UPUMBAVU WA MUNGU.

UPUMBAVU WA MUNGU.

1Wakorintho 1:25 “Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu’’.
 
Swali ni je! Mungu ni mpumbavu, au Mungu anao udhaifu?. Kwa mtu mwenye akili timamu akiangalia jinsi hii dunia ilivyoumbwa na sayari zake na nyota zake nyingi, akiangalia jinsi milima na mabonde na mito ilivyoumbwa kwa namna ya kushangaza, akaangalia vile vile Mungu alivyoumba vitu vyote na jinsi yeye mwenyewe alivyoumbwa na kupewa akili nyingi namna hii mpaka za kugundua ndege na kwenda huko juu mbali sana angani, hawezi kufiria kuwa Mungu ana upumbavu au anayo madhaifu yoyote..Na ndivyo ilivyo.
 
Lakini kwanini biblia inasema upumbavu wa Mungu, au Udhaifu wa Mungu?. Je! Inazungumzia katika Nyanja gani?..Inazungumziwa katika Nyanja yetu sisi jinsi tunavyomwona Mungu, hata wewe hapo kweli unaweza ukawa upo sahihi sana kwa kile unachokifanya, lakini hiyo haikufanyi watu wengine wote wakuone upo sahihi, wengine watakuona unafanya kitu cha kipumbavu haijalishi ni cha maana kiasi gani..Ndivyo ilivyo kwa Mungu wapo watu japo wanamfahamu kuwa Mungu ni mweza wa yote lakini wanayadharau mambo yake ya msingi ambayo yeye ndio kayatukuza..
 
Sasa ukisoma mistari ya juu yake kidogo utaona wayahudi walikuwa wanamtazamia Mungu kuwa atakuja kwa Ishara madhubuti itokayo mbinguni kama vile kung’aa kama jua,au kutoa Ishara kubwa zaidi hata ya zile za kina Musa na Eliya, lakini alipokuja na kumwona mbona ni mpole, mbona hajazaliwa kwenye familia ya kitajiri, mbona ni maskini, halafu, isitoshe hatma yake inaanishia kwenye kifo cha aibu cha kutundikwa msalabani uchi, moja kwa moja wakamdharau wakasema huyu hawezi kuwa masihi…Vile vile Wayunani nao (ambao wanawawakilisha watu wa mataifa yote), walitazamia kuona hekima ndani yake yaani walitazamia wasikie kutoka kwake kanuni mpya za ki-fizikia na kikemia na hesabati ambazo zitawafanya wafikie viwango vingine vya ustaarabu wa dunia na kuwafanya waishi maisha mengine ya kipekee..lakini walipomsikia anasema “Msisimbukie maisha watafakarini ndege, hawapandi wala hawavuni” wakamwona kama huyu ni kichaa kwao zikawa kama habari za kipuuzi zisizoongeza chochote katika jami..
 
1Wakoritho 1:22 “Kwa sababu Wayahudi wanataka ishara, na Wayunani wanatafuta hekima;
23 bali sisi tunamhubiri Kristo, aliyesulibiwa; kwa Wayahudi ni kikwazo, na kwa Wayunani ni upuzi;
24 bali kwao waitwao, Wayahudi kwa Wayunani, ni Kristo, nguvu ya Mungu, na hekima ya Mungu.
25 Kwa sababu upumbavu wa Mungu una hekima zaidi ya wanadamu, na udhaifu wa Mungu una nguvu zaidi ya wanadamu.”
 
Hivyo kwa ujumla Dunia nzima habari za Yesu zilikuwa kama za kipuuzi tu, haziingii akilini sio tu kwa watu wasiomjua Mungu lakini pia hata kwa watu wa kidini..Ni upuuzi..Ndio maana Bwana Yesu aliwaambia mahali Fulani makutano (HERI MTU YULE ASIYECHUKIZWA NAMI!… Mathayo 11:6), au kwa lugha nyingine heri mtu yule asiyechukizwa na ujio wangu au utendaji wangu kazi!
 
Lakini wayahudi na wayunani…hawakujua kuwa hapo ndipo misingi ya mbingu na nchi ilipolala, hapo ndipo chanzo cha hekima yao kilipo, hapo ndipo ukombozi wa Roho zao zilipo, hapo ndipo kiti cha enzi cha Mungu wao kilipo..Na chanzo cha vitu vyote na viumbe vyote..
 
