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments