Kwanini biblia inaitaja mara kwa mara dhahabu ya Ofiri?

Kwanini biblia inaitaja mara kwa mara dhahabu ya Ofiri?

SWALI:Kwanini biblia inaitaja mara kwa mara dhahabu ya Ofiri? Umuhimu wake ni upi?


Ofiri ni eneo, lililokuwa maarufu zamani enzi za biblia kwa biashara ya madini na vito, eneo hili lilikuwa maeneo ya huko Arabia. Kwamfano dhahabu zote Sulemani alizotumia kujengea hekalu alikwenda kuzichukulia huko Ofiri kwa merikebu zake (Wafalme 10:22)

Ni sawa na leo useme dhahabu ya Geita, Au Tanzanite ya mererani,. Ndivyo ilivyokuwa zamani dhahabu au mawe ya thamani yalikuwa yapatikana eneo hilo la Ofiri.

 Hivi ni baadhi ya vifungu ambavyo utaweza kukutana na Neno hilo;

1Wafalme 9:28 “Wakafika Ofiri, wakachukua toka huko dhahabu, talanta mia nne na ishirini, wakamletea mfalme Sulemani”.

1Wafalme 10: 11 “Tena merikebu za Hiramu, zilizochukua dhahabu kutoka Ofiri, zikaleta kutoka Ofiri miti ya msandali mingi sana, na vito vya thamani”.

1Wafalme 22: 48 “Yehoshafati akafanya merikebu za Tarshishi ziende Ofiri kuchukua dhahabu; walakini hazikuenda; kwa maana merikebu zilivunjika huko Esion-geberi”.

Ayubu 22: 24 “Nawe hazina zako ziweke mchangani, Na dhahabu ya Ofiri iweke kati ya mawe ya vijito”;

Soma pia, Ayubu 28:16,

Sasa tukilijua hilo, upo unabii ambao Isaya aliuzungumza kuhusu siku ile ya Bwana inayotisha, akasema jinsi Mungu atakavyoleta maangamizi, watu wataadimika sana, kama dhahabu, tena akaeleza kwa mifano kabisa akasema, wataadimika kama ile dhahabu ya Ofiri, watu wanaoifahamu sana,  ili watu wapate  picha yenyewe jinsi mambo yatakavyokuwa mabaya, ni sawa na leo tuseme, watu watakuwa adimu kama Tanzanite, ile Tanzanite ya mererani..

Tusome;

Isaya 13:9 “Tazama, siku ya Bwana inakuja, siku kali, ya hasira na ghadhabu kuu, ili iifanye nchi kuwa ukiwa, na kuwaharibu watu wake, wenye dhambi, wasikae ndani yake.

10 Maana nyota za mbinguni na matangamano havitatoa nuru yake; jua litatiwa giza wakati wa kucha kwake, na mwezi utaacha nuru yake isiangaze.

11 Nami nitaadhibu ulimwengu kwa sababu ya ubaya wake, na wenye dhambi kwa sababu ya hatia yao; nami nitaikomesha fahari yao wenye kiburi; nami nitayaangusha chini majivuno yao walio wakali;

12 nitafanya wanadamu kuadimika KULIKO DHAHABU SAFI, na WATU KULIKO DHAHABU YA OFIRI.

13 Kwa hiyo nitazitetemesha mbingu, na dunia itatikiswa itoke katika mahali pake, kwa sababu ya ghadhabu ya Bwana wa majeshi, na kwa sababu ya siku ya hasira yake kali”.

Siku hiyo  watu wengi sana watakufa,idadi isiyohesabika, watauliwa na Mungu mwenyewe, kiasi kwamba kumwona mwanadamu mwenzako ulimwenguni itakuwa ni kama vile kuona dhahabu..Kwa jinsi watakavyoadimika.

Leo hii duniani kuna watu si chini ya bilioni saba, hatushangai wakati huo wakabaki watu elfu moja tu, au hata chini ya hapo. Ni kama ilivyokuwa kipindi cha Nuhu kati ya mabilioni ya watu waliokuwepo duniani, walibaki watu nane tu, vivyo hivyo siku ile ya Bwana itakuwa kwa namna hiyo.

Siku hizo zipo karibu sana, kwasababu biblia inasema, uharibifu utakuja wa ghafla wakati ambao watu hawautarajii kabisa, wakati ambao  wanasema kuna amani. (1Wathesalonike 5:3)

Lakini habari njema ni kwamba mpaka hiyo siku ya Bwana ije duniani, unyakuo utakuwa tayari umeshapita, na watakatifu wameshanyakuliwa.

Vivyo hivyo na sisi wakati huu ni wa kujiweka tayari, kumtazama Bwana. Na kuhakikisha kuwa wokovu upo ndani yetu. Ili hata kama unyakuo utapita leo usiku basi, tuwe na uhakika hatubaki hapa duniani, kwenye ghadhabu na hasira ya Mungu.

Shalom

Ili kufahamu kwa undani siku hiyo itakavyokuwa tazama vichwa cha masomo mengine chini;

Tafadhali washirikishe na wengine habari hizi njema, na pia kama utapenda tuwe tunakutumia mafundisho ya Neno la Mungu ya mara kwa mara kwa njia ya email yako au Whatsapp basi tutumie ujumbe kwenye namba hii +255693036618 au +255789001312

Mada Nyinginezo:

MAPIGO YA VITASA SABA, NA SIKU YA BWANA.

KIAMA KINATISHA.

UTAWALA WA MIAKA 1000.

ROHO YA MPINGA KRISTO IKITENDA KAZI SIKU HIZI ZA MWISHO

Rudi nyumbani

Print this post

About the author

Admin administrator

Subscribe
Notify of
guest
0 Comments
Inline Feedbacks
View all comments