Na ndio maana Biblia inaweka wazi kabisa mfano laiti wangelijua hilo wasingedhubutu kumsulibisha Bwana wa utukufu..
 
1Wakorintho 2:7 “bali twanena hekima ya Mungu katika siri, ile hekima iliyofichwa, ambayo Mungu aliiazimu tangu milele, kwa utukufu wetu;
 
8 ambayo wenye kuitawala dunia hii hawaijui hata mmoja; maana kama wangaliijua, wasingalimsulibisha Bwana wa utukufu;”
 
Ni sawa tu na mtu asiyeijua Almasi, hata akikutana nayo shambani kwake atailima tu na kuitupa nje kama mawe mengine tu..Lakini kama angejua kuwa wapo watu wanaokaa miezi na miezi chini ya ardhi, usiku na mchana hawaona jua wala mwezi, wakipitia hatari nyingi za kufukiwa na vifusi vya udongo, kuitafuta, hawaipati lakini hawakati tamaa wakiamini siku moja watapata walau kipande kidogo tu cha dini hilo, kwasababu wanajua thamani yake ni zaidi ya hata ya mshahara wa watu elfu wanaolipwa mishahara mizuri ofisini kwa miaka mingi….Kama vile Yule mtanzania ambaye hajaenda shule aliyepata almasi ya sh. Bilioni Tatu, fedha ambayo mameneja 10 na wakurugenzi 10 wanaweza kuitafuta katika makumpuni yao mpaka kustaafu kwao na wasiipate…
 
Na hiyo yote ni kwasababu kaelewa tu thamani ya almasi. Vivyo hivyo na kwa Mungu, huwa anaificha thamani ya almasi yake yaani (YESU KRISTO) machoni pa watu wengi, na wakati mwingine inaonekana haina thamani kabisa, inaonekana kama ni upuuzi Fulani hivi, yaani mtu ambaye anampa leo Kristo maisha yake anaonekana kama kapoteza dira ya maisha, au amepungukiwa akili,..au mtu ambaye anataka kumjua Kristo na kulishika Neno lake, anaonekana sasa huyu ndio mpumbavu kabisa na mvivu..
 
Lakini hawajui kuwa jinsi mtu huyo anavyozidi kufikia kile kilele cha utimilifu wa kumjua Kristo ndivyo anavyozidi kuwa mbali kuliko upeo wa ufahamu wao ulipo..Kwasababu yeye kakiendea moja kwa moja chanzo cha mambo wanayoyatafuta wao kwa miaka mingi, hivyo uwezekano wa yeye kupata kila kitu ni mkubwa kuliko huyo akidharauye chanzo..
 
Nataka nikuambie hakuna mtu yeyote aliyemfuata Bwana Yesu akajuta baadaye, kwa upande wangu mimi sijaona, Daudi naye hakuliona hilo mpaka akasema
 
Zaburi 37:25 “Nalikuwa kijana nami sasa ni mzee, Lakini sijamwona mwenye haki ameachwa Wala mzao wake akiomba chakula.”
 
Na bado hatujaona utukufu alionao Bwana Yesu Kristo vizuri, tukifika huko ndio tutamwelewa kwanini anaitwa Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa wafalme, na wamwendeao wanaitwa makuhani wake, uzao mteule, watu wa Milki ya Mungu. Je! Unamkataa leo hii Bwana Yesu ambaye alikufia, ambaye alikupa uzima, ambaye mpaka sasa uhai wako upo mikononi mwake, unakimbilia vitu visivyokupa uhai, unavihangaikia hivyo kana kwamba siku ukifa vitakuhifadhia…kumbuka maandiko haya yanatimia juu yako 1 Wakorintho 1: 18 “Kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuzi, bali kwetu sisi tunaookolewa ni nguvu ya Mungu”.
 
Mgeukie Bwana Yesu akupendaye, anapokuita usikatae, yeye ni HEKIMA YA MUNGU, iliyokataliwa na ulimwengu lakini mbele za Mungu ni LULU YA THAMANI…Anakupenda UPEO kiasi kwamba hakuna mtu yeyote alishawahi kufikia kiwango hicho cha upendo.
 
Ubarikiwe.

UWEZA WA MUNGU UNAONEKANA WAPI?

BASI MUNGU AKAMUADHIMISHA SANA..

NJIA YA MSALABA

NI KWASABABU YA YESU KRISTO.


Rudi Nyumbani:

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments